Simiyu: Afisa Ustawi, Mwalimu wakwamisha tena kesi ya Askari kudaiwa kumpiga hadi kumjeruhi mtoto wake

JanguKamaJangu

JF-Expert Member
Feb 7, 2022
2,308
5,462
Kesi ya Jinai Namba 59, 2023 inayomkabili Askari wa Kituo cha Polisi Bariadi Mkoani Simiyu H.4178 Abati Benedictor anayedaiwa kumpiga hadi kumsababishia majeraha mtoto wake (07), jana imeshindwa kuendelea kusikilizwa katika Mahakama ya Wilaya ya Bariadi baada ya Mashahidi upande wa Mashtaka kushindwa kutokea mahakamani.

Katika kesi hiyo, upande wa Mashitaka ulikuwa unaendelea kuwasilisha mashahidi wake, na jana ilikuwa zamu ya Afisa Ustawi wa Jamii Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Bariadi Nance Joshua pamoja na Mwalimu wa darasa la mtoto huyo Katendele Benadestina.

Mashahidi hao walishindwa kutokea Mahakamani bila ya kutoa sababu za kufanya hivyo, licha ya kupewa taarifa za kuhitajika katika kesi hiyo kwa ajili ya kutoa ushahidi wao, kupitia Ofisi ya Ustawi wa Jamii Halmashauri ya mji wa Bariadi.
WhatsApp Image 2023-11-17 at 12.32.52_a2ce3ea4.jpg
Hata hivyo baada ya mashahidi hao kushindwa kutoa Mahakamani, Hakimu anayesikiliza kesi hiyo Caroline Kiliwa alihairisha kesi hadi Novemba 27, 2023 huku akitoa angalizo la kufuta kesi hiyo iwapo mashahidi hao watashindwa kufika mahakani tena.

Hii ni mara ya pili Mashahidi hao kushindwa kufika Mahakamani kutoa ushahidi wao, ambapo mara ya kwanza ilikuwa Novemba 02, 2023 hali iliyosababisha Hakimu kuahirisha kesi hiyo hadi Novemba 14, 2023 ambapo pia hawakutokea tena Mahakamani.

Kwa mujibu wa Mwendesha Mashitaka anayesimamia kesi hiyo kutoka Ofisi ya taifa ya Mashitaka Mkoa wa Simiyu Rehema Safaku baada ya kesi kuahirishwa alieleza kuwa mashahidi hao kila mmoja alipewa taarifa.

“ Kila Shahidi alipewa taarifa na jana kabla ya kesi niliwasiliana nao tukakubaliana wafike mapema Mahakamani, lakini nashangaa hadi kesi inaanza hakuna shahidi hata mmoja, nimejaribu kuwatafuta kwenye simu wote hawapokei simu zangu,” alisema Sakafu.

Alipotafutwa Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa Daniel Mapunda alisema kuwa naye amepata taarifa za Afisa wake kushindwa kutokea Mahakamani na kueleza kuwa bado hajapewa sababu za Afisa huyo kufanya hivyo.

“ Hata mimi nashindwa kuelewa nini tatizo, wakati taarifa alipewa mapema na akasisitizwa awepo mahakani, lakini nashangaa kusikua hakutokea, nafuatilia kujua sababu za yeye kufanya hivyo bila taarifa, isije kuonekana sisi ndiyo tunakwamisha hii kesi,” alisema Mapunda.

Afisa Ustawi wa Jamii Halmashauri ya Mji wa Bariadi Siwema Chungu alipoulizwa juu suala hilo, alisema kuwa Afisa Ustawi aliyetakiwa kwenda mahakani alishindwa kutokea kwa sababu hakuwa na taarifa ya wito (SORMOUS).

“ Hata sisi tulishangaa kwa nini hakutokea Mahakamani wakati taarifa tulimpatia, tulimpomuuliza alisema hakuwa na taarifa ya wito, tukamuuliza mbona ofisi ilikupatia taarifa??, akajibu asingeliweza kwenda bila taarifa ya wito,”

Siwema amesema kuwa kwa sasa wanatafuta barua yenye taarifa ya wito kutoka Ofisi ya Mashitaka kwa ajili ya kumpatia Afisa huyo wa Ustawi, pamoja na Mwalimu ili wahudhurie Mahakamani Novemba 27, 2023.

Askari huyo akabiliwa na shtaka moja ambalo ni kumchapa mtoto wake kwa fimbo na kumjeruhi maeneo mbalimbali ya mwili wake kinyume na kifungu Cha 169 A kifungu kidogo Cha 1 na Cha 2 Cha Sheria ya kanuni ya adhabu sura 16 marejeo ya mwaka 2022.

Chanzo: simiyupresstz.blogspot

Pia soma
= Shahidi Kesi ya Askari kumjeruhi Mtoto: Majeraha aliyokuwa nayo Mtoto yalitokana na kupigwa

= Simiyu: Utata kesi Askari Polisi aliyetuhumiwa kumjeruhi mtoto wake kisha kesi kufutwa
 
Back
Top Bottom