HALFANI SUDY anaandika HATARI
Sehemu ya 14
Ilipoishia...
Fikra za Martin Hisia zilikuwa maili nyingi sana kutoka pale sebuleni. Fikra zake kwa sasa zilikuwa zimefika Mikocheni jijini Dar es salaam, nyumbani kwa Daniel Mwaseba. Alikuwa hajui kitatokea nini endapo Daniel akigundua kama ameusaliti upande wake, alikuwa hajui Daniel atachukua hatua gani akijua kuwa Martin amefanya kitendo hiko kibaya kabisa cha usaliti. Kubwa zaidi, alikuwa anafikiria kazi ngumu iliyopo mbele yake, kazi ya kwenda kutega kamera ya siri katika chumba cha Rais Mark Mwazilindi, lakini, alikuwa tayari kwa chochote kile kitakachotokea, kwakuwa alikuwa ana ni ya dhati ya kutaka kumwokoa ndugu yake wa damu, Nato.
Songa Nayo...
DANIEL MWASEBA aliamka saa kumi na moja asubuhi. Alienda bafuni kupiga mswaki, alirudi chumbani kwake na kuvaa nguo za mazoezi. Moja kwa moja alielekea katika chumba cha mazoezi, alimkuta Hannan akifanya mazoezi ya kukimbia katika mashine maalum ya kukimbilia.
“Martin yuko wapi?” Daniel alimuuliza hata kabla ya salamu.
“Hata mimi nimeshangaa sana leo, sijamkuta Martin, labda amepitiwa na usingizi” Hannan alisema huku akiendelea kufanya lile zoezi la kukimbia katika mashine. Jasho lilikuwa linamtoka ishara kwamba alianza kufanya yale mazoezi kwa muda mrefu kidogo.
“Hii sio kawaida ya Martin. Siku zote yeye huwa wa kwanza kufika katika chumba cha mazoezi, hadi sisi tunapoingia tunamkuta ameshafanya mazoezi zaidi ya saa moja. Ngoja nikamwangalie chumbani kwake.” Daniel alisema huku akitoka nje ya chumba cha mazoezi na kuelekea kilipo chumba cha Martin. Alipigwa na butwaa baada ya kugundua kwamba mlango wa chumba cha Martin ulikuwa wazi. Alipoingia ndani, hisia zake zilikuwa sahihi, kweli haikuwa kawaida ya Martin. Martin hakuwepo chumbani!.
Moja kwa moja alirudi katika chumba cha mazoezi.
“Hannan, Martin hayupo chumbani kwake!” Daniel alisema mara tu baada yakuingia katika chumba cha mazoezi.
“Acha utani Daniel, Martin hayupo chumbani kwake?, kaenda wapi? au ameenda kupumzika bustanini?” Hannan alishangaa huku akitupa maswali mfululizo kwa Daniel.
“Ni kweli, inawezekana Martin yupo bustanini, ngoja nikamwangalie” Daniel alisema na kutoka tena nje ya chumba cha mazoezi. Alienda hadi bustanini, lakini Martin hakuwepo, akatafuta kila mahala ndani na nje ya nyumba yake, lakini bado hakumwona. Hali ya uwoga ikaanza kumpanda juu ya usalama wake, na kitu cha kwanza alichofikiria kichwani kwake ni Okello. Lazima Okello anahusika na kupotea kwa Martin.
“Okello hanijui vizuri mimi!” Daniel alisema kwa ghadhabu. alikuwa ameshakasirika. Moja kwa moja alielekea tena katika chumba cha mazoezi, alimkuta Hannan akimaliza kufanya mazoezi.
“Martin hayupo sehemu zote, nina wasiwasi na Okello!” Daniel alisema kwa hasira huku akiangalia darini.
“Inawezekana ukawa sahihi, lakini ngoja tukaangalie kwenye kamera zetu, zitatuonesha wapi alipo Martin?, au kama alitoka humu ndani pia tutaona” Hannan alitoa ushauri uliokubaliwa na Daniel.
Moja kwa moja walielekea katika chumba maalum cha mawasilino. Humo kulikuwa na kompyuta nne, runinga tatu, simu za mezani mbili na vifaa mbalimbali vya mawasiliano. Hannan alikaa mbele ya kompyuta moja na kuanza kuangalia matukio yaliyotokea tangu walipoenda kulala ule usiku. Kompyuta ilionesha kila tukio, hadi ilipofika asubuhi, lakini haikuonesha chochote kile juu ya upotevu wa Martin.
“Kitu gani kimetokea? kamera za ulinzi hazijanasa chochote kuhusu Martin!” Hannan alisema kwa mshangao mkubwa.
“Twende chumbani kwa Okello” Daniel alisema huku sauti yake ikionesha kwamba alikuwa amekasirika.
Bila ya kusita Hannan alifuata nyuma kuelekea chumbani kwa Okello. Walikuta mlango wa chumba cha Okello ukiwa umefungwa kwa ndani. Daniel aligonga taratibu, lakini hakuna aliyejibu. Akagonga tena, ikawa kimya tena.
Akagonga,
Akagonga,
Akagonga huku akiliita jina la Okello, bado kulikuwa kimya. Hakukuwa na dalili zozote zile za kuitikiwa.
“Nisubiri,” Daniel alisema huku akielekea chumbani kwake. Alirudi baada ya dakika tatu na rundo la funguo mkononi. Akauchagua funguo mmoja baada ya kuchagua kati ya funguo alizobeba. Akauingiza kitasani na kuuzungusha.
Mlango ukafunguka.
Wote wawili waliingia ndani wakiwa na shauku kubwa sana ya kujua watakutana na nini mle ndani. Lakini shauku zao zilipigwa na bumbuwazi zito sana, kwani mbele yao walikuwa hawamtazami Okello, bali walikuwa wanautazama mwili wa Okello ukiwa umelala hovyo sakafuni, michirizi myembamba ya damu ilikuwa imeelekea chini ya kitanda. Dalili zote zilionesha kwamba Okello alikuwa ameuwawa!.
Daniel aliusogelea mwili wa Okello akiwa hayaamini kabisa macho yake, kwa maana na tukio hili pia hawakuliona katika kamera zao licha ya kwamba kulikuwa na kamera za siri pia katika chumba cha Okello.
“Okello ameuwawa!” Daniel alisema baada ya kuuinamia kwa karibu mwili wa Okello. Aliona alama za kunyongwa shingoni kwake na mpini wa kisu ukiwa umepotelea kifuani mwake. Huku sura ya maiti ya Okello ikionesha kuwa ilipitia katika maumivu makali sana kabla haijakata roho. Swali jipya likaibuka,
“Ni nani aliyemuua Okello ndani ya nyumba ya Daniel Mwaseba?” Hili lilikuwa swali jepesi sana lakini lenye majibu magumu na tata kuliko unavyoweza kufikiria.
“Kwanini kamera za ulinzi hazikunasa matukio haya?” Hili lilikuwa swali kutoka katika mdomo wa Hannan ambalo aliliuliza kwa nguvu. Kitu ambacho alikuwa hakijui ni kwamba yeye hakupaswa kuuliza swali hilo, yeye ndiye alipaswa kutoa majibu endapo angeulizwa na Daniel , kwakuwa yeye alikuwa ni Mchawi wa Kompyuta. Pengine kwasasa alilisahau hilo kwa kwakuwa alikuwa amechanganyikiwa.
“Hannan kuna mambo hayapo sawa, kuanzia kupotea kwa Martin, kuuwawa kwa Okello na kamera zetu kutorikodi tukio lolote kati ya hayo, hii sio kawaida. Yatupasa tuchukue hatua za haraka sana kujua ni kitu gani kimetokea?” Daniel aliuliza huku akiuangalia mwili wa Okello uliolala sakafuni.