Ningependa kwanza Bwana Nape (MNEC-CCM),aniondolee shida ninayopata kufuatia tuhuma nzito (kama ni kweli) alizozitoa kwa uongozi wa UVCCM na kwa Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini wa UVCCM Mh.E.Lowasa.
Kimsingi ni tuhuma nzito sana ambazo kwa kweli zinapaswa kuangaliwa kwa undani sana.
Sina tatizo na hatua ya bwana Nape kutoa madai ya kuwatuhumu wahusika.Ni haki yake ya msingi.Lakini pia ni jambo jema haswa kama ni madai yenyewe ni ya kweli. Lakini maswali yangu yanajikita katika maeneo yafuatayo?
1.Mnauye ni mjumbe wa baraza kuu la UVCCM.je alishawahi kuhoji na kuomba kupewa ufafanuzi juu ya madai hayo ndani ya kikao halali na kukubwa kwa mujibu kanuni ya UVCCM?
2.Nape Mnauye,pia ni mjumbe wa NEC ya CCM.Je, kama kwa sababu moja ama nyingine alishindwa kuwasilisha hoja au madai yake hayo mbele ya baraza kuu la UVCCM,aliweza kuwasilisha madai hayo mbele ya NEC au uongozi wa chama kwa hatua za uchunguzi zaidi? Kwa sababu ni muhimu kufahamu kwamba jumuiya zote za CCM ziko chini ya CCM.Na kama kuna ukiukwaji wa maadili katika jumuiya husika,CCM inaingilia kati.Tumeshuhudia haya kwa jumuiya ya Wazazi na Wanawake(UWT).
3.Mwisho nadhani bwana Nape anafahamu kwamba kwa mujibu wa muundo wa jumuiya ya UVCCM,Mwenyekiti hawezi kufikia maamuzi mazito yeye binafsi bila vikao husika.Kwa hiyo kama ni tuhuma, basi ningeelewa zaidi kama angezielekeza kwa kamati nzima ya utekelezaji ya baraza kuu la UVCCM .Na angetoa wito kamati hiyo ijiuzuru.
Lakini pia kwa utaratibu,kamati ya utekelezaji nayo lazima iwasilishe mapendekezo yake kwa baraza kuu kwa baraka zake,ambako Nape ni mjumbe.Kwa hiyo kama baraza kuu lilibariki madai yanayotolewa ,basi bila shaka na yeye Nape ni sehemu ya maamuzi hayo.Kwa hiyo hata yeye anawajibika.
Iwe aliunga mkono hoja au hakuunga mkono hoja,ukweli unabaki kuwa naye alikuwa sehemu ya maamuzi kwa mujibu wa kanuni na taratibu za vikao. Sasa kama hakuridhika na uwajibikaji wa pamoja,basi njia pekee ya kunishawishi niamini kuwa anania ya dhati ya kuleta mageuzi ndani jumuiya,basi alipaswa kujiuzuru ujumbe wake wa NEC alioupata kwa tiketi ya UVCCM,kutokana na kutoridhishwa na ukiukwaji wa maadili,kanuni na taratibu ndani ya UVCCM.
Sasa anapokuja na madai hayo mazito wakati wa kuchukua fomu za kuomba uongozi,kunanipa tabu sana kushawishika kuamini kama kweli dhamira yake ni kuleta mapinduzi ndani UVCCM.Vingenevyo nashawishika kuamini kuwa huu waweza kuwa ni mkakati maalumu.