Riwaya: Sala ya Sarah

Riwaya: Sala ya Sarah

RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA SITINI NA TISA.

ENDELEA..................

Taita alienda mpaka hospitali na kwenda katika wodi aliyolazwa mlinzi wake wa getini, alimkuta tayari fahamu zimemrejea,

"ni nani aliyekuwa ndani ya nyumba kabla nyumba haijawaka moto?" Taita aliuliza moja kwa moja bila hata kumjulia hali mlinzi,

"nyumba haijawaka moto?, nyumba ipi?" Mlinzi aliuliza kwa maana wakati nyumba

ikiungua yeye alikuwa amepoteza fahamu kwa hiyo hakuna anachojua,

"wewe vipi?, hujui kuwa nyumba imeungua?" Taita aliuliza kwa hasira,

"mzee mimi nilipigwa na mwanamke ambaye simjui, nikspoteza fahamu, kwa hiyo sijui kitu kingine kilichoendelea" Mlinzi wa getini alijibu na kumfanya Taita ajiulize huyo mwanamke ni nani?

"huyo mwanamke yupoje?" Taita aliuliza,

"ana mwili wa wastani, ana nywele ndefu na ni mweusi" Mlinzi alijibu na kumfanya Taita ajiulize huyo mtu ni nani? Kwa maana Sarah hayupo hivyo, Sarah ni mwenye kiasi na mwili wake ni mwembamba,

"sasa huyo mwanamke alikuwa anataka nini? Au alikupiga tu bila sababu?" Taita aliuliza,

"alikuwa anamuulizia Trigger, na Trigger alinizuia nisiruhusu mtu aingie ndani, kwa hiyo nikagoma kumruhusu huyo mwanamke kuingia, ndio akanipiga" Mlinzi alijibu,

"Trigger alikuwa ndani?" Taita aliuliza kwa wasiwasi,

"ndio, alikuwa na wanaume watatu ambao alikuwa amewateka" Mlinzi alijibu na kumfanya Taita achanfanyikiwe, maana alizidi kuvurugwa na asijue ni nani aliyeungua,

"wapoje hao wanaume?" Taita aliuliza,

"mzee mmoja na vijana wawili" Mlinzi alijibu na kumfanya Taita ageuke na kuondoka, maana aliona mlinzi anamvuruga tu.

*************

Sajenti Minja fahamu zilipomrudia, sehemu ya kwanza aliyofikiria kwenda ni katika kambi ya Taita, maana hali aliyoiacha haikuwa hali salama.

Sajenti Minja alisimamisha boda boda iliyomchukua mpaka eneo lile la kambi ya Taita, aliukuta umati wa watu ukiwa unatawanyika baada ya moto kuwa umezimika, hata kikosi cha zimamoto hakukikuta, kilikuwa kimeshaondoka, kilichomshangaza Sajenti Minja ni Kukuta ile nyumba ikiwa imeteketea kabisa wakati yeye aliiacha ikiwa nzima kabisa, sasa swali alilojiuliza ni ule moto ni wa kuwashwa na mtu au umetokea bahati mbaya?

"aisee ndani ya nyumba kulikuwa na mtu kweli?" Sajenti Minja alimuuliza dada mmoja aliyekuwa jirani nae,

"wameukuta mwili wa mtu" Yule dada alijibu kwa huzuni,

"mwanamke au mwanaume?" Sajenti Minja aliuliza,

"wameukuta wa mwanaume" yule dada alijibu na kumfanya Sajenti Minja ahisi huenda Sarah ameamua kumchoma moto Trigger.

Sajenti Minja akatoka pale na moja kwa moja akaenda kwa Dokta Innocent Malle, akamkuta akiwa na Kijana wake, Sajenti Minja akawajulisha wanatakiwa wahame pale kwa muda kwa ajili ya usalama wao. Kisha Sajenti Minja akachukua gari yake na kwenda moja kwa moja nyumbani kwa Taita, akaingia moja kwa moja mpaka ndani na kumkuta Vin akiwa amekaa sebuleni huku akiwa bize kubonyeza simu,

"mzee yupo wapi?" Sajenti Minja aliuliza baada ya kuingia,

"ametoka, vipi?" Vin aliuliza,

"mzee nadhani yupo hatarini, muda wowote Sarah anaweza kumdhuru" Sajenti Minja aliongea,

"kwanini unasema hivyo?" Vin aliuliza,

"Sarah ametoka kumuua Trigger muda si mrefu, tena kile ni kifo kibaya" Sajenti Minja aliongea kwa masikitiko,..

.
.
..

"mzee nampigia hapokei simu, ila sitokubali Sarah amuue, nitamlinda mzee kwa nguvu zote, yule ni baba yangu hata kama sio wa halali" Vin aliongea kwa ukali,

"ila mimi hapa nimekuja kumkamata mzee wako, kwa maana baada ya kufuatilia kila kitu kuhusu vifo vya wazazi wako na Sarah nadhani nimeshakusanya ushahidi wa kutosha wa kumtia hatiani mzee wako" Sajenti Minja aliongea,

"hapana, hiyo kesi si inanihusu mimi kama mwenye wazazi waliouawa? Basi nasema nimemsamehe Taita, sitaki umkamate" Vin aliongea kwa ukali,

"usichukulie hasira, hii kesi ilifunguliwa na familia ya baba yenu, kwa hiyo mwenye uwezo wa kuifunga hii kesi ni babu yenu tu, pia nadhani endapo nitamkamata Taita, itakuwa salama kwake kwa kuwa kukaa kwake urahiani ni kukaa karibu na kifo, kwa maana inakuwa rahisi kwa Sarah kumfikia" Sajenti Minja alijaribu kumueleza Vin,

"hapana, usitumie kigezo hicho kumtia hatiani mzee wangu" Vin aliongea kwa kujiamini, na kipindi hicho Taita alikuwa amerudi na amekaa nyuma ya mlango akisikiliza maongezi kati ya Vin na Sajenti Minja.

"usibishane na sheria wewe, na hakuna mtu ambaye yupo juu ya sheria, Taita lazima nimkamate na akajibu mashtaka" Sajenti Minja aliongea kwa kujiamini pia,

"kwa ushahidi Upi?" Vin alihoji,

"ngoja nikujibu kwa kifupi tu, Sarah amenipa ushahidi wa maneno yote aliyoongea Harry kabla hajafa, pia kuna mtu anaitwa Strategic, amenipa maongezi yake na Trigger, aliyarekodi kupitia lap top yako, pia leo muda mfupi kabla Trigger hajafa, aliongea ukweli wote wakati akiwa ametuteka'" Sajenti Minja aliongea na kumfanya Vin achoke,

"Strategic nae amekupa ushahidi? Mbwa wangu mwenyewe leo amening'ata?" Vin aliongea kwa upole na wakati huo sasa Taita aliamua ajitokeze sebuleni,

"Trigger amekufa? Au nimesikia vibaya?" Taita aliuliza huku akimtazama Sajenti Minja,

"ndio amekufa, na wewe upo hatarini pia" Sajenti Minja alijibu,

"mzee ebu ondoka nchini, ikiwezekana chukua hata ndege ya kukodi muda huu" Vin alimwambia Taita,

"hiyo haiwezekani, mzee upo chini ya ulinzi" Sajenti Minja aliongea huku akimuangalia Taita,

"kwa kosa gani?" Taita aliuliza kwa dharau,

'"kwa mauaji yaliyotokea miaka ishirini iliyopita, uliua familia ya Isack kwa kuiteketeza na moto" Sajenti Minja aliongea,

"mzee, huyu anatuvuruga tu, mzee ingia ndani uangalie vitu muhimu na uondoke haraka, hii nchi haifai tena" Vin aliongea kwa msisitizo na kufanya Taita aanze kwenda chumbani kuchukua vitu vyake muhimu,

"simama mzee" Sajenti Minja aliongea huku akiichomoa bastola yake na kumuelekezea Taita, Vin akaona akifanya uzembe mzee wake atakamatwa, Vin akarusha teke nw kumpiga Sajenti Minja, Sajenti Minja akapepesuka, kisha Vin akaokota mto wa kochi na kuurusha kuelekea kwenye mkono wa Sajenti Minja, mto ukaipiga ile bastola na kudondoka chini, Vin akachomoa bastola yake na kumuelekezea Sajenti Minja,

"mzee harakisha uondoke" Vin aliongea baada ya kumzidi ujanja Sajenti Minja.

Taita akaingia chumbani na kisha alirudi sebuleni baada ya muda mchache huku mkononi akiwa na begi dogo,

"Vin mwanangu tuondoke" Taita aliongea huku akimtazama Vin,

"mzee wewe nenda, kwa hali ilivyo hapa, nikishusha bastola chini utakamatwa" Vin alimwambia Taita,

"mpige risasi huyo ili tuondoke, sitaki nikuache mwanangu" Taita aliongea kwa upole.

"hapana mzee, siwezi kumpiga risasi, cha muhimu wahi kuondoka na uende mbali, ukifika nitaharifu" Vin aliongea ila Taita aliweka msimamo waondoke wote, Vin alimbembeleza na mwisho Taita akakubali kuondoka, alimsogelea Vin na kumbusu katika paji la uso wake, kisha akageuka na kuanza kuondoka,

"mzee, ondoka peke yako, usimuamini mtu yoyote, hata Strategic" Vin alimsisitizia Taita ambaye aliitikia kwa kichwa na kisha akageuka na kutoka nje, sebuleni akawaacha Sajenti Minja ambaye alikuwa mateka wa Vin.

"elewa kuwa hili unalofanya ni kosa, unamsaidia muharifu kutoroka" Sajenti Minja alimwambia Vin ambaye alikuwa ametulia na bastola yake mkononi,

"sawa, acha nifanye kosa kwa ajili ya kumsaidia mtu anayenipenda" Vin alijibu na kumfanya Sajenti Minja acheke.

Baada ya nusu saa ya kumshikia bastola Sajenti Minja, Vin aliamini baba yake atakuwa ameshaondoka na kufika mbali, Vin akateremsha bastola na kuitupa chini, kisha akanyoosha mikono juu kujisalimisha kwa Sajenti Minja.

Sajenti Minja akashangaa, ila kwa haraka akamkimbilia bastola na kuikota, kisha akamfuata Vin na kumfunga pingu, kisha akaanza kutoka nae nje.

Alivyotoka nje, Sajenti Minja akatoa simu mfukoni na kumpigia Sarah, aliona huyo ndio mtu mzuri ambaye anaweza kumsadia kumkamata Taita kwa muda huo.

Sajenti Minja akatoa akapiga simu,

"sarah naomba unisikie kwa umakini mkubwa, nina ushahidi wa kutosha wa kumtia hatiani Taita, sasa basi hapa nipo kwake, Taita amenitoroka na nahisi ameelekea uwanja wa ndege, fanya ukamuangalie na ukimpata nitaharifu, usimfanye chohote" Sajenti Minja aliongea kwa kusihi,

"kama mmeamua kumfungulia kesi sawa, ngoja niende kumuangalia" Sarah aliongea kwa utulivu na kukata simu.

Muda huo wa jioni ndio muda ambao Sarah alikuwa amefika nyumbani kwake kutoka katika kambi ya Taita. Baada ya Sarah kupokea taharifa hizo kutoka kwa Sajenti Minja, alichofanya ni kuingia ndani na kubadili nguo, alivaa suruali nyeusi na koti jeusi la kike, kisha ile mask yake akaitia ndani ya mfuko wa koti, kisha akamuaga Dokta Pendo na babu yake na kuondoka zake huku akifurahi kitendo cha Sajenti Minja kuamua kumfungulia kesi Taita, aliamini haki itatendeka.

Ilimchukua muda mchache tu kwa Sarah kufika nje ya majengo ya Kiwanja cha ndege, aliamua kutumia usafiri wa boda boda kwa maana ndio ulikuwa wa haraka. Sarah alivyofika nje aliangaza kila upande aone kama anaweza kuiona gari yoyote ya Taita, kwa maana alikariri asilimia tisini ya magari ya Taita. Baada ya kuangalia kwa muda, hakuweza kuona gari katika eneo hilo.

Sarah hakuwa na uhakika kama ni kweli Taita anaweza kuwa yupo au hayupo, mwisho akajiaminisha huenda Taita labda alikuja na gari nyingine ambayo Sarah haijui, Sarah akaamua aingie ndani ya jengo huku akiamini labda Taita yupo ndani, ila wakati akiinua mguu ili aanze kuelekea ndani, alishuhudia gari ya Taita ikiegeshwa, Sarah akasita na kuanza kuifuata kwa kujificha ficha, na kwa kuwa giza lilikuwa linaanza kushika kasi, haikuwa rahisi kwa Taita kumtambua Sarah kwa urahisi.

Taita akafungua mlango, akashuka na begi lake, mara ghafla akawekewa bastola kichwani na Sarah,

"rudi ndani ya gari mjomba" Sarah aliongea huku akimuangalia, Taita akataka kupiga kelele, Sarah akamuwahi kwa kumpiga ngumi kali ya kisogo, Taita akalegea na kuanguka, Sarah akamuingiza ndani ya gari kisha akamvua koti la suti na kulichana, kisha akatengeneza kamba na kumfunga mikono, kisha akamfunga kwa kumuambatanisha na kiti cha gari, Sarah akaingia kwenye gari na kuliondoa.

Baada ya muda mchache Taita akazinduka na kujikuta na kamba mwilini,

"unaenda kuniua?" Taita aliuliza,

"hapana, nakupeleka polisi ili sheria ifuate mkondo wake" Sarah alijibu na kumfanya Taita acheke,

"sheria za nchi gani? Sheria za hii nchi zinafuata mkondo wa pesa, wewe unadhani nikipelekwa mahakamani nitafungwa" Taita aliuliza huku akicheka,

"utafungwa tu, ushahidi si upo" Sarah alijibu,

"ningefungwa siku nyingi tu kwa maana hata madawa ya kulevya nimekamatwa nayo mara nyingi tu, ila naachiwa, we unadhani serikali inaweza kumfunga mtu anayoisaidia fedha za kufanya mambo yao?" Taita aliuliza kwa dharau na kumfanya Sarah sasa abadili muelekeo wa gari, aliona ni kweli Taita hawezi kufungwa.

Sarah aliendesha gari mpaka nyumbani kwa Taita, kisha akashuka na kumkuta mlinzi yupo getini, Sarah akampiga mlinzi na kumfanya apoteze fahamu, Sarah akamshusha Taita na kumuingiza ndani, akamfunga kwenye kiti kama alivyomfanya Trigger, kisha yeye akakaa kwenye kochi,

"kazi nzuri" Taita aliongea huku akitabasamu,

"sipo hapa kwa ajili ya kuongea, nimekuja kuitimisha agano" Sarah aliongea huku akivaa kinyago chake,

"agano? Agano uliwekeana na nani?" Taita aliuliza,

"unaikumbuka ile sala niliyoomba nikiwa mdogo? Leo hii inatimia" Sarah aliongea huku akisimama,

"unawaka kama moto? Ebu waka nikuone" Taita aliongea kwa dharau na kumfanya Sarah atanue mikono yake, kisha akaikutanisha na moto ukatokea kwenye viganja vya mikono yake, Taita akashangaa,

"umeona sasa?" Sarah aliuliza huku akicheka na kumfanya Taita ashikwe na bumbuwazi, Sarah akamsogelea Taita na kuuweka ule moto kichwani, Taita akaanza kuungua, Sarah akawa anamtazama tu namna Taita anavyoangaika, kisha Sarah akauzima ule moto,

"moto ukiwaka kichwani utakufa mapema" Sarah aliongea na kisha akaanza kuchana makochi ya sofa na kuanza kumfunga nayo Taita mwilini, aliporidhika akawasha moto, Taita akaanza kuungua na kipindi hicho Sarah akaanza kuwasha moto kwenye kila chumba, nyumba nzima ikawa na moto sasa, Sarah akarudi na kumuangalia Taita namna anavyoungua.

Mkononi kwa Sarah alikuwa na pete ambayo ndio ilikuwa inatoa moto, alipewa na jeshi kama silaha pindi awapo kwenye hali ngumu.

****************

Sajenti Minja alifika polisi huku akiwa na vin, akamuingiza kwenye ofisi yake kwa ajili ya kumuhoji, ila kabla hawajaanza mahojiano, alifika mlinzi wa getini kwa Taita na kuwapa taharifa kuwa Taita ametekwa na mtekaji amejifungia ndani ya nyumba, Sajenti Minja akataka aende ila mkuu wa polisi akamzuia,

"kila siku unashindwa kumkamata huyo dada, leo hiyo kazi nitafanya mimi" Mkuu wa polisi aliongea kisha akatoka na askari katika gari tano, wote walikuwa na silaha.

Wale askari walifika mpaka nyumba kwa Taita na kukuta nyumba nzima inawaka moto na katika dirisha la sebuleni alisimama Sarah akiwa anawaangalia, kisha alivyoona ni askari, Sarah akashusha pazia.

Askari wakaamua watoe tangazo kuwa mtu yoyote aliyepo ndani ajisalimishe, lakini Sarah hakutaka atoke, badala yake alikuwa anatafuta njia ya kutoroka.

Sarah akatokea mlango wa nyuma, ila alipofungua mlango tu akakoswa na risasi, akagundua ameshazungukwa kila upande, Sarah akarudi mpaka dirishani na kutoa bastola yake, alikuwa ameshapaniki kwa kitendo cha kukoswa na risasi, Sarah akafyatua risasi iliyompiga askari mmoja na kuanguka chini.

mkuu wa polisi akaamuru vijana wake waishambulie, polisi wakaanza kufyatua risasi kuelekea dirishani, moja ikampata Sarah kifuani na kuanguka chini, huku risasi nyingine zilimpiga Taita aliyekuwa anafuka moshi baada ya moto kumteketeza, baada ya zile risasi kumpiga Taita, alikufa pale pale juu ya kiti.

Nje mkuu wa polisi akawaamuru askari wawili wasogee dirishani wakaangalie kama wamemuua mtekaji, wale askari wawili wakasogea mpaka dirishani, ila Sarah akawapiga risasi na wakafa palepale.

Mkuu wa polisi akaamuru tena washambulie, askari wakapiga tena risasi mfululizo na mbili zikampiga Sarah, moja ilimpiga Sarah mkononi na nyingine ikampiga kwenye mbavu, Sarah akaanguka chini na bastola ikamtoka, Sarah akawa anapumua kwa shida huku akiwa na mawazo ya kujisalimisha, kwa maana aliona ameshazidiwa, aliona akiendelea kupambana atafia ndani kwa kuwa alishazungukwa.

Kwa upande wa nje, mkuu wa polisi aliomba msaada wa jeshi, aliamini inawezekana mtu wanaepambana nae sio wa kawaida, na muda huo Vin na Sajenti Minja walikuwa wanawasili.

Vin alivyoona hali ilivyo, alianza kulia tu, aliamini Taita hawezi kuwa mzima kwa namna ule moto ulivyokuwa unawaka.

Baada ya muda mchache, wanajeshi walifika, wakawaambia askari warudi nyuma, kisha wao wakakaa mstari wa mbele, na amri ikatolewa kuwa lazima huyo mtekaji auawe kwa maana ameshaua askari watatu, wanajeshi wakajipanga kushambulia, na walikuwa na mabomu ya sumu, ndio walipanga kuyarusha ndani.

Sarah aliweza kuona kila kitu kupitia dirishani, alikata tamaa, aliona njia bora ni kujisalimisha,

Wanajeshi wakarusha bomu, likaingia kupitia dirishani, kisha wakasubiri kwa muda, mara ghafla mlango wa mbele ukafunguliwa, akatoka Sarah mikono ikiwa juu, ila kutokana na amri waliyopewa wanajeshi, walianza kumpiga risasi nyingi mfululizo na asilimia tisini ya hizo risasi zilimpiga kuanzia kichwani mpaka shingoni.

Sarah akapiga magoti, lakini bado waliendelea kumpiga risasi, mwisho Sarah akaanguka chini na kukata roho huku kile kinyago chake kikimuachia na kuanguka pembezoni mwake.

Kiongozi wa jeshi akaonesha ishara na wanajeshi wakaacha kupiga risasi, kisha kiongozi wa jeshi na polisi wakaisogelea ile maiti na kuigeuza, risasi zilikuwa zimemuharibu vibaya uso wake, alikuwa hatizamiki mara mbili.

Vin alikuwa analia huku akisikitika kuwapoteza watu wawili kwa wakati mmoja, yaani Taita, na Sarah ambaye ni dada yake.

Sasa askari wote wakaruhusiwa kwenda kuuangalia ule mwili, hapo Sajenti Minja ndipo akapata nafasi ya kuuangalia ule mwili,

"umekufa, ila hukustahili kufa, ungeachwa hai ili ulisaidie taifa, ni mtu muhimu sana wewe" Sajenti Minja aliongea kwa huzuni, kisha akaondoka huku akicheka.

Vin aliendelea kulia huku akiiangalia ile cheni ya Sarah shingoni, hakika ilimuuma, aliendelea kuuangalia ule mwili wa dada yake uliokuwa umelala chini,

"tuondoke, una kesi ya kujibu" Sajenti Minja alirudi na kumchukua Vin ambaye alikuwa na uchungu mkuu.

Huku nyuma mwili ule ulichukuliwa na kwenda kuhifadhiwa, huo ndio ukawa mwisho wa Sarah na Taita.

**********ITAENDELEA***********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH.

MTUNZI : ALEX KILEO.

SEHEMU YA SABINI. (MWISHO)

ENDELEA..................

Siku iliyofuata asubuhi, Sajenti Minja aliamkia hospitali, kuna kitu alikuwa anakihisi, ndio maana baada ya kuuangalia mwili wa Sarah siku iliyopita, alicheka ingawa aliongea maneno mazito.

Sajenti Minja alifika hospitali na kuonana na Daktari, bahati nzuri daktari wa zamu siku hiyo alikuwa ni Dokta Pendo, wakasalimiana,

"mmeshafanyia uchunguzi huo mwili wa Sarah?" Sajenti Minja alimuuliza Dokta Pendo,

"tayari, kila kitu kipo kwenye ripoti, ipo ofisi ya Dokta mkuu" Dokta Pendo alijibu, ila kilichomshangaza Sajenti Minja ni kuona Dokta hana hata uchungu wakati aliekufa ni rafiki yake.

Sajenti Minja akaelekea ofisi ya Dokta mkuu na kuchukua ripoti ya ya mwili wa Sarah, kisha akaondoka huku akiwa hana imani na ule mwili unaosemekana ni wa Sarah,.

Wakati Sajenti Minja akiwa anatoka, alisikia akiitwa kwa nyuma, alipogeuka alikutana na dokta Pendo,

"samahani, una namba ya Vin?" Dokta Pendo alimuuliza Sajenti Minja,

"ndio" Sajenti Minja alijibu,

"naomba unipatie" Dokta Pendo aliongea na kisha Sajenti Minja akatoa simu na kumsomea Dokta Pendo zile namba za Vin, Dokta Pendo akanakiri kwenye simu yake na kisha Sajenti Minja akaondoka huku akiwa na wasiwasi sana juu ya mwili wa Sarah.

Dokta Pendo baada ya kuridhika kuwa Sajenti Minja ameshaondoka eneo lile, aliipiga ile namba ambayo alipewa na Sajenti Minja, simu ikaanza kuita,

"hallow, naongea na Vin?" Dokta Pendo aliuliza baada ya simu kupokelewa,

"yeah, ndo mimi" Vin alijibu kwa sauti ya upole,

"unaweza kuonana na mimi leo?" Dokta Pendo aliuliza,

"wewe ni nani kwanza?" Vin aliuliza,

,

"ooh, kumbe sijajitambulisha? Mimi ni Dokta wa hii hospitali hapa yenye mwili wa dada yako Sarah" Dokta Pendo aliongea,

"kuna nini?" Vin aliuliza,

"tuonane kwanza, utajua tu" Dokta Pendo aliongea,

"nitakuja baadae hapo hospitali" Vin aliongea,

"hapana, sitaki tukutane hospitali, njoo kanisa kuu la roman, mjini nitakuwepo hapo saa moja jioni, ukifika ingia moja kwa moja ndani ya kanisa" Dokta Pendo alitoa maelezo,

"kwanini kanisani?" Vin aliuliza,

"nahitaji tukae eneo lenye amani ili tuongee vizuri" Dokta Pendo aliongea,

"sawa, nitakuja" Vin aliongea na kukata simu, kisha Dokta Pendo akashusha pumzi ndefu na kuirudisha simu mfukoni. Kisha akaenda kuendelea na kazi.

**************

Sajenti Minja aliibeba ile report mpaka ofisini kwa mkuu wake, mkuu wa polisi akaifungua ile report na kuanza kuisoma, aliisoma kwa muda wa dakika ishirini kisha akavua miwani na ile report akairudisha kwenye bahasha.

"ujue huyu mwanamke hajaua polisi watatu pekee?" Mkuu wa polisi aliongea huku akimtazama Sajenti Minja,

"kuna wengine tena?" Sajenti Minja aliuliza,

"kule ambapo kuna mlango wa nyuma, tumekuta polisi wote wamekufa, na pia kulikuwa na michirizi ya damu iliyoenea mpaka juu ya ukuta" Mkuu wa polisi aliongea,

"hapo una maana gani?" Sajenti Minja aliuliza,

"inawezekana watekaji walikuwa wawili, ila mmoja ametoroka" Mkuu wa polisi aliongea na kumfanya Sajenti Minja aanze kuziamini hisia zake juu ya ule wa Sarah,

"kwa hiyo unataka kusema tumtafute huyo mtekaji tena?" Sajenti Minja aliuliza,

"tena hiyo kazi ifanyike usiri mkubwa, yaani ni mimi na wewe, hatakiwi mtu mwingine kujua hii habari" Mkuu wa polisi aliongea,

"sawa mkuu" Sajenti Minja aliongea, kisha mkuu wa polisi akainuka na kutoka nje ya ofisi na kumuacha Sajenti Minja akicheka peke yake.

Sajenti Minja alikaa kwenye ile ofisi kama dakika tano hivi, kisha akainuka na kuelekea nje, akaingia kwenye gari na kurudi hospitali, safari hii alirudi kama mpelelezi, sio kama mtu aliyefuata report.

Sajenti Minja baada ya kufika eneo la hospital, aliingia ndani ya jengo na lengo lake kubwa lilikuwa ni kutaka kujua kama Dokta Pendo bado yupo hapo..

Baada ya Sajenti Minja kukagua kama dakika kumi, aliweza kugundua kuwa Dokta Pendo bado yupo. Sajenti Minja akatoka nje na kuingia kwenye gari lake, kisha akachukua gazeti na kuanza kusoma, kila mtu aliyekuwa anatoka ndani ya jengo la hospitali, Sajenti Minja alikuwa akimuangalia.

Baada ya masaa matato, Sajenti Minja alimshuhudia Dokta Pendo akitoka, kisha Dokta Pendo akaingia kwenye gari dogo na kuondoka, Sajenti Minja akaanza kuifuatilia ile gari.

Dokta Pendo aliendesha gari bila kufahamu kama anafuatiliwa, gari ilienda mpaka kwenye nyumba ya Sarah, kisha Dokta Pendo akatelemka na kuingia ndani ya geti.

Sajenti Minja kama kawaida yake akaegesha gari kwa mbali na kusubiri huku akijiwekea muda kuwa baada ya saa kadhaa atatelemka na kwenda kuchunguza kwa umakini zaidi.

Saa la kwanza likaisha, saa la pili likakatika, la tatu pia. Saa la nne likiwa mwishoni bila kuona mtu akiingia wala kutoka, Sajenti Minja akafungua mlango ili atoke, ila kabla hajashusha hata mguu, alishuhudia geti la nyumba ya Sarah likifunguliwa, Sajenti Minja ikambidi afunge mlango wa gari na kutupa macho getini kuona nani anaetoka.

Alimshuhudia Dokta Pendo akitoka huku akiwa ameongozana na babu yake Sarah, walionekana wakiongea na kucheka kwa furaha, ila Sajenti Minja hakuweza kujua wanachoongea kwa kuwa alikuwa mbali,

"Sarah amekufa kweli? Mbona wanaongea na kufurahi?" Sajenti Minja alijiuliza huku akiiangalia gari waliyopanda Dokta Pendo na babu yake, ile gari iligeuzwa na kisha ikawa inaondoka kuelekea upande aliopo Sajenti Minja, Sajenti Minja kuona hivyo, akalala kwenye siti ili wasimuone, ile gari ikapita na kisha Sajenti Minja akawasha gari yake na kuigeuza, akaanza tena kuifuatilia ile gari.

****************

Mishale ya saa moja usiku, Vin alitelemka Katika gari nje ya kanisa, kisha kwa hatua za haraka akawa anaelekea ndani ya kanisa, alifika na kuingia ndani, kisha akasimama nyuma ya kanisa na kuangaza macho, hakuweza kumuona mtu mwingine isipokuwa mwanamke mmoja aliyekuwa akibandua karatasi sehemu tofauti ndani ya kanisa, alikuwa akibandua kwa kufuata mstari kwa maana karatasi zilikuwa nyingi, Vin akatupa jicho kwenye karatasi moja iliyopo pembeni yake, ilionekana kufanana na zile karatasi zinazoondolewa na yule mwanamke.

Vin akatupia jicho ile karatasi na kuisoma,

"eee Mungu naomba nikiwa mkubwa niwe nawaka kama moto"

"sala hii iliombwa na mtoto mdogo aitwae Sarah Isack mnamo tarehe //-//-//"

Vin akajikuta anashangaa na kumtupia jicho yule mwanamke, kisha yule mwanamke nae akamtupia jicho Vin, Vin akazidi kushangaa kwa maana yule mwanamke alikuwa ni Aisha,

"itoe hiyo karatasi na uje nayo huku" Aisha aliongea na kugeuka kisha akaelekea benchi la mbele na kukaa.

Vin akaitoa ile karatasi na kwenda nayo moja kwa moja mpaka alipokaa Aisha na kisha akampatia ile karatasi,

"Mimi ndiye niliyetaka uje hapa, Kaa hapo" Aisha aliongea na kumfanya Vin ashangae,

"kuna nini?" Vin aliuliza huku akikaa,

"pole kwa msiba wa baba yako, nadhani umeumia sana kwa hilo" Aisha aliongea kwa huzuni,

"uchungu lazima uwepo, nimeumia kwa kweli, ila sina chuki dhidi ya dada yangu Sarah, ingawa amefanya hayo yote, ila nimeumia sana kwa namna alivyokufa, sikutaka afe, niliamini yeye ni mtu pekee mwenye upendo wa dhati kwangu" Vin aliongea kwa hisia,

"ile siku ya hilo tukio hata mimi nilifanikiwa kuingia ndani ya ule moto kuja kumuokoa sarah" Aisha aliongea na kumfanya Vin ashangae,

"kwanini hukumuokoa sasa?" Vin aliuliza kwa pupa,

"ilikuwa hivi, siku ile nilifika pale nikiwa na mtoto wa Trigger, tutakuta askari wamejaa mpaka kule nyuma ya nyumba, sasa itabidi tupambane nao, mimi na mtoto wa Trigger tukafanimiwa kuingia ndani, tukakuta Sarah ameshapigwa risasi tatu, tukambeba ili tutoke nae, tukakuta kule nyuma askari wengine wameongezeka, ikabidi tumuweke Sarah chini kwa maana alikuwa yupo kwenye hali mbaya, kisha mimi na mtoto wa Trigger tukaanza kupambana, mwisho askari tukawapunguza, tukakubaliana mimi nimbebe Sarah kisha mtoto wa Trigger atanilinda kwa kuendelea kuwapiga risasi askari wachache waliobaki.

Ila mtoto wa Trigger akasema njia rahisi zaidi ya kumsaidia Sarah baada ya kutoka, ni yeye mtoto wa Trigger kujisalimisha kwa maana polisi hawatoendelea kumtafuta Sarah kwa maana tulikuwa na wasiwasi huenda polisi wetakuwa wamewekwa njia zote za mtaa ule, basi tukakubaliana hivyo na kisha kile kinyago cha Sarah na mkufu nikampatia yule binti, kisha nikambeba Sarah na kutoka nae nje huku yule binti akipambana na askari kadhaa ambao wangeniletea madhara.

Nikafanikiwa kutoka na Sarah na kisha nikampeleka kwenye gari huku nikiwa na imani yule binti wa Trigger atakuwa amejisalimisha na nikapanga nitaenda kumuokoa usiku mkubwa, ila nikashangaa kusikia wanajeshi wamemuua yule binti" Aisha alimaliza kuongea kwa huzuni,

"kwa hiyo Sarah yupo hai?" Vin aliuliza,

"Sarah yupo" Aisha aliongea na kumfanya Vin apate furaha upya,

"yupo wapi?" Vin aliuliza,

"kabla sijakujibu, Sarah ameniagiza kuwa huo mwili wa huyo binti wa Trigger, uchukue na uuzike kwa heshima, jina la huyo binti anaitwa Sarah, hilo ni jina alilopewa na Taita, ni jina la bibi yao Taita, bibi yao Taita ndio aliowazaa baba yake Taita na mama yenu aliyeitwa Margret" Aisha aliongea,

"nitafanya hivyo, je Sarah yupo wapi?" Vin aliuliza,

"twende nikupeleke" Aisha huku Akiinuka na zile karatasi, Aisha akaelekea moja kwa moja mpaka kwenye shimo la taka na kuzitupa zile karatasi na kisha akazichoma moto, baada ya hapo akaingia kwenye gari la Vin na wakaanza safari, walikuwa wanaenda Kiwanja cha ndege.

Vin ilimbidi aendeshe gari kwa mwendo mkali ili kuiwahi ndege, walifika uwanjani na kisha wakatelemka na kuingia ndani ya jengo, kwa mbali Vin aliweza kumuona Sarah akiwa anaongea na dokta Pendo na mzee asiyemfahamu, Vin ikambidi akimbie kumuwahi Sarah, alipomfikia alimkumbatia kwa hisia,

"nakupenda sana Sarah" Vin aliongea kwa hisia huku akitokwa na machozi,

"nakupenda sana Sebastian isack" Sarah alijibu huku pia machozi yakimtoka, kisha wakaachiana na Sarah akamtambulisha Vin kwa babu yao, basi furaha ikaongezeka maradufu,

"ila huyu mzee naenda nae uingereza, atarudi baada ya miezi miwili" Sarah alimwambia Vin,

"na mimi nitakuja huko kwa ajili yako, nahitaji muda wa kukaa pamoja na nyinyi, baada ya wiki mbili nitakuja" Vin aliongea na wakati tangazo lilisikika likiwataka abiria wanaoenda uingereza kupitia Kenya waende wakafanyiwe ukaguzi ili waingie kwenye ndege, Sarah na babu yake wakaagana na watu pale, kisha Sarah akamsogelea Aisha,

"kuna gari range Rover nyeusi, Dokta Pendo atakupatia utembelee, alafu Vin akija uingereza, uje naye" Sarah aliongea huku akiwa amemkumbatia Aisha,

"usijali" Aisha alijibu huku akitabasamu.

Baada ya lisaa limoja, ndege aliyopanda Sarah iliruka na kuiacha ardhi ya Tanzania.

Vin, Aisha na Dokta Pendo wakatoka nje, kisha Vin akaagana nao na kuingia ndani ya gari na kuondoka, pia Aisha na Dokta Pendo wakaingia kwenye gari lao na wakaondoka.

Pale kwenye uwanja wa ndege kulikuwa na mwanaume akiyafuatilia yale matukio kwa umakini mkubwa, alikuwa ni Sajenti Minja, baada ya kila mtu kuondoka eneo lile Sajenti Minja alitabasamu na kuwasha gari yake,

"hakuna cha kufuatilia, Sarah kaondoka na mambo yamefika mwisho" Sajenti Minja aliongea na kuiondoa gari yake kuelekea upande tofauti kabisa na ule walioondokea wakina Aisha.

***********MWISHO************

the Legend☆
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom