Nape Nnauye atoswa kinyang'anyiro cha uongozi Vijana wa CCM
Na Mwandishi Wetu
Mwananchi
Date::8/19/2008
SAFARI ya Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa Chama hicho (UVCCM), Nape Nnauye kuwania nafasi ya Mwenyekiti wa Umoja huo Taifa, imeishia njiani baada ya Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM kumpa alama E inayoonyesha kwamba hafai kugombea nafasi hiyo.
Habari za uhakika zilizolifikia gazeti hili jana zinasema kuwa, kikao cha Kamati ya Utekelezaji cha Agosti 16 na 17 mwaka huu mjini Dodoma kimemuengua Nnauye katika kinyang'anyiro cha nafasi hiyo na kupendekeza majina ya watu watano kuwania nafasi hiyo.
Majina yaliyopendekezwa ni Zainab Kawawa, Said Mtanda, Benno Malisa, Hussein Bashe na Suleiman Suleiman.
Kwa mujibu wa habari hizo, Nnauye amewekewa alama ya kutofaa kugombea nafasi hiyo kutokana na kigezo cha umri, ingawa kuliibuka mjadala mzito ndani ya kikao hicho kabla ya kufikia maamuzi hayo.
Mjadala uliibuka na kuwagawa wajumbe katika makundi mawili yanayopinga na kukubali uamuzi huo, lakini kundi lililopinga lilionekana kuwa dhaifu kutokana na idadi yao kuwa ndogo.
"Haikuwa rahisi kufikia maamuzi hayo, kwani kamati iligawanyika katika makundi ya wajumbe kutoka Zanzibar na wale wa Bara. Zanzibar waligoma, lakini walishindwa kutetea uamuzi wao kutokana na idadi yao kuwa ndogo na hoja zao kuonyesha kwamba zinataka kuvunja kanuni ambao walijiwekea," kilisema chanzo cha habari.
Awali, imedaiwa kuwa kabla ya kuanza kikao hicho, Mwenyekiti wake, Dk Emmanuel Nchimbi aliwatahadharisha wajumbe kuwa kikao kingekuja na maamuzi ya kihistoria ya ama wajumbe kuondoka wakiwa wameungana ama kugawanyika kama wangevunja kanuni na kujali zaidi watu.
Sababu zilizotolewa na upande uliounga mkono kuondolewa kwa Nape ni kutetea maamuzi ya vikao vyake vilivyopitisha kanuni ya kikomo cha umri katika uwania nafasi hiyo.
Hata hivyo, Nape aliliambia gazeti hili jana kuwa Kamati ya Utekelezaji ya UVCMM haina mamlaka kisheria kukata jina la mgombea na kufafanua kuwa mamlaka ya maamuzi hayo yako katika kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM (NEC).
"Vikao vya chini havina mamlaka kukata jina la mgombea, wanachofanya ni kujadili na kuweka alama na mimi waliniwekea alama mbaya ya E ikimaanisha kwamba sifai. Hata hivyo, kikao chenye mamlaka ya kukata jina na Halmashauri Kuu ya CCM chini ya Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete," alisema.
Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM imefikia hatua hiyo baada ya kupitia vyeti halisi vya kuzaliwa vya wagombea hao na kubaini kuwa, Nape alizaliwa mwaka 1977.
Sambamba na kupitia vyeti hivyo, wagombea wote walihojiwa mmoja baada ya mwingine na kutakiwa kuwasilisha kadi ya uanachama na nyaraka zingine za kuthibitisha maelezo waliozaja kwenye fomu za maombi, ikiwa ni pamoja na vyeti halisi vya kuhitimu darasa la saba.
Kamati ya Utekelezaji ni kikao cha pili kujadili majina ya wagombea hao. Kikao cha kwanza ni Sekretarieti ya UVCCM iliyokaa jijini Dar es Salaam chini ya Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Francis Mtinga, ambako pia habari zinadai kuwa alipewa alama za chini.
Kwa mujibu wa kanuni za CCM katika uchaguzi huo, Kikao cha Kaamati ya Utekelezaji kitafuatiwa na Baraza Kuu la UVCCM kabla ya mkutano wa Sekretarieti ya CCM chini ya Katibu wake Mkuu, Yusuf Makamba.
Vikao vingine katika mchakato huo ni Kamati ya Maadili ya CCM na Kamati Kuu (CC) ambavyo vitakaa Agosti 20 na 21 mwaka huu chini ya Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete.
Vikao hivyo vitapitia maamuzi ya vikao vilivyopita na kutoa ushauri wake kwa Halmashauri Kuu (NEC), itakayokaa Septemba 2 na 3 mwaka huu kuchambua na kutangaza majina ya wagombea walioteuliwa.
Zengwe la umri ni kanuni iliyoingizwa kwenye taratibu za Uchaguzi wa UVCCM mwaka 2003 wakati Mwenyekiti wa sasa, Dk Emmanuel Nchimbi anawania nafasi hiyo kwa mara ya pili, ikilenga kumuengua, lakini busara ya Kamati Kuu ya CCM iliiweka pembeni kwa muda.
Kulingana na kanuni hiyo umri wa mwisho wa kugombea ni miaka 30 ili kiongozi husika asizidi miaka 35 akiwa madarakani umri ambao ni wa mwisho wa uanachma wa UVCCM.
Zengwe la umri safari hii linalekea kuwalenga baadhi ya wagombea machachari katika Uchaguzi wa UVCCM, ambao ni pamoja na Nape Nnauye.
Habari za ukahakika zanasema kwamba, baada ya hoja ya umri wa miaka 30 kuahirishwa mwaka 2003, kabla ya kutumika ilipaswa kwanza kupata baraka za vikao vya UVCCM kuanzia kwenye sekretariati, Kamati ya Utekelezaji na mwishowe kwenye Baraza Kuu. Hatua hizi hazikufuatwa ila ni NEC iliagiza tu kuanza kutumika.
Hata hivyo, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa UVCCM ambaye pia ni Kaimu Katibu Mkuu wa umoja huo, Francis Isaac, aliambia Mwananchi hivi karibuni kwamba, kanuni ya umri ilipitishwa na Kamati Kuu ya CCM miaka mitano ilyopita.
Isaac alisema kuwa, haikuweza kutumika katika Uchaguzi wa UVCCM uliopita kwa sababu wakati uamuzi unapitishwa wa kanuni hiyo tayari uchaguzi ngazi ya wilaya ulikwisha kufanyika na hivyo kuamuliwa ianze kutumika katika uchaguzi huu.
Isaac pia alisema kwamba mchakato wa kutungwa kwa kanuni hiyo ulifuata taratibu zote kuanzia kwenye sekretariati, Baraza Kuu, Kamati Kuu ya CCM, NEC na baadaye Mkutano Mkuu wa CCM uliofanyika miaka mitano iliyopita.
Nape aliyezaliwa Novemba 26, 1977, aliwasha moto ndani ya chama hicho siku amechukua fomu ya kuwania nafasi hiyo, baada ya kulipua bomu kwamba, mkataba wa kujenga jengo jipya la UVCCM umegubikwa na ufisadi.