Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

****SURA YA NNE****

(MSIMU WA 02)







Pembezoni mwa bahari, upepo ukiwa unavuma kwa kasi, kulikuwa kumepakiwa magari mawili, prado nyeusi. Vioo vyake vilikuwa tinted, na wanaume watatu wenye miili mikubwa wakiwa wamevalia miwani meusi na nguo zinazobana misuli yao walikuwa wameegemea magari hayo, mikononi walikuwa na bunduki.




Baada ya muda kidogo, gari ndogo ya kijivu aina ya Toyota Altezza ilifika eneo hilo tulivu ambalo watu hawakuwapo zaidi tu ya wale wanaume watatu. Gari hilo liliposimama, kioo cha nyuma kilishuka akaonekana Jombi, alivalia miwani akiegemea kochi. Baada ya hapo, kioo kilipandishwa na kufunga. Sauti ya inspekta ikasikika tokea kwenye radio call waliyokuwa wamebebelea wanaume wale wa shoka.



“Nami naomba nione familia yangu.”




Mwanaume mmoja aliyekuwa na bunduki akaligonga gari kama ishara, kioo kikashushwa mke na mtoto wa inspekta wakaonekana. Walikuwa na sura zenye hofu. Sauti ya inspekta ikaendelea kusema;
“Nipo peke yangu, mpo watatu tena wenye silaha, mtanipaje uhakika na uhai wangu na wa familia yangu endapo nikiwapa mtu wenu?”




Mwanaume aliyeshikilia radio call akamjibu,




“Hatuna shida na wewe wala familia yako, tunamtaka mtu wetu tu.”
“Okay. Nitahesabu mpaka tatu, utaachia familia yangu, nami nitamuachia mtu wenu. Sawa?”
“Sawa!”
“Moja…mbili…tatu!”




Milango ya magari ikafunguka. Mke na mtoto wa inspekta wakatoka kuifuata Altezza, Jombi naye akatoka akawa anaifuata prado huku akitembea kwa shida kama vile mtu mwenye mpango wa kudondokea kwa mbele. Wakati wanapishana, Jombi alinong’ona akamuambia mke wa inspekta;
“Ukiingia tu ndani endesha, potea.”





Kwa kuwa mwendo wa Jombi ulikuwa ni wa kusua sua alikawia kidogo kuwasili. Alipowafikia tu wanaume wale mabaunsa, Altezza ikawashwa na kuanza kuondolewa. Hapo hapo Jombi akamkamata Baunsa aliyekuwa karibu naye akampiga na kiwiko usoni. Pale tu mabaunsa wengine waliponyanyua silaha zao, ghafla, milio ya bunduki ilisikika, kufumba na kufumbua wote wakawa chini! Punde mwanaume mmoja akiwa amebebelea bunduki, akatoka majini. Alipovua mask yake akaonekana ni inspekta akiwa anatabasamu huku akimtizama Jombi.





Loh! Mara naye yule mwanaume aliyekuwa na sura ya Jombi akajishika shingoni na kuvuta kwanguvu ngozi yake, sura ya Jombi ikabanduka kama nyoka ajivuae gamba. Kumbe alikuwa ni mwanaume mwingine, kwa jina alikuwa anaitwa Kaguta, almaarufu kama “The red bullet”.




“Kazi nzuri sana, broh!” Inspekta alimpongeza mwenzie kwa kumkumbatia. “Naona sasa umerudi rasmi kazini.”
“Ahsante, Vitalis. Nilimiss sana hizi mishe. Natumai utanipa sehemu mujarabu za kutumia ujuzi wangu niliojifunza.”
“Ha ha ha na huko Cuba wamekuharibu kweli. Usikonde kazi zipo nyingi sana. Kuna mlima mkubwa upo mbele yetu unasubiri kusogezwa.”
“Mlima tu. Hata kama ni kukausha bahari am jus ready! Sema nini, sasa ninachokimiss ni warembo wa Cuba. Nawakumbuka kweli!”
“Ha ha ha umeanza Kaguta! Utaacha lini mambo yako?”
“Bado kidogo tu. Wewe si umeoa bwana!”
“Wewe nani kakukataza kuoa? Si hutaki.”
“Najua siwezi kutulia na bucha moja japo nyama ile ile. Vipi, tusepe, au?”
“Ngoja kwanza kidogo.” Inspekta alisema kisha akafuata miili ya watu waliowashambulia na kuanza kuipekua mifukoni huku akikusanya silaha zao. Kwenye mwili wa mmoja akakuta kitambulisho cha mpiga kura, na kwenye miili ya wengine akatohoa simu za mkononi.
“Sasa tunaweza tukaondoka.” Inspekta alimwambia mwenzake wakapanda gari moja wapo la majambazi wakaondoka eneo lile. Wakiwa njiani wakatoa taarifa polisi, ndani ya muda finyu polisi wakiongozana na magari ya kubebea majeruhi walifika sehemu ilipofanyikia tukio.



Jua likazama.




Ndani ya bar pana iliyoezekwa na makuti makavu watu wakiwa wamefurika na meza zikiwa zimechafuka na vilevi, kwenye upande mmoja wa ndanikidogo, alikuwa ameketi Inspekta na Kaguta. Bia kadhaa zilikuwa zimejaa mezani kwao. Kaguta alikuwa akipiga tarumbeta kama wasemavyo wanywaji, akiweka mdomo wa chupa kinywani na kumiminia humo, kwa upande wa inspekta alikuwa anatumia glasi kubwa akiwa anaijazia bia humo pomoni.




“Kama nilivyokuambia ndugu yangu, stori nzimandio hiyo. Nategemea kesho ama kesho kutwa nianze kufuatilia kile kitambulisho labda kinaweza nisaidia kujua hiyo gang inapatikana wapi na ipo chini ya nani.”




“Nakutakia kazi njema. Utakapohitaji msaada wangu, usisite kun’taarifu.” Kaguta alitia neno likafuatiwa na mafundo kadhaa ya bia.“Ila mwanangu kwa jinsi ulivyonambia, inabidi uwe makini. Inaonyesha jamaa wako very well equipped.”
“Hilo kweli, wako vizuri. Wanazo hadi mashine za kutengenezea sura bandia, Fake the face make up!”
“Ila kama isingekuwa yule mama, tusingeweza kufanya ile make-up vizuri.”
“Mama Miraji?”
“Huyo huyo. Yuko vizuri sana.”
“Ni kweli. Msaada wake umetusaidia sana.”
“Namuonea huruma hana mwanaume wa kumliwaza, lazima atakuwa mpweke sana.”
“Nani kasema? Au mawazo yako tu?”
“Kwani hilo nalo mpaka lisemwe? Hujui wimbo wa Yvonne Chakachaka ‘Every woman needs a man?” Aliuliza Kaguta kisha akaanza kuimba wimbo huo kwa sauti akiigiza kama mtu anayetumbuiza jukwaani. Inspekta akamzuia.
“Acha bana, huoni watu wote wanatutizama?”
“Aaaah!...unaogopa watu?”
“Zishapanda kichwani eenh?”
“Waaapi…bado sana, yani hapa wala sisikii. Sijui ni juice hizi au bia? Pombe Cuba bwana.”
“Kila kitu Cuba. Khaa!”




Kaguta akacheka baada ya kusikia hiyo kauli. Waliendelea kupiga soga hapo bar, giza likizidi kuwa nene. Lakini kinyume na muda, kadiri ulivyokuwa unasonga watu wakawa bado wanafurika eneo hilo kustarehe. Pale saa ya inspekta iliposema ni saa nane ya usiku, ndipo mabwana hao wawili waliponyanyuka na kuacha bar nyuma ya migongo yao kwenda kupanda gari la Kaguta, Toyota Mark 2.




“Utaweza ku-drive kweli, Kaguta?”
“Kwanini nisiweze?”
“Ah-ah! Umekunywa sana bwana, lete ufunguo niendeshe.”
“Vitalis, nipo sawa. Mbona muoga sana wewe.”
“Nina familia ndugu yangu.”
“We twende, nimekuambia nakuua mie.”





Walipanda kwenye gari, Kaguta akawa dereva. Kabla ya kuondoka, inspekta alihakikisha kafunga mkanda kwa usalama wake. Gari liliondolewa kwa kasi likawekwa kwenye barabara ya lami, mwendo ukawa wa ku-overtake. Ndani mziki mkubwa ukitema sauti ya Samba Mapangala na kibao chake maridhawa ‘Dunia tunapita’.




.Wakiwa wapo barabarani tayari wameshaacha bar kwa maili zisizopungua tatu, kwa mbali kidogo mbele yao upande waliokuwemo walishuhudia lori lililobebelea mifuko ya saruji, lilikuwa linatembea kwa mwendo wa taratibu huku mara kwa mara taa zake nyekundu za nyuma zikiwa zinawaka. Inspekta alitizama lile lori kwa makini na kwa sura ya woga;




“Angalia usiparamie ilo lori ndugu yangu.” Alitoa nasaha. Kaguta huku akiwa ametabasamu, alipindisha tairi ghafula akahamia upande wake wa kushoto toka upande lilipo lori, kisha akaongeza kasi kwa malengo ya kuliweka nyuma lori lile ili arudi upande aliokuwemo, wa kulia.





Gari la Kaguta lilipofika katikati ya lori, ghafula lori lilianza kusogea upande wao kwa kasi. Kaguta alipiga honi kutahadharisha lakini ilikuwa kazi bure. Lori lilizidi kuja! Upesi Kaguta alipunguza mwendokasi, bahati mbaya ama nzuri akakwangua taa za nyuma za lori za upande wa kushoto.





“We mshenzi wewe! Pita basi mbwa wewe!” Kaguta aliwaka kama moto wa kifuu.





Lori lilizidi kuja upande wao, ila kabla halijakaa vizuri kwenye mstari wa barabara waliopo wakina inspekta, lilikunja kona kali kurudi lilipotokea. Hapo sasa shughuli ikawa kubwa. Wakati kichwa cha lori kikirudi upande wake, mkia wake ulifuata gari la wakina inspekta kwa kasi ukabamiza kwa ubapa … buuh! Gari likapoteza dira, kama tamthilia kwenye runinga, lilipinduka likabiringita mara tatu! Bumbum!…bumbum!..bumbum!




Lori lililofanya tendo likapunguza mwendo na kusimama. Walishuka wanaume watatu waliobebelea bunduki kubwa ‘SMG’ mikononi mwao, wakalifuata gari la wakina inspekta na kuanza kulimiminia risasi za haja.





Tu!-tu!-tu!-tu!-tu!-tu!-tu!-tu!-tu!-tu!-tu!-tu!-tu!




Gari likawa nyambu nyambu kwa matundu, baada tu ya dakika moja likalipuka boooom! Moto mkubwa ukalitekeza ndani ya muda mchache. Wanaume wale baada ya kushuhudia hayo, walipeana tano za kupongezana kisha wakalirejea lori lao. Walipolifikia, mmoja wao alidanda akitaka kufungua mlango. Mara puh! Mlango ulisukumwa kwanguvu na teke kali tokea ndani ukawasomba na kuwaangusha wanaume wawili waliotoka kushambulia. Papo kwa papo, mwanaume mmoja akatoka kwenye lori kwa kasi akiruka kama ngedere akamvamia mwanaume aliyebakia amesimama kwa teke kali la kifuana kwenda naye mpaka chini akampokonya bunduki.





Hamaki, yule mwanaume alikuwa ni Kaguta! Wanaume wale wawili waliodondoshwa na mlangowalijikusanya na kushikilia bunduki wakiwa huko huko chini wakamnyooshea Kaguta. Katika hali ya wepesi, Kaguta alimgeuza mwanaume aliyedondokea naye chini akajiziba naye. Risasi zikamkosa wakati zikimiminika kwa mtu aliyemfanya ngao yake.





Haikuchukua muda sana, risasi zikakata, ni wazi nyingi ziliishia kwenye kulipua gari. Hapo ndio Kaguta kwa nguvu zake zote akamrusha mwanaume aliyemtumia kama ngao ya risasi kwa wenzake. Wenzake wakafanya kosa kwa kumtizama na kufungua mikono yao kumdaka mwenzao aliyerushwa, Kaguta akatumia mwanya huo mujarabu, haraka aliubeba mwili wake na mikono akaruhusu miguu yake iambae na kuwabetua wanaume wale wawili waliokuwa wamempokea mwenzao, kisha akawaweka chini ya ulinzi.




“Tulia hapo hapo. Sogeza hata kope muone!” Kaguta alitoa tisho kwa macho makali mithili ya mbwa mkali aliye mawindoni. Alipiga mluzi, mlango wa lori ukafunguliwa akatoka inspekta.



“Umemaliza?”
“Yap! Kazi ndogo sana hii?”
“Sasa tutatumia gari gani na wameshalipua letu?”
“Tutatumia lori lao. Tutafanyaje sasa?”




Inspekta alisogea vizuri akaanza kuwapekuwa wale wanaume, ambao ni wawili kati yao ndio walikuwa wazima. Mmoja alikuwa kitambo ameshafariki.





“Kwahiyo mlikuwa mnatufatilia, sio?” Aliuliza Kaguta kwa sauti kali.
“Ndio.”




“Hongereni sana. Bahati mbaya hamtokuwa na second chanceningewaelekeza kazi kama zile mnafanyaje.” Kaguta alimwaga maneno.“Ila labda mnaweza pata nafasi nyingine, ya Mungu mengi. Siku nyingine mkiwa mnataka kupindua gari hakikisheni mnaotaka kuwapindua wapo ndani ya gari. Nilikwangua taa za nyuma za gari lenu, ila hamkujali. Giza lililokuwepo lilitufanya sisi kuhamia kwenye trela bila nyie kufahamu. Mkapindua gari na kwenda kuliteketeza bila kuhakikisha tena kama kuna watu, kosa la pili. Kosa la tatu, hamkumuacha mtu kwenye lori. Poleni.” Alihitimisha Kaguta.





****

☆ Steve
 
***SURA YA TANO****

(MSIMU WA 02)







Waliwachukua wale wanaume wakawafunga kwa kutumia mashati na kuwatupia ndani ya lori kwa nyuma wakapeleka maiti mochwari na wengineo wakapelekwa eneo lililopo nje kidogo ya mji kwenye jengo fulani kubwa lililokuwa limemaliziwa nusu. Hapo wakawafungia wanaume wale wawili kwenye nguzo na kuondoka, wakawarudia kesho asubuhi na kuwakurupua kwa ndoo za maji.




“Habari za asubuhi?” Aliuliza inspekta kwa sauti ya mzaha. Kaguta alikuwa amekaa kwa mbali kidogo akivuta sigara na kupulizia moshi juu.




“Sasa tusipotezeane muda. Kuna maswali mawili matatu tu nataka kuyapatia majibu kutoka kwenu. Na natumai mtaonyesha ushirikiano bila kushurutishwa.” Alisema inspekta kisha akaweka kituo kidogo apate kumeza mate.




“Nani aliyewatuma na kawatuma kwa malengo gani?” Swali lilirushwa kwa watuhumiwa. Wanaume wale wawili kabla ya kusema lolote walitizamana kisha wakatabasamu, mmoja akajibu;
“Usipoteze muda wako, inspekta Vitalis Byabata. Hatutosema lolote, tuue tu.”
Inspekta akatabasamu na kutikisa kichwa. “Siwezi kuwaua. Ila mtakachokipitia, ni kheri ya kifo.”




Baada ya kusema hayo, inspekta alimtizama Kaguta na kumuelekezea wale watu kwa kichwa. Kaguta akadondosha sigara yake na kuisinya, kisha akawasogelea wanaume wale wawili na kuanza kuwasambazia kipigo kikali.Watuhumiwa wakavujishwa na kumiminwa damu. Walikua nyang’anyang’a kwa kipigo lakini bado hawakutereresha msimamo wao ‘Hatutosema kitu’. Mwishowe Kaguta alichoka. Hata pale inspekta alipompokea, hakufanikiwa, mambo yalikuwa ni yale yale mpaka watuhumiwa wakapoteza fahamu.






“Tuondoke. Tutawarudia baadae hapa mikono yote inaniuma!” Inspekta alishauri.
“Duuh! Kweli. Tuondoke tu.” Kaguta akamuunga mkono.





Ila kabla hawajaondoka, inspekta aliona kitu kiunoni mwa mwanaume mmoja mtuhumiwa. Alisogea akatizama vizuri alichokiona kwa kushusha kidogo suruali ya mlengwa, akaona ‘tattoo’. Ilikuwa ni tattoo ya mtu kivuli. Mtu aliyewasumbua vibaya mno Mtemvu na wenzake. Mtu wa ajabu aliyemaliza familia ya Ali wa Fatuma. Inspekta akaguna. Aliamua kumsogelea mwanaume mwingine akamtizama pia. Akakuta tattoo hiyo hiyo eneo hilo hilo. Hapo inspekta akapata walakini. Haraka waliondoka na Kaguta wakaelekea hospitali mpya walipowaamishia Jombi na Miraji kwa sababu za kiusalama.





Akiwa ameketi kwenye kitanda, Inspekta alishusha kidogo suruali ya Jombi akamtizama kiunoni. La haula! Aliona tattoo ile ile aliyoiona kwa wale watuhumiwa waliowateka nyara. Tattoo ya mtu kivuli; mtu muuaji, mtu mteketezaji!





“Vipi Vitalis, kuna nini?”
Kaguta aliuliza. Alitafuta nafasi naye akakaa juu ya kitanda.
“Hawa watu wanasharetattoo sehemu ya kiunoni…”
“Enhe?”
“Nashindwa kuelewa ina maanisha nini? Ila ni kithibitisho kuwa wapo pamoja.”
Kaguta alisogea karibu akatizama tattoo aliyonayo Jombi kwa macho ya umakini.
“Ina maana gani hii?”
“Sijajua, ila ni lazima itakuwa na maana yake.”




Ukimya fulani ukapita katikati yao. Baada ya muda kidogo walinyanyuka wakaelekea mgahawani kupata chakula. Walijadiliana mambo kadhaa kuhusu kesi yao. Walipomaliza waliagana, Kaguta alishika yake, inspekta Vitalis akaelekea ofisi ya mtaa wa Kilongawima mkononi akiwa na kitambulisho cha kupiga kura cha mmoja wapo wa wale wanaume waliopata kuwaua ufukweni mwa bahari.




“Samahani, naitwa Inpekta Vitalis Byabata.” Inspekta alionyesha kitambulisho kwa mwanaume mzee aiekuwa ameketi kitini, meza ndogo ikiwa mbele yake.
“Karibu, inspekta.”
“Ahsante.”
“Naweza nikakusaidia?”
“Bila shaka. Nimemkuta mwenyekiti?”
“Ndio mimi.”
“Ahsante.”





Inspekta alikiweka kitambulisho cha mpigakura cha mtuhumiwa wake juu ya meza akamsogezea mwenyekiti.




“Kwa mujibu wa maelezo yaliyo kwenye hiko kitambulisho, huyo ni mkazi wako. Kitambulisho hiko kimepatikana kwenye eneo la tukio la uhalifu, ningependa kupata taarifa zaidi juu yake kutoka kwako.”




Mwenyekiti alikitizama kile kitambulisho kwa umakini hasa sehemu za usoni, akasema;
“Ila huyu kijana ni marehemu kwa sasa, inspekta.”
“Najua.” Inspekta alijibu. “Nataka kufahamu wapi anaishi, wazazi wake na shughuli alizokuwa anajihusisha nazo.”



Mwenyekiti alirudia tena kutizama kitambulisho. Alishusha pumzi akasonya kimasikitiko;
“Kuhusu wazazi wake, ni mzazi mmoja tu ndiye amebakia ambaye ni baba. Mama alifariki muda tu. Na huyu kijana alikuwa anafanya shughuli za gym; haya mambo yao ya kupandisha na kushusha mavyuma.”
“Unaweza ukanielekeza nyumbani kwao na wapi hiyo gym ilipo?”
“Halina shaka hilo, ngoja nikupe kijana akupeleke huko mara moja.”




Mwenyekiti alimuita mesenja akampatia melekezo. Inspekta aliongozana na mesenja mpaka mbele ya nyumba moja kubwa kuukuu, walibisha hodi pasiwe na majibu, waliachana napo wakaelekea gym. Huko wakakuta wanaume wanne wakiwa wanapasha misuli.




Ilikuwa ni ndani ya jengo kubwa ambalo halikuonekana kama li tayari kwa ajili ya matumizi. Madirisha yalikuwa amefunikwa na matambaa. Ukutani kulikuwa kumechorwa chorwa matusi na michoro mingine ya ajabu. Watu wawili walikuwa wamelala kwenye mabenchi wakipandisha na kushusha vyuma, mmoja alikuwa akipiga push-up na aliyebakia akiwa anapandisha chuma akipeleka juu na kushusha chini. Ukutani kulikuwa na kitambaa kikubwa kikisomeka…NGOME YA MHARAMIA.





“Habari zenu?” Inspekta alipaza sauti. Wanaume waliokuwa wanapasha misuli waliacha shughuli zao wakamtizama kwa macho makali.



“Naomba niende.” Mesenja alisema kwa sura ya hofu. Kabla hajajibiwa, alikuwa tayari ameshapotea eneo lile.
“Wewe ni nani?”
“Inspekta Vitalis Byabata.”



Wanaume wale walitizamana baada ya kusikia hilo jibu. Ni kama vile macho yao yalitangaza vita.




“Unataka nini?”
“Nina shida na maelezo kadhaa kutoka kwenu.”
“Maelezo gani?”
“Kuhusu huyu mtu.”Inspekta alionyesha kitambulisho cha mpiga kura. Wanaume wale wakatizamana kwa mara nyingine kwa macho yaliyobeba tahadhari.
“Hatumjui!” Alijbu mwanaume alikuwa anapiga push-up. Inspekta alitabasamu kidogo kisha akaketi kwenye moja ya mabenchi yaliyokuwepo. Aliingiza mkono wake mfukoni akatoa pipi na kuirushia mdomoni.
“Awadhi ni rafiki yenu. Alikuwa anafanya hapa mazoezi, mtaa mzima unafahamu. Sijui mnapolikataa hilo mnaamanisha nini na ni kwa malengo gani?” Alinena inspekta huku akimung’unya pipi.
“Awadhi ameshakufa. Unamtakia ya nini?” Aling’aka mwanaume aliyekuwa amejilaza kwenye benchi hapo awali.
“Alikuwa anafanya shughuli gani ya kumuingizia kipato?” Inspekta aliuliza.
“Alikuwa anafanya kazi hapa gym.”
“Basi?”
“Ndio.”
“Kitambulisho hiki kimepatikana eneo la tukio la uhalifu, mna taarifa yoyote juu ya hilo?”
Wanaume walitizamana, mmoja akaropoka; “Hatuna. Hatujui chochote.”
“Mlikuwa hamjui kama rafiki yenu ni mhalifu?”
“Hatujui lolote!”





Inspekta aliona picha za watu zimebandikwa ukutani kwa mbali kidogo tokea eneo alipo. Alinyanyuka akaziendea na kuzitizama kwa umakini. Zilikuwa ni picha mbili za wanaume zikiwa zimeandikwa R.I.P kwa juu yake. Inspekta alinyanyua kitambulisho chake akafananishia picha ya kitambulisho na mojawapo ya zile.




Aliona zaendana. Picha zile zilikuwa ni za mojawapo ya watu waliouwawa kwenye tukio la kukomboa familia ya inspekta. Inspekta akiwa hapo anabung’aa, alisikia mlango unafungwa. Aligeuka akakuta wanaume wale wanne wamesimama mlangoni kama watu waliojiandaa na mapambano.




Inspekta alitoa simu yake mfukoni akaweka pembeni. Alitoa pipi nyingine mfukoni akabugia.





“Miili yote hiyo ni waoga kiasi hiki?”
“Nani muoga? Umeingia kwenye ngome. Hauwezi ukatoka kama ulivyoingia.”
“Hakika siwezi kutoka kama nilivyoingia, nitatoka nikiwa nimewamaliza wote. Kama mnajiamini njoo mmoja mmoja.”





Wanaume walitizamana kama vile wanajiuliza nani apate kutangulia. Mmoja wao alisogea mbele kumfuata inspekta. Alirusha ngumi yake ya kulia kwanguvu zote. Inspekta aliinama ngumi ikavuka kama upepo. Kwanguvu, inspekta alimkandika mwanaume yule konde la kifua chembeni mlengwa akadondokea kando akilalamika kwa maumivu.





Kwa mkupuo wanaume wawili walimfuata inspekta. Haraka inspekta aliinama akanyoosha mguu wake wa kulia na kuupitisha haraka kama feni ikamzoa mwanaume mmoja mpaka chini. Aliyebakia akisimama alinyanyua mguu wake kama mchezaji anayetaka piga shuti mpira, inspekta akawahi kutengua mguu uliosimama kwa kuugonga kwanguvu kwenye ugoko akitumia kisigino kigumu cha kiatu chake.





Haraka mwanaume wa nne alisogea na ngumi nzito imlengayo inspekta. Inspekta kwa upesi zaidi akaipiga teke ngumi ile na mguu wake wa kulia kisha akageuka na kuutumia mguu wake wa kushoto kukabidhi teke matata mno la tumboni akitumia kisigino cha kiatu; mwanaume alilalamika kwa maumivu huku akiyumba.






Ghafla, teke kali lilimpiga inspekta mgongoni likamdondosha. Wanaume wawili walimsogelea haraka, mmoja alimshika nguo akitaka kumnyanyua. Inspekta alivuta chuma kidogo kilichokuwa pembeni akamzaba nacho kwanguvu aliyemshika nguo. Damu ziliruka kama maji wakati mwanaume aliyepigwa chuma akidondoka chini kama mzigo. Akiwa bado yupo chini, inspekta alitumia kilekile chuma, alipiga mguu wa mwanaume wa pili kwanguvu … koooh!





Mwanaume yule alilia kama mtoto mdogo huku akishikilia mguu wake uliopinda. Mwanaume pekee aliyebakia akiwa amesimama akawa mmoja tu. Yule aliyekung’utwa teke la tumbo. Alimsogelea inspekta kisha akarusha teke na mguu wake wa kulia. Inspekta alidaka mguu kisha akausukuma kwa pembeni na kumfanya mwanaume yule azunguke kama pia. Alipokaa usawa wa inspekta, inspekta alimkandika tena teke la tumbo kwa kutumia kisigino cha kiatu. Mwanaume yule akadondoka chini damu zikimtoka mdomoni.





Inspekta alipogeuka nyuma akamkuta mwanaume aliyemkata mtama anaamka. Alimtizama mwanaume yule kwa jicho kali. Alimtishia kama anamfuata, yule mwanaume akarukia nje kwa kupitia dirisha lililo wazi na kutokomea. Inspekta alitikisa kichwa akatabasamu. Aliwatizama wanaume watatu waliobakia akawaona wote wapo chini wakiugulia kasoro mmoja aliyepigwa ngumi ya chembe, yeye alikuwa kimya tuli macho yamefumba.






Inspekta alisogea akamtizama mwanaume yule aliyetulia. Alipandisha body yake aliyoivaa akamtizama kiunoni akaona ile tattoo. Alifuata simu yake akapiga polisi, ndani ya muda mchache polisi wakafika na defender mbili. Wanaume wale watatu wakatiwa ndani ya gari polisi wakatokomea.



*****

☆Steve
 
***SURA YA SITA***



(MSIMU WA 02)





Kagiza chepesi kalikamata anga. Mataa ya nyumba mbalimbali yaliwashwa na kumetameta. Ila pembezoni kidogo mwa mji kwenye jumba walilofungiwa watuhumiwa lilikuwa ni kiza. Hakukuwa na taa. Giza lilikuwa totoro kama vile ni saa nane ya usiku. Mara ghafla taa kubwa iliwaka na kuwamulika watuhumiwa.





Hapo ikaonekana hawakuwa wawili tena kama hapo mwanzo, waliongezeka wanaume watatu wale waliokamatwa kwenye gym. Wote walikuwa wamefungwa kamba zikiwashikiza kwenye mistimu. Walikuwa wameinamisha macho yao chini huku wakikunja sura kutokana na mwanga mkali kuwapiga nyusoni.





“Mtasema hamsemi?” Sauti ya inspekta ilisikika lakini haikujulikana wapi imetokea.
“Najua mnaomba niwaue ila kama nilivyowaahidi, hamtokufa. Ila mtakachopitia ni kheri ya kifo. Hamtokula kwa muda wote mtakaokuwepo hapa. Chakula chenu kitakuwa ni kilio na maumivu. Kushiba kwenu itakuwa kuzirai.”




Baada ya kauli hiyo, vishindo vya miguu vilisikika. Inspekta alitokea akiwa na plies mkononi, nyuma yake aliongozana na Kaguta ama ‘The red bullet’ yeye akiwa amebebelea gongo kubwa mkono wake wa kulia. Walimsogelea mtu wa kwanza ambaye alikuwa ni mpya huku wakiwa wameipa migongo mwanga mkali umulikao.





“Ni nani mnayemfanyia kazi?”




Inspekta alimuuliza mtu aliye mbele yake huku akimsaidia kwa kumkingia mwanga na mgongo wake.
“Simfanyii kazi mtu yeyote.”





Inspekta alitabasamu baada ya kusikia hiyo kauli. Aliupisha mwanga ukammulika mwanaume yule usoni.




“Nilitegemea jibu la aina hiyo.” Inspekta alisema. Baada ya hapo kilifuata kilio kikali cha uchungu. Kaguta alimpiga mwanaume yule na gongo sehemu ya goti. Kama vile haitoshi, alimpiga zaidi na zaidi. Mwanaume yule alipiga kelele mno. Ni pale tu inspekta aliposema basi, Kaguta akaacha kuadhibu.



“Vipi, upo tayari kusema au tuhamie upande wa pili?”





Inspekta aliuliza. Mwanaume yule alikuwa analia kama mtoto achomwaye sindano. Makamasi na machozi vyote vilimtiririka.




“Tuhamia upande mwingine?”
“Hapanaaa!” Mwanaume alilia.
“Basi nijibu swali langu.”
“Naogopaa…siwezi!”
“Kwanini huwezi?”




Mwanaume yule alikaa kimya kwanza akipiga kwikwi na kuvuta makamasi. Inspekta alirudia kuuliza swali. Mwanaume yule akamjibu;
“Naogope. Kama nikikuambia nitauwawa.”
“Nani atakuua na upo hapa na sisi?”
“Kuna mtu atakuja kuniua.”
“Nani?”




Mwanaume yule hakusema tena kitu baada ya hapo zaidi tu ya kulia. Inspekta alimruhusu Kaguta aendelee na kazi yake ya kutwanga goti la pili, Kaguta alipopiga goti mara moja kwanguvu, mwanaume yule alipiga kelele kali mno;
“Nasemaaa…uuuuwii…nasemaaa!”






Uso wake ulieleza ni maumivu ya aina gani anayopitia. Hata kama angeachwa aondoke zake, alikuwa tayari ameshapata ukilema.
“Naogopa, nikisema nitauwawa! Naogopa jamani! Naumiaaa!”
“Unamuogopa nanii?”
“Tulikula kiapo cha damu. Hakuna yeyote anayeweza sema chochote. kama ukikiuka, damu yako itafuatwa popote ilipo. Huwezi ukakimbia wala huwezi kujificha.”
“Oooh sawa. Basi tutaendelea kutwanga huo mguu mpaka utakapo kiri. Kaguta, fanya kazi yako.”





Kabla Kaguta hajafikisha gongo kwenye goti, mwanaume yule alipayuka;
“Nasema…nasemaaa! Tunamfanyia kazi Mr Kim. Yeye ndiye anatulisha kutuvisha na kutupa chochote tunachotaka.”
“Mr Kim? … Yupi?”
“Mr Kim Salvatore; mfanyabiashara.”
“Mr Kim from Bermuda?”
“Ndio!”





Mwanaume huyo aliposema tu hayo, wenzake walipaza sauti kumshtumu. Walimtukana na kumuita mwanamke; amekiuka masharti na punde roho zao zitafuatwa.



“Tusamehe sio sisi! Tusamehee!” wanaume wale walilia. Inspekta na Kaguta walishangazwa na hilo.






Haukupita muda, mwanaume yule aliyefungua mdomo kusema alianza kulalamika anaungua. Alihangaika kutaka kujinasua lakini hakuweza. Alilalamika anaungua kiunoni moto unapandisha kwa juu. Inspekta alimvua suruali akiwa anatafuta huo moto upo wapi. Hamaki! Aliona tattoo inavuja damu.




“Kaguta, unaona?” Inspekta aliduwaa huku akionyeshea tattoo ile ivujayo damu. Kaguta alishangaa. Wakati huo bado yule mtu akilalamika anaungua mwili mzima sasa.





Ghafla, taa ilizima. Iliwaka ikazima tena. Iliwaka na kuzima, iliwaka na kuzima. Ilipowaka, mwanga haukuwa tena mweupe bali mwekundu kama damu. Kaguta alimtizama inspekta kwa macho ya mshangao. Wanaume wale kazi yao ilikuwa ni kulia tu huku wakiomba msamaha.





Punde katika mwanga ule mwekundu kilionekana kivuli cha mtu. Alikuwa na kichwa kikubwa kikiwa na vitu kama viluwiluwi vikichezacheza. Vidole vyake vilikuwa virefu na vyenye ncha kali. Na macho yalikuwa mekundu mno. Pap! Taa ilikata mwanga. Pap! Mwanga ukarudi, mwanaume yule aliyefungua mdomo wake alikuwa tayari ameshauwawa. Shingo yake ilikuwa inachuruza damu kama bomba la maji.





“Mungu wangu!”





Alitahamaki inspekta. Yeye na Kaguta walikuwa wametoa macho kama vile madunguri.





Pap! Taa ilikata tena. Mwanga uliporudi, mtu wa pili akawa tayari naye ameshaenda. Shingo yake ilikuwa inamwaga damu. Walibakia wanaume watatu wakiwa wamefungwa. Wote walikuwa wanalia kwa hofu ya kifo.





Tap! Taa ikazima na kuwaka, ikazima na kuwaka. Watu wawili wakaenda na kifo kilekile. Taa ilipozima tena, haraka inspekta aliwasha tochi na kummulikia mwanaume aliyebaki. Ajabu, hakukuwa na kitu kilichotokea.




“Tuondoke hapa! Tuondoke Vitalis!” Kaguta alinasihi.
“Ngoja kidogo.” Inspekta alijibu; macho yalikuwa yamewatoka huku wakihema pumzi yenye hofu.





Taratibu inspekta alianza kusogea akimfuata mwanaume aliyebaki huku akimmulika na mwanga wa tochi yake. Miguu ya inspekta ilikuwa inatetemeka lakini bado alisonga. Kaguta alibaki nyuma, hakutaka kusoea popote, alikuwa tayari ameshakaa kando na mlango.




Inspekta alimfikia yule mwanaume akamuona anavuja damu maeneo ya kiunoni. Lakini zaidi ya yote kulikuwa kama kuna kitu kinahangaika. Mwanaume yule alikuwa anapiga kelele za maumivu. Inspekta alishusha suruali ya mwanaume yule akaona kitu cha ajabu. Ilikuwa ni mtu si mtu, dubwana si dubwana likihangaika kutaka kutoka ndani ya tattoo. Inspekta alishtuka mno. Tochi ilimponyoka ikadondokea chini na kuzima papo hapo.





Inspekta alipapasa papasa kutafuta tochi. Alipoipata aliiwasha kummulika mwanaume yule mtuhumiwa. Akamkuta ameshauwawa. Shingo yake ilikuwa tayari imeshafyekwa. Na papo hapo taa kubwa iliwaka kama hapo mwanzoni. Inspekta alipepesa macho yake kumtafuta Kaguta, lakini hakuonekana.





“Kagutaa! Kagutaa!”






Inspekta aliita lakini hakukuwa na majibu zaidi tu ya mwangwi kumrudia. Pap! Taa kubwa ilizima. Ilipowaka, Inspekta hakuonekana. Chumba hakikuwa na mtu yeyote. Kilikuwa tupu na taa peke yake.





Ni huko nje ndipo inspekta alipoonekana akiwa anatizama tizama huku na huko kama mtu anayetafuta njia. Kwa mbali kidogo aliona taa za gari zimewaka, alikimbilia eneo hilo akiwa na uso wa hamu ya kufahamu. Aliposogea karibu zaidi, aligundua ni gari la Kaguta.





“Kaguta!”
Inspekta aliita.
“Ingia ndani tuondoke. Haraka!” Sauti ya Kaguta iliamuru. Inspekta aliingia ndani, gari likaondoshwa kwa kasi mno vumbi tu likitimka.
“Uliondoka saa ngapi mbona sikukuona?” Inspekta aliuliza.
“Niliona huna mpango wa kuondoka, mimi nikaondoka zangu. Taa ilikuwa imezima ndio mana hukuniona.”
“Ulintisha ujue. Mie nikajua umebebwa na lile jitu!”
“Wewe ndo’ ulikuwa unantisha. Nakuambia tuondoke hutaki, nikajua ushaingiliwa.”




****
☆Steve
 
****SURA YA SABA****




(MSIMU WA 02)





“Hapana. Kuna kitu niligundua, yule mtu alikuwa anajitokeza pale tu taa ilipozima. Uliona nilivyowasha tochi hakuonekana!”
“Sikuona. Labda tayari nilikuwa nishaondoka.”
“Labda. Huwezi amini zile tattoo walizochora si tu ni tattoo, bali ndio jitu lenyewe. Na hata Jombi anayo, sidhani kama ataweza kusema yale nitakayomuuliza.”
“Mmmh ngoma nzito! … ila, mbona lile jitu halikutumaliza sisi? Au ni bahati tu?”
“Hapana. Hatukuwa tu kwenye ratiba yake. Si unakumbuka wale wengine walianza kulia baada ya mwenzao kuongea?”
“Yap!”
“Ni kiapo wamekula. Tena kiapo cha damu.”
“Sasa kweli tutaweza kupambana nao?”
“Naamini kila kitu kina njia. Ila kupambana na lile jitu inabidi utumie akili mara mbili zaidi ya kawaida. Na kuna kitu chanishangaza, nashindwa kuelewa”
“Na vipi kuhusu Mr Kim?”
“Mmmh hapo ndipo kazi ilipo. Mr Kim ni mfanyabiashara mkubwa mno na anayeheshimika mpaka na serikali, ila sikuwahi kufikiria kama anaweza kujihusisha na mambo ya kidhalimu kama haya. Ila ninachotaka kukifahamu hasa ni kwanini Mr Kim yupo nyuma ya hili kundi, na ana kipi cha kuhusika na vifo vya Mtemvu na wenzake kwani kijana wake ni mmoja wa watu waliokuwa wanashughulikia hilo na bila shaka alikuwa anapata silaha toka kwenye kundi lake hili.”
“Sasa tutampatia wapi Mr Kim?”
“Ni ngumu sana kumpata Mr Kim. Si mtu wa kuonana naye hivi hivi. Cha kufanya inabidi tutafute sababu ya kufanya akutane nasi. Na Kuanzia sasa tuwe karibu na ratiba yake.”
“Sawa. Sasa? Mimi napitia bar mara moja nikastue. Siwezi nikalala hivi hivi.”
“Umeanza!”
“Nini sasa? Kwani nimefanya dhambi gani? Siwezi kulala kusema ukweli kama sijastua maana kile nilichokiona si kheri kabisa.”





Gari lilipaki kwenye bar kubwa. Kaguta pamoja na Inspekta walishuka na kufuata viti virefu vilivyokuwa vimeketi pembezoni mwa kaunta iliyokuwa imejaa kila aina ya vinywaji kuanzia maji, bia mpaka mvinyo na whisky. Kaguta aliagiza chupa ndogo ya Jack Daniels wakati inspekta akiagiza maji makubwa ya Kilimanjaro. Kila mmoja alipiga pafu moja, soga zikatwaa nafasi;





“Kwahiyo mke na watoto wako wapo wapi kwa sasa?”
“Nyumbani. Sema ni nyumba nyingine, niliwahamisha kule kwa usalama.”
“Unalala nao?”
“Ndio. Siwezi nikalala mbali nao. Hapa tu yenyewe nahofia huko walipo.”
“Pole. Usihofu Mungu yu nao. Kwani vipi haukuomba wapewe ulinzi?”
“Niliomba. Wapo polisi wawili hapo nyumbani ila bado siwezi nikajiamini kihivyo.”
“Usiogope rafiki. Kila kitu kitakuwa sawa.”




Waliendelea kunywa taratibu vinywaji vyao huku macho yao yakitizama wahudumu warembo waliokuwa wanakatiza hapa na pale. Kwa mara kadhaa walikuwa wanatekwa na runinga kubwa iliyokuwa inaonyesha mpira lakini hawakuonekana kuvutiwa sana na hilo, ni pale tu makelele ya watu wanaoshangilia yalipowika ndipo Kaguta na inspekta wakarushia macho yao kideoni kutizama kinachojiri.





Baada ya nusu saa inspekta akiwa kabakisha kiasi kidogo cha maji kwenye chupa yake, alinyanyuka akatoa pesa mfukoni mwake na kumkabidhi mwanamke aliyekuwa amejaa tele kaunta akihudumia.





“Ahsante dada.” Inspekta alisema kisha akamtizama Kaguta aliyekuwa bado ameketi asionekanehata na dalili ya kuondoka.
“Tuondoke, baba.”
“Mapema hii, mie siendi popote.”




Kaguta alisema kisha akamtizama mdada wa kaunta na kumkonyeza. Mdada alitabasamu akasogeza glasi kubwa mezani na kuimiminia kinywaji cha Jack Daniels.





“Hiyo glasi ya nani?” Inspekta alitahamaki.
“Yangu!” Kaguta alijibu na kuongezea, “Ngoja basi nimalizie hii alafu tuondoke.”
“Dah! Aisee.” Inspekta aliduwaa. “Kama unataka nikae kukusubiria unywe na hiyo, tukubaliane gari naendesha mimi.”
“Sawa. Haina shida. Utaendesha tu.”




Kaguta alimgeukia mdada wa kaunta akalamba lips zake na kurembua kidogo macho yake mekundu yaliyolowea kileo.





“Njoo basi kwa hapa.” Alisema Kaguta huku akionyeshea kiti kirefu cha pembeni yake. Mdada alitabasamu akasogeza glasi kwa Kaguta akisema;
“Nakuja.”




Alimuita mwenzake akamuomba asimamie kuuza vinywaji. Alitoka akaungana na Kaguta kwenye kiti alichoelekezwa. Inspekta alitikisa kichwa chake akanong’ona;
“Unafanya nini sasa, Kaguta?”




Kaguta alitoa ishara ya kumtaka inspekta atulie. Inspekta bila kuleta zogo alitulia. Wakati anasubiria, aliamua aagize kinnywaji laini kuvutia subira.




“Niambie mrembo.”
“Safi tu nakus’kiliza wewe.”
“Unaitwa nani?”
“Naitwa Bhoke.”
“Unatumia kinywaji gani mtoto?”
“Safari lager.”
“Agiza basi.”





Bhoke alimtizama mwenzake na kumtikisia kichwa. Mwenzake aliyekuwa kaunta alipangua safari mbili baridi toka kwenye jokofu akazifungua na kumpatia Bhoke. Taratibu Bhoke alianza kupanda mlima huku akiwa anapiga simulizi na Kaguta. Kaguta alikuwa anaongea kwa taratibu na macho yake yalikuwa yanatizama kifua cha Bhoke kilichojaa pamoja na miguu yake meupe iliyochomoza toka kwenye sketi fupi nyeusi aliyovaa.






“Umependeza kweli.”
“Aaah wapi na uniform?”
“Ndio. Kwani haiwezekani?”
“Sidhani.”
“Basi wacha nirekebishe kauli. Wewe ni mzuri, Bhoke.”
“Ahsante sana.”




Bhoke alitabasamu na kupeleka bia yake mdomoni akagida mafundo kadhaa.





“Vipi tunaweza tukaenda wote home?”
“Home mapema yote hii? Mbona una haraka?”
“Usiku mrefu mama. Nipo mpweke kazi kujigeuzia huku na kule, kitanda kikubwa.”
Bhoke alitabasamu tena; “Wewe una vituko kweli.”
Kaguta alimiminia kinywaji chake mdomoni, alipokiweka chini alifungua kinywa;
“Ni kweli ninayokuambia. Sasa mrembo, utaenda nami angalau usiku wangu leo ukawe wa kumbukumbu?”
“Naweza nikaenda nawe ila nitaachaje ofisi sasa?”
“Si kuna mtu mwingine anakaimu nafasi yako.”
“Hapana, ni zamu yangu hii nastahili kuwa hapo. Na pia kuna bosi, naye akisikia sipo ataleta matatizo.”



Bhoke alimwaga maelezo. Kaguta alitikisa kichwa akanywa fundo moja la ukweli. Aliingiza mkono wake mfukoni akatoa elfu kumi kumi kadhaa nyingi na kuzitupia mezani.





“Mpe bosi wako hiyo, mwenzako wa kukushikia zamu na wewe.”



Bhoke aliwahi kuchukua pesa na kuziweka kwenye sidiria yake.




“Sasa tunaondoka wote?” Kaguta aliuliza.
“Ndio. Nisubirie basi nikawape pesa zao tuondoke.” Bhoke alisema kisha akanyanyuka na kwenda. Kaguta akamsindikiza mwanadada na macho yaliyonawiri tamaa. Aligeuka kutizama nyuma yake alipokuwa amekaa inspekta, hakuona kitu. Alirusha macho yake huku na huko ndani ya bar kumtafuta inspekta lakini hakukuwa na sehemu alipoonekana.



Inspekta alikuwa yupo ndani ya gari kwenye kiti cha dereva akiwa amelala. Vioo vilikuwa vimepandishwa na ndani redio ilikuwa inapiga muziki kwa sauti ya chini.




Inspekta aligutuka toka usingizini aliposikia gari latikisika. Aliporusha macho yake nje alimuona Kaguta pamoja na Bhoke wakiwa wamesimama mlangoni mwa gari. Alifungua lock ya milango, Kaguta na Bhoke wakaingia kukaa viti vya nyuma. Inspekta aliwatizama kwa kupitia kioo kilichokaa juu yake akawaona wanatomasana na kupapasana. Alitikisa kichwa akaliondoa gari.




Ndani ya dakika ishirini, inspekta alishafika sehemu anaposhukia. Alizima gari akamkabidhi funguo Kaguta. Aliaga na kushika njia nyembamba isiyopitika na gari. Haikupita napo muda mrefu, Kaguta aliliondoa gari kuelekea kwake akiwa na mrembo wake aliyemnasibu toka bar.





Baada ya sekunde chache tangu Kaguta aondoke eneo aliposhukia inspekta, pikipiki kubwa ilisogea eneo hilo ikiwa imebebelea wanaume wawili waliovalia kofia ngumu nyeusi za pikipikina suti za jeans. Mwanaume aliyekuwa ameketi nyuma alitoa simu yake mfukoni akavua kofia yake na kupiga huku akishuka.



“Yes boss … ameshashuka … sawa … haina shida mkuu.”





Simu ilikata. Mwanaume yule alimtizama mwenzake na kutikisiana vichwa kisha akashika njia ile ile nyembamba aliyoenendea inspekta.




***
☆Steve
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom