RIWAYA; MKANDA WA SIRI
imeandikwa na Halfani Sudy
SIMU: 0674 395733
Sehemu ya Kumi na Tisa
Kina Malolo walifika katika kisiwa cha Pemba. Kila mmoja akiwa na ile picha ya mvuvi mkononi mwake.
Wale walikuwa ni watu makini, na walijua sehemu sahihi ya kwenda kumsaka yule mvuvi, walienda katika fukwe ya bahari. Na kutokana na umaarufu wa mtu waliyekuwa wanamtafuta hawakupata shida kabisa kumpata mvuvi aliyekuwepo katika picha ile. Mtu wa watatu tu kumuuliza aliwaambia kila kitu kuhusu mvuvi huyo, tena na kuwasindikiza hadi katika kibanda cha yule mvuvi. Ndani ya mioyo ya kina Malkia ilikuwa ni furaha isiyo na kifani, kazi yao ilitokea kuwa rahisi sana...walikuwa wanaamini ndani ya robo saa mkanda utakuwa tena mikononi mwao, iwe kistaharabu ama kwa nguvu. Wakichoamini wao huyo jamaa alipewa mkanda na yule msichana baada ya kutokea ile ajari mbaya ya meli ya MV Donors, kumbe wala haikuwa hivyo...
Ayoub Mbembati alikuwa ni mvuvi aliyejipatia umaarufu muda mfupi sana katika kisiwa cha Pemba. Hii ilitokana na hekima, busara, upole, uwajibikaji na uchapakazi. Uvuvi ilikuwa ni kazi yake kuu tangu alivyohamia katika kisiwa cha Pemba miaka kadhaa iliyopita...uvuvi ilikuwa ni kazi aliyoirithi toka kwa baba yake mzazi, mzee Mbembati. Na kutokana na makuu aliyoyapitia Ayoub ndomana alitokea kuwa na sifa hizo.
Ayoub alikuwa mvuvi, lakini mvuvi duni akiyetumia zana duni. Na bado maisha yake yaliendelea kuwa duni. Baba yake mzazi alifariki akiwa duni pia, tena alifariki kifo kibaya sana mbele ya Ayoub, ni Ayoub pekee ndiye aliyeijua sababu ya kifo cha baba yake. Kifo kilichoacha vitendawili kadhaa mpaka leo. Na sababu ya kifo hiko ambayo ilikuwa ndani ya kifua chake ndiyo iliyomfanya ahame kimyakimya katika mji wa Kilwa Masoko na kuibukia katika kisiwa cha Pemba, mzee Mbembati alifariki kifo kibaya sana akimfata mkewe mwezi mmoja tu baada ya kufariki kwa ugonjwa wa malaria.
Ayoub Mbembati, kitu pekee alichorithi toka kwa baba yake mzazi ni mkanda, mkanda ambao ulisababisha kifo cha kikatili cha baba yake, mkanda ambao ndio uliomfanya ahame bila kupenda katika mji aupendao na kwenda kuishi ugenini, lakini cha kusikitisha mkanda haukudumu sana mikononi mwake.....yaliyotokea hadi leo bado yalikuwa bado katika kichwa chake.
Shirika la W.W.F lilipeleka mradi wa kutunza mazingira ya bahari na maliasili za bahari Pemba, na mikoa mingi yenye bahari na maziwa katika nchi ya Tanzania. Mradi ulioleta matumaini kwa wakazi wa jamii za kivuvi, ikiwemo wakazi wa kisiwa cha Pemba. Wananchi walitakiwa kutunza na kulinda mali za bahari, hapo ndipo vilipoanzishwa vikundi vilivyojulikana kama Beach Management Unit ( BMU) kwa ajili ya kufanya doria baharini na nchikavu kwa lengo la kupiga vita uvuvi haramu, kulinda bahari na mali zake, na Ayoub Mbembati ndipo alipochaguliwa kuwa mwenyekiti wa BMU...Na cheo hiko ndicho kilichomfanya aonekane kwenye taarifa ya habari ya TBC akielezea umuhimu wa kuhifadhi bahari, na kuonwa na Binunu Issa.
*****
Kule Kisarawe hali ilikuwa mbaya sana kwa Binunu. Chifu shetani alikuwa kamkalia kohoni. Alikuwa anataka kumbaka Binunu. Sasa nguo ya ndani ya Binunu ilikuwa katikati ya mapaja yake.
Kichwani sinema ya ajabu ya Binunu iliendelea, alikumbuka jinsi siku ambayo mama yake alikuwa anafanyiwa kitendo kama kile. Sinema ilimuonesha kwamba nguo ya ndani ya mama yake mzazi ilipofika maeneo yale baba yake alikurupuka kwa hasira. Lakini hakufika akikotaka kwenda. Alipigwa kwa nguvu na kiwiko cha bunduki katika paji la uso wake.
Baba yake damu zilimbubujika!
Damu za kwenye sinema zilimkumbusha kitu kipya kabisa leo...
Naam...Binunu sasa alikumbuka !
Sasa haikuwa sinema, ilikuwa dhahiri shahri, Binunu alikumbuka mtu aliyekuwa anamfanyia vile mama yake alivuta vitu fulani kabla hajamfanyia kile kitendo kibaya mama yake mzazi, alivuta kama alivyovuta huyu wa leo. Tena aina ya vikopo walivyotoa hivyo vitu alivyokuwa anavuta huyu aliye mbele yake leo, na aliyembaka mama yake miaka kadhaa iliyopita vilikuwa vinafanana. Vikopo vyeusi vyenye rangi nyeupe, vikopo vilivyotengeneza taswira ya mnyama Pundamilia.
Na taulo la Chifu lilianza kufunguka...
Chifu alikuwa anaendeshwa na hisia zilizotokana na madawa ya kulevya zaidi badala ya akili zake za asili. Madawa ambayo siku zote humshauri kama yanamvyomshauri leo, baada ya kuvuta ni ngono. Kama ukipata nafasi ya kumuuliza Chifu faida ya unga ule angekwambia moja tu, unga ulimfanya ampate Wema Shayo, mwanamke aliyempenda zaidi hapa Duniani, baada ya hapo unga ulimsukumia Chifu katika engo mbaya sana, ulimtoa kwa kasi sana toka kuwa binadamu wa kawaida hadi kuwa mnyama. Na yote hayo yalisababishwa na pesa, ilimpasa apate pesa ili aweze kununua unga, ambao sasa ulikuwa umeweka kambi ya kudumu katika mishipa ya damu yake. Hapo ndipo alipoanza kuwa mwizi, tabia mbaya ambayo hakuwa nayo kabisa hapo kabla, alianza kuiba vitu vidogovidogo vya nyumbani kwao, aliporidhika alihamia vitu vikubwa, aliiba runinga, deki na friji, na kwenda kuuza kwa bei rahisi ili apate pesa ya kwenda kununulia unga. Maneno ya wazazi wake hayakusaidia kitu, ilikuwa ni kama wanampigia mbuzi gitaa. Alivyomaliza vitu nyumbani kwao alihamia katika nyumba za jirani, na hatimaye aliiba popote pale alipoona cha kuiba. Nguvu za madawa ya kulevya zilimpeleka vibaya, na hapo ndipo alipopanda ngazi rasmi, toka mwizi wa kawaida mpaka jambazi, kumbuka alikuwa na miaka kumi na nane tu hapo. Baada ya kupanda ngazi ndipo alipopata wazo jipya, wazo ambalo lilibarikiwa na mpenzi wake, Wema Shayo. Alizamia meli na kwenda Afrika ya kusini...eti kutafuta maisha. Huko ndiko Chifu alikobadilika hasa.
Kwa mara ya kwanza huko ndiko aliua mtu, Mzulu aliyemfanyisha kazi kwa ujira wa kupewa madawa ya kulevya. Baada ya Chifu kumaliza ile kazi, Mzulu alijifanya mjuaji kwa kudhani anaweza kumdhulumu mtoto yule...kumbe Chifu alikuwa mdogo kwa umri lakini mkubwa kwa matendo, hasa matendo ya kikatili. Kilichofuatia hapo Mungu pekee ndio anajua, lakini kwa alichomfanyia yule Mzulu kilimpeleka kaburini na yeye kuhukumiwa kifungo cha maisha jela akiwa mtoto mdogo sana. Jela ikamfundisha shurba Chifu, ukatili, umajinuni na ubabe, pamoja na umri wake mdogo lakini yeye nd'o alikuwa mwamba katika gereza lililokuwepo katika mji wa Soweto.
Na huko ndipo lilipoibuka jina la Chifu, Chifu sasa akawa Chifu wa Gereza la Soweto, na jina lake la awali la Abdullah kufutika kabisa masikioni mwake.
Na baada ya miaka miwili ya jela ndipo mfumo wa kubadilishana wafungwa kati ya Tanzania na Afrika Kusini ulianzishwa, na Chifu alikuwa mmoja wa wafungwa wa mwanzoni waliofaidika na mfumo huo hasa kutokana na umri wake kuwa mdogo, alirudishwa jijini Dar es salaam, alifikia katika gereza la Ukonga.
Hapo Chifu alikuwa na miaka ishirini....
Na sasa Chifu alikuwa yu tayari kumuingilia Binunu. Alimtanua miguu yake kwa nguvu pale chini na kuingia kwa kati.....
Sinema ya kutisha iliyopo kichwani mwa Binunu ilimkumbusha kitu, siku mama yake alivyofanyiwa kitendo kama kile. Siku mama yake alivyoingiliwa kwa kati namna ile alifanya kitu. Naye alifanya kitu hichohicho ambacho alichofanya mama yake miaka kumi na saba iliyopita. Naye aliamua kufanya kitendo hikohiko. Kitendo kama kilichofanywa na mama yake mzazi miaka kumi na saba iliyopita. Binunu alikumbuka vizuri sana kuwa mama yake alimng'ata shingoni upande wa kulia yule jamaa aliyekuwa amemuingilia kati kwa lengo la kumbaka. Naye alidhamiria kufanya hivyohivyo, kama alivyokuwa anaoneshwa katika sinema yake kichwani. Alimwangalia yule jamaa upande wa kulia shingoni kwa lengo la kumng'ata. Upande uleule wa shingo aliong'ata mama yake miaka kumi na saba iliyopita, jamaa alikuwa na kovu!
E bwana wee!
Binunu akili zake zote zilirudi.
"Wewe ndiye uliyembaka mama yangu" Binunu alisema kwa sauti nzito yenye kukwaruza. Chifu aliduwaa...ilikuwa kama ameona mdudu wa kutisha sana, na yeye hakuwa na uwezo wa kujitetea wala kujiokoa....ilikuwa kama mgonjwa ambaye amepigwa sindano ya ganzi lakini akishuhudia jinsi kidonda chake kibichi kikivyoshonwa huku yeye akiwa hasikii maumivu..Chifu hakuamini kabisa kama maneno yale yalikuwa yametoka kinywani mwa Binunu.
"Kwanini mlimuua baba yangu mzazi?" Binunu alibadilisha aina ya sentensi na maana ya sentensi, mwanzo ilikuwa kauli taarifa, sasa ilikuwa katika muundo wa swali. Mwanzoni alimuulizia mama yake, na sasa alimuulizia baba yake. Sasa Chifu alisimama wima, akiwa uchi wa mnyama. Akimwangalia Binunu kwa woga na mashaka. Raha iliyokuwa ikiletwa na madawa ya kulevya ilikata ghafla. Raha ambayo aliyoanza kuipata mara tu pale alipoanzisha uhusiano na Wema Shayo na hadi leo alikuwa anaipata kila avutapo unga. Raha ambayo alihakikisha inamfikia hadi katika gereza la Ukonga kwa njia yoyote ile. Na baada ya kuaminika na mtu aliyekuwa anaingiza kwa siri raha ile gerezani yeye ndiye aliyepata bahati ya kuwa msambazaji, kazi aliyoifanya kwa ufanisi mkubwa sana. Hadi wauzaji wa madawa wakubwa walipotamani kumtoa gerezani ili atoe huduma ya usambazaji nje ya gereza. Haikuwa kazi ngumu kutoka gerezani kama unavyoweza kufikiria. MONEY TALKS! na Chifu alirejea tena uraiani baada ya kukaa gerezani kwa muda wa miaka mitano.
Na hapo alikuwa na miaka ishirini na mitano tu.
Alivyotoka nje ya gereza alikuta kila kitu kimebadilika, wazazi wake wapendwa walikuwa wamehama walipokuwa wanakaa na nyumba ilikuwa imeuzwa. Wema Shayo, mwanamke aliyekuwa anampenda sana, alikuwa ameshafariki miaka mitatu iliyopita baada kupigwa na raia wenye hasira kali baada ya kukamatwa alipoenda kuiba katika duka la Mhindi mmoja Kariakoo. Hapo ndipo Chifu alipopata wazazi wapya, wazazi wake wapya walikuwa madawa ya kulevya, na Chifu alipata mpenzi mpya, mpenzi wake mpya alikuwa madawa ya kulevya. Hakujishughulisha kuwatafuta wazazi wake kama asivyojishughulisha kutafuta mpenzi mpya. Aliendelea na kazi yake mpya aipendayo ya kusambaza madawa ya kulevya katika mikoa yote ya Tanzania. Huku Chifu akiwa hamjui hata 'Boss' wa biashara hiyo. Lakini aliifanya kwa moyo wake wote na ufanisi mkubwa kama ilivyo ada yake. Na hapo ndipo Chifu alianza kuwa Chifu kweli.
"Ulimbaka mama yangu mbele yangu, mbele ya baba yangu, Mlimuuwa baba yangu mbele ya macho yangu, mbele ya macho ya mama....mlimpiga risasi kikatili sana, mama nimpendae mlimbaka kisha mlimuuwa kwa kumkaba shingoni, tena ni wewe ndiye ulimkaba..na kumuuwa mama yangu mpendwa bila huruma yoyote, niambie ni kosa gani kubwa walilowafanyia wazazi wangu? Hadi mkawafanyia vitendo vya kikatili namna ile? Baba alikuwa mwalimu mwema kwa wanafunzi wake na wananchi wote, alikuwa mshauri mwema kwa kila mtu, alikuwa tumaini jema, mtu asiye na ugomvi na mtu yeyote yule, mama alikuwa mama mwema asiyejua kabisa kugombana na watu, alikuwa mithili ya baba, labda ndomana walipendana na kuoana, walikuwa wanafanana tabia, na wahenga waliwahi sema " ndege wanaofanana huruka pamoja', kwanini sasa mliwafanyia vile ndege wale wazuri wafananao kwa tabia njema???" Binunu alikuwa anauliza maswali huku akinyanyuka sofani kumfuata Chifu.
"Hiyo tabia uiitayo njema ndiyo ilimponza marehemu baba yako..." Chifu aliongea kizembe bila kujitambua.
"Amma!" Unasemaje bwege wewe?" Binunu alimaka kwa hasira huku akiendelea kumsogelea Chifu akiwa kafura kwa hasira. Ama kwa lugha nyepesi tunaweza sema hatari ilikuwa inamsogelea Chifu. Tena hatari kubwa sana!
Binunu alikuwa anacheka kwa dharau huku akimsogelea Chifu. Chifu aliendelea kurudi nyuma taratibu. Huku moyo ukimdunda kwa kasi kubwa sana!
"Yaani mlimuuwa baba yangu kikatili namna ile, yaani ulimbaka mama yangu kisha ukamuua kinyama sana, eti leo unaniambia kizembe tu....ni tabia njema yake ndio sababu ya kumuua baba, nd'o sababu ya kumuua na kumbaka mama, ulisikia wapi tabia njema ikaleta matokeo mabaya tena ya kusikitisha namna ile, ngoja nikwambie kitu mzee.....tabia njema siku zote huleta matokeo mema, na tabia mbaya ndio huleta matokeo mabaya, iko hivyo.... matokeo mabaya kama yatakayokukuta wewe leo hii na hii yote ni kutokana na tabia yako mbaya ya kuuwa watu wenye tabia njema.." Binunu alisema kwa jazba sasa, wakiwa wamekaribiana kabisa na Chifu.
Sebuleni sasa palikuwa hapatoshi, Binunu alikuwa amerudiwa na akili zake zote zilizokuwa zimeenda kusikojulikana, tena na akili za ziada zilikuwa zimerudi. Amerejewa na kumbukumbu zake zilizopotea tangu siku ile ilipotokea ajari ya kupangwa ya MV donors. Kitu ambacho Chifu labda alikuwa hajui. Binunu sasa hakuwa Binunu yule aliyekuwa anamfahamu kabla...
Je nini kitatokea? Sehemu ijayo ni sehemu ya mwisho kwa season 1 ya Riwaya hii. Season 2 ipo tayari na inapatikana WhatsApp kwa Sh 1500 tu, ni 0674 395733.