RIWAYA : SALA YA SARAH.
.
MTUNZI : ALEX KILEO.
SEHEMU YA SITA.
ILIPOISHIA.
Siku iliyofuata ambayo ilikuwa ni jumapili, Mark alienda kanisani huku akiambatana na Sarah, uzuri ni kuwa siku hiyo hata Taita na wenzake walikuwa wamehudhuria kanisani hapo.
Wakati misa ikiwa mwishoni, ni kawaida kwa kanisa hilo itoe nafasi kwa mzee mmoja, kijana mmoja na mtoto mmoja kwa ajili ya kwenda mbele na kusali kwa niaba ya wenzake.
Alianza Mzee akaomba, akafuata kijana na nafasi ya mwisho ilimuangukia Sarah, Sarah alienda mbele ya kanisa na kuwekewa kipaza sauti mdomoni, kisha akawaomba waumini wafumbe macho, kisha kwa hisia na sauti ya kawaida kabisa, Sarah alisema,
"Mungu naomba niwe mkubwa, na niwe nawaka kama moto" Sarah alipomaliza kusema hivyo alirudisha kipaza sauti na kuacha waumini wakishangaa na wengine walicheka kabisa, ila Taita peke yake aliyekaa kiti cha mbele ndiyo alionekana ameguswa na hiyo sala ya Sarah..........
***********ENDELEA************
Taita aliinuka katika kiti hata kabla misa haijsisha na kuelekea nje, alipofika aliingia katika gari lake na kuchukua simu na kumpigia Trigger,
" uko upande gani?" Taita aliuliza baada ya simu kupokelewa,
"Niko nje ya uzio wa kanisa" Trigger alijibu,
"Njoo kwenye gari yangu" Taita aliongea kisha akakata simu.
Baada ya dakika Trigger alikuwa ndani ya gari ya Taita,
"Aisee yule Mzee wa kizungu yupo kanisani na Sarah, sasa itabidi umfuatiliea na ujue anapokaa" Taita aliongea,
"Yupo na Sarah kivipi wakati ulisema jana mlikubaliana Sarah abaki kwa babu yake?" Trigger aliuliza,
"Hilo limenishangaza, wewe fanya nilichokuagiza na mimi nitalifuatilia hilo" Taita aliongea na wakati huo na waumini wengine walianza kutoka ibadani ikiwa na maana misa imekwisha.
Taita aliweza kumshuhudia Mark akitoka ndani ya kabisa huku akiwa amemshika mkono Sarah na kuelekea kwenye gari la kifahari lilikuwa limeegeshwa eneo husika na kisha lile gari likatoka taratibu huku Taita akiliangalia,
"Imekuaje yule Mzungu yupo na Sarah?" Harry aliuliza huku akiingia ndani ya gari,
"Wamenigeuka wale wazee wapuuzi sana, ebu twende uko" Taita aliongea kisha akawasha gari na safari ilipangwa iishie kwa baba isack.
Iliwachukua takribani dakika kumi kufika nyumbani kwa Baba Isack, na bahati nzuri waliweza kuikuta na gari ya Mark ikiwa imeegeshwa nje ya ile nyumba.
"Nisubiri, nakuja" Taita aliongea na kutelemka katika gari kisha akaelekea ndani huku akionekana mwenye hasira.
Aliingia moja kwa moja sebuleni na kuwakuta baadhi ya ndugu wa marehemu Isack wakiwa wamekaa, Taita akawasalimia na kisha akakaa kwenye kochi,
"Sasa Mzee wangu imekuwaje huyu Mzungu amchukue Sarah? jana tulikubaliana nini au mmenigeuka?" Taita aliuliza maswali mfululizo huku akimtazama Baba Isack,
"Mwanangu bora umuache mtoto aende kusoma uko, kwa maana huyu bwana Mark amekuja na mikataba aliyoingia na baba Sarah kuhusu huyo mtoto na pia gharama alizotumia ni kubwa katika kushughulikia hiyo safari na shule atakayoenda kusoma uko" Baba Isack aliongea kwa upole,
"Kwa hiyo mmeuza mtoto?" Taita aliuliza,
"Hapana hajauzwa, ila baada ya masomo atarudi na utakaa nae kama unavyotaka" Mark alijibu,
"Kwani gharama ulizotumia ni shilingi ngapi?" Taita aliuliza huku akimuangalia Mark,
"Milioni mia hamsini tu" Mark alijibu,
"Nitazilipa" Taita alijibu,
"Sioni sababu ya kuingia hasara kuzilipa, muache akasome tu" Baba Isack alijibu,
"Kwa hiyo mpo upande wa huyu Mzungu?" Taita alihoji,
"Tupo upande wa mtoto, tunataka awe na maisha mazuri" Baba Isack alijibu,
"K wangu hatokuwa na maisha mazuri?" Taita aliuliza,
"Sijamaanisha hivyo, ila mimi kama babu nimependekeza mtoto akasome uko uingereza" Baba Isack aliongea na kufanya Taita ainuke na kuondoka kwa hasira na kuwaacha watu wakimshangaa.
Taita alitoka mpaka katika gari yake na kumkuta Trigger akiwa na Harry,
"Mtoto anatakiwa aende uingereza, tena safari ni kesho" Taita aliongea baada ya kuingia katika gari,
"Na wewe umekubali?" Harry aliuliza,
"Nimepinga ila watu wote ndani wanataka mtoto aende akasome uko" Taita alijibu kinyonge,
"Huyu Mzee wa kizungu anatakiwa afe leo, yeye na Sarah" Harry aliongea,
"Wanakufaje sasa?" Taita aliuliza,
"Trigger hakikisha unamfuatilia huyu Mzungu kila hatua leo mpaka upajue kwake na kisha usiku utaenda kummaliza, ni lazima atakuwa na Sarah tu" Harry aliongea,
"Hilo jambo ni zuri, ebu Trigger fanya hivyo" Taita aliongea,
"Sawa bosi" Trigger alijibu,
"Sasa sisi acha tuondoke, wewe endelea kumfuatilia huyu mzungu" Taita aliongea kisha akawasha gari na kuondoka.
Trigger aliendelea kuwepo maeneo yale, alisubiri kwa muda saa nzima na ndipo alipoweza kumuona Mark akitoka ndani huku akiwa na Sarah, walipotoka walielekea moja kwa moja katika gari na kuingia kisha wakaondoka.
Trigger akasubiri sekunde kadhaa kisha nae akaingia katika gari yake na kuanza kushika uelekeo ule ule ilipoelekea gari ya Mark.
Kwa mbali aliweza kuiona gari ya Mark. Trigger akapunguza mwendo na kuanza kuifuatilia kwa mbali ile gari ya Mark. Walitembea hivyo kwa dakika nyingi mpaka ile gari ya mark ilipoenda kuingia katika nyumba moja ndogo ila ya kisasa.
Trigger akasimamisha gari kwa mbali na kuanza kuangalia lile geti la nyumba ile na pia alikuwa anajaribu kuona kama atajua idadi ya watu wa mule ndani, kwa maana mpaka hapo alikuwa ameshajua idadi ya watu watatu ambao ni Mark, Sarah na mlinzi wa getini.
Trigger akiwa bado yupo pale akisoma mazingira, aliweza kuna gari jingine dogo la rangi nyeusi likiingia ndani ya ile nyumba, Trigger ikaendelea kusubiri, alipanga kujua kila kitu kwa muda huo ili usiku akija aje huku akiwa anajua pa kuanzia na pa kumalizia.
Baada ya masaa mawili Trigger aliweza kuna geti la ile nyumba likifunguliwa na akaiona ile gari ndogo nyeusi ikitoka na kusimama nje ya geti kisha Mark akatoka ndani ya geti na kuongea kidogo na yule dereva wa gari ambaye alikuwa ni kijana wa kizungu kisha wakaagana na ile gari ikaondoka na Mark akabaki peke yake kisha akarudi ndani na kurudishia geti.
Trigger ikaendelea kukaa pale mpaka giza lilipoanza kuingia na yeye akawa amepata kitu akitakacho, akawasha gari na kuondoka huku akijiaminisha kuwa ndani ya nyumba ile wapo watu watatu tu, ambao ni mlinzi, Mark na Sarah.
Trigger alirudi mpaka nyumbani kwa Taita na kuwakuta Taita na harry wamekaa katika bustani huku wakinywa kahawa,
"Umefanikisha?" Taita alimuuliza Trigger,
"Nimefanikisha kujua anapokaa na nimeweza kuangalia mazingira ya pale na nimeona panaingilika kirahisi tu" Trigger alijibu,
"Hakuna mlinzi hapo anapokaa?" Harry aliuliza,
"Yupo security guard mmoja tu pale getini, najua jinsi kumuingilia" Trigger alijibu,
"Inabidi hii mission ifanyike usiku wa leo" Taita aliongea,
"Tena naenda saa mbili tu" Trigger aliongea,
"Saa mbili mbona mapema?" Taita aliuliza,
.
"Ukienda usiku sana unaweza kufanya mlinzi aingie wasiwasi, inabidi niwahi ili niingie kama mgeni" Trigger alijibu,
"Utaenda peke yako au nikupe vijana wa kukuongezea nguvu?" Taita aliuliza,
"Mwenyewe tu, watu watatu hawawezi kunishinda" Trigger alijibu huku akitabasamu,
"Basi sawa, nenda kajiandae na hakikisha gari ni nzima na ina mafuta ya kutosha" Taita aliongea,
"Sawa" Trigger aliongea na kisha akaondoka zake na kuwaacha Taita na Harry wakimuangalia,
"Hili Jamaa ni jembe sana, mchezo ya kuua linaiweza sana" Harry aliongea wakati Trigger akiondoka,
"Sijui kama atafanikiwa leo, maana huyu mtoto kumuua imekuwa ngumu" Taita aliongea kivivu huku akijikuna kitambi chake.
********************
Mishale ya saa mbili usiku ilimkuta Trigger akiwa anajongea kwenye nyumba ya mark, alipofika aligonga geti na mlinzi akafungua,
"Habari yako bwana" Trigger alitoa salamu,
"Safi, nikusaidie nini?" Mlinzi aliuliza huku akimuangalia Trigger,
"Nataka nionane na boss" Trigger aliongea kwa upole,
"Una mihadi nae?" Mlinzi aliuliza,
"Ndio" Trigger alijibu huku akitabasamu,
"Ngoja nikamuulize. Unaitwa nani kwanza?" Mlinzi aliuliza,
"Mr Danny" Trigger alijibu na mlinzi akawa anaelekea ndani, ila kosa alilofanya mlinzi ni kuacha mlango wa geti ukiwa wazi,
Baada ya sekunde chache mlinzi alirudi getini na kukuta hamna mtu, akatoka nje ya geti ili kuangalia, na ndipo hapo hapo Trigger akatoka haraka kwenye kibanda cha mlinzi na kuingia sebeleni kwa Mark, akamkuta Mark akitazama runinga, Trigger akafunga mlango kwa ndani na kuchomoa bastola na kumuelekezea Mark, na muda huo huo vikasikika vishindo vya mtu akija katika mlango wa mbele,
"Boss" Sauti ya mlinzi ilisikika ikiita na Trigger akampa ishara Mark akimtaka aitike,
"Sema" Mark aliitika,
"Mtu mwenye ameondoka" Sauti ya mlinzi iliongea,
"Sawa, kuwa makini getini hapo, usiruhusu mtu kuingia" Mark alijibu,
'Sawa boss" Mlinzi alijibu na vikasikika vishindo vyake akielekea getini.
"Boss nimekuja kwa jambo moja tu, namtaka Sarah" Trigger aliongea huku akiwa amemkazia macho Mark,
"Mmewaua wazazi wake na bado mnaitaka roho yake" Mark aliongea huku akimtazama Trigger,
"Sijaja kujadiliana hapa" Trigger aliongea kwa jeuri,
"Mimi najua kila kitu, Sarah ameniambia yote" Mark aliongea kwa lengo la kumuogopesha Trigger,
"Unajua kila kitu eee? Kama nini unachokijua?" Trigger aliuliza huku akitabasamu,
"Wewe ni kibaraka tu wa Taita, nyie ndiyo mlimchoma Isack na familia yake ndani na mkamuiba mtoto wake mdogo wa kiume, Sarah anajua vyote na msidhani ni mdogo kiasi kwamba ashindwe kuwajua" Mark aliongea huku akimtupia jicho Trigger,
"Kweli unajua kila kitu, nimeridhika" Trigger aliongea na kutabasamu,
"Hakuna cha kuficha, najua kila kitu, siri zenu zote" Mark aliongea,
"Sawa unajua kila kitu, ila hujui kitu kimoja tu" Trigger aliongea na kuacha kutabasamu,
"Nini nisichokijua?" Mark aliuliza,
"Hujui kifo" Trigger aliongea na kukaza macho,
"Unamaanisha nini?" Mark alihoji huku hofu ikimshika, lakini Trigger wala hakuongea kitu, akairuhusu risasi utoke katika bastola yake na kwenda kumpiga Mark katika kichwa, Mark akafa pale pale,
"Hiyo ndiyo maana yangu" Trigger alijibu na wakati huo huo huko nje vilisikika vishindo vya mlinzi akija mbio baada ya kusikia mlio wa bunduki, kwa mawazo ya Trigger alijua mlinzi hawezi kuingia ndani kwa kuwa mlango umefungwa.
Trigger akaiweka bastola kiunoni na alikuwa anataka sasa kuanza kupekua ile nyumba amtafute Sarah, lakini ghafla alishtuka mlango umefunguliwa na mlinzi alikuwa amesimama mbele ya Trigger huku akiwa amemuelekezea bunduki,
"Weka Mikono juu muuaji wewe" Mlinzi alimwambiaTrigger huku akimuangalia boss wake Mark aliyekuwa amekaa juu ya kochi huku mwili ukiwa bila roho........
**********ITAENDELEA***********
the Legend☆