Riwaya: Huba la miss Tanzania

HUBA LA MISS TANZANIA-PART 23

"Ooh my God.....looh salaleee...! picha yangu kabisaaa au mtu anayefanana na mimi?" aliuliza kwa mshtuko Shebby baada ya kusimuliwa na Sada juu ya ujio wa mtu wanayemhisi ni afisa usalama, ambaye alikuwa hana asili wala fasili mtu huyo machoni mwao. Mtu huyo alikuwa si mwingine bali ni Kachero Manu alikuwa amefika kazini kwao RAJA SAFARI TOURS kufanya taftishi na baadhi ya watumishi wa hapo. Kilichomleta hapo kwenye kampuni hiyo ni kujaribu kufanya taftishi kama muuaji wa Profesa Kaganda ndio huyo huyo muuaji wa Bwana Pateli! Taftishi ambayo ilizaa matunda asiyoyategemea kwa Kachero Manu. "Ni sura yako wewe nakufahamu vizuri sibahatishi na sijaja hapa kuleta maneno ya mkahawani au kwenye vijiwe vya kahawa" Sada alikazia maneno kwa ukali akionyesha kutopendezewa na ubishi wa Shebby. "Nisamehe bestito sijakusudia kukubishia, haya tuyaache kwanza, ehee...! Akasemaje sasa huyo jamaa kuwa nimefanya tukio gani? " aliomba msamaha Shebby huku akiendelea kumdodosa Sada. "Kapita kuhoji kila mtu pale kazini huku anamuonyesha picha yako, sasa Mzee Sheni yule mpishi wako uliyekuwa unaenda nae mbugani karopoka maneno ya sumu hata yasiyohusu, sijui oooh...! Ulikufukuzwa kazi kwa sababu mkichangia bibi na Bosi wetu marehemu Pateli, hapo ndio huyo mgeni akavutika na udaku wa Mzee Sheni kaondoka nae ofisini katokomea kusipojulikana... kila mtu anasikitika juu yake yule Mzee sijui ataacha lini taarifa za lolololo, zitakuja kumponza siku za usoni" alizidi kupasua maneno Sada bila mficho kwa Shebby bila kuelewa kuwa amemfaa vilivyo. "Naanza kuogopa sasa mie nimefanya kosa gani mpaka nasakwa kwa udi na uvumba! " alijisemesha kwa huzuni Shebby hali ya kuwa anajua kila kitu kinachoendelea. "Dalili zinaonyesha ni usalama wa taifa huyo mtu, maana kaja na gari zao nyeusi zile" alizidi kuweka tashididi ya mazungumzo yake. Shebby sasa taharuki ilimkamata vilivyo, alitambua sasa polisi wameshafika mbali kwenye uchunguzi wao wa mauaji ya mfululizo kuanzia kwa Bosi Pateli na Profesa Kaganda. Hivyo akizubaa kidogo tu itakula kwake atashindwa kutekeleza kisasi chake kwa Dr.Sonko. "Inabidi bestito Sada unipe hifadhi nyumbani kwako la sivyo nitaumbuka! " alivunja ukimya Shebby kwa Sada akiomba auni ya ulinzi. Sada alivuta pumzi ndefu baada ya kusikia maneno yake ya Shebby. "Unanipa mtihani mzito sana Shebby, maana hujaniambia umefanya nini mpaka unatafuta, lakini pia hata mie unanipa mashaka unaonekana mambo yako kiuchumi sasa yapo bambam unasukuma ndinga la gharama huenda kuna tukio zito umefanya unatafutwa!" Sada alitikisa kiberiti kwa Shebby huku akionyesha kama hatokubali kirahisi. Lakini uhalisia wa mambo Sada alikuwa anampenda kwa dhati Shebby alikuwa hawezi kupindua kwa chochote atakachomwambia. Kwa zaidi ya miaka 6 tokea wamefahamiana, Sada alikuwa moyoni anaungua kwa joto la mapenzi kwa Shebby, na ndio maana alipoona kuna mtu anamsaka Shebby alishindwa kujizuia kutokumpa taarifa. Miaka yote alikuwa anajipa moyo ipo siku tu, huenda Shebby atamtakia kuwa anampenda. Aliposikia Shebby amenasa kwenye huba la Miss Tanzania na kishatangaza ndoa, aliugua karibia mwezi mzima, yu mahamumu hoi bin taabani hajiwezi kitandani. Alipopata nafuu na kurudi kazini alianza kuzoea kuwa Shebby ndio kapuruchuka sio wake tena, lakini walipoonana siku Shebby amekuja kuchukua barua yake toka kuzimu pale ofisini, ugonjwa wake wa huba kwa Shebby ukaibuka upya. Meseji cha chombezo zile za umeamkaje, umeshindaje na za usiku mwema zilikuwa hazikauki katika simu ya Shebby toka kwa Sada. "Hata wewe Sada, mwandani wangu huniamini unaniona kama mimi ni mjuba nishakua mtu wa ovyo sasa nani ataniamini tena?" alijifaragua kujilalamisha mbele ya Sada huku akijivika usoni mwake huzuni kubwa na kujitia kuinama chini. "Baby.....usinidhanie vibaya, sikuwa na nia mbaya nikihofia tu nikataka unitoe wasiwasi mimi nakuaminia zaidi ya asilimia 100% huwezi kuniingiza matatizoni" alijibu Sada huku moyoni akiwa na mlipuko wa furaha wa kuitwa mwandani na Shebby kwa mara ya kwanza kwa muda wa miaka 6. Shebby akawa anachekea tumboni kwa namna alivyomnasa kiulaini Sada kwenye mtego wake wa kumpa hifadhi mpaka anaitwa 'baby'. Maana alifahamu fika sasa msako dhidi yake wakimkosa nyumbani kwake, utahamia kwenye mahoteli na nyumba za kulala wageni hivyo hatokuwa salama kabisa. Kimbilio pekee ambapo ni salama palibaki nyumbani kwa Sada na ingekuwa ngumu kwa vyombo vya usalama kuleta hisia kuwa Shebby yupo nyumbani kwa Sada." Nilikuwa nataka kushangaa sana kama na wewe Sada ni rafiki mnafiki yule mkia wa fisi, ambaye wakati wa shida anakuepa kama mkoma vile" alizungumza Shebby kwa kujiamini huku anamalizia 'Ice-cream' yake kushushia mlo wake kabambe. Wakaendelea kusogoa hadithi moja mbili tatu huku wakijiandaa kuondoka kuelekea nyumbani kwa Sada huku furaha ya Sada ikiwa ni sheshe kama kumsukuma mlevi akijua fika Shebby akifika kwake vibwanga na vitimbi atakavyomfanyia hawezi kupindua kwake.

Ulikuwa ni usiku mbichi wa saa 2:30 usiku katika maeneo ya 'Mbezi Juu-Kwa Pembe' siku hiyo ya Jumamosi,Kachero Manu alikuwa ndio kwanza anaegesha kwenye eneo la maegesho la 'LIBRA SOCIAL HALL' gari yake aina ya 'Toyota Crown Royal Saloon' rangi ya maziwa. Aliegesha eneo ambalo hatapata usumbufu pindi atakapohitaji kuliondoa gari lake kwa haraka hasa ukichukulia siku hiyo ni ya mwishoni mwa juma, kadamnasi ya watu walikuwa wamefurika kuja kustarehe mpaka che. Ilikuwa dalili zinaonyesha ndani ya ukumbi ule kulikuwa kuna tafrija ya harusi inafanyika. Wahudhuriaji walikuwa wanazidi kumiminika huku wakiwa wamevalia mavazi yao nadhifu huku wakionekana wana furaha kubwa. Ghafla wakati Kachero Manu anajiandaa kuvuka upande aingie kwenye moja ya mashine za kutolea fedha zilizopo hapo hapo 'LIBRA SOCIAL HALL' usafiri wa Bwana na Bibi harusi ulikuwa unaingia. Fahari ya macho ikabidi Kachero Manu akodoe macho kuwaangalia wapendanao hao waliokuwa ndio wanashuka kwenye gari yao ya kifahari huku Bibi harusi akionekana kupendeza mpendezo wa Shamsi Matlai. Wakawa wanatembea masi masi kwa mwendo wa pole kuingia ukumbini mule,huku nyimbo mbalimbali za muziki zkipigwa kuchagiza uingiaji wao ndani ya ukumbi. Kachero Manu akapuuzia kuendelea kufuatilia yasiyomhusu akavuka ng'ambo ya pili na kuingia kwenye moja ya mashine ya kutolea fedha ya katikati inayomilikiwa na benki ya NBC, huku yasari kwake kulikuwa na mashine ya benki ya NMB na yamini kwake kuna mashine ya benki ya CRDB, na zote zilikuwa na watu wanachukua fulusi zao wakafanye mapochozi ya usiku huo kwenye starehe zao za mwishoni mwa juma. Akachukua kiasi cha pesa anachohitaji kisha akatoka na kuifuata barabara ya giza ya upande wa kulia kama alivyoelekezwa nyumbani kwa Shebby. Alitembelea kwa mwendo wa mashi mashi kwa takribani robo saa, mpaka akakutana na kibanda umiza kimejaza watu kibao wanashuhudia mchuano wa mechi za ligi kuu ya uingereza kabumbu uwanjani wachezaji wanamenyana katika runinga. Akapita na hamsini zake na hamna hata mmoja hata aliyegeuka kumtazama yeye. Alivyoenda mbele zaidi akaanza kuteremka bonde kushuka chini kwa mbali akawa ameziona nyumba nga'mbo ya pili zimejitenga. Akaenda mubashara kwenye baiti mojawapo ya kati kati ambayo ni duka la kuuza bidhaa ndogondogo. Alipofika dukani, alikuta wateja wanahudumia bidhaa mbalimbali za mahitaji yao ya siku, akazuga nae pia ni kama mhitaji wa bidhaa huku macho yake yote yanakodoa nyumba ya pili yake ambayo ndio nyumba haswa anayoishi Shebby. Alimuona mama mmoja yupo nje ya kibaraza anachoma maandazi. Akafanya maamuzi ya kumvaa yule kumuulizia kama Shebby yupo kwenye baiti. "Mama shikamoo...mimi ni mgeni wa mpangaji mwenzenu Shabani Zomboko sijui nimemkuta? " aliuliza Kachero Manu kwa yule mama. "Marhaba mwanangu, wala sifahamu maana huyo Shebby kutoka kwake na kurejea kwake anajuaga mwenyewe, labda umpigie simu au pita moja kwa moja na veranda hiyo chumba chake kimejitenga peke yake utakiona tu! " alijibu yule bila kumtazama usoni Kachero Manu huku akiweka maandazi mapya ya kuchoma kwenye karai linalochemka mafuta ikiwa ni ishara hana haja ya maswali zaidi yupo kikazi zaidi. Kachero Manu akajiongeza akaanza kutembea na veranda huku akigusa kiunoni kuhakikisha mguu wa kuku wake upo salama tayari kwa kutumika kama ikibidi. Kwa bahati baiti yote ilikuwa kimya kasoro chumba kimojawapo kulikuwa na muziki unapigwa kwa sauti ya chini. Akafika kwenye kile chumba kilichoungana na sebule alichopanga Shebby akakuta taa zimezimwa ishara ya kwamba hamna mtu ndani. Akaanza kubisha hodi kujiridhisha kama kweli hamna mtu. Aligonga kama mara tatu ukimya ukawa umetamalaki. Akaangalia muda kwenye saa yake ya mkononi, saa ikasoma ni saa 3:15 usiku juu ya alama. Himahima akachomoa mkungu wa funguo zake malaya mfukoni akaanza kukorokochoa kwa funguo hizo kwenye kitasa hicho cha mlango. Funguo wa tatu kujaribisha ukakubali kukifungua kitasa kile sasa mlango ukawa umefunguka. Haraka haraka akaingia ndani na kuurudishia mlango ule bila kufunga tena na ufunguo, alijua hatopoteza wakati mrefu. Akawasha kurunzi yake ndogo ya kumuwezesha kupata nuru ya kutosha kumuongoza chumbani mule huku mkono mwingine ukiwa umebeba bastola tayari kwa kushughulika ikibidi. Alipotupa macho kwenye sebule ile kwa haraka haraka hakuona chochote kitakachokuwa msaada kwake akaamua aelekee chumbani kwa Shebby. Kwa bahati alipokanyaga tu zulia la kujifutia miguu akahisi kama kuna kitu kigumu chini yake. Akanyanyua zulia lile akaona funguo mbili moja kubwa na nyingine zimeunganishwa kwa silsila nyembamba. Akatabasamu kwa jinsi mambo yanavyokwenda bambam. Akafungua mlango wa chumba kile akaingia bila hata kuubugaza mlango kwa pupa yake aliyokuwa nayo. Alipomulika kurunzi kitandani akakuta picha zimezagaa pale kitandani akasogelea na kuokota picha mojawapo. Ilikuwa ni picha ya Profesa Kaganda ikiwa imewekwa alama ya vema kuonyesha tayari ameshashughulikiwa. "Shabaaashi...! Huyu ndio muuaji asiyejulikana maluhuni mkubwa Shebby utanitambua mimi ni nani! " alijikuta anaropoka kwa sauti ya taratibu. "Tupa silaha yako chini na nyoosha mikono juu" ilikuwa ni sauti ya kama muungurumo wa radi katika masikio ya Kachero Manu huku mtutu baridi wa bastola ukiwa umegusa sikio lake la kushoto. Alishtukizwa kwa namna asiyoitarajia hata kidogo mpaka akajilaumu kwa kutochukua tahadhari ya kutosha. Bila ubishi wowote akatupa chini bastola yake na kunyoosha mikono yake, likawa ni kosa la kujutia la pili kwa Kachero Manu. Mtu yule aliyemuweka chini ya ulinzi akamnukiza puani kwa kitambaa, hanchifu kilicholowa kemikali. Pale pale Kachero Manu akajikuta anaishiwa nguvu na kuanguka chini puuuh kwa kupigiza kichwa kwenye tendegu la mguu wa kitanda kama papai lililoiva sana. Akapoteza fahamu chumbani mule mwa Shebby.

Mbona utatupa kidunyukidunyu
 
HUBA LA MISS TANZANIA-PART 24

"Ripu ripu! " aliropoka Shebby maneno hayo kuashiria furaha ya kumshinda adui yake Kachero Manu. Kachero Manu alikuwa amelala kigogo pale sakafuni huku damu zinamvuja puani, hajui kinachoendelea duniani. Shebby hakuwa na muda wa kupoteza hakutaka kufanya mambo yake aste aste hata kidogo, akawasha taa ya chumbani mule kisha akaanza kumpekua mifukoni Kachero Manu hakumkuta na chochote cha maana zaidi ya pesa za Kitanzania shilingi milioni moja taslimu ambayo alikuwa ametoka kuichukua kwenye mashine ya benki kitambo kifupi kilichopita. "Kiendacho kwa mganga hakirudi" akajisemea maneno hayo Shebby huku anatabasamu na kuifutika pesa hiyo kibindoni mwake kwenye pochi maalumu. Akachapuka chap chap toka chumbani mule mpaka kwenye mlango wa kuingilia sebuleni kwake akahakikisha umefungika ki ki ki kisha akarudi chumbani kuendelea na maandalizi ya kuutoa mwili wa Kachero Manu nje ya chumba chake. Ghafla bin vuu...!
Ngo...Ngo...Ngo....Ngoooh.....!...Ngo..Ngo...Ngooh...! ikasikika sauti ya hiyo ya kugongwa kwa mlango kwa tashididi iliyo kubwa. "Fungua mlango Bwana Shabani Zomboko..Mahepe! Mahepe! yako ya gizani tumeyashuhudia, tumekuona huna ujanja leo umekwisha fungua mlango tumalizane na wewe leo" ilisikika sauti ya kipolisi ikivuma tokea nje ya mlango wa sebule wa Shebby, polisi ambaye alikuwa amekuja kidari nje huku anabubujikwa na maneno kama bisi anamtia jamba jamba Shebby. Kipindi hicho Shebby alikuwa kwenye harakati za kumtia kamba Kachero Manu ili akimaliza aende kutafuta magunia ya kumbebea Kachero Manu ili akamshughulikie vizuri. Alipanga kumhoji kinagaubaga ili kujua kitu gani kimemfanya mpaka amfuatefuate sako kwa bako kiasi kile kuanzia kazini kwake kwa zamani kule RAJA SAFARI TOURS mpaka nyumbani kwake. Sasa hiyo hodi ya watu asiyowajua nje ya chumba chake ilimkata maini kabisa na kusababisha mapigo ya moyo kwenda matiti. Furaha yake sheshe ilipotea mithili ya mvuke unavyotokomea angani. Ikawa ni furaha mithili ya starehe ya mbwa kukalia mkia wake, sio furaha ya kudumu. Akawa amepwaya kama mtu aliyetoka ugonjwani. Jasho jekejeke likaanza kumtiririka mwilini mithili ya mtumishi wa tanuri la kuoka mikate. Sakata lake sasa alikuwa analiona ni sawa na kuweka maji maziwani. "Nipo ndotoni au dhahiri hiki nilichokisikia kuwa eti ameniona" alikuwa bado yupo kwenye fikra nzito hajafanya maamuzi kama asalimu amri kwa polisi huyo au apambane mpaka tone lake la mwisho la damu. "Wewe Shabani fungua mlango unajitia mjuba eeeh...sasa chamoto utakiona leo tumekuzingira kila kona ujanja wako wote leo umekwisha" ilikuwa ni sauti ya Mwenyekiti wa mtaa wa Mbezi juu Bwana Madogori, sauti ambayo ilikuwa si ngeni katika masikio ya Shebby. "Mpaka na kiongozi wa mtaa nae ndani kweli kila lenye mwanzo halikosi mwisho..nimekwisha sina ujanja" Shebby alikuwa amezama kwenye bahari yenye kina kirefu cha mawazo, huku akijutia kwanini alifanya maamuzi ya kutoka usiku ule nyumbani kwa rafiki yake Sada na kurudi kwake. Sada alikataa katakata Shebby asitoke nyumbani usiku ule kwa sababu za kiusalama, lakini Shebby akalazimisha kutoka, alikuwa mwingi wa siasa mpaka Sada akalainika. Alitoa sababu za uwongo na kweli ili mradi atoke lakini lengo lilikuwa ni kurudi nyumbani kupoteza ushahidi wote. Alijua fika huyo mtu anayemtafuta akifanikiwa kuingia nyumbani kwake atadaka ushahidi wote wa kumhusisha yeye na tukio hilo. Ilibidi afike mapema nyumbani kwake kabla ya Kachero Manu lakini foleni za barabarani jijini Dar es Salaam ndizo zilimchelewesha Shebby. Mama mchoma maandazi ndio aliyemtonya Shebby pindi alipomuona kibarazani. Kwa kumpa taarifa kuwa kuna mgeni wake alikuja kumuangalia muda mfupi uliopita. Shebby aingie chumbani kwa tahadhari zote ndipo akakutana uso kwa uso na adui yake Kachero Manu chumbani kwake akiwa katika harakati za kufanya speksheni chumbani humo. Sasa kabla hajamalizana vizuri na Kachero Manu ghafla bin vuu askari polisi akiwa na Mwenyekiti wa serikali ya mtaa wamekuja kumtia mbaroni. "Tunatoa mbiu ya mgambo kwa mara ya mwisho, fungua mlango kwa hiari yako mwenyewe vinginevyo tunavunja mlango mara moja" alizungumza yule kwa sauti isiyo na hata chembe ya mzaha. "Naa..ku...ujaaa. " Shebby aliitikia wito kwa sauti ya kitetemeshi akionyesha amekubali kujisalimisha. Hakutaka kufanya fujo na purukushani bila kwanza kuangalia ukubwa wa nguvu ya adui. Alikuwa ana kanuni kuwa urefu wa kina cha maji haupimwi kwa macho.
 
HUBA LA MISS TANZANIA-PART 25
Shebby akajikaza kisabuni akapata nguvu za ghafla za ujasiri wa kukabiliana na janga lililo mbele yake, akausukumiza mwili wa Kachero Manu chini ya uvungu kisha akazima taa ya chumbani kwake na kusogelea dirishani mwake. Akapekenyua pazia kuchungulia nje ya chumba chake. Kwa msaada wa nuru ya mbalamwezi akaona kwa mbali kama meta 5 mpaka 7 kuna vijana wamesimama vikundi na silaha za jadi.

Akapatwa na pumbao la nafsi pale pale dirishani huku anawaza haelewi kitu gani kinachoendelea kwake "Mbona hao askari walionizunguka kila kona mbona siwaoni". Ghafla akiwa kwenye hali hiyo ya kuduwaa akastushwa na vishindo kama vya kutaka kuvunja ule mlango wake wa sebuleni huku nje sauti za akina mama zikishangilia kuchagiza uvunjwaji wa mlango huo, haraka haraka akachomoka chumbani na kukimbilia mlangoni pake. "Nimejasilimisha kwa amani nifungeni pingu muondoke na mimi! " alizungumza Shebby huku anawapa mikono wamfunge pingu. "Ukishindwa kutimiza masharti kweli utatiwa pingu, wewe mtu gani huonekani kwenye vikao vya mtaa wala sungusungu hulindi upo upo tu" alisema Mzee Madogori. Sasa sisi tumekuja kukupiga faini ya kukwepa kulinda sungusungu kwa muda wa wiki mbili, faini yako ni elfu hamsini hauna anakubeba kwa tanganyika jeki Bwana afande anaenda na wewe kituoni ukaimbe nae" alizungumza nia na madhumuni ya ujio wao pale kwenye chake.

"Abebwe huyooo akalipie jela amezidi ujanja kama sungura" baadhi ya majirani walipiga makelele wakionyesha wanataka faini ikalipiwe polisi huku wakiwa na raghba ya kumuona akibebwa mzobemzobe, wakimtafuta Shebby muhali kwa maneno yao ya kifedhuli. "Samahani sana Bwana Mwenyekiti kazi tu ndio zinatubana lakini tupo pamoja faini nitalipa na nitatoa pesa za ziada kama posho ya walinda amani wetu wa sungusungu wanaotufanya tulale kwa amani" aliongea Shebby akitaka shufaa kwa kutega kwake ulinzi huku akiwa amechangamka baada ya kugundua ujio wao sio wa kumkamata kutokana na kumshambulia Kachero Manu bali ni kumlipisha kutokana na kutega ulinzi wa sungusungu.

Akachomoa burungutu la milioni moja aliyomchomolea Kachero Manu akamkabidhi Mwenyekiti wa serikali ya mtaa. Mwenyekiti yule wa mtaa burungutu lilipotua mikononi mwake akawa anatetema kama mgonjwa degedege macho yake hayaamini. Anataka kuzungumza maneno yanagoma kutoka kinywani anabaki kukenua meno tu. "Sasa mie nataka kujipumzisha ndani kidogo naomba mniache mkiwa na shida yoyote ya ulinzi shirikishi labda mnahitaji makoti, filimbi, buti na vikorokoro vingine msisite kunitaarifu" alizungumza Shebby kwa sauti ya kupiga malapa na madahiro kisha akafunga mlango na kuegemeza mgongo wake kwenye mlango kwa sekunde kadhaa.

Alishusha pumzi ndefu za kutetwa huku akiwa amefumba macho yake haamini kama amesalimika kutoka mikononi mwa afande yule mwenye mikwara bubu. "Shebby wewe kulinda sungusungu basi tumekusamehe kimoja, wewe rudi tu hata asubuhi hawa wanawake tunawaambia waume zao wanaorudi nyumbani saa 12 jioni wakishamaliza kusaidiana kukuna nazi na kupika chakula cha usiku na wake zao ndio watalinda sungusungu" aliropoka maneno kali ya kebehi na kupiga vijembe Mwenyekiti yule wa serikali ya mtaa kwa kiwewe cha burungutu la milioni moja za Shebby.

Umati ule wa watu waliokuja usiku ule kushabikia kukamatwa kwa Shebby walilolitaka liliposhindikana ikabidi warejee matao ya chini kwa aibu na fedheha vichwa chini mithili ya jogoo mwenye ugonjwa wa mdondo. Shebby sasa hakutaka kumchelewesha Kachero Manu isije kibao kikamgeukia akanaswa kikweli hivyo akarudi chumbani na harakati zake za kumuandaa Kachero Manu ili amtie kwenye gunia akamtelekeze maporini huko.

Mamia na maelfu ya watu wa rika zote na jinsia zote kuanzia wakubwa mpaka watoto, wote walikuwa wanaonekana kumiminika kwa wingi katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa, wilayani Temeke, Jijini Dar es Salaam. Kama wewe ni mgeni katika viwanja hivyo na ndio mara yako ya kwanza kushuhudia kadamnasi ile kubwa ya watu lazima ungevutika kutaka kufahamu kulikoni ni kitu gani chenye mvuto kinachoendelea kwenye viwanja hivyo. Kama ungebahatika kuuliza swali hilo kwa mtu yoyote wa maeneo hayo, awe mzima au majinuni majibu yao yangefanana na yangekuwa ni mepesi tu, angekufahamisha kuwa hapo kunafanyika maonyesho ya kimataifa ya biashara maarufu 'Sabasaba'.

Muonekano wa baadhi ya Wafanyabiashara wengine kwenye viwanja hivyo walikuwa bado hawajamalizia ujenzi wa mabanda yao vizuri hivyo wakawa wametingwa na ujenzi ili kuyapa mabanda yao muonekano wenye mvuto. Vijana waadilifu wasio na kazi nao ulikuwa ni msimu wao wa kupata vibarua vya muda mfupi vinavyowasaidia kupunguza ukali wa maisha kwa muda. Chambilecho ganda la muwa la jana chungu kaona kivuno, vibaka na matapeli nao kwao ilikuwa pia ni fursa ya kutimiza nia zao ovu za kujipatia kipato cha haramu, walikuwa wanawapora watu simu zao, pesa na vifaa vinginevyo vya thamani, tafrani mtindo mmoja.

Maonyesho hayo ya sabasaba huwa yanakuwa ni kama nyota jaha kwa wakazi wa wilaya ya Temeke na Jiji la Dar es Salaam kwa ujumla katika harakati zao za kupambana na umasikini. Viwanja hivyo kwa kawaida huwa vinafurika mtiti wa watu kila mwaka kuanzia tarehe 1/07 siku ya ufunguzi rasmi wa maonyesho hayo mpaka tarehe 10/07 siku rasmi ya kufunga maonyesho hayo. Mamlaka ya maendeleo ya biashara Tanzania 'Tantrade' kwa mwaka huo walikuwa wamejiandaa vilivyo kushinda miaka yote ili kuhakikisha maonyesho hayo yanafana na kuwa bambam. Wafanyabiashara na Wajasiriamali, wakubwa kwa wadogo wanaotokoa ndani ya nchi na nchi za ng'ambo walikuwa tayari wameshachukua nafasi zao kwenye mabanda yao tayari kwa kuchuana ubora wao.

Siku ya fainali wa mchuano huo washindi walikuwa wanapewa tuzo na mgeni rasmi ambaye mara nyingi alikuwa anakuwa Rais wa nchi. Gumzo kubwa la wahudhuriaji wengi wa maonyesho hayo lilikuwa kwenye banda la wahandisi wa kike wa vyuo vikuu mbalimbali, ambao walikuja kuonyesha bidhaa mbalimbali za ubunifu zilizokonga vilivyo nyoyo za wahudhuriaji hao. Kifaa kilichowavutia wengi ni mashine ndogo yenye uwezo wa kutoa sauti yenye masafa 'frequency' mshabaha na sauti ya paka wa majumbani. Kifaa hicho chenye ukubwa mshabaha na pasi ya majumbani lengo ni kuwafukuza panya ndani ya nyumba bila hata Kulazimika kufuga paka.

Pia walikuja na kemikali ya kimiminika yenye harufu kama mkojo wa paka, kemikali ambayo ukinyunyizia katika nyumba panya wanakimbia wakinusa harufu yake. Wazo hili la ubunifu walikuja nalo baada ya kufanya utafiti na kugundua baadhi ya watu hawapendi kufuga paka majumbani mwao kutokana na uwoga au kushindwa gharama za matunzo na pia wengine wana mzio na paka lakini wanasumbuliwa na panya majumbani mwao.

Pia kwenye maghala makubwa ya kuhifadhia chakula moja ya tatizo kubwa linalosababisha upotevu wa mazao mbalimbali baada ya uvunaji ni panya. Hivyo kwa pesa chache tu Kitanzania ulikuwa unaweza kupata kifaa hicho ambacho kilikuwa na uwezo wa kutoa mlio wa paka kwa kupishana mda unaoupangilia wewe mtumiaji. Kifaa hicho kipya na rafiki kilikuwa kinachajiwa kwa kuanikwa juani masaa matatu tu na kina uwezo wa kukaa na chaji kwa muda wa wiki nzima. Uzinduzi rasmi wa mauzo ya vifaa hivyo ulipangwa kuanza tarehe 5/07 chini ya mlezi wa wahandisi hao Naibu Waziri Mkuu Dr.Sonko pindi atakapotembelea banda hilo.

Walijinasibu kuwa na mzigo wa kutosha kutoka kiwandani China, mzigo ambao tenda ya kuuagiza na kuutoa bandarini ilikuwa mikononi mwa Shebby. Shebby na yeye alipanga maangamizi ya adui yake nambari wani, Dr.Sonko yafanyikie ndani ya banda hilo hilo la wahandisi wa kike. Shebby aliziteka nafsi za wahandisi hao kwa kujifanya atawafadhili gharama zote za kuagiza na kutoa mzigo wao baada ya kupendezwa na wazo lao la ubunifu huo. Hivyo alitaka afe hadharani mbele ya kadamnasi ya watu huku mahawara zake, ambao ni wanachuo washuhudie jinsi danga lao linavyokata roho.

Kachero Manu katika speksheni zake chumbani kwa alifanikiwa kuona nyaraka ya mpango mzima namna Naibu Waziri Mkuu Dr.Sonko atakavyouliwa lakini bahati haikuwa yake hakufanikisha kuchomoka na nyaraka hiyo ndio yakamkuta yaliyomkuta chumbani kwa Shebby. Usilolijua ni kama usiku wa giza nene, kifo cha Dr.Sonko kilikuwa kinahesabiwa siku kadhaa tu. Shebby alitaka kama vile vile vyombo vya habari vilivyoripoti kwa uzito wa juu kifo cha mpenzi wake Zabibu basi na kifo cha huyu Bwana mkubwa buda nacho kipewe uzito ule ule na vyombo hivyo. Kisha atakapokamilisha adhima yake hiyo atakuwa tayari kufa kwa raha mustarehe, moyo wake ukiwa umetungamana.

Taifa la Tanzania lingeingia tena kwenye maombolezo ya Kitaifa ya kiongozi wake wa juu. Kiongozi ambaye alijipambanua kama kipenzi cha vijana, aliyeonekana anajali maslahi yao kumbe ni poyoyo tu mwenye kutaka sifa na kujali maslahi yake binafsi kwa malengo ya kuja kugombea Urais miaka ya usoni. Kwa mtazamo wa juu juu, Shebby alishashinda vita maana mzigo toka China ulikuwa unatua kesho yake. Mtu pekee ambaye amefanikiwa kumtambua Shebby kuwa ni mhusika wa mauaji ya borongoborongo ya watu maarufu ni Kachero Manu, lakini tayari yameshamkuta ya kumkuta hakuwa tena na uwezo tena wa kumdhibiti Shebby.
 
HUBA LA MISS TANZANIA-PART 26

"Usinilazimishe nikufanyie kitu mbaya ambacho utaenda kunisimulia huko jongomeo kwa malaika wa adhabu" Shebby alikuwa anazungumza kwa sauti iliyojaa hasira, inayounguruma kama radi, sauti ambayo haikuwa na hata chembe wala tone la huruma la huruma wala shufaa kwa Kachero Manu." Sijui chochote unachoniuliza, fanya utakacho kwangu" aliongea Kachero Manu kwa dharau na jeuri huku analamba damu ya midomo yake kwa ncha ya ulimi wake.

"Kwa hiyo nikulazimishe kunijibu sio? " aliongea Shebby kwa jazba akiwa ameshapoteza uvumilivu tayari, macho yake yamekuwa mekundu kama jua lichomozalo kwa hasira. "Nimekuambia amua chochote unachotaka kunifanya" alijibu Kachero Manu huku paji la uso wake likiwa limejaa matuta. Shebby alifanikiwa kumtoroshea Kachero Manu katika pindi pindi la usiku wa manane na kumfikisha katika msitu wa Mabwepande. Msitu huo ni maarufu sana kwa wakazi wa Jijini Dar es Salaam.

Umaarufu wake haupo katika uzuri wa miti yake wala nyasi zake, bali ni kwa vitendo vya kigaidi ambapo vinafanyikiwa katika msitu huo. Inasemekana zamani msitu huo wa Mabwepande uliikuwa ukiiitwa Mawepande kwa sababu kulikuwa na mawe makubwa mawili na msitu wa Pande, lakini ujio wa Wazungu ulibadilisha jina hilo kwa sababu walikuwa hawawezi kulitamka vizuri na kupelekea kuitwa Mabwepande.

Kachero Manu alipofikishwa Mabwepande Akafungwa ndi ndi ndi, vizuri kabisa miguu yake na mikono kwenye mti wa Msonobari katikati ya kichaka cha msitu huo kisichofikika kiurahisi usiku huo. Ilipofika majira ya alfajiri ya siku ya Jumapili, Kachero Manu alipata fahamu, ndipo mahojiano ya kibabe na mtifuano mkali kati ya Kachero Manu na Shebby yakaanza. Kachero Manu alikuwa anajifanya kichwa ngumu hataki kutoa ushirikiano wowote kwa hiari, ndipo Shebby akawa anamtishia kutumia nguvu.

"Nakuuliza kwa mara ya mwisho, nani alikutuma unifuatilie mpaka nyumbani kwangu? " aliuliza Shebby huku mkononi ameukamatia mjeledi wa samaki taa mithili ya ule uliokuwa ukitumika kuchapia watumwa enzi za ukoloni. Kachero Manu akabaki ametumbua macho tu kwa kiburi huku uso wake umevaa tabasamu la dharau.

"Aaaah....Aaaah....Aaaaaah....ntaaa...se...maaah..!" alilalamika Kachero Manu kwa sauti ya juu kuonyesha tashididi ya maumivu makali anayoyapitia kila mikwaju hiyo ilipokuwa inatua mgongoni mwake. Alikuwa amefungwa kwa mtindo ambao sehemu kubwa ya mgongo wake ilikuwa kwa nje, hivuyo kumpa urahisi Shebby.

"Kefle! Mburukenge wewe ngoja nikushikishe adabu kwanza, ukome kufanya ushushushu kwenye majumba ya watu" alizungumza Shebby kwa hasira huku anamshushia mijeledi ya kutosha mwilini mbaya wake. Baada ya mateso kama ya robo saa hivi, Kachero Manu alikuwa hatamaniki mwilini mwake, amelowa damu chepe chepe. Ngozi yake ilikuwa imechanika chane chane hasa maeneo ya mgongoni kwa vipigo hivyo. Kama hivyo haitoshi, Shebby akatoa mfukoni kiberiti chake cha gesi na kukiwasha kisha akakisogeza karibu na ndevu za Kachero Manu na kuanza kuziunguza, huku Kachero Manu anapiga kelele za maumivu.

"Haya sasa nadhani utazungumza bila usumbufu ha.. ha.. ha...pumbavu sana wewe, hao viongozi wenu badala ya kuwaelekeza waishi kwa maadili nyie mpo mpo tu kuwalinda kwa hali na mali hata kama wanatukosea sisi makapuku. Mnatuona sisi ni mazumbukuku ulimwengu uko huku eeh...rasilimali zetu za taifa wanazitumbua hatuwasumbui kama haitoshi mpaka wake zetu wanataka kujimilikisha wao.. !Sasa leo ndio mwisho wako na huyo aliyekutuma zinahesabika siku tu wote mtaenda kulindana upya huko jongomeo" alifoka Shebby kwa hasira huku anacheka kwa kwa kwa akiwa amemkaribia kwa karibu kabisa Kachero Manu.

"Nani kakutuma na umenijuaje kama mimi ndio mtuhumiwa mpaka ukafika nyumbani kwangu? " aliuliza swali Shebby huku amemshikia kisu shingoni anatishia kumchoma nacho asipojibu kiusahihi. "Familia ya unaowaua bila hatia ndio wamenituma...!" alijibu kiunyenyekevu Kachero Manu huku kila sekunde inayoondoka akianza kukata tamaa ya kuishi tena. "Ha... ha.. .ha.... ha...mbwa koko wewe unasemaje? Eti familia imekutuma ya niliowaua bila hatia..!. Hivi damu ya mpenzi wangu Zabibu waliyosababisha imwagike watalipaje?.

Mimi mwenyewe ni marehemu mtarajiwa napambana na kumeza mbaazi kila siku nasubiri muda tu wa kufa hao unaowapambania ndio chanzo cha yote. Kumbe wewe ni kibaraka wao wanakufanya jeta sio eeh....Yasin Mkubwa! ngoja nikupe kipigo kitakatifu, kama huko kazini unasifiwa kuwa una mkono mwepesi sifa zimekuponza! " alishapandisha mori kama Madai Shebby na kuanza kumdunda kwa mateke na mangumi yasiyo na idadi mpaka Kachero Manu akaanza kulegea taratibu huku macho yake hayafunguki mpaka akawa amezimika kabisa hana kauli.

Shebby alipojiridhisha kuwa Kachero Manu hajiwezi kabisa, sio wa kupona tena na hawezi kupata msaada katikati ya msitu huo akakimbilia kwenye gari lake na kutimka katika msitu ule wa Mabwepande na kutokomea zake. Jua sasa lilikuwa tayari limeshachomoza vizuri kabisa katika majira hayo ya mafungulia ng'ombe. Alikusudia Kachero Manu afe kifo asilia kwa njaa na kiu au kuvamiwa na wanyama wakali.

Dhamira yake Shebby ilikuwa inamsuta kumuua mtu asiye na hatia ambaye hajamkosea moja kwa moja. Alifahamu huyu Kachero Manu alikuwa anatimiza majukumu yake ya kikazi tu ili kulijaza tumbo lake tu. Shebby mipango yake asubuhi hiyo ang'avu ilikuwa kwanza ni kwenda kwa kushughulikia mzigo wake kutoka bandarini kisha alikuwa anachukua sampuli mbili tatu za hivyo vifaa kuelekea nazo gereji kuna kitu alikuwa anarekebisha kwenye hizo sampuli anazotaka kuziweka mbele ya mgeni rasmi, Dr.Sonko. Uzuri Shebby ni mtu wa magari hivyo utundu wa kukorokochoa vifaa alikuwa mahiri haswa.

"Ukisikia bahati ya mtende kuota jangwani ndio hii, huyu tulishakata tamaa kama atapona, mapigo yake ya moyo yalikuwa chini sana, kapoteza damu nyingi sana. Anatakiwa akipona amshukuru sana Mungu wake kwa kumpigania mpaka dakika hii, achinje hata ng'ombe atoe sadaka" yalikuwa ni maneno ya daktari bingwa wa upasuaji katika hospitali ya taifa ya Muhimbili akiongea na afisa upelelezi wa wilaya ya Kinondoni ambaye alikuja kumuangalia Kachero Manu.

"Sawa basi afya yake ikiimarika usisite kunifahamisha haraka ili niweze kuja kumuhoji kujua kulikoni!" alizungumza afisa yule wa polisi na kuagana na daktari yule aliyempokea Kachero Manu asubuhi ya Jumapili akiwa hajitambui na kuwekwa katika chumba cha watu mahututi. Siku hiyo ya Jumanne asubuhi ndio afya yake Kachero Manu ilianza kuimarika vizuri kabisa na kutolewa katika chumba hicho cha watu mahututi (ICU).

Alikuwa amekaa kwenye chumba kwa zaidi ya masaa 24 na ushee tokea alipoletwa hospitalini hapo na polisi waliomuokota kwenye msitu wa Mabwepande. Kugundulika kwake kulikuwa ni kwa bahati nasibu tu, akina mama wanaopitapita maporini kuokota kuni za kupikia majumbani kwao, ndio walimuona Kachero amefungwa kamba kwenye mti katikati ya msitu majira ya adhuhuri. Ndipo akina mama hao kwa usamaria wema wao wakakimbilia serikali ya mtaa kutoa taarifa juu ya uwepo wa mtu asiyejulikana kwenye msitu huo wa hatari akiwa hajitambui.

Ndipo harakati za kutoa taarifa polisi zikafanyika na Kachero Manu kukimbizwa haraka kwenye hospitali ya taifa ya Muhimbili ili kujaribu kuokoa uhai wake. Mazungumzo yote kati ya daktari na afisa wa polisi yaliyokuwa yanafanyika mle wodini alipolazwa, alikuwa anayasikia Kachero Manu kiufasaha kabisa, ndipo akatanabahi kuwa yupo hospitalini, kumbe amelazwa. Akaanza kufanya kumbukizi ya matukio yote tokea akiwa Chuo kikuu cha Dar es Salaam kule Nkrumah Hall mpaka kuanzisha safari iliyomfikisha nyumbani kwa mtuhumiwa wake Bwana Shabani Zomboko.

Alijilaumu kwa kumdharau adui yake Shebby na kimchukulia poa sana kumbe sivyo kama alivyotarajia, chambilecho mdharau mwiba guu huota tende ndio yaliyomkuta Kachero Manu. Lakini akajipa moyo kuwa majuto ni mjukuu haitomsaidia chochote majuto yake kubadilisha hali ilivyo hapa anachotakiwa ni kuhakikisha anatoroka ili awahi kwenda kuokoa uhai wa Naibu Katibu Mkuu, Dr.Sonko na si vinginevyo. Alikuwa anawaza taharuki aliyokuwa nayo Bosi wake wa usalama Bwana Mathew Kilanga kwa kutopata mrejesho wowote kwa muda wote tokea akabidhiwe jukumu hilo.

Bosi wake alikuwa ni mtu wa kupenda kupewa taarifa ya kila kinachoendelea ili na yeye akibanwa kwa wakubwa zake huko juu apate cha kujitetea. Hivyo ukimya wa Kachero Manu wa muda mrefu ulikuwa ni pigo kubwa kwa Bwana Kilanga. Alipotupa jicho ukutani, akaona kalenda inasoma ni tarehe 4/07 siku ya Jumanne. Kwa mnasaba huo maana yake ni kuwa yamebaki masaa kadhaa tu kufikia Jumatano siku ya Jumatano. Siku ambayo kwa mujibu wa ratiba ya viongozi ya kuzuru mabanda ya maonyesho hayo ya biashara ni siku ambayo amepangiwa Naibu Waziri Mkuu, Dr.Sonko. Kwa mujibu wa nyaraka alizosoma kwa haraka haraka chumbani kwa Shebby, ndio siku ambayo Shebby kapanga kumshughulikia mbaya wake Dr.Sonko. Alipogeuza macho yake juu kuangalia dripu ya damu inayoingiza damu mwilini mwakea akabakia machozi yanamtiririka bila kikomo.

Aliona kabisa dalili za kushindwa zipo wazi wazi kama asipopandisha soksi zake vizuri azichange vyema karata zake. Akiwa kwenye msitu wenye giza nene la mawazo anapanga na kupangua namna atakavyoteleza mle wodini ghafla akashtuliwa na sauti ya nesi anayemhudumia.

"Unaendeleaje kwa sasa?, pole sana! " . "Ahsante naendelea vizuri sana, bora mnipe ruhusa tu! " alijibu Kachero Manu kwa raghba ya kutaka kuondoka tu hospitalini pale. "Utaruhusiwa tu usijali, hili linaloishia ndio dripu la mwisho, alfajiri nitakuwekea dripu la maji hilo ndio litakupa nguvu kabisa. Daktari akipita raundi asubuhi atakuandikia dawa za kwenda kutumia nyumbani lakini pia kuna afisa wa polisi tumeambiwa atakuja asubuhi kufanya mahojiano na wewe ili waweze kujua sababu ya maswaibu yaliyokukuta" alifafanua nesi yule kwa ufasaha mkubwa juu ya muendelezo wa matibabu ya Kachero Manu.

Baada muda kikaletwa chakula cha usiku, ulikuwa ni mtori, hapo Kachero Manu hakujivunga alikuwa na ubao mkali akaushambulia mtori huo kama anafukuzwa vile. Baada ya kumaliza sasa akawa na nguvu za kutosha akawa anapanga mipango ya kupiga tukio la kutoroka. Uzuri kwenye wodi ile ya watu wawili alikuwa peke yake kitanda kingine kilikuwa tupu. Kwa makisio yake muda kipindi hicho killikuwa ni kati ya saa 3-4 usiku. Akanyanyuka na kwenda kwenye bafu lililomo ndani mle na kufungulia maji kwa nguvu kisha akatoka bafuni kuelekea mlango wa kutoka nje ya chumba cha wodi.

"Hamna ruhusa kutoka wodini usiku mbona nyie wagonjwa wabishi sana! " alikoroma mlinzi wa kampuni anayelinda wodi hiyo aliyolazwa Kachero Manu iliyopo ghorofa ya nne. Alikoroma baada ya kumuona Kachero Manu anamfuata huku akiwa amevaa pajama za hospitali na mkononi ana kanula ya kuingizia dripu mwilini. "Samahani kwa usumbufu kuna tatizo chumbani kwangu nahitaji msaada wako! " aliongea Kachero Manu kwa sauti ya kuigiza upole ambayo kama ungeisikia lazima ungemsikiliza. Mlinzi yule kwa mwendo wa mashi mashi akaharakia kumfuata Kachero Manu bila kujiuliza mara mbili mbili.

Kachero Manu akamua atangulie kwa mbele yake huku yeye anamfuata kwa nyuma huku anamng'ong'a kisogoni kuwa habari yake imekwisha tayari. Walipoingia tu Kachero Manu akaubugaza mlango kisha akaendelea kumfuata kisengesenge yule mlinzi. "Kuna tatizo gani mbona sioni kitu? "aliuliza mlinzi yule kwa mshangao huku anamgeukia Kachero Manu. "Ni hapo bafuni kama maji yananii vilee..." kabla hajamaliza, mlinzi yule kwa tunumba tunumba zake akafungua mlango wa bafu, hamadi akateleza kabla hajaanguka kachero Manu akamdaka na kumtuliza na kareti moja matata ya shingoni iliyosababisha apoteze fahamu mlinzi yule.

Hima hima akamburuza mpaka nje ya bafu akamvua nguo zake za kampuni ya ulinzi kisha akavua pajama zake na kumvisha yeye. Bila kupoteza muda akatinga zile nguo, buti na kofia za kampuni ya ulinzi za yule mlinzi tahamaki alipojiangalia kwenye kioo utasema mlinzi kweli. Uzuri vimo vyao vilikuwa vinaendana hivyo nguo haikumpwaya kabisa. Pia akachukua simu ya tochi ya mlinzi yule iweze kumsaidia kuwasiliana na wadau wake muhimu ikibidi.

Akamlaza kitandani yule mlinzi akamfunika vizuri na shuka kama mgonjwa kweli. Kachero Manu anataka kufungua mlango atoke nje akachungulia kidogo kwa nje akaona mtu yoyote kwenye ile varanda haraka haraka akaanza kutembea na kushuka ngazi za jengo lile. Aliposhuka mpaka alipofika ngazi za roshani ya pili mbele yake akawaona maafisa wa polisi wawili na daktari wake Kachero Manu wanakuja kwa kupanda ngazi. Kachero Manu akajifanya hawajali akapishana nao huku ameinamisha kichwa chini ili asije kugonganisha macho na daktari wake.

Akapishana nao bila vikwazo vyovyote, huku akijua fika wanamfuata yeye wakiwa wamebadilisha muda wa kumfanyia mahojiano. Lakini sasa wameula wa chuya hawatomkuta wataona manyoya tu kitandani. Kachero Manu akatoka nje ya geti kuangazaangaza, mara moja akapata taksi iliyopo jirani na hospitali hiyo ya Muhimbili. "Nipeleke Posta tafadhali" alizungumza Kachero Manu akiwa ameshaingia siti ya nyuma ya gari lile. "Hamna noma ni buku kumi tu usiku huu..." alijibu yule dereva huku anaanza kulitoa gari lile kwa mwendo wa taratibu. Kachero Manu hakutia neno kuonyesha amekubaliana na bei hiyo.
 
HUBA LA MISS TANZANIA-PART 28
Dr.Sonko alikuwa alikuwa anajipeleka kwenye mdomo wa mamba bila kujua.

"Alipoona msimamo wangu ni thabiti sitaki katakata kuvunja uchumba na wewe, akakasirika sana. Akaamua anidhihirishie waziwazi kuwa yeye ni mgonjwa, ana virusi vya UKIMWI. Nilikuaga siku moja kuwa ninasafiri kikazi kwenda Mwanza kwa muda wa siku mbili. Yeye Dr.Sonko akapewa taarifa na mnyetishaji wake wa pale kazini kwetu kuwa nipo Mwanza kikazi.

Nikiwa sina hili wala lile nikashtukia Dr.Sonko amekuja hotelini nilipofikia. Nilikuwa nimeshachoshwa nae ila sina jinsi ya kujivua nae. Kwa madaraka yake alikuwa na uwezo wa kunidhuru vyovyote apendavyo kuanzia kunifukuzisha kazi mpaka hata kuondosha uhai wangu kama angependa.

Sikuwa na jinsi nikalala nae usiku wake huo. Asubuhi wakati anaenda kuoga kujiandaa aondoke zake, kwenye mkoba wake mezani nikaona kitu kama vidonge. Nikapatwa na tashwishi ya kupekenyua kujua ni vidonge vya nini. Nilipoviona tu moyo wangu ulinilipuka na kuanza kwenda mbio mbio.

Vilikuwa ni vidonge vya wagonjwa UKIMWI, ARV. Alipotoka bafuni akanikuta machozi yananitiririka mashavuni huku nimeshika mkononi vile vidonge vyake. Akacheka sana akaniambia kashaniambukiza UKIMWI hawezi kunisaidia chochote. Akaondoka zake na mimi nikakatisha safari yangu na kurejea Dar es Salaam. Sikutaka kupima UKIMWI kujua kama nimeathirika. Nilikuwa ninajipa matumaini huenda Sijaambukizwa.

Chambilecho mficha ugonjwa mauti humuumbua, siku tuliyopima wakati tunataka kufunga pingu za maisha ndipo nikagundulika nina virusi vya UKIMWI. Lawama zote nazibebesha kwa Dr.Sonko....", Shebby alikuwa amezama kwenye dimbwi la mawazo amejisahau kabisa kama mbele yake kuna mgeni mahashumu.Alikuwa anairejea kichwani barua ya mpenzi wake aliyoiacha kabla hajajitoa uhai wake.

" Hellow....mrembo hongereni kwa ugunduzi mzuri" ilikuwa ni sauti ya Naibu Katibu Mkuu, Dr.Sonko akiwa yupo mbele ya Shebby ndio iliyomzindua kutoka kwenye lindi la mawazo.

"Karibu sana Mheshimiwa sisi tumekuja na teknolojia ya paka mashine unaweza kushika umjaribu.." alizungumza Shebby kwa sauti ya kuigiza kama mwanamke kwa kuzungumzia kwenye tundu za pua huku machozi yanamtiririka.

"Ondosha uwoga binti jiamini, msaidizi wangu atachukua mawasiliano yako kwa ajili ya kuona namna nitakavyokuendeleza ha...ha... ha.. " alizungumza Dr.Sonko kwa madahiro huku anacheka na kumpigapiga mgongoni yule anayemdhania ni mwanamke kumbe ni mbaya wake Shebby.

Sasa ilifika wakati wa mgeni rasmi huyo, Dr.Sonko kujaribisha hiyo mashine paka. "Nooo... Noooo.... Noooo........." ilikuwa ni sauti ya Kachero Manu akimkataza Naibu Waziri Mkuu asijaribishe hiyo mashine huku tayari akishafyatua risasi kwenye mkono wa Dr.Sonko na risasi nyingine akimlenga Shebby kifuani mwake.

"Aaaaaaah......nakuf... aaah......"ilikuwa ni sauti ya Dr.Sonko akipiga kelele huku mlipuko mkubwa wa bomu ukitokea eneo lile la maonyesho. Mtifuano, timbwili na mkanyagano ukaibuka eneo lile, huku kila mmoja Yalabi toba! anapiga kelele kwa Mungu wake kuomba kuokolewa na madhara ya mlipuko huo huku walionusurika wakitafuta mlango wa kutokea.

Maonyesho yenyewe yakavurugikia hapo huku watu wakijeruhiana kwa kukanyagana na kupoteza mali zao za thamani.

Shambulio hilo la bomu lililotokea katika viwanja vya Sabasaba lilivurumisha kivumbi kizito nchi nzima ilikuwa inazizima. Taarifa rasmi ya idadi ya watu waliofariki kwenye shambulio hilo ilikuwa bado haijajulikana. Vidinga popo na wale habari kauzwa ndio ulikuwa uwanja wao wa kusambaza taarifa za uzushi na uwongo ili kuchochea hofu na taharuki katika jamii.

Ilipofika majira ya usiku mbichi wa saa 2:00 usiku wananchi walikuwa wamejikusanya kwenye runinga zao majumbani na kwenye kumbi za starehe kusubiria taarifa ya habari ili kujua taarifa rasmi ya serikali ya juu ya tukio hilo.

Taarifa rasmi iliyotolewa na msemaji wa serikali ilieleza kinagaubaga kuwa Shabani Zomboko ndio mhusika wa utegeshaji wa bomu hilo akiwa amejigeuza kama mwanamke na tayari ameshauawa pale pale na afisa wa usalama. Ilieleza kuwa marehemu Shabani Zomboko ndio pia mhusika wa matukio ya mauaji ya mfanyabiashara Pateli na mhadhiri wa chuo cha fedha, Profesa Kaganda. Pia ikaelezwa kuwa barua yenye maelezo ya sababu ya marehemu Shabani Zomboko kufanya mauaji hayo ya kutisha ipo mikononi mwa dola.

Pia ikatangazwa kuwa jeshi la polisi linawashikilia baadhi ya wanafunzi wa kike wa vyuo mbalimbali kwa kula njama ya kushiriki shambulio hilo ovu kwa kumruhusu mtu asiye mwanachuo kukaa kwenye banda lao. Ilitajwa kuwa idadi ya watu zaidi ya 20 wamepoteza uhai kutokana na mkanyagano wa hapo uwanjani.

Pia ikaelezwa kuwa Naibu Waziri Mkuu Dr Sonko yupo hai amesalimika kwenye shambulio hilo isipokuwa amejuruhiwa vibaya kwa kukatika mikono yake yote miwili na mguu wake mmoja, pia amepofuka macho yote mawili. Taarifa hiyo ikaishia huku ikawataka wananchi waendelee kuwa watulivu huku wakiviachia vyombo vya dola viliendelea na uchunguzi wao.

THE END OF THE STORY
 
HUBA LA MISS TANZANIA-PART 28
Dr.Sonko alikuwa alikuwa anajipeleka kwenye mdomo wa mamba bila kujua.

"Alipoona msimamo wangu ni thabiti sitaki katakata kuvunja uchumba na wewe, akakasirika sana. Akaamua anidhihirishie waziwazi kuwa yeye ni mgonjwa, ana virusi vya UKIMWI. Nilikuaga siku moja kuwa ninasafiri kikazi kwenda Mwanza kwa muda wa siku mbili. Yeye Dr.Sonko akapewa taarifa na mnyetishaji wake wa pale kazini kwetu kuwa nipo Mwanza kikazi.

Nikiwa sina hili wala lile nikashtukia Dr.Sonko amekuja hotelini nilipofikia. Nilikuwa nimeshachoshwa nae ila sina jinsi ya kujivua nae. Kwa madaraka yake alikuwa na uwezo wa kunidhuru vyovyote apendavyo kuanzia kunifukuzisha kazi mpaka hata kuondosha uhai wangu kama angependa.

Sikuwa na jinsi nikalala nae usiku wake huo. Asubuhi wakati anaenda kuoga kujiandaa aondoke zake, kwenye mkoba wake mezani nikaona kitu kama vidonge. Nikapatwa na tashwishi ya kupekenyua kujua ni vidonge vya nini. Nilipoviona tu moyo wangu ulinilipuka na kuanza kwenda mbio mbio.

Vilikuwa ni vidonge vya wagonjwa UKIMWI, ARV. Alipotoka bafuni akanikuta machozi yananitiririka mashavuni huku nimeshika mkononi vile vidonge vyake. Akacheka sana akaniambia kashaniambukiza UKIMWI hawezi kunisaidia chochote. Akaondoka zake na mimi nikakatisha safari yangu na kurejea Dar es Salaam. Sikutaka kupima UKIMWI kujua kama nimeathirika. Nilikuwa ninajipa matumaini huenda Sijaambukizwa.

Chambilecho mficha ugonjwa mauti humuumbua, siku tuliyopima wakati tunataka kufunga pingu za maisha ndipo nikagundulika nina virusi vya UKIMWI. Lawama zote nazibebesha kwa Dr.Sonko....", Shebby alikuwa amezama kwenye dimbwi la mawazo amejisahau kabisa kama mbele yake kuna mgeni mahashumu.Alikuwa anairejea kichwani barua ya mpenzi wake aliyoiacha kabla hajajitoa uhai wake.

" Hellow....mrembo hongereni kwa ugunduzi mzuri" ilikuwa ni sauti ya Naibu Katibu Mkuu, Dr.Sonko akiwa yupo mbele ya Shebby ndio iliyomzindua kutoka kwenye lindi la mawazo.

"Karibu sana Mheshimiwa sisi tumekuja na teknolojia ya paka mashine unaweza kushika umjaribu.." alizungumza Shebby kwa sauti ya kuigiza kama mwanamke kwa kuzungumzia kwenye tundu za pua huku machozi yanamtiririka.

"Ondosha uwoga binti jiamini, msaidizi wangu atachukua mawasiliano yako kwa ajili ya kuona namna nitakavyokuendeleza ha...ha... ha.. " alizungumza Dr.Sonko kwa madahiro huku anacheka na kumpigapiga mgongoni yule anayemdhania ni mwanamke kumbe ni mbaya wake Shebby.

Sasa ilifika wakati wa mgeni rasmi huyo, Dr.Sonko kujaribisha hiyo mashine paka. "Nooo... Noooo.... Noooo........." ilikuwa ni sauti ya Kachero Manu akimkataza Naibu Waziri Mkuu asijaribishe hiyo mashine huku tayari akishafyatua risasi kwenye mkono wa Dr.Sonko na risasi nyingine akimlenga Shebby kifuani mwake.

"Aaaaaaah......nakuf... aaah......"ilikuwa ni sauti ya Dr.Sonko akipiga kelele huku mlipuko mkubwa wa bomu ukitokea eneo lile la maonyesho. Mtifuano, timbwili na mkanyagano ukaibuka eneo lile, huku kila mmoja Yalabi toba! anapiga kelele kwa Mungu wake kuomba kuokolewa na madhara ya mlipuko huo huku walionusurika wakitafuta mlango wa kutokea.

Maonyesho yenyewe yakavurugikia hapo huku watu wakijeruhiana kwa kukanyagana na kupoteza mali zao za thamani.

Shambulio hilo la bomu lililotokea katika viwanja vya Sabasaba lilivurumisha kivumbi kizito nchi nzima ilikuwa inazizima. Taarifa rasmi ya idadi ya watu waliofariki kwenye shambulio hilo ilikuwa bado haijajulikana. Vidinga popo na wale habari kauzwa ndio ulikuwa uwanja wao wa kusambaza taarifa za uzushi na uwongo ili kuchochea hofu na taharuki katika jamii.

Ilipofika majira ya usiku mbichi wa saa 2:00 usiku wananchi walikuwa wamejikusanya kwenye runinga zao majumbani na kwenye kumbi za starehe kusubiria taarifa ya habari ili kujua taarifa rasmi ya serikali ya juu ya tukio hilo.

Taarifa rasmi iliyotolewa na msemaji wa serikali ilieleza kinagaubaga kuwa Shabani Zomboko ndio mhusika wa utegeshaji wa bomu hilo akiwa amejigeuza kama mwanamke na tayari ameshauawa pale pale na afisa wa usalama. Ilieleza kuwa marehemu Shabani Zomboko ndio pia mhusika wa matukio ya mauaji ya mfanyabiashara Pateli na mhadhiri wa chuo cha fedha, Profesa Kaganda. Pia ikaelezwa kuwa barua yenye maelezo ya sababu ya marehemu Shabani Zomboko kufanya mauaji hayo ya kutisha ipo mikononi mwa dola.

Pia ikatangazwa kuwa jeshi la polisi linawashikilia baadhi ya wanafunzi wa kike wa vyuo mbalimbali kwa kula njama ya kushiriki shambulio hilo ovu kwa kumruhusu mtu asiye mwanachuo kukaa kwenye banda lao. Ilitajwa kuwa idadi ya watu zaidi ya 20 wamepoteza uhai kutokana na mkanyagano wa hapo uwanjani.

Pia ikaelezwa kuwa Naibu Waziri Mkuu Dr Sonko yupo hai amesalimika kwenye shambulio hilo isipokuwa amejuruhiwa vibaya kwa kukatika mikono yake yote miwili na mguu wake mmoja, pia amepofuka macho yote mawili. Taarifa hiyo ikaishia huku ikawataka wananchi waendelee kuwa watulivu huku wakiviachia vyombo vya dola viliendelea na uchunguzi wao.

THE END OF THE STORY
Ahsante sana kaka
 
Back
Top Bottom