Nape: Nchi kwanza chama baadaye
Mwandishi Wetu Septemba 17, 2008
Tanzania Daima~Muungwana ni Vitendo
KATIKA kauli ambayo inaweza kuibua mjadala ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya chama hicho (NEC), Nape Moses Nnauye, amesema siasa ni utumishi kwa umma na katika hilo anaamini katika uzalendo kwa nchi kwanza kisha chama baadaye.
Akizungumza na Raia Mwema katika mahojiano maalumu, Nape ambaye pia ni mtumishi wa chama hicho amesema uzalendo wake unamsukuma kuamini kwamba chama kinaweza kupita lakini nchi ikabaki milele.
"Tunakuwa na nchi kwanza tunayotaka kuijenga, ndipo tunaunda chama cha kujenga nchi tunayoitaka, kwa hiyo uzalendo kwa nchi unapaswa kuvuka mipaka ya itikadi zetu," anasema.
Kauli hiyo ya Nape ambayo inaweza kuzua mtafaruku mwingine na chama chake, ameitoa huku akiwa katika msigano mkubwa na jumuiya ya vijana ya chama chake ya UVCCM kuhusiana na kauli yake ya kuukosa hadharani mradi wa jengo la umoja huo.
Katika mahojiano hayo ambayo yamechapishwa kwa kirefu ndani ya toleo la leo, Nape anasema suala la mradi wa jengo hilo lililopo eneo la Faya barabara ya Morogoro, Dar es Salaam halina uhusiano na uamuzi wake wa kuwania nafasi ya Uenyekiti wa UVCCM.
"Kimsingi kwanza kuna mambo mawili yanachanganywa na kuwa moja. Si sawasawa. Ugombea wangu wa Uenyekiti wa UVCCM na mradi wa ukarabati wa Makao Makuu havihusiani.
"Mradi ule nilivyosema na hata kama nitaendelea kusema ni katika kutimiza wajibu wangu kama mjumbe wa NEC na Baraza Kuu la UVCCM ninayewawakilisha Vijana, lakini pia kama kijana mzalendo wa CCM na Tanzania.
"Naamini matokeo ya vikao viwili vikubwa vya chama yaani, Kamati Kuu na NEC vimeweka wazi ukweli wa mambo wa kile nilichokuwa nikikilalamikia juu ya mkataba mzima na matokeo yake ni kamati ya kina Dk. Abdallah Kigoda, Pindi Chana na Andrew Chenge.
" Naamini wanaoendelea kusema juu ya hili na kutafsiri watakavyo baada ya taarifa rasmi kutolewa na Naibu Katibu Mkuu Zanzibar Saleh Ramadhan Feruzi wana ajenda zao binafsi. Wito wangu kwao tuheshimu maamuzi ya vikao halali vya chama na kuacha kulumbana katika jambo moja, tunayo mengi ya kufanya," alisema.
Nape amezungumzia pia msimamo wake wakati wa mchakato wa uteuzi wa mgombea urais wa CCM mwaka 2005 kwa kusema kwamba baada ya uteuzi makundi yalikwisha na yeye binafsi alisimama kidete kumpigia debe mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete.
"Msimamo wa chama ni kuwa katika uchaguzi kila mtu ana uhuru wa kuunga mkono mtu anayeamini anafaa kuliko mwingine, isipokuwa baada ya uteuzi wote tunakuwa kitu kimoja. Huu ni msimamo wa chama, hivyo sioni kosa la kuwa na chaguo fulani kabla ya uteuzi.
"Linakuwa kosa uteuzi ukiisha kupita watu wakaendelea na mambo yao kinyume na mteule wa chama. Ndiyo maana baada ya uteuzi ni mimi ndiye nilisimama kidete kwenye radio na hata mikoani kumtetea Kikwete kwamba ndiye chaguo la chama, hivyo anafaa kuwa Rais wa Tanzania," anasema.
Kuhusu uhusiano kati yake na Mwenyekiti wa UVCCM anayemaliza muda wake, Emmanuel Nchimbi, Nape anasema kwamba hana ugomvi na kiongozi huyo bali wanatofautiana katika baadhi ya mambo tu.
Alisema hana ugomvi binafsi na Nchimbi, wala yeyote ndani ya CCM bali mara nyingi anapishana nao kimtazamo, hali ambayo anasema inachukuliwa kuwa ni msigano.
"Siyo kwamba pia Nchimbi kafanya yote mabaya, hapana, yapo mazuri machache, lakini naamini katika Umoja wa Vijana ambao unajua kuwa hatma ya nchi yao ipo mikononi mwao na kwamba wana wajibu wa kuamua kesho yao iweje na si kuamuliwa na mtu au kikundi cha wachache," alisema na kuongeza;
" Tukatae utaratibu unaoanza kujengeka wa kuviza akili na mawazo ya vijana wa Bara letu, athari za maamuzi yoyote waathirika wakubwa ni vijana na wanaathirika leo na kesho, so they have to be bold to stand for their rights (wanatakiwa kusimama kidete kutetea haki zao). Tujifunze kuacha unafiki, kisu kiitwe kisu, na uma uitwe uma, maana ukiwa mnafiki ujanani uzeeni utakuwa mchawi".