Halfani Sudy anaandika HATARI
Mawasiliano 0652 212391
Mahali Mafinga-Iringa
“Ninaitwa John Masalu, ni mlinzi mkuu hapa, na pia ni mlinzi mkuu wa Mfalme Mrombo. Wewe hauna haja ya kujitambulisha kwangu. Tulikuwa tunajua kwamba utakuja, pia tulikuwa tunajua kwamba utapitia upande ule ndio maana tukazima taa. Ninajua unaitwa Martin Hisia. Ninajua kuwa wewe ni mpelelezi wa kujitegemea ambaye unafanya kazi zako kwa kushirikiana na kijana mpumbavu anayeitwa Daniel Mwaseba. Sasa kama wewe ni mpelelezi wa kujitegemea naamini utajitegemea leo, badala ya kila siku kumtegemea yule kijana Mpumbavu. Dakika tano zijazo, atakuja Mfalme Mrombo mbele yako, utamsikiliza kwa umakini kila atakachokwambia, narudia tena, utamsikiliza kwa umakini kila atakachokwambia na utatekeleza maagizo yake yote bila kuuliza swali. Ujue kwamba, huruhusiwi kuuliza swali lolote lile mbele ya Mfalme Mrombo. Kwa maana, hapa kuna mgawanyo wa majukumu, jukumu letu kukupa maelekezo, jukumu lako ni kutekeleza maelekezo yetu. Kinyume na hapo ni sawa na kukisaka kifo chako mwenyewe kwa makusudi!” Mrombo alisema huku akimlingishia kwa madaha bastola usoni.
Hii ni Sehemu ya Kumi na Mbili
Martin Hisia alimsikiliza John Masalu, lakini moyoni mwake alipatwa na hamu kubwa sana ya kuonana na Mrombo, ambaye yeye alijua kuwa ni ndugu yake wa damu, Nato.
“Martin, kauli ya kwanza ya Mfalme Mrombo baada ya kuvuta funda la kwanza la sigara ni amri, nakushauri itekeleze! Usipoitekeleza litakalokutokea tusilaumiane!” John Masalu alisema maneno hayo kwa msisitizo.
Hapo ndipo Martin alikumbuka hadithi za Babu Ogutu kuhusu Mrombo walipoenda kuvamia gari la abiria, na hiyo ndio ilikuwa tabia ya ndugu yake Nato, hivyo alitamani huyo Mrombo aje haraka ili amwone ndugu yake.
Mara, mlango wa kuelekea vyumbani ulifunguliwa, wale madada watatu ambao walikuwa wakimwangalia tu Martin tangu alipoingia pale sebuleni walisimama wima na kuelekea mlangoni. Mara akatoka mtu wa kwanza, alikuwa ni mzee Maloto, kisha akafuata mtu wa pili, yeye alikuwa mtu mfupi na mwenye rangi nyeusi ya kukoza. Ilichukua dakika zipatazo kumi ndipo mtu watatu alipotokea pale mlangoni. wakatu wale watu waliotoka awali Mzee Maloto na mwenzie wakiwa wamesimama kila upande wa mlango, mzee Maloto upande wa kushoto na yule ntu mfupi mwenye rangi nyeusi ya kukoza alisimama upande wa kulia wa mlango. Na mtu watatu aliyetoka ndiye alikuwa Mrombo, Mrombo Hisia!
Wale wanawake watatu walifuata nyuma ya Mrombo, wakati Mrombo akielekea kukaa sofani taratibu. Alipokaa, mwanamke mmoja alisimama upande wake wa kushoto, huku kimahaba akilichua bega lake la kushoto na yule mwanamke mwengine alikaa upande wake wa kulia wa Mrombo, naye akilichua bega lake la kulia kwa madaha, na yule mwanamke wa wtatu alisimama alisimama nyuma ya Mrombo, akiichua shingo yake.
Wakati hayo yakifanyika, kulikuwa na mshangao mkubwa sana katika sura ya Martin Hisia. Macho yake yalikuwa yamemtoka pima, mdomo wake ulibaki wazi, huku mikono yake yote miwili ikimtetemeka. Alijua kwamba, mtu alikuwa mbele yake, ndiye mtu aliyekuja kumpa maelekezo lakini yeye hakuruhusiwa kumuuliza swali. Ndio, alikuwa Mrombo Hisia lakini kwa bahati mabaya sana hakuwa mtu aliyemfikiria, hakuwa ndugu yake wa damu, hakuwa Nato. Hata kama watu hubadilika, lakini Nato asingeweza kubadilika kwa namna ile na kuwa katika umbo la Mrombo. Swali kuu lililopita katika kichwa chake ni, huyu Mrombo ni nani? Na kwanini ana tabia kama za ndugu yake Nato? Hayo maswali yalipita kichwani kwake harakaharaka lakini kumbuka alikuwa haruhusiwi kuuliza maswali, kama alivyosema John Masalu hapo awali, jukumu lake lilikuwa ni kufuata maelekezo ya Mrombo na sio kumuuliza maswali Mrombo.
“Karibu sana Martin Hisia, mbele yako, unayemwangalia kwa macho yako ni Mfalme Mrombo, Mfalme Mrombo alikuwa na shida sana na wewe ama Daniel Mwaseba, kwa bahati nzuri sana umeanza kufika wewe kabla ya Daniel Mwaseba. Najua Daniel yupo njiani kuja hapa, na utaungana naye muda si mrefu. Kuna maelekezo machache tu ambayo Mfalme Mrombo atakupa, na jukumu lako ni moja tu, kuyatekeleza, kama nilivyokwambia awali hapa hakuna nafasi ya wewe kuuliza swali” John Masalu alisema taratibu akimwangalia Martin Hisia.
“Martin….” Sauti nzito ya Mfalme Mrombo ilisema, kisha akaingiza mkono wake wa kulia kwenye mfuko wa shati, akatoa pakiti la sigara, akaligonga kwa juu na kutoa sigara moja iliyochomoza kwa juu. Alipoitoa na kuiiweka mdomoni tu, John Masalu alikuwa ameshafika na kuwasha kiberiti cha gesi, Mrombo akapiga funda la kwanza la sigara na kusema
“Washa runinga,”
John Masalu alikimbia mbio kuwahi kuiwasha runinga, runinga ikawaka, video fupi ikaanza kuonekana. Ilikuwa ni video iliyochukua dakika moja tu, ikamalizika, narudia tena, video ilichukua dakika moja tu, ikaisha, lakini ilimuuumiza sana Martin Hisia kuliko wakati wowote ule katika maisha yake.
“Nato,” Martin alishindwa kuvumilia na kujikuta akiita baada ya dakika moja ya ile video kuisha. Mashavu yake yalikuwa yameloa machozi. Mwili wote ulikuwa unamtetema kwa hasira. Mapigo yake ya moyo yalikuwa yanapiga kwa kasi kubwa sana haijawahi kutokea hapa duniani.
“Umemwona ndugu yako Nato? Nato yupo katika mateso makali sana. Yupo katika chumba cha mateso ambacho si rahisi kwa mtu wa kawaida kujua kilipo. Uhai wa ndugu yako upo mdomoni mwangu. Mimi ni Mungu wake kwasasa, nikishika simu yangu na kupiga chumba cha mateso, nikasema tu Nato afe, basi anakufa sekunde hiyohiyo. Sasa mimi sitaki uhai wa Nato uwe mdomoni mwangu, nataka uhai wa Nato uwe mikononi mwako. Nitakupa kazi, ukiitelekeza kazi hiyo, Nato aanaenda kuwa huru. Nato anatoka katika chumba cha mateso na kurudi duniani…..”
“Kwanini mmetesa ndugu yangu kiasi kile?, ni watu gani ninyi msio na huruma hata kidogo? amewafanya nini ndugu yangu?” Martin alisema huku akibubujikwa na machozi.
“Martin, wewe ni mwanaume, sijawahi kufikiria kama unaweza kumwaga chozi namna hiyo kama mtoto wa kike. Wewe ni kijana jasiri sana. Hupaswi kulia hata kidogo, kama nilivyokwambia awali, uhai wa Nato upo mikononi mwako, una nafasi ya kuchagua, Nato aishi ama afe?” Mrombo alisema kwa sauti yake ya taratibu huku akimwangalia Daniel Mwaseba.
“Una kazi ndogo tu Martin, kazi ndogo sana. Najua kwamba, wewe na Daniel Mwaseba mna nafasi ya kwenda ikulu kwa Rais Mark Mwazilindi wakati wowote ule mtakapohitaji, pia mna uwezo wa kuonana na Rais Mark Mwazilindi hata chumbani kwake. Sasa huko chumbani kwa Rais Mark Mwazilindi ndipo tunapokutaka sisi. Tutakupa kamera ya siri uende ukaiweke kwa siri chumbani kwa Rais Mark Mwazilindi. Endapo tukianza kuona picha za chumba cha Rais Mark Mwazilindi hapa sebuleni kwetu, basi ndugu yako Nato atakuwa huru” Mrombo alimwangalia kwa umakini Martin kuhakikisha kama maneno yake yamemwingia Martin.
Mrombo anampa kazi ngumu sana Martin ya kwenda kuweka kamera ya siri katika chumba cha Rais Mark Mwazilindi. Je Martin atakubali kwenda kuweka? Kwanini Mrombo anataka kamera ya siri ikawekwe katika chumba cha Rais?
LAKO JICHO!