Riwaya: Sala ya Sarah

Riwaya: Sala ya Sarah

RIWAYA : SALA YA SARAH.

MTUNZI : ALEX KILEO.

SEHEMU YA NNE.

ILIPOISHIA.

Trigger akafuata maelekezo na kwenda moja kwa moja mpaka sehemu husika, alipofika alisukuma mlango na kumkuta Sarah akiwa amelala huku amefunikwa shuka zito mwilini.
Trigger akamsogelea kwa tahadhari na kumfikia, Sarah akafungua macho na kukutana na sura ya Trigger, uzuri ni kuwa alimkumbuka, Sarah akaanza kupiga kelele, Trigger akamuwahi na kumziba mdomo kwa mkono mmoja,
"Sssssssshiiii" Trigger aliongea huku akiwa ameweka kidole chake cha shaada kwenye midomo yake, alikuwa anatoa ishara ya kutaka Sarah ahache kelele, lakini Sarah aliendelea kukuruka pale kitandani, Trigger akajiona kama anapoteza muda, akachukua mikono yake na kuikamata shingo ya Sarah, Trigger akaongeza nguvu mikononi ili atimize lengo lake, alidhamiria kummaliza huyu malaika hasiye na hatia......

*********ENDELEA**********

"Mwachie mtoto na ugeuke taratibu bila usumbufu wowote" Sauti ilisikika na Trigger akaisikia vyema masikioni make, Trigger akamuachia Sarah na kugeuka huku akitabasamu na kukutanisha macho yake na mtu aliemuelekeza wodi muda mfupi uliopita, alikuwa ni yule mpelelezi na mkononi alikuwa na bastola, na muda huo huo mtoto Sarah alitoka kitandani na kukimbilia nyuma ya mpelelezi,

"Shida nini tena, mbona kuna amani tu" Trigger aliongea huku mikono ikiwa juu

"Unamjua huyu?" Mpelelezi alimuuliza Sarah,

"Ndio" Sarah alijibu,

"Kwanini asinijue wakati mimi ni baba yake mdogo?" Trigger aliuliza huku akitabasamu,

"Ni baba mdogo kweli?" Mpelelezi alimuuliza Sarah,

"Sio, huyu alikuja jana usiku nyumbani" Sarah alijibu na ubongo wa mpelelezi ukafanya kazi haraka, akahisi kabisa huyu huenda anahusika na tukio la moto,

"Nenda nje, mtafute dokta yoyote ukakae nae" Mpelelezi aliongea na kumfanya Sarah atoke mbio mbio ndani ya wodi,

"Unataka kufanya nini sasa?" Trigger aliuliza huku tabasamu likiwa bado limemkaa,

"Upo chini ya ulinzi, hutakiwi kufanya chochote, geuka nyuma na uweke mikono nyuma ya kichwa" Mpelelezi aliongea kwa amri,

"Chini ya ulinzi kivipi? Kwanza angalia kidole chako ulivyokiweka kwenye kifyatulio, hakiko sawa na nikiamua kukufanya lolote naweza" Trigger aliongea kwa dharau na kufanya mpelelezi atupie jicho kidole kilichokuwepo kwenye trigger, ilo ndilo lilikuwa kosa lake, Trigger alituka juu na kuipiga teke ile bastola, bastola ikaseleleka mpaka mlangoni, kisha kwa ufundi wa hali ya juu akaachia ngumi Kali iliyotua sawia kwenye mdomo wa mpelelezi, mpelelezi akaenda chini na kutema damu, Trigger akaona hiyo ndio nafasi ya kuiwahi bastola, wakati anaanza kukimbia, mpelelezi akamdaka mguu na kumvuta, Trigger akaenda chini na kisha akarusha teke lingine lililomkuta shingoni mpelelezi, mpelelezi akamuachia, Trigger haraka akasimama na kwenda kuichukua ile bastola na kumuelekezea mpelelezi,

"Nyanyuka" Trigger alimwambia, mpelelezi akatii huku mikono ikiwa juu,

"Unachofanya unadhani ni sahihi?" Mpelelezi alimuuliza Trigger huku mikono ikiwa juu,

"Usahihi wa mtu upo kulingana na akiwazacho" Trigger alijibu huku akitabasamu,

"Sawa, shusha silaha chini" Mpelelezi alimwambia Trigger,

"Daima Trigger akimnyooshea mtu silaha uwa haishushi silaha chini mpaka risasi itoke" Trigger aliongea na safari hii hakuwa na tabasamu tena,

"Unamaanisha nini?" Mpelelezi aliuliza lakini hakupewa jibu, Trigger alifyatua risasi ilienda moja kwa moja katika kichwa cha mpelelezi, mpelelezi akarushwa mpaka dirishani, dirisha likapasuka vioo na mpelelezi akatokea dirishani mpaka chini, aliporomoka umbali wa ghorofa saba.

"Maana yangu ni hiyo" Trigger aliongea kisha akaitupia chini ya kitanda ile bastola na kisha akatoka ndani huku akikimbia. Alijiunga na watu wengine waliokuwa wanakimbia baada ya kusikia mlio ule wa bastola, Trigger akajichanganya nao na kuanza kukimbia kama na yeye ni mmoja wao vile, njiani wakati akishuka ghorofani alipishana na askari kadhaa wenye silaha wakipandisha juu.

Trigger alikimbia mpaka chini na kwenda eneo lile lile alipoanguakia yule mpelelezi, watu walishalizunguka eneo lile, Trigger akajisogeza na kupangua watu wawili watatu na kufanikiwa kuweza kumuona mpelelezi yule, alikuwa sio mtu tena, ulikuwa ni mwili tu usio na nafsi, yaani tayari mpelelezi alikuwa ni marehemu, Trigger akatoa tabasamu dogo na kisha akaanza kupangua watu ili aweze kutoka, aliwapangua na kutoka kwenye lile kundi la watu, akaanza kuelekea nje ya geti, alitoka nje ya geti la hospitali na kusimamisha usafiri, akapanda na kupelekwa moja kwa moja mpaka nyumbani kwa Taita.

Alimkuta Taita akiwa anajiandaa na safari ya kwenda msibani,

"Nadhani umemaliza kazi" Taita aliongea huku akifungua mlango wa gari lake,

"Misheni imefeli" Trigger aliongea kwa sauti tulivu na kufanya Taita ashtuke na asitishe mpango wa kufungua mlango wa gari,

"Kipi kilichokufanya ukashindwa?" Taita aliuliza kwa ukali,

"Wakati natekeleza mpango alitokea askari mwenye silaha, ndio alinikwamisha" Trigger alijibu,

"Oooh shit, alafu nini kikafuata mpaka umerudi Salama?" Taita aliendelea na maswali,

"Nilimdhibiti yule askari, nikamuua ndipo nikafanikiwa kukimbia" Trigger alijibu,

"Safi, je mtoto hukumuona tena?" Taita alihoji,

"Sijabahatika kumuona tena, nadhani alienda kujiweka sehemu Salama zaidi" Trigger alijibu,

"Sawa, mimi naelekea msibani, nadhani wewe unapaswa kurudi kule hospital ili ukaendelee kufuatilia nyendo za mtoto" Taita aliongea huku akiingia ndani ya gari,

"Sawa, Harry yupo wapi?" Trigger aliuliza,

"Nitamkuta mbele uko, kuna sehemu ameenda" Taita alijibu,

"Safari hii inabidi niende na gari ili niwe huru zaidi" Trigger aliongea na kufanya Taita ajisachi na kutoa ufunguo wa gari na kumkabidhi Trigger,

"Chukua ile harrier nyeusi, ipo hapo mtaa wa nyuma inaoshwa, kuna tatizo jingine?" Taita aliuliza,

"Hakuna, kama litatokea tutawasiliana" Trigger aliongea kisha Taita akawasha gari na kuliondoa taratibu na kupotea eneo hilo na kumuacha Trigger akimtazama.

Taita aliendesha gari mpaka mtaa unafuatia na kumkuta harry akimsubiri hapo, akampakia kwenye gari na kisha wakaanza safari ya kwenda msibani.

Ndani ya gari Taita alimueleza Harry kila kitu kuhusu Trigger kutofanikisha mpango wa kumuua Sarah na kisha akamueleza ni kitu gani amemuagiza akakifanye.

"Hili jambo la kummaliza linatakiwa liwe la haraka, maana yule mtoto ni mkubwa na anajua kila kitu kilichotokea kuhusu wazazi wake" Harry aliongea,

"Ila nitafanikisha tu, maana nikishamchukua na kuishi nae ndipo nitamuua kirahisi" Taita aliongea,

"Hiyo usiiwaze, anaweza kutuchoma hata kabla hujamchukua, wewe fikiria kama aliweza kumtambua Trigger anashindwa vipi kukutambua wewe?" Harry aliuliza,

"Madaktari wamesema kumbukumbu zake haziko sawa" Taita aliongea,

"Upuuzi mtupu, kama kumbukumbu zake hazipo sawa amemtambuaje Trigger, ni ujinga kuendelea kufikiria hivyo" Harry aliongea huku akionekana kutofurahishwa na mawazo ya boss wake,

"Ebu ngoja tukitoka uko msibani tutapanga vizuri" Taita aliongea kwa utulivu,

"Mmh sawa" Harry aliishia kuguna tu kisha ukimya ukatawala.

Gari lilitembea kwa mwendo mrefu na atimae lilifika eneo lenye msiba. Taita aliposhuka tu, wanawake ambao walikuwa wakifahamu uhusiano wake na magreth wakaanza kuangusha kilio upya, yaani utasema wamepokea habari hizo muda huu.

"Broo unatakiwa uingie ndani moja kwa moja" Kijana mmoja aliongea sikioni kwa Taita, inaelekea huyu kijana ni ndugu wa Isack ambaye ni baba yake Sarah.

Taita akaelekea moja kwa moja sehemu aliyotakiwa na kuingia ndani ambapo aliwakuta wazazi wa Isack na ndugu wengine, Taita akawasalimia na kuoneshwa sehemu ya kukaa,

"Mbona umechelewa mwanangu?" Baba Isack alimuuliza,

"Asubuhi niliamkia hospitali ili nikamuangalie Sarah hali yake ipoje" Taita akajitetea,

"Vizuri, anaendeleaje mjukuu wangu?"Baba Isack aliuliza,

"Mzima kabisa, kesho anaweza kuruhusiwa, nitamchukua na kuishi nae" Taita alijibu,

"Na yule mwingine mdogo yeye ndio ameteketea kabisa kawa majivu" Baba isack aliongea kwa uchungu,

"Dah, ni mipango ya Mungu" Taita alijibu,

"Sasa hapa sisi tumeshapanga maziko, tumeamua kupanga mapema baada ya kukusubiri muda mrefu na hukutokea, kwa hiyo hapa tunachongoja kutoka kwako ni kuridhia na kubariki mipango yetu" Baba Isack alizungumza na kumtupia jicho Taita,.

"Mmepanga yafanyike lini?" Taita aliuliza,

"Leo hii saa kumi" Baba Isack alijibu,

"Kwanini tusimsubiri mtoto aruhusiwe hospitali hili naye ashiriki maziko ya wazazi wake?" Taita aliuliza,

"Hata sisi tulitaka iwe hivyo, ila kwa jinsi ile miili ilivyoharibika, ni ngumu sana kuacha mpaka kesho" Baba Isack alijibu

"Sawa, mimi nimeridhia" Taita aliongea kwa upole,

"Nashukuru sana kijana wangu, nadhani cha muhimu ni kwenda tu monchwari kuisafisha miili ili mpaka saa saba iwe imefika hapa na mipango ya kuaga miili ianze" Baba Isack alizungumza na watu kadhaa wakamuunga mkono, kisha wakatoka baadhi ya ndugu wa marehemu wakiambatana na Taita na wakaelekea hospitali kwa ajili ya kuitayarisha miili ya marehemu.

*********************

Trigger alikuwa ameegesha gari lake ndani ya uzio wa hospitali huku akijaribu kuyasoma mazingira ya pale vizuri. Wakati akiwa bado anapiga hesabu zake ndipo alipomuona daktari akiwa ameongozana na Sarah na mwanaume wa makamo ambaye ni Mzungu. Trigger akayaweka macho yake umakini mkubwa, akaweza kuona daktari akitoa maelezo kwa yule Mzee wa kizungu, ila Trigger hakuweza kusikia neno lolote kwa kuwa alikuwa mbali kidogo.

Trigger aliendelea kushuhudia daktari akiongea na yule Mzee Mzungu na kisha akaona wakipeana mikono, alafu yule Mzee wa kizungu akaondoka huku akiwa ameongozana na Sarah na kuingia kwenye gari moja la kifahari, kisha ile gari ikaondoka kwa mwendo wa taratibu.

Baada ya lile gari kutoka nje ya geti, Trigger nae aliondoa gari lake na kuanza kuifuata ile gari huku akiwa anaangalia namna ya kupanga mashambulizi ya kummaliza Sarah.

Zile gari ziliendelea kufuatana huku zikiwa zimeachana umbali kidogo, walipofika eneo ambalo kulikuwa na pori kidogo, Trigger akaongeza mwendo na kuipita kabisa ile gari ya Mzee wa kizungu, tena akaiacha mbali kiasi kwamba hakuiona, alifanya hivyo makusudi baada ya kutengeneza mipango yake.

Trigger alienda na kusimamisha gari pembeni ya barabara, akashuka na kuanza kusubiri. Baada ya dakika tano ilitokea ile gari ya Mzee wa kizungu na Trigger akajifanya kama anatengeneza gari lake, yaani aliigiza gari lake limeharibika.

Gari la Mzee wa kizungu lilipomkaribia Trigger akalipiga mkono na likasimama pembeni ya barabara, Trigger akatazama kioo cha mbele kwa jicho la chini ili aone watu waliomo ndani ya gari, akamuona ni yule Mzee wa kizungu na Sarah tu, akajikuta anatabasamu na kuishusha kofia yake chini zaidi ili Sarah asimtambue.

Trigger akawa anasogea katika gari ya yule Mzee wa kizungu,

"Samahani Mzee gari yangu imeniharibikia, naomba msaada" Trigger aliongea huku akiwa amesimama katika dirisha la gari.

"Unataka msaada gani sasa?" Mzee wa kizungu aliuliza,

"Nataka maji, nahisi rejeta imeisha maji" Trigger aliongea huku mkono wake ukianza kuivuta bastola ndogo iliyopo kiunoni upande wa nyuma, Trigger mtu mbaya alidhamiria kuua, na kawaida yake ni kwamba akikunyooshea bastola uwa haishushi mpaka itoe risasi.......

*********ITAENDELEA**********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH.

.
MTUNZI : ALEX KILEO.

SEHEMU YA TANO

.

.

ILIPOISHIA.

Trigger alienda na kusimamisha gari pembeni ya barabara, akashuka na kuanza kusubiri. Baada ya dakika tano ilitokea ile gari ya Mzee wa kizungu na Trigger akajifanya kama anatengeneza gari lake, yaani aliigiza gari lake limeharibika.
Gari la Mzee wa kizungu lilipomkaribia Trigger akalipiga mkono na likasimama pembeni ya barabara, Trigger akatazama kioo cha mbele kwa jicho la chini ili aone watu waliomo ndani ya gari, akamuona ni yule Mzee wa kizungu na Sarah tu, akajikuta anatabasamu na kuishusha kofia yake chini zaidi ili Sarah asimtambue.
Trigger akawa anasogea katika gari ya yule Mzee wa kizungu,
"Samahani Mzee gari yangu imeniharibikia, naomba msaada" Trigger aliongea huku akiwa amesimama katika dirisha la gari.
"Unataka msaada gani sasa?" Mzee wa kizungu aliuliza,
"Nataka maji, nahisi rejeta imeisha maji" Trigger aliongea huku mkono wake ukianza kuivuta bastola ndogo iliyopo kiunoni upande wa nyuma, Trigger mtu mbaya alidhamiria kuua, na kawaida yake ni kwamba akikunyooshea bastola uwa haishushi mpaka itoe risasi.......

*********ENDELEA**********

"Rejeta imechemka sio?" Mzee wa kizungu aliuliza huku akifungua mlango wa gari na kipindi hicho hicho kulikuwa na gari ya polisi ikija eneo hilo na kufanya Trigger ahache kufanya alichotaka,

"Ngoja nikupe maji kijana, uwa natembea na maji ya kutosha" Mzee wa kizungu aliongea huku akifungua mlango wa nyuma wa gari na kuchukua chupa moja ya maji ya dukani na kumpatia Trigger na kipindi hicho lile gari la polisi lilikuja na kusimama hapo hapo.

"Vipi Mzee kuna usalama?" Polisi mmoja aliuliza huku akimtazama yule Mzee wa kizungu,

"Hapa kuko Salama, huonekani siku hizi" Mzee wa kizungu alijibu na kuonesha kuwa anafahamiana sana na yule polisi,

"Hili eneo sio zuri, tulidhani umepata tatizo mheshimiwa" Polisi yule alizungumza,

"Msipate shida, nilikuwa namsaidia kijana maji, gari yake imemuhishia maji, hata hivyo nimemaliza tayari" Mzee wa kizungu aliongea huku akiingia kwenye gari lake na kisha akaagana na polisi na kuliondoa gari taratibu, na polisi nao hawakuwa na kitu cha ziada, nao wakaondoa gari lao na kufuata uelekeo ule ule alioenda nao yule Mzee wa kizungu.

Akabaki Trigger akiwa ameinamia injini ya gari lake huku pia akiwatizama polisi kwa jicho la chini chini wakati polisi hao wakiondoka.

"Mbona amenitoka kipumbavu hivi?" Trigger alijiuliza huku akifunga boneti ya gari lake na kuifungua ile chupa ya maji na kunywa yale maji mpaka yalipofika nusu chupa, akauendea mlango wa gari na kuufungua kisha akaingia, akawasha gari na kutulia huku akionekana kuna kitu anafikiria,

"Bado nina nafasi, ngoja nijaribu kuifuata njia aliyoondoka nayo, naweza kumuona" Trigger aliongea peke yake kisha akaiingiza gari barabarani na kuishika ile njia aliyoelekea yule Mzee wa kizungu.

Baada ya dakika tano Trigger aliweza kuliona kwa mbali gari la yule Mzee wa kizungu, Trigger akaongeza mwendo na kulisogelea ingawa sio kwa karibu sana.

Na pia trigger alishindwa kufanya kitu eneo hilo kutokana na eneo kuwa na watu na pia msongamano wa magari tofauti na lile eneo la kichakani ambalo alishindwa kutimiza adhma yake.

Trigger aliendelea kulifuatilia lile gari huku sasa dhamira yake ikimtuma kuwa huenda yule Mzee wa kizungu anaenda nyumbani kwake, akapanga atamfanyia shambulio Sarah endapo hiyo gari itasimama nje ya nyumba ya huyo mzee wa kizungu.

Trigger akaishuhudia ile gari ikikunja kushoto ambapo barabara haikuwa na lami, na yeye Trigger akakunja kisha ile gari ikanyooka na njia ile mpaka katika nyumba moja ambayo magari yalikuwa yameegeshwa mengi nje ya ile nyumba na pia kulionekana watu wamejaa, ni eneo ambao kulionekana na msiba. Kitu kilichomshtua Trigger ni kuikuta na gari ya Taita, hapo sasa akajua kuwa ametokezea msibani, nyumbani kwa baba yake Isack ambaye ndiye babu yake na Sarah.

."Huyu mtoto ana nini?" Trigger alijiuliza kwa hasira huku akiuma meno baada ya kumkosa Sarah kwa Mara nyingine tena.

Na wakati huo Sarah alikuwa anashushwa kwenye gari na yule Mzee wa kizungu, Sarah alipotelemka tu na vilio vya kinamama vikaanza upya, kila mmoja alilia kwa uchungu huku wakimtazama Sarah, bahati mbaya Sarah wala hakuonekana kujali, sijui ni kutokana na utoto wake au alihisi uchungu ila hakujua namna ya kuufikisha kwa hadhira.

Trigger hakuwa na sababu ya kutoka eneo hilo, aliona bora aendelee kuwepo na isitoshe aliliona gari la bosi wake hapo, akaamini kabisa Taita atakuwepo hapo. Trigger akatelemka ndani ya gari na kwenda kuliegemea gari la Taita huku akiitoa simu yake mfukoni na kuanza kuicheza game.

*******************

Mzee wa kizungu aliposhuka na Sarah alielekea moja kwa moja kwa moja ndani ambapo aliwakuta watu wengine wapo huko baada ya kutoka kuichukua miili ya marehemu hospitali. Mzee wa kizungu alipofika aliwasalimia na kukaa juu ya kochi.

Huyu Mzee anaitwa Mark McFadden, ni boss wa Isack ambaye ni baba yake Sarah, ni mtu aliyekuwa anampenda sana Isack kutokana na utendaji wake wa kazi, na hata Isack alipokatika miguu kutokana na ajali aliyopata wakati akiwa katika shughuli za kikazi, bado aliendelea kupokea mshahara wake ingawa alikuwa haendi tena kazini, na huyu Mzee alikuwa karibu sana na familia ya marehemu Isack na kila mwisho wa wiki alikuwa anajumuika na familia hii. Mark ni raia wa uingereza na familia yake ipo huko, hapa Tanzania kuweka tu tawi la kampuni yake ambayo inajihusisha na mambo ya kusafirisha mizigo kutoka nchi mbalimbali.

Baada ya Mark kukaa, Sarah alikimbilia kwa babu yake, na muda wote alikuwa anamtupia jicho Taita, na kila wakikutanisha macho na Mjomba wake huyo, Sarah alikimbilia mgongoni kwa babu yake, hiyo hali ilizidi kumuongezea hofu Taita, ila uzuri ni kuwa hakuna aliyeona kitu kilichokuwa kinaendelea isipokuwa Mark pekee ambaye muda wote macho yake yalikuwa kwa Sarah.

"Na huyu ni nani?" Taita aliuliza huku akimuangalia Mark,

"Huyu ndiye bosi wa Isack baba yake Sarah" Baba Isack alijibu,

"Naitwa Mark" Mark aliongea na kunyanyuka na kewnda kumpa mkono Taita,

"Sawa" Taita alijibu huku nae akipeana mikono na Mark.

"Nadhani sasa ni wakati wa kuitoa miili ya marehemu ili watu waage tayari kwa maziko" Baba Isack aliongea,

"Waage vipi tena? Mzee huoni miili ilivyoharibika vile kwa moto?, mi naona tukazike tu" Mdogo ake Isack aliongea,

"Kweli, mimi nadhani ikazikwe tu, ile miili haifai watu waione, maana inatisha sana" Taita aliunga mkono,

"Basi sawa, nadhani mkawaambie watu wajitayarishe uko nje, baada ya dakika kumi tutaelekea kuipumzisha miili ya wapendwa wetu" Baba Isack aliongea na kisha Mzee mmoja wa makamo akaelekea nje kuyafikisha maneno hayo kwa watu waliohudhuria hapo msibani.

Baada ya robo saa majeneza yalitolewa nje na kupakiwa katika gari, safari ya kwenda kuwapumzisha ikaanza.

Makaburi haya kuwa mbali sana, iliwachukua dakika tano kufika makaburini na shughuli nyingine za maziko zikaanza, wapo waliozimia baada ya kushuhudia majeneza yale yakifukiwa na udongo na wapo waliolia sana, basi ilikuwa ni huzuni mkubwa miongoni mwa ndugu, Jamaa na marafiki.

Baada ya muda mrefu kidogo ule msafara ulikuwa umeshamaliza kuwazika wapendwa wao na sasa walikuwa wanarudi nyumbani, iliwachukua chache kufika nyumbani na baadhi ya watu walitawanyika baada ya maziko, kwa hiyo walibaki watu wachache tofauti na mwanzo.

Ndani ya nyumba walikuwepo ndugu na watu wa karibu wa familia, kulikuwa na majadiliano,

"Jamani najua dunia ya sasa hivi ilivyo ya pilika pilika ni ngumu sana kama tukisema tusubiri mpaka siku ya tatu ndio tujadili hili suala, naona tujadili muda huu tukiwa tumekamalika hapa, tujadili mustakali wa Sarah pamoja na mali zake" Baba Isack aliongea na kuwatazama wanandugu,

"Suala la Sarah lisikuumize kichwa, nitaishi nae mimi" Taita aliongea kwa kujiamini,

"Huyu mtoto tayari anatakiwa nisafiri nae niende nae uingereza, kabla baba yake hajafa tulishaongea nae hilo na akakubali na hivi ninavyoongea na nyinyi tayari tulishamuombea nafasi ya masomo na amekubaliwa, baadhi ya fomu tumeshajaza na gharama pia nimetumia, jumatatu anatakiwa asafiri kwa ajili ya hilo" Mark aliongea kwa unyenyekevu,

"Hilo haliwezekani, kwanza unaongea kama nani? wewe sio ndugu ni rafiki tu wa familia" Taita aliongea kwa jazba,

"Ila ameongea jambo zuri, suala la masomo ni kitu vizuri, mimi ningeshauri umkubalie tu aende uko uingereza akasome" Baba Isack aliongea kwa kusihi huku akimuangalia Sarah,

"Swali ni kwamba yeye amchukue Sarah kama nani?" Taita aliuliza kwa ukali,

"Basi silazimishi kumchukua, kama mnaona ni sawa kubaki nae haya" Mark aliongea huku akilazimisha tabasamu,

"Ila shemeji, ni bora mtoto aende kusoma uko uingereza, si unajua elimu za wenzetu zipo juu kidogo" Mdogo wake Isack aliongea,

"Kwani shemeji mimi siwezi kumsomesha huyu mtoto uingereza?" Taita aliuliza huku akimtazama shemeji yake huyo,

"Sikuwa na maana hiyo, ila kama inawezekana kumsomesha uko sawa" Mdogo wake Isack aliongea kwa upole,

"Sawa tunefikia makubaliano kuhusu hilo, mtoto ataondoka na Mjomba wake. Je na vipi kuhusu mali za marehemu mama yake?" Baba Isack aliuliza huku akimtazama Taita,

"Zipo zote, uzuri ni kwamba kila kitu kupo wazi na uzuri zaidi ni kwamba mwanasheria wa mama yake nae ana ushahidi" Taita aliongea huku akitabasamu,

"Sawa, tutaongea na mwanasheria wa mama yake" Baba Isack aliongea,

"Na vipi kuhusu Mali zake, ambazo zimeachwa na wazazi wake kwa ujumla?" Taita aliuliza,

"Zipo Salama, na makabrasha yote yenye kuelezea mali ziliachwa na familia yake, ninayo" Mark aliongea huku akiweka mkoba ulioonekana una makaratasi,

"Huu mkoba utabaki hapa" Baba Isack aliongea huku akiuangalia ule mkoba,

"Huu nimeuleta ili mkae nao" Mark aliongea huku akitabasamu,

"Sasa nadhani vya muhimu vyote tumevimaliza, kikao kiishe na hivyo vilivyobaki tutaongea siku nyingine" Baba Isack aliongea,

"Sawa, naomba niondoke sasa" Taita aliongea huku akisimama,

"Nenda na mwanao, au unamuacha kwanza nikae nae?" Baba Isack aliongea huku akitabasamu,

"Naenda nae" Taita aliongea na kumuita Sarah, cha ajabu Sarah alimkataa kabisa, yaani kila Taita alipomuita, Sarah alikimbilia nyuma ya mgongo wa babu yake. Walimbeleza na wakatumia ukali lakini mtoto alikataa, Taita akatumia ubabe akambeba, Sarah alipiga kelele ikabidi babu yake amwambie Taita amuache,

"Utakuja kumchukua kesho" Baba Isack aliongea baada ya Sarah kushushwa na kukimbilia mapajani kwa Mark,

"Sawa" Taita aliongea na kuondoka huku akijilaumu kumkosa Sarah, Taita akaenda nje na kukutana na wenzake kisha wakaondoka.

Mark nae akaona aondoke, ila Sarah akawa anamlilia, mwisho wakamruhusu aende nae kwa makubaliano ya kumrudisha siku itakayofuta ambayo itakuwa jumapili.

Mark akaondoka na Sarah.

*****************

Siku iliyofuata ambayo ilikuwa ni jumapili, Mark alienda kanisani huku akiambatana na Sarah, uzuri ni kuwa siku hiyo hata Taita na wenzake walikuwa wamehudhuria kanisani hapo.

Wakati misa ikiwa mwishoni, ni kawaida kwa kanisa hilo itoe nafasi kwa mzee mmoja, kijana mmoja na mtoto mmoja kwa ajili ya kwenda mbele na kusali kwa niaba ya wenzake.

Alianza Mzee akaomba, akafuata kijana na nafasi ya mwisho ilimuangukia Sarah, Sarah alienda mbele ya kanisa na kuwekewa kipaza sauti mdomoni, kisha akawaomba waumini wafumbe macho, kisha kwa hisia na sauti ya kawaida kabisa, Sarah alisema,

"Mungu naomba niwe mkubwa, na niwe nawaka kama moto" Sarah alipomaliza kusema hivyo alirudisha kipaza sauti na kuacha waumini wakishangaa na wengine walicheka kabisa, ila Taita peke yake aliyekaa kiti cha mbele ndiyo alionekana ameguswa na hiyo sala ya Sarah..........

*********ITAENDELEA**********

the Legend☆
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom