BIBIANE -- IV
Wakati Willy anafika nyumbani kwa
Bibiane. Col. Gatabazi alikuwa
akifunguliwa lango la mbele nyumba hiyo
akatoka na kuondoka akihofia matatizo
aliyokumbana nayo kwa Luteni Biniga.
Willy alichukuwa hadhari kubwa sana
maana alichukuwa vifaa vya kazi si
mchezo. Kwa vile nyumba ya Bibiane
ilikuwa kwenye kona ya barabara mbili,
Willy alibana kwenye kona moja na
kuchungulia mbele ya nyumba na kuona
lango likifunguliwa. Alimuona mtu mmoja
akitoka na kukatisha barabara na
kuelekea kwenye uchochoro na
kutokomea. Willy alirudi nyuma kidogo na
kuhisi kuwa sehemu ile ndiyo ilikuwa
nyuma ya nyumba hii. Kwa hadhari sana
alikwea ukuta uliozungishiwa vyuma
vilivyochongoka juu. Kwa vile Col.
Rwivanga alimweleza kuhusu hilo. Willy
alikuwa amejitayarisha vizuri kabisa kwa lolote. Alikwea na kuchungulia ndani, baada ya kuangaza vizuri macho yake aliweza kuona kivuli cha mtu amebana kwenye ukuta wa nyumba hii karibu na upande wa pale alipokuwa yeye. Mtu huyu
alikuwa amebeba bunduki kubwa. Hivyo,
Willy alihisi ni mlinzi wa pale nyumbani.
Baada ya muda kidogo, Willy alimuona
mtu mwingine anakuja akitokea upande
wa mbele kuja upande huu ambao huyu
mwingine alikuwa amebana. Willy
alijining'iniza juu ya ukuta kwa nje ili asionekane huku macho yake yakiwa
usawa wa ukuta. Yule mtu alikuja moja
kwa moja mpaka usawa wa yule
mwingine alipokuwa amesimama.
"Unataka sigara?", yule aliyekuja eneo hilo
alimuuliza mwenzake.
"Sitaki, hao jamaa ndani si wamalize
mambo yao haraka ili waondoke na sisi
twende zetu, maana hapa tunapoteza
muda na huku kazi yenyewe bado", yule
wa pili ajibu.
"Mbona kama una wasiwasi, vipi
unaogopa?".
"Kwanini nisiogope, mimi si binadamu
bwana?".
"Acha woga wewe, wajuwa Kaisari
alisema watu waoga mara nyingi hufa
kabla ya tarehe ya vifo vyao kufika,
komaa mtoto wa kiume", mwenzake
alisema kwa kujiamini.
"Bwana, hebu nenda kalinde sehemu yako
na umwambie huyo Nkubana aharakishe
kutoka sehemu hii".
Baada ya kuelezwa, yule mtu aliyekuja
sehemu hii kutoka mbele aliondoka
kimyakimya kurudi kule alikotoka huku
mwenzake akimsindikiza. Willy akatumia
nafasi hiyo. Kama tumbili aliukwea ule
ukuta haraka sana. Kufumba na
kufumbua akaruka juu ya vile vyuma na
kujitosa ndani bila hata kusababisha
kishindo na kujibanza kwenye ukuta. Kwa
vile Willy alikuwa amevaa nguo nyeusi
pale alipokuwa amejibanza ilibidi
umsogelee karibu sana ndipo uweze
kumtambua maana upande huu wa
nyumba hapakuwa na mwanga. Mara
akamsikia yule mlinzi akirudi upande
wake, kutokana na mazungumzo
aliyokuwa ameyasikia alihisi hawa nao
bila shaka walikuwa kundi lilelile kama
alilopambana nalo kwa Luteni Biniga. Bila
shaka walikuwa wamekuja kwa malipo
kwa huyu mwanamke. Willy alijitayarisha
na kujibanza kwenye ukuta utafikiri
buibui. Yule mtu alikuja akinyata taratibu
utafikiri alikuwa amehisi kitu. Willy
alikuwa amebana kwenye kona kabisa ya
upande wa pili wa nyumba. Huyu mtu
alipofika hapo tu, kama Simba
anapomrukia Swala, Willy alimtia kabali
kwa nguvu zake zote. Yule mtu hakuweza
hata kuguna maana kabali ile ilikuwa kali,
na huku akitumia utaalam kumuua
kimyakimya kwa kumnyonga, Willy
alimuua yule mtu. Kisha, alimvuta mpaka
kwenye ua wa nyumba na kumvua shati,
akavua lake na kuvaa la yule mtu kwani
ukubwa wa mwili na urefu walikuwa
wanalingana. Akatwaa silaha yake ya AK
47 'Machinegun' ya Kirusi na kuelekea
mbele.
Alipofika kwenye kona ya mbele, Willy
alimuona yule mtu mwingine akichungulia
dirishani, si mbali na aliposimama Willy.
Willy alikohoa kidogo na yule mtu
akageuka kuangalia. Alionyesha ishala ya
kumwita. Na yule, akijuwa fika kuwa
alikuwa mwenzake, alikuja haraka bila
hadhari. Alipokaribia, na kwa ajili ya giza
aliamini ni yule mwenzake, alianza
kusema, "Huko ndani naona mambo
yanaa...", kabla hajamalizia sentesi yake,
Willy alimrukia na kumpiga karate ya
shingo na kumuua palepale. Alianguka
chini kwa kishindo, na Willy alipomrukia
pale chini akammaliza. Baada ya Willy
kumkagua alimkuta na Bastola mbili,
moja yenye kiwambo cha sauti na
nyingine ya kawaida. Vilevile alimkuta na
kisu ambacho ukikibonyeza kinachomoka
na kutoka urefu wa nchi tisa. Kile kisu
kilikuwa silaha hatari sana ikitokea watu
wanapigana huku mmeshikana. Willy
alijihisi mtu mwenye bahati kwani silaha
kama hii kama ingebidi kumenyana bila
kujuwa kuwa mtu anayo anakuondoa
duniani haraka sana.
Sasa Willy alikimbia mbele kuangalia
kama kulikuwa na mtu mwingine, lakini
hakukuwa na kitu. Alipozunguka upande
mwingine tena hakuna kitu. Kisha
akachukua dakika chache kuhakikisha
kuwa hakuna hatari nyingine, na
alipohakikisha ndipo alipokwenda pale
dirishani alipokuwa anachungulia yule
mtu wa pili. Dirisha lile lilikuwa sebuleni
na lilikuwa wazi kidiogo. Pazia la dirisha
lilikuwa limerudishiwa kidogo kiasi
kwamba ungeweza kuona ndani na
kusikia maneno yote yaliyokuwa
yanazungumzwa.
Willy alishangazwa kuwaona wanaume
watatu na mwanamke mmoja ambaye
mara moja alimtambua kwani alikuwa
Bibiane. Hawa wanaume wote walikuwa
wametoa Bastola zao wakizungumza na
yule mwanamke. Wawili walikuwa
wamesimama na mmoja ameketi kwenye
kiti kilichokuwa kinaangaliana uso kwa
uso na alichoketi Bibiane.
"Nakwambia hivi, sisi tumetumwa kuja
kukuua na huyo huyo bwanako Jean.
Faida yako kwake imesisha sasa wewe ni
mzigo na yeye hataki kubeba mzigo", yule
aliyeketi alimweleza yule mwanamke huku
akionyesha kwenye sura yake maudhi na
usongo wa ajabu.
"Wewe unatania. Jean! hawezi kusema
hivyo. Kwa yote niliyomtendea na jinsi
tunavyopendana, Xavier sema jingine
kama wewe na Col. Gatabazi mmeamua
kuniua basi niuweni, msimsingizie Jean,
Jean ni wangu wa kufa na kuzikana",
Bibiane alijibu huku akionyesha sura ya
hofu maana aliwajuwa hawa jamaa ni
wauaji.
"Wanawake ni watu wa ajabu. Epa", yule
mtu ambaye Bibiane alimwita Xavier
alimwita mmoja wa wale waliosimama.
"Eee", yule mtu alijibu kwa woga vilevile.
"Siku zote nakwambia wanawake ni
wajinga, wewe huamini. Huyu anafikiri eti
Jean alikuwa anampenda, Jean alikuwa
anamtumia tu kama chombo. Kwanza
alikuwa anakutumia kwa mambo yake ya
kazi zake za kumwingizia pesa na pili,
anapokuwa huku Afrika alikuwa akijisaidia
kutimiza haja zake za kimwili; hata siku
moja hajawahi kukupenda. Pale tu wewe
na Col. Gatabazi mlipomweleza kuwa
wewe umemwona Willy Gamba na Willy
Gamba kukuona mara moja alijuwa Willy
Gamba atakutafuta na akikupata utatoa
siri, na ukitoa siri si ndiyo mambo yetu
yameisha! kwa hiyo, mara moja ametoa
hukumu ya kifo kwako na sisi tumekuja
kutekeleza amri. Kwa kweli ni uhalibifu
kwa kiumbe kizuri kama wewe kuuawa,
lakini wewe sasa ni mzigo kwetu nasi
hatubebi mzigo," Xavier alieleza.
Kwa maelezo haya Bibiane alijua kweli
hukumu imetoka kwa Jean na huo ndio
ulikuwa mwisho wake. Pamoja na ujuzi
wake wote wa kupigana hakuthubutu
mbele ya Xavier na wenzake kwani
aliwajuwa vizuri, walikuwa wabaya mara
kumi yake, na alijuwa kuwa hao
hawabembelezeki hivyo, alikata tamaa na
hasira zikampanda dhidi na Jean na
machozi yakaanza kumtoka.
"Ukionana naye mwambie atakufa kifo
kibaya sana. Nami naamini kuwa huyo
Willy Gamba anayemuogopa kweli ndiye
atakayenilipia kisasi", Bibiane alisema
huku akitetemeka kwa hasira.
Xavier alisimama na kurudisha kiti chake
nyuma. Bibiane naye akataka kusimama.
"Hapana, kaa hapohapo, usilete ujanja
hapa. Huyo Willy baada ya muda si mrefu
mtaonana ahera, nasikia huko watu
huonana tena. Hamtapishana zaidi ya
masaa mawili na yeye atakuwa
marehemu kama wewe".
Willy, ambaye alikuwa anasikia na kuona
yote haya akiwa dirishani, alipoangalia
usoni mwa yule aliyeitwa Epa, akajuwa
huyu ndiye akayemuua Bibiane. Aliangalia
nafasi aliyokuwa, akajuwa angeweza
kumpiga risasi Epa na yule mwingine,
lakini si Xavier. Kwa vyovyote Xavier
angemmaliza Bibiane, lakini hakukuwa na
njia. Hawa walikuwa ni wauaji wataalam,
tena huenda wa kulipwa. Hivyo, ilikuwa ni
afadhali kwake kupambana na mmoja
kuliko watatu na kwa maajabu ya Mungu
angeweza kumponyesha Bibiane ambaye
akili yake ilimweleza kuwa angeweza
kuwa mtu muhimu kwake.
Xavier alimkonyeza Epa. Yeye akavuta kiti
na kuanza kugeuka. Bibiane akafumba
macho, lakini kabla Epa hajafyatua risasi,
palepale Willy akiwa dirishani na mikono
yake yote ikiwa na Bastola, alimpiga
risasi ya kichwa Epa na yule mwingine
kifuani, na Bibiane akajirusha nyuma ya
kiti, Nkubana kama umeme akamimina
risasi dirishani. Lakini Willy alikuwa tayari
amejitupa chini na kujiviringisha na kisha
kuchukua AK 47 akamimina risasi kama
hamsini hivi kumtia kiwewe Nkubana.
Haya mambo yote yalitokea haraka sana
kama kufumba na kufumbua. Nkubana
alipoangalia akajuwa Epa na Karekezi
walikuwa wamekufa na hakujuwa
wamezungukwa na watu wangapi.
Alijirusha kwenye dirisha upande wa pili
ambalo lilikuwa la kioo kitupu na
kuangukia nje na kisha kujiviringisha
tena. Bibiane alichukua Bastola
iliyodondoka kutoka kwa Epa na kujaribu
kumpata Xavier lakini naye alijitosa nje
akaurukia ukuta wa mbele kwa nanma ya
ajabu na kuangukia uapnde wa
barabarani. Willy alipokimbia upande ule
wa pili ili kumuwahi Nkubana alikuwa
amechelewa, Xavier naye alikuwa ndio
anaishia baada ya kuruka ule ukuta.
Bibiane alipoinuka pale alipokuwa
amejitupa kumfuata Xaviar akajikuta
anaangalia kwenye mdomo wa AK 47.
"Tupa silaha yako mama, uko chini ya
ulinzi", Willy alimweleza Bibiane.
"Aheri ya Musa kuliko ya Firauni, Bila
shaka wewe ni Willy Gamba".
"Naamini wewe ni Bibiane".
Willy alimshika mkono Bibiane na bila
hata kumwelezana wanaelekea wapi,
wakakimbia kwa tahadhari kuwa kutoka
eneo hilo kabla askari na watu wengine
hawajafika kuangalia kilichotokea hapo
kwani mlio wa risasi za Ak 47 ulikuwa
umetikisa eneo hilo na kusikika vibaya
sana wakati huo wa usiku.
ITAENDELEA COL. NI AFISA WA JESHI
MWENYE CHEO CHA KANALI