Riwaya: Mateka

Riwaya: Mateka

RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA KUMI)

Yalikuwa majira ya saa tatu usiku. Japokuwa ulikuwa wakati wa giza lakini mji uling`aa mataa kila kona. Giza lilipigwa kikumbo kizito na mwanga uliozalishwa na mataa ya barabarani, nyumba pamoja na vyombo vya moto vilivyokuwa vikitumiwa na raia waliokuwa wakijongea kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Mmoja wa watu waliofanikiwa kuufukuza mwanga kupitia chombo cha usafiri alikwa daktari Johnson, gari lake lilikuwa mwendo kasi kuelekea mtaa wa Bungero, mtaa alikuwa akiishi binti wa kiarabu, Nasrat Abdul al Aziz. Alihisi gari likimsaliti, japokuwa alikuwa mwendo kasi lakini alihisi akitembea kwa miguu. Alitamani gari lipae kama ndege lakini haikuwezekana. Alichukua simu yake ya mkononi kisha akampigia Nasrat Abdul al Aziz, simu iliita pasipo mafanikio. Hakuchoka, alipiga tena na tena lakini jibu halikubadilika. Hakuogopa kupata ajali alipokuwa akiendesha gari kwa mwendo kasi kwa mkono mmoja. Alirudisha simu mfukoni kisha mkono wa pili ukarudi katika usukani wa gari na safari ya kwenda kwa Nasrat Abdul al Aziz ikaendelea. Aliamini lazima amkute Nasrat Abdul al Aziz nyumbani kwake muda huo, mara nyingi Nasrat Abdul al Aziz huwa nyumbani kwake Bungero muda kama huo. Mara chache huwa katika ngome yake. Mara chache hizo ni mpaka itokee dharura iliyomuhitaji yeye mwenyewe, kwa sababu dharura zingine alimwachia Zimwi akabiliane nao. Mungu siyo Athumani, daktari Johnson alifanikiwa kufika katika nyumba ya Nasrat Abdul al Aziz. Alipiga honi mara kadhaa pasipo mafanikio. Akachukua simu yake akampigia kwa mara nyingine, mara hiyo simu ilipokelewa

“Dogo mbona hupokei simu?”

Siku zote alizoea kumuita dogo tangu enzi za uhai wa mzee Abdul al Aziz. Japokuwa Nasrat Abdul al Aziz alikuwa ndiye bosi wake lakini haikubadilisha jina la dogo, wala Nasrat Abdul al Aziz hakuumizwa wala kuchukizwa na jina hilo kwa sababu aliamini lilikuwa likimuenzi baba yake. Mara zote aliitika, na mara chache daktari yule alipomwita jina lake (Nasrat) au jina la heshima (bosi) Nasrat Abdul al Aziz alikataa kuitika na kumwambia amuite jina alilozoea kumuita tangu enzi za utoto wao. Walicheka na kundelea na shughuli iliyowakutanisha. Nasrat Abdul al Aziz alijibu hoja ya daktari Johnson

“Samahani sana daktari, nilikuwa bafuni naoga. Samahani sana”

Nasrat Abdul al Aziz alimuheshimu sana daktari Johnson, heshima hiyo ndiyo iliyoongeza upendo wa daktari kwa Nasrat Abdul al Aziz. Daktari Johnson alimwambia Nasrat kuwa yupo nje ya geti la nyumba yake, anahitaji geti lifunguliwe ili aingie. Kabla Nasrat Abdul al Aziz ajajibu kauli ya daktari Johnson alitazama saa ya ukutani ikamuonesha ilikuwa saa tatu usiku. Alishangaa kusikia daktari yupo nje ya nyumba yake muda huo, haikuwa kawaida hata kidogo. Alijibu kauli ya daktari

“Kuna kheri kweli? Au umeniongezea nguvu uliyoniambia?”

Daktari alielewa maana ya maswali ya Nasrat Abdul al Aziz kwa sababu siku iliyopita alimwambia afanye juu chini kuboresha ulinzi katika nyumba yake, alimwambia kauli hiyo baada ya kusikia Derrick Edward amekamatwa na watu wasiojulikana. Daktari Johnson alihofia usalama wa Nasrat Abdul al Aziz. Alijua Nasrat Abdul al Aziz akiongeza ulinzi katika nyumba yake atakuwa salama kwa kiasi kikubwa. Daktrari Johnson alihisi akicheleweshwa kuingia ndani, alikuwa na ujumbe mzito wa kumueleza Nasrat Abdul al Aziz. Japokuwa alikuwa ameshafika katika nyumba ya Nasrat Abdul al Aziz na angeweza kusubiri mpaka kuingia ndani ndiyo aongee dhamira ya kufika usiku ule, lakini hakuwa tayari kusubiri. Alianza kuongea kupitia simu. Alimwambia binti wa Kiarabu

“Leo nina majibu kuhusu Derrick, hakika kwa alipo Derrick hutakiwi kuishi katika makazi yako. Yakupasa kuishi katika ngome yako. Kwakweli yakupasa kuishi kule ili uweze kulindwa na kujidhatiti katika njia za kumkomboa mpenzi wako”

Kauli ya daktari Johnson ilisababisha mwili wa Nasrat Abdul al Aziz usisimke kwa hofu baada ya kusikia habari za Derrick Edward, hasa aliposikia kauli iliyomwambia suala la kumkomboa mpenzi wake. Alihisi kama alisikia vibaya lakini akili yake iliyokamilika ilimuhakikishia kuwa alisikia vizuri kwa asilimia mia moja. Alijiuliza

“Nani aliyemteka Derrick? Eti mpenzi wangu! Kuna mapenzi hapo, mapenzi na mpelelezi!”

Akili ya Nasrat Abdul al Aziz ilikataa kabisa kuhusu suala la mapenzi na askari mpelelezi aliyempenda lakini akili hiyo hiyo ikamkumbusha juu ya mtoto wa askari huyo aliye tumboni kwake. Kichwa kikawaka moto. Sasa aliamini alikuwa kwenye mtego mgumu katika maisha yake, alishindwa atetee upande gani. Alikumbuka kauli ya daktari Johnson, kauli iliyohitaji kufunguliwa geti la nyumba hiyo ili aingie kumpa taarifa kamili kuhusu Derrick Edward na watekaji. Taratibu alipiga hatua kuelekea nje ya nyumba yake, alifika getini kisha akafungua. Mwili ulikuwa mkakamavu ukichukua maamuzi lakini akili ilielemewa kwa mzigo mzito wa mawazo. Alifungua mlango wa geti lakini aliendelea kukaa katikati ya mlango huo, kitendo kile kilisababisha daktari Johnson kushindwa kuingiza gari ndani ya geti hilo. Siyo kwamba Nasrat Abdul al Aziz alipenda au alijua kama amemzuia daktari Johnson, hapana, alisimama njiani pasipo kujua. Daktari Johnson alimtazama Nasrat Abdul al Aziz akaelewa alikuwa mbali sana kimawazo, alikuwa dunia nyingine tena dunia iliyo mbali na upeo wa macho yake. Daktari Johnson alipiga honi, honi ilimshitua Nasrat Abdul al Aziz na kumrudisha katika dunia yake halisi. Nasrat Abdul al Aziz alielewa maana ya honi ya daktari Johnson, alisogea pembeni kuruhusu gari kuingia. Ndivyo ilivyokuwa, daktari Johnson aliingiza gari lake kisha akaliegesha sehemu ya maegesho, sehemu ambayo Nasrat Abdul al Aziz huegesha magari yake.

Baada ya tukio lile waliongozana mpaka sebuleni wakakaa kwenye viti vya sofa, hapo ndipo ufafanuzi ulipotolewa. Daktari Johnson alimsimulia Nasrat Abdul al Aziz kuwa Derrick Edward yupo mikononi mwa Amani Collence, hakuishia hapo bali alifafanua zaidi kuwa hali aliyomkuta nayo Derrick Edward ilieleza wazi kuwa alipigwa sana mpaka akapoteza fahamu. Walimpasua sehemu nyingi za mwili wake hasa kichwani wakasababisha apoteze damu nyingi. Daktari Johnson hakuishia hapo bali alifafanua namna alivyochukua sampuli ya damu ya Derrick Edward na kuondoka nayo kwenda kuipima katika hospitali yake, alipofahamu grupu la damu yake akarudi katika ngome ya Amani Collence na kumuongezea damu. Alifafanua zaidi kuwa alikubaliana na Amani Collence atakuwa akienda kuangalia maendeleo ya Derrick Edward kila asubuhi na usiku mpaka atakapopata nafuu au kupona kabisa. Ufafanuzi wa daktari Johnson ulimpa picha kamili Nasrat Abdul al Aziz. Aliamini Amani Collence ameanzisha vita aliyopanga siku nyingi.

Suala la Derrick Edward kukamatwa halikumuumiza Nasrat Abdul al Aziz kwa sababu Derrick Edward alikuwa adui yake kipindi hicho, kilichompa hofu aliamini Derrick Edward alikamatwa kwa ajili yake hivyo basi aliamini lengo kuu la Amani Collence siyo Derrick Edward bali ni yeye. Alifikiria hivyo kwa sababu aliamini Amani Collence hajamkamata Derrick Edward kwa kigezo cha kuwa askari mpelelezi, alijihakikishia kuwa hiyo haikuwa sababu kwa sababu Amani Collence alikuwa afahamu suala hilo. Kichwa kilimuuma sana Nasrat Abdul al Aziz. Akili ikamwambia lazima amuue Derrick Edward ili awe salama. Kwake Derrick Edward alikuwa adui mkubwa kuliko Amani Collence, aliamini Derrick Edward akiwa hai anaweza kumsumbua katika kazi zake kwa sababu askari na muuza madawa ya kulevya hawawezi kukaa zizi moja, vile vile aliamini suala la Derrick Edward kuwa hai akiwa katika ngome ya Amani Collence ni tishio la usalama wake na siri zake. Aliamini Derrick Edward anaweza kutoa taarifa zake za namna yoyote kwa Amani Collence, taarifa zinazoweza kuwa chanzo cha kutekwa au kuuliwa na kundi hilo. Aliona maamuzi ya kumuua Derrick Edward yalikuwa sahihi kwa asilimia mia moja, lakini moyo ulikataa baada ya kufikiria kiumbe kilichokuwa tumboni kwake. Alifikiria namna ya kumuua baba wa mwanae. Alijiuliza swali kichwani kwake

“Nitamwambia nini mwanangu akiwa mkubwa? Hivi nitakuwa na ujasiri wa kumwambia nilimua baba yake kwa sababu alikuwa adui yangu?”

Alikosa jibu la swali lake, lakini hakubadilisha mawazo ya kwanza. Aliamini alichopanga awali ndicho sahihi. Lazima aondoe maisha ya Derrick Edward ili ajiweka mazingira salama. Nasrat Abdul al Aziz alimtazama vizuri daktari Johnson aliyekuwa pembeni yake akichezea simu kisha akatabasamu, akainuka akachukua jagi la maji lililokuwa juu ya meza akamimina katika glasi akanywa fundo tatu. Akarudisha glasi mezani. Akatabasamu kwa mara nyingine kisha akamwambia daktari Johnson

“Yatupasa kuchukua maamuzi magumu, yatupasa kuondoa maisha ya Derrick haraka iwezekanavyo”

Kauli ya Nasrat Abdul al Aziz ilizua utata katika kichwa cha daktari Johnson, kauli ile ilimaanisha daktari Johnson achukue jukumu la kumuua Derrick Edward kwa sababu yeye pekee ndiye aliyekuwa na idhini ya kuingia na kutoka katika ngome ngumu iliyo chini ya mtukutu Amani Collence. Japokuwa daktari Johnson alikuwa bega kwa bega na Nasrat Abdul al Aziz lakini katika suala la kumuua Derrick Edward aliingiwa na hofu. Alijua lazima Amani Collence atabaini na atakuwa amejiweka wazi dhidi ya maadui zake. Kifo kingekuwa halali yake

“Unamaanisha nimuue Derrick?”

Nasrat Abdul al Aziz alitikisa kichwa juu chini akimaanisha ndicho alichomaanisha. Daktari Johnson aliinamisha kichwa chini kisha akakiinua, akamkazia macho mrembo wa Kiarabu kisha akamwambia

“Unafikiri itakuwaje endapo wakibaini kuwa nahusika na suala hilo?”

Nasrat Abdul al Aziz alicheka kwa sauti, kicheko chake kilimaanisha aliulizwa swali la kitoto. Alimjibu daktari Johnson kwa bashasha ya hali ya juu

“Hakuna atakayeweza kukugusa ukiwa katika himaya yangu, nafikiri unaelewa nguvu ya kundi langu. Nafikiri unajua kila kitu”

Daktari Johnson hakuwa na swali lolote, aliafiki kauli ya Nasrat Abdul al Aziz. Mpango wa kuumua Derrick Edward uliiva, waliafikiana daktari Johnson akienda kumuangalia Derrick Edward asubuhi ya siku inayofuata lazima atimize kazi ya mauaji. Katika makubaliana yao, Nasrat Abdul al Aziz alimwambia daktari Johnson kuwa kabla hajaondoa uhai wa Derrick Edward amfahamishe kuwa ana kiumbe chake katika tumbo la Nasrat Abdul al Aziz, lazima Derrick ajue kama ana mimba. Nasrat Abdul al Aziz alimwambia daktari Johnson suala hilo kwa sababu aliamini ni jambo la kheri Derrick Edward kufahamu juu ya mtoto wake aliye njia kuingia katika uso wa dunia.

Ndege wa angani walisikika wakipiga kelele za kuikaribisha siku mpya, hakika ilikuwa siku mpya haswa, tarehe ya jana haikuwa tarehe ya siku hiyo. Walitoka tawi moja na kuhamia tawi lingine, furaha waliyokuwa nayo haikuwa kifani. Furaha ya ndege hao ilikuwa tofauti sana na mioyo ya watu wengi, watu wengi hawakuwa na furaha hata kigodo, walikuwa kwenye mawazo mazito ya kufanya mauaji ya kijana mbichi aliye mikononi mwa Amani Collence. Ilikuwa imefika asubuhi iliyoandaliwa kuondoa maisha ya Derrick Edward, kila mpango ulioandaliwa ulikuwa ukienda kama ulivyopangwa. Dokta Johnson alikuwa akipiga hatua ndani ya ngome ya Amani Collence akielekea katika chumba alicholazwa Derrick Edward, akili yake iliwaza kuuwa na siyo kutibu. Siku hiyo alipanga kuisaliti kazi yake, kazi aliyoifanya miaka mingi ya kuokoa maisha ya watu kupitia taaluma yake. Siku hiyo alikuwa tayari kuuwa kwa kutumia sumu aina ya ‘Strychinine’. Sumu hiyo hupatikana kwenye mmea uitwao ‘Dog Button Plant’, kitaalamu mmea huo hufahamika kama ‘Strychnos nux – vomica’.

Mmea huo huzalisha sumu kali sana ambayo hushambulia misuli ya mwili mzima, hufanya misuli yote ya mwili wa binadamu kukakamaa sana na kupelekea kifo baada ya masaa mawili mpaka matatu. Mmea unaozalisha sumu hiyo hupatikana bara la Asia katika nchi za India, Sri Lanka, Australia na baadhi ya mataifa mengine yanayopatikana kwenye bara hilo. Sumu ya ‘Strychnine’ ni chungu na isiyo na rangi ambayo huweza kutengenezwa katika mfumo wa hewa (breathed in) au kama poda inayoweza kuchanganywa katika kimiminika na kuchomwa mtu katika mshipa (intravenously). Sumu hiyo ina nguvu sana kwa sababu hata kiasi kidogo sana hutosha kuondoa maisha ya watu. Mtu anayechomwa au kuvuta suu hiyo humchukua robo saa mpaka saa moja kuonesha dalili za kuathirika.

Daktari Johnson aliingia katika chumba alicholazwa Derrick Edward, alimkuta akiwa macho wazi. Suala lile lilimaanisha fahamu zake zilirudi mahala pake, alitabasamu usoni lakini moyoni alikuwa na hofu. Alitamani amkute akiwa amelala fofofo ili amchome sumu ya ‘Strychnine’ kwa urahisi pasipo kuulizwa maswali yoyote na mgonjwa huyo. Kwa upande wa pili suala la kumkuta macho Derrick Edward ilikuwa hatua nzuri ya kutimiza kazi aliyopewa, kazi ya kumfahamisha kuwa Nasrat Abdul al Aziz alikuwa ana ujauzito wake. Derrick Edward alikuwa peke yake chumbani, hapakuwa na mtu yeyote ambaye angeweza kuharibu mpango wa daktari Johnson. Ilikuwa furaha kwake. Daktari Johnson alifika mbele ya Derrick Edward kisha akamsalimia, Derrick Edward aliitika kwa shida sana. Kipindi Derrick Edward akiitika salamu ya daktari Johnson akilini alikuwa akiwaza wapi alipowahi kumuona mtu huyo, haikuwa sura ngeni hata kidogo. Aliumiza kichwa, kumbukumbu ikamjia kuwa alishawahi kumuona daktari huyo katika makazi ya Nasrat Abdul al Aziz. Kichwa kilimuuma zaidi, akashindwa kuelewa daktari yule anafanyaje kazi kwa mabwana wawili wenye chuki kati yao. Aliamini kuna siri nzito iliyojificha. Ghafla alishitushwa na kauli ya daktari Johnson

“Wajionaje na hali kijana?”

Derrick Edward alijibu kuwa anajisikia vizuri lakini kichwa na mbavu vinauma sana. Daktari Johnson alielewa sababu ya hali hiyo, alielewa kipigo alichokipata kilisababisha hali hiyo. Hakujali jibu la Derrick Edward, yeye alikuwa tayari kutimiza kazi iliyompeleka mahali pale, kazi ya kuondoa maisha ya Derrick Edward. Daktari Johnson alimkazia macho Derrick Edward kisha akamwambia

“Sikiliza kwa makini kijana, nina habari njema toka kwa Nasrat”

Kauli ya daktari Johnson ilimshangaza sana Derrick Edward, alishangaa kusikia kuwa daktari huyo alikuwa na habari njema kutoka kwa Nasrat Abdul al Aziz. Akili ya Derrick Edward ilienda mbali sana. Aliamini hakuwa salama hata kidogo, kauli ile ilimaanisha kifo mbele yake, aliamini Nasrat Abdul al Aziz alishafahamu kama yeye ni polisi mpelelezi hivyo basi lazima afanye mpango wa kumuua kabla ya kupambana na maadui wengine. Alitamani apige kelele za kuomba msaada kutoka kwa majambazi lakini mwili ulikataa, maumivu makali yalisambaa ghafla toka kidoleni mpaka utosini. Mapigo ya moyo yakaongezeka maradufu, macho yakamtoka pima. Derrick Edward aliamini hawezi kukwepa kifo kilichokuwa mbele yake. Alimtazama daktari Johnson kwa jicho la hasira kisha akaongea kwa tabu sana

“Coward! Today I`ll be dead, tomorrow is your time” (Mwoga! Leo nitakufa, kesho ni wakati wako)

Ilikuwa kauli ya kishujaa, kauli iliyomaanisha hakuogopa kuuliwa wala hakuogopa kifo. Kauli yake haikubadilisha mawazo ya daktari Johnson, daktari Johnson alikuwa tayari kutimiza kazi aliyopewa na Nasrat Abdul al Aziz. Alitabasamu kama mtu aliyefurahishwa na kauli ya Derrick Edward lakini tabasamu lake halikuwa na uhalisia wa aina yoyote, alijaribu kuukwepa ukweli uliotamkwa na mgonjwa, ukweli uliomaanisha kuwa alikuwa muoga. Hakika aliuona uwoga wake, uwoga wa kutimiza kauli za magaidi kuliko kufanya kazi zake. Aliendelea kutabasamu kinafiki, akakaa katika kiti alicholala Derrick Edward kisha akavua begi dogo lililokuwa mgongoni. Hakutaka kujibu kauli ya Derrick Edward kwa sababu alihofia kuharibu kila kitu, yeye alihitaji kutimiza kazi aliyopewa. Alikumbuka msisitizo wa Nasrat Abdul al Aziz, msisitizo wa kumwambia Derrick Edward kuhusu mtoto wake aliye tumboni. Daktari Johnson alimshika mkono Derrick Edward akauchezesha chezesa juu chini, Derrick Edward alilalamika kuumia kwa kitendo kile. Mwili wa Derrick Edward ulikuwa kama donda, ulimuuma sana kila uliposumbuliwa. Daktari Johnson aliurudisha mkono wa Derrick Edward mahali pake.

Siyo kwamba daktari Johnson alishika mkono wa Derrick Edward na kuuchezesha chezesha bila sababu, hapana, bali kipindi alipoushika na kuuinua macho yake yalikuwa makini kuangalia misuli ya Derrick Edward inayopatikana kwenye mkono ule, alikuwa akiangalia msuli upi autumie kupitisha dawa yake. Hakuna msuli aliouona, misuli yote ilikuwa imesinyaa kabisa. Misuli ilirudi ndani zaidi. Suala hilo halikumuumiza kichwa daktari Johnson, alijisemea moyoni kuwa ataichanganya sumu katika dripu ya maji aliyopanga kumuwekea mgonjwa wake. Hakuona sababu ya kushindwa kutimiza zoezi lake. Alitabasamu kwa mara nyingine kisha akamkazia macho Derrick Edward, akamwambia

“Sikiliza kijana, nilikwambia nina habari njema kutoka kwa Nasrat lakini kabla sijakwambia habari yenyewe ukaanza kuongea mambo ya ajabu. Mimi ni mgeni mwema kwako, nimetumwa na Nasrat nijaribu kuokoa maisha yako, lakini jambo la msingi unalotakiwa kujua ni kwamba Nasrat Abdul al Aziz ana ujauzito wako”

Ilikuwa kauli ya kumshangaza sana Derrick Edward, alimkazia macho daktari Johnson kama mtu aliyemwambia hajaelewa chochote alichomwambia lakini haikumaanisha chochote. Daktari Johnson aliendelea kutoa ufafanuzi wa kauli yake, ufafanuzi ulioendelea kumshangaza na kumstaajabisha Derrick Edward

“Nasrat anakupenda sana ndiyo maana kanituma nije kutafuta njia ya kuokoa maisha yako, nipo katika njia hiyo na nina uhakika lazima njia hiyo ifanikiwe. Baada ya masaa mawili tutakuwa nje ya jumba hili, namaanisha utakuwa kwa Nasrat”

Kauli ya daktari Johnson ilikuwa na maana tofauti sana, hakumaanisha kuwa Derrick Edward ataonana na mpenzi wake baada ya masaa mawili, hapana, bali iliamini baada ya masaa hayo lazima Derrick Edward atakuwa maiti baada ya kushambuliwa na sumu ya ‘Strychnine’. Derrick Edward aliendelea kumkazia macho daktari Johnson huku akilini akiendelea kufikiria kauli aliyoambiwa kuhusu ujauzito wa Nasrat Abdul al Aziz, alifikiria uadui ulioibuka kati yake na Nasrat Abdul al Aziz akaishiwa nguvu kabisa.
Derrick Edward hakuwa mjinga wa kuamini maneno ya daktari Johnson kuwa eti Nasrat Abdul al Aziz amemtuma kumuokoa toka kwenye mikono ya Amani Collence, aliamini kuwa siri ipo katikati. Aliamini siri hiyo itakuwa imezungukwa na kauli ya kifo, aliamini lazima auliwe japokuwa Nasrat Abdul al Aziz alikuwa na ujauzito wake. Derrick Edward alikumbuka kauli aliyowahi kuambiwa na Nasrat Abdul al Aziz kipindi mapenzi yao yalipokuwa moto, aliwahi kumwambia

“Huwa sipendi kumficha mtu kitu halisi anachotakiwa kujua, hata kama mtu huyo yupo hatua ya mwisho ya maisha yake. Lazima nifanye juu chini ajue”

Derrick Edward alitabasamu, sasa aliamini kauli hiyo ilikuwa na maana kubwa kwake siku hiyo. Aliamini Nasrat Abdul al Aziz alimtuma daktari huyo amfahamishe kuhusu ujauzito wake lakini kumfahamisha huko siyo sababu ya kuokoa maisha yake. Alielewa lazima wampoteze. Derrick Edward akamfikiria mtoto wake aliye tumboni mwa adui yake, moyo ulimuuma sana endapo akiuliwa na kumuacha mwanae katika sura ya dunia. Alijisemea moyoni

“Mungu niokoe kijana wako”

Machozi yalitengeneza mifereji katika mashavu yake, hakutoa sauti ya kilio lakini kilio kilikuwa moyoni, kilio kilimpeleka mbali sana na kumkumbusha maisha aliyopitia. Machozi yaliendelea kutiririka kama maji yateremkayo bondeni kila alipokumbuka maisha yake. Alikumbuka kauli ya shangazi yake, kauli aliyoapa kuiishi nayo mpaka siku ya mwisho ya maisha yake. Machozi yakaendelea kutiririka kama maji. Kilikuwa kitendo cha kustaajabisha na kushangaza kwa daktari Johnson, lakini aliapa kutokurudi nyuma, aliapa kutimiza kazi ya Nasrat Abdul al Aziz.

ITAENDELEA
FB_IMG_1652590582916.jpg
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA KUMI NA MOJA)

RWAMA MWISHO – MWAKA 1995
Baridi kali iliendelea kupenya katika mishipa ya msichana mrembo aliyeinama chumbani kwake akilia kilio kikali kilichoambatana na kwikwi, siyo kwamba alikosa mtu wa kumtuliza au kumnyamanzisha, hapana, bali hakuhitaji kusikia kauli ya mtu yeyote katika chumba chake. Alidhamiria kujitesa na ikiwezekana kuchukua maamuzi magumu, maamuzi ya kuiacha dunia. Alikuwa amefunga mlango wa chumba chake ili kuzuia mtu kuingia. Kitendo kile kilimuudhi sana mama yake mzazi aliyekuwa akiendelea kugonga mlango huo kwa lengo la kuingia kumtuliza binti yake, binti hakujali mahangaiko ya mama yake. Moyo ulimuuma sana kwa kilichokuwa kikiendelea, kitendo cha kumzuia mama yake kuingia chumbani lakini aliendelea kuwa na msimamo wake. Mama yake alijenga nyumba hiyo kwa shida iliyokithiri, aliunga unga pesa na kufanikiwa kujenga nyumba ya vyumba vitatu. Nyumba iliyoanza kujengwa tangu binti yake akiwa mtoto wa miaka minne mpaka kipindi hicho akiwa na miaka ishirini na mbili ilikuwa haijakamilika kwa asilimia mia moja. Ilikuwa haijapakwa rangi yoyote, matofari yalikuwa wazi yakiwasalimia kila siku iliyoitwa leo. Magreth Peter aliendelea kulia kama kawaida, alisikia kauli ya mama yake ikimwambia

“Unataka kuniua kwa presha we mtoto, unataka nife”

Hakika mama yake alimaanisha kauli aliyoongea, alikuwa akiumwa ugonjwa wa moyo kwa miaka mingi, tangu Magreth Peter akiwa shule ya msingi. Daktari alimshauri ajiepushe na mawazo yasiyo na kichwa wala miguu, alitakiwa kuishi kwa amani ili autulize moyo wake. Suala la mwanae kulia akiwa kajifungia chumbani ilikuwa ni sawa na kumsogeza katika mlango wa kaburi. Mwanae alimpa mawazo kemkem, mawazo aliyoshindwa kuyakwepa kwa sababu yeye ndiye aliyestahili kupambana nayo. Kauli ya mama yake iliendelea kusikia katika masikio yake, sasa aliamini anaweza kumpoteza mama yake kisa tatizo lake. Magreth Peter alisogea taratibu mpaka mlangoni kisha akafungua. Alimkuta mama yake akiwa amekaa mlangoni, machozi yakiwa yamelowanisha mashavu yake. Mama yake alimtazama kwa jicho la huruma mwanae kisha akamwambia

“Wewe siyo mtu wa kwanza kuachwa katika hali kama hii. Yakupasa kumlea mwanao kama nilivyokulea mimi. Yakupasa upambane ili mwanao ajivunie kuwa na mama kama wewe”

Maneno ya mama yake yaliyoathiriwa kwa sauti ya kilio yalipenya vizuri katika masikio ya Magreth Peter. Magreth Peter alikuwa na mimba ya miezi tisa, alikuwa mbioni kujifungua lakini hali ilikuwa tofauti kwa upande wa mwanaume. Ukoo wa mwanaume haukutaka kulisikia hata jina lake. Alichukiwa na kila mmoja kwa sababu waliamini amemrubuni mtoto wao. Walisema hivyo kwa sababu Magreth Peter alikuwa mtoto wa kimasikini lakini mtoto wao alitoka familia bora yenye pesa kemkem. Tena siyo familia pekee, bali hata kijana wao alijiweza kwa kila kitu. Kijana huyo aliyefahamika kwa jina la Edward Lewis alikuwa Kapteni (Captain) wa jeshi mwenye nyota tatu begani katika jeshi la taifa la Malosha. Japokuwa familia ya Edward Lewis haikumpenda wala kumjali Magreth Peter, hali ilikuwa tofauti kwa Edward Lewis. Yeye alimpenda Magreth Peter kichwa kuuma, alikuwa haambiliki kuhusu mwanamke huyo aliyekuwa akinuka umasikini uliokithiri. Mara kadhaa alipishana kauli na familia yake kwa sababu ya Magreth Peter.

Penzi lao lilikumbwa na vikwazo lakini vikwazo hivyo viliwaongezea nguvu ya kulipigania. Vikwazo vilizidi, ikafika kipindi mama Magreth Peter vilimuudhi, akampiga vita mwanae kuendelea kujihusisha kimapenzi na Edward Lewis kwa sababu aliona namna walivyokuwa wakidharauliwa na kutishiwa kuondolewa maisha. Magreth Peter mara kadhaa aliiambia akili yake kuwa mama yake alikuwa sahihi hivyo lazima ikubaliane nae, akili haikuwa na shida ilikubali kwa asilimia mia moja lakini moyo ulikataa. Moyo ulikataa kumuacha Edward Lewis, mwanaume aliyeapa kuishi nae milele. Vikwazo vilipozidi waliachana mbele ya macho ya watu lakini mafichoni waliendelea kukutana na kufurahia penzi lao. Waliapa kufunga ndoa ya serikali ili kukwepa vikwazo vya ndugu zao. Walikuwa na lengo la kuishi pamoja. Japokuwa simu zilikuwa adimu na gharama kipindi hicho lakini Magreth Peter aliimiliki, alinunuliwa na mpenzi wake kwa lengo la kurahisisha mawasiliano.

Miezi ilisogea kama kawaida. Sijui ilikuwa bahati mbaya au nzuri kwa Magreth Peter kwa sababu alipata mimba pasipo kutarajia. Awali aliogopa kumwambia Edward Lewis kwa sababu hawakupanga kupata mtoto kipindi hicho, alihofia kupewa majibu mabaya. Alijikaza kisha akamueleza mpenzi wake kuhusu ujauzito wake. Usilolijua ni kama usiku wa giza, Edward Lewis alifurahi sana kusikia mpenzi wake alikuwa na ujauzito wake. Alijiona akielekea kuitwa baba. Aliamini sababu hiyo labla ingetuliza mchecheto wa familia yake. Kila alipopanga kuwaambia alihairisha kwa sababu kipindi hicho familia ilifahamu alikuwa ameshaachana na Magreth Peter miezi kadhaa nyuma, hawakujua kama penzi lilikuwa likiendelea mafichoni. Magreth Peter alimwambia mama yake, japokuwa ilikuwa ngumu kueleweka lakini mwisho wa siku alieleweka. Mama ni mama siku zote, mama hawezi kumtupa mwana. Miezi ilisogea tena na tena. Miezi tisa ilifika na walitegemea kupata mtoto ndani ya siku yoyote, lakini kipindi chote hicho Edward Lewis alikuwa hajaifahamisha familia yake kuhusu suala la ujauzito wa Magreth Peter.

Siku hiyo Magreth Peter alikuwa akilia sana baada ya kupokea taarifa mbaya kutoka kwa dada yake Edward Lewis, mtu aliyekuwa akimchukia siku zote. Alishangazwa sana kupokea ujumbe toka kwa mwanamke yule, lakini suala hilo halikuwa sababu ya yeye kuangua kilio, bali ujumbe aliotumiwa ndiyo uliomuumiza sana. Ujumbe ule ulisema

“Habari, najua hatupo sawa kimahusiano lakini nachotaka kukujulisha ni juu ya suala la kaka. Edward amelazwa hospitali ya taifa. Kama umesikia kuna wanajeshi waliopambana kwa kurushiana risasi na kundi la wauza madawa ya kulevya lakini kwa bahati mbaya wawili wakashambuliwa vibaya, basi mmoja kati ya hao wanajeshi wawili ni kaka Edward. Kaka ana hali mbaya sana, ameniambia kabla hajafumba macho anataka kuongea na wewe. Najua nimekukosea sana lakini naomba unisaidie jambo hili. Nakuomba sana Magreth. Ni mimi Catherine”

Magreth Peter aliogopa sana baada ya kupokea ujumbe ule kutoka kwa Catherine Lewis, alielewa hali ya Edward Lewis inawezekana kuwa mbaya zaidi ya alivyoelezwa. Aliamini suala la Catherine Lewis kumtumia ujumbe ukimuomba na kumbembeleza aende kuonana na Edward Lewis lilimaanisha kifo cha Edward Lewis, lilimaanisha Edward Lewisbalikuwa kwenye hatua za mwisho za kuupigania uhai wake. Magreth Peter aliamini ule msemo wa ‘mbuzi wa masikini hazai’ alitungiwa yeye. Alijiona kuwa na gundu au mkosi. Alifikiria hivyo hata kabla hajachukua maamuzi ya kwenda alipoitwa. Akili nyingine iliwaza kwanini Catherine Lewis hakumpigia simu? Kwanini amtumie ujumbe kama jambo hilo ni muhimu sana kiasi hicho? Alihisi labda kuna namna au mtego ametegea na familia ile, lakini moyo ulikataa kuhusu mtego. Alijiuliza mwenyewe

“Hivi Catherine angenipigia simu ningepokea?”

Jibu la swali hilo lilikuwa hapana, sasa alipata jibu la kwanini Catherine Lewis aliamua kumtumia ujumbe badala ya kumpigia simu. Kipindi ujumbe ule ukiingia kwenye simu yake, alikuwa jikoni na mama yake wakisaidizana kuandaa chakula cha usiku huo. Sura ilimbadilika ghafla, akajikuta akishindwa kuendelea kuandaa viungo vya mboga vilivyokuwa mbele yake. Alianza kutetemeka kama mtoto mdogo, mama yake aliona hali ile akamuuliza mtoto wake

“Kuna nini Magreth? Mbona umebadilika ghafla!”

Magreth Peter alitamani amuelezee mama yake kwa kutumia kinywa chake lakini mdomo uligoma kufungua, alijitahidi kuulazimisha lakini alikuwa akitwanga maji kwenye kinu. Mdomo ulimtetemeka sana. Hali ile ilimpa hofu sana mama yake, akasogea haraka alipokaa mwanae kisha akamshika bega, alishuhudia mwanae alivyokuwa akipambana kutaka kuongea lakini kinywa kikiwa kigumu. Alikuwa amechanganyikiwa kabisa. Mama yake alimlazimisha amwambie chochote ili apate mwanga wa kumsaidia. Magreth Peter hakuwa na kauli yoyote, alimkabidhi mama yake simu. Mama yake aliipokea kwa mkono wa kulia kisha akaiangalia. Simu ilikuwa kwenye uwanja wa ujumbe. Hapo ndipo alipokutana na ujumbe mzito, ujumbe uliobadili taswira ya mwanae ndani ya muda mfupi.

Kipindi mama yake akiendelea kuruhusu mshangao katika sura yake, ghafla Magreth Peter aliinuka na kukimbilia chumbani kwake akilia kama mtoto. Hakuishia kuingia chumbani tu, la hasha, bali alifunga mlango kwa ufunguo. Hakutaka kunyamanzishwa na mtu yeyote. Alivua nguo zilizomkinga na baridi akazitupa ovyo, hakujali hali ya baridi iliyokuwa ikiushambulia mwili wake, hakujali kabisa kwa sababu aliamini hata kama akijali hali hiyo haitabadilisha maana yoyote. Aliendelea kulia huku akilini akifikiria kujidhuru. Wazo la kujiua lilimjia kichwani. Muda wote aliendelea kusikia sauti ya mama yake ikimbembeleza kwa shida sana afungue mlango ili wazungumze mawili matatu yatayoweza kuwapa njia ya kupita. Sauti ya mama yake iliendelea kumuita mpaka ikaanza kukauka, sauti ya mwisho ya mama yake ilikuwa

“Unataka kuniua kwa presha we mtoto, unataka nife”

Hakutaka kumuuwa mama yake kwa presha, alifungua mlango na kukutana naye uso kwa uso. Mama yake alimsihi maneno mawili matatu kisha akamchukuwa na kuelekea jikoni. Alimkalisha kwenye mkeka aliokuwa amekaa awali kisha akarudi chumbani kwa Magreth Peter akachukua blanketi nzito na kurudi nayo jikoni, alimfunika mwanae ili asiendelee kuadhibiwa na baridi iliyozaliwa na hali ya mvua iliyokuwa ikiendelea. Mama Magreth Peter alipohakikisha mwanae alikuwa salama kimavazi, alikaa kitako kisha akamwambia kwa msisitizo

“Mimi na wewe tunajua namna tunavyodharauliwa na familia ya yule kijana, mbaya zaidi hawajui kama mimba uliyoibeba ni ya kijana wao. Wao wanakutusi na kukuita malaya kwa kukusema eti umebebeshwa mimba ukiwa nyumbani na vijana wa mtaani…Hawajui kama mimba ni ya mtoto wao. Sikutaka kuisumbua familia yake kwa sababu nilihofia usalama wako na wangu, bora nipambane na wewe mpaka siku ya mwisho”

Mama Magreth Peter akaangalia mapishi yake yaliyokuwa jikoni, alipoona yalikuwa salama salimini akamgeukia mwanae kisha akaendelea

“Ujumbe uliotumiwa unasema Edward ana hali mbaya, amelazwa katika hosiptali ya taifa na unahitajika kwenda ukaonane naye. Kumbuka huendi kuiangalia familia ya Edward, familia iliyokukataa toka awali, bali unaenda kumtazama mwanaume aliyekupigania tangu siku ya kwanza. Usisite kwenda, nenda kamuone kijana wa watu, anaweza kuwa kwenye hali ya uhai au kifo. Nenda mwanangu usije kujuta kuacha kwenda, nenda mama”

Maneno ya mama yake yalimuingia vizuri. Aliona umuhimu wa kwenda kumuona Edward Lewis, aliona umuhimu wa kwenda kumuona mwanaume aliyempatia ujauzito wake. Alilitazama tumbo lake lililokuwa limeshatimiza miezi tisa, tumbo lililokuwa tayari kutoa mtoto na kumleta katika sura ya dunia. Magreth Peter alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha ilikuwa saa nne na robo usiku. Mapigo ya moyo yakaongeza kasi, akaona alikuwa nje ya muda wa kuona wagonjwa. Aliamini hata akienda hospitali hataruhusiwa kuingia ndani. Alimtazama mama yake huku machozi yakimtoka kimya kimya. Alikuwa tayari kulia kama awali. Alimwambia

“Mama, hata nikienda sitaruhusiwa kuingia kumuona Edward, nipo nje ya muda wa kuona wagonjwa”

Ilikuwa zamu ya mama yake kustaajabu. Alishika kichwa akakiachia mara akashika kiuno, bado hali ilikuwa tete. Walichanganyikiwa. Akili ya Magreth Peter ilimsisitiza kwenda hospitali, ilimwambia suala la kuingia au kutoingia litafahamika akifika eneo la hospitali. Magreth Peter alimwambia mama yake

“Naenda hospitali, mpigie yule kijana wa Taxi aje kunichukua”

Ilikuwa kauli ya kishujaa sana, kauli iliyomuacha mdomo wazi mama yake. Hakuwa Magreth Peter aliyekuwa akilia dakika chache zilizopita, bali alikuwa Magreth Peter jasiri aliye tayari kupambana na hali yoyote itakayojitokeza mbele yake. Kipndi mama yake akitafuta jina la kijana wa Taxi, ghafla simu ya Magreth Peter ikaanza kuita. Magreth Peter aliichukua haraka kisha akatazama jina la aliyekuwa akimpigia, haikuwa namba ngeni bali ilikuwa namba iliyomtumia ujumbe kuhusu Edward Lewis. Alikuwa Catherine Lewis. Magreth Peter alielewa Catherine Lewis aliamini lazima atapokea simu baada ya kusoma ujumbe ule, ndivyo ilivyokuwa. Magreth Peter alipokea simu kisha akaweka sikioni. Alikutana na salamu iliyojaa hofu, salamu iliyoonesha iliathiriwa na kilio cha muda mrefu. Magreth Peter alijikaza na kuitikia salamu ile, Catherine Lewis alimuuliza

“Umechukua uamuzi gani kuhusu ujumbe niliokutumia?”

Swali lilimaanisha anaenda kumuangalia Edward Lewis au haendi, hakika ndivyo lilivyomaanisha. Magreth Peter alibaki na bumbuwazi, akatazama saa yake ya mkononi kwa mara nyingine ikamuonesha kuwa ilikuwa saa nne na nusu. Akapata jibu la kumjibu Catherine Lewis. Akamwambia

“Nipo nje ya muda, hata nikienda siwezi kuruhusiwa kuingia”

Catherine Lewis alielewa hofu ya Magreth Peter na aliona alivyokuwa sahihi kwa upande wake. Catherine Lewis alimfafanua

“Hivi tunavyoongea nipo nje ya nyumba yenu. Kama upo tayari twende ukaonane na kaka yangu, kuhusu suala la wewe kuingia saa hizi usiwe na hofu. Hakuna asiyejua kuhusu taarifa yako, walinzi wote pamoja na watoa huduma za afya walio zamu wanafahamu unavyosubiriwa kwa hamu kubwa…usituangushe Magreth”

Kuali hizo zilimchanganya sana Magreth Peter, eti kila mmoja anafahamu umuhimu wake wa kwenda hospitali kumuangalia Edward Lewis, hakuna wa kumzuia hata kama yupo nje ya muda. Eti Catherine Lewis amemfuata kumchukua kama yupo tayari kwenda! Sasa aliona umuhimu wa kwenda, aliona asipoenda anaweza kujutia kipindi chote cha maisha yake yaliyobaki duniani. Alimtazama mama yake aliyekuwa kimya akisubiria kuambiwa kilichokuwa kikiendelea kwenye simu kisha akamwambia

“Catherine yupo nje ya nyumba amekuja kunichukua niende hosiptali”

Mama yake alikubali kwa kichwa, kipindi Magreth Peter akimuelezea mama yake simu ilikuwa bado ipo sikioni hivyo Catherine Lewis alisikia mazungumzo yao. Magreth Peter akamwambia

“Nakuja sasa hivi”

Ndivyo ilivyokuwa. Baada ya dakika kadhaa Magreth Peter aliyeongozana na Catherine Lewis waliingia katika chumba alicholazwa Edward Lewis. Alikuwa amelazwa katika wodi maalumu, wodi ambayo hulazwa watu wenye nyadhifa serikalini au watu wenye pesa. Chumba kilikuwa na watu wanne, baba na mama yake Edward Lewis, daktari mmoja pamoja na muuguzi aliyekuwa akimsaidia daktari kutoa huduma. Wazazi wa Edward Lewis walipomuona Magreth Peter walikunja ndita wakidhihirisha chuki ya wazi dhidi yake. Hawakuwa na jinsi kuruhusu binti yule kuingia ndani ya wodi hiyo kwa sababu lilikuwa shinikizo la mtoto wao. Baada ya salamu Catherine Lewis alimsogeza Magreth Peter mpaka jirani zaidi ya kitanda alicholala kaka yake kisha akaongea

“Kaka, Magreth amefika”

Kauli ya Catherine Lewis ilisababisha Edward Lewis afumbue macho yake aliyokuwa ameyafumba. Alimtazama Magreth Peter aliyekuwa na sura ya hofu baada ya kuona chuki ya wazi kutoka kwa wazazi wa Edward Lewis, akajilazimisha kutabasamu lakini mwili ulikataa. Maumivu yalimwambia hapaswi kutabasamu. Akarudisha tabasamu lake mahali lilipokuwa kisha akaongea kwa shida sana

“Baba, mama na dada napenda mjue kuhusu mwanamke huyu, najua mnajua nilikuwa kwenye mahusiano nae lakini hamjui ujauzito alionao ni wangu. Napenda ifahamike hivyo”

Ilikuwa kauli ya kushangaza hasa, hakuna aliyetegemea kuisikia. Siyo kwamba walishangaa ndugu wa Edward Lewis pekee, hapana, hata Magreth Peter hakutarajia kusikia kauli ile, kauli ya Edward Lewis kuwaelezea suala la mimba yake katika mazingira yale. Lilikuwa tukio la kushangaza lililochukua hisia za kila mmoja ndani ya chumba kile cha matibabu. Edward Lewis hakujali hali zao, yeye alitaka kuongea ukweli kuhusu uhusiano wake na Magreth Peter, alitaka familia yake ijue kila kitu kabla hajaingizwa katika chumba cha upasuaji mkubwa kilichokuwa kikimsubiri kwa lengo la kuondoa risasi mwilini mwake. Hakuwa na uhakika wa kutoka salama. Ulikuwa ni mchezo wa kifo na kupona kwa sababu aliambiwa risasi zilipenya katika sehemu hatari sana, daktari hawakumwambia ni sehemu gani. Wao walimwambia anahitaji utulivu wa mwili na akili kabla hajaingizwa kwenye chumba cha upasuaji. Edward Lewis alielewa maana ya kauli za madaktari, alielewa maisha yake yalikuwa njia panda ndiyo maana alifichwa hali yake halisi. Aliamini endapo akifariki kabla ajaacha neno lolote kwa familia yake juu ya Magreth Peter angekuwa hajafanya jambo la maana katika kipindi chote cha maisha yake. Baba yake alitaka kuropoka baada ya kusikia kauli ya mwanae lakini kabla sauti haijatoka alizuiliwa na mke wake. Mke wake alielewa kuwa baba Edward Lewis alitaka kuongea nini, alikuwa akielewa kuwa mzee huo alikuwa kikwazo kikuu cha mahusiano ya Edward Lewis na Magreth Peter. Hivyo kama angeruhusu sauti ya mume wake itoke ingeleta sura mbaya mbele ya daktari na muuguzi waliokuwa wakiendelea kuandika taarifa ya Edward Lewis.

Mzee Lewis Kalikumbi alikuwa akimiliki magari mengi ya masafa marefu, alikuwa tajiri aliyesafirisha watu kutoka nchini Malosha mpaka nchi za jirani. Alikuwa tajiri sana kipindi hicho. Mzee Lewis Kalikumbi alihitaji mwanae amuone mtoto wa rafiki yake aliyekuwa na hisa katika biashara yake, alitaka afanye hivyo ili aendelee kulinda mali zake. Alifanikiwa kumshawishi rafiki yake kuwaunganisha watoto wao. Mwanzo alipata kipingamizi cha rafiki huyo lakini siku zilivyozidi kwenda hali ilikuwa nzuri kwa upande wake. Mtoto wa rafiki yake alikubali kuolewa na Edward Lewis, hakuwa na kipingamizi chochote. Pingamizi lilikuwa kwa Edward Lewis aliyezama katika penzi la mwanamke asiye na mbele wala nyuma kiuchumi, mwanamke aliyeishia darasa la saba baada ya kufaulu vizuri mitihani ya mwisho lakini akakosa pesa ya kuendelea kielemu. Akaamua kuwa msichana wa mtaani aliyeishi maisha duni, maisha ya kumsaidia mama yake kufanya biashara ndogo ndogo. Huko katika biashara hizo ndipo alipofahamiana na Edward Lewis. Edward Lewis hakuwaona wasichana warembo wa mitaani na kazini walijipamba na kupambika, yeye macho yake yalimuona msichana aliyeonekana wa kawaida sana mbele ya macho ya watu. Alipeleleza tabia za msichana huyo, hapo ndipo alithibitisha kuwa binti yule alikuwa dhahabu iliyohitaji moto ili iweze kung`aa. Hakuficha hisia zake, alimfuata na kumueleza hisia zake, haikuwa kazi rahisi kupata moyo wa binti yule. Alipanda akashuka mpaka akaweza kumpata Magreth Peter. Suala la Edward Lewis kuzama penzini kwa Magreth Peter kulimaanisha kuharibu mpango wote wa baba yake. Hapo ndipo vita ilipoanza, vita baridi yenye harufu ya damu iliyoweka kando amani na upendo. Derrick Lewis alimwambia Magreth Peter pasipo uwoga wowote

“Wewe ndiye mwanamke wangu”

Magreth Peter alikosa jibu la kutoa, alibabaika kama mtoto mbele ya wazazi na dada yake Edward Lewis. Aliuona upendo wa Edward Lewis, upendo uliomaanisha kuisaliti familia yake kwa ajili ya kulinda na kutetea penzi lao. Edward Lewis alipoona Magreth Peter akikosa uhuru wowote wa kuongea naye, pasipo uwoga wala hofu ya aina yoyote Edward Lewis aliwaambia watu wote waliokuwa ndani ya chumba chake cha matibabu

“Samahani jamani, nataka kuongea na Magreth…samahani naomba mtupishe kidogo”

Kauli hiyo iliongeza hofu katika moyo wa Magreth Peter, alitamani kumzuia Edward Lewis kuongea lakini alikuwa ameshachelewa. Sauti ya Edward Lewis ilikuwa imeshasikika kwa kila mmoja. Daktari na muuguzi walikuwa wa kwanza kuondoka. Baba, mama na dada yake walibaki na bumbuwazi. Baba yake alitoka kauli kali, kauli iliyomaanisha kuwa hawezi kuondoka kumpisha Magreth Peter kuongea na mwanae, alihisi kudharauliwa na kijana wake. Alifura hasira kama simba aliyejeruhiwa na muwindaji. Hasira zake hazikumaanisha kitu kwa Edward Lewis aliyekuwa tayari kuongea na Magreth Peter pasipo uwepo wao. Catherine Lewis aliwashika wazazi wake akawaomba waondoke mara moja kisha baada ya dakika kadhaa watarudi. Awali baba yake alikuwa mbishi lakini hakuwa na jinsi zaidi ya kutii amri ya kijana wake. Waliondokaa na kuwaacha Edward Lewis na Magreth Peter. Edward Lewis alimtazama Magreth Peter aliyekuwa haamini wala kuelewa matukio yaliyokuwa yakiendelea. Aliongea kwa shida sana

“Unajua nakupenda Magreth, najua unanipenda pia lakini maamuzi ya mapenzi yetu yataamuliwa na upasuaji wangu nitakaofanyiwa kesho asubuhi. Sijui kama nitatoka salama katika upasuaji huo, hali inaonesha kuwa tete lakini wamenificha…nachojua mimba yako ina miezi tisa, vyovyote itakavyokuwa, namaanisha niwe mzima ama nimekufa, naomba sana mtunze mwanangu”

Maneno ya Edward Lewis yalianza kumtoa machozi Magreth Peter, alihisi akiambiwa maneno ya mwisho kabla ya kifo cha muhusika. Alianza kulia kimya kimya lakini maneno ya Edward Lewis yalivyoendelea ndivyo kilio cha Magreth Peter kilipoongezeka maradufu. Edward Lewis aliendelea kumwambia

“Familia yangu haikupendi hata kidogo, hicho kipo wazi lakini usirudi nyuma. Lazima usimame kama mama katika malezi ya mwanao, lazima uwe mama bora…nilijaribu kuongea na Catherine akusaidie katika hatua zako za kujifungua lakini hakutaka kunisikia, ni mdogo wangu lakini kamezeshwa maneno mabaya na wazazi wetu. Anafanya vitu kuwaridhisha baba na mama. Anataka aonekane mwema, hajui kama ananikosea sana”

Japokuwa aliongea kwa shida lakini hakuchoka kuongea maneno aliyohisi ni msingi bora kwa Magreth Peter. Aliendelea kufafanua zaidi

“Familia ilitamani kunisafirisha nikatibiwe nje ya nchi lakini madaktari wamegoma. Wamesema hali yangu siyo nzuri, naweza nisifike wanapotaka kunipeleka. Wamesema watanishughulikia wenyewe hapa hapa kwa sababu tatizo kama langu wameshawahi kuwashughulikia watu wengine na wakapona”

Aliongea mengi sana yaliyoendelea kumtoa machozi Magreth Peter, kati ya mambo hayo Edward Lewis alimsisitiza Magreth Peter

“Naweza nisiwe hai leo au kesho, japokuwa siombi iwe hivyo lakini ikitokea, mtafute kijana mmoja anaitwa Abdul Said atakusaidia njia ya kupita. Atakusaidia kuhisi uwepo wangu”

Yalikuwa maneno magumu sana kueleweka lakini alibidi kuyaelewa hivyo hivyo, Magreth Peter hakutaka kumuuliza maswali Edward Lewis ili amfafanulie kwa sababu aliona namna alivyokuwa akiongea kwa shida sana. Aliamini akiendelea kumuhoji atakuwa akimuumiza mpenzi wake. Edward Lewis hakuishia kumpa jina la muhusika bali alimpatia mpaka namba yake ya simu. Baada ya maongezi mengine yaliyohusu mapenzi yao, Magreth Peter aliaga na kuondoka zake eneo la tukio na kumuacha Edward Lewis akiwa na amani ya moyo. Edward Lewis alihisi ameutua mzigo alioubeba muda mrefu. Alihisi hakuna kilichobaki moyoni.

Edward Lewis ni kama alitabiri kifo chake, asubuhi ya siku iliyofuata muda mfupi kabla hajaingizwa kwenye chumba cha upasuaji alifariki. Kwakuwa alikuwa mwanajeshi mwenye cheo kikubwa jeshini, habari za kifo chake zilisambaa haraka. Vile vile, waandishi wa habari walio tangaza juu ya kupigwa kwake risasi walikuwa mstari wa mbele kutangaza juu ya kifo chake. Catherine Lewis hakuwa na jinsi, aliamua kumfahamisha Magreth Peter juu ya kifo cha kaka yake. Ilikuwa taarifa mbaya sana katika masikio ya Magreth Peter, taarifa iliyompa mshituko mkubwa wa moyo. Akahisi kushindwa kupumua vizuri. Mama yake aliona hali hiyo, akaomba msaada wa majirani. Wakamchukua Magreth Peter mpaka katika kituo cha afya kilichokuwa jirani yao. Hali ilikuwa mbaya zaidi kwa sababu uchungu wa uzazi haukumuacha apumzike. Magreth Peter alijifungua mtoto wa kiume kwa njia ya kawaida, lakini alivuja damu sana suala lililopelekea kuongezewa damu mara kwa mara. Mtoto alizaliwa akiwa na afya tele lakini hali ya mama yake ilidhoofu siku hadi siku. Mawazo ya kifo cha Edward Lewis yaliendelea kumtesa. Alisisitizwa kupunguza kuwaza lakini hali ilikuwa tofauti, kila alipomuona mwanae alimkumbuka Edward Lewis. Siku ya tatu baada ya kifo cha Edward Lewis aliletewa taarifa na mama yake kuwa Edward Lewis amezikwa kwa kufuata misingi ya kazi yake, amezikwa kwa utaratibu wa kijeshi. Magreth Peter aliumia sana kushindwa kuhudhuria mazishi ya mwanaume alimwachia zawadi ya mtoto.

Baada ya wiki moja Magreth Peter akiwa katika kitanda cha kituo cha afya alicholazwa alikuwa hawezi kuinuka kabisa, hali ilikuwa tete. Alitenganishwa na mtoto wake ili asije kumpa magonjwa nyemelezi, hakuwa na jinsi yoyote zaidi ya kuvumilia na kukubaliana na hali. Magreth Peter alihisi kulichungulia kaburi, siku zilivyozidi kusogea ndivyo alivyozidi kupunguza matumaini ya kuishi. Moyo ulimuuma sana alipofikiria maneno aliyoambiwa na Edward Lewis, maneno yaliyomsisitiza kumtunza mwanae. Machozi yalimtoka. Siku moja alitembelewa na mgeni katika kituo cha afya alicholazwa, alipomtazama mgeni huyo aliishiwa nguvu kabisa. Akilini akawaza labda mgeni huyo ameenda kummalizia yeye na mwanae. Hakuwa mwingine bali alikuwa Catherine Lewis, mdogo wake Edward Lewis. Catherine Lewis alifika kumuomba msamaha Magreth Peter, aliongea machozi yakimtoka kama maji. Alimwambia Magreth Peter

“Kaka aliniambia nikusaidie kukuhudumia kabla na baada ya kujifungua kwako, nilikataa katakata kwa sababu sikukupenda hata kidogo, sikutaka kaka akuoe wewe. Leo najuta maneno yangu, siwezi kumuomba msamaha kaka kwa sababu ameshatangulia mbele ya haki. Napaswa kukuomba msamehe wewe na ikiwezekana nitimize nilichotumwa na kaka ingawa nimeshachelewa”

Magreth Peter hakuwa na kauli yoyote, aliendelea kutumbua macho kama kibaka aliyefumaniwa. Alifikiria namna Catherine Lewis alivyokuwa akimdhalilisha kipindi cha nyuma, alihisi akiota, alihisi labla ni mtu mwingine aliyevaa sura ya Catherine Lewis. Aliendelea kumtazama huku akiruhusu machozi kutoka pasipo sauti ya kilio. Catherine Lewis akamuuliza Magreth Peter

“Umeshamtafuta Abdul Said?”

Magreth Peter alihisi kuna namna, alihisi labda Catherine Lewis alikuwa akimfahamu kwa lengo la kumjua mtu huyo. Alifikiri labda alitaka kuharibu mpango wa kaka yake dhidi yake. Mpango wa yeye kusaidiwa na kijana huyo. Catherine Lewis alielewa mawazo na hofu ya Magreth Peter, aliamini asipofafanua atamtengenezea hofu zaidi. Akaendelea kutoa ufafanuzi

“Simjui kabisa mtu huyo na wala sikuwahi kumsikia awali, nilimsikia kaka akikwambia umtafute endapo ukihitaji msaada wowote. Siku ile nilisikia kila kitu alichokwambia kaka…nilisimama mlangoni kipindi mkiendelea kuongea. Hamkujua kwa sababu mlikuwa mmezama kwenye maongezi mazito”

Maneno ya Catherine Lewis yalizua maswali mengi katika ubongo wa Magreth Peter. Hakuamini alichosikia, aliamini lazima Catherine Lewis atakuwa ameshamtafuta Abdul Said au yupo kwenye mpango wa kumtafuta. Magreth Peter alitamani ainuke achukue simu yake iliyokuwa mbali kidogo na mkono wake lakini alishindwa. Aliitazama kwa hasira akakosa namna ya kufanya. Alitaka aichukue kisha amtafute Abdul Said muda huo huo. Alitaka kuthibitisha kauli ya Catherine Lewis kabla hajaondoka mahali pale. Catherine Lewis aliona namna Magreth Peter alivyokuwa akiitazama simu yake, alielewa aliihitaji muda ule. Alisogea zaidi katika kitanda alicholala Magreth Peter kisha akachukua simu ile akampatia huku akiisindikiza kwa maneno zaidi

“Nilimsikia kaka akikwambia ukihitaji msaada umtafute Abdul Said, alikuwa sahihi kulingana na mazingira ya familia yetu inavyokuchukulia. Alielewa hutaweza kusaidiwa chochote kutoka kwetu, lakini kwangu hali imebadilika. Sipo tayari kuona mtoto wa kaka yangu akilelewa kwa hisani ya mtu mwingine wakati naweza kumlea kwa nguvu yangu. Nipo tayari kuonekana mjinga mbele ya familia yangu lakini nimfurahishe kaka mahali alipo, lazima kaka aone ninatimiza majukumu aliyoniambia”

Magreth Peter hakujali maneno ya Catherine Lewis, yeye alikuwa bize akitafuta jina la Abdul Said katika simu yake. Alipolipata alipiga na kuweka simu sikioni, aliyepigiwa alipokea haraka sana. Magreth Peter alishindwa aanze na kauli gani, alibabaika kwenye simu mpaka akasikia ya Abdul Said ikisema

“Samahani ndugu, nani wewe? Mbona huongei chochote!”

Magreth Peter alishituka kutoka katika umati wa uwoga na hofu uliokuwa umemzunguka. Aliongea haraka haraka ili kukidhi maswali aliyoulizwa

“Samahani kaka, naitwa Magreth Peter. Nilipewa namba yako na marehemu Edward Lewis”

Aliweka kituo kikubwa kusikiliza upande wa pili wa shilingi kama ulikuwa ukielewa maneno yake. Abdul Said alishangazwa sana na simu ile, alibabaika kama mtoto. Alitaka kuongea neno hili ulimi ukakataa, akajaribu lingine hali ikawa kama awali. Kimya kifupi kikapita ndipo alipopata ruhusa ya ulimi wake kutamka neno, Abdul Said alisema

“Ndiyo, nina nyaraka zako muhimu sana. Tena muhimu hasa, zinatakiwa zikufikie muda wowote utakaohitaji”

Magreth Peter alimueleza Abdul Said kuhusu hali yake, lengo la kumueleza alitaka afahamu kuwa hakuwa na uwezo wa kuinuka kitandani ili kufatilia nyaraka hizo. Alimuhitaji Abdul Said afanye namna yoyote nyaraka hizo zimfikie pale kitandani alipolala. Walikubaliana hivyo, simu ikakatwa. Hakuuliza ni nyaraka gani na wala hakutaka kujua mbele ya Catherine Lewis, alijua lazima zitakuwa nyaraka muhimu sana katika maisha yake na mwanae. Kwa maneno aliyoambiwa na Abdul Said alielewa Catherine Lewis alimwambia ukweli kuwa hajawasiliana na Abdul Said, aliuona ukweli huo. Akarudisha macho kumtazama Catherine Lewis kisha akamuuliza

“Unataka nini hasa kutoka kwangu?”

Catherine Lewis aliachia tabasamu angavu, tabasamu lililoonesha meno yake ya dhahabu yaliyopendezesha kinywa chake kisha akajibu

“Hali yako ni mbaya sana, na upo katika kituo kidogo cha afya. Nataka nikusaidie wewe na mwanao, nataka nikupiganie kama utakubali. Nataka uone upande wangu wa pili, upande wa upendo na huruma tele. Naomba tufunike na kufukia kabisa upande wa chuki, napenda kuwa shangazi bora kwa mwanao”

Awali Magreth Peter alikuwa mbishi kuelewa maneno ya Catherine Lewis lakini mwisho wa mchezo aliamua kuchukua maamuzi magumu, maamuzi ya kukubali alichoambiwa. Alimfahamisha mama yake kwa njia ya simu kisha mama yake akaongea na Catherine Lewis na kujihakikishia maneno aliyoambiwa. Nusu saa baadae Magreth Peter alikuwa ndani ya hospitali kuu ya taifa akipatiwe matibabu. Hakika Catherine Lewis alibadilika kwa asilimia mia moja, alimjali Magreth Peter pasipo mfano. Alitimiza kila kilichohitajika na kuhakikisha akipatiwa huduma bora lakini hali ya Magreth Peter iliendelea kuwa dhoofu siku hadi simu. Kilifika kipindi Magreth Peter akawa hawezi kuongea tena, alipooza upande wa kushoto wa mwili wake, akawa akihitaji kuongea anapewa karatasi kisha anaandika hitaji lake. Lilikuwa pigo kubwa sana kwa Catherine Lewis na mama Magreth Peter. Kuna siku Magreth Peter alitaka kuongea kitu, alimuomba Catherine Lewis katarasi kwa kutumia ishara. Catherine Lewis alimpatia karatasi na kalamu ya wino. Magreth Peter aliandika kwa shida sana, ilimchukua muda mrefu kuandika maneno yale. Baada ya kumaliza kuandika alimtazama mama yake aliyekuwa akilia kisha akarudisha macho kumtazama Catherine Lewis. Akamkabidhi Catherine Lewis karatasi lenye maandishi, Catherine Lewis alisoma maandishi yale, maandishi yalisema

“Nakukabidhi mwanangu, nilitamani nimlee mwenyewe kama nilivyoagizwa na baba yake lakini naona sitoweza kutimiza. Mimi ni wa kufa tu, hilo halipingiki. Sijampatia jina mpaka sasa, napenda umpe jina la Derrick. Niliambiwa na kaka yako kuwa ni jina la baba yako mdogo. Nilipenda nimuite Frank lakini siwezi, nikifanya hivyo nitakuwa nimepingana na baba wa mtoto. Muite Derrick kama nilivyoagizwa. Usisite kumtafuta Abdul Said, mtafute ili ufahamu kusudio la kaka yako. Usisite kunitunzia mama yangu, naomba afurahie uwepo wako, nakuomba sana”

Catherine Lewis alishindwa kuvumilia maneno yale, aliinuka akatoka ndani ya chumba kile akilia kama mtoto mdogo. Alilia kwa sauti pasipo kujali wingi wa watu waliokuwa wakimuona. Catherine Lewis aliumizwa na maneno yale hasa baada ya kuona upendo wa Magreth Peter, upendo wa kukubali kumpa jina mwanae la mtu aliyekuwa akimchukia sana. Hakujali chuki za ndugu wa Edward Lewis, yeye alitimiza kila agizo alilopewa. Catherine Lewis aliona jinsi kaka yake alipokuwa kwenye mikono salama, kilio kilizidi alipokumbuka alivyokuwa akimnyanyasa na kumnyanyapaa Magreth Peter. Taratibu alianza kuichukia familia yake, alijisemea moyoni

“Sitakuwa tayari kuona familia ya Magreth ikihangaika, sitakuwa tayari. Bora familia initenge”

Catherine Lewis alirudi wodini, alikuta kilio kipya. Hakikuwa kilio cha kitoto, hapana, kilikuwa kilio kikubwa zaidi ya alichoondoka nacho. Alimkuta mama Magreth Peter akigalagala chini kama chizi. Nesi alikuwa akimfunika shuka Magreth Peter, kitendo kile kilimaanisha roho ilikuwa imeshauacha mwili. Magreth Peter alikuwa maiti muda huo. Catherine Lewis alizubaa asijue cha kufanya, alibabaika ovyo. Alihisi kama alikuwa akiota ndoto za mchana lakini haikuwa kweli. Alikuwa macho kabisa na wala haikuwa ndoto. Alikitazama kipande cha karatasi alichopewa na Magreth Peter, akakikunja kwa hasira. Alitamani kukichachana vipande vipande lakini roho ilikataa, roho ilimwambia asichane ujumbe wa marehemu. Alikipakia katika mkoba wake na kuendelea kuomboleza kifo cha Magreth Peter.

ITAENDELEA

NB: KITABU KINAPATIKANA KWA NAMBA 0758 195 890
IMG_20220520_203952_475.jpg
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

( KIPANDE CHA KUMI NA MBILI)

BAADA YA MWAKA MMOJA (RWAMA MWISHO – 1996)
Mziki laini uliendelea kuliteka anga lote la chumba kilichojaa midoli ya watoto, siyo kwamba chumba hicho kilimilikiwa na mtoto, hapana, bali kilimilikiwa na msichana wa makamo. Msichana yule alipenda kujaza midoli akiamini itakuwa furaha kwa mtoto aliyekuwa akikuwa kila baada ya siku moja. Mziki ule ilipenya ipasavyo katika masikio ya msichana yule akaanza kutikisa kichwa kushoto na kulia kuashiria kukongwa moyo wake. Mkononi alishika glasi iliyojaa juisi ya matunda, glasi yenye mshikio mrefu kama zile zitumikazo sehemu za starehe.

Alikunywa funda moja baada ya lingine huku akiendelea kuburudishwa na mziki. Alisikia sauti ya mtoto akilia, kilio cha mtoto kilikuwa juu kikameza sauti ya mziki laini uliokuwa ukimburudisha. Aliweka glasi juu ya meza kisha akaelekea kitandani na kumchukua mtoto. Alijaribu kumbembeleza kwa kumchezesha chezesha lakini mtoto alikuwa mbishi. Hakuelewa somo lililokuwa likiendelea. Msichana yule akaamua kubadilisha zoezi la kumtuliza mtoto, alichomoa titi lake katika sidiria akaanza kumnyonyesha. Mtoto alinyonya kwa fujo sana kitu kilichomaanisha alikuwa na njaa. Msichana yule akatabasamu huku akichezea chezea kichwa cha mtoto. Mtoto alinyonya mpaka akasinzia katika titi lake. Msichana yule alimrudisha mtoto kitandani, akamlaza na kumfunika vizuri.

Mwanzo alipata shida sana kumlea mtoto yule, hakuwa mtoto wake wa kumzaa na alikuwa hajawahi kuzaa mtoto hivyo basi suala la kunyonyesha lilimpa tabu sana. Aliomba ushauri kwa daktari namna atakavyoweza kumnyonyesha mtoto angali hana mtoto na matiti yake hayakuwa na maziwa ambayo huzalishwa pindi mama anapojifungua. Daktari alimwambia amnyonyeshe mtoto maziwa yake japokuwa hana maziwa ya kutosha, alimwambia akifanya hivyo homoni zinazozalisha maziwa zitapeleka taarifa katika ubongo kuwa kuna mtoto hunyonya maziwa yake, hivyo basi lazima maziwa yatazalishwa taratibu. Alimwambia kuwa homoni hiyo inayoitwa estrojeni ikishirikiana na homoni za ukuzi (human growth hormone) husaidia sana suala la kunenepesha na kujaza maziwa katika matiti ya mwanamke ili awe tayari kwa kunyonyesha.

Ndivyo alivyofanya, alianza kumnyonyesha mtoto kwa shida sana lakini siku zilivyozidi kusogea mbele kifua chake kilianza kujaa maziwa ya kutosha. Kitu pekee alichojivunia ni suala la mtoto yule kukubali kunyonya maziwa yake, alijivunia suala hilo kwa sababu daktari alimwambia baadhi ya watoto hukataa kunyonya maziwa yasiyo ya mama zao. Alikubali kifua chake kitumike kama chakula cha mtoto yule asiye na wazazi, asiye na baba wala mama. Yeye ndiye alikuwa baba na mama yake baada ya kuamini mtoto yule asingeweza kuishi pasipo uwepo wake.

Halikuwa jambo dogo kwa Catherine Lewis kuamua kuvaa viatu vya marehemu kaka yake katika suala la kumlea mtoto Derrick Edward, ndugu zake waliompinga Edward Lewis kumuoa Magreth Peter walimpinga pia Catherine Lewis kumlea mtoto wa kaka yake pamoja na bibi yake. Walisema Derrick Edward hakuwa mtoto wao wa damu, na kama alikuwa mtoto wao basi alikuwa mtoto wa nje ya ndoa, mtoto haramu. Walisema hawawezi kukaa na haramu katika ukoo wao, walikataa katakata. Kikwazo kikubwa kilikuwa baba Catherine Lewis, mzee Lewis Kalikumbi baada ya kuona zoezi lake la kujaribu kumuunganisha mwanae na mtoto wa rafiki yake kutofanikiwa. Catherine Lewis aliendelea kuwa mbishi mbele ya wana familia yake, alilisitiza msimamo wake wa kumlea Derrick Edward na mama Magreth Peter.

Kitendo kilikuwa kama kuchezea sharubu za simba dume aliyekuwa mawindoni. Mzee Lewis Kalikumbi alifura hasira, alipanga njama za kumuangamiza Derrick Edward na bibi yake. Kipindi hicho Catherine Lewis alikuwa amempangishia mama Magreth Peter nyumba nzuri ya kisasa. Japokuwa alikabidhiwa mtoto na Magreth Peter lakini alishindwa kuishi nae. Alimuacha akae na bibi yake katika nyumba ile aliyowapangishia. Catherine Lewis alikuwa mstari wa mbele kuratibu kila kitu kilichohitajika ili mtoto akue.

Nyuma ya pazia hakujua kama baba yake alipanga njama za kumteketeza Derrick Edward na bibi yake baada ya kuona mwanae akiwahangaikia. Alitaka kufuta aibu, kwake kuwa na mjukuu kama Derrick Edward ilikuwa aibu kubwa. Aliamini lazima afanikiwe kwenye mpango huo kama alivyofanikiwa kuwapachika manesi wa uongo waliomchoma sindano ya sumu Magreth Peter. Kipindi kile kila mmoja aliamini Magreth Peter alifariki kwa sababu ya maradhi yaliyotokana na uzazi pamoja na mawazo juu ya taarifa za kifo cha mpenzi wake. Hawakujua kama nyuma ya pazia kulikuwa na mchezo wa siri ukifanyika. Mzee Lewis kalikumbi kupitia taarifa za vijana wake wa kazi alifahamu makazi aliyopangishiwa mama Magreth Peter. Kazi ya mauaji ilipangwa na kupangika.

Siku moja usiku wa saa tatu mama Magreth Peter alisikia vishindo nje ya nyumba. Alipuuza vishindo vile kwa sababu alikuwa amechoka sana kutokana na mizunguko aliyoifanya siku hiyo, siku hiyo alizunguka masoko mbalimbali kununua nguo za mjukuu wake. Vishindo viliendelea kusikika, vilisikika kwa sauti kubwa. Vikamtengenezea hofu kubwa. Akasimama na kwenda kuchungulia nje kupitia dirishani, hali ilikuwa shwari kabisa. Kitendo kile kilimuongezea maswali kwa sababu kama angeona kitu au mtu angedhani ndiyo chanzo cha vishindo hivyo. Alibaki njia panda. Akaamini kuna kitu hakipo sawa. Aliwaza afungue mlango atoke ndani ili akaangalie usalama wa nje lakini akili ikakataa, akili ikajenga hali ya hofu zaidi. Bahati haikuwa yake siku hiyo, alishuhudia mlango alioufunga ukifungua pasipo ridhaa yake.

Mfunguaji alivunja mfumo wa kitasa cha mlango kwa risasi, mlio wa risasi haukusikika kabisa kitu kilichomaanisha bastola ilifungwa kizuia sauti na aliweka kitambaa kizito kati ya kitasa na bastola. Kijana aliyevaa kofia aina ya kepu iliyoficha sura yake aliingia ndani kwa fujo. Alimkuta mama Magreth Peter akitetemeka. Muuaji hakuwa na kazi kubwa, hakuongea neno lolote zaidi ya kumpiga risasi ya moyo. Muuaji alisimama mbele ya mama yule akashuhudia alivyokuwa akitupa tupa mikono na miguu mpaka roho ilipoacha mwili. Muuaji alianza kumtafuta mtoto Derrick Edward ndani ya nyumba ile, alipekua kila chumba, kila kona lakini hakumuona mtoto. Hofu ikamjaa, akaamini alifanya ujinga kumuua bibi yule kabla hajajihakikishia wapi alipokuwa mtoto. Alirudi mbele ya maiti ya mama Magreth Peter, alitamani aifufue ili imwambie alipo mtoto lakini alikuwa akitwanga maji kwenye kinu.

Kipindi akiendelea kutafakari jambo la kufanya, ghafla aliona mwanga mkali wa taa za gari ukisimama nje ya nyumba. Kitendo kile kilimaanisha kuna mtu au watu walikuwa ndani ya gari lililosimama eneo lile. Muuaji alifikiria kwa haraka namna ya kukimbia, akaona akichukua maamuzi hayo lazima ataonwa na ujio huo. Kichwa chake kilifikiria kwa haraka sana, akapata jawabu. Jawabu lilikuwa kujificha pembeni ya kabati lililokuwa sebuleni. Sekunde zilivyosogea ndivyo vilivyozidi kusikika vishindo vikisogea eneo lile, muuaji hakubahatika kujua vishindo hivyo vilikuwa vya watu wangapi. Aliendelea kujifutika alipokuwa. Mlango ulikuwa wazi. Hatua nne kutoka usawa wa mlango kulikuwa na mwili wa mama Magreth Peter uliochakaa damu mbichi. Catherine Lewis alipiga hatua taratibu mpaka hatua kadhaa kutoka usawa wa mlango, alishangaa kuona mlango ulikuwa wazi wakati siku zote walikubaliana kufungwa mpaka atakapoandaa mpango wa kuwasafirisha mbali ya jiji hilo. Hofu ilimjaa Catherine Lewis, akahisi hali ya hatari. Alipiga hatua kwa tahadhari kubwa mpaka mlangoni. Alishuhudia maiti ya mama Magreth Peter ikimtazama kwa macho wawili yaliyo wazi, kifuani ikiwa imechakaa damu kweli kweli.

Kengele ya hatari iliendelea kusikika katika kichwa cha Catherine Lewis, kengele ile ilimwambia pale siyo mahali salama na hakutakiwa kuendelea kupoteza muda. Alimfunga vizuri mgongoni mtoto Derrick kisha akapiga hatua haraka kurudi nyuma. Alitimua mbio mpaka ndani ya gari lake. Akawasha gari huku mikono ikitetemeka kwa hofu, gari likaitika akaondoka kwa mwendo kasi. Nyuma alisindikizwa kwa risasi zilizopiga kioo cha nyuma cha gari na kukipasua. Catherine Lewis hakujali aliongeza kasi ya gari. Alikuwa tayari kupata ajali ya gari kuliko kukamatwa au kuuliwa na muuaji yule ambaye hakufanikiwa kuona hata sura yake. Mtoto alianza kulia kwa fujo kama vile alielewa walikuwa vitani, Catherine Lewis hakujali kilio cha mtoto, yeye alijali usukani wa gari. Aliamini akifanikiwa kumtoka adui atakuwa ameokoa maisha yake na maisha ya mtoto. Alifanikiwa kumtoka adui wake.

Catherine Lewis aliandamwa na mawazo juu ya mtoto, alifikiria namna mtoto alivyonusurika kifo. Aliuona ukuu wa mwenyezi Mungu kwa sababu kama asingeenda kumchukua mtoto yule asubuhi ya siku hiyo ili bibi yake apate muda na uhuru wa kwenda kununua nguo za mjukuu wake lazima mtoto angeuliwa kama bibi yake. Catherine alikuwa akiendesha gari huku machozi yakimtoka. Alimfikiria mama Magreth Peter machozi yakaendelea kumtoka kama maji. Alihisi familia yake ikihusika kwa namna moja ama nyingine. Alifikiria atampeleka wapi mtoto yule usiku ule, kichwa kilikosa majibu. Alifikiria kwenda naye nyumbani anapoishi na wazazi wake akaona hapakuwa na usalama hata kwa asilimia moja. Aliamini lazima atampoteza mtoto wa kaka yake. Kichwa kiliwaka moto. Alisimamisha gari pembeni ya barabara, akaendelea kulia kama mtoto. Alilia akipokezana na mtoto wa kaka yake. Kipindi akiendela na kilio alikumbuka kitu, alikumbuka maagizo aliyopewa na Magreth Peter kuhusu kumtafuta Abdul Said. Sasa aliamini huo ndiyo wakati muafaka wa kumtafuta na kumfuata usiku huo huo. Alichukua simu yake akatafuta jina la muhusika, alipolipata akapiga na kusikiliza sikioni. Simu iliita kwa sekunde chache kisha Abdul Said akaitikia kwa kauli iliyosema

“Hallo ndugu! Samahani nipo bize kidogo nitakutafuta baada ya saa”

Japokuwa ilikuwa namba ngeni kwa Abdul Said lakini hakujali, siyo kwamba hakutaka kuongea na aliyempigia, hapana, bali alikuwa akiandaa mpango wa kwenda kufanya tukio mahali, tukio la kuwakamata wahalifu wanaofanya biashara ya madawa ya kulevya. Catherine Lewis hakukubali jibu alilopewa, aliongea haraka haraka

“Samahani kaka, najua hunijui na kama unanijua basi namba yangu huna. Naitwa Catherine Lewis Kalikumbi, mdogo wa marehemu Edward Lewis Kalikumbi. Nina shida sana na wewe kwa sababu kaka alimwambia Magreth Peter akiwa na shida akutafute wewe. Magreth alishafariki na kaniachia mwanae”

Kilio kiliendelea kama kawaida, alishindwa kuendelea kuongea akawa akiuma uma maneno huku kwikwi zikimwandama pasipo kumpumzisha msichana yule. Sasa ilikuwa zamu ya Abdul Said kupatwa na bumbuwazi. Alishindwa kuelewa vizuri habari ile, siyo kwamba maneno yalikuwa na misamiati, la hasha, bali tangu awali Edward Lewis alimwambia kuwa familia yake ilikuwa haimpendi kabisa Magreth Peter na miongoni mwa watu waliokuwa mstari wa mbele ni huyo mdogo wake. Taarifa ya kifo cha Magreth Peter haikuwa ngeni katika masikio yake, aliisikia siku ile ile aliyofariki. Akawatuma vijana wake kufanya uchunguzi wa maiti (post mortem) na kubainika Magreth Peter alipewa sumu. Siku ile ile Abdul Said alianza uchunguzi wa kimya kimya kuhusu familia ya mzee Lewis Kalikumbi, katika uchunguzi wake alishindwa kuelewa mahali alipokuwa akiishi mama Magreth Peter na mjukuu wake. Hakujua kama Catherine Lewis alipewa jukumu la kumlea mtoto. Abdul Said alijiuliza maswali mengi yasiyo na majibu, lakini kwakuwa alivaa jukumu la kipelelezi nje ya kazi yake aliamini anaweza pata chochote kutoka kwa binti yule. Kauli ya Catherine Lewis ikajirudia akilini kwake. Alisikia sauti ya mtoto akilia sana kipindi alipokuwa akiendelea kuongea na Catherine Lewis. Abdul Said aliacha kazi aliyokuwa akiifanya, akili yote akaihamishia katika mazungumzo yaliyoanzishwa na Catherine Lewis. Akamuhoji

“Mbona sikuelewi! Kuna nini kinachoendelea”

Catherine Lewis aliamini akielekea kushinda zoezi lake, alijikaza kisha akaendelea kuongea kwa sauti iliyoathiriwa na kilio cha muda mrefu

“Tumevamiwa na maadui, wamemuua mama Magreth Peter. Nipo na mjukuu wake hapa mtaa wa barabara ya Makutano, jirani na kituo cha magari ya masafa marefu”
Abdul Said alijibu kwa kauli moja
“Nisubiri hapo hapo”

Abdul Said alikuwa amevaa kombati zake za jeshi huku bastola ndogo ikiwa kiunoni kwake, awali alitaka kubadilisha mavazi hayo lakini alihisi atachelewa alipokuwa akielekea. Aliona suala la kuokoa familia ya matehemu rafiki yake lilikuwa na msingi sana kuliko mpango aliokuwa akiuandaa, alijisemea moyoni

“Nikirudi nitaendelea nilipoishia, ngoja niaangalie usalama wa mtoto wa jamaa yangu”

Baada ya dakika kumi Abdul Said alifika mtaa wa barabara ya Makutano. Aliliona gari lililoegesha mahali alipoelekezwa. Alisogea taratibu tena kwa umakini wa hali ya juu mpaka usawa na gari lile, alishusha kioo kisha akapiga honi kumjulisha aliyekuwa akimsubiri kuwa amefika. Hakutaka kushuka haraka kwa sababu alitaka kujihakikishia usalama wake. Bastola ilikuwa mkononi tayari kwa lolote baya litakalojitokeza dhidi yake. Catherine Lewis alielewa maana ya Abdul Said, alifungua mlango wa gari akatoka akiwa kambeba mtoto mikononi. Abdul said alikuwa makini akifatilia hatua za Catherine Lewis mpaka zilipofika katika mlango wa gari lake. Catherine Lewis alimtazama Abdul Said lakini ilikuwa sura ngeni, hakuwahi kuiona mahali popote. Hakujiuliza maswali mengi kuwa jamaa huyo alikuwa na urafiki gani na kaka yake kwa sababu alipata majibu baada ya kuona mavazi aliyokuwa amevaa. Alitazama begani akaona nyota mbili zikimtazama kwa amani na utilivu. Catherine Lewis akajitambulisha kwa mara ya mbili

“Naitwa Catherine Lewis, mtu pekee mwenye jukumu la kumlea mtoto huyu”

Abdul Said alimtazama Catherine Lewis kisha akarudisha macho kumtazama mtoto aliyekuwa mikononi mwake akiendelea kulia. Alikosa kauli ya haraka. Akarudisha macho juu kutazama sura ya Catherine Lewis iliyoandamwa na makunyanzi ya kilio na hofu, akamuulia

“Nikusaidie nini?”

Swali la Abdul Said lilimaanisha alihitaji maelezo ya kutosha kuhusu mambo yaliyokuwa yakiendelea, alikuwa hana uaminifu uliokamilika kwa Catherine Lewis. Kwakuwa Catherine Lewis alikuwa akihitaji msaada wa hali kutoka kwa mwanajeshi yule mwenye nyota mbili begani, alikuwa mpole, hakuwa na papara yoyote kwa sababu aliamini akiweka papara anaweza kupoteza msaada uliokuwa njiani. Macho yake yalimtazama Said Abdul, kwa sauti ya upole aliuliza

“Waweza niruhusu niingie ndani ya gari lako nijielezee vizuri?”

Kipindi chote mtoto alikuwa akiendelea kulia. Kwakuwa ulikuwa usiku na kulikuwa na hali ya baridi ambayo siyo salama kwa mtoto, mwanajeshi alilitambua hilo. Akamuhurumia mtoto. Akamjibu Catherine Lewis

“Waweza ingia”

Kauli hiyo ilitoka ikiambatana na kitendo cha Abdul Said kufungua mlango wa gari wa upande aliokuwa amesimama Catherine Lewis. Catherine Lewis aliingia na kukaa kitako upande wa pili wa Abdul Said. Sasa ulikuwa umefika wakati wa kujielezea, hakika alijielezea vizuri. Alieleza matukio yote kwa mtiririko uliofaa. Alieleza namna yeye na familia yake walivyompiga vita kaka yake katika suala la kujihusisha kimapenzi na mwanamke masikini asiye na mbele wala nyuma kiuchumi. Alieleza pia jinsi kaka yake alivyomuomba asimamie uangalizi wa Magreth Peter katika suala lake la kujifungua lakini akakataa. Hakusahau kumuelezea namna alivyoamua kumuunga mkono Magreth Peter mpaka akakabidhiwa jukumu gumu la kumlea mtoto Derrick Edward siku aliyofariki Magreth Peter. Alisimulia kila kitu alichohisi kingeweza kuleta mwanga na kusababisha kujengeka kwa uaminifu kati yake na mwanajeshi aliyekuwa pembeni yake. Ilikuwa zamu ya Abdul Said kuinamisha kichwa ili kuruhusu tafakari zake zimpe majibu sahihi, majibu yalikuwa magumu kupatikana. Aliona namna Catherine Lewis alivyokuwa njia panda. Abdul Said aliinua kichwa chake akamwambia Catherine

“Magreth alinipigia simu na kunieleza alivyoambiwa na kaka yako kuhusu mimi, alikuwa sahihi kabisa kunitafuta. Nilipanga kumpatia kila nilichokabidhiwa lakini kabla sijafanya hivyo hali ilikuwa tofauti, Magreth aliuliwa kinyama”

Ilikuwa habari mpya na ya kushangaza katika masikio ya Catherine Lewis. Midomo ilimtetemeka kama mtoto mdogo, alitaka kuongea akashindwa akabaki kamkodolea macho Abdul Said. Mwanajeshi yule alielewa hali aliyokuwa nayo Catherine Lewis, hakujali chochote bali aliendelea kumshangaza mtoto pekee wa mzee Lewis Kalikumbi aliyebakia hai.

“Wauaji ni watu waliowazunguka, watu waliowajua vizuri Magreth na mama yake. Nina hakika waliomuua Magreth ndiyo waliomuua mama yake, nina hakika kabisa”

Maneno ya Abdul Said yaliendelea kumuaminisha Catherine Lewis kuwa familia yake ilihusika kwa namna moja ama nyingine, familia yake itakuwa ilituma watu kufanya mauaji au inafanya mauaji yenyewe pasipo kutumia mtu. Catherine Lewis aliingiwa na hofu kali. Alishindwa kumwambia Abdul Said mawazo yake, aliiona hatari, aliiona vita ilivyokuwa kubwa. Alibaki akijiuliza mwenyewe

“Kwanini wanafanya mauaji wakati hakuna kinachoendelea kati yao? Kaka ameshafariki, sasa kwanini waendelea kuteketeza watu?”

Alikosa majibu ya maswali yake. Kipindi akiendelea kuandamwa na mawazo ghafla alisikia sauti kali ya Abdul Said, sauti iliyoamua kusema kila kitu kilichokuwa moyoni pasipo kuficha

“Familia yako itakuwa nyuma ya matukio haya. Nikuweke wazi msimamo wangu, sipo tayari kumtetea mhalifu, nakusanya taarifa kamili. Nikipata mwanga mzuri nitajua nini cha kufanya”

Catherine Lewis alihisi kama alisikia vibaya lakini haikuwa kweli, alisikia sahihi kabisa. Alimtazama Abdul Saidi akakuta macho yake yakitizama sura yake, mwanajeshi hakupepesa macho kitu kilichomaanisha hakuwa na walakini na maneno aliyotamka. Awali Catherine Lewis alifikiri yeye pekee ndiye aliyevihusisha vifo hivyo na familia yake, kumbe hata Abdul Said. Mapigo ya moyo yaliongeza kasi, alifikiria cha kufanya lakini kichwa kilikataa kumpa majibu. Alijikuta akimwaga machozi kama mtoto aliyepigwa na mzazi wake. Abdul Said alichukua kitambaa chake akampatia Catherine Lewis kisha akamwambia

“Ulishalia sana Catherine, huu ni wakati wa kuchagua sehemu ya kupigania. Ukichagua kumlinda mtoto wa kaka yako ujue utakuwa unaendeleza vita na familia yako, vita ya uhai na kifo”

Maneno ya Abdul Said yalikuwa sahihi sana, maneno hayo yalizidi kumuweka Catherine Lewis mbali na familia yake. Catherine Lewis alimtazama mtoto aliyechokuwa mikononi mwake, alikuwa ameshanyamaza muda mrefu. Alikumbuka kauli ya Magreth Peter, kauli iliyomwambia amtunzie mtoto wake. Kilio kiliendelea, kilikuwa kilio cha kwikwi. Mwanajeshi hakujali kilio cha Catherine Lewis, aliwasha redio ili kupoteza kilio cha Magreth. Hakutaka watu waliokuwa wakipita eneo lile wasikie kilio kilichokuwa kikiendela. Hakutaka kutengeneza maswali katika vichwa wa watu. Catherine Lewis aliongea kwa sauti ya kulia

“Nitapambana usiku na mchana kumkuza Derrick. Watamuua Derrick wakishafanikiwa kuniua mimi”

Abdul Said alitabasamu. Siyo kwamba alifurahishwa na kauli ya Catherine Lewis, hapana, bali aliuona ujasiri ndani ya mwanamke yule. Aliona namna alivyoamua kumpigania kaka yake. Alimwambia Catherine Lewis

“Najua tuna mengi ya kuongea lakini hapa siyo mahala pake. Yakupasa kwenda nyumbani, kesho asubuhi tutawasiliana”

Catherine Lewis alimtazama Abdul Said kisha akarudisha macho kumtazama mtoto aliyekuwa mikononi mwake. Kitendo kile kilimaanisha alikuwa hana sehemu ya kumpeleka mtoto yule. Abdul Said alielewa maana ya Catherine, akatabasamu kama kawaida yake kisha akamwambia

“Usihofu Catherine, niachie mtoto. Nitapita super market kununua maziwa, nitampatia na atafurahia. Kesho usisahau kunitafuta”

Catherine Lewis alimkabidhi mtoto mwanajeshi yule kisha akashuka na kupiga hatua kuelekea alipoegesha gari lake. Kipindi yupo nyuma hatua moja kulifikia gari lake mara simu yake iliita. Akaingiza mkono katika mfuko wa suruali yake ya jinzi kisha akachomoa. Ilikuwa namba ya mama yake yake mzazi. Aliitazama pasipo kuipokea, akarudisha simu mfukoni. Alielewa alikuwa akitafutwa na mama yake kwa sababu alichelewa kurudi nyumbani. Alijidanganya mwenyewe. Laiti kama angelijua simu ile ilikuwa ikimaanisha nini angeliipokea haraka. Alipanda ndani ya gari lake akashuhudia gari la Abdul Said likiondoka mahali pale kwa mwendo wa wastani, alilitazama mpaka lilipotoweka kwenye upeo wa macho yake. Alifungua mkoba kisha akatoa kioo, alijitazama na kuona namna alivyoharibika sura yake kwa kilio. Alijifuta machozi kisha akarekebisha nywele zake. Akawaza gari na kuanza kuelekea nyumbani huku akitafakari tukio la siku hiyo.

Baada ya nusu saa alifika nyumbani kwao, alishangaa kukuta geti likiwa wazi kabisa. Haikuwa kawaida kwa nyumba ile kuwa wazi hata kipindi cha mchana, ilikuwa lazima upige honi au hodi ndiyo ufunguliwe mlango na mlinzi wa geti. Aliingiza gari taratibu, alizidi kushangaa zaidi. Alikuta umati mkubwa wa watu uwani kwao. Kati ya umati ule alimuona mama yake akiwa kashikwa kulia na kushoto huku akilia kama mtoto mdogo, kitendo kile kilimaanisha mama yake hakuwa na nguvu za kuuhimili mwili wake. Hofu ilizidi katika moyo wa Catherine Lewis. Alifungua mlango wa gari haraka na kushuka, alipita hatua mbili kuelekea alipokuwa mama yake lakini kabla hajafika mama yake alimuona, akaanza kulia kwa sauti

“Njoo mwanangu njoooo mwanangu, ooooooh mwanangu. Mambo gani haya mwananguu”

Catherine Lewis alizidi kuchanganyikiwa, aliongeza kasi mpaka alipokaa mama yake. Mama akamkumbatia mwana huku akiendelea kulia kwa sauti kubwa. Aliongea maneno mengi yaliyokuwa kama mafumbo kwa Catherine Lewis. Catherine Lewis alihisi mama yake amechanganyikiwa. Watu waliokuwa wamemshika mama yake kushoto na kulia muda huo walimuachia ili awe huru na mtoto wake. Catherine Lewis aliwatazama mmoja baada ya mwingine lakini wakakwepesha macho, hakuna aliyekuwa tayari kuongea nae. Catherine Lewis alipaza sauti kwa nguvu

“Mama kuna nini? Mbona mnanichanganya!”

Mama yake aliendelea kulia huku akitamka maneno yaliyoendelea kutengeneza maswali katika akili ya Catherine Lewis. Alitamka kwa nguvu

“Baba yako Catherine, baba yako…yani baba yakooo”

Catherine Lewis aliuliza baba yake amefanya nini lakini hakupata jawabu zaidi ya kilio. Akapata wazo la kuelekea ndani ya nyumba yao ili akamshuhudie baba yake kama yupo na kama hayupo arudi kuuliza mpaka aambiwe kilichokuwa kikiendelea. Alimwacha mama yake akaanza kuzihesabu hatua kuelekea ndani, alipofika katika mlango wa kuingilia ndani alikuta kuna kamba imezuia watu kuingia, kamba ile iliandika maneno yaliyosomeka 'POLICE LINE: DO NOT CROSS' (MSTARI WA POLISI: USIVUKE). Alistaajabu sana, akasimama kisha akatupa macho ndani. Aliwaona polisi watatu wakiwa mbele ya kitu kilichofunikwa, kitu kile kilikuwa kimetapakaa damu. Hofu ikazidi kumuingia Catherine Lewis. Alihisi kitu kile kilichofunika kikiwa kimeshamiri damu utakuwa mwili wa baba yake. Alijisemea moyoni

“Hapana, hawezi kuwa baba. Hapana”

Alivuka kamba ya polisi akaanza kupiga hatua kuelekea walipokuwa polisi wale, alifanikiwa kufika lakini kabla hajaongea chochote alikumbwa na polisi mmoja akambeba juu juu mpaka nje pasipo kuongea naye chochote. Akambwaga mbele ya umati ule wa watu kisha akatoa tamko

“Tuache tufanye kazi yetu, mtataarifiwa kila kitu kilichotokea…msituingilie katika majukumu yetu”

Catherine Lewis alielewa ukubwa wa tatizo lililotokea. Alishangaa kuondolewa kwa nguvu katika nyumba ya wazazi wake. Alielewa kwanini alimkuta mama yake nje ya nyumba, aliamini hata yeye alizuiliwa kuingia ndani. Picha ya kitu kilichokuwa sakafuni kimefunikwa na kimeathiriwa na damu mbichi ikamrudia kichwani. Akamgeukia mama yake haraka kisha akamuuliza

“Baba ameuliwa?”

Kilio cha mama yake kilimthibitishia mawazo aliyokuwa nayo, aliafiki furushi lililokuwa likiendelea kumwaga damu ulikuwa mwili wa baba yake kipenzi, aliamini atakuwa ameuliwa. Alithibitisha hilo kutokana na mavazi waliokuwa wamevaa polisi, polisi walivaa mavazi yaliyozuia miili yao kuanzia miguuni mpaka kichwani. Mikononi walivaa soksi kwa lengo la kutoacha alama za vidole katika kitu chochote watakachogusa au shika. Machozi yalianza kutengeneza njia katika mashavu ya Catherine Lewis, alihisi dunia imemuangukia. Alimtazama mama yake kisha akamuuliza

“Nani aliyemuua baba? Kwanini lakini!”

Mama yake alimkumbatia huku akiendelea kulia, kilio kilizidi kwa sababu hata waliponyamanzishwa na majirani zao hawakunyamanza. Walilia kama walikuwa kwenye mashindano ya kulia. Catherine Lewis alikumbuka kauli ya Abdul Said, kauli iliyosema

“Familia yako itakuwa nyuma ya matukio haya. Nikuweke wazi msimamo wangu, sipo tayari kumtetea mhalifu. Nakusanya taarifa nikipata mwanga mzuri nitajua nini cha kufanya”

Alihisi labda Abdul Said atakuwa nyuma ya tukio hilo lakini akili ikakataa. Akahisi kuna siri nzito asiyo ifahamu kuhusu baba yake, au familia yake. Alijiuliza wapi atapata kufahamu? Akakosa jibu. Walikuwa wamekaa huku wakiendelea kulia kama kawaida. Ghafla walisikia gari likisimama nje ya nyumba yao, wakashuhudia vijana wanne wakiwa na machela ya kubebea majeruhi au maiti wakielekea ndani ya nyumba yao. Vijana wale walisalimia lakini hawakujibiwa na yeyote aliyekuwa nje, raia walikuwa wamefura hasira baada ya kucheleweshwa kuambiwa kilichokuwa kikiendelea. Vijana wale hawakujali chochote. Walivuka mstari wa polisi ulioandikwa 'POLICE LINE: DO NOT CROSS' (MSTARI WA POLISI: USIVUKE) na kutokomea ndani ya nyumba hiyo. Hazikupita hata dakika nne, vijana wale walitoka ndani wakiwa wamebeba mwili wa mzee Lewis Kalikumbi katika machela walioingia nayo. Mwili ulifunikwa sehemu yote pasipo kuacha hata ukucha nje. Catherine Lewis alijaribu kuinuka kwenda kuhakikisha kama aliyebebwa alikuwa baba yake lakini alizuiliwa na mama yake. Kauli ya mama yake ilimzuia. Alisema

“Huo ni mwili wa baba yako Catherine…huyo ni baba yako”

Catherine Lewis aliduwa kama mtu aliyepigwa shoti ya umeme. Alihisi akili imesimama kufanya kazi yake. Aliwasindikiza kwa macho vijana wale mpaka walipotoweka nje ya nyumba yao. Alisikia gari likipata moto kisha likaondoka. Baada ya dakika kadhaa polisi waliokuwa ndani ya nyumba ile waliondoa kamba iliyokuwa ikizuiwa watu kuingia kisha mmoja wao akaongea kwa niaba ya wenzake

“Tunashukuru kwa ushirikiano mliotupa. Sisi kama jeshi la polisi kuna vitu tumebaini lakini hapa siyo mahali husika pa kusemea. Mtajulishwa kila kila kitu uchunguzi utakapokamilika. Kuna vitu tumebaini ndani ya nyumba hii, vitu ambavyo vitakuwa sehemu ya uchunguzi wetu”

Aliwaonesha mfuko wa plastiki raia waliokusanyika eneo lile, raia hawakuweza kuona kilichokuwa ndani lakini walielewa kauli ya polisi yule kuwa vitu alivyovizungumzia vilikuwa ndani ya mfuko huo. Walikuwa sahihi kwa ailimia mia moja. Polisi akaendelea kutoa ufafanuzi zaidi

“Kwa kifupi zimebainika risasi mbili katika paji la uso la marehemu. Pembeni ya mwili wake ilikutwa bastola ndogo. Hatufahamu kama ni bastola yake au siyo…kwa sababu hiyo hatufahamu kama ameuliwa au amejiua mwenyewe. Mtapewa taarifa”

Minong`ono iliibuka kati ya watu waliokuwa sehemu hiyo. Hawakuafiki na suala la kujiua kwa mzee Lewis Kalikumbi, waliamini atakuwa ameuliwa. Wengi walimfahamu mzee yule kama mtu mpole na mkarimu sana kwa jamii. Aliyependa kujitoa kwa hali na mali kuwasaidiwa wengine. Na mara kadhaa alikuwa mshauri wa watu wenye shida mbalimbali, hivyo asingeweza kujiua wakati alikuwa na uwezo wa kupambana na matatizo ya watu wengine akiyafanya kuwa yake. Catherine Lewis alihamaki kwa hasira baada ya kusikia kuwa baba yake inawezekana alijiua mwenyewe. Alisema kwa jazba

“Hapana afande, hapana…namfahamu vizuri baba yangu hawezi fanya hivyo. Hapana”
Kauli yake ilipokelewa kwa kilio kizito kutoka kwa mama yake. Umati wote uliafikiana na kauli ya Catherine Lewis kuwa mzee wake hakujiua. Polisi hakuwa na neno lolote lakini alipata kuelewa kitu, alielewa namna mzee yule alivyojenga imani nzuri kwa jamii yake. Aliwageukia Catherine Lewis na mama yake kisha akawaambia

“Muda wowote tukihitaji ushirikiano wenu, tafadhari naomba muitikie”

Hakuna aliyepinga, waliafiki kwa kutigisa kichwa juu chini. Polisi waliaga na kuondoka eneo lile la tukio wakiacha vilio vikiendelea pasipo kupumzika. Mwili wa marehemu mzee Lewis Kalikumbi ulihifadhiwa katika hospitali kuu ya Taifa. Ulifanyiwa uchunguzi ili kubaini chochote kitakachoweza kulisaidia jeshi la polisi katika uchunguzi uliokuwa ukiendelea. Uchunguzi ulipokamilika ilibainika mwili wa marehemu ulikuwa na michubuko shingoni na kwenye mbavu kitu kilichomaanisha kulikuwa na purukushani kabla ya kifo chake. Hawakubaini alama za vidole katika mwili wa marehemu, Suala hilo liliongeza udadisi uliokosa majibu. Kilibaki kuwa kitendawili kigumu sana. Polisi walipojiridhisha na uchunguzi wa mwili wa marehemu waliruhusu mwili uzikwe. Zilikuwa zimepita siku tatu tangu igundulike maiti yake. Ndugu walifuata utaratibu wa mazishi chini ya usimamizi wa mdogo wa marehemu, ndugu Derrick Kalikumbi, mdogo pekee wa marehemu aliyebaki. Siku mbili baada ya kuupumzisha mwili wa mzee Lewis Kalikumbi katika nyumba yake ya milele, polisi walitoa taarifa ya uchunguzi wao waliokuwa wakiufanya. Taarifa ya polisi ndiyo iliyozua tafrani na hali ya sitofahamu. Mkuu wa jeshi la polisi katika mkoa huo wa Rwama Mwisho alisimama mbele ya vyombo vya habari na kueleza

“Tulikuwa kimya kwa siku kadhaa ili kupisha uchunguzi dhidi ya tukio la kukutwa kwa mwili wa Lewis Kalikumbi katika nyumba yake. Kifo chake kimezungukwa na mambo mengi. Moja ya mambo hayo, tulikuta soksi ambayo huvaliwa usoni na mtu au watu tunaoamini wapo nyuma ya matukio mengi ya mauaji na uuzaji wa madawa ya kulevya. Soksi ilikuwa na alama za vidole vya marehemu na alama zingine za mwili wake mwenyewe. Hivyo, kulingana na majibu ya soksi ile inatuaminisha marehemu ndiye aliyekuwa akisimama kama kiongozi wa magenge haramu au kama siye, basi waliomuua walimlazimisha kuishika soksi ile kabla hawajaondoa uhai wake. Ukiacha suala hilo kuna suala lingine, pembeni ya mwili wa marehemu ilikutwa bastola ndogo ya mkononi. Tulipoifatilia ilionesha ilikuwa ikimilikiwa kihalali na kijana mmoja aliyekuwa mfanyabiashara ya vito vya dhahabu lakini aliuliwa katika mazingira ya kutatanisha. Silaha hiyo ilikutwa pembeni ya marehemu na tulipoichunguza tulibaini alama za vidole vya mzee Lewis Kalikumbi, kitu kinachomaanisha alikuwa akiitumia au alishikishwa…swali tunalojiuliza ni kuhusu michubuko iliyokutwa katika mwili wa marehemu”

Yalikuwa maelezo mengi yaliyogawa watu sehemu mbili, baadhi ya watu waliamini mzee yule alikuwa mwema na aliuliwa na majambazi lakini kundi lingine lilikinzana na kundi hilo. Wao waliamini alikuwa jambazi sugu aliyejificha kwenye biashara za usafirishaji watu nchi za nje. Catherine Lewis alibaki njia panda. Alishindwa kukubali au kukataa upande wowote. Alikataa kuamini kama baba yake alikuwa mwema baada ya kumuhusisha na vifo vya Magreth Peter na mama yake lakini alikataa kukubali kuwa baba yake alikuwa muuaji alipofikiria namna alivyokuwa mtu wa watu. Hali ilikuwa tofauti kwa mwanajeshi Abdul Said. Yeye aliamini moja kwa moja kuwa mzee Lewis Kalikumbi alikuwa jambazi sugu aliyejificha nyuma ya soksi kwa lengo la kuficha uhalisia wake. Kwake ilikuwa furaha sana baada ya kusikia na kujihakikishia kifo cha mzee yule.
Mara kadhaa Catherine Lewis na Abdul Said walikutana na kuongea mawili matatu, makutano yao yalikuwa ya siri sana. Hawakutaka jamii ifahamu kama walikuwa kwenye muungano wa jambo fulani. Walifanya hivyo ili kulinda usalama wa mtoto. Waliamini japokuwa mzee Lewis Kalikumbi alikuwa ameshafariki lakini haikumaanisha amani kwa mtoto kwa sababu waliokuwa wakimpinga mtoto Derrick Edward walikuwa wengi. Mara zote walizokutana Abdul Said hakuchoka kumpa pole Catherine Lewis kwa kupoteza nguzo mbili za familia yake katika kipindi kifupi. Waliamini kulikuwa na kidudu mtu kikitembea katika familia. Mtoto aliendelea kukaa kwenye mikono ya Abdul Said aliyeamua kumuajiri msichana kwa ajili ya kumuhudumia.

BAADA YA WIKI MOJA
Taarifa mbaya zilienea kila kona ya jiji la Rwama Mwisho, hakika zilikuwa na vigezo vya kuitwa taarifa mbaya. Ukoo wa mzee Kalikumbi uliendelea kupata pigo la kutisha, pigo lililomshangaza kila mmoja aliyesikia taarifa hizo. Pigo hilo lilimaanisha hatari dhidi ya kila mwana familia au ukoo wa Kalikumbi, hakuna aliyekuwa na uhakika wa usalama wake. Ulikutwa mwili wa baba yake mdogo Catherine Lewis aliyekuwa akifahamika kwa jina la Derrick Kalimbuki ukiwa umechomwa kisu cha moyo katika ofisi yake ya usambazaji wa nafaka. Ofisi iliyokuwa ghafla kama uyoga siku hadi siku. Pembeni ya mwili huo ilikutwa soksi ya kuvaa usoni, soksi kama iliyokutwa kwenye maiti ya kaka yake, mzee Lewis Kalikumbi. Pembeni ya maiti ilikuwa flashi nyeusi iliyofungwa kamba maalumu yenye maandishi yaliyosomeka

“In our line of work, trusting people costs lives” (Katika kazi yetu, kuamini watu hugharimu maisha)

KITABU KINAPATIKANA KWA TSH 20,000 TU, WASILIANA NAMI KWA NAMBA 0758 195 890 KUPATA NAKALA YAKO. KINA PAGE 363. KIMECHAPWA KWA KARATASI ZA OFF-WHITE ZISIZOUMIZA MACHO. KINA UBORA ULIOTUKUKA.

MWISHO WA KUPOST JF. NAKALA ZIPO SOKONI, NATUMA MIKOA YOTE TANZANIA.

ASANTE SANA.
IMG-20220522-WA0005.jpg
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI

CAPE TOWN, AFRIKA KUSINI
Ingawa hali ya hewa ilikuwa tofauti na nchi aliyozaliwa na kukulia lakini alikuwa ameanza kuizoea. Kipindi cha wiki moja alichokaa jiji la Cape Town kilitosha kutengeneza mazingira ya kuzoea hali ya hewa ya jiji lile. Japokuwa kilichompeleka sicho alichokikuta. Alipandikizwa na daktari Johnson katika ngome ya mzee Masiya akaambiwa ikiwa atafanya vizuri kazi aliyopewa atakabidhiwa mtoto wake akiwa hai. Aliambiwa kazi hiyo ilikuwa ya mwisho katika harakati zake za kupigania uhai wa mtoto wake. Aliambiwa atawasilisha zawadi kwa mzee Masiya, kisha afanye juu chini kumchunguza mzee huyo na mifumo yake yote ya biashara za madawa ya kulevya kisha taarifa hizo aziwasilishe katika kundi lililokuwa chini ya Nasrat Abdul al Aziz, lakini kipindi hicho lilikuwa chini ya daktari Johnson baada ya taarifa za kifo cha Nasrat Abdul al Aziz. Hali ilikuwa tofauti. Mara baada ya kuwasili nchini Afrika Kusini, akashikiliwa na mzee Masiya kisha akafanywa kuwa kibaraka wa kusambaza madawa ya kulevya katika mitaa ya Cape Town. Hivyo suala la kurudi nchini kwake lilikuwa ndoto za mchana. Mzee Masiya aliamua kuchukua maamuzi hayo baada ya kuwasiliana na Amani Collence.

Amani Collence alimuhakikishia mzee Masiya kuhusu kifo cha Nasrat Abdul al Aziz, hivyo wakakubaliana kumtumikisha David Samson kama wanavyotumikishwa wafanyakazi wengine wanaowafanyia biashara zao za madawa ya kulevya. Hawakuona umuhimu wa kuendelea kulichunguza kundi lililopoteza kiongozi wake aliyekuwa adui yao. Kwa sababu mara kadhaa walipojaribu kulipeleleza kundi lile hakuna majibu waliyopata, walijihakikishia kundi lililokuwa chini ya Nasrat Abdul al Aziz limesambaratika baada ya kifo cha muasisi wao. Suala hilo lilikuwa pigo kubwa sana kwa David Samson kwa sababu lilizima mwanga wa kurudi nchini kwake. Alimfikiria mpenzi wake kisha akili ikawaza juu ya kichanga chake kilicho mikononi mwa daktari Johnson. Suala la kubadilika kwa mambo hayo lilimjengea hofu ya kumkosa mtoto wake na hivyo kumuweka mtoto huyo katika hatari ya kukulia kwenye genge la wahalifu au kuuliwa kama alivyoahidiwa.

Japokuwa David Samson hakuwa na muda mrefu Cape Town lakini alikuwa ameshaanza kazi ya kusambaza madawa ya kulevya kwa walengwa, kwakuwa alikuwa mgeni aliambatana na vijana wenyeji wa jiji na wazoefu wa biashara hiyo. Ilikuwa biashara ngumu kwake ingawa aliwahi kuifanya kwa kipindi kifupi alipokuwa chini ya himaya ya Amani Collence. Alipewa kazi ya kupeleka mzigo wa madawa ya kulevya katika hotel ya Premier. Kazi hiyo aliifanya kwa uangalizi mkubwa chini ya usimamizi wa wenyeji wenyeji. Aliyafikisha chumba namba 125 kilichokuwa kikimilikiwa na msichana mrembo wa kizungu. Msichana yule alikuwa mrefu wa wastani, hakustahili kuitwa mrefu wala mfupi. Alikuwa na umbile la kibantu hasa, aliongea Kimalosha vizuri kilichoathiriwa na lafudhi ya Kizungu. Suala hilo lilimshangaza sana David Samson kwa sababu lilimuaminisha kuwa msichana yule aliwahi au anaishi katika taifa la Malosha. Alipojaribu kufikiria kwa kina bado alikosa jibu sahihi, bali aliendelea kutengeneza maswali ya kutosha.

Awali alikuwa akienda mara mbili kwa wiki lakini ghafla ratiba yake ikabadilishwa. Akaambiwa atakuwa anapeleka madawa ya kulevya mpaka atakapoambiwa na mkuu kiongozi wa eneo lake. Kipindi chote alichopeleka mzigo hakupewa nafasi ya kumzoea yule mzungu, alikuwa akitoa mzigo kisha anaondoka. Alikuwa akiingia ndani ya chumba kile pamoja na wenyeji wake wawili. Wenyeji wake walikuwa wakifahamiana na msichana yule wa kizungu, waliongea naye hasa kwa lugha ya kiingereza. Kitu kilichoonesha walikuwa washirika wa muda mrefu katika biashara hiyo. David Samson alipojaribu kuchangia chochote katika mazungumzo yao, alikatishwa juu juu tena kwa dharau iliyopitiliza toka kwa msichana yule wa Kizungu. Heri udharauliwe na mbantu mwenzako kuliko udharauliwe na mzungu katika bara lako. Ilimuuma sana lakini hakuwa na jinsi zaidi ya kufanya kilichompeleka.
Chuki dhidi ya msichana yule ilijitengeneza taratibu, msichana yule wa Kizungu alielewa hali ya David Samson. Alifurahia sana lakini furaha yake hakuionesha mbele za watu. Alipofikiria kwa umakini, hata yeye hakuona sababu ya msingi ya kumdharau David Samson lakini alikuwa ameshaamua kumdharau. Akaendelea alipoishia.

David Samson hakufanikiwa hata kujua jina halisi la msichana yule wa kizungu, mara zote alisikia akiitwa kwa jina la ‘The White Mafia’. Ulipita mwezi mzima pasipo kupeleka madawa ya kulevya katika hoteli ile, wala hakusikia habari yoyote kuhusu msichana yule wa Kizungu kutoka katika kundi la wahuni alilokuwa akienda nalo na akiishi nalo. Alijiuliza maswali mengi sana, lakini swali lililomsumbua sana lilikuwa

“Au The White Mafia ameelekea Malosha?”

Hakupata jawabu kamili. Kipindi chote hicho hakufanikiwa kumuona mzee Masiya kwa mara nyingine, alimuona siku ya kwanza aliyofika jijini Cape Town. Siku hiyo hiyo David Samson alikabidhiwa kwa kijana wa Kizulu aliyefahamika kwa jina la ‘The Eye’. Kijana huyo alikuwa na jicho moja bovu, jicho la upande wa kushoto. Sehemu ya jicho hilo kulikuwa na kovu kubwa. Sura yake ilitisha sana, haikuwa rahisi kumtazama mara mbili kwa sababu hata yeye hakupenda kutazamwa hivyo. Kasoro yake ilitengeneza chuki kwa wengine, aliwaadhibu kila alipohisi wakimdharau. Hakika cheo dhamana. Jina la The Eye lilikuwa kubwa sana jijini Cape Town na Afrika Kusini kwa ujumla. Alikuwa akitafutwa kila kona ya nchi, alikuwa mhalifu aliyefanya mauaji kila alipojisikia kufanya. Kila aliyejaribu kuzuia mpango wake wa kihalifu alitangulia mbele ya haki. Taifa nzima la Afrika Kusini na majirani zake walimchukia The Eye kama shetani. Iliaminika mtu huyo alikuwa akimiliki genge la wauza madawa ya kulevya na unyang`anyaji wa kutumia silaha za moto.

Taifa halikujua kama nyuma ya The Eye alikuwepo mzee Masiya. Mzee aliyejikita kwenye siasa kupitia chama kikuu cha upinzani. Awali habari zilisambaa karibu Afrika nzima kuwa mzee Prince Siyabonga alimaarufu kwa jina la Mzee Masiya anajihusisha na biashara ya madawa ya kulevya, lakini habari hizo zilikosa mashiko baada ya kukosekana kwa ushahidi wa kina. Wanaharakati mbalimbali waliibuka na kumtetea mzee Masiya, wana harakati hao waliikashifu serikali ya Afrika Kusini kwa kumchafua mwanachama wa chama kikuu cha upinzani, mwanachana aliyekuwa na nguvu ya ushawishi mkubwa ndani ya taifa hilo. Watu wakaanza kuamini taratibu kuwa serikali ilimvisha upepo mchafu mzee Masiya ili achafuke na raia wamkatae. Kitendo kile kilitengeneza huruma kwa wananchi. Upendo dhidi ya mzee Masiya ukaongezeka maradufu.

Mara kadhaa mzee Prince Siyabonga ‘mzee Masiya’ katika kampeni zake za kisiasa aliwaambia wananchi wampigie kura ya ndiyo ili aweze kuwapigania, aliwaahidi kupambana na wahalifu wote. Jina la The Eye lilikuwa sehemu ya kampeni zake, alisema lazima atafanya juu chini kumkamata au kumteketeza kabisa mwanaharamu huyo. Watu walimpenda zaidi na zaidi. Jina la mzee Masiya lilizidi kupaa, jina hilo hakujipa mwenyewe bali alipewa na raia wa jiji la Cape Town. Alikuwa msaada kwa wana Cape Town, alitoa huduma nyingi za kijamii katika jiji lile zaidi ya serikali iliyokuwa madarakani. Alikuwa mwiba wa serikali iliyokuwa madarakani. David Samson aliiona nguvu ya mzee Masiya, kitendo kile kilimaanisha hakuwa na nguvu yoyote ya kumchunguza mzee yule kwa sababu uchunguzi wake ungemaanisha kifo chake endapo akigundulika.

Genge alilopelekwa David Samson lilipatikana jirani ya mgahawa wa Damascus, mgahawa unaopakana na barabara kuu ya M61. Genge hilo lilikuwa na vijana kumi tu, David Samson alikuwa wa kumi na moja. Katika genge hilo walifanikiwa kuonana na The Eye kwa wiki mara moja au kwa wiki mbili mara moja. Katika kipindi chote David Samson alichoishi na vijana hao aligundua wana genge wote waliamini kiongozi wa genge hilo alikuwa The Eye. Hakuna hata mmoja aliyekuwa akijua nyuma ya The Eye alikuwepo mzee Masiya. Kitendo kile kilimshangaza sana David Samson, lakini hakufungua mdomo kuongea chochote kwa sababu hakuna aliyemuamini miongoni mwa wana genge wale. Na hakujua kwanini hakuambiwa na mzee Masiya kuwa vijana wale hawafahamu chochote kuhusu umiliki wake, David Samson alihisi kuna siri iliyojificha. Alihisi labda alikuwa mtegoni. Aliufunga mdomo wake kwa zipu ya chuma.

Siku zikasogea, mwezi ukapita pasipo kumuona The Eye katika ngome yao. Ngome nzima ilishangaa kwa kitendo hicho kwa sababu haikuwa kawaida. Mara zote The Eye huwapa taarifa za mabadiliko ya ratiba zake lakini kipindi hicho hali ilikuwa tofauti. Hofu iliendelea kutanda katika umoja wao. Hofu yao ilikata baada ya kutokea kwa The Eye usiku wa maneno, siku hiyo The Eye hakuwa na maneno mengi. Alifika akagawa mzigo wa madawa ya kulevya kwa vijana wake. David Samson alishangaa kwanini siku hiyo hakukabidhiwa mzigo wowote, alitamani kuuliza lakini akaona akifanya hivyo atakuwa mpuuzi wa mwili na akili. Akakaa kimya. Alidhani alikuwa amepata hisani kumbe The Eye alikuwa na mpango dhidi yake. The Eye alimgeukia David Samson kisha akamwambia kwa lugha ya kiingereza

“You have to meet with The White Mafia right now” (Yakupasa kukutana na The White Mafia sasa hizi)

Siyo kwamba The Eye alikuwa hajui kabisa kuongea Kimalosha, hapana, alikuwa akikiongea kwa shida ndiyo maana mara nyingi alipendelea kutumia lugha ya kiingereza alipokuwa akiongea na David Samson. Mara chache alipoongea na vijana wake alitumia lugha ya Afrikaans. Kauli ya The Eye ilimshangaza sana David Samson, alikosa jibu la kutoa. Alibaki kamtumbulia macho kama mtu aliyegandishwa na barafu. David Samson hakuona uhusiano wowote wa kwenda kukutana na The White Mafia wakati ule kwa sababu hakupewa mzigo wowote wa madawa ya kulevya, vile vile hakuwa na uhusiano mzuri na mtu huyo. The Eye alielewa alichokuwa akikiwaza David Samson, alifumbua mdomo kwa mara ya pili kisha akaongea kwa sauti yake ya kukwaruza

“I know The White Mafia does not like you, she told me everything about you and her, but this job needs people who can speak Malosha language well, you and her can do it” (Najua The White Mafia hakupendi, alishaniambia kila kitu kuhusu wewe na yeye, lakini hii kazi inawahitaji watu wanaoweza kuongea lugha ya Malosha vizuri, wewe na yeye mnaweza kuifanya)

Jibu la The Eye halikukidhi maswali ya David Samson, lakini kwakuwa David Samson hakuwa na sauti yoyote katika umoja ule alibaki kimya kusubiri kitachofuata. The Eye aliwageukia vijana wake aliowapa madawa ya kulevya kisha akawasihi wajitahidi siku inayofuata wasambaze katika vituo walivyoambiwa. Baada ya kauli hiyo The Eye alimuamuru David Samson amfuate nyuma. David Samson alitii kauli, akawa nyuma kama mkia wa mnyama. Walitembea mpaka nje ya nyumba hiyo. Kulikuwa na gari aina ya Toyota LandCruiser toleo jipya. The Eye alifungua mlango wa mbele akaingia, muda huo David Samson alikuwa akifungua mlango wa nyuma. Alipoingia alikutana uso kwa uso na The White Mafia. Msichana wa kizungu aliyekua akimpelekea mzigo wa madawa ya kulevya. David Samson alishituka moyoni lakini usoni alionekana jasiri kwa asilimia mia moja. Msichana yule wa Kizungu akaachia tabasamu baada ya kumuona David Samson, kilikuwa kitendo cha kushangaza sana kwa David Samson kwa sababu toka awali wawili hao hawakuwa na uhusiano mzuri. Kwanini leo aoneshe furaha dhidi yangu? Lilikuwa swali ngumu sana katika akili ya David Samson. The White Mafia hakuishia kutabasamu tu, bali mlimkaribisha kwa kauli iliyosema

“Karibu sana kijana, karibu tuendelee tupoishia”

David Samson hakujibu kauli ya msichana yule, alijiweka vizuri kitini kisha macho yakatazama mbele usawa wa dareva. The White Mafia hakujali chochote, akilini akiwaza vitu vingi kuhusu David Samson. Aliamini lazima avipatie majibu ndani ya siku za usoni. Gari lilishika mafuta na kuanza kuondoka kwa mwendo kasi. David Samson alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha ilikuwa saa nane kasoro dakika kumi na mbili. Usiku mnene. The White Mafia alibadilisha nguo ndani ya gari, hakujali uwepo wa David Samson pembeni wala The Eye aliyekuwa nyuma ya usukani. Alivaa mavazi ya kikahaba, mapaja wazi na kitovu nje. David Samson alishangazwa na kitendo kile, aliamini kuna mchezo mchafu mbele ya safari. Akapiga moyo konde, safari ikaendelea. Gari lilisimama jirani kabisa na eneo maarufu jijini Cape Town, eneo linaloitwa Studio 47, studio yenye hadhi ya kisasa. Studio ambayo mara nyingi hutumiwa na watu maarufu kuandaa kazi zao.

The White Mafia alishuka akaingia ndani ya studio ile kisha baada ya dakika moja alirudi ndani ya gari akiwa na begi dogo la mgongoni. Safari ikaendelea. Ukimya ukatawala mpaka walipofika mtaa maarufu kwa jina la Louis Grandner. Fujo za hapa na pale zilikuwa zikiendelea mtaani pale utafikiri haukuwa usiku wa manane. The Eye aliyekuwa ameshika usukani wa gari hakujali fujo zile, aliendesha gari mpaka nje ya Kasino iliyokuwa na bango kubwa lililosomeka ‘GrandWest Casino and Entertainment World’. Bango lile lilikuwa likiwaka mataa ya rangi mbalimbali, mataa yaliyopendezesha maandishi yale kwa ustadi wa hali ya juu. Kwa macho ya nje tu ilionekana kuwa Kasino ghari jijini humo. Gari lilifunga breki jirani zaidi ya mlango wa kuingia kwenye Kasino hiyo kisha The Eye akachukua kofia aina ya kepu akavaa vizuri, ikaweza kuficha sura yake. Akageuka nyuma walipokaa David Samson na The White Mafia kisha akawaambia

“Mnatakiwa kufuata hatua zangu na si vinginevyo”

Baada ya kauli hiyo hakusubiri jibu, alifungua mlango wa gari kisha akashuka. Alikuwa mbele akifuatwa nyuma na The White Mafia kisha David Samson. Waliingia ndani ya Kasino, hali ilikuwa tete kwa David Samson aliyekuwa hajazoea kuingia kwenye Kasino za namna ile. Wanawake walikuwa wakitembea vifua wazi, wachache sana waliovaa sidiria nyepesi zilizoonesha maumbile ya matiti yao. Bikini zilisitiri nyeti zao huku zikiacha wazi sehemu yote ya makalio yao. Watu walikuwa bize wakifanya starehe mbalimbali zilizobeba dhambi na laana juu yao. Hatua za The Eye zilielekea kwenye moja ya choo cha Kasino hiyo, hakikuwa choo cha kila mmoja. Choo kile kilikuwa kikitumiwa na kijana mdogo wa miaka takribani ishirini na saba pamoja na rafiki zake alioambatana nao.

Kijana huyo alifahamika kwa jina moja maarufu la Mr Kasino, kijana aliyeaminika kuwa mmiliki wa Kasino hiyo. Mara chache sana watu waliingia ndani ya choo kile na kukitumia, lakini kwa sababu maalumu. Japokuwa kilikuwa hakifungwi mlango lakini haikuwa rahisi kwa mtu kuingia. Hata mara chache hizo watu walizoingia ndani ya choo hicho walipewa ruhusa na walinzi wawili waliokuwa na kazi ya kulinda mlango ule. Iliaminika kilikuwa choo kama vyoo vingine, kumbe ndani ya choo hicho kulikuwa na mlango wa siri wa kuingia ndani ya chumba cha siri kilichopatikana chini ya Kasino hicho.

The Eye alipofika mlangoni mbele ya walinzi wale, wala hakuinua sura yake kuwatazama bali alitoa kadi fulani mfukoni iliyokuwa na maandishi yaliyosomeka PSE akawaonesha, kisha akatoa ishara ya vidole vitatu akimaanisha kuwa wapo watatu. Walinzi hawakujibu salamu yake, walibaki kama walivyo. The Eye alifungua mlango wa choo akaingia, kisha akafatiwa na The White Mafia alafu David Samson akawa wa mwisho. Kitendo kile cha watu wa jinsia tofauti kuingia kwenye choo kimoja hakikuwashangaza watu wengine kwa sababu ilikuwa kawaida sana watu kufanya mapenzi katika mazingira yoyote waliyohisi yaliwafaa kufanya hivyo. Hakuna aliyejali mambo ya mtu mwingine.

Walipofika chooni, The Eye alifungua mlango wa siri kisha akatangulia kuingia. Kitendo kile kilimshangaza sana The White Mafia, hakujua kama kuna mlango mahala pale. Hakuwa akifahamu siri ile muda wote aliokuwa akisambaza madawa ya kulevya ya kundi hilo. Waliingia ndani ya chumba kikubwa cha kifahari, chumba kile kilikuwa na watu watatu pekee. Mmoja kati ya watu hao alikuwa mzee Masiya, pembeni yake alisimama msichana mrembo wa Kiafrika mwenye umri chini ya miaka thelathini. Alionekana goigoi kwa namna alivyokuwa na umbo zuri la kuvutia. Mwingine alikuwa kijana mwenye umri usiozidi miaka arobaini, alivaa begani silaha ya moto aina ya AK 47. Muda wote alikuwa amekunja sura mithili ya mtu aliyetafuna mbegu ya limao. Muonekano wake ulimaanisha alikuwa kijana wa kazi hasa, kijana mwenye jukumu la kulinda uhai wa mzee Masiya. The Eye alienda moja kwa moja mpaka mbele ya mzee Masiya, akainama kuonesha ishara ya kutoa heshima kisha akaongea kwa sauti iliyojaa adabu na heshima

“They are waiting for your statement, tomorrow morning they will finish everything” (Wanasubiri kauli yako, kesho asubuhi wamalize kila kitu)

Mzee Masiya aliinua kichwa akawatazama David Samson na The White Mafia kwa zamu kisha akatabasamu. Kipindi mzee Masiya akitafakari neno la kuongea, The White Mafia alikuwa mbali sana kimawazo. Alikuwa haamini kama alikuwa mbele ya mzee Masiya, siku zote alikuwa haamini kama mzee ule alikuwa akihusika na biashara za madawa ya kulevya. The White Mafia alikuwa akifanya kazi pasipo kumfahamu mkuu halisi wa kazi hizo japokuwa toka awali alijua The Eye siyo kiongozi halisi, alilitambua hilo toka kwa The Eye. Japokuwa The White Mafia alishangazwa sana na uwepo wa mzee yule mahala pale pa anasa na uhalifu lakini mshangao huo hakuuonesha usoni kwake. Usoni alikuwa vizuri kama alivyoingia. David Samson hakushangazwa na uwepo wa mzee yule mahala pale kwa sababu alikwisha onana naye ndani ya chumba kile kile siku ya kwanza aliyowasili jijini humo. Siku iliyobadilisha ndoto ya maisha yake.

Mzee Masiya alichomoa sigara toka kwenye pakiti ya kutunzia sigara, ilikuwa sigara aina ya Camel. Sigara zinazotengenezwa nchini Marekani na Japan. Aliiweka mdomoni kisha yule mwanamke mwenye umbile goigoi akachukua kibiriti kilichokuwa juu ya meza na kukiwasha, alikipeleka mpaka kwenye usawa wa mdomo wa mzee Masiya kisha akawasha sigara ile. Mzee Masiya alivuta pafu moja kwa nguvu, akasikilizia namna moshi ule ulivyokuwa ukipenya kwenye mapafu yake kisha akautoa nje kupitia puani. Sasa aliona alikuwa sawa kimwili na kiakili. Alimtazama The White Mafia kisha akamwambia

“The task before you is simple if you do it skillfully, but very difficult if you do it carelessly. It can cost lives of each of you, and put us in a very dangerous situation” (Kazi iliyo mbele yenu ni rahisi mkiifanya kwa ustadi, lakini ni ngumu sana mkiifanya kwa uzembe. Inaweza kugharimu maisha ya kila mmoja wenu, na kutuweka katika mazingira hatarishi sana)

Muda wote The White Mafia alikuwa akiangalia namna mdomo wa mzee Masiya ulivyokuwa ukitamka haraka namna ile, kitu kilichomaanisha mzee yule alikuwa akijua nini alichokuwa akikiongea. Alikuwa akiifahamu vizuri kazi iliyokuwa mbele yake kwa ajili ya kuikabili. The White Mafia alikuwa hajui kazi gani ilikuwa mbele yake, kazi gani ya kushirikiana na David Samson. Akili ilienda mbali sana, akakumbuka siku ya kwanza aliyoingia katika mtandao huo wa madawa ya kulevya. Alipewa kazi ya kusambaza madawa hayo katika mataifa ya matano yaliyokuwa yakizungumza lugha ya Kimalosha. Siku zote alikuwa akiifanya kazi peke yake pasipo uwepo wa mtu mwingine kama msaidizi au mshiriki, alishangazwa kushirikishwa na David Samson. Alibaki njia panda. Mzee Masiya aliendelea kutoa ufafanuzi wa kazi waliyotakiwa kuifanya

“I have been informed that, a detective from Malosha will arrive by plane tomorrow morning. The detective is coming for two jobs. One, about David, and second, about my network. We have to destroy him before he gets any information about us” (Nimepewa taarifa kuna mpelelezi kutoka Malosha atafika kwa usafiri wa ndege kesho asubuhi. Mpelelezi huyo anakuja kwa kazi mbili. Moja, kuhusu David, na pili, kuhusu mtandao wangu. Inatakiwa tumuangamize kabla hajapata taarifa yoyote kutuhusu)

Kauli ya mzee Masiya ilizidi kutengeneza taswira tofauti katika ubongo wa The White Mafia, alifikiria mbali sana akaona kuna vita kali ipo mbele. Aliamini ameingia katikati ya vita ya nchi mbili. Vita ya taifa la Malosha na Afrika Kusini. Upande wa David Samson alihisi faraja, alifurahia moyoni baada ya kusikia kauli hiyo. Aliamini ukombozi upo njiani. Furaha yake ilibaki moyoni pasipo kuionesha usoni. Muda huo The Eye, David Samson na The White Mafia walikuwa wamesimama wima kama milingoti ya umeme. Mzee Masiya aliwaamuru wakae, wakatimiza kauli ya mkuu wao. Mzee Masiya aliwafafanulia njia iliyoandaliwa ya kumkamata adui yao aliyekuwa njiani. Vile vile aliwaeleza kuwa kazi hiyo ilikuwa mikononi mwao kwa sababu wao wawili walikuwa wazuri sana katika kuongea lugha ya Malosha.

Japokuwa mtego uliotegwa haukulenga kumhusisha David Samson moja kwa moja katika mazungumzo na adui yao aliyekuwa njiani lakini ulimuhitaji David Samson aonekane katika uwanja wa ndege atakaotua mpelelezi huyo. Walihitaji umakini na taharuki ya mpelelezi huyo ihamie kwa David Samson kisha ashambuliwe na kuuliwa pale pale uwanjani. Huo ulikuwa mpango wa kwanza. Walikubaliana, endapo mpango huo ukifeli lazima The White Mafia afanye juu chini mpaka apate mwanya wa kuonana na kuongea na mpelelezi huyo, ili aweze kumuweka karibu na kumsambaratisha mara moja. Hapo ndipo David Samson na The White Mafia walipoelewa kuwa kazi hiyo haikuwahitaji waongeaji wa lugha ya Malosha kwa asilimia kubwa kama walivyoambiwa awali. Hofu ya kusababisha mauaji ilimuingia David, alijiona namna alivyokuwa akifanywa chambo kwa ajili ya kumuangamiza mpelelezi kutoka katika taifa lake. Alitamani kugoma kufanya kazi hiyo lakini hakuwa na sauti yoyote, alijua akifanya hivyo atasababisha kifo chake. Kichwa cha The White Mafia kiliwaza namna ya kukabiliana na tukio lililokuwa mbele yake, aliwaza na kuwazua namna ya kupambana nalo. Alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha ilikuwa saa tisa na nusu usiku. Akakumbuka kauli ya mzee Masiya, kauli iliyosema mgeni wao atawasili na ndege ya saa tatu asubuhi. Waliagana. Muda huo kila mmoja alikuwa chumbani kwake akisubiri pakuche akatimize jukumu alilopewa. Walilala katika vyumba vinavyopatikana katika Casino hiyo. Vyumba ghari sana katika jiji la Cape Town

Yalikuwa majira ya saa tatu kasoro dakika kumi, mvua ndogo iliyoambatana na upepo iliendelea kusalimia sura ya nchi. Hali ile ya hewa iliruhusu watu kuvaa majaketi makubwa ya kuhifadhi joto. Watu waliendelea kujitokeza katika uwanja wa ndege wa Cape Town unaofahamika kwa jina la ‘Cape Town International Airport’, wengi walifika kuwapokea watu wao waliotoka sehemu mbalimbali. Ulinzi ulitukuka kama kawaida, polisi walitapakaa eneo lile kama ilivyo ada yao ya kila siku. Gari la kisasa aina ya Toyota LandCruiser toleo la kisasa lililoendeshwa na The Eye usiku wa siku iliyopita lilipiga breki jirani kabisa na uwanja ule wa ndege. Nyuma ya usukani alikaa The White Mafia, pembeni yake alikaa David Samson aliyekuwa akiendelea kutafunwa moyoni kwa hofu kali. The White Mafia alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha zilikuwa bado dakika nne kufika saa tatu kamili. Alishusha kioo cha gari kisha akatazama nje kupitia dirishani. Aliona namna watu walivyokuwa bize kutembea tembea nje ya uwanja kwa lengo la kuwasubiri wageni wao. The White Mafia alimgeukia David Samson kisha akamwambia

“Umefika wakati wa kukaa nje sehemu ya wazi ili kumuhadaa mpelelezi wako, hapa kuna watu wengi sana yaweza tusimuone lakini yeye akakuona. Hapo ndipo tutapata wasaa wa kumuona na kumshambulia kwa sababu lazima atatafuta namna ya kukupata au kuongea na wewe”

David Samson alielewa kauli ya The White Mafia. Akafungua mlango pasipo kutoa jibu lolote kisha akakaa nje kama alivyoagizwa. Kipindi David Samson akishuka kutoka ndani ya gari simu ya The White Mafia ilinguruma, The White Mafia aligundua ujumbe ulikuwa umeingia. Akaichukua na kuitazama, ilimuonesha ulikuwa ujumbe kutoka kwa The Eye. Alijua utakuwa ujumbe muhimu sana kuhusu kazi iliyokuwa mbele yao, akaufungua kisha akausoma

“After killing the detective, kill David too” (Baada ya kumuua mpelelezi, muue David pia)

Ujumbe ule ulimshitua sana The White Mafia, akainua kichwa na kumtazama David Samson aliyekuwa eneo la wazi kama chambo cha kumkamatisha au kumuua mpelelezi aliyekuwa njiani. Alimtazama kwa jicho la pekee sana akakosa jibu la maswali aliyokuwa akijiuliza mwenyewe. Akapekua simu yake mpaka katika sehemu ya kutunzia picha. Aliitazama picha ya mpelelezi aliyekuwa njiani, mpelelezi aliyetakiwa kumuua. Ilikuwa sura ya kijana mtanashati aliyeandamwa na tabasamu, macho ya duara ya kijana yule yalimtazama pasipo kuchoka. Akarudisha macho kumtazama David Samson aliyekuwa amesimama akichezesha chezesha miguu yake kama mtoto wa miaka kumi au kumi na mbili. The White Mafia alijiuliza mwenyewe

“Huyu kijana ni nani hasa mpaka atafutwe na mpelelezi kutoka Kuwainia? Kwanini The Eye anataka nimuue? Hapa kuna namna”

The White Mafia alichomoa bastola toka kiunoni kwake kisha akaibusu, akaiweka juu ya mapaja yake huku macho yakiendelea kumtazama David Samson. Akili ya The White Mafia ilikuwa tayari kutimiza alichopanga kufanya. Aliliwasha gari likawa linanguruma muda wote kama mtu aliyekuwa akihitaji kuondoka lakini alibaki pale pale. Alifanya vile ili kuwa tayari kuondoka pindi atakapotimiza azma yake. Alitazama saa ya kwenye gari ikamuonesha ilikuwa saa tatu na dakika mbili, aliamini muda wowote mtego upo mbioni kumnasa mhusika wao. Alipata wazo jipya, hakujiuliza mara mbili. Alitafuta jina fulani katika simu yake kisha akapiga, aliyepigia alipokea. The White Mafia aliongea haraka haraka pasipo salamu

“Cape Town International Airport, don’t be late” (Uwanja wa Kimataifa wa ndege wa Cape Town, usichelewe)

Baada ya kauli hiyo alikata simu haraka. Alianza kujipiga piga mapajani kama mtu aliyekuwa akiomba aliyempigia simu apae haraka sana. Aliendelea kutazama nje eneo ambao wasafiri hulitumia kutoka. Akatazama saa yake ya mkononi ikamuonesha ilikuwa saa tatu na dakika kumi, mapigo ya moyo yakaongezeka, akahisi anaweza kufeli mpango wake lakini alijipa moyo. Hakika ukijipa moyo lazima ushinde, ndivyo ilivyokuwa. Dakika moja baadae simu yake ilianza kunguruma, alipoitazama alikuwa yule mtu aliyempigia simu dakika chache zilizopita. Akaipokea haraka haraka, mtu yule mwenye sauti nzito yenye hadhi ya kuitwa sauti ya dume la mbegu aliongea taratibu

“Where are you?” (Upo wapi?)

The White Mafia alimuelekeza haraka haraka mwanaume yule mwenye sauti nzito. Baada ya sekunde kadhaa Taxi ilipiga breki jirani kabisa na gari alilokuwemo The White Mafia. Dereva Taxi alifungua kioo cha gari cha upande wa gari la The White Mafia. Alikutana uso kwa uso na The White Mafia, alitegemea salamu lakini haikuwa hivyo. The White Mafia alifungua mlango wa gari kisha akashuka. Akamuamuru dereva Taxi ashuke garini kisha achukue gari lake (Toyota LandCruiser toleo) na kuondoka mahali pale mara moja. Kilikuwa kitendo kilichomshangaza kidogo dereva Taxi lakini kwakuwa alikuwa akimfahamu vizuri The White Mafia hakubisha, alishuka haraka na kuingia ndani ya Toyota LandCruiser na kuondoka kwa mwendo kasi. Kipindi mambo hayo yakiendelea David Samson hakufanikiwa kuona chochote, macho yake yalikuwa mbele yakiendelea kutazama umati wa watu kama anaweza kumuona mpelelezi aliyekuwa mtegoni. Alishangaa kuona gari lao likiondoka kwa mwendo kasi lakini kabla hajaongea chochote alisikia sauti nyuma yake ikimwambia

“Njoo uingie ndani ya gari haraka sana, hatuna muda wa kupoteza”

David Samson alihisi kuchanganyikiwa, alibabaika kama mtoto lakini hakuwa na muda wa kuendelea kushangaa. Alisogea haraka na kupata ndani ya Taxi. The White Mafia alimwambia akae kiti cha nyuma, David Samson akatekeleza. Alitamani kuuliza kitu lakini kabla hajasema chochote, The White Mafia alimwambia

“Yakupasa kukaa kimya. Lazima nifanye juu chini mpelelezi apande gari langu. Lazima aamini hili ni gari la biashara”

David Samson aliendelea kushangaa. Hakuelewa namna gari lile lilivyopatikana. Kipindi mshangao ule ukiendelea, ghafla walishuhudia windo lao likipiga hatua taratibu kusogea sehemu yenye maegesho ya Taxi za kubebea abiria. The White Mafia alitia moto gari, kisha akaanza kuondoka mahali pale taratibu. Alihesabu hatua za mpelelezi kwa ustadi wa hali ya juu, akajua atatumia sekunde ngapi kufika sehemu zenye maegesho ya magari ya abiria. The White Mafia aliongeza kasi kidogo. Hakika hesabu zake zilikuwa sahihi, sekunde tano baada ya Taxi yao kufika eneo la kuegesha magari ya abiria, mpelelezi alifika. The White Mafia alimuita mpelelezi kwa sauti ya kupiga debe

“Hi brother, where are you going? Let me take you” (Habari kaka, unaenda wapi? Nikupeleke)

Mpelelezi aligeuza shingo akatazama sauti ilipotoka, japokuwa aliitwa sehemu nyingi lakini sauti ile ilimvutia baada ya kumshangaza. Ilikuwa sauti ya kizungu kwa asilimia mia. Alimtazama na kujihakikishia alikuwa mzungu kama alivyohisi, alishangaa mzungu kwa dereva Taxi, tena mwanamke! Akaupuuza mshangao wake baada ya kukumbuka yupo jijini Cape Town, jiji lisilo chagua jinsia katika mambo ya usafirishaji. Akashawishika kupanda Taxi ya dada wa Kizungu. Kwakuwa alikuwa na begi dogo la mgongoni hakuwa na haja ya kufunguliwa buti ya gari. Aliingia garini na kutulia pembeni ya binti wa kizungu. The White Mafia alipoona mteja wake amekaa vizuri alimuuliza

“Unamjua huyo kijana aliyekaa nyuma yako?”

Ilikuwa kauli ya lugha ya Kimalosha, hakuongea kiingereza kama awali. Kitendo kile kilimshangaza sana mpelelezi. Alijikuta akigeuka nyuma haraka kumtazama kijana aliyeonesha. Hakuamini macho yake alipokutana uso kwa uso na David Samson akimtazama kwa macho yaliyojaa hofu na mashaka. Mpelelezi yule alihamaki, akaamini amenasa mtegoni. Aligeuka haraka kwa lengo la kujihami na kujilinda lakini alikuwa ameshachelewa. Bastola ilikuwa ikitazama paji la uso wake, kisha The White Mafia aliongea kwa sauti kali

“Naitwa The White Mafia, umeingia katika rada zangu”

Kipindi mpelelezi akitafakari haraka kupata njia ya kujinasua, alipigwa kwa nguvu kichwani. Akahisi nyota, alipigwa pigo lingine mahala pale pale. Akazimia. David Samson alihamaki kwa mshangao, alitaka kupiga kelele lakini kabla mdomo wake haujafunguka aliona mdomo wa bastola ukimtazama. Hakucheleweshwa, alipigwa kama alivyopigwa mpelelezi, naye fahamu zikamtoka. Akazimia. The White Mafia alikuwa mzoefu wa kazi yake, alifahamu mahali gani akupige ili upoteze fahamu. Aliwasha gari huku sura yake ikiandamwa na tabasamu, moyoni alijiona mshindi. Aliamini alikuwa njiani kutekeleza majukumu yake. Gari liliondoka kwa mwendo wa wastani, hakuwa na haraka yoyote kwa sababu alikuwa amekamilisha kazi.

(HII NI KURASA YA 300 NA KUENDELEA)

KITABU KINAPATIKANA KWA TSH 20,000 TU. WASILIANA NAMI KWA NAMBA 0758 195 890.
IMG_20220522_223131_555.jpg
 
#MATEKA

Licha ya baridi kuwa kali kwa sababu ya mvua iliyokuwa ikiendelea kunyesha, lakini bi Nadia Ali Rayan aliendelea kutokwa na jasho huku moyo wake ukimwenda mbio kama mtu aliyekimbia mashindano ya mbio ndefu. Hakuwa tayari kushuhudia mtoto wake akiangukia mikononi mwa vyombo vya usalama au magenge ya kihalifu. Mtoto wake alikuwa akisakwa usiku na mchana na vyombo vya usalama ili ashitakiwe na kuhukumiwa kwa makosa ya jinai aliyokuwa akiyafanya, vile vile alikuwa akisakwa na magenge ya kihalifu ili yamteketeze kwa usaliti na mauaji aliyokuwa akiyafanya dhidi yao. Bi Nadia Ali Rayan alikuwa tayari hata kuua kila atakayemsogelea mwanae kwa lengo la kumkamata au kumdhuru.

Japokuwa mwanae alikuwa mhalifu na alilitambua hilo lakini hakuhalalisha kifo chake. Aliamini mwanae hakuzaliwa kuwa mhalifu bali dunia ndiyo iliyoamua awe hivyo. Aliamini mwanae alikuwa akilipiza kisasi cha maisha ya nyuma aliyoyaona au kusimuliwa kuhusu familia yake. Kumbukumbu za bi Nadia Ali Rayan zilisafiri miaka mingi iliyopita, akakumbuka kifo cha mume wake kilichosababisha atengeneze taswira mpya ya maisha yake, ilikuwa kumbukumbu mbaya sana ambayo kila anapoikumbuka huhisi kumwaga damu za maadui zake. Ni heri mume wake angeugua akamuuguza mpaka akafariki kuliko kilichotokea. Mume wake aliuliwa mchana kweupe. Bi Nadia Ali Rayan aliamini kwa asilimia mia moja kuwa magenge ya wauza madawa ya kulevya yaliyokuwa yakishirikiana na mume wake ndiyo yaliyosababisha kifo hicho. Uchunguzi wa kifo cha mume wake ulifichwa fichwa, ukapakwa mafuta mpaka ushahidi ukakosekana.

Miaka ilisogea, bi Nadiya Ali Rayan akapotezana na familia yake iliyobaki. Hata hivyo mtoto wa bi Nadiya Ali Rayan alikuwa akiishi chini ya kivuli cha mama yake pasipo yeye mwenyewe kujua, alijua alikuwa akipambana na wahalifu waliomuua baba yake kwa nguvu zake mwenyewe, kumbe nguvu za mama yake zilihusika kwa asilimia kubwa kwa kila hatua na tukio alilokuwa akilifanya. Siku hiyo mtoto aliangukia mikononi mwa mama yake baada ya dunia nzima kumuangukia ikihitaji kuondoa maisha yake, na siku hiyo hiyo ndiyo alibaini ukweli kuhusu mama yake mzazi. Ukweli kuwa mama yake alikuwa hai na alikuwa akimiliki genge kubwa la kigaidi lililokuwa likiendelea kufanya kazi za kigaidi nyuma yake pasipo yeye mwenyewe kujua. Bi Nadiya Ali Rayan alimtazama kwa huzuni mwanae aliyekuwa kitandani akiipigania roho yake baada ya kujeruhiwa vibaya kwa kitako cha bastola alichopigwa usiku uliopita. Walikuwa wameshaongea mara chache lakini mara chache hizo hawakufikiana muafaka mzuri kutokana na hali ya mtoto wake. Chozi lilimtoka kisha sauti nyembamba toka moyoni kupitia mdomoni mwake ikasikika

“Kuanzia siku uliyotoweka mikononi mwangu nilikupatia jina la Aqsa, sitaki kukuita jina lako la zamani kwa sababu sio kitu tena mbele yangu. Kwa sasa, Jina Aqsa linafahamika nchi nzima lakini hata wewe ufahamu kama ni jina lako”

Japokuwa mwanae alikuwa hoi kitandani lakini aliisikia vizuri kauli ya mama yake, alifumbua macho na kumtazama mama yake aliyekuwa ametengeneza mifereji ya machozi usoni mwake. Mtoto akalazimisha kutabasamu lakini mbavu zake zikamsaliti, mbavu zilimuuma sana. Tabasamu likaishia njiani. Akafungua mdomo wake na kuongea huku akimtazama mama yake usoni

“Sasa leo hii nimemfahamu Aqsa ni nani? Nilikuwa sijui chochote kuhusu neno Aqsa…sasa nimetambua nastahili kuitwa Aqsa”

Akakohoa kikohozi kikavu kilichosababisha afumbe macho kwa maumivu aliyoyasikia, kisha akaendelea kuongea na mama yake

“Lazima nimalize kazi niliyoianza mama, lazima niwasambaratishe wote watakaojaribu kunizuia…nashukuru kwa jina jipya mama. Sasa naitwa Aqsa, jina toka kwa mama yangu niliyempoteza miaka mingi. Asante mama”

Huzuni iliyokuwa imetawala sura ya bi Nadiya Ali Rayan ilianza kupotea taratibu baada ya kusikia mtoto wake akimuita ‘mama’, ilikuwa imepita miaka mingi pasipo kusikia akiitwa namna hiyo. Vile vile alifurahishwa zaidi na kauli kutoka kwa mtoto wake, kauli iliyojaa ujasiri wa kupambana. Kauli iliyokosa chembe ya hofu japokuwa alikuwa kitandani akiugulia maumivu makali yaliyosababishwa na harakati za mapambano yake. Ndivyo alivyohitaji bi Nadiya Ali Rayan. Mtoto jasiri kwake ndiyo mtoto. Suala la mtoto wake kuongelea jina lake jipya hakulipa nafasi ya kuanza kulijadili. Hakutaka maongezi marefu kuhusu mada hiyo, alichotaka ni mtoto wake kufahamu kuwa jina la Aqsa ni jina lake na siyo vinginevyo. Lilikuwa jina zuri sana kwa upande wake kwa sababu jina hilo lenye asili ya Kiarabu lilikuwa na maana ya ‘mwenye akili’ au ‘intelligent’ kwa watu wa mataifa ya magharibi.

Japokuwa lilikuwa jina lenye maana nzuri lakini jina hilo lilikuwa na sifa mbaya sana katika taifa hilo, lilikuwa ni miongoni mwa majina yaliyokuwa yakitafutwa usiku na mchana kwa lengo la kudhibitiwa na mamlaka zenye dola lakini ilishindikana. Hakuna aliyekuwa na ushahidi wa kumfahamu Aqsa, japokuwa wapelelezi waliendelea kuwatilia mashaka baadhi ya watu. Akili ya mama na mtoto iliamini kuendelea kufanya mauaji kila inapowezekana, wao waliamini mauaji watakayofanya dhidi ya maadui zao yatakuwa faraja kwa wapendwa wao waliouliwa kinyama miaka mingi iliyopita. Walinuka roho ya visasi na waliamini hakuna mtu au idara itayoweza kuwazuia kutimiza azma yao. Waliimba mauaji.

HIZI NI KURASA MBILI ZA MWANZO

KITABU KIPO SOKONI KWA TSH 20,000. TUNATUMA KILA MKOA. WASILIANA NAMI KWA NAMBA 0758 195 890 KUPATA NAKALA YAKO.
20220527_082520.jpg
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom