mpasta
JF-Expert Member
- Jan 17, 2011
- 917
- 1,997
Mtunzi: Badi .M.Bao
Email: badi.bao11@gmail.com
Mobile: 0625920847
HUBA LA MISS-TANZANIA-PART 01
Mchakamchaka chinja la mgambo limelia, asiye na mwana aeleke jiwe, hoi hoi, shamrashamra, vifijo na nderemo vilitawala nyumbani kwa bwana na bibi Shamsi Sakuzindwa aliyekuwa anaozesha binti yake mpendwa mwenye kupendeza kama lilivyo tamu jina lake, Zabibu.
Ilikuwa ni siku ya hitimisho la uchumba wao wa zaidi ya miaka mitatu mfululizo wa kijana Shebby na Zabibu. Vijana ambao penzi lao lilikuwa mithili ya mapacha au kumbikumbi wanaoambatana pamoja kila wakati kwenye kila kiunga cha jiji la Dar es Salaam. Kijiji kizima cha Mzundu kilichopo wilayani Handeni, mkoani Tanga, siku kilikuwa kimepiga kambi nyumbani hapo karibia juma zima kuhakikisha ndoa hiyo inapita kwa amani na usalama. Walikuja kuwapongeza wawili hao kwa kuonyesha mfano halisi wa ujasiri wenye busara wa kufunga ndoa na kuishi kama mke na mume na si mahawara kwenye uchumba sugu kama ilivyo kwa vijana wengi ambao wanaiogopa ndoa kama ukoma.
Kama ujuavyo, ndoa si kitu cha mchezo mchezo kwa kuwa ni kutimiza amri ya Mwenyezi Mungu na kudhihirisha kukua kiakili na kimwili pia. Usiku wake kulikuwa na mkesha wa ngoma za jadi za kabila lao la Wazigua, ngoma za Mkweso na Machindi zilizovurumishwa mpaka liamba zikiburudisha wageni waalikwa. Asubuhi yake sherehe ya kitamaduni ikatamatishwa, ikawa sasa ni sherehe rasmi ya ndoa ya kiislamu ikihitimisha sherehe nzima za juma lote. Dufu, ngoma maarufu katika hafla za kiislamu zikawa zinapigwa na kuchezwa kwa mitikisiko yenye kuvutia katika masikio na macho ya mtazamaji toka kwa vijana wa madrasa ya hapo hapo kijijini Mzundu. Sauti za kuvutia za nyimbo za kaswida zinazoimbwa kwa lafudhi ya lugha ya kiarabu na kiswahili zilisikika. Sauti ambazo zilikuwa zikiambatana na milio ya nai na zumari huku midundo ya dufu za aina mbalimbali kama ogani, namba wani, besi, kibakubaku na nyinginezo nyingi zikawa zinadundwa kwa ustadi wa hali ya juu.
Siku hiyo mashamushamu yake yalikuwa sio ya kawaida, hata ndege angani na wanyama porini nadhani nao walipashika habari ya sherehe hiyo kuwa Zabibu kapata mchumba sasa anaolewa, kutokana na hekaheka na pilikapilika zilizoambatana na furaha sheshe ya wanakijiji hao. Waoaji walikuwa wanatokea jijini Dar es Salaam, na tayari walikuwa wameshawasili katika viunga vya kijiji hicho wanavinjari na motakaa zao za gharama tayari kumnyakua mwali, fujo zao tu kila mtu alijua, majogoo ya mjini hayooo yamekuja kuwika kijijini.
Walikuwa wamekuja na sanduku zima la vihendo maalumu kwa ajili ya bibi harusi, na familia yake, kama nguo, seti za mapambo ya dhahabu, viatu na vikorokoro vingi tu vya kuchombeza shughuli hiyo ili mradi ifane vile inavyopaswa kutokana na hadhi ya mrembo Zabibu. Bila kusahau moja ya bidhaa za mahari ya kimila walizoagizwa kuja nazo siku ya harusi kama tundu la mwigazi, ambaye ni kuku mtetea na vifaranga vyake saba, blanketi na mkongojo wa babu.
Mama mzaa chema hakuwa nyuma katika tafrija hiyo, furaha yake ilikuwa fokofoko akijifunga kibwebwe kiunoni kusakata burudani mbalimbali zilizokuwa zimeipamba siku hiyo adhimu kwa familia yao. Ndugu, jamaa na majirani kila wakati walikuwa wanamzingira na kumsukasuka kwa ajili ya kumpa mkono wa pongezi, wengine wanampa tuzo ya pesa, vitenge na kuitakia sherehe hiyo iwe ya heri na fanaka. Kwenye upande wa maakuli na mashrabu nako kulikuwa ni moto wa gesi, hii bila kusahau ni sekta muhimu kabisa kwenye sherehe yoyote ile ipate kufana. Si unajua Tanga kwa misosi ndio kwenyewe!. Sasa unafikiria nini kwenye mambo kama hayo? Usipime unaambiwa, wanawake wao mikono yao ina uchawi maalumu wa upishi wa ngano, basi kupitia ngano wanaweza kukutengenezea sambusa, visheti, maandazi, chapati, kalimati na vinginevyo vingi katika mahanjumati.
Kwa waliokuwepo hapo kijijini siku hiyo, walifaidi hadi kusaza mahanjumati. Kama ilivyozoeleka katika sherehe nyingi, huwa kuna muda maalumu wa chakula na mara nyingi huwa ni katikati au mwishoni mwa sherehe. Sasa unaambiwa kwenye sherehe hiyo ya ndoa ya Zabibu, hayo mambo hayakuwepo, chakula kilikuwa kinaliwa mwanzo mwisho, yaani watu walikuwa wanakula huku ratiba nyingine zikiendelea. Kwenye sekta hiyo familia ilijipanga haswa ng'ombe liliofutwa kodi na mbuzi wa kutosha waliangushwa, kupikia madikodiko na masontojo ya anuwai mbalimbali kuanzia samaki wa kupaka, rosti za nyama, rosti maini, chai ya maziwa, chai ya rangi, chapati, maandazi, vitumbua, na mbwembwe kochokocho za mapishi ya ngano.
Ilikuwa ni sherehe ambayo ilipangwa iache gumzo kijijini hapo karibia miongo kadhaa. Minyoo ya matumbo ya wanakijiji siku hiyo ilishtuka kwa kuvamiwa na chakula jadidi wasichokizoea. Maana vyakula vya asili vinavyopendelewa kuliwa na kabila la Wazigua ni ugali. Ambao unapikwa kutokana na unga wa mahindi yaliyokobolewa na kuvundikwa kwa muda mrefu kabla ya kusagwa au kutwangwa. Baada ya kusagwa hutoa unga mweupe na laini sana. Ugali huo huliwa na mboga za asili kama vile, Kungujulu, Sunga, Kididi, Mnavu, nyama za pori na uyoga, lakini siku hiyo walikuwa wanalishwa chakula cha tabaka aali katika jamii.
Gharama za fujo zote hizo zilibebwa na ofisi anakofanyia kazi binti yao Zabibu. Alikuwa ameajiriwa kwenye moja ya benki za kigeni inayovuma kwa sasa nchini Tanzania ijulikanayo kama 'Turkish Commercial Bank' (T.C.B) akiwa kama afisa uhusiano. Mbali ya ufadhili huo walimuandalia pia sherehe kabambe ya kukata na shoka jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Mlimani City Hall punde tu atakaporejea jijini Dar es Salaam. Sherehe ambayo vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi vilishanunua haki miliki ya kurusha tukio hilo kwa mamilioni sufufu.
Wataachaje kurusha tukio hilo la ndoa ya Miss Tanzania kipenzi cha wananchi, jina lake lilikuwa tamu kama peremende midomoni mwao, asiye na skendo yoyote ya ufuska, wala tabia mbovu za kuchefua jamii!. Hayawi hayawi sasa yakawa, muda uliokuwa unasubiriwa kwa hamu wa kupitishwa kwa nikaha hiyo baina ya Zabibu na mumewe mtarajiwa Shabani Zomboko dereva taksi za UBBER, mzawa wa Kariakoo au maarufu kwa rafiki zake kwa jina la 'Shebby-Zoo' ukawadia. Vyombo vya habari kochokocho kuanzia magazeti, televisheni, redio, blogu mbalimbali za mitandao za kijamii nazo hazikuwa nyuma kuja kurusha taarifa ya hafla hiyo kutoka kijijini.
Vyombo hivyo vilitaka kupaisha habari hiyo ya ndoa ya mlimbwende Zabibu Shamsi, mshindi wa taji la mrembo wa nchi, Miss Tanzania. Motakaa za kila aina zilitapakaa kijijini pale, kupamba mandhari ya sherehe hiyo, zikitokea pande mbalimbali za Tanzania kujua kushuhudia tukio hilo adhimu. Yalikuwa ni magari ya mashoga zake Zabibu na rafikize Shebby walikuja kuwaunga mkono kwenye tukio ambalo hata malaika wa mbinguni hupiga vigeregere kwa furaha pindi wapendanao wanapofunga ndoa.
Pia Mwenyezi Mungu, khalaka wa ardhi, mbingu na vilivyomo baina ya mbingu na ardhi nae anafurahi sana, pindi wanaadamu wanapochukua maamuzi ya kufunga pingu za maisha. Lakini aksi yake Ibilisi, shetani mkuu anakuwa na huzuni na hasira za kupitiliza pindi ambapo watu wanapofanya maamuzi ya kuungana kuwa mwili mmoja. Kwasababu anakosa wateja wake katika dhambi yake pendwa ya uzinifu, anaona wamemuacha solemba kwenye mataa. Nikaha hiyo ilipangwa kufungwa majira ya dhuhaa katika wakati wa mafungulia ng'ombe, baina ya saa 2-3 asubuhi katika msikiti wa ijumaa wa hapo kijijini, kisha sherehe zote kwenda kuhitimishwa nyumbani kwa bibi harusi. Huko kwa bibi harusi ndipo watu watakula, watakunywa na kucheza kutwa nzima mpaka majira ya usiku mbichi ndio itakuwa tamati yake.
Bwana harusi Shebby-Zoo akiwa amesindikizwa na wapambe zake ithnani wa chanda na pete, wa toka utotoni. Wamecheza mpira wa chandimu wote mpaka sasa wamekuwa wakubwa bado ni maswaiba. Walikuwa tayari wamewasili msikitini wanasubiri kukabidhiwa jiko lao la Kizigua warudi nalo jijini Dar es Salaam wakaendekeze libeneke la sherehe upya. Walikuwa wamevalia kanzu zao nyeupe nadhifu na majoho ya rangi ya kijani yenye ufito wa rangi ya samawati kwenye kola zake, huku vichwa vyao vikifunikwa na kofia za kuziua kwa mkono za rangi ya kahawia. Bwana harusi alikuwa anatembea na mkongojo wa urembo ili mradi kuleta nakshinakshi na mvuto wa muonekano wake. Kwa ujumla Bwana harusi na wapambe wake walipendeza sana machoni pa watazamaji.
Sheikh Ayoub Makoja, shaibu kiumri, unaweza kumkadiria miaka 50-55 kama ukipewa mtihani wa kumpachika umri wake, imamu mkuu wa msikiti huo nae alikuwa nadhifu katika vazi la kanzu yake nyeupe na kilemba kichwani, huku akiwa ana kitabu cha rejista ya ndoa na kitabu kingine maaalumu cha hotuba ya ndoa huku anahesabu tasbihi mkononi. "Salaam Aleikum nyie Wazaramo, karibu sana Handeni, ha.. ha... ha.." Sheikh Ayoub aliwasalimia waoaji, akawataniana kwa bashasha huku pia anapeana nao mikono. "Waleykum salaam Sheikh, ndio tumekuja kumbeba jumla jumla tumpeleke Uzaramoni, binti yenu wa Kizigua" walijibu salamu kwa pamoja kisha mmoja wa mpambe wa Bwana harusi akaujibu utani huo wa Sheikh. "Mmemaliza mahari lakini? Maana zamani enzi sisi tupo vijana kama hujamaliza mahari huondoki na mke!. Unabakia hapo hapo ukweni" alizungumza Sheikh Ayoub na waoaji wale huku wakisubiria watu wazidi kujazana msikitini kushuhudia akidi hiyo.
"Aaaah...Sheikh unatuonaje sisi, Wazaramo hatujazoea kuishi kwa mikopo, sisi ni maskini jeuri tumemaliza mahari yote na vihendo juu tumezidisha" alijibu mpambe yule ambaye alikuwa ni fundi wa matani. "Vizuri sana mnaonyesha mmepania, ila zamani hali ilikuwa tete sana. Wazee wa mila walikuwa wanaandaa tukio linaitwa Kulagasama. Hilo ni tukio la kuagwa kwa waliooana mara baada ya kukamilisha mahari na taratibu zote za kimila. Katika mila za Kizigua, ilikuwa mtu anapofunga nikaha, yeye na mkewe hutakiwa kukaa katika familia ya mke wake huyo kwa muda fulani ili aweze kukamilisha mahari kama alikuwa hajamaliza. Hivyo akimaliza kulipa mahari na mambo mengine yanayohitajika, huomba ruhusa toka kwa wakwe zake ili akaanzishe maisha yake na mkewe. Alikuwa kama akishindwa kulipa ataendelea kuishi upande wa mkewe kwa maisha yake yote na hata kama akifariki atazikwa upande wa ukweni kama ukoo wa upande wa mume hautamlipia, ila kama wakimlipia watapewa mwili kuzika upande wa mume. Lakini sasa mna raha sana mila na desturi sehemu nyingi hazifuatwi ipasavyo" alisimulia kwa uso wa bashasha Sheikh Ayoub mambo jinsi yalivyokuwa enzi zao wako barobaro mambo yalivyokuwa.
"Sheikh unachosema ni ukweli kabisa wala hatukubishii, kila zama na kitabu chake, siku hizi kuanzia sherehe za unyago, jando, harusi hamna tena ngoma za asili, sasa ni mwendo wa muziki wa singeli tu kwenda mbele" alizungumza kuchangia mazungumzo mpambe mwingine wa Bwana harusi, huku Bwana harusi mwenyewe akiwa amejiinamia chini, amefumbata viganja vyake vya mkononi. Inaonyesha alikuwa kwenye tafakuri nzito juu ya jambo analotaka kulielekea katika historia ya maisha yake. Tukio ambalo litambadilisha sasa na kuitwa mume wa Zabibu, pia tukio ambalo Mwenyezi Mungu akiwabariki watapata matunda ya ndoa, ambayo ni watoto, hivyo atakuja kuitwa baba fulani.
"Assalamu alaykum warahmatullah wabarakaatuhu jamiaaa.." Sheikh alikatisha mazungumzo baada ya kuona idadi ya watu wameshajazana pomoni msikitini wanasubiria shughuli ya kufungisha ndoa ianze, kisha akawasalimia kwa salamu maarufu kwa waislamu. "Waalekum salaam warahmatullah wabarakatuhu" wakajibu wote kwa nidhamu na taadhima salamu toka kwa Sheikh wao. "Sasa tunataka tuanze ibada ya kufungisha ndoa.
Mtume wetu Muhammad (S.A.W) ametufundisha kuwa Kukamilika ndoa lazima kwanza yatimie masharti yafuatayo:
kwanza ipatikane Idhini ya Walii. Alhamdulillahi baba mzazi wa muolewa yupo hapa Mzee Shamsi kashafika msikitini. Pili, Kuridhika kwa bibi harusi mtarajiwa. Hivyo hili sharti tutatuma watu nyumbani kwa bibi harusi kumuuliza kama hii ndoa anaifahamu na ameridhia. Sharti la tatu ni kutimia kwa tamko la ndoa yaani Ijaab na Qabuul, yaani iijab na qubuul iliyounganishwa kwa tamko la ndoa au yenye kufidisha maana hiyo. Sharti la nne ni kuwepo kwa mashahidi wawili waadilifu. Na mwisho Kubalighi na kuwa na utambuzi baina ya wanandoa, hivyo haifai kuwepo kwa ndoa ikiwa mmoja wapo ni mwendawazimu au mdogo kwa umri na bado hajabaleghe. Sasa kabla sijaanza khotuba ya ndoa, ningependa shahidi mmoja wa upande wa muoaji na mwingine kutoka kwa muolewa waelekee mubashara mara moja nyumbani kwa Bibi harusi wakamuulize kama anazo habari ya hili tukio linalotaka kuendelea hapa msikitini.
Tunawapa muda wa nusu saa muwe mmesharejea, Inshallah maa-salaaam" alitoa maelezo yenye ufasaha Sheikh Ayoub, mara moja akanyanyuka mmoja wa wapambe wa Bwana harusi na mwakilishi wa kikeni wakaelekea nyumbani kwa Mzee Shamsi, baba wa Zabibu. Baba mzazi wa Zabibu na waumini wengineo wakabakia ndani ya msikiti wanabadilishana mambo mawili matatu. Zikapita sekunde, dakika, sasa yakawa masaa walioenda nyumbani kwa mwali hawajarejea. Taharuki ikaanza kutawala mule msikitini, zogo la minong'ono likaanza kusambaa mle msikitini.
JE NDOA ITAFUNGWA KWELI AU BIBI HARUSI KALALA MITINI??
Email: badi.bao11@gmail.com
Mobile: 0625920847
HUBA LA MISS-TANZANIA-PART 01
Mchakamchaka chinja la mgambo limelia, asiye na mwana aeleke jiwe, hoi hoi, shamrashamra, vifijo na nderemo vilitawala nyumbani kwa bwana na bibi Shamsi Sakuzindwa aliyekuwa anaozesha binti yake mpendwa mwenye kupendeza kama lilivyo tamu jina lake, Zabibu.
Ilikuwa ni siku ya hitimisho la uchumba wao wa zaidi ya miaka mitatu mfululizo wa kijana Shebby na Zabibu. Vijana ambao penzi lao lilikuwa mithili ya mapacha au kumbikumbi wanaoambatana pamoja kila wakati kwenye kila kiunga cha jiji la Dar es Salaam. Kijiji kizima cha Mzundu kilichopo wilayani Handeni, mkoani Tanga, siku kilikuwa kimepiga kambi nyumbani hapo karibia juma zima kuhakikisha ndoa hiyo inapita kwa amani na usalama. Walikuja kuwapongeza wawili hao kwa kuonyesha mfano halisi wa ujasiri wenye busara wa kufunga ndoa na kuishi kama mke na mume na si mahawara kwenye uchumba sugu kama ilivyo kwa vijana wengi ambao wanaiogopa ndoa kama ukoma.
Kama ujuavyo, ndoa si kitu cha mchezo mchezo kwa kuwa ni kutimiza amri ya Mwenyezi Mungu na kudhihirisha kukua kiakili na kimwili pia. Usiku wake kulikuwa na mkesha wa ngoma za jadi za kabila lao la Wazigua, ngoma za Mkweso na Machindi zilizovurumishwa mpaka liamba zikiburudisha wageni waalikwa. Asubuhi yake sherehe ya kitamaduni ikatamatishwa, ikawa sasa ni sherehe rasmi ya ndoa ya kiislamu ikihitimisha sherehe nzima za juma lote. Dufu, ngoma maarufu katika hafla za kiislamu zikawa zinapigwa na kuchezwa kwa mitikisiko yenye kuvutia katika masikio na macho ya mtazamaji toka kwa vijana wa madrasa ya hapo hapo kijijini Mzundu. Sauti za kuvutia za nyimbo za kaswida zinazoimbwa kwa lafudhi ya lugha ya kiarabu na kiswahili zilisikika. Sauti ambazo zilikuwa zikiambatana na milio ya nai na zumari huku midundo ya dufu za aina mbalimbali kama ogani, namba wani, besi, kibakubaku na nyinginezo nyingi zikawa zinadundwa kwa ustadi wa hali ya juu.
Siku hiyo mashamushamu yake yalikuwa sio ya kawaida, hata ndege angani na wanyama porini nadhani nao walipashika habari ya sherehe hiyo kuwa Zabibu kapata mchumba sasa anaolewa, kutokana na hekaheka na pilikapilika zilizoambatana na furaha sheshe ya wanakijiji hao. Waoaji walikuwa wanatokea jijini Dar es Salaam, na tayari walikuwa wameshawasili katika viunga vya kijiji hicho wanavinjari na motakaa zao za gharama tayari kumnyakua mwali, fujo zao tu kila mtu alijua, majogoo ya mjini hayooo yamekuja kuwika kijijini.
Walikuwa wamekuja na sanduku zima la vihendo maalumu kwa ajili ya bibi harusi, na familia yake, kama nguo, seti za mapambo ya dhahabu, viatu na vikorokoro vingi tu vya kuchombeza shughuli hiyo ili mradi ifane vile inavyopaswa kutokana na hadhi ya mrembo Zabibu. Bila kusahau moja ya bidhaa za mahari ya kimila walizoagizwa kuja nazo siku ya harusi kama tundu la mwigazi, ambaye ni kuku mtetea na vifaranga vyake saba, blanketi na mkongojo wa babu.
Mama mzaa chema hakuwa nyuma katika tafrija hiyo, furaha yake ilikuwa fokofoko akijifunga kibwebwe kiunoni kusakata burudani mbalimbali zilizokuwa zimeipamba siku hiyo adhimu kwa familia yao. Ndugu, jamaa na majirani kila wakati walikuwa wanamzingira na kumsukasuka kwa ajili ya kumpa mkono wa pongezi, wengine wanampa tuzo ya pesa, vitenge na kuitakia sherehe hiyo iwe ya heri na fanaka. Kwenye upande wa maakuli na mashrabu nako kulikuwa ni moto wa gesi, hii bila kusahau ni sekta muhimu kabisa kwenye sherehe yoyote ile ipate kufana. Si unajua Tanga kwa misosi ndio kwenyewe!. Sasa unafikiria nini kwenye mambo kama hayo? Usipime unaambiwa, wanawake wao mikono yao ina uchawi maalumu wa upishi wa ngano, basi kupitia ngano wanaweza kukutengenezea sambusa, visheti, maandazi, chapati, kalimati na vinginevyo vingi katika mahanjumati.
Kwa waliokuwepo hapo kijijini siku hiyo, walifaidi hadi kusaza mahanjumati. Kama ilivyozoeleka katika sherehe nyingi, huwa kuna muda maalumu wa chakula na mara nyingi huwa ni katikati au mwishoni mwa sherehe. Sasa unaambiwa kwenye sherehe hiyo ya ndoa ya Zabibu, hayo mambo hayakuwepo, chakula kilikuwa kinaliwa mwanzo mwisho, yaani watu walikuwa wanakula huku ratiba nyingine zikiendelea. Kwenye sekta hiyo familia ilijipanga haswa ng'ombe liliofutwa kodi na mbuzi wa kutosha waliangushwa, kupikia madikodiko na masontojo ya anuwai mbalimbali kuanzia samaki wa kupaka, rosti za nyama, rosti maini, chai ya maziwa, chai ya rangi, chapati, maandazi, vitumbua, na mbwembwe kochokocho za mapishi ya ngano.
Ilikuwa ni sherehe ambayo ilipangwa iache gumzo kijijini hapo karibia miongo kadhaa. Minyoo ya matumbo ya wanakijiji siku hiyo ilishtuka kwa kuvamiwa na chakula jadidi wasichokizoea. Maana vyakula vya asili vinavyopendelewa kuliwa na kabila la Wazigua ni ugali. Ambao unapikwa kutokana na unga wa mahindi yaliyokobolewa na kuvundikwa kwa muda mrefu kabla ya kusagwa au kutwangwa. Baada ya kusagwa hutoa unga mweupe na laini sana. Ugali huo huliwa na mboga za asili kama vile, Kungujulu, Sunga, Kididi, Mnavu, nyama za pori na uyoga, lakini siku hiyo walikuwa wanalishwa chakula cha tabaka aali katika jamii.
Gharama za fujo zote hizo zilibebwa na ofisi anakofanyia kazi binti yao Zabibu. Alikuwa ameajiriwa kwenye moja ya benki za kigeni inayovuma kwa sasa nchini Tanzania ijulikanayo kama 'Turkish Commercial Bank' (T.C.B) akiwa kama afisa uhusiano. Mbali ya ufadhili huo walimuandalia pia sherehe kabambe ya kukata na shoka jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Mlimani City Hall punde tu atakaporejea jijini Dar es Salaam. Sherehe ambayo vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi vilishanunua haki miliki ya kurusha tukio hilo kwa mamilioni sufufu.
Wataachaje kurusha tukio hilo la ndoa ya Miss Tanzania kipenzi cha wananchi, jina lake lilikuwa tamu kama peremende midomoni mwao, asiye na skendo yoyote ya ufuska, wala tabia mbovu za kuchefua jamii!. Hayawi hayawi sasa yakawa, muda uliokuwa unasubiriwa kwa hamu wa kupitishwa kwa nikaha hiyo baina ya Zabibu na mumewe mtarajiwa Shabani Zomboko dereva taksi za UBBER, mzawa wa Kariakoo au maarufu kwa rafiki zake kwa jina la 'Shebby-Zoo' ukawadia. Vyombo vya habari kochokocho kuanzia magazeti, televisheni, redio, blogu mbalimbali za mitandao za kijamii nazo hazikuwa nyuma kuja kurusha taarifa ya hafla hiyo kutoka kijijini.
Vyombo hivyo vilitaka kupaisha habari hiyo ya ndoa ya mlimbwende Zabibu Shamsi, mshindi wa taji la mrembo wa nchi, Miss Tanzania. Motakaa za kila aina zilitapakaa kijijini pale, kupamba mandhari ya sherehe hiyo, zikitokea pande mbalimbali za Tanzania kujua kushuhudia tukio hilo adhimu. Yalikuwa ni magari ya mashoga zake Zabibu na rafikize Shebby walikuja kuwaunga mkono kwenye tukio ambalo hata malaika wa mbinguni hupiga vigeregere kwa furaha pindi wapendanao wanapofunga ndoa.
Pia Mwenyezi Mungu, khalaka wa ardhi, mbingu na vilivyomo baina ya mbingu na ardhi nae anafurahi sana, pindi wanaadamu wanapochukua maamuzi ya kufunga pingu za maisha. Lakini aksi yake Ibilisi, shetani mkuu anakuwa na huzuni na hasira za kupitiliza pindi ambapo watu wanapofanya maamuzi ya kuungana kuwa mwili mmoja. Kwasababu anakosa wateja wake katika dhambi yake pendwa ya uzinifu, anaona wamemuacha solemba kwenye mataa. Nikaha hiyo ilipangwa kufungwa majira ya dhuhaa katika wakati wa mafungulia ng'ombe, baina ya saa 2-3 asubuhi katika msikiti wa ijumaa wa hapo kijijini, kisha sherehe zote kwenda kuhitimishwa nyumbani kwa bibi harusi. Huko kwa bibi harusi ndipo watu watakula, watakunywa na kucheza kutwa nzima mpaka majira ya usiku mbichi ndio itakuwa tamati yake.
Bwana harusi Shebby-Zoo akiwa amesindikizwa na wapambe zake ithnani wa chanda na pete, wa toka utotoni. Wamecheza mpira wa chandimu wote mpaka sasa wamekuwa wakubwa bado ni maswaiba. Walikuwa tayari wamewasili msikitini wanasubiri kukabidhiwa jiko lao la Kizigua warudi nalo jijini Dar es Salaam wakaendekeze libeneke la sherehe upya. Walikuwa wamevalia kanzu zao nyeupe nadhifu na majoho ya rangi ya kijani yenye ufito wa rangi ya samawati kwenye kola zake, huku vichwa vyao vikifunikwa na kofia za kuziua kwa mkono za rangi ya kahawia. Bwana harusi alikuwa anatembea na mkongojo wa urembo ili mradi kuleta nakshinakshi na mvuto wa muonekano wake. Kwa ujumla Bwana harusi na wapambe wake walipendeza sana machoni pa watazamaji.
Sheikh Ayoub Makoja, shaibu kiumri, unaweza kumkadiria miaka 50-55 kama ukipewa mtihani wa kumpachika umri wake, imamu mkuu wa msikiti huo nae alikuwa nadhifu katika vazi la kanzu yake nyeupe na kilemba kichwani, huku akiwa ana kitabu cha rejista ya ndoa na kitabu kingine maaalumu cha hotuba ya ndoa huku anahesabu tasbihi mkononi. "Salaam Aleikum nyie Wazaramo, karibu sana Handeni, ha.. ha... ha.." Sheikh Ayoub aliwasalimia waoaji, akawataniana kwa bashasha huku pia anapeana nao mikono. "Waleykum salaam Sheikh, ndio tumekuja kumbeba jumla jumla tumpeleke Uzaramoni, binti yenu wa Kizigua" walijibu salamu kwa pamoja kisha mmoja wa mpambe wa Bwana harusi akaujibu utani huo wa Sheikh. "Mmemaliza mahari lakini? Maana zamani enzi sisi tupo vijana kama hujamaliza mahari huondoki na mke!. Unabakia hapo hapo ukweni" alizungumza Sheikh Ayoub na waoaji wale huku wakisubiria watu wazidi kujazana msikitini kushuhudia akidi hiyo.
"Aaaah...Sheikh unatuonaje sisi, Wazaramo hatujazoea kuishi kwa mikopo, sisi ni maskini jeuri tumemaliza mahari yote na vihendo juu tumezidisha" alijibu mpambe yule ambaye alikuwa ni fundi wa matani. "Vizuri sana mnaonyesha mmepania, ila zamani hali ilikuwa tete sana. Wazee wa mila walikuwa wanaandaa tukio linaitwa Kulagasama. Hilo ni tukio la kuagwa kwa waliooana mara baada ya kukamilisha mahari na taratibu zote za kimila. Katika mila za Kizigua, ilikuwa mtu anapofunga nikaha, yeye na mkewe hutakiwa kukaa katika familia ya mke wake huyo kwa muda fulani ili aweze kukamilisha mahari kama alikuwa hajamaliza. Hivyo akimaliza kulipa mahari na mambo mengine yanayohitajika, huomba ruhusa toka kwa wakwe zake ili akaanzishe maisha yake na mkewe. Alikuwa kama akishindwa kulipa ataendelea kuishi upande wa mkewe kwa maisha yake yote na hata kama akifariki atazikwa upande wa ukweni kama ukoo wa upande wa mume hautamlipia, ila kama wakimlipia watapewa mwili kuzika upande wa mume. Lakini sasa mna raha sana mila na desturi sehemu nyingi hazifuatwi ipasavyo" alisimulia kwa uso wa bashasha Sheikh Ayoub mambo jinsi yalivyokuwa enzi zao wako barobaro mambo yalivyokuwa.
"Sheikh unachosema ni ukweli kabisa wala hatukubishii, kila zama na kitabu chake, siku hizi kuanzia sherehe za unyago, jando, harusi hamna tena ngoma za asili, sasa ni mwendo wa muziki wa singeli tu kwenda mbele" alizungumza kuchangia mazungumzo mpambe mwingine wa Bwana harusi, huku Bwana harusi mwenyewe akiwa amejiinamia chini, amefumbata viganja vyake vya mkononi. Inaonyesha alikuwa kwenye tafakuri nzito juu ya jambo analotaka kulielekea katika historia ya maisha yake. Tukio ambalo litambadilisha sasa na kuitwa mume wa Zabibu, pia tukio ambalo Mwenyezi Mungu akiwabariki watapata matunda ya ndoa, ambayo ni watoto, hivyo atakuja kuitwa baba fulani.
"Assalamu alaykum warahmatullah wabarakaatuhu jamiaaa.." Sheikh alikatisha mazungumzo baada ya kuona idadi ya watu wameshajazana pomoni msikitini wanasubiria shughuli ya kufungisha ndoa ianze, kisha akawasalimia kwa salamu maarufu kwa waislamu. "Waalekum salaam warahmatullah wabarakatuhu" wakajibu wote kwa nidhamu na taadhima salamu toka kwa Sheikh wao. "Sasa tunataka tuanze ibada ya kufungisha ndoa.
Mtume wetu Muhammad (S.A.W) ametufundisha kuwa Kukamilika ndoa lazima kwanza yatimie masharti yafuatayo:
kwanza ipatikane Idhini ya Walii. Alhamdulillahi baba mzazi wa muolewa yupo hapa Mzee Shamsi kashafika msikitini. Pili, Kuridhika kwa bibi harusi mtarajiwa. Hivyo hili sharti tutatuma watu nyumbani kwa bibi harusi kumuuliza kama hii ndoa anaifahamu na ameridhia. Sharti la tatu ni kutimia kwa tamko la ndoa yaani Ijaab na Qabuul, yaani iijab na qubuul iliyounganishwa kwa tamko la ndoa au yenye kufidisha maana hiyo. Sharti la nne ni kuwepo kwa mashahidi wawili waadilifu. Na mwisho Kubalighi na kuwa na utambuzi baina ya wanandoa, hivyo haifai kuwepo kwa ndoa ikiwa mmoja wapo ni mwendawazimu au mdogo kwa umri na bado hajabaleghe. Sasa kabla sijaanza khotuba ya ndoa, ningependa shahidi mmoja wa upande wa muoaji na mwingine kutoka kwa muolewa waelekee mubashara mara moja nyumbani kwa Bibi harusi wakamuulize kama anazo habari ya hili tukio linalotaka kuendelea hapa msikitini.
Tunawapa muda wa nusu saa muwe mmesharejea, Inshallah maa-salaaam" alitoa maelezo yenye ufasaha Sheikh Ayoub, mara moja akanyanyuka mmoja wa wapambe wa Bwana harusi na mwakilishi wa kikeni wakaelekea nyumbani kwa Mzee Shamsi, baba wa Zabibu. Baba mzazi wa Zabibu na waumini wengineo wakabakia ndani ya msikiti wanabadilishana mambo mawili matatu. Zikapita sekunde, dakika, sasa yakawa masaa walioenda nyumbani kwa mwali hawajarejea. Taharuki ikaanza kutawala mule msikitini, zogo la minong'ono likaanza kusambaa mle msikitini.
JE NDOA ITAFUNGWA KWELI AU BIBI HARUSI KALALA MITINI??