Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Maana ya baradhuli unaijua?
Baradhuli kwa kiswahili ni mwanaume mwenye Hiba ya kuwaingilia wanaume wenziwe
 
Daah Jumapili inakatika hii, huku bado Kaguta na Vitalis hawajakinukisha!
 
***SURA YA KUMI NA TANO***




(MSIMU WA 02)





“Mungu wangu Bakari mimi!”




Mvuvi aliweka mikono kichwani. Puh! Akajirushia kwenye maji na kuanza kupiga mbizi kuufuata mtumbwi wake. Ajabu, mtumbwi ukazidi kusogea kila ulipokaribiwa. Mwishowe Bakari akachoka, alitizama kisiwa akaona ndio sehemu pekee karibu kwake, akarudi haraka kwa mbizi na kuwakuta wakina inspekta bado wamesimama wakimsubiri.




“Bakari kwani kuna nini?” Inspekta alitaka kujua. Bakari hakujibu kitu, aliketi kitako machozi yakibisha hodi. Inspekta, Kaguta na Jombi wakamsogelea.
“Bakari, mbona unatuweka njia panda? … Unaweza ukatuambia nini kinaendelea?” Inspekta aliuliza huku akimshika bega Bakari.
“Najuta kuja hapa! Najuta! Najua nitakufa tu!”
“Kwanini ufe?”
“Hiki kisiwa kina majini! Unadhani kwanini wenzangu walikuwa hawataki kuja huku? … Masikini mie!”



Inspekta akatizamana na wenzake kwa macho dunguri.




“Mmesikia? Sasa tunafanyaje?” Inspekta aliuliza.
“Tuondokeni tu!” Jombi alijibu bila ya kufikiria kwamba hakuna usafiri.
“Tunaondokea na nini?” Kaguta aliuliza. “Kama tumeamua kuja hapa, tufanye kilichotuleta.”
“Wewe huogopi?” Jombi aliuliza.
“Hata kama naogopa itasaidia nini tena na tushafika hapa na mtumbwi umekwisha kwenda?”
“Si tunaomba msaada wa kuokolewa?”
“Hatokuja mtu yeyote hapa!” Bakari akadakia, “hakuna mvuvi anayesogelea hiki kisiwa.”
“Kwahiyo? … Tutakaa hapa hapa ama tutajaribu kufanya jambo?” Kaguta alishawishi. Kwa muda wa dakika moja watu wakawa kimya, inspekta ndiye akalonga kwa kujiamini;
“Twendeni. Tusiruhusu Imani zitukate maini.”
Jombi, Kaguta na inspekta wakashika njia kuelekea ndani wakifuata kabarabara kadogo. Bakari yeye akakataa kwenda.
“Nyie nendeni, mie nitabaki mwenyewe hapa!”




Alipoona wenzake wanaishia alinyanyuka akawakimbilia.



“Yani ndo’ mnaniacha kweli nibaki mwenyewe!”
“Si umetaka?” Kaguta alimjibu.
“Sasa nikiwaelekeza mtaniongezea pesa?”
“Unapajua?” Inspekta aliuliza.
“Ndio, napajua. Mtaniongezea pesa?”
“Ndio. Tupeleke huko.”




Bakari akachukua nafasi na kujiweka mbele ya wote. Aliongoza njia wakipanda na kushuka. Baada ya dakika kumi na mbili, upepo ulipuliza kwa ukali wakadondoshwa chini na kuanza kubiringishwa. Wakajitahidi kujishkiza kwenye miti na kung’ang’ania vichaka lakini upepo ukaonekana na nguvu mno kwani ulizidi kuwaburuza ukiwapeleka upande wa magharibi. Kwa muda wa dakika mbili upepo ukavuma. Ulipokoma, kila mtu alikuwa mwenyewe asimuone mwenzake. Kila mtu alikuwa amepeperushwa pande yake.





Inspekta alipepesa macho yake kushoto na kulia, juu na chini hola! Hakujua hata aelekee wapi. Alikuwa katikati ya msitu wenye nyasi na miti mirefu.Alivuta na kushusha pumzi ndefu, akaita;




“Kagutaaaaa!” mara mbili lakini hakukuwa na majibu. Ghafla, akasikia vishindo vya miguu nyuma yake, kugeuka akakutana na jitu nene mwenye mwili wa mti! Macho yake yalikuwa makubwa kama ngumi ya mtu mzima. Mikono ilikuwa minene yenye kiganja kikubwa. Miguu ilikuwa mifupi minene yenye nyayo pana. Mdomo wake ulikuwa mkubwa kama beseni.





Inspekata akatoa macho kwa mshangao. Taratibu akaanza kurudi nyuma huku akimtizama jitu mti.




“Unadhani unaenda wapi?”
“Wewe ni nani?”
“Huna haja ya kunijua maana muda si mwiingi utakuwa mfu!”
“Nimekuja kuonana na Alwatan!”
“Una mualiko?”
“Hapana!”
“Wewe ni mvamizi!”




Baada tu ya hiyo kauli, jitu mti lilianza kumkimbiza inspekta kwa kasi. Inspekta alikimbia kuokoa maisha yake. Alikunja kunja kona huku akaenda kule, kule akaenda huku. Ila baada ya muda, alikamatwa akaning’inizwa juu chini.





“Nadhani leo utakuwa kifungua kinywa changu!”





Alisema jitu mti kisha akaanza kumpeleka inspekta mdomoni. Upesi inspekta akatoa bunduki yake kiunoni akafyatua macho yote mawili ya jitu mti. Jitu likamuachia inspekta huku likilalamika kwa maumivu. Inspekta akaanza kukimbia. Hamaki, jitu mti nalo likaendelea kumkimbiza inspekta likifuatisha sauti ya vishindo. Kila inspekta alipokata kona, jitu hili hapa. Kila inspekta alipokanyaga, jitu likapita.





Baada ya kukimbia kwa dakika saba, inspekta akaona mto mkubwa mbele. Ulikuwa unapitisha maji kwa kasi mno. Aliinama akaokota mawe matatu makubwa akaendelea kukimbia. Alipofika kwenye kingo ya mto alisimama na kusonga kando akarusha mawe yale matatu majini. Jitu likapitiliza kufuata vishindo vya mawe. Kama unyoya maji yakambeba na kumpoteza. Inspekta akashusha pumzi. Akarusha macho yake kuangaza mandhari ya kisiwa kwa uso wa kuduwaa. Akaona miti ya kijani isiyoonyesha dalili za ukomo. Alitikisa kichwa akatizama alipotokea. Aliita tena;





“Kagutaaa!” kwa sauti ya juu lakini hakusikia kitu. Alichuchumaa akakinga maji na kiganja chake akanawa uso. Akakinga tena na kunywa, ptuuuh! Akatema.
“Chumvi. Shit!” Alilaani.
“Ila huu mto unatoka wapi?” Alijiuliza huku akijitahidi kuangaza maji yanapotokea.
“Mbona hiki kisiwa kinaonekana kikubwa mno na nilikiona kidogo?” Aliendelea kujiuliza maswali ambayo hakuyapatia majibu.
“Wakina Kaguta watakuwa wapi? Na sasa naelekea wapi?”
Haikusaidia jambo, alibakia amesimama kama mnara. Mbali yake kabisa ndipo alipokuwepo Kaguta naye akibung’aa bung’aa na akihangaika kuita jina la mwenzake bila ya majibu. Hata pale alipobadili na kuita jina la Jombi ama Bakari majibu yalikuwa yale yale, kimya. Wakati anatembea kwa mbali kidogo upande wa kushoto, Kaguta aliona mti wa machenza. Aliusogelea akachuma moja na kuanza kulimenya apate kula.





Ghafla sauti inasikika;
“Nani kakuruhusu?” Kaguta akashtuka. Akatizama nyuma asione kitu. Akatizama pembeni asione kitu.




“Nani kakuruhusu uchume?” Sauti ya kuuliza ikajirudia.




Kaguta akadondosha chenza na kuanza kusogea taratibu kurudi nyuma huku akiutizama mti wa mchenza kama vile amesikia sauti ikitokea hapo. Hatua ya kwanza nyuma, ya pili, tatu, nne, mti wa mchenza ukaanza kunyanyuka! Mizizi yake ikachipuka kwa kasi!


Kaguta aligeuka akaanza kukimbia. Hakufika mbali, mzizi ulikamata kiatu chake na kumburuza kuelekea kweye mti. Kaguta akanyanyua jiwe, akapiga mzizi uliomkamata bila ya mafanikio. Akazidi tu kusogezwa kuufuata mti.



Haraka, akili ikamjia. Alifungua kamba za kiatu, mzizi ukaenda na kiatu. Alinyanyuka akakimbia kwa kasi, nyuma yake mizizi ikimkimbiza. Alipoona inamkaribia, alikunja kona akauzunguka mti mmoja mkubwa mara nne mizizi ikajiviringitia hapo na kukoma. Kaguta akatabasamu.




“Shenzi!”


****


☆Steve
 
***SURA YA KUMI NA SITA***






(MSIMU WA 02)







Mara ghafla, mzizi mmoja ukamfuata kwa kasi toka kwenye mti wa mchenza na kumchapa kwanguvu mgongoni. Ile anaugulia maumivu, mzizi ule ukamdaka mguu wake maeneo ya gotini na kuanza kumvuta kwa kasi kuufuata mti wa mchenza. Wakati Kaguta anaburuzwa kuufuata mti wa mchenza, alidaka shina la mti mmoja akaung’ang’ania. Huku mzizi ukivuta mguu kwanguvu, naye aling’ang’ania shina kwanguvu asitake kuachia hata kidogo.





Kadiri muda ulivyokuwa unaenda, Kaguta alianza kupoteza uvumilivu. Mzizi ulimvuta kwanguvu dhidi ya mikono yake. Aling’ata meno kwa uchungu. Alirusha macho yake pembezoni kutafuta pembejeo ya kujiokolea akaishia tu kuona mawe ya mduara yasiyo hata na ncha. Akili yake ikakokotoa. Aliacha kushika shina la mti akakwapua mawe yale mawili. Huku akivutwa kuelekea kwenye mti, aligongesha yale mawe kwanguvu yakapasuana na kutengeneza ncha. Akanyanyua mkono wake kwanguvu na kuukata mzizi.






Alipofanikiwa alijinyanyua akakimbia toka eneo lile. Alifika mbali akautizama ule mchenza kwa macho ya kuduwaa. Akastaajabu mizizi ikiwa inajirudisha chini ya ardhi na mazingira yakarudi vile vile kama yalivyokuwa hapo mwanzoni. Chenza alilolidondosha akiwa kalimenya kidogo, lilirudisha ganda lake na kurudi mtini! Mdomo wa Kaguta ukaachama. Haraka akakimbia toka eneo lile akielekea mbele kwa mbele.




Nyuma ya Kaguta kilomita kede, alikuwapo Jombi macho yake yakiangaza kutafuta njia, miguu yake ikipambana na nyasi ndefu na vichaka ambavyo vilikuwa vinamzonga mara kwa mara. Masikio yake hayakuwa yanasikia kitu chochote isipokuwa milio ya ndege tena kwa mbali ikitokea kwenye viota vilivyoketi kwenye matawi ya miti mirefu. Kwa taratibu, alitembea. Muda mwingine alisimama na kutambaza macho yake kila pande. Mkononi mwake alikuwa kashikilia gongo kubwa alilokuwa analitumia kutawanyia majani na vichaka apate kupita kwa ahueni.






“Watakuwa wapo pande gani hawa?” Jombi alisimama akashika kiuno. Ni kama vile alichoka kutembea.






Alifuta jasho kwenye uso wake na kuvuta pumzi kadhaa. Alipotizama pembeni mita kadhaa akaona jambo. Alisogea vizuri kushuhudia akaona nyayo kubwa juu ya udongo. Alichuchumaa akaitizama vizuri ile nyayo. Aliingiza mguu wake kwenye ile nyayo ukazama wote. Akajiuliza;






“Huu mguu wa nani?” Huku akitizama alama za madole yale manene. Alinyanyuka akarusha macho yake kufuatilia nyayo zile akaona zaelekea mbali upande wake wa magharibi. Akataka kuzifuatilia ila akasita. Akabakia akitizama kwa uso wenye maswali mchanganyiko wa mashaka na hofu.







Akiwa hapo bado hajaelewa cha kufanya, ghafla vuuup! Akanyanyuliwa na ndege mkubwa mithili ya popo! Alikuwa ni mweusi ti mwenye mdomo mrefu kama chuchunge. Mabawa yake yalikuwa mapana na yenye nguvu ingali macho yake yakiwa mekundu yenye mfumo wa paka.





Jombi alifurukuta lakini hakufua dafu kwenye kucha za miguu ya yule ndege wa ajabu. Kucha mbili zilikuwa zimekamata bega lake kwa kupenya. Kucha zingine zilikuwa zimekamata shati kwa nguvu. Sasa alikuwa juu ya msitu, hata ile miti aliyokuwa anaiona ni mirefu akaiona mifupi kutokana na kimo alichopelekwa na yule ndege. Kila alipotizama chini aliishia kufunga macho kwa woga, hata mapigo yake ya moyo yalilipuka. Akaogopa hata kufurukuta kwa kuhofia akidondoshwa itakuwaje.





Vuup! Vuup! Vuuup! Vuup! Mabawa ya yule ndege yalitoa mlio huku yakizalisha pepo kali. Uso wa Jombi ulijawa na hofu, hata hema yake ilikuwa ni dhahiri ya woga. Alitizama kila pande lakini hakuona mwisho wala mwanzo wa kisiwa. Alitizama chini, napo hakuona hata wenzake. Ila kwa chini, juu ya ardhi, Kaguta alimuona ndege huyo kwa mbali angani akiwa amebebelea mtu. Bila kupoteza wasaa akaanza kukimbia akimfuatisha ndege yule aelekeapo.






Huko juu kwa mbali, Jombi akaona mto mkubwa. Aliutizama ule mto uso wake ukionyesha kama mtu awazaye jambo. Na kweli, ndege alipokaribia mto, Jombi aliushika miguu ya yule ndege kwanguvu akaanza kuhangaika kwa nguvu zake zote akienda huku na huko. Ndege akayumba yumba mwishowe ashati la Jombi likachanika na kumuacha ndege yule wa ajabu akiwa amembebelea Jombi kwa mguu mmoja tu, wa kulia. Hapo Jombi akageuza shingo akiyavumilia maumivu, akang’ata mguu wa yule ndege kwanguvu, ndege akamuachia. Huyooo Jombi akaanza kushuka chini akielekea kwenye mto.




Puuuv!






Sauti ya maji ikasikika wakati Jombi akitua. Alipopanda tu juu ya maji, kwa fujo maji yakaanza kumburuta kumpeleka asipokujua. Wakati anahangaikia uhai wake kwa kupiga mbizi akamuona Kaguta kwenye kingo ya mto akikimbia naye sambamba.





“Jisukumie huku! Jisukumie hukuu!”




Kaguta alielekeza huku akionyeshea nchi kavu. Jombi akaanza kujisukuma taratibu huku akikinzana na maji yaendayo kwa kasi. Kaguta akarukia tawi refu la mti akalivunja, akawa anakimbia nalo. Jombi aliposogea karibu naye alielekezea ule mti mtoni ili Jombi audake. Mara puuh! Akajikwaa na kudondoka chini. Bahati jema mti hakuuachia, ila sasa Jombi akawa amemuacha kwa umbali mrefu hatua kama ishirini za mtu mzima. Alinyanyuka akaendelea kukimbia akiongeza kasi zaidi na mti wake ulio mkononi.






Baada ya muda alimfikia tena Jombi. Alisogeza mti wake kwa muhusika, Jombi akaukamata. Lakini sasa Kaguta hakuwa na nguvu za kutosha, labda alikuwa amechoshwa na purukushani alizozipitia. Alimvuta Jombi lakini nguvu ya maji ikamshinda.





Mungu si athumani! Mbele yao wakamuona inspekta. Kaguta alipaza sauti kumjulisha inspekta ujio na uhitaji wao wa kusaidiwa. Inspekta akajiweka tayari. Alimkata kwa nguvu Kaguta wakamvutia Jombi nje.





Wakiwa wanahema hata hawajaulizana nini cha kujifanya na wapi walipotokea, walisikia vishindo vikuu nyuma yao. Walipogeuza shingo wakastaajabu. Waliona mbwa mwitu wanne wenye rangi ya fedha, mgongoni wakiwa na rangi nyeusi. Miili yao ilikuwa mikubwa kuliko mbwa mwitu wa kawaida. Ndimi zao zilikuwa zimetoka nje zikichuruza mate. Jombi akasema huku akitetemeka;





“Jamani … Jamani twafa!”






Wakatizamana kwa hofu. Inspekta akapayuka; “Turukie majini!” Kabla wenzake hawajajibu, alikuwa tayari asharukia majini. Jombi na Kaguta nao wakafuatia. Mbwa mwitu wakapiga kelele kali za malalamiko kwa kukosa kitoweo. Lakini kama vile haitoshi, walianza kuwafukuza wakina inspekta pembezoni mwa mto wakienda nao sambamba kwa kasi kubwa.






Baada ya muda wa dakika ishirini, mbwa mwitu wakachoka. Wakasimama na kuwatazama wakina inspekta wakizidi kupelekwa na maji yasiyoonekana kikomo kwa macho. Dakika kumi tokea hapo, mto ulifikia kwenye maporomoko yake makuu, inspekta na wenzake wakamiminwa kwa nguvu. Na kutokana na maji kupunguza kasi, wakaogelea kwenda nchi kavu na kujipumzisha wakiwa wamechoka mno, wanahema kwanguvu kama wametoka mbioni.




Pumzi kadhaa zilipovutwa, wakaanza kuteta;
“Bakari yupo wapi?” Kaguta aliuliza.
“Sijui yupo upande upi wa kisiwa, na sijui kama atakuwa mzima huko.” Inspekta alieleza.
“Tangu upepo ule ulivyopuliza na kunipeleka nisipopajua, sijamuona tena Bakari.” Jombi naye akapata kusema.
“Sasa, tunaelekea wapi? Maana sijui hata hapa tulipo.”Kaguta aliuliza huku akiangaza angaza macho.
“Tuifuate ile njia!” Inspekta akaonyeshea njia fulani nyembamba aliyoiona kwa juu kidogo. “Hamna anayejua tulipo, tuifuate ile njia tuone itatupeleka wapi!”



Walikubaliana wakanyanyuka na kuifuata njia elekezi. Taratibu wakaanza kuifuatisha ikiingia ndani ya msitu.Sauti za ndege zilikuwa zinapaza huku na kule, milio mingine ikiwa ya ajabu na migeni. Zilipotimia dakika nane wanaume hao watatu wakiwa wanatembea kwenye ile njia nyembamba, ghafla mawingu yakaanza kufunga anga na punde tu giza likawa limetawala. Wakina inspekta wakapigwa na duwaa. Giza limeingiaje ghafla vile?Wakiwa katika hilo duwazo, ghafla mwanga mkali kama wa gari ukawamulika usoni na kuwafanya vipofu kwa muda wasione chochote. Hapo sauti nzito ambayo haikujulikana wapi inatokea ikawauliza;
“Mnafanya nini katika hiki kisiwa?”




***

☆Steve
 
***SURA YA KUMI NA SABA***





(MSIMU WA 02)





Inspekta, huku akiwa amekinga uso wake dhidi ya mwanga mkali ummulikao, akajibu;
“Tumekuja kuonana na Mzee Kombo!”
“Mna miadi naye?”
“Hapana!”
“Basi nyie ni wavamizi. Je, hamkupata kusikia yale yaongelewayo kuhusu hii mahali?”
“Tumesikia ila tuna shida?”
“Shida isiyo ambatana na miadi kwetu ni ukaidi. Poteeni kwenye hiki kisiwa. Tafuteni njia mtokomee la sivyo kila baada ya dakika kumi na tatu, mtapata jaribu mpaka pale mtakapokwisha kabisa!”
“Basi tunaomba utuonyeshe njia!” Jombi akasema huku akitizama chini, uso wake ameukunja na kauziba na kiganja.
“Kama mlivyokuja, ndivyo mtakavyotoka. Hamkupewa mualiko kuingia na hamtosindikizwa mkitoka. Kumbuka, ni kila baada ya dakika kumi na tatu, hesabu tokea sasa!”



Paap! Mwanga ukapotea. Taratibu mawingu yakaanza kufunguka na kukawa mchana kama awali. Inspekta akanyanyua mkono wake wa kushoto kutizama saa, akaona ni saa nane na nusu. Akawaambia wenzake hayo majira.




“Sasa tunafanyaje? Tunatokea wapi?” Jombi aliuliza.
“Mi nadhani tutumie akili zetu tu.” Inspekta alipendekeza, “mi ninavyojua, mto huwa unamwagia maji baharini. Tuufuatishe mto huu mpaka pale unapomwagia maji yake.”



Kaguta na Jombi wakaafiki. Hao wakaungana na inspekta kuanza kufuatilia maji ya mto yaendako. Huku wakiruka viunzi kama mawe na mabanzi ya miti wakasonga. Baada ya dakika kadhaa, saa ya mkononi ya inspekta ikapiga alarm … ti! ti! Inspekta akaitizama. Akaona sasa ni saa nane na dakika arobaini na tatu. Kabla hajafungua mdomo kulonga lolote, Jombi alipaza sauti huku akionyeshea upande wa pili wa mto;
“Bakari! Bakari yulee!”







Inspekta na Kaguta wakatizama upesi. Wakaona mwili wa mtu ukiwa umejilaza pembezoni mwa mto, nguo na hata umbo likiwa la Bakari.






“Atakuwa amekufa nini?” Kaguta aliuliza.
“Labda. Twendeni tukamtizame, hatuwezi tukamtelekeza.” Jombi alitoa wazo. Haoo, yeye na Kaguta wakaanza kuongozana wakiruka juu ya mawe waende upande wa pili. Inspekta yeye akasita. Jombi na Kaguta walipovuka mto, wakamtizama.
“Njoo bana! Kumbuka huyu jamaa alijitolea kutuleta hapa!” Kaguta alieleza. Inspekta akaamua avuke na kuungana nao wakausogelea mwili wa Bakari uliokuwa umelala kifudifudi.
“Kuna kitu kitakuwa kimemkuta.” Jombi alisema kwa uhakika. Alichuchumaa akataka kumgeuza Bakari alale chali. Upesi, inspekta akamkataza kufanya hilo baada ya kuona kucha ndefu kwenye vidole wa Bakari. Kufumba na kufumbua, Bakari akaamka na kumkwaruza Jombi kifuani! Macho yake yalikuwa mekundu mno kama bendera, meno yake yalikuwa kama ya popo na kuchaze zikiwa ndefu mno. Jombi akasogea haraka huku akimtizama Bakari wa ajabu.






“Bakari, vipi?” Jombi alitahamaki. Kifua chake kilikuwa kinachuruza damu toka kwenye mikwaruzo.
“Huyo si Bakari!” Inspekta aling’aka. “Hilo ni jaribu, dakika ya kumi na tatu imeshatimia.”





Kauli hiyo ilipokoma, Bakari wa ajabu akamrukia inspekta na kwenda naye chini. Bakari yule wa ajabu akanyanyua mkono wake wa kuume amrarue inspekta, Inspekta akauzuia mkono huo na kumtupa Bakari mbali kwa teke. Bakari akanyanyuka haraka, ila kabla hajamrukia tena inspekta, Kaguta akakabiliana naye kwa kwa kumrushia teke, Bakari akalidaka na kumtupia Kaguta pembeni kama karatasi. Jombi akasogea na kurusha ngumi, Bakari akadaka mkono na kuuviringita kisha akampa teke matata Jombi, Jombi akarukia kando.





Inspekta aliokota gongo akalirusha kwa Bakari wa ajabu, Bakari akalidaka. Inspekta akarusha teke, nalo likadakwa kisha Bakari akafunguka kumpa teke la kifua inspekta,inspekta akarushwa kando! Haraka Kaguta alinyanyuka akamsogelea Bakari wa ajabu, Jombi naye akajongea, wakamuweka Bakari kati. Kaguta alirusha ngumi, Bakari akakwepa. Jombi alirusha teke, Bakari akainama kisha ghafla akaruka na kujizungusha hewani akifungua miguu yake ambayo iliwanasiibu vizuri Kaguta na Jombi kwenye mapaji yao ya uso, wakadondokea kando!





Upesi inspekta akanyanyuka na kumrudia Bakari. Alirusha ngumi yake ya kulia, Bakari akaipangua. Alirusha ngumi yake ya kushoto, Bakari akaitoa. Alirusha tena ya kulia, Bakari akaidaka na kumzungusha inspekta kama mtu achezaye blues kisha akamtupia huko kwa teke kali. Sasa wanaume wote watatu; Kaguta, inspekta na Jombi wakawa wapo chini wakigugumia maumivu.





Bakari wa ajabu akacheka sana. Kisha akauliza kwa kebehi;
“Hiko ndicho mlicho nacho?”





Kaguta akakunja sura kwa hasira. Akataka kunyanyuka ila inspekta akamshika mkono na kumuambia;
“Hiyo si suluhishi. Kwa mmoja mmoja hatutoweza, twende kwa pamoja ila kwa akili nguvu na zaidi.”





Kaguta akatikisa kichwa kukubali. Wakanyanyuka na kumfuata Bakari wa ajabu, inspekta akakaa kwa mbele, Kaguta akakaa nyuma yake. Inspekta akatishia kurusha ngumi, Bakari akasogea kidogo. Inspekta akanyanyua mguu wake wa kushoto akitishia kurusha teke, Bakari akajiandaa kulipokea, haraka inspekta akabadili maamuzi, aliruka juu akiwa amekunja goti lake kumshambulia Bakari, Bakari akawahi kujikinga kichwa, na hapo ndipo Kaguta akatelezesha mguu wake kumkata mtama Bakari. Wakati Bakari anaanguka alifungua mikono yake iliyokuwa imemkinga kichwa, huo ukawa upenyo kwa inspekta akampatia goti la meno na kumvujisha damu.






“Pumbavu!” Bakari aling’aka baada ya kutema damu pembeni. Aliwatizama wakina inspekta akawaona wamejipanga vile vile, inspekta mbele Kaguta nyuma. Alipotizama kando, akamuona Jombi, alikuwa ameketi kitako kama mtu atizamaye sinema.





Bakari akaguna huku akibinua mdomowe. Haraka akatumia mikono yake kujifyatua na kusimama. Akakunja ngumi na kuwapa ishara wakina inspekta washambulie. Inspekta bila kulaza damu akakunja goti na kurusha teke, Baraka akalidaka, ila kabla hajafanya lolote na mguu alioudaka, Inspekta akautumia huo mguu kujinyanyulia juu na kurusha teke lingine lililombamiza Bakari usoni na kumpeleka chini. Baraka akanyanyuka tena kwa hasira, alirusha ngumi inspekta akaikwepa Kaguta akaidaka.






Alipotaka kunyanyua mguu arushe teke, inspekta akazuia mguu kisha akampiga Bakari ngumi ya tumbo, wakati Bakari wa ajabu akiguguma na maumivu ya tumbo, mkono wake uliorusha ngumi ulivutwa na Kaguta kisha akapewa ngumi kubwa ya uso akadondokea mti, ukampenya kifuani na kutokea mbele, huo ukawa mwisho wa Bakari wa ajabu.





Inspekta, Kaguta na Jombi wakapongezana. Inspekta akatizama saa yake ya mkononi akaona ni saa nane na dakika hamsini na tatu. Zilisalia dakika tatu tu kutimia dakika kumi na tatu ya pili. Inspekta akawashika wenzake mkono na kuwavuta.






“Tuna dakika tatu tu kabla ya jaribu lingine kuja!”





Kama upepo wakaanza kukimbia kwa haraka mno kuufuata mto. Baada ya muda kidogo, mto ulikata kona wakina inspekta wakashangaa kuona shimo kubwa mno mbele yao. Ndani ya shimo hilo kubwa, ndipo maji yote ya mto yakawa yanamiminikia humo.






“Duh! Sasa tunafanyaje?” Inspekta akauliza huku akihema. Kaguta akainama akashika magoti yake. Jombi akashika kiuno huku akitota jasho. Hawakusema kitu chochote zaidi ya kujitahidi kuvuta pumzi walizoziteketeza mbioni. Ila zoezi lao hilo kabla halijakamilika, lilikatishwa na mlio wa saa ya inspekta. Ilikuwa ni saa nane na dakika hamsini na sita! Inspekta aliwaambia wenzake wakaanza kupepesa macho yao pande zote nane za dunia.





Ajabu hawakuona kitu. Ila baada ya sekunde kadhaa, kwa mbali upande wa kusini wakaanza kushuhudia tukio la ajabu. Miti ilikuwa inadondoka kwa kasi. Ndege walikuwa wanaruka na kukimbia ila hakikuonekana ni kitu gani chafanya hayo!Hapo, inspekta akashauri warukie shimoni mule maji ya mto yaendako. Kaguta na Jombi wakachungulia shimo wasipate kuona kikomo chake. Kidogo wakatia ashki.






“Hakuna njia nyingine, guys. Mmekiona hiko kinachokuja?” Inspekta alionyeshea kidole anapopaongelea.
“Ila unajuaje kama humo shimoni ni salama kuliko hiko kijacho?” Jombi aliuliza.
“Ukiona maji yanaingia mahali, ujue kuna sehemu yanatokea. Simple geography.” Inspekta alisema lakini muda huu hakungoja tena maswali, alishika mikono ya Kaguta na Jombi akajirushia shimoni. Walikuwa hewani kwa takribani dakika tano kabla hawajafika chini walipozama na kuibukia baharini. Walipotizama nyuma yao, wakakiona kisiwa kwa mbaali, kikiwa na udogo wake ule ule.





Walivuka mtihani. Ila sasa tabu ikawa je, watafikaje nchi kavu na hawana chombo chochote? Waliulizana pasipo kupata majibu. Bahati jema, kwa mbali kidogo inspekta akaona mtumbwi wa Bakari. Wakaufuata na kupanda. Huku wakitumia mikono yao kama mapakuo ya maji, wakasogea taratibu taratibu mpaka wakafika nchi kavu.Waliposhuka tu, wavuvi wakawazingira.





“Mwenzetu yupo wapi?”






Inspekta akatizamana na wenzie. Hakuna aliyejibu, wote walitoa tu macho. Wavuvi wakarudia swali;
“Bakari yupo wapi, au mmeshamtoa kafara?”
“Hapana. Kusema ukweli hatujui alipo.” Inspekta alijbu.
“Hamjui alipo? Si mmeondoka naye hapa!” Mvuvi mmoja aliuliza kwa jazba.
“Ndio, tumeondoka naye. Lakini tulipofika kule kisiwani akatupotea. Hatujajua atakuwa wapi.” Kaguta alieleleza. Wavuvi wakatizamana, mvuvi mmoja akawaonyeshea ishara wenzie kwa kupandisha nyusi moja, ghafla wavuvi wakawavamia wakina inspekta na kuanza kuparangana.






Bahati mbaya hawakufua dafu, wakagaragazwa na kufanywa mahututi kwa mateke na ngumi za haja. Inspekta akawaomba radhi kwa usumbufu kisha akashika njia yeye na wenzake waondoke zao. Walipopiga hatua sita mbele, sauti ikawafikia;
“Majambaaaziii!”




****

☆Steve
 
Kasome wewe mimi, ndio mswahili, na ukipata maana nyingine ya hii nilio kupa, mtunzi wa kamusi yako hajui kiswahili
 
Kasome wewe mimi, ndio mswahili, na ukipata maana nyingine ya hii nilio kupa, mtunzi wa kamusi yako hajui kiswahili
Kwahiyo wewe wajua kiswahili kuliko BAKITA au? Usidhani kila mtu anakurupuka mzee.
 
Molel, achana na kujiamini na viswahili vya mitaani, kama unabishia nenda BAKITA ukawaulize maana ya BARADHULI wata kupa jibu.
na bila shaka kwa kiswahili chako cha mitaani MCHIZI WANGU, unaweza ukaitafsiri RAFIKI YANGU kumbe maana halisi ni MWENDAWAZIMU WANGU
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom