Riwaya: Machinga mimi Masikini

Logikos

JF-Expert Member
Feb 26, 2014
12,513
19,569
Utangulizi
Maisha matamu sana, haya ni maneno ambayo nisingeweza kuyatamka miaka ishirini iliyopita, sikujua cha maisha wala uzuri…, na si mimi tu wengi tulikuwa kwenye dhahama hizo…

Nasogea kwenye bustani na kuketi napigwa na upepo mzuri naona wanafamilia wakitembea kutoka makwao kuelekea sokoni kwa ajili ya matumizi yao… kwa mbele kidogo naona vijana wanasubiri usafiri (kuna basi la umeme linapita kila baada ya dakika tano) ili waelekee sehemu ya uzalishaji kujipatia kipato chao…, ingawa ni saa kumi na mbili jioni lakini katika huu mji uzalishaji hufanyika kwa masaa 24.

Naangalia kwa mbali nyumba yangu ninayoishi, sio mimi tu kila mkazi wa hapa anayo makazi, majengo ya nyumba ni ghorofa nne zenye nyumba nne kwenye kila ghorofa yaani jumla nyumba 12 kwa kila jengo.

Nyumba na mazingira ni masafi…, lazima yawe masafi ukizingatia kuna watu wa kufanya usafi na kwa kufanya hivyo wanajipatia kipato… Hizi nyumba (apartment blocks) kwa haraka haraka unaweza kudhani ni makazi ya watu pekee, lakini ukiangalia kwa karibu ni viwanda!!! Kwenye kila jengo kwa juu kuna solar panels zinazokusanya nishati ya jua, kila tone la mvua ikinyesha pia linakusanywa na kuhifadhiwa kwa matumizi, vyoo vyote vya nyumba zote vimeunganishwa na uchafu wake unapelekwa sehemu unahifadhiwa kwa muda na baadae unatumika kama mbolea kwa mazao yasiyo ya chakula yaliyopo huko nje ya huu mji ambao umezungukwa na miti ya misitu.

Kila nyumba ina sehemu za kutupia uchafu tofauti tofauti baada ya matumizi, wasafishaji hupitia huu uchafu na mabaki ambayo mwisho wa siku hutumika tena kutengenezea bidhaa nyingine yaani kwa ufupi kila uchafu wa kitu kimoja ni malighafi ya kingine.

Maji ya kuoga na kusafishia vyombo na nguo nayo hayapotei bure ndio haya yanamwagilizia hizi bustani na haya maua ambayo yananiburudisha hapa nikiwa nimepumzika… Aahh Maisha Matamu sana.

Kwa mbali naona migahawa ya kutosha nikitoka hapa niende nikajipatie mlo wangu, sina tatizo wala woga wa kulala njaa au kukosa milo mitatu nina bili ya chakula bora kwa mwezi mzima…, aahh huenda ukasema sasa si ni gharama kwanini usipike mwenyewe lakini utagundua kwamba gharama ya kula nje ni ndogo kuliko hata kujipikia…

Ninachukua simu yangu na kuangalia ukurasa wa kazi kwa mwezi huu ili niweze kupata kipato changu cha dola 600 nilitakiwa nifanye kazi kama masaa 30 tu kwa mwezi yaani kama lisaa limoja kwa siku, ila mimi niliamua kufanya kwa wiki sasa nimepumzika. Nina wiki kama mbili za kupumzika mke wangu yeye nadhani ameamua kufanya kidogo kidogo.

Watoto wangu wawili wote wapo Chuo baada ya kumaliza Sekondari ambapo walisoma na kupata elimu ya vitendo, ingawa elimu sio bure lakini gharama zote zinatoka kwenye kipato changu na mke wangu. Nina nyumba ambayo tumekuwa tukiilipia kutoka kwenye vipato vyetu. Nimeshamaliza mkopo wa hiyo nyumba ambao haukuwa na riba. Nadhani baada ya miaka mitano nitastaafu, mafao yangu ya uzeeni yatanipatia stahiki zangu zote za kuweza kuishi, na nyumba ambayo tumeshailipia tukiamua mimi na mwenza wangu tunaweza kuiweka sokoni ili jiji liweze kuinunua sababu nitakuwa na uamuzi wa kuhamia kwenye nyumba za wazee wanzangu ambapo kuna uangalizi mzuri zaidi.

Naangalia watoto wakiwa kwenye baiskeli zao wanaendesha huku wakifukuzana kwa furaha… kwa mgeni wa huu mji anaweza kushangaa kwa kutokuona magari wala parking nje ya nyumba zaidi ya vituo vya mabasi!!! Sio kwamba hakuna magari kwenye huu mji bali magari yote yanapaki nje ya mji yaani parking zipo nje na hayaruhusiwi kuingia ndani kuepusha msongamano. Hapa mjini barabara ni za watembea kwa miguu, waendesha baiskeli na mabasi ya jamii.

Ukizingatia huu mji wa watu takribani elfu 50 wenye nyumba za makazi 833 na familia 10,000. Umbali wa kutoka kwenye nyumba ya mbali kabisa mpaka katikatika ya mji ni mwendo wa kutembea au kuendesha baiskeli basi utaona hakuna haja ya kutegemea usafiri binafsi wa gari, ukizingatia mabasi yanapita kwenye barabara nje ya kila nyumba kila baada ya dakika tano…. Kweli Maisha ni Matamu Sana…

Sio kwamba kwa wapenda magari hawana wala hawawezi kupata, bali kwenye sehemu ya kutokea na kuingilia mjini kuna parking ya magari kila mgeni au mwenye gari huyapaki huko na sio kuingia nayo mjini, vilevile kuna mpango wa kukodi magari. unachagua gari lolote unalotaka na unaweza kulikodi na kulitumia iwe kwa masaa, siku miezi au muda wowote ule na Jiji ndio linahakikisha ufanyaji kazi na ufanisi wa hilo gari.

Natembea polepole kuelekea kujipatia mlo wa jioni, nilishapiga simu nadhani leo natuchukua take away nikalie nyumbani au sijui nimpigie mke wangu na watoto tukutane huko huko tukapate chakula..., ngoja nitawauliza tufanye maamuzi.

Nadhani hapa unaweza ukashangaa iweje Machinja mimi Masikini naongelea utajiri huu mkubwa wa kwangu na jamii yote hii inayonizunguka ?

Kupata majibu inabidi nirudi nyuma miaka kadhaa, nikikumbuka kweli nilikuwa nimekata tamaa! Nilikuwa Machinga Masikini katika lindi la masikini wenzangu, Nilikuwa sina kipato cha uhakika, nafukuzwa kila kona, sina makazi wala malazi, bila mafao ya uzeeni sikujua nikizeeka nigekuwa mgeni wa nani, nguvu zangu ndio zilikuwa mtaji wangu na lishe yangu duni ilikuwa ni suala la muda tu kabla hata nguvu hazijanitupa mkono.

Itaendelea...

Get Your Free Copy
1687092882069.png
 
Machinga Mimi Masikini

Maisha gani haya…, kweli nimepitia mengi hapo mwanzo nilikuwa natembeza hizi bidhaa duka kwa duka, mtu kwa mtu yaani mtu unachomwa jua, unatoka jasho linakaushwa na hilo jua mpaka unaanza kutengeneza chembe chembe za chumvi kwenye ngozi, hali ilikuwa mbaya kipindi hicho…, nakumbuka kutokana na ukata bwana mdogo mmoja alikuwa anauza maji anapata kiu kutokana na shida anashindwa hata kunywa maji yake mwenyewe kwa kuogopa kukata mtaji wake wa kuunga unga.

Walikuwepo wataalamu wa hii kazi, unajua kila kazi ina kanuni zake na hakuna biashara mbaya kwa kila mtu, kuna jamaa mmoja enzi hizo alikuwa anauza mitumba, yeye ni kutembelea watu maofisini na begi lake lenye nguo chache alizochagua, ukimuona yeye mwenyewe alivyo mtanashati wakati mwingine wateja hadi wananunua nguo alizovaa, kwamba mkuu niachie hio uliyovaa niletee kesho. Jamaa alikuwa hatari leo akimuuzia mtu shati anarudi wiki kesho na suruali inayoendana na lile shati.., “Kaka unakumbuka lile shati na vile viatu nilivyokuuzia ?, basi vinaendana na hii suruali…” ilikuwa ni burudani ukimuona akiwa kazini.

Ila hata huyo Jamaa yangu nilikutana nae juzi anasema hali sio shwari, biashara imeingiliwa kuna wadau wengi wanafanya kile alichokuwa anafanya yeye, yaani hata huko maofisini wanauziana wenyewe kwa wenyewe, watoa huduma wamekuwa wengi kuliko wahitaji.

Tumbo linaunguruma jana usiku sikula chochote nililala baada ya kubugia maji ya bomba, hii hali imezidi kujirudia tangu nimshauri mke wangu na watoto wetu wawili waende kumtembelea mama yake kijijini huu mwezi wa tano sasa…., kila nikipokea simu ya mama mkwe ni shutuma na kulalamikiwa, ila siwezi kuwalaumu sababu ni majukumu yangu nimehamishia kwao.

Mambo lazima yabadilike…, haya sio Maisha na hii njaa leo siwezi kulala tena njaa unaweza ukadhani unabana matumizi kwa kujinyima lakini kumbe unatengeneza magonjwa ya kukufanya usiingie kazini kwa muda, na sisi tunaoishi kwa kupata na kutumia ukiugua siku moja tu unaweza kujikuta umetoka barabarani.

Nawaza wapi sina deni angalau niende nikope sahani moja ya ugali na maharage ninywe na maji siku iende. Mpaka dakika hii sijauza kitu zaidi ya kuambulia vumbi tupu na nikiangalia kushoto na kulia wauzaji wote tunauza vitu vilevile. Sioni ni nani ananufaika na huu mpangilio, wanunuzi wanatuona sisi wachafua miji ingawa hawajui kwa namna moja au nyingine tunachangia uchumi.

Ingawa Rafiki yangu mmoja asingekubaliana na hayo nisemayo, unachangia uchumi wa nani?, bidhaa zote unazoziuza zimetoka ughaibuni, na usingeziuza wewe mchuuzi…, mteja angezifuata dukani…, Kwani si nikiuza akinipa pesa si na mimi nanunua chakula kwa mama lishe au mchicha kwa mkulima ? Kijana acha kuwa na upeo mfupi badala ya kuchuuza ungekuwa mzalishaji unalima huo mchicha huenda ungemnufaisha mama lishe kwa kumpa bidhaa na kuwalisha wote hata hao wanakuona wewe ni mchafua mji… Mara nyingi sikupenda kubishana nae huyu bwana ila kwa kuangalia mwenendo wa haya maisha naanza kujiuliza, sisi kama nguvu kazi ya hili taifa tunatumika vema kweli ? Hiki tunachofanya kwa kuchomwa jua asubuhi mpaka jioni kuna tija ya muda mrefu au ni kuhahirisha matatizo tu.

Sijui leo nikamkope nani ambapo sina deni kubwa Mama Aisha au Ashura? Ingawa najua kabisa kwa kukaa na madeni ya hawa wabangaizaji wenzangu ni kuwaangusha kibiashara, lakini nitafanyaje, najipa moyo ngoja nile leo nipate nguvu huenda kesho nikabahatisha na kuweza kuwalipa wahanga wenzangu na sio kuwadumbukiza kwenye lindi la matatizo.

Ghafla naona vurugu kwa mbali na karandinga limepaki!!, naona wachuuzi wenzangu wanachukua vitu vyao na kutoka mbio…., vipi tena namuuliza mwenzangu wa karibu, si walituruhusu kukaa hapa mbona tena tunafukuzana kama wakimbizi ? , “Hivi wewe jamaa tangia uuze TV yako hata redio hausikilizi? Haukusikia matangazo kuwa inabidi tuondoke hapa kupisha ujenzi wa upanuzi wa barabara ?

Nanyanyuka kwa kasi na kukusanya vichache vilivyopo ila kwa hii njaa niliyonayo naanguka na kuteleza jambo la mwisho kuona ni giza nene huku nikihisi kukanyagwa na wenzangu waliokuwa wanajitahidi kuokoa mitaji yao isikumbwe na kusanya kusanya ya mgambo.
 
Ng'ombe wa Masikini Hazai
Nafumbua macho najiona nipo hospitalini nimelazwa, pembeni namuona mke wangu akiwa amejiinamia analia…, baada ya kuona nimezinduka anajitahidi kutoa tabasamu, ingawa naona kabisa kuwa ni tabasamu la kulazimisha… anaonyesha uchovu wa hali ya juu.

Naanza kujilaumu kwa ujinga niliofanya mpaka kujikuta hapa, najua kabisa hatuna Bima sasa hizi gharama analipa nani, ila isiwe tabu kuna shamba la urithi kijijini ambalo niliachiwa na Babu naweza kuliweka rehani kulipia haya matibabu…, ingawa ningejua kilichokwishatokea wakati nawaza hayo nadhani ningekufa kwa mshituko.

Kwa ufupi pale nilipokuwa wakati nazinduka nilikuwa sina kijiji wala shamba na mke wangu pia alilazimika kuuza kiasi cha shamba la mama yake ambaye alimshauri na kumsihi afanye hivyo, eti hakuna jambo lenye gharama kuliko Maisha ya binadamu….

Niliendelea kuugua pale kama mwezi mzima, kwa ufupi nilivyopona nikahadithiwa kilichotokea…, baada ya kupoteza fahamu nilipelekwa hospitali nikalazwa, machinga wenzangu walijitahidi kunichangia hapa na pale ila huduma kubwa za hospitalini na kukosa kwangu Bima hawakuweza kuzimudu, mama yangu mzazi kijijini baada ya kupata habari za ugonjwa wangu mjini alianza kukopa huku na huko na kutuma pesa ambazo mwisho wa siku zilikwisha, mke wangu pia ambaye aliitwa aje kuniuguza akawa anatumiwa pesa na mama yake toka kijijini kwao mpaka kupelekea kuuza nusu ya shamba lao. Ama kweli nilianza kujiona kama mzigo na nisijue ni vipi talipa fadhila za kuingiza familia hizi mbili katika lindi la umasikini wa kutupwa.

Niliambiwa baada ya matibabu ya wiki tatu bila kupata fahamu wala kujitambua ilihitajika pesa zaidi…, mama kijijini madeni yamemzidi hana la kufanya, ingawa mke wangu aliwasihi washirika waliokuwepo pale wasimpe taarifa mama kijijini na wamfiche ili isije kumletea matatizo na pressure za uzeeni. Lakini baada ya kuona kimya na kuhisi anadanganywa aliamua kufunga safari na kuja mpaka mjini, kwa hali aliyonikuta nayo hakusubiri wala kuaga akafunga safari kurudi kijijini, alichokifanya baada ya kufika ni kuuza kila kilichokuwepo akapata pesa kidogo ili aweze kurudi mjini kuniuguza. Wakati akiwa njiani kwenye basi anarudi mjini vibaka wakamuibia mizigo yake yote pamoja na pesa. Mama kwa kupata mshituko huo akaaga dunia.

Siku ninaamka toka kwenye kupoteza fahamu ilikuwa ni siku tatu tangu mke wangu atoke kumzika mama yangu kijijini.

Hayo yote niliambiwa siku nimeruhusiwa kutoka hospitali. Niligundua ghafla kwamba sina Kijiji wala pa kukimbilia, pia nilisikia kwamba wajomba zangu hawataki hata kuniona wakinishutumu nimemuua dada yao yaani mama yangu.

Sina Kijiji wala pa kukimbilia na zaidi ya hayo nimemuweka mke wangu katika matatizo ya kuwatia hasara ndugu zake na mama yake kwa kuuza nusu la shamba lao ili wanihudumie hospitalini. Haya nilikuwa nikiyawaza huku nikiwa nimehifadhiwa kwenye chumba cha kupanga anachopanga Rafiki yangu ingawa yeye alikuwa na vyumba viwili tu vya kupanga alituhifadhi mimi na mke wangu kwenye chumba chake cha ziada, watoto walikuwa kwa bibi yao. Niliambiwa baada ya kuugua mwenye nyumba baada ya kuona kuna dalili ya mimi kutorudi aliamua kumpangisha mtu mwingine chumba changu ukizingatia nilikuwa nina deni la miezi ya kutosha sikuweza kumlaumu.

Mke wangu alikuwa anatoka asubuhi kwenda kumsaidia mke wa Rafiki yangu kuuza maandazi na chai mtaani. Rafiki yangu yeye alikuwa anauza mitumba na viatu huko mjini hata wao hali zao zilikuwa ni za kuunga unga bila uhakika wa leo wala kesho.

Kwakweli mda wa siku mbili ambao nilikaa nyumbani kwa Rafiki yangu niliwaza na kuwazua mengi sana, ila jambo ambalo nilikuwa na uhakika nalo ni hali haiwezi kuendelea kama ilivyo. Na ni ukweli usiopingika mimi kama mimi pekee nisingiweza kutuondosha au kujiondosha kwenye huu mtego wa umasikini ila kwa kuchangia nguvu na masikini wenzangu tunao uwezo wa kutoka katika Maisha ya kubangaiza.

Swali lilikuwa tunaanzia wapi, na je wenzangu watanielewa. Mchana huo nikatoka hadi mtaani walipokuwepo mke wangu na mke wa Rafiki yangu nikawaeleza kuwa kuna jambo leo jioni ningependa kuwahusisha, baada ya hapo nikaelekea kwa Rafiki yangu mjini anapouzia mitumba, nilipofika huko niligundua hata yeye hali sio shwari, mizigo aliyokuwa amebaki nayo kwa kweli haikuwa na ubora na inavyoonekana ingawa alikuwa ananificha, alikuwa hana pesa ya kuongezea mzigo. Alijikuta amegeuka kuwa kama dalali, anachukua baadhi ya vitu mfano viatu anachukua mguu mmoja kutoka kwa Rafiki zake ili angalau mtu akinunua aambulie hata pesa ya mkate wa kila siku.

Namuona Tatu muuza chai kwa mbali…, nahisi huyu ananidai chai maharage niliyokula najihisi vibaya sana sina uwezo wa kumlipa, ananisogelea na kunipa pole na yaliyonipata...,” Asante Nashukuru…, Tatu sio kwamba nimesahau najua unanidai, tajitahidi kukulipa”

“Aahh yote maisha kaka tuombe uzima tu”.

“Vipi Biashara “, namuuliza… Ahh kaka hakuna mzunguko yaani hapa nimeuza kikombe kimoja tu kuna hatari ya hii chai kulala, nikiendelea hivi lazima takata mtaji, yaani sijui takuwa mgeni wa nani na watoto wanafukuzwa shule sijapata pesa za karo.

Natingisha kichwa kwa masikitiko..., lazima kuna mbadala wa hii hali haya sio maisha ya binadamu kuishi, kukosa kwangu kwa Bima na uhakika wa kesho yangu umemfanya mama apoteze maisha, umewadumbukiza wazazi wa mke wangu katika dimbwi la umasikini na kwa kutokuwalipa watu kama kina Tatu nimewapunguzia mtaji wao, bila kusahau mzigo ninaompa rafiki yangu na mke wake kwa kutuhifadhi

Vipi kaka naona upo vizuri…, angalia bana usije kuingia mtaani mapema kabla mwili haujakaa vema, aliniambia rafiki yangu. Kaka nitakaa mpaka lini ?, binafsi sina anasa hiyo kila siku ninavyokaa bure ndio nazidi kudumbukia kwenye shimo ambalo ni vigumu kutoka, Na hapa nimekuja ndugu yangu tushauriane jinsi ya kuodoka kwenye hili lindi la umasiini.

Rafiki yangu kwa jina Huruma aliniangalia kwa upole na majonzi…,kwa upole akaniambia, “Kaka unajua kabisa mimi na shughuli za kuvunja sheria ni mbali mbali, tamaa mbaya kaka tunaweza kujikuta tunaozea jela, sasa sijui mke wangu, wako na watoto wako watakuwa wageni wa nani.

Kaka hivi unadhani kwa yote niliyopitia na shida nilizomweka mke wangu naweza kujitumbukiza kwenye hatari kama hio ? Hapana kaka naongelea mbinu za kujikomboa mimi, wewe wake zetu , ndugu zetu na jamii yote inayotuzunguka sio sisi tu na hawa wabangaizaji wote hapa waliotuzunguka.

Huruma akaniangalia kwa muda mrefu sana…, nadhani alikuwa anawaza labda nimepata maradhi fulani kichwani kutokana ma masahibu yaliyonikuta…, mwishowe akasema Kaka unataka kuingia kwenye siasa nini? sababu huko ndio unaweza kutoka kwenye hili lindi la umasikini na wala sio kututoa sisi bali kujitoa mwenyewe lakini kwa bahati mbaya bila pesa sidhani kama utafanikiwa…, mkono mtupu haulambwi ndugu yangu.

Kaka nimewaza hili kwa marefu na mapana kwenye haya matatizo umoja ni nguvu na ni aidha wote tupona kwa umoja au tutakufa mmoja mmoja hakuna njia nyingine

Kaka upo sawa kweli ?, mbona unanitisha ?

Jioni kaka nitakuwa na mengi ya kuwaambia naomba masikio yako mkewe na mke wangu, kwanza niwaambie nyie kabla ya kuwahusisha na wengine.

Kutwambia nini ?

Jinsi ya kutokomeza Umasikini Wetu?

Nini ?
 
Mzee wa Busara

Naondoka kutoka kwa Rafiki yangu naona ngoja nizunguke zunguke kupoteza mawazo, ingawa najua ni hatari na aibu takutana na wanaonidai... ila tafanya nini bora nianze kuzalisha na kuwalipa kidogo kidogo kuliko kuendelea kuhahirisha tatizo.

Sijui cha kufanya, takimbilia wapi, tafanya nini Maisha yangu yote nilikuwa najichanga ili mwisho wa siku nikimbilie kijijini na familia yangu, hilo sasa ni historia, sina pa kwenda wala kukimbilia.

Inabidi sisi machinga tuwe wamoja, inabidi tupate misaada, inabidi tuwezeshwe, tupate mikopo isiyoumiza inabidi na sisi tuwe kama wananchi huru katika nchi yetu…,

Samahani Mzee….!!! Katika lindi la mawazo yangu nilijikuta natembea bila kuangalia mbele na kujikuta nimemkanyaga mzee mmoja wa makamo…, hii sio sura ngeni kwangu huwa namuona ona anatembea tembea hapa na pale hakuna ajuaye alitokea wapi wala anafanya nini alikuwa mzee wa umri kama miaka 70, mvi zimejaa mpaka kwenye nyusi, sura ya makunyanzi na muda wote alikuwa akionekana kama mtu mwenye fikra sana…

Usihofu kijana wangu…, pamoja na kwamba huyu bwana nilikuwa namuona kila siku kwa muda kama wa miaka miwili hii ndio ilikuwa mara ya kwanza kusikia sauti yake na kusemeshwa nae, wengine walikuwa wanamuogopa labda ni mchawi au usalama wa taifa, au alitelekezwa na ndugu zake, au alikuwa mwizi, sababu ingawa hakuna aliyejua anafanya nini ila alionekana ameshiba, na nguo zake ingawa hazikuwa za gharama (kanzu, kibaraghashee na kandambili) lakini vilikuwa nadhifu na visafi.

Mbona unaonekana unatazama bila kuona, vipi unawaza nini?

Mzee sifurahishwi na hali iliyopo, nimechoka kuishi Maisha ya kubangaiza, hapa sina mtaji… mke watoto wananitegemea, nikienda benki siwezi pata mkopo, taishi vipi mimi, nikisema nifanye uharifu tafia gerezani.

Unasema mkopo?

Ndio Mzee…..

Ili uchukue nini au ufanye nini ?

Bidhaa mbona nyingi mzee?

Naam najua bidhaa ni nyingi si unaona umati huu wote wana bidhaa?

Unamaanisha?

Unaona yule kijana pale mchonga vinyago…, kweli ana kipaji na anafanya anachokipenda…, anatumia muda mwingi kutengeneza kinyago chake ila bei anayouza haikidhi mahitaji yake, Nina uhakika ingawa wewe ni mpenda vinyango, ila unaishia kuangalia tu kwa macho sababu hauna uwezo wa kununua…, sasa huyu akipewa pesa itasaidia…

Ndio Mzee itasaidia kununulia vifaa na…

Kasema hana vifaa ? huoni kwamba msaada zaidi kwake ni kama angekuwa amezungukwa na watu wenye kipato na uwezo wa kununua…

Unamaanisha masoko ?

Ndio masoko, ila masoko hayo yatatoka wapi iwapo watu hata mkate wa kila siku unawashinda kupata, kweli watanunua vinyango?, alisema mzee wa Busara kwa masikitiko…, au mpaka tungojee watalii wakija ndio huyu bwana apate faida ya jasho lake, yaani uhai wetu unategemea hisani ya mtu wa magharibi ya mbali…

Niliwaza kwamba ni kweli hata Ashura tukisema apewe mtaji labda akafungua mgahawa je wateja wake watabadilika au tutakuwa kina sisi…, na hata Ashura akitoka kwenye huu ubangaizaji itakuwa bora kwake ila tutawasaidia kina Ashura wangapi iwapo hata Mangi ni mwaka juzi tu kafunga mgahawa wake kwa kukosa wateja. Hivi anachohitaji Ashura ni kuboresha huduma au kupata wateja? sababu hapo mwanzo alikuwa mpaka anaishiwa chai na vitafunio kwa huduma hii hii wala hajaibadilisha!!!

Aliendelea Mzee Busara…., sifurahishwi na ninachokiona ingawa bidhaa zipo hakuna wanunuzi, nguvu kazi inapotea bure, kuna wasamaria wema huwa wanajitahidi kutoa kamsaada hapa na pale ila misaada hiyo haitatui tatizo, ni kama inawasaidia hawa masikini kuendelea kuwa masikini…

Kwahio mzee wangu hukubaliani na kazi nzuri wanazofanya hawa wahisani kusaidia watu?!! Niliuliza kwa hasira.

Unadhani hata kama ingewezekana, ingawa haiwezekani kuwapa watu wote hawa pesa ingesaidia? aliuliza Mzee Busara.

Naam, shida ya hawa wengi ni mitaji na… na….

Hata kama kungekuwa na uwezo wa kuwapa masikini wote pesa isingesaidia… kwa Maisha haya wanayoishi wengi wangecheza kamari ili kufikia ndoto zao ambazo hazifikiki au wengine wangetumia vilevi ili kujisahaulisha matatizo yao…, alisema Mzee Busara

Sikuelewi Mzee!!! nilimjibu kwa hasira.

Mtu pekee wa kumsaidia masikini ni masikini mwenyewe, na kwa masikini kumtegemea mwenye nacho ili amuondoe katika lindi la umasikini ni kama muwindwa kutegemea hisani ya muwindaji ili amsaidie kwenye maisha yake. Kwenye dunia ya leo ya ushindani ni vigumu kwa aliyenacho kumsaidia asiyenacho ili na yeye awe kama yeye…

Unamaanisha nini Mzee mbona kama unazungukazunguka?

Ni vigumu mwenye nyumba kumsaidia mpangaji ajenge nyumba yake, hata wachache wakifanya hivyo, ni kwa sababu wanajua wapangaji ni wengi, akitoka huyu kesho atakuja yule…, ila kwa mawazo hayo ni vigumu kutegemea mtu mwenye fikra hizo kusaidia kutokomeza umasikini sababu anaona ni jambo la kawaida na ni lazima kuishi nalo, yaani wasionacho lazima wawepo na wataendelea kuwepo.

Lakini mzee ni kweli, wote hatuwezi kuwa sawa, watu tunatofautiana… Wachache wakianzisha viwanda hata sisi huku chini tutafaidika na ajira, bidhaa na... na…

Kijana ulimwengu wa sasa wa mashine yaani sayansi na teknolojia hauhitaji nguvu kazi kama zamani, ili kiwanda kiweze kutoa bidhaa zenye ushindani katika soko lazima zipunguze gharama za uzalishaji na moja ya hizo gharama ni kutumia mashine na teknolojia na sio kuajiri watu wengi…

Kwahio ni kwamba hakuna cha kufanya, yaani tukate tamaa na kungojea kifo…, au kila mtu ajitahidi kutoka kivyake kwa kuwakanyaga na kuwakandamiza wengine? Nilijibu kwa dhihaka.

Hapana Kijana, Umasikini wowote kwa yoyote ni hatari kwa wote popote…, yaani wewe uliyenacho ukizungukwa na wasionacho muda wowote watakuja kuchukua kilicho chako.

Aliendelea mzee kuzungumza taratibu na kwa masikitiko…, ila nakubaliana na wewe, wote hatuwezi kuwa sawa, ingawa sidhani tunapoongelea usawa, tunaongelea kitu kimoja.

Mzee sikuelewi!!

Wakati wewe unaongelea utofauti wa matabaka (walionacho na wasionacho), utofauti niuonao mimi ni kwenye ujuzi na uwezo…. Hivyo basi kwangu mimi utofauti huo ndio unaofanya kikundi au jamii ya watu kuwa yenye nguvu na sio sababu ya kutengeneza matabaka.

Mzee Sikuelewi!!

Umesema wote hatuwezi kuwa sawa…, nadhani umesema hivi kwa sababu watu tuna uwezo tofauti, lakini mimi naona utofauti huo wa uwezo ni faida na sio mapungufu.

Mzee unazidi kunichanganya!!!

Kama mwili ulivyo na viungo mbalimbali ili uweze kufanya kazi au mkono ulivyo na vidole vyenye urefu na umbo tofauti ili tuweze kushika vitu vizuri…

Mzee kuna cha maana chochote unachotaka kumaanisha zaidi ya kunichanganya

Maana yangu ni kwamba tukiunda timu ya mpira yenye kina Pele 11, au Ronaldo au Maradona au Messi haiwezi kuwa timu bora, timu bora inahitaji golikipa, walinzi na watu wanaojituma sio wenye vipaji pekee…., hivyo basi hata kwenye jamii tuna watu tofauti wenye nguvu tofauti, wengine ni wabunifu, wengine wana maono na wengine wanaweza wakabadilisha nadharia kuwa uhalisia…, mmoja mmoja hatuwezi kufika popote ila kwa umoja wetu hakuna cha kutuzuia.

Na kama nilivyosema awali, kwavile hakuna wa kutusaidia au kukusaidia ni aidha tunaishi kwa umoja au tunakufa mmoja mmoja… hakuna mbadala…., alimalizia mzee huku machozi yakimlengalenga.

Mzee tunahitaji msaada ili kuondokana na hii hali nilisema kwa msisitizo huu sio muda wa kukata tamaa

Msaada kutoka kwa nani?

Serikali!!!

Ili ikufanyie nini? Aliuliza mzee kwa hasira…, tofauti kati ya walionacho na hawa ombaomba ni fursa ya kujipatia kipato cha uhakika…, watu wakiwa na kipato cha uhakika watamudu mahitaji yao yote bila kutegemea au kusubiri hisani ya Fulani wala serikali.

Sasa mzee naona tunazunguka… nilimjibu kwa hasira…, sasa si tukiwezeshwa tutafanya biashara na kupata hicho kipato…

Cha uhakika ? Aliuliza Mzee

Unasema?

Kwanza unawezeshwa vipi, na nani anawezeshwa na nani?, na kama ni mkopo una uhakika wa unachokifanya kwamba utalipa huo mkopo au ni kudumbukizana kwenye lindi la matatizo juu ya matatizo. Alisema mzee kwa hasira.

Wewe mpaka leo umeshakopa mikopo mingapi kutoka Saccos, Vicoba n.k. Aliendelea Busara…., unaweza ukasema labda ilikuwa ni mikopo ya kuumiza, ila hata ungepewa pesa bure kwa shughuli hizi za kubahatisha una uhakika huo mtaji hautakatika ? Hata kama wawili katika kumi wakifanikiwa…, kweli kwa marejesho hayo tunaweza kusema kama jamii tunafanikiwa. Hivi wewe na marafiki zako wote, hata wale wachache wenye bahati za ajira za uhakika baada ya kulipia kodi, elimu kwa watoto wao na chakula ni wangapi wanabaki na akiba au wengi wao ni kukopa mwezi kesho kulipia madeni ya mwezi huu… aliendelea kusema mzee kwa hasira.

Kwahio mzee ni nani wa kutukomboa naona kama vile unazidi kunikatisha tamaa…

Hakuna wa kuwakumboa sio wewe, serikali au mtu binafsi yoyote.

Unasema ?!!

Hakuna mtu mmoja mwenye uwezo wa kuwakomboa bali nyie masikini wenyewe ndio wa kujikomboa kwa kutumia nguvu ya wingi wenu…

Mzee sikuelewi nilisema kwa hasira!!!

Hivi wazalishaji ni kina nani? aliuliza Mzee

Viwanda, Matajiri, Wamiliki na Mataifa ya mbali nilijibu…

Ambao ni WATU alisema Mzee Busara kwa kusisitiza wazalishaji wote, wakulima wafanyakazi, wabunifu waliotengeneza hizo mashine… wote ni WATU…. Na watumiaji? aliendelea kuuliza

Ni Watu… nikajibu kwa kusita.

Naam wazalishaji ni Watu na Watumiaji ni watu, tena unaweza ukasema uzalishaji unaweza kufanyika kwa kutumia mashine, lakini mwisho wa siku ni watu ndio watumiaji, na ni watumiaji hao ambao wanafanya wazalishaji waendelee kuzalisha.

Mzee aliendelea…, Kwahio kijana utaona kwamba watu ndio mtaji mkubwa kuliko chochote kile katika jamii, na kwa watu kutokupata fursa ili kuchangia na kufikia tamati ya uwezo wao ni upotevu mkubwa wa rasilimali katika jamii husika.

Sasa mzee mbona sikuelewi unasema hakuna wa kutusaidia alafu unaongelea kwa watu kama sisi kukosa fursa ni hasara kubwa kwa jamii… sasa hizo fursa zinatoka wapi.

Mzee aliendelea kama vile hajanisikia…, kwahio kwa kuwawezesha watu yaani (wale wasio na makazi, wasio na ajira, watoto wa mtaani na masikini wa kutupwa) ili waingie katika kundi la wazalishaji na kupata kipato ili waweze kumudu mahitaji yao (yaani wanunuzi) itakuwa ni njia bora ya kubadilisha hiki ambacho tunakiona kama mzigo wa taifa na kuwa faida yenye mchango mkubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Mzee aliendelea…, kama wanajamii watakuwa na ujuzi wa kufanya kazi zilizopo kwenye jamii zao na wakawa wazalishaji kipato wanachopata kitawasaidia kuishi na kujikimu katika jamii husika.

Lakini mzee si ndio maana kuna mashule, veta n.k. na serikali na watu binafsi wanahangaika kila siku kutengeneza ajira kwa kukaribisha wawekezaji.

Mzee aliniangalia kama vile nimechanganyikiwa…, unamaanisha shule ambazo zinahitaji kuwa na utajiri au kipato ili upate elimu bora au ajira ambazo unahitaji darubini kuziona? Mzee aliendelea…, wote tutakubaliana kwamba kinachofanyika sasa hakikidhi mahitaji.

Nini kifanyike mzee wangu…, nilimuuliza kwa dhihaka, sababu naona sasa unakuwa kama mwasiasa kuorodhesha matatizo ambayo wote tunayajua bila kuleta suluhisho lolote.

Kijana takupa hizi kurasa zangu…, akanionyesha kakitabu kachafu ambako amekuwa akiandika andika kwa muda mrefu, na kufuta futa…, inaonekana kama ilikuwa ni kazi yake ya muda mrefu na amekuwa akifikiria hili tatizo kwa muda sasa…, nikaanza kutabasamu kwamba huenda mzee anajua njia ya mkato ya haya matatizo yangu…. Mzee akakirudisha mfukoni kitabu chake na kuendelea… humu ndani nitakuelezea HATUA KUMI za kuchukua ambazo zitahakikisha huu umasikini unatoweka bila kumwacha mtu yoyote nyuma.

Aah!!! Tabasamu langu likayeyeka…, mzee naona sasa unaleta nadharia wakati tunachohitaji ni uhalisia…

Sikiliza kijana, na hizi hatua sio tu zitaufanya umasikini kuwa historia, bali hakutahitajika ruzuku au kodi kutoka kwa baadhi ya watu ili kufanikishwa. Ila kabla sijakupa kitabu changu kwanza naomba nikuonyeshe jinsi tunavyoishi Maisha yasiyo na Ufanisi.
 
Tunaishi Maisha Yasiyo na Ufanisi
Tunaishi kwenye dunia yenye utajiri wakati wengi wetu hawana kitu…., (Mzee akatoa simu janja yake akanionyesha sehemu kuna mashamba ya mazao, kwenye ma-supermarket kumejaa chakula, watu wanatupa chakula…., alafu akanionyesha picha nyingine ya watu wana njaa na wanaonekana hawajala siku kadhaa…)

Wakati katika watu saba duniani takriban mmoja ana njaa…., wakati huo huo theluthi tatu ya chakula duniani kinapotea. (ananionesha kwenye simu watu wa mataifa mengine wametupa chakula kwenye majalala, ila hata mimi nawaza ni vyakula vingapi vinaharibika kwa utunzaji mbovu na vingine kuozea mashambani kwa kukosa wanunuzi kwa wakati).

Maji mengi machafu yanayotoka kwenye viwanda, kwenye majumba na sehemu nyingine nyingi yangeweza kusafishwa na kutumika kwa umwagiliziaji, lakini yanaachwa na kuingia kwenye vyanzo vya maji hivyo kusababisha vifo vya viumbe vya majini na kusababisha maradhi kwa binadamu… wakati huo huo kilimo cha kutegemea mvua kinasabibisha njaa sababu ya ukame jambo ambalo lingeweza kurekebishika kwa matumizi ya umwagiliziaji.

Wakati uchafu kutoka majumbani na mijini ungeweza kutumika kutengeneza gesi asilia (Biogas) unaachwa na kuchafua mazingira…., wakati huohuo kuna upungufu wa nishati unaopelekea watu kutumia nishati mbadala kama kuni ambazo zinaharibu misitu au kutumia mafuta ambayo ni gharama na uchimbaji wake unaharibu mazingira.

Wakati ukosefu wa nishati unasababisha kukwama kwa shughuli nyingi za uzalishaji kwenye jamii…, wakati huo huo kuna maeneo matupu kwenye kila paa za nyumba katika kila jamii ambayo kama yangewekewa solar panels tungepata mahekali na mahekali kwa kuvuna umeme wa nishati ya jua… lakini maeneo hayo hayatumiki.

Watu wengi wanapoteza muda mwingi kwenye foleni wakitoka au kwenda kwenye shughuli zao za kila siku, muda ambao wangeutumia kwenye uzalishaji au starehe…, jambo ambalo lingeweza kuepukika kwa kuwa na mpango miji mzuri, wenye sehemu za uzalishaji unaofikika kwa usafiri mzuri wenye uhakika.

Uzalishaji unaendelea kutumia malighafi ambazo ni non-renewable (hazirejesheki) jambo ambalo linaharibu mazingira kwa kutengeneza uchafu/mabaki ambayo yanatupwa…, Wakati mabaki hayo/ uchafu ungeweza kutumika kama rasilimali ya bidhaa nyingine hivyo kuondoa uhitaji wa kutafuta rasilimali mpya kila wakati hivyo kupunguza gharama na kuokoa mazingira.

Kuna kazi nyingi za kufanya katika jamii ambazo hazifanyiki kwa sababu moja au nyingine…, mfano uzalishaji wa chakula, usafi, ukarabati, upishi, burudani n.k., wakati huo huo katika jamii hio hio watu hawana kazi au kipato cha aina yoyote. Hii ni kwa sababu kazi nyingi zinaonekana duni na watu hawataki kuzifanya na ujira wake ni mdogo.

Ingawa kutumia mashine na teknolojia kunaleta ufanisi, mara nyingi jamii zinasita kuwekeza kwenye mashine sababu ya upotevu wa ajira unaoweza kutokea…, hii ikiwa ni fikra potofu sababu kazi hazipaswi kufanyika ili watu wapate cha kufanya bali zifanyike ili kuzalisha kinachohitajika.

Lakini Mzee…, niliamua kumkatisha katika mahubiri yake marefu…, watu wengi wamepoteza kazi kutokana na teknolojia Rashid pale alikuwa anafanya kazi Benki sasa hivi wamepunguzwa…, hizi ATM malipo ya simu n.k. yamekuwa mwiba kwa waajiriwa.

Mzee aliendelea kama vile hajanisikia…, badala ya kulalamika au kuogopa upotevu wa kazi ambao unaweza kutokea ingebidi tufurahi na tuendelee kutumia mashine kadri inavyowezekana…

TUFURAHII !!! Upotevu wa Ajira???

Ndio Kijana inabidi tufurahie mashine na teknolojia sababu inatupunguzia kazi, kazi zikipungua tutapata muda mchache wa kazi kwa wote na muda zaidi wa kustarehe.

MUDA MCHACHE WA KUFANYA KAZI KWA WOTE!!!, Muda mwingi wa KUSTAREHE!!?? Niliuliza kwa mshangao.

Ndio…, mzee aliendelea tunakoelekea kama wazee wanaongezeka na nguvu kazi zinapungua huenda mashine ndio zikawa mkombozi wetu…

Sasa Mzee yaani unasema tutafanya au tufanye kazi kwa ujira ule ule au ujira unapungua!!! Sababu sioni kama ukipunguza ufanyaji kazi bado ujira utabaki palepale.

Sijasema uzalishaji nimesema ufanyaji kazi…, kama mashine zitatupunguzia kazi za kufanya, itakuwa ni uchizi kuacha kutumia mashine ilimradi tu tupate cha kufanya.

Dah!!! Haya…. Basi endelea kunionyesha jinsi Maisha yetu yasivyo na ufanisi nilimjibu huku nikiangalia muda kwenye simu yangu na kujiuliza kama hapa nimeokota au nimeokotwa…

Mzee aliendelea…, Ni wanunuzi wanaofanya Wazalishaji waendelee kuzalisha, na ni WATU amabo ni nguvu kazi katika uzalishaji… tunajua fika bila kuwapa ujuzi watu ili waweze kuzalisha kile kinachotakiwa na wanunuzi ni upotevu wa nguvu kazi…. LAKINI watu wengi ambao wangekuwa wanazalisha, wanapata kipato na kufanya manunuzi wametelekezwa au hawajishughulishi…, jambo ambalo linapelekea upotevu mkubwa wa nguvu kazi ya kuzalisha na wanunuzi wa bidhaa ambazo zingezalishwa.

Mzee!!! Nilimjibu kwa hasira yaani unataka kusema watu ni wazembe? Huoni hapa watu wote wanabangaiza asubuhi mpaka jioni wengine mpaka usiku wakijaribu ku… ku…

Kufanya nini ? Mzee aliuliza, Kuzalisha ? ni kweli wengi huko kijijini wanafanya hivyo ila hapa wengi ni wachuuzi…

Kwani wachuuzi hawana faida?

Wanafaida ndio ila je ni wazalishaji? Ukiangalia kwa undani wanachofanya ni kujitahidi kujipatia kipato ili wapate matumizi yao na kama nilivyosema hapo juu wanunuzi / watumiaji ni watu muhimu sana katika uchumi, bila wanunuzi hakuna wazalishaji… hivyo basi nakubaliana na wewe hawa watu wengi hapa wana faida kubwa sana ingawa faida hiyo haionekani vizuri sababu ni kama ulivyowaita wengi ni wabangaizaji, hakuna uhakika wa kipato hapa. Hivyo basi tunapoteza nguvu kazi na kukosa ufanisi. Laiti kama hawa watu wangekuwa wanazalisha kinachotakiwa na wanapata wateja wanaopelekea kupata kipato, na kwa kutumia kipato chao wananunua kwa wengine ili nao waendelee kuzalisha.

Kwahio tatizo sio uwepo wao ? niliuliza

Hapana kijana, tatizo sio uwepo wao; uwepo wao ni rasilimali kubwa…, tatizo ni sisi kama jamii kutokuitumia rasilimali hio kubwa… hawa wangepata kipato wangekuwa wanunuzi na kukidhi mahitaji yao, na kwa kufanya hivyo wangesaidia uzalishaji uongezeke…, vilevile badala ya kuendelea kubangaiza wangetumika kufanya uzalishaji unatakiwa ili kila muhitaji asikose mahitaji..

Mzee sina tatizo na unyosema ila sijajua unayosema yanawezekana vipi nilimjibu Mzee Busara ila endelea Mzee nakusikiliza….

Swali lako la kwamba inawezekana vipi nitakupatia orodha ya zile hatua kumi kama nilivyotoa ahadi…,

Haya endelea Mzee…

Ingawa kilimo Mzunguko (Crop Rotation) kinaongeza mavuno, na kupunguza matumizi ya mbolea na madawa, tunalima mazao yaleyale, sehemu ileile mwaka baada ya mwaka, jambo ambalo linapunguza mavuno, linaongeza matumizi ya mbolea na matumizi ya madawa ili kupambana na vijidudu ambavyo vinarundikana mwaka baada ya mwaka.

Ingawa tuna uwezo wa kujua nini kinahitajika, kiasi gani na kwa wakati gani… tunazalisha bidhaa nyingi kuliko mahitaji jambo ambalo linaleta gharama ya matangazo ili kuwashawishi watu wanunue vitu ambavyo hawavihitaji au wasingevinunua…., Wakati huo huo kuna watu wanakosa bidhaa muhimu ambazo wanazihitaji lakini hawawezi kuzinunua kwa sababu hawana kipato…

Bila kujijua nilianza kukubaliana na Mzee…, badala ya kuona wingi wa watu hawa wabangaizaji na masikini, kama hasara inabidi tuwaone kama rasilimali. Wazalishaji na wanunuzi ni hawa hawa watu…, tatizo hawajawezeshwa ipasavyo. Yaani ni kama mbegu zinazosubiri kupandwa ili ziweze kuleta mazao.

Huku nikiwa na furaha ya kuona kwamba huenda sipotezi muda wangu nilimwambia kwa furaha…, endelea mzee wangu.

Unaonekana kama vile haujala siku nzima…, aliniambia mzee kwanza kaagize sahani ya wali na maharage kwa yule dada pale urudi na sahani yako tumalizie mjadala…

Nilimuita muuzaji aniletee sahani ya wali maharage nikaanza kula huku nikimuhimiza mzee aendelee.

Nilikuwa wapi?

Kwamba wazalishaji na wanunuzi ni watu hivyo hata hawa wabangaizaji wanaweza kubadilika kuwa wazalishaji na wanunuzi hivyo kupelekea ustawi wa jamii.

Kweli Kabisa…, Hata kwenye nchi zilizoendelea mfano Marekani kuna watu hawana makazi ingawa kuna uwiano wa nyumba kama tatu kwa kila mtu mmoja ambaye hana makazi… Hapo utaona kwamba tatizo sio nyumba, bali ni kipato cha kukuwezesha kuishi kwenye hizo nyumba, yaani uwezo wa kulipia gharama za nyumba kama bili za maji, umeme, usafi, ukarabati na manunuzi ya muhusika.

Mzee ni kweli usemayo… unajua hata leo ukisema unipe nyumba pale mtaa wa uzunguni, kule hakuna mama ntilie, hakuna genge wala siwezi kupata hii sahani ya wali maharage kwa bei kama hii…, sasa si takufa na njaa au itabidi kila siku nitembee ile nije kula huku, ukizingatia hata daladala kule hakuna.

Ni kweli kijana, jitihada nyingi zinazofanywa na wadau pamoja na mashirika mbalimbali haziwasaidii masikini ili wawe wazalishaji zinawafanya waendelee kuishi na umasikini… bila kuondoa umasikini wao kwa kuwawezesha ili kuondokana na utegemezi, jitihada hizi zitaendelea kuhitaji michango na hisani za wadau…, jambo ambalo haliwatendei haki wale wanaotoa hiyo michango au wale wanaopewa michango kwa kuendelea kujiona kwamba Maisha yao yanategemea hisani ya wengine.

Nimekuelewa mzee….

Sasa kijana chukua hili daftari, humu ndani nimeweka hizo hatua kumi ambazo zinaweza kubadilisha mwelekeo wako na wabangaizaji wenzako na kuwa watu wenye uhakika wa Maisha yenu na wazalishaji wenye tija kwa taifa kwa ujumla.
 
Usiku wa Mawazo
Nilichukua kile kijidaftari ambacho Mzee Busara alisema kina hatua kumi za kutuondoa kwenye huu ubangaizaji na kuwa wazalishaji kwa kutupa uhakika wa kipato, malazi, mavazi na mafao ya uzeeni.

Kabla nilikuwa nimepanga nikutane na Rafiki yangu mke wake na mke wangu tujadili jinsi ya kuongea na wenzetu tuone ni vipi tunaweza kupata mikopo ya riba nafuu ili tujikwamue kwenye hii hali…, ila baada ya kuongea na mzee na mimi kufikiri zaidi niliona hata tukipata hio mikopo huenda mwaka kesho tukawa hapa hapa tunatafuta ni wapi pa kupatia mikopo ya riba nafuu. Yaani kupata kwetu mikopo ya kuongeza bidhaa huenda kusisaidie kupata masoko.

Nilikumbuka Mjomba wangu Hussein alivyochanganyikiwa baada ya kuweka rehani nyumba zake mbili na kwenda kukodi shamba la kulima mahindi, kwa bahati mbaya mvua hazikuwa upande wake hivyo nyumba yake iliishia kupigwa mnada…, nilikuwa nawajua wengi waliokwenda kulima wakitegemea bei za masoko ya mwaka huu ila mwaka unaofuata bei kushuka mpaka wakashindwa kurudisha hata gharama ya kulimia. Kweli tunahitaji njia mbadala zenye uhakika.

Nilijihisi mtu mwenye nguvu na ari mpya…, nilipofika nyumbani nikaamua kuanza kusoma kijidaftari moja kwa moja sikutaka kuhatarisha kukisoma usiku kama Luku ikiisha na umeme kuzimika au wapangaji kuanza kulaumu kwamba Jirani anatumia sana umeme hazimi taa mpaka usiku wa manane…, niliwaomba Rafiki yangu, mke wake na mke wangu tuongee kesho asubuhi kabla hawajaondoka kuhusu nilichotaka kuwaambia…, badala ya kuwaambia mawazo yangu ya kutafuta mikopo ya riba nafuu kwa wahisani mbalimbali niliamua niwape mawazo ya mzee.

Nilisoma hizo hatua kumi kwa ufasaha, kijidaftari kilikuwa ni kidogo…, nikarudia tena mara ya pili alafu nikapanga mikakati ya jinsi ya kuwaeleza jamaa zangu bila kuonekana kichaa au tapeli. Kuwa na wazo ni jambo moja ila kulifanya hilo wazo likubalike na lieleweke huenda ni vigumu kuliko hata kuwa na wazo lenyewe.

Ilikuwa mida ya saa nne nilimwangalia mke wangu kwenye mkeka alikuwa ameshalala…, haya Maisha kulala hoi ndio faida pekee iliyopo yaani huitaji vidonge vya usingizi hata kama kuna mbu au una mawazo lukuki unajikuta tu unapata usingizi, vinginevyo bila kuzunguka na kuchoka watu wangekuwa hawalali kwa mawazo au kupelekea kutumia vileo ili viwasaidie kupata usingizi.

Naamua kujipumzisha ili saa kumi niamke wakati hawa wanatayarisha maandazi ya kwenda kuuza niwasaidie na kabla Rafiki yangu hajaondoka ikibidi niende nae nikamsaidie huku tunajadili nini cha kufanya, ingawa nilijua huko kwenye kijiwe chake haitaji msaada wangu zaidi ya mimi kwenda kuongeza tu idadi.

Niliamua kujipumzisha ingawa sikulala kwa mawazo ya kama nitaweza kubadilisha hii nadharia na kuwa uhalisia, na ngumu zaidi sio kufanikisha uhalisia huo, sababu nilijua peke yangu nisingeweza, hivyo mtihani mkuwa zaidi ulikuwa ni jinsi ya kuwaambia wenzangu na wakanielewa, ingawa hakuna mtu ambae alikuwa haoni kuwa hali ya sasa haifai ila kuwaambia njia hii huenda ikatutoa hapa mpaka pale inahitaji nguvu ya ziada.

Saa kumi alfajiri niliamka wengine walivyoamka, wakati tunasaidiana kutayarisha vitu niliwaambia wote kuhusu mawazo ya Busara na zile hatua kumi za kuweza kutondoa kwenye hili lindi la umasikini.

Wote walifurahia matokeo yatakavyokuwa ila kila mtu alikuwa na wasiwasi na uhalisia, na swali kubwa ni jinsi gani ya kupata hayo matokeo, wote walielewa bila nguvu zetu wote hii itabakia kuwa hadithi.

Rafiki yangu aliniambia hizo ni nadharia nzuri ila tunafikaje huko unatokata tufike, ni ipi hatua ya kwanza ya kuchukua?

Nilimjibu sababu leo ni ijumaa, nitaorodhesha wenyeviti wa machinga na vikundi tofauti, pamoja na wenyeviti wa vijiwe vya bodaboda ili tuitishe mkutano keshokutwa Jumapili Saa kumi pale kwenye eneo la wazi karibia na kijiwe chao. Kwa hesabu ya haraka haraka nilipanga nipate wenyeviti kama thelasini wa vikundi tofauti tofauti, ingawa nilijua ni kazi kuwaelewesha watu ila ni nani kwa Maisha haya asingetaka uhakika wa kipato ili kupelekea uhakika wa kumudu makazi kwa wote, uhakika wa elimu kwa watoto, matibabu, chakula, mafao ya uzeeni, burudani na baada ya hayo yote kubaki na chenji ya matumizi mengine.

Binadamu sio Mbuzi wala Kondoo
Nilikusanya majina ya wenyeviti na makatibu wa vikundi mbalimbali, jumla majina kama 30. Siku iliwadia lakini haikwenda kama nilivyotegemea…

Siku njema uonekana asubuhi, na kama ningefuata ushauri huo wa wahenga nadhani ningeahirisha mkutano. Nilipanga waje watu kama thelasini ila kama utamaduni wetu ulivyo baada ya nusu saa nzima iliyopangwa mkutano uanze kulikuwa na watu kama kumi tu… kwa mbali nilisikia watu wakiongea kwa chini chini…

Hivi tunakutana kuhusu nini ?

Nasikia sijui kukwamuana

Kukwamuana?

Kujikwamua kiuchumi…

Hivi kweli kuna posho kweli hapa sioni hata maji ya kunywa, wengine tupo busy na kazi zetu hatuna muda wa kupoteza.

Baada ya kama dakika arobaini na tano na kujaribu kuwapigia simu watu wawahi na kuulizia wapo wapi na kuwahamasisha waje tulifika idadi ya watu 25 jambo ambalo niliona kwamba ni jema, angalau nimepata watu hata kama wamechelewa ila angalau wamekuja

Niliwaita ndani waketi ili nianze kuwaelezea nilichowaitia, ila kwakweli baada ya kuona sura zao za hasira za kucheleweshwa, kujiamini kwangu kwote kuliisha. Kidogo niondoke na kukimbia, lakini kile nilichokuwa nakisimamia na kukipigania kilikuwa ni kikubwa zaidi ya woga wowote. Kipato cha uhakika, uwezo wa kulipia elimu, malazi, mavazi na kupata mafao ya uzeeni na baada ya hayo yote kubaki na pesa ya burudani na kufanya chochote nikitakacho.

Haya tueleze ni kipi unatuambia…, aliuliza mmoja wapo wa waalikwa kwa hasira, tushapoteza muda wa kutosha

Nilimwangalia mke wangu ili nipate nguvu za kuongea nilishangaa sauti imekuwa kavu na inashindwa kutoka…, mikono inatetemeka na ghafla nimesau nilitaka kuongea nini… nilitafuta karatasi yangu niliyokuwa nimeandika dondoo za kuongea... nilikohoa kidogo ingawa sauti haikutoka lakini nilijitahidi.

Ndugu wajumbe…, nimewaita hapa tuongee na kupanga jinsi ya kujikwamua kiuchumi, ni kweli maisha yetu yamekuwa magumu na hayaridhishi, hatujui kesho yetu, ni mwendo wa kubahatisha… nguvu zetu ndio mtaji wetu…

Tunajua yote hayo ndugu mjumbe…, sisi sio wageni wa maisha yetu, kuokoa muda tuambie tusichokijua… alisema mmoja wa waalikwa kwa hasira…, nadhani kama ulivyosema umekuja kuleta utatuzi na sio kutueleza matatizo yetu…, aliongezea mwingine.

Ndio ndugu zangu nimewaita hapa kuwaeleza…, tuelezane jinsi ya kujikwamua…

Tunajikwamuaje na pesa inatoka wapi ? Aliuliza mjumbe mmoja

Pesa?, alidakia mwingine… mimi nilidhani tunakuja kupata pesa (posho) katika huu mkutano, kumbe kuna kuchangishana….

Hapana ndugu zangu…. hakuna michango nilidakia kwa haraka…..

Hamna michango yaani hakuna posho ya huu mkutano? Yaani tumekuja kulishana brah brah brah zisizo na tija.

Tafadhali ndugu zangu naomba mnisikilize…, niliendelea kwa haraka…, nimekuja kuwashirikisha jinsi ya kujikwamua kutoka katika umasikini, jinsi ya kujipatia kipato, jinsi ya kupata malazi, mavazi na mafao ya uzeeni…..

Tunayapataje hayo ? Wewe ndio unatupa?

Huyu jamaa anataka kutupiga…, wanasema ukiitwa kwenye fursa ujue wewe ndio fursa, alidakia mwingine.

Kwanza huyu jamaa nina hasira nae sana alisema mwingine, tangia matatizo yake yametokea ametugharimu sana michango ya hapa na pale… watu hata hatujapumzika ameshakuja na ngonjera nyingine, watu wengine bwana utapeli umewajaa...

Nilianza kuhisi kizunguzungu midomo kukauka na kukosa cha kusema…

Mjumbe mmoja mzee wa makamu alianza kuongea jamani tuwe wastaarabu tumsikilize ndugu mjumbe atueleze alichotuitia kuendelea kujibizana hapa ni kupotezeana muda… haya kijana tafadhali endelea kutuelewesha, hayo yote mazuri unayotaka kuyafanya utatoa wapi pesa ya kuyafanikisha….

Sikiliezeni ndugu zangu, niliendelea kwa kusita huku kujiamini kwote kumeisha, kwa ushirikiano wetu na kwa pamoja ninataka niwaeleze hatua kumi za kuchukua ili tuondokane na huu ufukara, na

Hatua za kuchukua, nina uhakika katika hatua zako zinajumuisha kuchukua michango kwetu na kuhamishia kwako ili wewe ndio unufaike na kuondokana na umasikini wako, alidakia mjumbe mmoja kwa hasira…, tafadhali kuweni na huruma yaani huna hata aibu kutaka kutupiga masikini wenzako, si bora uende ukatapeli wenye nazo au mabenki…

Hapana ninawahakikishia sitochukua hata senti kutoka kwenu!!

Aahh hapa tunapotezeana muda, bora ningekuwa naangalia game la leo na sio kusikiliza wala kupoteza muda kwenye mikutano isiyo na posho alisema mmoja huku akinyanyuka na kutaka kuondoka….

Nilisikia kizungungu na ule mshituko wa kugundua nilichopanga kukifanya kimeshindikana na mkutano niliouwaza kwa siku kadhaa unaelekea kuharibika nilisikia nguvu zinaniishia kwenye magoti na kuanguka, kwa bahati mbaya wakati naanguka kichwa kilijigonga kwenye meza…

Ahh huyu jamaa anaanza tena utapeli wake wa kujifanya amezimia ili tumchangie…, hio ndio ilikuwa sauti ya mwisho kuisikia kabla sijapoteza fahamu.

Nilizinduka baada ya muda ambao nadhani ilikuwa masaa kadhaa sababu nilijikuta nipo sehemu ambayo siitambui kwenye chumba ambacho sikitambui na pembeni alikuwepo mke wangu amekaa kwenye kiti na Mzee Busara.

Naona umezinduka, alisema mzee Busara… ingawa haukunialika kwenye mkutano wako ila nilikuwepo kwa nje nakusikiliza…, Kijana, binadamu sio mbuzi wa kuwaswaga unavyotaka au kondoo wa kuwaambia chochote ukitegemea watakusikiliza.

Sikuelewi mzee wangu…

Badala ya kuwaambia watu nataka muende kule ni rahisi kama watapaona kule na faida za huko wenyewe tu watakwenda…

Sasa kama kule hakupo, na uwezo wa kupapata huko peke yangu sina nitawezaje kuwaonyesha kitu ambacho hakipo, nilijibu kwa kukata tamaa.

Inabidi kuanza kidogo kidogo hatua kwa hatua anza peke yako au na wachache baadae watu wataongezeka…, hata safari ndefu huanza kwa hatu moja….

Pa kuanzia ndio tatizo mzee wangu nilidhani huo mkutano ndio ilikuwa hatua ya kuanzia…

Mzee alitikisa kichwa na kuendelea…, karibu hapa ni kwangu ila kesho takupeleka sehemu wewe na mke wako mtakuwa wageni wangu jisikieni mpo nyumbani mkeo atakutayarishia chakula ule na upumzike nadhani ulivyoanguka hakukuwa na madhara makubwa.

Rafiki yangu na mkewe wapo wapi?

Baada ya wewe kuanguka nilijitolea kuleta usafiri nikakuchukua, niliwaambia tunafahamiana na nitachukua jukumu la kukuangalia, ukizingatia na wenyewe wapo katika shida sidhani kama ingekuwa vema kuendelea kukaa nao. Hii minongono ya kwamba wewe ni tapeli isije ikawaletea na wao matatizo kwamba mlipanga nyote kuwatapeli wanajamii.

Haya maisha haya, hivi nimekosea wapi au nimekosa nini? Mbona mikosi inaniandama nilisema kwa masikitiko.

Kijana acha kukufuru unaweza ukawa unalalamika kwa kukosa viatu, kumbe unayemlalamikia hana hata miguu. Nikikueleza kisa changu huenda chako kikawa ni kidogo, ulipopitia na mimi nimepita tena huenda kwa shida zaidi. Nimepata vingi, nimepoteza vingi zaidi, nimefungwa mpaka jela, nimetengwa na kuogopwa zaidi ya mkoma, mbaya zaidi nimeshutumiwa kwa makosa yasiyo yangu, nimelazimika kuhamia uhamishoni na kutengana na jamii yangu yote, kinachoniuma zaidi ni kwamba yote niliyoyafanya yalikuwa ni kwa nia njema ya kusaidia jamii ingawa matokeo yake imekuwa ni kuumiza wengi.
 
Kupanda Mchicha kuvuna Bangi
Maisha yangu yote nimekuwa mtu wa kupenda kusaidia na kujaribu kuweka sawa pale ambapo naona hapako sawa… Alianza kunihadithia Busara huku machozi yakimlenga…

Ila somo nililojifunza tena kwa gharama kubwa,ni kwamba uzuri wa wazo au njia nzuri ya kufanya jambo ni hatua moja, ila hatua muhimu zaidi na ya maana ni utekelezaji na utendaji wa hilo wazo, ingawa wanasema huwezi kupanda bangi ukategemea kuvuna mchicha ila kiukweli unaweza kupanda mchicha na usipouangalia vizuri unaweza kuzidiwa na magugu, na badala ya kuvuna mchicha wako ukajikuta shamba limejaa magugu.

Mimi ni Muumini wa Umoja na naamini kwamba Umoja ni Nguvu hususan katika watu ambao hawana nguvu umoja wao ndio nguvu zao za kuwawezesha kupambana na mazingira yao.

Nilisaidia kuanzisha kampuni ya umoja wa vyama vya kusaidiana na kuwekeza katika kilimo, viwanda, usafirishaji na kupeana mitaji.

Kampuni ilikuwa kubwa sana na ilisaidia wengi, tulikuwa na vyama kama 4000, vyenye idadi ya wanachama tofauti tofauti ambavyo vilikuwa vimewekeza katika sekta tofauti.

Kinadharia wazo lilikuwa zuri sana, ila kiutendaji kutokana na kukosa uaminifu kwa viongozi na tamaa ya kujitajirisha walianza kufuja mali. Baada ya kuanzisha kampuni sikuendelea na mambo ya uendeshaji bali niliwaachia wasaidizi na watendaji.

Kutokana na umimi wa viongozi wakageuza kampuni kama ATM ya kujichotea pesa na kujilipa mishahara minono. Michango ya wanachama na faida za miradi vyote vikanyakuliwa na kufujwa, miradi ikabaki kwenye makaratasi wakati kwenye akaunti hakuna kitu, watu wakatumia kampuni kuchukulia mikopo, bidhaa zikauzwa kwa mikopo ambayo haikulipwa wala kudaiwa kwa sababu ya kupeana rushwa na bakshishi.

Kwenye makaratasi na kimuonekano kampuni ilionekana kutengeneza pesa ingawa kiuhalisia ilikuwa inapumulia mashine, miradi mingi ilianzishwa sio sababu inahitajika au ingeleta faida, bali ilianzishwa ili kuwatengenezea faida waanzishaji kwa kupewa rushwa na kazi za uzabuni.

Baada ya muda madeni yakazidi. Wadai na baadhi ya mabenki yalipoanza kudai pesa zao ukweli ukajulikana, ufujaji ulikuwa mkubwa watu walijitajirisha na kampuni haikuwa imara kama ilivyodhaniwa. Ili kulipa madeni kampuni ikabidi ifilisiwe, vikundi vingi ambavyo watu wake walikuwa wananchangia ili kupata mgao wa faida wakapoteza mabilioni ya pesa. Na mimi kama mwanzilishi ikaonekana nilihusika na ubadhirifu na kufuja pesa za wanajamii.

Ingawa ningeweza kushinda mashitaka hayo kwa kutumia wanasheria, sikutaka kufanya hivyo sababu nilijua fika kile nilichokianzisha kimewapotezea watu pesa zao na kuwaharibia maisha, hivyo sikupingana na mashitaka na mwishowe nilipewa kifungo cha miaka mitatu.

Kifungo hakikuniumiza sana, ila yaliyotokea nje yaliniumiza zaidi, ndugu zangu na wazazi wangu walikuwa watu wa Mungu, kwa mimi kushitakiwa kwa ufujaji na utapeli lilikuwa pigo kubwa sana kwao na mbaya zaidi baadhi ya watu waliopeteza mali zao waliamua kumalizia hasira kwa familia yangu.

Katika wale waliopeza mali zao, niliambiwa kuna mama mmoja kwa kuamini sana faida iliyokuwa inatolewa na kampuni yetu alichukua mikopo na kuweka nyumba yake rehani ili kuwekeza na sisi, mama huyo baada ya kugundua kampuni ilikuwa inafilisika hivyo yeye kupoteza kila kitu aliamua kujinyonga.

Watoto wa huyo mama nilikuja kuambiwa baadae ingawa sikuwa na ushahidi, waliamua kwenda kuchoma nyumba yangu moto, nadhani sababu ilikuwa mchana walidhani mke wangu atakuwa kazini na watoto shuleni, bahati mbaya watoto wangu hawakwenda shule siku hiyo na mke wangu alitoka kidogo kwenda kuwachukulia dawa, alivyorudi na kukuta nyumba inawaka moto aliingia ndani ya nyumba ili kuwaokoa, ila huo ndio ukawa mwisho wake. Yeye na watoto wangu wawili wote waliteketea kwa moto.

Busara alishindwa kujizuia kwa mbali niliona machozi yanamtiririka na aliyafuta haraka na kuangalia pembeni…, maumivu aliyokuwa nayo niliyahisi pia, nilikumbuka kifo cha mama yangu ambaye sikupata hata uwezo wa kumzika. Busara alikaa kimya kama dakika kumi, nilivyodhani labda amemaliza aliendelea… Unajua inaweza kuwa rahisi kukimbia watu au matatizo, lakini unawezaje kuikimbia nafsi yako? Unawezaje kujikimbia wewe mwenyewe wakati nafsi inakusuta? Wanasema fursa huzaa fursa lakini kwa upande wangu imekuwa kila nikitaka kutenda jema baya linatokea, nikipanda mchicha navuna bangi…. Kuna watu wanafanya maamuzi mabaya kwenye maisha yao, ni uchaguzi wao hivyo wanastahili matokeo, ila upande wangu kila nikitaka kufanya maamuzi mazuri matokeo yake sio ya kuridhisha.

Busara alikaa tena kimya huku akifikiria, baadae akaendelea…, haya yote yalitokea nikiwa jela kifungoni ndani ya miezi mitatu, kwahio kifungo ambacho nilikuwa nimekikubali kama toba ya kampuni yangu kuwapa majonzi watu, kiligeuka kuwa kigumu zaidi, nilikuja kuambiwa wazazi wangu waliapa kunitenga na kutotaka kuniona tena kwa kuwaulia wajukuu wao, na baba mkwe nasikia aliapa kwamba akiniona lazima anitoe roho…, kwa miaka yote niliyokaa ndani hakuna hata ndugu mmoja wala rafiki aliyekuja kuniona.

Pamoja na yote yaliyonitokea mimi, wengi pia maisha yao yaliangamia. Kampuni ilikuwa na wafanyakazi kama elfu tano ambao wote walijikuta hawana kazi ghafla, yaani leo upo kazini hujui hili wala lile wiki inayofuata upo mtaani hauna kazi wala kipato. Mfano kijana mmoja aliyekuwa mchapakazi mzuri na mshahara wake ulikuwa mnono hivyo kumwezesha kupeleka watoto wake shule za gharama, na kuishi maisha mazuri, kwa uhakika wa kazi na kipato alichukua mkopo mkubwa ili aweze kuwekeza. Yaani kuchumia juani ujanani aweze kulia kivulini uzeeni… ila huyu kijana kilichomkuta baada ya kazi yake kuota mabawa baada ya kampuni kufilisika, wenye mikopo yao walianza kudai, mwisho wa siku ilibidi nyumba yake iuzwe kuweza kulipa mikopo, mke wake akachukua mali zilizobaki na kumfukuza huyo kijana, mara ya mwisho nilisikia amechanganyikiwa na anaokota makopo. Wenye hadithi za hivyo ni wengi, na kila nikifumba macho usiku badala ya kulala ninapata ndoto zao na jinsi nilivyohusika kuharibu maisha yao.

Baada ya kutoka gerezani, sikuweza kuendelea kuishi sehemu ile sio kwamba niliogopa jamii ingenimaliza kwa hasira bali nilikuwa nikipata maumivu kila nikiona mradi au jengo ambalo tulikuwa tunamiliki na sasa limepigwa mnada ili kulipa madeni.

Niliamua kuondoka hapo na kwenda mji mwingine, kwa miaka kama kumi nikawa nikifanya biashara za hapa na pale za kuweza kunilisha huku nikiwaza ni kipi ninaweza kufanya kuweka sawa kile nilichoharibu. Nimetengeneza pesa kidogo, na sasa naona nguvu zimeniishia na uzee umeniingia na sijaweza kufanya lolote nililokusudia. Niliondoka kwenye huo mji nikahamia kwenye huu mji wenu…

Na sasa nipo hapa…, busara alivuta pumzi ndefu na kumalizia kwa sauti ndogo ambayo sikujua kama bado anaongea na mimi au anaongea mwenyewe…, ni kweli mengi yanaweza kufanyika hapa kama yatafanywa kwa utaratibu mzuri na sio kufanywa na baadhi ya watu kwa niaba ya watu bali watu wenyewe kwa manufaa yao.
 
Duniani Hakuna cha Bure, hata Ukikipata kuna Anayekilipia
Kesho yake tuliamka mapema na kuanza safari kuelekea alikotwambia Busara. Mimi yeye na mke wangu, jambo ambalo katika yote ninashukuru ni kupata mke mwema kama huyu, katika yote haya hakuwahi wala hajawahi kulaumu wala kulalamika. Ingawa sio tu nimesababisha familia yake ipunguze mawasiliano nae kwa kuona ninampoteza na kumharibia maisha yake bali pia nilisababisha wauze baadhi ya mali zao wakati wa matibabu yangu, kweli nina deni kwake ambalo haliwezi kulipika.

Tulipanda gari kuelekea vijijini, baada ya kama masaa sita ndani ya basi nilishangaa kumsikia Busara akimwambia Konda, “Tushushie hapa tafadhali…”, basi zima walishangaa na Konda kuuliza hapa wapi unajua hakuna kituo, mzee upo sawa kweli?

Kwa kusitasita Kondakta alimwambia dereva atoe msaada wa kutushusha, wakati tunashuka nilisikia minongono watu wakiambiana…. “hawa watakuwa wachawi, wanaloga ili wapate mali…,” kweli mali inatafutwa kwa udi na uvumba mwingine alisema, watu wanawaua hadi watoto wao acha kabisa…, mwingine alidakia.

Tulishuka kwa aibu, nilianza kuwaza isije ikawa kweli huyu mzee anataka kutuingiza katika mambo ya ushirikina, mawazo haya yalizidi kushika mizizi baada ya kupita kwenye vichochoro ambavyo ilionekana huwa havipitwi mara kwa mara tulianza kuangaliana na mke wangu, nadhani na yeye alikuwa ameingiwa na hofu. Nilianza kujilaumu ujinga wangu huenda sio tu tunataka kuingizwa kwenye ushirikina bali tunataka kutolewa kafara, nilijipa moyo kwamba mzee hawezi kufanya hivyo kutokana na mashahidi ambao walikuwepo kwenye basi na walituona, hivyo ataogopa.

Baada ya kama masaa mawili tulifika kwenye uwazi ambao kulikuwepo na nyumba ndogo ya udongo, ilikuwa nzuri ingawa ilionekana ni muda watu wameishi hapa kutokana na magugu na vichaka vilivyokuwepo kwenye mazingira yake.

Haya tumefika, alisema Busara.

Tumefika wapi? Niliuliza?

Tumefika ambapo utaweza kutimiza matakwa yako, kwa kujenga na kutengeneza kile ambacho umekusudia cha kukusaidia wewe, watu wako na wale wote ambao kwa sasa hawana fursa za kuishi maisha ya uhakika na furaha.

Hapa? Unamiliki hili shamba na hii sehemu yote?

Ndio, hapa kuna hekari zangu kama mia moja, ila nilichagua hii sehemu sababu imezungukwa na hekari za kutosha, kwahio siku ukitaka au mkitaka kuongeza zaidi itakuwa rahisi na kwa gharama nafuu.

Unataka kunipa hii sehemu ili niweze kuwekeza na kufanya kile ambacho tumepanga, yaani zile hatua kumi za kujikomboa kutoka katika hali duni tuliyonayo?

Kukupa? Duniani hakuna cha bure kijana, hata ukikipata kuna anayekilipia… hata hiyo hewa unayovuta unaweza kusema ni ya bure ila inapatikana kutokana na kutunza mazingira, miti n.k., kama tukiendelea kuharibu mazingira usishangae watu wakaanza kutembea na mitungi yao ya oxygen mgongoni na kujaza katika vituo kama vile magari yanavyofanya. Sisemi kwamba tutafikia huko, ninajaribu tu kukuelewesha kwamba hakuna bure, kila kinachopatikana kinapatikana kutokana na kuwekeza kitu, inaweza isiwe pesa bali nguvu kazi.

Busara, aliendelea baada ya kunyamaza kwa muda, vilevile tatizo la kutoa vitu bure huenda wanaopewa wasivithamini kama wangekuwa wameweka nguvu zao, pia huenda mtoaji akawa amepata furaha kwamba anasaidia au anamwezesha mpewaji, lakini kwa mpewaji inampunguzia utu, inaleta dhana ya Mabwana na Watwana, mimi nikikupa hii sehemu bure huenda nikashurutisha matakwa yangu kwa lazima sababu tu nilikuwezesha. Kwahio kijana utaona kwamba unachodhani ni cha bure huenda kikawa na gharama kuliko kama ungetoa chochote kukipata hicho kitu.

Kwahio mzee nitakulipa vipi na unaona hali yangu ilivyo?

Utanilipa kwa kufanikisha unachotaka kufanikisha kwa kutumia nguvu zako na kukamilisha kile ambacho ulipanga kukikamilisha. Mwisho wa siku utakuwa na kipato cha kuweza kulipia chochote unachokihitaji bila kuhitaji hisani wala msaada.

Nilimwangalia mzee kwa mshangao, mzee mbona kama tunahesabu vifaranga hata kabla kuku hajataga wala jogoo hatujanunua?

Kidogo, kidogo kijana…., Haba na Haba Hujaza Kibaba.


Haba na Haba Hujaza Kibaba
Nilimuangalia mzee kwa mshangao hapa hakuna pa kuanzia, taanzia wapi nilimuuliza mzee?

Mzee aliangalia kwa muda mrefu alafu akanijibu, hapa unacho kila kitu cha kuweza kuanza na kufanikiwa, unakosa jambo moja tu ambalo na lenyewe utalipata kama ukiweka misingi ya uhakika.

Jambo gani hilo? niliuliza kwa shauku.

Unakumbuka nilikwambia ni kitu gani cha muhimu kuliko vyote kinachohitajika ili kupata ustawi wa jamii?

Nilijibu kwa kusita, Watu?

Naam Watu, alijibu mzee Busara.

Sasa mzee si ndio maana niliitisha ule mkutano ili nipate hao watu ila wote tunajua yaliyotokea jambo ambalo kwakweli ningependa kulisahau.

Wewe uliwaita watu ili wafanye nini?

Niwaelekeze jinsi ya kufanya, nilijibu.

Uwaelekeze na sio uwaonyeshe? Unawezaje kuwaelekeza watu kitu ambacho hata wewe haujafanya au hauna uhakika nacho? Si watakuona tapeli? Tena ukitaka matokeo bora zaidi sio wewe ufanye alafu uwaonyeshe au uwape bali uanze na uwashirikishe katika ukamilishaji hapo ndio mtapata kitu chenu na sio kitu chako wewe kama bwana na wenyewe watumikiaji yaani watwana.

Niliangalia mazingira yalivyo hakuna kitu bali vichaka, hivi kuna hata chakula hapa kweli nilijiuliza…, kama vile mzee Busara alikuwa anasoma mawazo yangu, alisema humo ndani kuna chakula mahindi maharage na jiko la gesi ya kupikia nadhani kwa upande wa chakula mtakuwa vizuri, na baada ya muda nadhani itakuwa vizuri ukiwaleta na watoto wako kuja kuishi huku, kuhusu maji kuna kisima sio mbali sana na hapa.

Watoto wangu kuja hapa niliwaza hivi kweli nimetoka mjini kuja kuishi kama watu wa zama za kale, niliwaza. Kama vile alisoma mawazo yangu Busara aliendelea kama nilivyokwambia hapa kuna kila kitu cha kufanikisha ndoto zako ni watu tu ndio wanakosekana na hao sio tu watakuja bali watamiminika iwapo kuna misingi na uhakika wa maisha yao.

Misingi ?

Watu lazima wawe na uhakika wa kipato ambacho kitahakikisha wanakidhi gharama za makazi, mavazi, wanapata huduma zao zote wanazohitaji, watoto wao wanasoma na uzeeni wanapata mafao ya kuwawezesha kufurahia maisha yao. Na hizo hatua kumi nilizokupa zitahakikisha yote hayo yanafanikiwa.

Ni wapi pa kuanzia mzee wangu?

Anzia mwanzo, anza kidogo kidogo, anza wewe na familia yako, alafu watu wa karibu, muda si muda watu watakuja wenyewe. Msingi ni kitu muhimu sana…, kwahio uamuzi ni wako kama unataka kutengeneza msingi wa kuweza kuhimili jamii yenye ustawi au bora liende kila mtu kivyake mwenye nguvu mpishe.

Ingawa sikumuelewa Busara kwa haraka ila miaka ilivyofuata nilimuelewa vizuri na hatua tulizochukua zilikuwa sahihi vinginevyo nisingekuwepo hapa sasa hivi napanda ngazi ya hili jengo la ghorofa nne lenye nyumba yangu upande wa mbele, ghorofa ambalo ni moja kati ya maghorofa mia nane na thelasini na tatu ambayo wakazi wa mji huu tunakaa na familia zetu. Naliangalia tena jengo vizuri nakumbuka mwanzo kulikuwa na kale kajumba ka-udongo ambako nililala siku ya kwanza na mke wangu baada ya kuingia kwenye huu mji uliokuwa kichaka na msitu hapo awali.

Tuliingia kwenye kale kajumba, palikuwa na vitanda na jiko la kupikia na store ndogo ambapo kulikuwa na magunia ya nafaka za kututosha kama mwaka mzima. Sababu ya uchovu wa safari tulipika haraka haraka tukala wote watatu baadae Busara alituaga na kusema kuna kajumba kengine sio mbali na pale atakwenda kulala, kwamba kuanzia wakati huo hapa ndio palikuwa kwetu, tupumzike kesho yake tukiamka tuanze kuweka mipango yetu katika uhalisia.
 
Mji unaojiendesha kwa Uwazi
Kwa mgeni mjini anaweza kushangaa jinsi mambo yanavyojiendesha vizuri, wengi huwa wanashangaa ni nani anayepanga nini kifanyike. Ufanisi huu hauna kiongozi wala mpangaji, hauna bosi wa kupanga wala Muelekezaji.

Yote yanafanyika kwa uwazi na kwa kutumia teknolojia. Kazi zote zinazohitajika kufanywa kwa mwezi mzima zipo wazi kwenye mtandao, kila bidhaa zikipungua mfano kuna juice inayopendwa sana na inapatikana kwenye supermarket na kwenye migahawa kila inaponunuliwa idadi inapungua kwenye takwimu, taarifa hii inapelekwa kwa wazalishaji ili kujua kiasi gani zaidi kinahitaji kuzalishwa na wasambazaji ili kujua ni idadi gani inabidi ipelekwe kwenye mgahawa husika au supermarket. Na uzalishaji huo unaotakiwa unapelekea kupanga ni idadi gani ya wazalishaji wanatakiwa.

Miamala yote ya pesa inafanyika kwenye mtandao, malipo na mishahara yote ni kwenye mtandao, ingawa malipo haya yanasaidia shughuli za ndani na kuwezesha wakazi, ila kuna pesa inayotakiwa kununua bidhaa zinazohitajika na hazizalishwi ndani, hivyo bidhaa zote zinazozalishwa na kuuzwa nje pesa huwa inahifadhiwa ili iweze kutumika kununua bidhaa kutoka nje.

Mji huu ingawa hauna kiongozi, bali kuna mikutano ya mara kwa mara ya kupanga mikakati ambayo mtu yoyote anaweza kuhudhuria na katika kila uamuzi wa uwekezaji wazo linaweza kutoka kwa yoyote baada ya kufanya upembuzi yakinifu lakini kabla ya kufanya uwekezaji huo mijadala huwa inafanyika kuona kama uwekezaji huo unafaida za kiuchumi na kimazingira. Na ili kutumia busara na ujuzi wa wazee wetu huwa tunawatumia sana kwenye mambo ya ushauri.

Kwahio utaona kuwa katika mji wetu hakuna uwezekano wa ufujaji wala ufisadi, kila kitu kipo wazi na yoyote yule anaweza kuangalia na kuona ustawi wetu kama jamii.

Tuliamua kila kitu kiwe kwa uwazi na kutumia teknolojia ili mji ujiendeshe kuepuka ufujaji na lile lililomtokea Busara na Kampuni yake lisijirudie tena.

HATUA YA KWANZA; Miundombinu Sahihi
Katika hatua alizonipa Busara ya kwanza ni uwepo wa Miundombinu sahihi. Ili kuwa na ufanisi kunahitajika miundombinu sahihi ya kuhakikisha mahitaji yote ya jamii yanapatikana. Ili kupata jamii inayojitegemea, kunahitajika sehemu ya makazi yaani kuishi na sehemu za watu kujipatia kipato na kuzalisha mahitaji yanayohitajiwa na watu.

Busara alisisitiza kwamba hii hatua ni muhimu kuliko zote, hata kama tusipofanya yote kuanzia mwanzo ila ni vema kuwa na mipango ya wapi tunatarajia kufika ili kila ujenzi utakaofanyika, ufanyike kulingana na mipango iliyopangwa ambayo itazingatia ufanisi na utunzaji wa mazingira.

Nilimkumbuka Busara, na machozi yalinitoka rafiki yangu wa karibu na nguzo muhimu iliyofanikisha uwepo wa huu mji na sasa hayupo kuona matunda ya mawazo yake, huenda kuna vizazi vijavyo havitasikia hata jina lake. Hapo ndipo nilipata wazo la kuandika hiki kitabu “Machinga Mimi Masikini” ili kuelezea hatua kwa hatua jinsi jamii nzima ya watu ambao hawakuwa na uhakika wa maisha yao, mafukara na wategemea hisani, walivyotoka kwenye hali ya uduni na hivi sasa ni matajiri wenye pesa ya kupata mahitaji yao yote na kubaki na ziada ya pesa.

Kwenye miundombinu sahihi ni muhimu kuwa na sehemu ya uzalishaji, yaani viwanda. Pia ni muhimu sehemu za makazi zisiwe mbali sana na sehemu za uzalishaji, na hizo sehemu ziwe zinafikika kwa usafiri wa uhakika (mabasi ya abiria).

Sababu watu tofauti walikuwa wanatoka shift tofauti tofauti kufanya kazi, nilitoka nje ya jengo la nyumba yangu, ambapo kila dakika tano mabasi yalikuwa yanapita na mengine yanazungukia sehemu za uzalishaji. Nilipanda basi na kumuonyesha dereva ticket yangu ya kusafiria sehemu yoyote mjini, gharama ya ticket ilikuwa dollar 20 kwa mwezi ambazo zilikuwa zinakatwa kwenye kipato changu cha dollar 600 kila mwezi Viwanda havikuwa mbali sana na mji mwendo kama wa robo saa mpaka nusu saa.

Viwanda hivi vilikuwepo sehemu ambapo kwa lugha ya kigeni inajulikana kama (Eco-Industrial Park); sehemu hii viwanda vyote vilivyopo vinashirikiana vyenyewe kwa vyenyewe pamoja na jamii husika ili kupunguza uchafu na uharibifu wa mazingira. Vinashirikiana kwa kutumia malighafi, nishati, maji, miundombinu n.k. Ushirikiano huu pamoja na kuongeza ufanisi na kupunguza uchafuzi wa mazingira unapunguza pia gharama sababu mabaki ya kiwanda au uzalishaji mmoja unaweza kutumika kama malighafi kwenye uzalishaji mwingine. Naangalia sehemu ya mifugo (concentrated animal farming) hapa mifugo mingi inafugwa kwenye sehemu ndogo, ufugaji huu ungekuwa peke yake ungeharibu mazingira kwa kuzalisha uchafu mwingi lakini kwenye huu mji badala ya uchafu huo kuharibu mazingira unatumika kwenye mtambo wa kutengeneza nishati na mbolea (Biogas Plant).

Mji huu pia ungeweza kuitwa kwa lugha ya kigeni kama (Smart), kila takwimu (data) zinajulikana kwa wakati, mfano mahitaji ya wakazi. Maelezo ya nini kinahitajika, kiasi gani, na kwa watu gani na kufanikisha hayo mahitaji kutahitajika nguvu kazi kiasi gani…, yote haya yanajulikana kwa wakati. Takwimu hizo zinapatikana kwa kutumia teknolojia inayokusanya habari kutoka kwa wakazi, wanunuzi, vifaa na bidhaa mbalimbali hivyo habari kuhusu afya za watu, mahitaji na matumzi ya watu, idadi ya bidhaa, matumizi ya nishati n.k. yanapatikana kwa wakati ili yaweze kufanyiwa kazi.

Kama nilivyoeleza hapo awali huu mji una nyumba za makazi kwa kila mkazi, mji una watu kama elfu hamsini, wastani wa kila nyumba una watu watano; mama, baba na watoto wawili, hapo nimeweka na mzee mmoja kwenye kila nyumba, ingawa wazee wana sehemu zao za makazi ya wastaafu ambayo wakitaka wanaweza kwenda kuishi. Nikistaafu nadhani takwenda huko sababu hayo makazi yana vifaa na mahitaji ya wazee pamoja na uangalizi wa masaa ishirini na nne kutoka kwa waangalizi. Ingawa ninachokipendea zaidi ni kukutana na watu wa rika moja, kubadilishana mawazo, na kukumbushana enzi zetu. Vilevile pamoja na kustaafu wazee hapa mjini wanatumika kama washauri (Thinktanks) hii inasaidia kuwafanya waendelee kutumika kwa manufaa ya jamii na kutokujiona kama mzigo.

Nyumba za makazi ni ghorafa tatu zenye nyumba 12 kwenye kila jengo, nyumba nne kila orofa. Tuna takriban maghorofa 833 na yote yapo pembezoni mwa barabara ambazo mabasi ya usafiri yanapita kila dakika tano.

Ingawa watu wengi hawapendi kuishi kwenye ghorofa na wanapendelea zaidi nyumba, ila watu wa huu mji muda mwingi wanautumia wakiwa nje na sio ndani ya nyumba. Kuna vitu vingi vya kufanya nje, maeneo yote ya jamii, mazingira ya mji na mandhari ni ya kuvutia, kuna migahawa na sehemu nyingi za kustarehe na zenye bei nafuu, sehemu ambazo familia wanaweza wakakutana na kukaa pamoja, sehemu za michezo, kuburudika n.k. Watu wa hapa mara nyingi wanakwenda makwao kupumzika tu, muda wao mwingi wanakuwa nje wakistarehe.

Mpango wa huu mji haukuja kwa bahati mbaya, kuanzia mwanzo tulijua tutakuja kuwa na wakazi kama elfu hamsini mpaka laki moja, ingawa siku ya kwanza tulianza tukiwa watatu. Hata hayo maghorofa tulipanga yawe maghorofa ili tusichukue nafasi kubwa sana ambayo ingetumika kwa misitu, bustani na mazingira. Tulipanga idadi ya wakazi lazima iendane na idadi ya ajira na uzalishaji unaofanyika katika sehemu ya viwanda. Yaani uzalishaji lazima uendane na mahitaji ya wakazi ambayo yataendana na idadi yao katika mji.

Kila mtu katika huu mji ana maisha mazuri wala haitaji kutegemea gari kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Huduma zote zinapatikana katika maeneo ya wakazi, na nyumba ya mbali kabisa mpaka katikati ya mji ni mwendo wa kutembea au kutumia baiskeli, hata hivyo kuna mabasi ya kutosha kila dakika tano yanapita katika makazi ya watu.

Chakula kwenye migahawa ni cha ubora na bei nafuu kuliko hata kujipikia nyumbani na kwa muitikio mkubwa wa watu kula kwenye migahawa na hoteli kunafanya mji uongeze idadi ya ajira na kuwafanya wakazi kuburudika na kukutana mara kwa mara hivyo kujenga mshikamano.

Huu mji hauna kupoteza muda kwenye foleni wakati wa kutoka na kwenda kwenye ajira, magari ya kuwapeleka watu kutoka kwenye makazi kwenda kwenye uzalishaji huchukua muda sio zaidi ya dakika kumi na tano mpaka nusu saa.

Katikati ya mji kuna soko kubwa ambalo watu wanajipatia mahitaji yao tofauti, kuna supermarket kubwa ambayo ni ya ghorofa, kila orofa ina bidhaa tofauti hivyo kufanya urahisi wa watu kujua kitu gani kipo upande gani, na kwa wale ambao wanapenda kuletewa mpaka mlangoni, huduma hizo pia zinapatikana.

Kwenye huu mji hakuna tatizo la kukosa soko, kila bidhaa ina uhakika wa wateja wengi, na wingi huo wa wateja unaupa mji uwezo wa kupata bei nafuu hata ya bidhaa isizotengeneza kutokana na uwezo wa kununua vitu kwa bei ya jumla. Hili la bidhaa kutokukosa soko linasababishwa na mfumo wetu wa kuzalisha kulingana na mahitaji ya wakati… kwa lugha ya kigeni tunaweza kuita mfumo huu (Just in Time Production).

Miundombinu sahihi imehakikisha wakazi wana makazi ya kuishi, kazi za kuwapatia ajira na mahitaji yao yote wanayapata ndani ya mji.

Haya yote yanayopatikana sasa miaka ishirini iliyopita yalikuwa ni nadharia.

Baada ya kulala kwenye ile nyumba ya udongo kesho yake niliamka mapema, mke wangu tayari alikwisha amka na kutayarisha chai Busara alipowasili tulikunywa wote kabla ya kutoka nje. Nilimwangalia Busara nikisubiri majibu ya wapi tunaanzia.

Busara aliniangalia kwa muda huku akiangalia mazingira, wapi tutaanzia, nilimsikia akisema ingawa sikujua kama ni swali anauliza au ni mwanzo wa mazungumzo. Tuanze kwa kuhakikisha tunakidhi mahitaji yetu na kupata ziada ya kuweza kuuza na kujipatia kipato.

Tuanze na ufugaji na sio ufugaji wa holela holela bali ufugaji wa viwanda (industrial / intensive farming) ufugaji huu unahitaji sehemu ndogo kwa idadi kubwa ya mifugo, na pa kuanzia tuanze na kuku wa mayai, na kuku wa nyama, baadae tuhamie kwenye ng’ombe.

Sehemu ya kufugia itakuwa kwenye eneo ambalo hapo baadae litakuwa sehemu ya viwanda, ambapo baadae tutakuwa na mtambo wa kubadilisha mabaki na uchafu wa hii mifugo kuwa gesi asilia na mbolea. Na kama nilivyosema mahitaji na uzalishaji lazima viendane, nadhani huu utakuwa muda muafaka wa kumuita rafiki yako na mke wake ili waje wasaidie kwenye huu ufugaji nadhani hawa kuku wa mayai na nyama vitatosha kuweza kuwapatia chakula na kipato kwa kuweza kuuza ziada.

Kusema ilikuwa rahisi ila utekelezaji ulikuwa ni mgumu sana wiki zilizofuata tulifanya kazi kubwa sana, kabla ya kuanza kufuga tulipaswa kuwa na uhakika wa chakula cha kulishia hio mifugo na kupunguza gharama tuliona vema kuchanganya chakula wenyewe, sehemu ya viwanda ambapo ndio tuliweka sehemu ya ufugaji haikuwa mbali na barabara hivyo kwa msaada wa busara tulijenga mabanda ya kuku, tuliamua kuhusu ng’ombe na mifugo mingine tutafuga baadae pindi idadi ya watu ikiongezeka.

Mwisho wa siku tulipanga chakula cha kuku tutakuwa tunatengeneza wenyewe kutoka kwenye mabaki na mazao mengine, ila kwa kuanzia tulipanga kununua chakula cha jumla na kuchanganya wenyewe. Sababu sehemu ya viwanda ilikuwa mbali kidogo na sehemu ambapo tulikuwa tunakaa tualiamua kuhamia na kuishi sehemu ya viwanda tulipojengea mabanda ya kuku, ili iwe rahisi kuwahudumia pamoja na kuwalinda kuku hao.

Kwa kuanzia na ili tupate ujuzi kabla ya kupanuka zaidi tulianza na kuku wachache, tulipanga kwa siku tuwe tunauza kuku kama elfu moja, yaani kuku elfu thelasini kwa mwezi. Kwa kufanikisha hilo tulikuwa tunatotoresha vifaranga kama elfu moja kila siku, hivyo kuhakikisha kwamba kuku hao wanakua kwa nyakati tofauti na hivyo kuweza kukidhi soko kwa mwaka mzima. Ingawa tungeweza kuongeza idadi ya kuku ila hatukuwa na uhakika wa soko hivyo tuliamua kuanza kidogo kidogo huku tukiongeza ujuzi.

Baada ya mwezi tulikuwa tumeshaanza kuzalisha na kuuza kuku kwa order, haya yote tuliweza kuyafanya tukiwa wanne, mimi, mke wangu, rafiki yangu na mke wake. Ingawa bidhaa tulikuwa nayo na tuliweza kuuza kwa mikataba kwenye migahawa ila bado soko lilikuwa sio la uhakika.

Baada ya miezi mitatu tulianza kupata maombi kutoka kwa watu waliokuwa wanataka kujiunga na jamii yetu, maombi yalikuwa mengi sana ila tulishauriana tuchukue kwanza familia kama kumi, na kabla ya kufanya hivyo kwanza tuongeze kazi za kufanya. Tuliamua tuongeze ufagaji wa ng’ombe na kilimo cha mboga mboga pili katika hizo familia tulichagua familia kama nne zenye waalimu ambao tangia wamalize masomo walikuwa hawajapata ajira, hivyo sababu familia zetu wote zilikuwa na watoto tukaona itakuwa vyema kama tukianzisha sehemu ya kuwafundishia hao watoto na hawa waalimu wangesaidia sana kufanya kazi hio.

Tulianzisha mashamba ya mboga mboga kwa umwagiliziaji na kuongeza ufugaji wa ngombe wa kisasa wa maziwa, wale waalimu wanne waliokuwepo kati yetu walianza kutoa mafunzo kwa watoto wetu, ambapo tulijenga mahema yawe ndio kama shule, tulijua hili lilikuwa suluhisho la muda mfupi wakati tunapanga mikakati ya muda mrefu. Tulikuwa tunajitosheleza kwa chakula, na kupata ziada ya kuweza kuuza na nishati ya kupikia tulikuwa tunapata kutoka kwenye gesi asilia iliyokuwa inapatikana kutoka kwenye mifugo yetu.

Tulikuwa tunaishi maisha ya kijijini, ingawa tulikuwa kwenye njia sahihi ila bado tulikuwa hatujafika hata robo ya tulipotaka kuelekea, tulikuwa hatuna njaa na tuna uhakika wa chakula ingawa kazi, zilikuwa nyingi lakini mengi ya kufanya tulikuwa hatujayafanya na bado hatukuwa na uhakika wa soko jambo ambalo lingepelekea uhakika wa kipato.

Wakati tunaanza tatizo kubwa lilikuwa ni kupata watu ingawa kwa sasa tulikuwa tunapata maombi mengi toka kwa wenzetu tuliowaacha mjini wanabangaiza, tungeweza kuwachukua ila tulijua kwamba bila misingi imara tungekuwa tunahamishia ubangaizaki kutoka huko mjini kuja huku kijijini.

Kabla ya kupanda gari kurudi kwenye makazi, niliangalia mabanda ya kuku wa nyama nikakumbuka yale mabanda tuliyoanza nayo…. kwa sasa tuna mabanda kama kumi ya kuku wa nyama ambayo kila banda lina ukubwa wa mita 146 kwa mita 43, nakumbuka mipango ya huu ujenzi tuliutoa Denmark, katika haya mabanda kila banda moja lina uwezo wa kutoa kuku laki moja na elfu thelasini kwa kila mzunguko, na yote haya yanafanyika kwa kuwa na wafanyakazi wachache sana sababu chakula na maji vyote vinapita kwenye mifereji na mabomba ambayo yanafanya kazi automatic, hivyo kupelekea urahisi wa lishe kwa mifugo na upotevu mchache wa chakula.

Kweli tumetoka mbali sana…
 
HATUA YA PILI: Idadi Sahihi ya Wakazi Wazalishaji
Mji wetu ulikuwa na idadi ya watu sahihi. Idadi iliyohakikisha kuna watu wa kutosha kufanya kazi zilizopo hivyo kila mkazi kuwa na uhakika wa kupata kipato kwa kufanya kazi zinazohitaji kufanywa ili kuweza kujikimu kwenye maisha yao. Pia kazi zilizopo zilihakikisha mahitaji yote ya wakazi yanatekelezwa. Makazi na Kazi lazima viendane, wakazi wawe na kazi, na wenye kazi wawe na makazi.

Nakumbuka maneno ya Busara, aliwahi kuniambia kuwa na makazi ya watu bila watu hao kuwa na kipato ni kutengeneza jamii ya waharifu (ghettos), na kuwa na kazi bila makazi ni kutengeneza makazi duni (slums)

Niliwahi kumuuliza…, hivi kweli tunaweza kuwakatalia watu kuhamia kwenye mji wetu, si tutakuwa hatuwetendei haki? Busara aliniambia kama mji mmoja ukijaa unaweza kutengeneza mji mwingine sehemu nyingine…, hakuna maana kuwa na watu ambao hawana uhakika wa kipato cha kuwawezesha kuishi katika sehemu husika, kufanya hivyo ni mwanzo wa kupoteza ufanisi, muda si muda utashangaa jamii nzima inakuwa ya wabangaizaji kwa kugombania kidogo kilichopo badala ya kupeana fursa ya kutengeneza zaidi ili kila mtu anufaike. Kama unakumbuka kitu muhimu kuliko vyote katika jamii ni watu, na kuwarundika watu sehemu moja badala ya kuwapa fursa ya kuzalisha ni kupoteza nguvu kazi. Hakuna sababu ya kuwa na wakazi ambao hawana kipato au watu wenye kipato ambao hawana makazi.

Kumbuka kijana ili huu mji ufanikiwe ufanisi ni wa muhimu sana na jamii yenye idadi sahihi ni kiungo muhimu sana katika ufanisi…, aliendelea Busara, ili kufanikiwa kunahitajika kuwe na mabaki / uchafu wa kutosha ili kutengeneza gesi asilia, lazima kuwe na watu wa kutosha kuzalisha na kufanikisha mahitaji ya watumiaji na pia ufanikishaji huo uhakikishe unatoa kipato kwa wazalishaji ambao ni wakazi.

Mji wetu ulifuata ushauri wa Busara, kwenye wastani wa watu elfu hamsini, wazazi elfu ishirini, watoto elfu ishirini na wazee elfu kumi…, wazazi wote wana fursa ya kufanya kazi hivyo kujipatia kipato.

Tumehakikisha wakazi wa kila nyumba (wazazi) wanafursa ya kufanya kazi na kujipatia kipato kwa kufanya kazi zinazohitaji kufanywa. Wazazi wote wanao ujuzi wa kufanya kazi zilizopo kwenye jamii. Tuna miundombinu ya shule na vyuo vya kuwawezesha watoto elfu ishirini kupata ujuzi na elimu na wazee elfu kumi wana fursa ya kuangaliwa na kufurahia maisha yao ya uzeeni baada ya kustaafu.

Kazi zote ngumu zimerahisishwa hivyo kuweza kufanyika hatua kwa hatua kwahio watu wengi zaidi wanaweza kuzifanya, mashine zinatumika kufanya kazi zote ambazo zinaweza kufanywa na mashine, na kazi chache zinazobaki zinafanywa na wakazi ambao tuna ujuzi wa kazi mbalimbali ili tuweze kujipatia kipato.

Kwa kutumia mashine kadri inavyowezekana kumepunguza sana kazi, mambo mengi yanafanywa na mashine, hivyo kunabakia kazi chache ambazo zimewekwa wazi ili kila mmoja aweze kufanya na kujipatia kipato. Uchache wa kazi hizo umesababisha watu tuwe na muda mchache sana wa kufanya kazi na muda mwingi wa starehe.

Faida kubwa ya kurahisisha kazi husasan kwenye uzalishaji umefanya kazi ngumu kuwa rahisi hivyo hata watu ambao hawana utaalamu wa kazi husika kuweza kuzifanya, na hivyo kujipatia kipato. Yaani kila hitaji la mkazi, kama linaweza kufanywa na wakazi, lilifanywa na wakazi, na katika ufanyaji huo linatoa fursa ya kipato wakazi hao.

Kwa kila mtu kupata kipato na kwa kufanya kazi chache na kwa muda mchache iwezekanavyo kumeondoa uhitaji wa misaada au kutegemea kutoza kodi kwa wachache ili kusaidia wengine, kila mtu anaweza kugharamikia maisha yake.

Tangia awali tulijua kutoa misaada au kuwapa watu vitu bila kuvifanyia kazi kunaweza kuleta utegaji, kama binadamu anaweza kupata kitu bila kukihangaikia ni wachache sana watafanya kazi au kuhangaika. Na sababu kila mtu ana fursa ya kufanya kazi yoyote, sehemu yoyote kulingana na nini kinatakiwa kufanyika kwa wakati huo, na sababu tumehakikisha watu wote wamepata ujuzi wa kufanya kazi nyingi iwezekanavyo, hakuna sababu ya kutoa misaada. Hata kwa wale wasio na nguvu au walemavu wanaweza kufanya kazi ambazo hazihitaji nguvu, na kwa matumizi yetu ya mashine ni kazi chache sana zinahitaji nguvu.

Kila mtu ana maamuzi ya lini afanye kazi, lini apumzike au achukue likizo, ingawa kutokana na ukweli kwamba kazi ni chache na muda mwingi ni wa kustarehe, watu wengi hawahitaji kuchukua likizo mara kwa mara sababu kila siku ni kama likizo.

Sababu kila mtu anauwezo na fursa ya kupata kipato na kumudu maisha yake, mji hauhitaji kutumia gharama kutoa misaada au marupurupu kila mtu anakidhi mahitaji yake mwenyewe.

Kila mkazi ana uhakika wa mambo yafuatayo

  • Kipato cha kutosha kuweza kujikimu.
  • Kuishi / Kumiliki nyumba bora.
  • Watoto wake kupata elimu na yeye kuongeza ujuzi kila inavyohitajika.
  • Matibabu kwake na familia yake
  • Akizeeka na kustaafu anapata mafao ya uzeeni hivyo kumuhakikishia maisha ya furaha uzeeni.
Hayo yote yamefanya tuwe na jamii isiyo na hofu ya kesho hivyo kutufanya tuwe wazalishaji na watumiaji wenye furaha bila msongo wa mawazo, au hofu ya kesho yetu.

Baada ya miezi kama mitano kwenye kijiji chetu tuliendelea kufuga na kulima mbogamboga na nafaka kwa manufaa yetu na kuuza ziada kidogo, ingawa bado makazi yetu hayakuwa mazuri sababu tulikuwa tumejenga makazi ya muda, tulijua ni ya muda sababu kuanzia mwanzo tulipanga makazi lazima yawe yenye ufanisi wa kuhakikisha tunavuna nishati na kutokuharibu mazingira.

Tuliendelea kuongeza familia kidogo kidogo lakini kabla ya kuongeza familia yoyote tulihakikisha familia hio inayokuja au watu wanaokuja wanakidhi hatua ya Tatu.
 
HATUA YA TATU: Kuongeza Ujuzi
Watu wote kuwa na uwezo wa kufanya kazi nyingi iwezekavyo katika mji wetu haikuwa bahati mbaya bali ilipangwa tokea mwanzo. Kabla ya kuongezea familia na watu katika kijiji chetu tulihakikisha kwamba wana ujuzi wa kufanya kazi zote zilizokuwepo katika kijiji, na kila mara tulivyoongezea mradi au shughuli mpya tulihakikisha watu wanafundishwa na kupewa ujuzi huo. Ujuzi na mafunzo yalikuwa yanafanyika kwa vitendo kwenye kazi husika kwa wenye ujuzi kufundisha wenzao.

Na hata sasa shule zetu na vyuo zina masomo ya vitendo ambapo mara kwa mara wanafunzi wanazungukia sehemu zote za uzalishaji kujifunza na kufanya kazi kwa vitendo, hii inahikikisha siku wakimaliza elimu zao wanauwezo wa kufanya kila aina ya kazi katika mji.

Kuanzia mwanzo tulihakikisha kazi zote zinaheshimiwa sababu ni muhimu katika kufanikisha mahitaji ya watu, na sio kuona kazi nyingine kama duni za kufanywa na watu ambao hawana uwezo wa kufanya jambo lingine. Naangalia jinsi barabara zilivyo safi na bustani zinapendeza, haya yote yanawezekana sababu hata hizi shughuli zipo kwenye kapu la ajira za mji, masaa ya kufanya hizi shughuli yanakuwepo kwenye mtandao wa ajira ili yoyote aweze kuchagua kuyafanya na kujipatia kipato chake cha mwezi.

Haya nilikuwa nayafikiria nikiwa hapa kwenye hili jengo la chuo. Hapa tuna wakufunzi ambao nao wanajipatia ujira wao kwa kutoa elimu kwa wakazi. Chuo hiki kazi yake sio kutengenezea watu vyeti kwamba wamehitimu hiki au kile bali kuwapa elimu na kuwaongezea ujuzi. Vilevile ni sehemu yakufanya uchunguzi na kutatua changamoto za mji, yaani changamoto zote na jinsi ya kuboresha utendaji na uzalishaji wa shughuli zote unafanyiwa uchunguzi na wakufunzi, wanafunzi au mkazi yoyote anayetaka kufanya uchunguzi. Milango ya hiki chuo ipo wazi wakati wote kwa yoyote kuweza kuingia na kutumia miundombinu ya chuo ili kujiongezea maarifa.

Nilikumbuka mpaka kuja kupata hili jengo ilichukia miaka mingi sana, tulianza polepole kwa watu kujifunzia kwenye mahema na wakufunzi tulio anza nao walikuwa ni wale waalimu wachache waliotoka kati ya zile familia kumi za mwanzo kuhamia kijijini.

HATUA YA NNE: Chochea Uzalishaji kwa kutokuzawadia Uzembe
Uwezekano wa kupata faida au mahitaji na kuofia uduni wa maisha au kukosa mahitaji ndio motisha ya watu kufanya kazi., ukiondoa hofu ya maisha duni au kukosa mahitaji kwa kuzawadia uzembe kutasababisha watu wengi kutokufanya kazi. Tulijua kuwa watu hutumia udhaifu wa mipango iliyopo, mfano aliniambia Busara…, Uswizi ingawa ni kati ya nchi yenye watu wenye afya katika bara la Uropa lakini kuna idadi kubwa ya watu wanaokosa kazi kwa kisingizio cha kuugua, hii inawezekana inasababishwa na mpango wao wa kuwapa wagonjwa asilimia themanini ya mshahara wao wanapokosa kazini.

Kwahio tofauti ya kipato cha anayefanya kazi na asiyefanya kazi kikipungua, wengi watachagua kutokufanya kazi. Hivyo tuliamua badala ya kutoa faida, misaada na marupurupu ambayo ni gharama na yanaweza kutumika ndivyo sivyo, njia bora ni kuhakikisha watu wamewezeshwa na wana fursa ya kupata kipato cha kuweza kumudu mahitaji yao bila kutegemea misaada wala marupurupu. Kiufupi mji huu una mahitaji yote ingawa sio ya bure, lakini ni ya gharama nafuu, ambazo kila mkazi anaweza kumudu.

Mfano badala ya kutoa elimu bure kwa watoto wa wakazi, wazazi wao wanachangia gharama kutoka kwenye mishahara yao, hii pia inasaidia kuwa na wazazi wanaowajibika na kujali uzazi wa mpango.

Pia uwepo wa kazi ambazo zinaweza kufanywa na yoyote wakati na muda wowote, imefanya watu waweze kufanya kazi kila wanapotaka bila kulazimishwa au kuambiwa ni wakati gani wafanye kazi au wakati gani wachukue likizo. Mji umehakikisha shughuli na kazi za kufanya zipo kwa wote ili wapate kipato. Na sio uwepo wa kazi pekee bali kuanzia mwanzo tulikuwa tunahakikisha watu wanao ujuzi wa kuweza kufanya kazi zilizopo, hivyo ilibakia kuwa jukumu la wakazi kufanya kazi ili waweze kumudu maisha yao katika mji.

Tuna jamii yenye kupenda kujituma na inayoona kufanya kazi ni sifa, hii ni tangia enzi za huu mji ulivyokuwa kijiji. Kila kinachofanyika kina manufaa kwa jamii, hakuna shughuli ambayo haina tija na kila anayeifanya anaona sifa na kujivunia akijua fika bila shughuli ile kufanyika mji utasimama na hautaendelea kustawi kama ulivyo.

Watu wanafanya shughuli ili waweze kupata kipato cha kuwawezesha kuishi na kustarehe katika mji, bila kulazimishana wala kushutumiana wakazi wote wanafanya kazi zilizopo, na hio ndio njia pekee ya wao kumudu maisha yao.

Hata kama mtu akiamua kuchukua likizo ya miaka kumi anaweza kufanya hivyo, ila akiba kwenye akaunti yake itamlazimu kufanya shughuli ili aweze kuendelea kuishi, ingawa wengi hawahitaji likizo za muda mrefu…, ukizingatia watu wana muda mchache wa kufanya kazi na mwingi wa kupumzika na kustarehe, kila siku ni kama likizo kazini.

Maisha yetu kijijini yaliendelea kuwa rahisi siku baada ya siku, kila tulivyoongeza familia zenye ujuzi ndio maisha yetu yaliendelea kuwa rahisi. Sababu tulikuwa tunaongeza wazalishaji na watumiaji, yaani nguvu kazi na soko la nguvu kazi hizo. Tuliendea kupokea watu na familia ila kwa kuhakikisha kila anayeingia anapewa ujuzi wa kufanya shughuli zilizopo ili apate kipato cha kumuwezesha kumudu maisha yake kijijini.
 
HATUA YA TANO; Fursa ya Kupata Kipato
Mji wetu una watu takribani elfu hamsini, familia kama elfu kumi. Wazazi wote na watu wazima wana fursa ya kupata kipato kwa kufanya kazi zilizopo. Hivyo katika huu mji watu takribani elfu ishirini wana fursa ya kufanya kazi na kupata kipato kwa kulipwa kila mwezi.

Nakumbuka wakati Busara ananiambia kuhusu hili suala, nilimuuliza, unasema kila mtu apate ujira kwa kufanya kazi, je kama hakuna kazi?

Unamaanisha watu watakuwa hawahitaji wala kutaka chochote aliniuza Busara…

Unamaanisha? Niliuliza kwa mshangao.

Sababu ya watu kufanya kazi ni kuwapatia watu mahitaji yao, sasa kama watu wanahitaji au kutaka vitu basi huwezi kusema hakuna kazi za kufanya. Hivyo kazi zote ambazo zinaweza kufanywa na mashine zitafanywa na mashine na zile chache zitakazobaki zitafanywa na wakazi,

Na huo ndio mfumo tulioutumia, na kwa kutumia kauli mbiu yetu ya kutumia mashine kila inapowezekana, kazi chache zinazobaki baada ya kufanya hesabu zitahitaji masaa mangapi zinagawanya kwa watu elfu ishirini ili kila mtu apate fursa ya kufanya kazi kwa muda mchache iwezekanavyo. Ukizingatia matumizi ya teknolojia katika kuchagua na kugawa kazi, shughuli hii inafanyika kwa ufanisi bila kuhitaji mtu wa kupanga nani afanye nini na wapi, bali mtu mwenyewe anachagua ni shughuli ipi ipo wapi na lini ili aweze kukidhi masaa yake machache ya kazi kwa mwezi husika ili aweze kujipatia kipato chake.

Nakumbuka nilimuuliza Busara wakati tunaongea… mzee vipi kama kazi ambazo zinaweza kukidhi mahitaji na matakwa ya wakazi haziwezi kufanywa na wakazi waliopo?

Busara alijibu…, ndio maana kuongeza ujuzi ni hatua mojawapo, ukiongezea na kurahisishwa kwa kazi ili watu wengi zaidi waweze kuzifanya utagundua kwamba kazi nyingi zitaweza kufanyika. Lakini pia kuna kazi muhimu kama uzalishaji na utayarishaji wa chakula, usafi na ukarabati, uburudishaji na kazi nyinginezo zinahitaji kufanyika kwenye kila jamii na ufanyaji wake utahakikisha watu wanajipatia kipato kwa kufanya kile kinachohitaji kufanywa.

Na nikiangalia tunavyoishi sasa nakubaliana na alichosema Busara, kuna fursa sawa za kazi kwa kila mkazi, vilevile kazi zinavyopungua mfano kila tukileta mashine na hivyo kupunguza huitaji wa nguvu kazi ndio inakuwa furaha yetu kama wakazi, sababu upungufu huu wa kazi unamaanisha muda wa kustarehe unaongezeka. Jambo muhimu ni malipo ya hizo kazi kuwawezesha wakazi kukidhi mahitaji yao na kubakia na pesa za ziada kwa ajili ya starehe.

Kwa ufupi wazazi wote takribani elfu ishirini wanafanya kazi chache zilizopo baada ya nyingine kufanywa na mashine. Kwa kufanya hivyo wazazi hao kila mmoja analipwa dollar mia tano. Kumbuka hapa natumia neno dollar ili iwe rahisi kuelezea, lakini hizi pesa tungeweza kuziita chochote, (voucher, credit, pesa ya mji n.k.) ukizingatia pesa hizi sio noti wala sarafu, mji wetu tunaweza kuuita kwa lugha ya kigeni (cashless) miamala yote inafanyika kielekroniki, nadhani mara ya mwisho mimi kushita noti ni pale nilivyokuwa natoka kwenye huu mji kwenda mji mwingine ilibaidi kubadilisha credit zangu nipate pesa ya huko niendako sababu hawakuwa na mfumo kama wetu.

Kwahio wazazi wote ambao ni takribani elfu ishirini kila mmoja baada ya kufanya hizo kazi chache analipwa dollar mia tano kila mwezi, hivyo kupelekea mji kuwa na gharama za kulipa mishahara (watu 20,000 x 500USD) kiasi cha dollar milioni kumi. Kwahio familia takriban elfu kumi zilizopo katika huu mji, mke na mume wote wanapata dollar mia tano, hivyo kila familia ina uwezo wa kupata dollar elfu moja kwa mwezi kwa kufanya kazi chache kadri iwezekanavyo ili kukidhi mahitaji ya uzalishaji.

Ukizingatia malipo ya nyumba ni ya muda mrefu bila riba, mahitaji yote yanapatikana mjini kwa bei nafuu, na kuna uhakika wa mafao ya uzeeni pesa hii tunayolipwa inatosha na kubaki hata baada ya kununua mahitaji ambayo sio ya lazima na starehe.

Baadhi ya kazi tunazohitaji kuzifanya hivyo kutupatia kipato sisi wakazi ni uzalishaji wa chakula, uchakataji wa bidhaa (product recycling), burudani/starehe, huduma za afya, utoaji elimu, ukarabati na usafi, uangalizi/ukarabati wa nyumba na mji.

Nakumbuka mahojiano yangu na Busara, baada ya kuniambia mji wetu utakuwa unawalipa wakazi wote kwenye kila nyumba, yaani baba na mama kila mmoja dollar 500, nilihoji kama mtu kulipwa sawa na mke wake hakutaleta mifarakano katika ndoa yao, Busara alinijibu kama mkeo anakaa na wewe sababu ya kipato chako huenda sio mwenza wako bali mfungwa wako. Niliacha hilo lipite ila nikamuuliza swali lililokuwa linanikereketa…, kwahio unamaanisha daktari atakuwa na uwezekano wa kulipwa sawa na… na…

Mchimba Makaburi? Alijibu Busara kwa dhihaka.

Nilijibu kwa hasira, hivi unadhani unaweza kuvutia vipaji kwa kuwalipa sawa na… na…

Kwanza kabisa kwanini kuwe na mchimba kaburi na sio mtu mwenye ujuzi tofauti wa kuweza kuchimba kaburi, kunyoa nywele, kufundisha kile anachoweza kufanya, kupika, kuzalisha chakula, kufanya kazi viwandani n.k. Yaani kwa ufupi mtu anayeweza kufanya kazi tofauti zilizopo.

Nilianza kukubaliana na Busara ni kweli mzee mchimba kaburi anayechimba kaburi pekee ataanza kuombea watu wafe zaidi ili aweze kujipatia kipato.

Busara aliendea…, Pili, kama tuna daktari bingwa wa upasuaji katika kipindi ambacho hakuna wanaohitaji upasuaji, kwanini asifundishe wengine au kufanya kazi zilizopo kwa wakati huo? Hata kama mji wetu utakuwa hauna daktari wa upasuaji tunaweza tukamkodi kutoka nje ya mji kuja kufanya upasuaji wa mara moja kwa malipo ya mara moja bila faida nyingine ambazo angezipata kama angekuwa mkazi wa mji. Lakini nina uhakika chochote ambacho atakuwa analipwa huko nje hakitalingana na faida ambazo angezipata kama angekuwa mkazi wa mji, yaani nyumba ya makazi, huduma za afya, mafao ya uzeeni, bei nafuu za bidhaa na muda mchache wa kufanya kazi kadri inavyowezekana hivyo kupelekea kupata muda mwingi wa starehe.

Niliendelea kuuliza utapangaje muda wa kazi na nani afanye nini na saa ngapi?

Busara aliendelea kwenye karne hii ya sayansi na teknolojia kuna kazi ambazo hazihitaji watu bali computer na mashine zinaweza kuzifanya kwa ufanisi, kazi hizo ni pamoja na uhasibu, ulipaji mishahara, upangaji kazi n.k. Kwanza kabisa mji wetu utakuwa hautumii pesa yaani miamala yote itafanyika kidigitali. Mfano kama Bakari akilipwa mshahara itajulikana na kila akitumia mshahara wake itakuwa inajulikana ametumia wapi saa ngapi na kiasi gani kwa kufanya hivyo kutahakikisha kwamba hakuna mambo ya rushwa wala upotevu wa pesa.

Kuhusu kupanga muda wa kufanya kazi itakuwa rahisi, kumbuka masaa yatakayohitajika ili kufanikisha uzalishaji na mahitaji ya mwezi husika yatakuwa yanajulikana, na idadi ya wanaotaka kufanya kazi kwa mwezi huo itakuwa inajulikana pia. Kwahio hayo masaa machache ya kazi zilizobaki baada ya nyingine kufanywa na mashine yatagawanywa kwa watu wote wanaohitaji kazi, hii itahakikisha watu wanafanya kazi muda mchache kadri inavyowezekana.

Ingawa kuna kazi ambazo zinategemea maeneo husika na zinaweza kufanywa kwa ufanisi zaidi sehemu nyingine mfano kuna mazao yanategemea mazingira na hayawezi kustawi sehemu zote, kwahio kwa zile bidhaa ambazo kutakuwa na ufanisi zaidi kutengenezwa sehemu nyingine zitakuwa zinazalishwa sehemu hizo na kama mji utazihitaji utakuwa unazinunua kwa bei ya jumla.

Ila kuna baadhi ya kazi na huduma ambazo zinaweza kutengenezwa kwenye kila mji ili kuhakikisha watu wanapata kipato, kuongeza ufanisi na kupunguza gharama za usafirishaji. Baadhi ya kazi hizo ni kama; Ufundishaji na Kuongezea watu Ujuzi, Uzalishaji wa Chakula, Uchakataji wa Bidhaa (product recycling), Ukusanyaji wa Nishati (Jua, Gesi Asilia/Biogas n.k.), Kuburudisha na Kustarehesha, Huduma za Afya, Kupendezesha na mambo ya Mitindo, Ukarabati wa Nyumba na Mji, Usafiri na Usafirishaji.

Nakumbuka kuna siku wakati tunaongelea mambo ya ajira na kazi, Busara aliniuliza, Hivi kwanini tunafanya kazi?

Binafsi nafanya kazi ili nipate pesa ingawa kuna vitu navifanya kama burudani ambavyo kwa macho ya wengine wanaweza kuviona kama ni kazi, nilijibu huku namshangaa kwanini anauliza swali ambalo jibu analo.

Busara aliniangalia kwa dakika kama tatu alafu akasema, nadhani pesa ni kiwezeshaji na si vinginevyo, Je unaweza ukala pesa zako ?, Unaweza kuzivaa?, Zinaweza kutibu magonjwa yako?

Ahh Mzee najua pesa haziwezi kufanya hayo ila pesa ndio inaniwezesha kupata mahitaji yangu, au tuseme zinatakiwa kuniwezesha, ningependa kwa kipato ninachopata niweze kumudu kupata nyumba, chakula, mavazi, elimu kwa watoto wangu na madawa pindi ninapougua, sitaki mengi, kwangu mimi hayo yangetosha.

Busara aliendelea… ni kweli wewe binafsi hayo ndio yanakufanya ufanye kazi ili upate pesa, ila kwa jamii kukidhi mahitaji ya watu ndio jambo la muhimu, ukizingatia sio kila njia ya kujipatia kipato zina faida kwa jamii, unaweza ukapata pesa nyingi sana kwa kuwauzia madawa ya kulevya mateja, lakini kwa gharama ipi ?

Ni kweli mzee pia unaweza ukapata faida ya muda mfupi kwa kuharibu na kuchafua mazingira, au kugombanisha mataifa tofauti ili uwauzie silaha, kama mataifa mengine yanavyotufanyia.

Ni kweli kijana, kwahio kwa macho ya jamii ni vema watu wapate kipato, ila kipato hicho kiwe kwa njia sahihi zenye manufaa ya jamii, njia zitakazowatengenezea utajiri wao na vizazi vyao vijavyo bila athari yoyote.

Nakumbuka kama vile ilikuwa jana, Busara alivyoniambia aina Tisa za kazi ambazo mji wetu lazima uwe nazo ili kuhakikisha kila mkazi anajipatia kipato.
 
KAZI YA KWANZA: ELIMU (Kutoa Mafunzo, Kuongezea Watu Ujuzi / Mafunzo Kazini)

Ili wakazi wa mji waendelee kuwa na uwezo wa kufanya kazi zilizopo wanahitaji kuwa na ujuzi wa kufanya vitu mbalimbali, mji wetu umehakikisha kila mtu anapata fursa ya kuongezea ujuzi wake kila pale inapobidi ili aweze kuendelea kufanya kila kinachotakiwa kufanyika.

Kwenye mji wetu wa takribani watu elfu hamsini kuna wanafunzi kama elfu ishirini tokea chekechea mpaka chuo kikuu, ili kuhudumia namba yote hio kuna miundombinu ya chuo na mashule. Ingawa tulianza na mashule ya mahema na waalimu kama watatu sasa hivi tuna chekechea mpaka chuo kikuu kwenye majengo ya kisasa.

Mji unatoa ajira za muda kulingana na mahitaji kwa wakufunzi mbalimbali na zaidi ya mafunzo kutoka kwa wakufunzi kuna zamu za wanafunzi kutembelea kazi tofauti tofauti kwenye mji ili wapate mafunzo kwa vitendo. Hii ni kuhakikisha vijana hawa wakihitimu wanakuwa wameiva na wana uwezo wa kufanya kazi zote zilizopo katika mji. Hii imepelekea vyuo vyetu kuzalisha wahitimu wenye ujuzi unaotakiwa na sio vijana ambao hawana cha kujivunia zaidi ya vyeti na madeni lukuki ya mikopo ya elimu.

Watoto wote katika mji wana uhakika wa elimu, na kila mkazi anafursa ya kuongezea ujuzi wake.

Ili kuchangia elimu watoto ambao sio yatima wazazi wao wanakatwa kwenye mapato yao ya mwezi jumla ya dollar mia moja kwa kila mwanafunzi, hivyo kwa hesabu ya sasa ya wanafunzi takriban elfu 20 mji unakusanya kila mwezi dola milioni mbili.

Tulijua kuanzia mwanzo na Busara alikuwa ananikumbusha kila mara, kuwekeza kwenye watu ni muhimu sana kama jamii husika inataka kuvuna faida ya milele… hivyo chaguo ni letu aidha tunawekeza mapema mara moja au tunagharamika milele kwa kutoa misaada na kutegemea hisani za wengine.

Haya yote nilikuwa nayawaza huku natembelea mazingira ya chuo na kuangalia maabara, maktaba na majengo mengine ya chuo…, chuo ni cha kisasa na tunategemea sana teknolojia, vitabu karibia vyote vipo kwenye mtandao na kila anayetaka anaweza kusoma, mafunzo yanatolewa kwa njia zote, kwa kuangalia video, kusikiliza kwenye redio na kusoma kwenye maandiko. Kila masomo anayotoa mwalimu yanarekodiwa ili mwanafunzi yoyote kwa muda wowote anaweza kurudia kuangalia ni nini kilisemwa, hata yule kwa namna moja au nyingine aliyekosa kipindi au anataka afanye marudio, anaweza kuangalia video za marudio.

Vijana, wakufunzi na wakazi wote wanahamasishwa kujiendeleza na kuongeza uelewa…, kila mtu anaelewa elimu haina mwisho, na chochote kile kinaweza kuboreshwa. Mtu yoyote au sekta yoyote yenye tatizo inaweza kuorodhesha changamoto wakati wowote ili ziweze kufanyiwa kazi na kupatiwa ufumbuzi. Hivyo hii sekta ya elimu ni nguzo kuu ya kutatua changamoto za jamii mbali na kuelimishana.

Wakati natoka kwenye maeneo ya chuo namwona daktari mmoja kutoka magharibi ya mbali, alikuwa amekuja mjini kwetu kupumzika na kufanya uchunguzi kuhusu mazao na aina tofauti za mbegu, tulikuwa tunapata maombi ya wageni kama hawa kwa wingi, walipenda mandhari ya utulivu na fursa za kuweza kufanya uchunguzi wa mambo mbalimbali huku wakijua fika watapewa ushirikiano.

Kutoka kwenye ile shule ya hema na waalimu watatu mpaka sasa tuna majengo ya mashule mpaka chuo na idara ya uchunguzi na maendeleo katika chuo chetu inayotatua kero na changamoto zetu…, kweli tumetoka mbali.
 
KAZI YA PILI; Uzalishaji wa Chakula
Hii ndio ilikuwa kazi mama iliyoanzishwa kwenye kijiji chetu ambacho sasa ni mji, nakumbuka yale mabanda yetu ya kufuga kuku wa nyama na mayai na baadae kuongezea ng’ombe na mifugo mingine. Sehemu hii kwa sasa ambayo ni sehemu ya viwanda ina majengo mengi ya mifugo tofauti tofauti na karibu na haya mabanda kuna mtambo wa kubalisha mabaki ya uchafu wa mifugo na mabaki mengine kutoka vyanzo mbalimbali ili kutengenezea gesi asilia na mbolea.

Ukiondoa yale mazao ambayo yanahitaji sehemu maalumu ili yastawi, mazao mengi yanaweza yakalimwa ndani ya majengo (greenhouses au sehemu yoyote ile).

Sababu tunajua mahitaji yetu ya chakula kwa siku, mwezi hadi mwaka, mazao ambayo hatuzalishi na tunahitaji kuyanunua huwa tunanunua kwa bei ya jumla nyakati za msimu wa hayo mazao na kuyahifadhi kwa mahitaji ya muda mrefu. Kwasababu ya kununua mazao mengi kwa wakati mmoja huwa tunapata bei nafuu sana ukizingatia tunanunua wakati wa msimu ambapo bei ni za chini.

Mazao mengine kama mbogamboga, na yale yote ambayo yanaweza kulimwa kwenye greenhouses yanalimwa ndani ya mji. Kilimo chetu kwa lugha ya kigeni kinaweza kuitwa (intensive farming) yaani mazao mengi kadri inavyowezekana yanalimwa katika sehemu ndogo iwezekanavyo. Ingawa kilimo hiki kinaweza kuleta madhara ya mazingira hususan kwenye mifugo kwa kuzalisha uchafu mwingi kwa wakati mmoja, (Concentrated Animal Farming) lakini sababu uchafu na mabaki hayo yanatumika kutengeneza gesi asilia na baadae mbolea mwisho wa siku kilimo na ufugaji huu ni faida sana kwetu.

Mahitaji yetu yote ya mboga, nyama na maziwa tunazalisha wenyewe hivyo kujitosheleza kwa chakula, kupata gesi asilia na mbolea vyote ambavyo vinatumika kwenye mji wetu.

Mwaka juzi, baada ya kupata faida kubwa mwaka hadi mwaka na kumalizia kulipia madeni ya kampuni zilizosaidia katika ujenzi wa nyumba za makazi, maofisi, mahoteli n.k. tuliamua kuanza ufugaji wa samaki ndani ya ghala (warehouse fish farming). Aina hii ya ufugaji wa samaki inapunguza sana uharibifu wa mazingira, kuepusha kuambukiza magonjwa vizazi vya samaki, kuchafua vyanzo vya maji kwa madawa n.k.

Kwa kufuga samaki kwenye hili ghala, tunahakikisha maji hayapotei bali yanatumika tena na tena (recycling), vilevile hakuna uchafu wowote unaotupwa (waste disposal) bali uchafu wote wa samaki unatumika kama mbolea kwenye mazao.

Tangia tuanze kufuga samaki tumeongeza aina za vyakula kwa watumiaji ambao sasa wana uhakika wa kupata samaki kwenye mlo wao, wakati hapo kabla tulihitaji kununua toka sehemu nyingine.

Kabla ya kuanza ufugaji huu tulifanya uchunguzi wa kampuni kubwa ya ufugaji wa samaki aina ya sato, kampuni hii inaitwa Blue Ridge Aquaculture, hawa ni wazalishaji wakubwa wa samaki aina ya sato, ingawa na sisi tumejifunza kutoka kwao nadhani siku si nyingi tutakuwa na uwezo wa kuzalisha kama wao. Blue Ridge wanahakikisha maji yanayotumika baada ya kuchafuliwa na samaki yanasafishwa kwa kuondoa uchafu, kuongezewa oxygen na vijidudu kuuliwa, mfumo huu unahakikisha hakuna hitaji kubwa la maji masafi wala hautengenezi maji taka.

Kila mwaka kampuni ya Blue Ridge Aquaculture inatoa kilo kama milioni mbili za samaki, kwa siku wanasafirisha kati ya kilo 5,000 mpaka 10,000, na haya yote yanafanyika kwenye eneo la ekari 2.3 na kutoa ajira kwa watu thelasini na tano tu.

Unaweza kuona watu 35 ni wachache sana kwa mji wa watu elfu ishirini wanaohitaji kipato, ila utakumbuka kwamba malengo sio kufanya kazi nyingi iwezekanavyo bali ni kuwa na kazi chache iwezekavyo…, na kazi hizo zifanywe na wote kwa muda mchache ili kila mkazi abaki na muda mwingi iwezekanavyo kwa starehe. Yaani kuanzia mwanzo malengo ya huu mji yalikuwa ni kufanikisha mahitaji ya watu kwa muda na nguvu kazi chache kadri iwekanavyo.

Hili limewezekana sababu ya ufanisi wa mji na matumizi ya mashine na teknolojia kila inapowezekana

Pia tuna uhusiano mzuri na wa karibu sana na watu wa Uholanzi. Hawa wenzetu wana aina ya kilimo ambacho kwa lugha ya kigeni kinaweza kuitwa kama (precision farming). Hawa ndugu zetu waholanzi wameweza kutoa mara mbili ya zao la viazi ulaya (yaani wakati wengine wanapata kama tani 9 kwa eka, hawa jamaa wanatoa zaidi ya tani 20 kwa eka), zaidi ya hayo wakulima wao wengi wameweza kupunguza mahitaji ya maji kwenye mazao mengi kwa zaidi ya asilimia 90, wamepunguza na wengine kuacha matumizi ya madawa ya kemikali kwenye vitalu na tangia 2009 wafugaji wao wamepunguza matumizi ya madawa kwa mifugo yao zaidi ya asilimia 60. Haya yote wameweza kuyafanya sababu ya uchunguzi wa muda mrefu kwenye taasisi zao, jambo ambalo hata sisi katika chuo chetu, wanafunzi na wakufunzi wanafanya.

Niliangalia mashamba haya ya greenhouses na majengo ya mifugo na jengo kubwa kwa mbali la ufugaji wa samaki, nilikumbuka kuwa hapo awali hapa kulikuwa na banda la kuku na majengo madogo ya sisi kuishi, kweli tumetoka mbali.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom