Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

***SURA YA THELATHINI NA SABA***





(MSIMU WA 02)





*** HUNA HAKI YA UHAI ***


Glasi za vinywaji ziligongeshwa … Klang! Klang! … Zikafuatiwa na kelele sasa za binadamu zikishangilia … Hureeeee! Hawakuwa wengine bali wahusika wa kundi la WAGENI. Nyuso zao zilijaa tabasamu. Baada ya kunywa vinywaji, waliketi chini wakamuacha Vitalis pekee akiwa amesimama.
“Ni jambo la kufurahia kufanikiwa kwa hatua yetu ya kwanza tangu tukutane na kuunda familia hii. Nadhani wote hapa mnaamini msemo wa nyota njema huonekana asubuhi, hatua yetu hii ya kwanza ni nyota njema na tunaamini tutamaliza kama tulivyoanza.” Vitalis aliweka kituo, wenzake wakapiga makofi kisha akaendelea;
“Sasa ni wakati wa kujipanga kukabili hatua yetu ya pili. Kazi iliyo mbele yetu ni kuhakikisha tunasafisha uchafu wote uliopo kwenye jeshi la polisi. Sisi wote hapa ni mashahidi kwamba kwa njia moja ama nyingine ujihusanishaji wa polisi na kundi hili haramu la bwana Kim inawia vigumu mapambano ya kufuta uhalifu huu juu ya uso wa dunia. Kwahiyo basi, nguvu ile ile tuliyoiweka kwenye pambano letu la kwanza tutaihamishia huku. Tutatumia nguvu na akili zetu zote kunyofoa mizizi mirefu ya uhalifu huu bila kujali utatugharimu nini. Hatuna cha kupoteza zaidi ya hofu zetu. Sisi ni wageni wasio na mualiko, mgeni njoo mwenyeji apone kwetu hilo ni mwiko.”
Makofi yalipigwa tena baada ya Vitalis Byabata kumaliza kunena. Wote waliweka ngumi zao hewani wakasema kwa pamoja:
“Hakuna wa kutuzuia!”
Wakagongesha tena glasi zao kisha wakazipeleka mdomoni.
Masaa matatu baada ya tafrija hiyo fupi, Bakari alikuwa yupo kwenye kiti cha kazi mbele yake ikiwa imeketi tanakilishi mpakato. Pembeni ya tanakilishi hiyo kulikuwapo na karatasi nyeupe ikiwa imeandikwa namba ya simu na maneno yasomekayo ‘OCD’. Bakari aliiweka hiyo namba ya simu kwenye tanakilishi yake ndani ya kichumba kidogo cha bluu kilichotokea kwenye skirini, alafu akabonyeza kitufe kikubwa kilichoandikwa ‘enter’. Mara ramani ya Dar es Salaam ikaja na kuonyesha kidoti chekundu eneo fulani mtumiaji wa namba hiyo anapopatikana. Bakari akatabasamu,punde tu Vitalis akatokea chumbani akaungana na Bakari.
“Umeipata?”
“Ndio, nimekwishaipata. Eneo alilopo ni hilo hapo kwenye ramani.”
“Vyema. Sasa mtumie ujumbe wake aupate.”
“Sawa, mkuu.”
Ndani ya muda mfupi simu ya OCD iliwaka taa na kutoa sauti ndogo … Ting! Ting! OCD alifungua simu yake akakuta ujumbe: “Maisha yako yatapotea muda si mrefu endapo hautotubu maovu yako unayoyafanya na Bwana Kim.”
OCD akashtuka kwa kuachama mdomowe. Alitoa macho akatizama kando yake kama vile kuna mtu ilhali yupo chumbani. Ujumbe haukuonyesha umetoka namba gani, OCD alikosa cha kufanya zaidi ya kutupa simu yake pembeni na uso wake kuunda ndita.
“Mshenzi gani huyu ananifuatilia?” OCD alijiuliza, alitabasamu kisha akabinua lips za mdomo wake.
“Amekosa watu wa kuwatishia. Kama ni kifo anatafuta atakipata.”
Usiku ukaenda.
Kesho yake nyumba ya OCD ikawa imezungukwa na walinzi kumi. Wote walikuwa wamebebelea bunduki mikononi mwao huku wakiwa wanatizama huku na kule kuhakikisha usalama. Kuanzia getini mpaka ndani ya uzio ulinzi ulikuwa kabambe.Umbali wa kilomita moja toka nyumba hiyo ya OCD ilipo, lilisimama gari la Kaguta. Ndani yake walikuwepo Jombi na Miraji wakiwa wamevalia ovaroli la bluu likiwa na chapa ya DAWASCO vifuani mwao.Walishuka garini wakavisha vichwa vyao kofia. Walitoa jembe, shoka na chepe kwenye gari kisha wakasogea hatua kama saba, wakatizamana.
“Itakuwa ni hapa.” Jombi alisema huku akionyeshea kidole chini. Miraji akatikisa kichwa kukubali. Eneo walilokuwepo lilikuwa na ubichi kidogo tofauti na sehemu zingine za kando. Waliinamisha migongo yao wakaanza kuchimba lile eneo kwanguvu wakitumia jembe na chepe. Baada ya dakika chache wakakutana na mabomba matatu chini. Jombi akakata mabomba hayo kwa jembe mara moja, maji yakaanza kumwagika. Walirudishia kifusi walichokiweka pembeni wakapanda gari na kuondoka.
Baada ya muda mfupi.
“Haloo! … Eeeh nyie Dawasco, mbona mmenikatia maji?” OCD alifoka. “Nipe niongee na meneja wenu … Hayupo? … Anakuja saa ngapi? … Mje haraka iwezekanavyo! … Natumai mtakuwepo hapa ndani ya muda mfupi!”
OCD alisonya baada ya kukata simu. Kitu ambacho hakujua ni kwamba alikuwa anaongea na Bakari ambaye pembeni yake alikuwa ameketi na Vitalis. Vitalis alimgusa begani Bakari, Bakari akampigia simu Jombi.
“Nendeni sasa.”
Taratibu Jombi na Miraji wakiwa wamebebelea mfuko wao wa vifaa wakaanza kusogelea jengo la OCD. Walifika getini wakaonyesha vitambulisho vyao vya DAWASCO, walinzi wakapiga simu ndani na kuuliza kuhusu huo ugeni, wakaambiwa wawaruhusu. Miraji na Jombi wakaingia ndani walipokutana na OCD.
“Nini shida?” OCD aliuliza.
“Itakuwa humu ndani kwako.” Miraji akajibu, “Bomba la kuleta maji lipo salama tokea huko tulipotoka, na majirani zako wanapata maji kama kawaida.”
“Embu tengenezeni basi haraka.”
“Sawa. Usihofu mheshimiwa.”
Miraji alitangulia mbele akielekea jikoni lakini Jombi alisita kumfuata hivyo wakampa fursa OCD kuwa wa pili kwenye msafara na kutimiza adhma yao ya kumuweka polisi huyo katikati. Baada ya hatua kadhaa wakiwa koridoni, Jombi alimkaba na kumziba mdomo OCD, Miraji akageuka na kutizama uso wa OCD uliokuwa umekunjamana ukisikilizia maumivu ya kubanwa kwa mishipa ya shingo;
“Mkuu, huwezi ukakimbia wala kujificha. Tubu maovu yako unayofanya na bwana Kim mbele ya kadamnasi. La sivyo pumzi yako itaacha mwili muda si mrefu. Huu ni ujumbe wako wa mwisho.”
Baada ya kusema hivyo, Jombi alipiga shingo ya OCD, OCD akadondoka na kuzirai. Jombi na Miraji wakapachika kamera kwenye nyumba ya OCD kila kona, walipomaliza wakaondoka wakipita kwenye msitu wa walinzi ambao walikuja kufahamu kilichoendelea dakika kumi baada ya wahusika kupotea.


****

☆Steve
 
***SURA YA THELATHINI NA NANE***


(MSIMU WA 02)





Saa tano na robo usiku.
Vitalis alikuwa juu ya kitanda akiwa amefunga macho kama mtu aliyelala. Alikuwa amevaa kaptula fupi huku kifua chake kikiwa wazi. Ni kama vile kuna kitu kilikuwa kinamsumbua kwani alikuwa akijigeuzia huku na huko huku akiwa amekunja sura yake. Baada ya muda mfupi akiwa anajibiduabidua Vitalis alianza kutota mno. Jasho lilimvuja na kulowanisha kitanda. Kama hilo halitoshi alianza kugugumia lakini ajabu sauti aliyokuwa anaitoa haikuwa iliyozoeleka, bali ya kunguruma kama simba. Jeraha lake la meno ya mbwa mwitu mkononi nalo lilianza kuvuja likitoa ute mzito wa maji maji, na wakati yote hayo yanafanyika macho ya Vitalis yalikuwa yamefumba.
Zilichukua dakika tano zoezi likiwa ni hilo hilo lajirudia. Vitalis alikuja shtuka akawa anahema kwanguvu. Alitizama viganja vyake na miguu, mishipa ilikuwa imedinda. Alijishika shingo kama vile anaugulia. Alinyoosha viungo vya mwili huku akiwa amekunja sura. Akajiuliza,
“Nini kimetokea?” huku akitizama vinyweleo vyake vilivyokuwa vimesimama dede.

Saa moja na nusu asubuhi.

Bakari alikuwa anapiga mswaki huku akiwa anatizama tanakilishi yake iliyokuwa inamuonyesha ndani ya nyumba ya OCD. Baada ya punde alimuona OCD akiwa anamkaribisha mtu ndani kwake. Bakari alivuta karibu picha ya kamera, akamuona bwana Isaac Makongo akiingia ndani na kuketi kwenye kochi akifuatiwa na OCD aliyeketi kando naye. Hapo Bakari akaamua kufuta picha za kamera zingine kwenye kioo cha tanakilishi yake na kukuza picha ya kamera moja tu ambayo ilikuwa karibu na wahusika wake. Alipofanya hivyo, alitoa mswaki mdomoni mwake akapaza sauti kumuita Vitalis, Vitalis akaja punde.
“Rekodi, haraka!” Vitalis alimuagiza Bakari, haraka zoezi hilo likaruhusiwa kisha wote macho yao yakawa yanatizama.
“Naomba mnipatie ulinzi ndugu zanguni nipo hatarini.” Sauti ya OCD ilivuma ikimuambia Isaac.
“Usihofu, tupo na wewe mwanzo mpaka mwisho. Fadhila zako kwetu si za kusahaulika. Umetusaidia sana kukamata hii nchi na tunakuahidi kukulinda.”
“Ahsante sana, Isaac. Ila unadhani ni nani aliye nyuma ya mpango huu wa kuniua?”
“OCD, Mr Kim ni mtu mkubwa sana ulimwengu mzima. Ni mtu mwenye mafanikio na kama unavyojua biashara zake, hawezi akakosa maadui. Maadui hao ndio wanaokutafuta kwakuwa wanajua mchango wako kwa bwana Kim. Ila ondoa hofu ushanipa taarifa.”
“Sawa. Nakuamini.”
“Mengineyo?”
“Hakuna lingine, mkuu. Labda tu niliulizie fungu langu, umepita mwezi sasa.”
“Lingine?”
“Hakuna.”
“Ok. Pesa yako itakuja kesho, kuna kijana wangu atakuletea ofisini kwako. Ila kumbuka kuna mzigo unakuja ukitokea Brazil, hakikisha unapita airport pasipo na shaka. Ni mzigo wa milioni mia tano, unga wa high class.”
“Niachie hiyo kazi, mkuu. Unajua huwa sikuangushi.”
Baada ya maongezi hayo walinyanyuka wakapeana mkono kisha wakatoka ndani. Bakari alimtizama Vitalis wote wakajikuta wanatabasamu.
Siku iliyofuata saa kumi na moja na dakika tano jioni, mlango wa OCD uligongwa. OCD alpofungua alimkuta mlinzi wake akiwa amebebelea kasha la CD. Mlinzi akamkabidhi kasha hilo na kumuambia:
“Kuna mtu amepitisha nje, amesema ni mzigo wako.”
“Nani?” OCD aliuliza.
“Simjui.” Mlinzi akajibu.
“Unaruhusuje mtu usiyemjua akupe kitu na ulete kwangu? Kama bomu je?”
“Hapana, mkuu. Nimekikagua nikaona ni CD tu.”
OCD alichukua ule mzigo akauweka ndani ya DVD player alafuakaketi pembeni ya runinga yake. Baada ya CD kucheza machozi yalianza kumtoka OCD. Aliona kila kitu ambacho alikifanya na kuongea na Isaac. Picha ya CD ilipokwisha, maandishi yalijionyesha yakisomeka: TUBU MAOVU YAKO KABLA HATUJASAMBAZA KANDA HII KWENYE VITUO VYA HABARI.
Uso wa OCD ukabadilika ghafla na kuwa mweusi zaidi. Alidondosha runinga yake akaipasua. Akatafuta kamera zote zilizopachikwa ndani kwake akazitoa na kuzipasua. Ujumbe ukaingia kwenye simu yake;
“It is too late.”
Nayo simu akairushia ukutani na kuipasua. Akapiga yowe kali la hasira. Jasho la hamaki na woga likamtoka. Machozi yakazidi kumbubujika, mwishowe akakaa kwenye kiti na kushika tama uso wake ukiwa na mikanganyiko ya hofu na hasira. Hakika ndege alikuwa tunduni sasa. Tena tundu bovu.
Baada ya masaa kumi na mbili, chaneli za runinga zikaanza kurusha matangazo ya moja kwa moja. Kanda ya OCD ilisambazwa kwenye kila kituo cha chaneli za runinga. Kwenye kila kioo cha runinga picha ya OCD na Isaac Makongo ikatapakaa, wananchi wakaona kwa macho yao. Haikuchukua muda mrefu, magari ya polisi yakaongozana kwenda kwa OCD. Walikuta mwili tu, OCD akiwa tayari ameshajimaliza kwa kunywa madawa. Ni msiba ndio ukafuata baada ya hapo, watu wengi wakahudhuria ikiwemo waliokuwa wafanyakazi wenzake na OCD, lakini wengiwao walikuwa wananchi wa kawaida ambao waliguswa na taarifa za OCD na eidha walitaka kumuona mtu huyo kwa sura kabla hajamezwa na udongo wa dunia.
Vitalis Byabata alikuwa ni miongoni mwa wahudhuriaji wa msiba. Alikuwa amevaa nguo nyeusi na miwani yenye vioo vya kahawia. Kidogo alikaa mbali na wenzake, alikuwa ametulia tuli akitikisa kichwa chake. Kulikuwa na makelele mengi watu wakiruruma huku na kule, ila kuna sauti fulani iliteka masikio Vitalis.
“Hili jambo linatutisha sasa, nani atakayefuata baada ya mkuu wetu? … Inabidi sasa tujitizame vizuri ndugu yangu bila hivyo tutakwisha.”
Vitalis akageuza shingo yake kutafuta makazi ya hiyo sauti. Kwa mbali toka kwake akaona watu wawili wananong’onezana. Kabla ya kujiuliza kwanini wale watu wanaongelea yale mambo, Vitalis alishangaa amesikiaje sauti toka mbali vile, tena ya watu wanaonong’onezana? Haikuwa kawaida. Badala ya kushughulikia wale watu Vitalis akaanza kukumbuka usiku ule aliokuwa anahangaika kitandani, je una mahusiano na yale mabadiliko yake? Mwishowe akaamua kupuuzia na kuweka akili yake kwa wale watu wawili ambao muda mfupi baada ya kuaga mwili wa marehemu waliagana na kuondoka. Mmoja wao aliyekuwa mfupi, jina Morgan, akiwa amevalia shati jeusi na suruali ya jeans alifuata gari lake Harrier akaingia ndani. Kabla hajaipa moto gari, alikabwakwanguvu na mtu tokea viti vya nyuma. Akaulizwa;
“Wewe ni nani? Na OCD na Bwana Kim ni nani zako?”
Morgan akaleta ngumu kusema kitu. Alikabwa kwanguvu zaidi, akaamua kusema;
“Naitwa Morgan, ofisa wa polisi.”
“OCD na Kim ni nani zako?”
“Mabosi wangu … Ni mabosi wangu.”
“Sawa sawa. Sasa basi, tunakupa nafasi ya kutubu ili uwe hai. La sivyo uhai wako utakuwa haki yetu.”
Baada ya hicho kitisho, mkabaji alishuka gari likaondoka. Kumbe alikuwa ni Vitalis Byabata, alitoa simu yake mfukoni akampigia Bakari.
“Nimepachika kifaa kwenye mojawapo ya gari, unaweza ukakiona hapo kwenye mashine yako? … Hakikisha unaifuatilia hiyo gari, naamini baada ya kumtishia atafanya move itakayotusaidia kuwapata wote.”
Simu ikarudishwa mfukoni. Kaguta akaondoka kurudi nyumbani, alimkuta Bernadetha akiwa chumbani pamoja na Kaguta. Walikuwa wamevaa gloves nyeupe. Juu ya meza kulikuwapo na sindano nyingi, madawa yaliyokuwa yamepondwa na kabeseni ka maji. Kaguta alikuwa anatwanga madawa, wakati Bernadetha akichukua madawa na kuyaweka kwenye maji kisha anayafyonza na sindano na kuziweka pembeni. Vitalis akawapa pole kwa kazi. Alivua miwani yake akasema;
“Kuna mambo nahisi hayapo sawa mwilini mwangu.”
Kaguta na Bernadetha wakaacha kazi yao na kumtizama Vitalis.
“Mambo yapi?” Bernadetha akauliza.
“Usiku nimekuwa nahangaika sana, natota jasho. Alafu ajabu, nimekua na uwezo mkubwa wa kusikia. Sijui imekuaje?”
“Vipi jeraha lako limepona?” Bernadetha akauliza, kabla Kaguta hajajibu, Bernadetha akanyanyua mkono wa Vitalis na kuutizama. Jeraha halikuwapo. Lilikuwa limekauka pasijulikane hata kama kuna kitu kilitokea. Bernadetha alimtizama Vitalis kwa uso wa butwaa. Akauliza;
“Imekuaje jeraha limepotea haraka hivyo?”
Mara sauti ya Bakari ikaingilia ikiwaita. Wote walitoka wakaenda sebuleni.
“Lile gari limeelekea msitu wa Pande!” Bakari alitoa taarifa. “Kutakuwa kuna kitu kinafanyika huko.”
Vitalis akamuita Jombi na Miraji akawataka wajiandae waende kazini.
Huko ndani ya msitu wa pande, Morgan akiwa na wenzake wanne walitoka kwenye gari wakatembea hatua kadhaa. Kisha wakaanza kujadili. Waliona msituni ni salama kuliko ndani ya nyumba kutokana na yale yaliyomkuta OCD. Ila baada tu ya muda mfupi, WAGENI wakawa tayari wamewasili eneo la tukio. Vitalis alisafisha koo lake, wakina Morgan wakageuka na kuwakuta wanaume wawili ndani ya vinyago; Kaguta na Vitalis. Morgan akatabasamu.
“Hatimaye mpo kwenye mikono yetu. Mlidhani sisi wajinga, sio? Kuja huku msituni huku mkiwa mmepachikatracker kwenye gari letu?Poleni sana. Kwa taarifa yenu tuliona mlichokiweka kwenye gari, na tumewavuta huku ili muwe historia. Tutawaua na kuwazika huku huku, hakuna atakayewajua.”
Vitalis akatikisa kichwa naye akasema:
“Unadhani hilo linawafanya msiwe wajinga? Bado nyie ni wajinga kwasababu, moja; mmesahau kwamba mmeacha alama za matairi ya magari matatu manne, alafu mkaacha moja hapo ili ionekane mpo wenyewe wakati mmekuja wengi, matokeo yake tumeshaharibu magari hayo. Pili, mmesahau kufuta nyayo zenu zilizoingia humu msituni, inaonekana mpo watu hamsini tano na hapo mnajidanganya kwa kutuonyesha mpo watano. Sasa unadhani na sisi ni wajinga kiasi cha kuja kupambana na watu hamsini na tano kwa wawili?”
Morgan alitizama wenzake, alafu akapiga mluzi. Mara wakatokea watu hamsini tokea gizani waliobebelea bunduki. Wote wakanyooshea bunduki kwa Vitalis na Kaguta. Vitalis naye akapiga mluzi, mara taa za gari zikawaka na kuwamulika wakina Morgan na kuwafanya vipofu kwa muda. Milio ya risasi ikavuma. Taa zilipozima, watu wote hamsini waliobebelea bunduki wakawa wapo chini wamekufa. Walibakia Morgan na wenzake wanne tu. Walipepesa macho yao huku na huko, waliposikia kishindo wakaelekezea bunduki zao huko na kufyatua risasi. Mara taa za gari zikawamulika tena usoni na kuwafanya vipofu, zilipozima wote wakawa wameuwawa kasoro Morgan ambaye alichomekwa sindano ya dawa shingoni na kupokonywa bunduki.
“Sasa sikia.” Kaguta alimwambia Morgan. “Dawa uliyowekwa mwilini itakumaliza pole pole. Bahati nzuri dawa ya kukuponya tunayo. Ila ili uipate, nenda katubu maovu yako mbele ya kadamnasi, la sivyo uhai wako utakuwa mali yetu.”
Baada ya hapo, Vitalis na Kaguta wakapotea.
Kwa siku mbili Morgan akawa mtu wa kukakamaa na kutema mapovu macho yakiwa yamemtoka na jasho likimchuruza. Siku ya tatu akaita vyombo vya habari akaeleza ushiriki wake na OCD na bwana Kim. Baadae mzigo wa boksi ukatumwa nyumbani kwake ukiwa umeandikwa ‘antidote’ kwa juu. Ndani yake alikuta kichupa kidogo chenye kinywaji rangi nyekundu. Akanywa.
“Mmmh … Mbona kama Fanta?”
Alipotizama kwa makini akakuta ujumbe kwenye kikaratasi cha chupa … HUNA HAKI YA UHAI. Polisi walipokuja kumkamata Morgan walimkuta tayari yu mfu. Alikuwa chini amekakamaa kama gogo kavu.



***

☆Steve
 
***SURA YA THELATHINI NA TISA***


(MSIMU WA 02)







**** MSAKO WA MAHAYAWANI ****

Mada moto katika vyombo vya habari ilikuwa ni kuhusu kujitokeza na kuuwawa kwa wahalifu. Picha ya OCD na wenzake kama Morgan na wengineo waliouwawa zilikuwa zaonyeshwa ama kuongelewa na wachambuzi mbalimbali. Lakini je kwanini wahalifu hao wamevuliwa nguo na kupokonywa uhai kwa muda huo? Nani yupo nyuma ya huo mchezo ambao ulionekana kukamata hisia za watu wengi? Hakukuwa na majibu. Vitalis alitabasamu akazima runinga kisha akawageukia wenzake waliokuwa wameketi wakielekeza macho yake kwake.
“Hongereni sana kwa kazi kubwa mliyoifanya. Sasa tunahamia kazi kwenye kazi nyingine pevu: Msako wa mahayawani. Wapo watatu, tutaanza na bwana Isaac Makongo. Lazima tumkamate ila akiwa hai kwasababu tunahitaji maelezo mengi toka kwake ambayo yatatusaidia kumpata mlengwa wetu, Kim Salvatore.”
“Kwahiyo tunapitia mpango gani?” Miraji akauliza. Vitalis akamgeukia Kaguta na kusema.
“Plan yetu ya sasa itaanza na Kaguta. Anajua sehemu ambayo Isaac huenda kumtizama mpira mara kwa mara. Pazuri kuanzia hapo.”
“Naomba na mimi nihusike!” Sandra akapendekeza, “Nataka na mimi nimshikishe adabu huyo mpumbavu!”
“Najua una hasira na Isaac, ila sidhani kwa sasa kama ni wasaa wa kuruhusu hasira hiyo iokoteze vya kutosha ndani yako.” Kaguta akashauri alafu akamgeukia Vitalis.
“Kwahiyo what’s the plan?”
“Plan ni kuhakikisha unatia pin kwenye tairi la gari la Isaac.” Vitalis akaonyesha pini ndogo nyembamba ndefu. “Pini hii itakuwa inapenya taratibu kwenye tairi na mwishowe tairi litapasuka, hapo atakuwa tayari ametoka eneo la mpira, matumaini yetu atakuwa mwenyewe na hivyo tutatokea na kumkamata. Cha umuhimu kuwasiliana.” Vitalis akaeleza, Kaguta akatikisa kichwa kukubaliana.
Siku tatu baadae ndani ya Samaki-Samaki Makonde, Mbezi beach, kukiwa ni usiku, Kaguta na Isaac wakawepo hilo eneo. Isaac alikuwa amejitenga kidogo na umati wa watu, alijiweka kando akiwa anatizama vyema runinga na kuishushia na bia baridi. Kaguta alikuwa ameketi upande wa kushoto wa Isaac, hakuwa naye amejichanganya na watu, zaidi alikuwa anamtizama Isaac katika kila tendo alilokuwa anafanya. Punde akanyanyuka na kwenda nje sehemu ya kupaki magari, akapepesa macho yake kushoto na kulia kutafuta gari la Isaac, hakuona kitu. Akarejea ndani na kuketi sehemu yake.
“Hajaja na gari leo?” Kaguta akajiuliza. Alipeleka mkono wake kidevuni akawa anajikuna-kuna huku akitafakuri. Alimtizama Isaac akaona anaagiza kinywaji kingine baada ya cha mwanzo kuisha, hiko kitu kikampa mawazo Kaguta ambaye aliishia kutabasamu na kuanza kuzingatia kinywaji cha Isaac huku pia akichungulia dakika za mpira uliokuwa unaonyeshwa.
Ikiwa ni dakika ya hamsini na tano ya mpira, chupa ya kinywaji ya Isaac ilikuwa tayari imeteremka karibia na sakafu yake. Kaguta alinyanyuka akatokomea. Isaac akanywa fundo moja la mwisho alafu akanyoosha mkono kutaka kuita muhudumu, haraka Kaguta akatokea akiwa amevalia sare za wahudumu na mkononi mwake ana sahani iliyobebelea bia baridi. Aliweka bia mezani akaifuta na kuifungua kisha akaondoka, Isaac akadaka kinywajiche na kuanza kukishughulikia. Kaguta aliyetokomea akarejea akiwa na nguo zake za awali, aliketi eneo lake moja kwa moja akatizama dakika za mpira zasemaje, dakika sabini kamili, akatabasamu.
“Okay, sasa tutizame mpira.” Kaguta akajisemea.
Ilipofikia dakika ya themanini na tano ya mpira, Isaac akaanza kuona giza. Alitikisa kichwa chake huku akikipiga lakini haikusaidia kitu. Macho yalikuwa mazito hata kichwa pia, akaishia kulala juu ya meza. Alipokuja kufungua kope zake, alijikuta yupo kitini amefungwa ndani ya jengo kuukuu. Vitalis na Kaguta wakatokea na kumsogelea.
“Pole sana mheshimiwa.” Kaguta alisema huku akiigiza sura ya mtu anayesikitika, “Hatimaye upo mikononi mwetu. Tunaweza kukufanya lolote lile kuanzia sasa, ila tusingependa kufikia huko kwakuwa najua tutamalizana kwa amani. Mr Kim Salvatore ni nani kwako?”
Isaac akatabasamu.
“Kama mmenikamatia hilo, nawapa pole maana sitasema lolote. Nawashauri mniue msipoteze nguvu zenu.”
Vitalis akatabasamu.
“Tunajua haitokuwa rahisi kwako kusema. Ila nasi tumejiandaa sana kwa hilo.”
“Narudia tena, mnapoteza nguvu na muda wenu bure, sitosema chochote.” Isaac akasisitizia. Vitalis akakunja shati lake akamtandika ngumi Isaac tumboni. Tena na tena, tena na tena, Isaac akatema damu.
“Utasema husemi?” Vitalis akauliza kwa ukali. Isaac akatabasamu na kutikisa kichwa chake kukataa. Vitalis akamuwasha kofi kali Isaac kisha akasonya.
“Huu ni mwanzo tu, utasema nakuambia!”
Ghafla vikopo vitatu vya chuma vikarushwa ndani ya chumba walichokuwepo wakina Vitalis na mateka wao. Havikujulikana vimetokea wapi. Vikopo vile vilianza kutema moshi mzito mweupe na haikuchukua muda mrefu kutapakaa, wakaingia wanaume watatu wenye kimo sawa waliovalia suti nyeusi na vinyago vya kuzuia gesi usoni, wakapambana na Vitalis na Kaguta ambao walikuwa dhaifu kila walipozidi kuvuta hewa. Ndani ya sekunde chache tu, Vitalis na Kaguta wakawa wameshalazwa chini, hawajielewi. Wanaume wale watatu wakamfungua kamba bwana Isaac Makongo, mmoja akamuweka begani na kutangulia kutoka nje, wengine wawili wakasogelea miili ya Vitalis na Kaguta, wakaionyeshea midomo ya bunduki. Kabla ya kufyatua risasi, sauti ya gari inayoserereka ilipasua masikio yao, wakashtuka. Punde wakasikia vishindo vya miguu na sauti za watu, haraka wanaume wale wawili wakaondoka lile eneo.
Kwenye mida ya saa tisa ya jioni, Bakari kama afanyavyo mara kadhaa alikuwepo mbele ya tanakilishi yake. Alifungua mtandao akapachika jina la Isaac Makongo kisha akabofya kitufe cha kutafuta majibu, muda mfupi picha za Isaac, anwani na maelezo kadhaa yakajiri yakisema ni mfanyabiashara wa nyama za kusindika na mchezaji wa zamani wa mpira. Bakari akaandika maelezo hayo kwenye notebook yake kisha akanyanyuka na kuondoka.
Kwenye mida ya saa kumi na robo ya jioni, Vitalis alianza kugugumia akiwa kitandani amelala. Jasho lilikuwa lamchuruza. Alikuwa anakunja-kunja uso wake kama mtu asikiliziaye maumivu makali. Aling’ata meno akaamka kwa pupa. Alijitizama mikononi mwake akaona kucha zake zimekuwa ndefu kuliko kawaida. Kifuani kulijaa nywele. Meno yake chonge yaliongezeka urefu, ya chini na juu. Ila punde akarudi katika hali yake ya kawaida, kila kiungo kikaa sawa. Vitalis akanyanyuka toka kitandani akavaa shati na kwenda nje. Kibarazani akamkuta Miraji anacheza na mdogo wake, Marietta.
“Shikamoo Uncle!” Marietta alimsalimu Vitalis kwa sauti ya juu. Vitalis akaitikia kwa furaha kisha akamnyanyua binti huyo juu juu na kumrusha-rusha. Alimkabidhi shilingi mia tano akamtaka aende kununua anachokitaka, Marietta akaondoka upesi kuelekea dukani.
“Nini kilitokea asubuhi baada ya kupoteza fahamu?” Vitalis aliuliza. Miraji akamtizama Vitalis.
“Waliondoka na mateka, tulishindwa kuwafukuza kwasababu hali yenu haikuwa nzuri.”
Vitalis akashusha pumzi ndefu. Miraji akauliza:
“Unadhani gesi waliyoitumia itakuwa na madhara kwenu?”
Vitalis akatikisa kichwa. “Sidhani. Hawawezi wakafanya hivyo kwasababu mkuu wao naye alikuwemo ndani. Mlipata kuona nyuso za hao watu waliovalia suti?”
“Hapana!” Miraji akajibu, “Ila tulichokigundua ni ufanano wao wa kimo na rangi pia.”
“Walijuaje kama tupo ndani ya lile jengo?”
“Hapo ndipo hatujapatia jibu.”
Kimya kikakatiza katikati yao. Mara kwa mbali akaonekana Bakari akija na Marietta. Bakari alikuwa amebebelea mkoba mweusi wakati Marietta akiwa ameshikilia pipi kubwa ya kijiti mkononi.Marietta alipitiliza mpaka ndani, Bakari akajiunga na Vitalis na Miraji kibarazani.
“Kuna kitu nataka muone.” Bakari alisema huku akiufungua mkoba wake. Alitoa karatasi nne nyeupe zenye picha na maandishi akawakabidhi Vitalis na Miraji, wakaanza kuzipekua na macho yao. Baada ya sekunde chache Miraji akalipuka kwa kusema:
“Namjua huyu!”
Alionyeshea picha moja karatasini. Vitalis na Bakari wakaitizama.
“Huyu ni baba yangu mkubwa! Anaitwa Tahid. Mara yangu ya mwisho kumuona ni kipindi kile cha msiba wa baba.” Miraji akasema kwa tahamaki.
“Huyu ni mshirika wake Isaac Makongo!” Bakari akasema, “Ni mshirika wake mkubwa wa biashara yao ya nyama.”
“Wanasindikia hizo nyama zao wapi?” Vitalis aliuliza.
“Eneo lao la kiwanda ni Tegeta.” Bakari akajibu.



***

☆Steve
 
***SURA YA AROBAINI***



(MSIMU WA 02)






“Baba mkubwa yako alikuwa ni mfanyabiashara tangu muda gani?” Vitalis alimuuliza Miraji.
“Sijui.” Miraji akajibu, “Ninachojua ni kwamba alikuwa mwalimu. Habari za kuwa mfanyabiashara ndio nazisikia hapa!”
“Basi atakuwa anafanya kwa siri.” Vitalis akabashiri kisha akaongezea; “Hii kazi nadhani itafanywa vyema na wewe, Miraji, na mama yako. Yatupasa tuutumie huo udugu wenu kama njia ya kumvuta Tahid kwenye mwanga na ya kutupatia Isaac Makongo.”
“Sawa.” Miraji akaitikia.
Siku iliyofuata asubuhi Bernadetha akiwa amejivika khanga alienda nyumbani kwa shemeji yake, bwana Tahid. Alikaribishwa na mke wa shemeji wake, akaketi sebuleni, punde akaungana na mlengwa wake ambaye alikuwa anajiandaa apate kwenda kazini.
“Karibu sana, shemeji.”
“Ahsante.”
“Mbona ghafla hivyo?”
“Nimekukumbuka tu. Ni kitambo sasa tangu mume wangu amefariki na hatujapata kuonana kabisa.”
“Kweli kabisa, ni muda mrefu: kazi zinabana. Hapa yenyewe ungechelewa, usingenikuta. Vipi maisha lakini?” Tahid aliuliza huku akitengenezea tai yake shingoni.
“Maisha hivyo hivyo tu, yanasonga.”
“Ashukuriwe Mungu. Karibu sana.”
“Nimeshakaribia, shemeji. Lengo langu kubwa la kuja hapa ni kupata kufahamu mambo kadhaa toka kwako.”
Tahid akakaza macho.
“Yapi tena?”
“Ya kawaida tu, shemeji. Kwani kuna shida?”
“Wala!” Tahid alipandisha mabega yake.
“Sawa. Nataka tu kufahamu kama umepata taarifa yoyote juu ya wale waliomuua mume wangu. Hakuna chochote ulichopata? Hakuna yeyote unayemjua anahusika kwa njia yeyote ile?”
Tahid akatikisa kichwa chake huku akiubinua mdomo wake.
“Kusema ukweli hakuna ninachokifahamu … Hakuna nilichokipata!”
“Kabisa?”
“Kabisa! Ningepata kujua chochote nisingesita kukujuza.”
Bernadetha akashusha pumzi ndefu.
“Sawa, shemeji. Naomba nikuache, tutaonana kadiri muda unavyotaka.”
Bernadetha akaondoka. Tahid akabakia kwenye kiti uso wake ukiwa umetulia tuli. Ni kama vile alisahau kujiandaa kwa ajili ya kwenda kazini mpaka pale mke wake alipokuja kumshtua.
Zikapita siku mbili.
Siku ya tatu, Bernadetha akarudi tena kwa shemeji yake, bwana Tahid. Ilikuwa ni jioni kavu, anga lilikuwa jekundu kwasababu jua lilikuwa lazama hivyo hata mawingu yalikuwa na rangi nyeusi. Bernadetha alikuwa kavalia suruali ya jeans isiyombana, pamoja na shati jeupe lililobebelea tangazo la bia, huku miguuni akijivika raba nyeupe.
“Karibu.” Bwana Tahid alisema huku uso wake ukiwa na makunyanzi. Bernadetha akaingia na kwenda kuketi pale alipoketi mara yake ya mwisho. Bwana Tahid akaungana naye huku akiwa analazimisha tabasamu.
“Karibu tena shemeji.”
“Ahsante, nimekaribia. Samahani sana kwa ugeni wa ghafla.”
Tahid akacheka kiuongo alafu akauliza:
“Hapana, unakaribishwa muda wote, shemeji.”
“Ahsante. Nimekuja kwa suala langu lile lile, shemeji.”
“La kifo cha mumeo?”
“Haswaa.”
Tahid akatikisa kichwa.
“Nadhani shemeji huu ni muda wa kusahau yaliyopita na kuganga yajayo. Sioni kama kuna haja ya kufukua tena maiti ambayo imeshasagwa na kumumunywa na udongo.”
“Shemeji, mume wangu aliuwawa. Siwezi kulala wala kukaa kwa amani mpaka pale nitakapohakikisha wote wanaouhusika wanaenda kaburini.”
“Umepangaje kuhakikisha hilo, shemeji?”
“Lipo kapuni.”
“Nakutakia kila la kheri.”
“Ahsante. Nimekuja kwako kwa mara ya mwisho, bwana shemeji. Naomba uniambie kama kuna lolote unalolijua kuhusu kifo cha mume wangu.Lolote ambalo unajua silijui.”
Uso wa Tahid ukaumuka.
“Unadhani nakuficha kitu, shemeji?”
“Labda.” Bermadetha akajibu kwa macho makavu.
Tahid akatabasamu kwa dharau. Akakuna kidevu chake mara tatu na kusema kwa sauti ya taratibu.
“Naomba uondoke, shemeji.”
Bernadetha akanyanyuka.
“Naenda. Ila jua utamfuata kaka yako muda si mrefu.”
Mwanamke akaondoka akitembea kwa kujiamini. Tahid akamsindikiza kwa macho makali akiwa amevimba kama mtu aliyekabwa na gunzi la moto kooni. Bernadetha alipotoka tu mlangoni, Tahid akanyofoa simu yake mfukoni, akaweka namba na kuiweka sikioni.
“Listen Puzo. Kuna mtu nataka mummalize haraka iwezekanavyo! … Hilo swala la pesa, niachie mimi.” ….
Siku iliyofuata watu wawili wakiwa ndani ya gari aina ya Noah walipaki karibu kabisa na nyumba ya marehemu bwana Malale. Kabla hawajatoka ndani walificha nyuso zao na vinyago vyeusi, wakakoki bunduki zao na kushuka haraka kwenda ndani. Hatua kadhaa mbele ya Noah kulikuwepo na gari la Kaguta, ndani walikuwepo Kaguta mwenyewe na Vitalis. Walikoki bunduki zao, Vitalis akasema:
“I love you Bernadetha. Mtego umekubali.”
Wakashuka wakitembea kwa tahadhari, waligawanyika mmoja akaenda mbele mwingine nyuma. Wakavamia ndani na kuwaweka watuhumiwa wao chini ya ulinzi. Waliwaweka kwenye gari na kuondoka nao mpaka kwenye jengo lao la maumivu. Wakawafunga kamba kwenye nguzo, wakavaa vinyago na kuwapa kipondo kizito kabla hawajakiri aliyewatuma ni bwana Tahid.
“Mmemfanyia kazi ngapi bwana Tahid mpaka sasa?” Kaguta aliuliza.
“Tumefanya kazi mbili tu.” Mateka mmoja akajibu kwa huruma huku akichuruza damu mdomoni.
“Ipi na ipi?”
“Kazi ya kumuua bwana Yudu Makombo na hii.”
“Kwanini mlimuua Yudu?”
“Bosi wetu Tahid aliambiwa afanye hivyo ili apate tenda ya nyama kwa bwana Isaac Makongo.”
Vitalis akatikisa kichwa chake. Alimtizama Kaguta na kumpa ishara ya kuondoka. Walifuata kamera yao iliyokuwa inarekodi kila kitu walichokuwa wanakifanya, wakaizima.
Jua la siku iliyofuata likachomoza, Tahid akiwa anataka kwenda kazini alitoka ndani kwake akajiweka ndani ya gari. Ila ghafla kabla hajatimka, kioo chake juu ya kichwa kikamjulisha kuna mtu kwenye viti vya nyuma. Aligeuka haraka akakutana na Miraji.
“Unaendeleaje baba mkubwa?”
Tahid akatoa macho ya hofu.
“Umeingiaje humu? Unataka nini?”
“Si la muhimu sana kujadili hilo, ila kwakuwa umeniuliza nitakujibu. Nimekuja kukuchukua, na kwasababu huko tunapoenda tunahitaji gari ili tuwahi ikabidi nikungojee humu uje na ufunguo.”
Miraji akatoa kitambaa cheupe mkononi akamziba nacho pumzi bwana Tahid. Kitambaa kilikuwa kina dawa, Tahid alipovuta pumzi mara moja tu, akazirai. Miraji akahamia viti vya mbele, gari likaondoshwa.
Tahid alikuja kujikuta ndani ya jengo kuukuu akiwa amefungwa kamba kwenye nguzo. Alipotizama pembeni yake akawaona watu wake aliowatuma, akashtuka. Walikuwa wamechoka mno kwa kipigo. Nyuso zao zilikuwa zimetapakaa damu, haikueleweka wamekufa ama wamezirai.
“Puzoo!” Bwana Tahid aliita, lakini ikawa bure. Punde akaja Vitalis, Kaguta, Miraji na Bernadetha, wakasimama mbele ya bwana Tahid.
“Kumbe ni wewe mshenzi Bernadetha na mwanao! Nitawafunda adabu, nitawaonyesha nawaambia!”
Bernadetha akasogea mbele zaidi kumkuta Tahid. Akamuwasha kofi matata alafu akamuuliza:
“Utaninyoosha kama mume wangu?”
Tahid akaishia kutoa macho.
“Unadhani sijui kwamba ulihusika na kifo cha mume wangu? Unadhani sijui kwamba wewe ndiye ulikuwa unatoa taarifa za mdogo wako kwa maadui auwawe ili upate ujira na kujikomboa toka kwenye kazi uliyoidharau ya ualimu? Sio wewe uliyeshauri mdogo wako ahamishiwe Royal hospital kwa usalama? Sio wewe uliyekuwa karibu na Dokta Rajesh? Unadhani sikukuona wakati mnapongezana wakati mimi nalia na kusaga meno? Yote hayo ili upate hisa tu kwenye kiwanda cha nyama cha baradhuli Isaac? Mshenzi wewe!”
Bernadetha akamtandika kibao kingine bwana Tahid, tena na tena. Miraji akaja kumtoa na kumpeleka nje.
“Kwahiyo kulikuwa na haja gani kwa wakina Mtemvu kumuhonga dokta asiseme ukweli wakati dokta mwenyewe yupo upande wa Mr Kim?” Kaguta alimuuliza Vitalis.
“Dhamira ya bwana Kim ni kufanya na kutengeneza mazingira ya kisasi kwa mauaji ya wakina Mtemvu, watu wasijue kama ni yeye yupo nyuma ya huo mchezo. Lakini kiuhalisia yeye ndiye aliyekuwa anapanga na kufanya kila jambo.” Vitalis akajibu kisha akamfuata bwana Tahid.
“Sisi hatuhusiani na mambo yenu ya kifamilia, sisi tunamtaka Isaac Makongo. Tunajua wewe unaweza ukatupatia.”
“Mimi?”
“Ndio!”
“Kivipi?”
“Tunajua Isaack ni mshirika wako kibiashara. Ukimuhitaji, unampata.”
“Samahani, siwezi kufanya hivyo.”
Vitalis alinyoosha mkono wake kwa Kaguta, akapewa kamera. Aliifungua kamera akamuonyesha video bwana Tahid jinsi vijana wake walivyokiri maovu yake. Baada ya hapo, Vitalis akamuambia:
“Hii video itasambazwa kwenye vituo vya habari. Bado hutofanya tunayoyataka?”
Tahid kimya.
“Okay. Labda hilo halijakugusa. Umeona hii?” Vitalis akaonyesha picha kwenye kamera ikiwa inaonyesha bomu lililopandikizwa nyumbani kwa Tahid.
“Endapo tukibofya kitufe tu, nyumba yako yote pamoja na mke na watoto wako wataenda, hutopata hata majivu yao. Vipi hapo, bado?”
Uso wa Tahid ukanywea.
“Nitawasaidia. Lakini naomba msijeruhi familia yangu.”


***

☆Steve
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom