RIWAYA: Kesho iliyoondoka (Gone Tomorrow)

RIWAYA: Kesho iliyoondoka (Gone Tomorrow)

SEHEMU YA NANE

Theresa alitoa karatasi moja na kuigeuza upande ambao ninaweza kuisoma kabla ya kunipatia. Ilikuwa imeandikwa kwa mkono majina ya mashahidi. Yalikuwa ni majina manne. La kwangu, jumlisha Rodriguez, Flrlujlov na Mbele.

“Abiria wanne.” Alisema.

Nilianza kuongea, “Mimi nilikuwemo kwenye treni na niliwahesabu. Nina uhakika kulikuwa na abiria wangapi.”

Halafu nikaanza kuliangalia tukio kwenye kichwa changu. Namna tulivyoshuka kwenye treni, tukiwa tunawasubiria askari. Na mimi ndiye nilikuwa wa kwanza kukamatwa.

“Labda jamaa alitoroka.” Nilisema.

Dochery alisema, “Huyo jamaa ni nani?”

“Jamaa tu. Hakuna cha zaidi kwake, ila alionekana tu sio maskini.”

“Waliwasiliana kwa namna yeyote na marehemu?”

“Hilo sikuona.”
“Yeye ndiye alimpiga risasi huyo mwanamke?”

“Hapana. Yule mwanamke alijipiga mwenyewe.”

“Basi huyo jamaa hana umuhimu wowote. Labda hataki kuhusishwa na hili sakata kuepusha ugomvi na mke wake muda kama huu alikuwa anatokea wapi kupanda treni. Haya mambo yanatokea sana.”

“Jamaa ametoroka, lakini mnamwacha aende na sababu mnamtengenezea ila mmenikamata mimi?”

“Si umekiri mwenyewe kuwa hakuhusika?”

“Na mimi pia sikuhusika.” Nilijibu.

“Hayo umesema wewe.”

“Kwahivyo unaamini ushuhuda wangu kuhusu mtu mwingine, ila hauamini ushuhuda wangu kuhusu mimi mwenyewe?” Halafu nikaongeza, “Hapa tunapotezeana muda.”

Na ni kweli tulikuwa tunapotezeana muda, halafu nikagundua kitu. Nikagundua Theresa na Dochery walikuwa wananifanyia huruma fulani. Hili jambo lote lilikuwa limepangwa.

Kuna zaidi ya kinachoweza kuonwa kwa macho.

Niliongea, “ Huyo mwanamke alikuwa ni nani?”

“Kwani lazima awe nani?” Theresa aliongea.

“Kuna sikielewi. Najua kuna mtu kawaambia mniweke hapa hadi afike. Ndiyo maana hakuna mnachokifanya zaidi ya kuniweka hapa na huu upuuzi wenu.”

“Kusema kweli upo sahihi.”

“Kwahivyo huyu msichana alikuwa ni nani?”

“Inavyoonekana alikuwa anaifanyia kazi serikali. Na hapa kuna bwana mmoja wa F.B.I yupo njiani anakuja kuzungumza na wewe.”

Walipomaliza kuniambia hivyo walinyanyuka na kuniacha peke yangu. Chumba chenyewe kilikuwa kipo sawa tu. Kulikuwa na meza na viti vitatu. Viwili kwaajili ya maafisa na kimoja kwaajili ya mhojiwa. Wakati mwingine ni vigumu kutabiri nini humtokea mtu anayewekwa kwenye chumba kisichokuwa na madirisha.

Nilianza kuhesabu muda kwenye kichwa changu. Saa la kwanza likapita, na la pili. Hawa watu waliokuwa wanakuja kuniona lazima walikuwa wanatokea D.C. Niliacha kufikiria nikainua miguu yangu kwenye meza na kusinzia.

Alfajiri ya saa kumi na moja, jamaa watatu wakiwa ndani ya suti nyeusi walikuja na kuniamsha. Walikuwa na nyuso za upole. Suti zao zilikuwa ni za gharama. Nywele zao ilionesha wametoka kuzinyoa siku sio nyingi. Niliomba kuona vitambulisho vyao, lakini walinisomea sherfia moja kuwa walikuwa hawaruhusiwi kujitambulisha. Nilianza kufikiria kuwasumbua, lakini ni kama waliyasoma mawazo yangu na kunipatia mstari mwingine ambao ulinipatia picha moja tu, kwamba endapo ningeleta usumbufu kuna matatizo makubwa yalikuwa yananisubiria mwisho wa barabara. Kusema kweli mimi ni muoga wa vitu vichache sana, lakini kwa vitimbwi vya leo, ilinipaswa niwe mpole. Kwahivyo niliinua mabega juu na kwaambia waendelee na maswali yao.

Walianza kwa kusema walikuwa wanatambua rekodi yangu ya jeshi na walikuwa wanaiheshimu pia. jambo ambalo lilimaanisha walikuwa wananipaka mafuta kwa mgongo wa chupa au wao pia walikuwa ni askari wa wanajeshi. Na hakuna mtu anamheshimu askari wa wanajeshi isipokuwa askari wa wanajeshi mwenzake. Halafu wakaniambia watakuwa wananiangalia kwa ukaribu sana kujua kama nilikuwa nasema uongo au naongea ukweli. Ambao nao ulikuwa ni uongo mtupu. Kwasababu ni wachache kati yetu tunaoweza kufanya hivyo, na kama wao wangekuwa ni wazuri kwa kiwango hicho basi wangekuwa wapo nyumbani wamelala kuliko kuwa hapa asubuhi hii na mapema.

Lakini sikuwa na jambo lolote la kuficha, hivyo niliwaambia waendelee na maswali yao.

Walikuwa na maeneo matatu makuu waliyotaka kujua. Kwanza: Je, Nilikuwa nafahamiana na yule mwanamke aliyejiua? Nilikuwa nimewahi kuonana naye hapo kabla?

Niliwajibu, “Hapana.” Jibu fupi na tamu, kwa utaratibu ila kwa mkazo pia.

Hawakufuatisha maswali. Jambo ambalo liliniambia wao walikuwa ni akina nani haswa. Walikuwa ni timu B ya mtu fulani. Walikuwa wametumwa kwa kazi moja ya kufunga uchunguzi wa jambo lililokuwa linaendelea. Walikuwa wanazika kila kitu. Walikuwa wanataka jibu hasi kwenye kila swali walilokuwa wananiuliza, ili faili lifungwe na jambo lizikwe kabisa. Basi.

Swali la pili lilikuwa: Je, nilikuwa namfahamu mwanamke anayeitwa Lila Hoth?

Nilijibu, “Hapana,” Kwa sababu ni kweli nilikuwa simjui. Kwa wakati huo.

Swali la tatu lilileta mjadala kidogo. Aliyeliuliza alikuwa ni kiongozi wao. Alikuwa mzee kidogo. Pengine na mwenye akili kuliko wale wengine. Alianza kwa kusema, “Ulimfuata yule mwanamke kwenye treni.”

Sikusema neno lolote. Nilikuwa pale kujibu maswali, na sio kutoa hoja zangu kwenye maoni yake.

“Ulimsogelea kwa ukaribu kiasi gani?”

“Futi sita,” Nilijibu. “Umbali wa kuweza kupokea au kutoa kitu kwa mtu.”

“Ulimsogelea kwa ukaribu wa kuweza kumgusa?”

“Hapana.”

“Kwa mfano angenyoosha mkono wake, na wewe ukafanya hivyo pia, mngeweza kugusana mikono?”

“Labda,” Nilijibu.

“Nichukulie jibu lako kama ndiyo au hapana?”

“Lichukulie kama labda. Ninaufahamu urefu wa mkono wangu. Lakini sifahamu urefu wa mikono ya yule mwanamke.”

“Sawa. Je, alikupatia kitu chochote?”

“Hapana.”

“Je, ulichukua kitu chochote kutoka kwake alipokufa?”

“Hapana.”

“Je, kuna mtu mwingine labda alichukua kitu chochote kutoka kwake.”

“Sikuona hilo tukio.”

“Uliona labda akiangusha kitu chochote kutoka kwenye mkono, kwenye begi, au kwenye nguo zake?”

“Hapana.”

“Je, alikuambia jambo lolote?”

“Hakuna cha maana alichoniambia.”

“Je, aliongea na mtu mwingine?”

“Hapana.”

Yule mwanaume akatulia kidogo kabla hajaniambia, “Kama hautojali, toa mifuko yako ya suruali.”

Nilikubali. Sikuwa na kitu au jambo lolote la kuficha. Nilitoa mifuko yangu yote na kuweka kila kilichokuweko mfukoni juu ya ile meza. Kulikuwa na kiasi kidogo cha pesa zilizokunjwakunjwa. Passport yangu kuukuu. ATM card na mswaki wangu wa kukunja. Na business card ya Theresa Lee.

Yule mwanaume akakagua vitu vyangu kwa kidole kimoja na kutikisa kichwa chake kama ishara ya kuwaambia vijana wake wasogee kunikagua vizuri. Walinikagua kwa umakini bila kupata kitu chochote,

Yule bwana akasema, “Asante, bwana Kichaka.”

Halafu wakatoka nje wote watatu. Nilishangazwa kidogo, lakini pia nilifurahi. Niliweka vitu vyangu mfukoni na kuelekea ulipo mlango nitoke nje. Nilimuona Theresa akiwa kwenye dawati lake. Halafu Dochery alikuwa anaongea na bwana mmoja ambaye alionekana amechoka usoni kwa kukosa usingizi. Theresa aliniona nilivyokuwa nimemkazia macho yule mwanamume.

“Huyo ni kaka yake na yule mwanamke.” Theresa aliniambia. “Tulizipata namba kwenye waleti ya marehemu tukampigia aje. Yeye pia ni askari polisi.”

“Maskini.”

“Tumemshauri asihangaike kuutambua mwili maana una hali mbaya sana. Tumemshauri achukue tu jeneza. Na ameelewa.”

“Kwahivyo mna uhakika ni dada yake?”

“Tumechukua alama za vidole.”

“Kwani alikuwa ni nani haswa?”

“Siruhusiwi kusema.” Theresa alinijibu.

“Kwahivyo mimi naruhusiwa kuondoka?”

“Kwani wale wamemalizana na wewe?”

“Nadhani.”

“Basi wewe nenda tu.”

Nilipiga hatua kadhaa hadi kwenye ngazi ya kutokea halafu akaniita. Nilipogeuka akasema, “Niliposema wewe ndiyo chanzo cha kifo chake sikuwa ninamaanisha.”

“Ulimaanisha.” Nilisema. “Na unaweza ukawa ulikuwa upo sahihi.”

Niligeuka na kuanza kupiga hatua za kuondoka. Nilipokunja kona ya mtaa wa 35 nikajiambia hapa umemaliza. Upo huru. Lakini kumbe sikuwa huru. Kwenye kona hiyohiyo niliyokunja, kulikuwa na mabwana wengine wanne wanasubiria kuongea na mimi. Walikuwa wanafanania kama wale niliomaliza kuongea nao, ila hawa suti zao zilikuwa ni ghali mno.
 
THE SPIRIT THINKER.
SEHEMU YA TISA

Labda nikuambie kitu, Dunia yetu ni kama pori moja kubwa hivi, lakini New York ni msitu. Hivyo, ukiona wanaume wanne walioshiba wamesimama kukusubiria wewe, kuna mambo mawili ya kufanya. Moja, ukimbie kurudi ulipotokea kwa kasi ya ajabu sana au uendelee kutembea kuwafuata waliposimama - kama vile hauna wasiwasi au uoga.

Na ukweli ni kwamba jambo zuri na ambalo litafanywa na mtu yeyote mwenye akili ni kukimbia, lakini mimi sijawahi kusema mahala popote kuwa nina akili sana. Hivyo niliendelea kutembea kuelekea walipokuwa wale wanaume.

Suti zao zilikuwa za rangi ya bluu na mionekano yao ilionesha walikuwa ni wanaume wa kazi. Wanaume wanaojua mambo ya ulimwengu. Aina ya wanaume ambao walikuwa tayari kuvunja na kuipindisha sheria ili watimize malengo yao.

Walijigawa katika vikundi vya wawiliwawili nilipokaribia takribani hatua nne kutokea walipokuwa wamesimama. Wakaniachia nafasi ya kupita katikati yao, kama ningehitaji, lakini jamaa mmoja wa mbele akapunga mikono yake kuashiria nisimame. Ilikuwa ni ama nisimame au nipite kwa kasi. Na kwa wakati huo nilikuwa na uwezo wa kufanya lolote kati ya chaguzi hizo mbili. Ningeweza kusimama au kuendelea kutembea. Na kama wangejifanya kunizuia wangejikuta wamechakazwa ghafla.

"Tunaweza kuzungumza kwa dakika kadhaa?" Kiongozi wao alisema.

Nikasimama na kumjibu, "Kuzungumza kuhusu nini?"

"Wewe ulikuwa shahidi kwenye hili tukio la treni?"

"Na nyie ni akina nani?"

Yule mwanaume alijibu kwa kuingiza mkono wake kwenye mfuko wa koti la suti yake, hivyo niligundua hakuwa na bunduki wala silaha yeyote. Alipoutoa mkono alitoka na business card. Kwa juu ilikuwa imeandikwa: Sure and Certain Inc. Mstari wa pili ulisema: Protection and Investigation. Mstari wa tatu ulikuwa na namba ya simu iliyoanza na 212. Namba ya Manhattan.

"Marekani ipo mbele sana kwenye teknolojia," Nilianza kuongea na kuongeza. "Sitashangaa kuona kadi zimeandikwa Nelson Ntimba, Mfalme wa dunia."

"Hii kadi ni ya kweli," Yule jamaa alijitetea.

"Mnamfanyia nani kazi?"

"Haturuhusiwi kusema."

"Basi sitoweza kuwasaidia."

"Ni bora uongee na sisi kuliko mkubwa wetu..."

"Duh! Mmeanza kunitisha." Nilitania.

"Tuna maswali machache tu. Tunaomba utusaidie kuyajibu kwasababu tunachofanya ni kazi kama wewe unavyofanya kazi ili upate chochote."

"Mimi sifanyi kazi yeyote. Nipo nakula tu maisha."

"Basi tuonee huruma utusaidie."

"Maswali gani mnayotaka kujibiwa?"

"Alikupatia kitu chochote?"

"Nani?"

"Unafahamu tunamzungumzia nani. Je, alikupa kitu chochote?"

"Swali jingine?" Nilisema.

"Kuna kitu alikuambia?"

"Niliongea naye mambo mengi tu. Kutokea Bleeker mpaka mwisho wa stesheni tulikuwa tunaongea."

"Alikuwa anasema nini?"

"Sikuwa hata namsikiliza kwa makini."

"Haukumbuki hata ujumbe mmoja?"

"Sikusikia ujumbe wowote."

"Alikutajia jina lolote labda?"

"Nadhani, ila silikumbuki."

"Alitaja Lila Hoth?"

"Hapana."

"John Sansom?"

Sikujibu. Yule mwanaume akauliza tena, "eti?"

"Nimewahi kulisikia hilo jina pahala fulani."

"Kutoka kwa yule mwanamke?"

"Hapana."

"Je, alikuonyesha kitu chochote?"

"Kitu? Kama nini?" Nilihoji.

"Kitu chochote tu."

"Kwanini mnauliza?"

"Mkubwa wetu anataka kujua."

"Mwambieni aje kunihoji yeye mwenyewe."

"Ni bora uzungumze na sisi."

Nilitabasamu na kuanza kutembea kuondoka kuupita uwazi waliokuwa wameuacha. Lakini mmoja wao alijitokeza na kujaribu kunisukuma nirudi. Nilimshika bega kwa nguvu na kumsukuma kabla hajafanya alichokusudia. Hapo nilimuona anapepesuka kidogo halafu alipotulia akarudi tena. Sasa hivi niliinama kumkwepa na kujipitisha nyuma yake na kumgonga kiwiko mgongoni. Akiwa bado hajatulia niliushika mkoti wa suti yake kwa nyuma na kuurarua halafu nikamsukuma tena.

Nikapiga hatua tatu kwenda mbele kabla sijageuka. Ingekuwa jambo zuri kuendelea kutembea, lakini waliosema kinga ni bora kuliko tiba hawakuwa wajinga.

Wale wanaume wawili walikuwa wameshtushwa. Hawakuwa wakitegemea ningefanya nilichokifanya. Na wote wanne walikuwa na wakati mgumu wa kuamua - walitamani wafanye jambo, lakini hapa tulipokuwepo ilikuwa ni katikati ya mtaa wa 35 majira ya alfajiri. Polisi wangekuwa doria. Hakuna ubishi juu ya hilo, hivyo waliishia kuniangalia kwa hasira tu na kuondoka wakiniacha nimesimama palepale. Walikata kona ya kwanza na kupotelea kwenye macho yangu.

Upo huru.

Lakini kumbe bado sikuwa huru. Nilipogeuka na kuanza kutembea, ghafla akatokea mwanaume mwingine akinikimbilia. Alikuwa ni yule mwanaume niliyemuona na Dochery mule kituoni. Kaka yake na yule mwanamke aliyejifyatua risasi kwenye treni. Aliponifikia akaniambia jambo jingine. Kwamba dada yake hakuwa amejiua, alikuwa ameuliwa na watu!





TUENDELEE BAADAE TENA.
 

SEHEMU YA KUMI

Labda nikuambie, zamani za kale niliwahi kupelekwa kwenye kozi fupi huko Dodoma kujifunza kuhusu hisia za watu ambao wamepoteza wapendwa wao. Kuna muda nilipokuwa mtumishi ilitakiwa sisi askari tufikishe taarifa mbaya kwa ndugu na jamaa.

Tulikuwa tunaziita taarifa za vifo. Na kusema kweli mimi sikuwa najua namna ya kutoa taarifa hizi kwa ndugu. Ningemwendea tu na kumwambia bila kuuma maneno. Nilikuwa nadhani hivyo ndivyo taarifa ilipaswa kutolewa. Lakini kumbe nilikuwa nakosea. Kwahivyo nilipelekwa Dodoma kwaajili ya kufundishwa namna sahihi ya kutoa taarifa mbaya kwa mtu. Huko nilijifunza mambo mengi sana. Nilijifunza kujali hisia za watu wengine. Na kubwa zaidi nilijifunza hakuna mazingira mazuri ya kumpatia mtu taarifa mbaya kama migahawa na hoteli.

Ingawa nilihitaji chakula pia, lakini sikuagiza kwasababu mgeni wangu hakuagiza. Ingeonekana kama utovu wa nidhamu. Kwahivyo nilikaa tu kimya na kusubiri. Waache waanze kuongea wao, ndiyo moja kati ya sheria nyingi alizotupatia mwalimu wetu kule Dodoma.
Alianza kwa kuniambia jina lake lilikuwa ni Jacob Marky. Babu yake alikuwa anahusika kwenye biashara ya ujenzi. Aliniambia ninaweza kumuita Jake. Na mimi nilisema anaweza kuniita Kichaka. Aliniambia alikuwa ni askari. Na mimi nilimwambia kwa wakati mmoja niliwahi kuwa askari pia, wa wanajeshi lakini. Aliniambia hajaoanna anaishi peke yake. Nilimwambia hali yangu kwenye mahusiano ni kama ya kwake tu.

Alivuta pumzi ndefu na kuniambia jina la dada yake lilikuwa ni Susan Mark. Ingawa kuna kipindi aliitwa kwa jina la Susan Molina, ila walipoachana na mumewe akaacha kutumia hilo jina. Alimuongelea dada yake huyo katika wakati uliopo. Alikuwa mbali sana na kuukubali ukweli uliotokea.

"Dada yangu hakujiua. Haiwezekani." Alisema.

"Jake, Mimi nilikuwepo wakati wa tukio."

Mhudumu alileta kahawa tuliyokuwa tumeagiza na tukapiga funda kadhaa. Tukiuacha muda uruhusu ukweli ukubalike kwetu sote.

"Basi niambie nini kilichotokea?"

Nilimuuliza, "Wewe unatokea wapi?"

Alinitajia jina la kijiji kimoja kilichopo mashariki mwa New Jersey. Alipomaliza nilimuuliza kama anaifahamu orodha ya tabia za mtu anayetaka kujitoa mhanga. Alinijibu baada ya shambulio la Twin Towers kila askari ilikuwa ni lazima ajifunze hii orodha.

Nilianza kuongea, "Dada yako alikuwa anaonesha tabia ya ajabu sana. Kila kitu alichofanya kilimuashiria alikuwa anataka kujitoa mhanga."

"Ujinga mtupu," Aliiongea kama kaka anayejali.

"Kiukweli hakuwa na lengo la kujitoa mhanga," nilimjibu na kuongeza. "Lakini kwa mujibu wa ile orodha alikuwa anaonekana hivyo."

"Kwahivyo lengo lake lilikuwa ni kutoa uhai wake?"

"Ndiyo inavyoonekana kwa sasa."

"Mbona hakuwa kuonesha kama hana furaha na maisha yake?"

"Labda hakukuambia tu."

Hapa hakujibu kitu. Tulikaa hivyo muda ukaendelea kusonga. Watu wakaingia na kutoka mgahawani humo. Bili zikalipwa na chenchi zikaachwa.

Nilianzisha mazungumzo tena, "Embu niambie zaidi kuhusu dada yako."

"Alitumia bunduki aina gani kujipiga risasi?" Aliniuliza.

"Ilikuwa ni Ruger speed-six toleo la zamani kidogo." Nilijibu.

"Hiyo aliirithi kutoka kwa baba."

"Okay. Alikuwa anaishi wapi hapa New York?"

Alitikisa kichwa kukataa, " Alikuwa anaishi Virginia."

"Ulikuwa unafahamu labda kwanini alikuja huku?"

Jake alitikisa kichwa chake tena.

"Kwanini sasa alikuwa amevaa koti kubwa kiasi kile?"

"Sifahamu." Alijibu.

Nilisema, "Kuna bwana mmoja wa FBI kanifuata na kuanza kunihoji maswali. Halafu kabla sijakutana na wewe kuna hawa mabwana nao wamenifuata wananiuliza maswali. Wote wametaja jina Lila Hoth, umewahi kusikia hilo jina?"

"Hapana."

"Na jina John Sansom?"

"Huyo jamaa ni Congressman kutokea North Carolina. Anataka kuwa Seneta."

Nilikubali kwa kichwa. Ulikuwa ni msimu wa uchaguzi na hilo jina nilikuwa nimelisoma kwenye gazeti mahali fulani. Kwamba Sansom alikuwa ni mfanyabiashara aliyefanya vizuri kwenye jeshi pia kabla ya kuamua kuwa mwanasiasa. Iliandikwa kama mtu mwenye mafanikio makubwa sana jeshini bila kuwekwa taarifa kamili kwa sababu mengi wanayofanya hawa wa vitengo maalum jeshini hudhaniwa ni siri.

Niliuliza, "Dada yako aliwahi kutaja jina la Sansom?"

"Hapana."

"Walikuwa na uhusiano wowote labda?"

"Sioni wangeweza vipi kuwa na uhusiano." Jake alijibu.

Niliuliza, "Kwani dada yako alikuwa anafanya kazi gani?"

Hakunijibu. Hata hivyo hakuhitaji kunijibu kwani kuna alama nilikuwa nimekwishaanza kujumlisha. Mbili ongeza mbili, ni nne
.
 
KAKA ANAKANUSHA KIFO CHA DADA YAKE ETI HAJAJIUA. MI NAMTAZAMA KAMA ANASEMA KWELI. SIJUI WEWE UNA MAONI GANI?
 

Attachments

  • KESHO ILIYO ONDOKA.jpg
    KESHO ILIYO ONDOKA.jpg
    574.3 KB · Views: 17

Similar Discussions

Back
Top Bottom