GISENYI-IV
Ilikuwa saa kumi na moja na nusu jioni,
Jeana na wenzake walipowasili kwenye
uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Goma.
Baada ya kuwasiliwa, walipokelewa na
Col. Gatabazi aliyesindikizwa na askari
wake. Jean aliwasili akiwa pamoja na
kiongozi wa Akazu, Bwana Anatoile
Kabuga, Bwana John Ngeze, ambaye ni
Mjumbe wa Baraza la Akazu, Jenerali
Kasongo, ambaye ni mshauri wa Rais wa
Zaire, Meja Karongo, Mkuu wa kikosi cha
jeshi linalomlinda Rais wa Zaire, Bwa,
George Karikutis, ambaye ni dalali wa
mamluki aliyefanya mipango yote ya
kuwawezesha Jean na wenzake wa Akazu
kupata askari wa kukodi.
Baada ya kuwasili uwanja wa ndege
walipelekwa moja kwa moja hadi Ikulu,
ambako Rais alitoa kibali Jean na
wenzake wafikie kwenye jumba hilo. Ikulu
hii ilikuwa ya kifahari sana. Ili uweze
kuelewa kwa kifupi, vyoo, bafu na vyumba
vya kulala alivyokuwa akitumia Rais
vilijengwa kwa vito vya dhahabu tupu.
Sasa naamini utakuwa umeelewa maana
yake. Karibu na Ikulu hii kulikuwa na
Jumba jingine kubwa ambalo Majemedari
wa jeshi wa ngazi za juu walikuwa
wakifikia. Ndani ya jumba hilo ambalo pia
lilikuwa la kifahari sana, ndimo alipofikia
Col. Gatabazi na wenzake. Kisha,
wakaenda kukaa kwenye sebule ya
kifahari ajabu. Wasichana warembo sana
wapatao kumi hivi walijitokeza kwa ajili
ya kutoa huduma, wakiwa wamevaa
kaputula fupi, matiti nje, yaani asilimia
tisini walikuwa uchi.
"Hivi ndivyo mzee anavyoishi hapa
duniani Jean, hapa panaweza kuwa
peponi ukitaka. Mzee ameyafanya maisha
yake hapa duniani kuwa sehemu ya
peponi. Hivyo, na wewe onja pepo kidogo
ukiwa hapa", Jenerali Kasongo
alimweleza Jean, ambaye wakati huo
alikuwa akitikisa kichwa, maana pamoja
na utajiri wake mkubwa usio kifani
alikuwa hajawahi kukalia viti na meza za
kahawa vilivyotengenezwa kwa dhahabu
tupu, ukiacha sehemu za kukaa ambazo
zilivishwa kwa ngozi ambazo hata yeye
hakuwahi kuziona kabisa duniani.
Huku wale wasichana wakiendelea
kuwahudumia, kila mmoja alikuwa
amejichagulia mrembo wa kumhudumia,
wakileta vinywaji vya kila aina
vilivyokuwa ndani ya jumba hilo. Baada
ya muda mazungumza yalianza.
"Ehe, hebu Nkubana tueleze ilikuwaje hata
huyu Willy Gamba akachafua mipango
yetu namna hii, maana inaniuma sana
kufikia hatua ya Bibiane kuwa mikononi
na mshenzi huyu. Hebu tueleze", Jean
aliuliza kwa hasira.
Huku akitetemeka Nkubana alieleza jinsi
mambo yalivyokuwa huku wote
wakimsikiliza kwa makini sana, kisha
akamalizia kwa kusema, "Tulichukua
tahadhali ya kila aina, lakini nafikiri huyu
Willy Gamba alikuwa na bahati kuliko sisi.
Katika biashara kama hii yetu, wakati
mwingine ni bahati tu inaweza
kukusaidia", Nkubana alijitetea.
"Unafikiri huyu mtu ana mipango gani
sasa?", Jenerali Kasongo aliuliza.
"Sijui, lakini naamini Bibiane anaweza
kumleta huku. Hizi ni hisia zangu, maana
Bibiane atakuwa na uchungu wa kutaka
kulipiza kisasi na siri zetu zote anazijua.
Hivyo, atataka amtumie Willy Gamba
baada ya kuona umahiri wake, alipize
kisasi", Nkubana alijibu.
"Mbona hiyo itakuwa raha, maana nitaua
ndege wawili kwa jiwe moja, Col.
Bazimaziki na Meja Massamba, moja ya
kazi zenu ni kuweka kikosi imara chenye
wapiganaji jasiri cha kuweza kuwakamata
hawa watu wawili, nataka Nkubana
akiongoze kikosi hicho, Nkubana,
ukiweza kuwakamata usiwaue hao ni
halali yangu. Nataka niwafanyie kitu
ambacho wakiwa ahera wasinisahau
milele", Jean aliamru.
"Sawa bosi", Nkubana alijibu hku Col.
Bazimaziki na Meja Massamba wakiitikia
kwa vichwa vyao.
"Ratiba ikoje?", Jean alimuuliza Col.
Gatabazi.
"Nafikiri kwanza twendeni wote
tukaangalie hali ya vikosi vyetu ilivyo,
hasa hapa Kibumba, maana mtapata
mwanga baada ya kuona jinsi
tulivyojiandaa tayari kwa vita. Tumetuma
habari kwa vikosi vyetu vingine vilivyoko
karibu na Bukavu, navyo vijiweke tayari.
Ile simu moja kati ya simu nne za Satellite
ulizoleta tuliwapelekea na sasa
tunawasiliana vizuri sana kati ya hapa na
sehemu zingine zote ambako kuna vikosi
vyetu, lakini kwa kuwa nguvu yetu kubwa
iko hapa nafikiri twende mara moja
Kibumba mkajionee wenyewe, kwani ni
kilomita thelathini tu kutoka hapa Goma.
Halafu tukirudi tutakula chakula hapa na
baadaye kidogo tutaanza mkutano wetu.
Mimi naamini kuwa mkishaona kama
nilivyoona mimi mkutano wa leo
utaruhusu tuanze uvamizi leoleo", Col.
Gatabazi alimalizia.
Wote walikubaliana naye. Kabla
hawajaondoka alichukua simu ya Satellite
akapiga simu Tanzania. Nia yake ilikuwa
kumpata JKS ili ampatie habari za wakati
ule kuhusu nyendo za Willy Gamba kama
alikuwa amezipata kutoka kwenye vyanzo
vyake vya habari. Kwa mshangao alipata
habari kutoka kwa mke wa JKS kuwa
alikuwa ameumwa ghafla na kuondoka
jioni ile Tanzania kuelekea Uingereza kwa
ajili ya matibabu. Na mama huyo alieleza
kuwa mumewe aliondoka kwa ndege ya
shirika la ndege la Uingereza. Mara moja
Jean alihisi kuna tatizo. huku akitingisha
kichwa huku wengine wakimwangalia kwa
kustaajabu, Jean aliwaambia wenzake
wote wamsubiri nje.
Walipotoka nje Jean alipiga simu zingine
tatu zilizomchukua dakika kama kumi hivi
na baada ya kuzipiga aliagua kicheko
kwa sauti mpaka askari aliyekuwa karibu
akashangaa akifikiri kuwa huyu mzungu
alianza kupata uchizi kwa kucheka peke
yake hivi. Jean alipoangalia saa yake
ilikuwa yapata saa moja na nusu jioni,
hivyo aliungana na wenzake wakaondoka
kuelekea Kibumba.
ITAENDELEA