CABO-DELGADO-PART 39
Dr.Anabella akili yake ilifanya kazi haraka sana baada ya kukataliwa kuingia pale getini. Alifahamu taarifa zake za usaliti zitawafikia wakubwa zake na haitachukua muda atakamatwa kilaini. Hivyo moja kwa moja alikimbilia kwenye ofisi ya mchumba wake Inspekta Mark Noble. Alipoingia alimkuta Katibu Muhtasi wake Edina ameinamia kompyuta anaandika andika nyaraka mbalimbali.
Katibu muhtasi Edina na Dr.Anabella walikuwa wanafahamiana kitambo hasa kutokana na Dr.Anabella kuja ofisini kwa Mark mara kwa mara. "Samahani naingia ofisini kwa Mark kuna nyaraka za kumsafirishia mgonjwa, Mark kanielekeza nizifuate huku, zinahitajika haraka sana" aliomba Dr.Anabella kwa yule sekretari. Bila kipingamizi alijibiwa "hamna shida shemeji ingia tu kuwa na amani tu bila samahani, unataka nikuzuie kesho nikute barua ya kuachishwa kazi" wote kwa pamoja wakaangua kicheko cha nguvu, huku Dr.Anabella akielekea kufungua mlango. Dr.Anabella alitumia mwanya huo huo kujipenyeza ofisini kwa Mark.
Alipoingia moja kwa moja akaelekea kwenye kabati la mtoto wa meza karibu na kiti cha Mark, akavuta droo akautana na funguo nyingi pamoja na rimoti ndogo rangi nyeusi akaibeba akaihifadhi kwenye koti lake kisha akakizunguka kiti cha Mark. Akavuta kwa mbele kabati dogo la kuwekea mafaili ya taarifa za kipolisi alizokuwa anazishughulikia na vitabu mbalimbali.
Chini ya lile kabati kulikuwa na mfuniko wa chuma kama wa kufunikia chemba za choo. Akazitoa marumaru zilizoegeshwa juu ya ule mfuniko akaziweka pembeni. Akavuta ule mfuniko ukafunguka kisha akaingia kwenye shimo lile mpaka alipogusa ngazi ya kwanza ya kushukia chini akarudishia ule mfuniko vizuri kisha akaanza kuteremka ngazi kuelekea kwenye ofisi ya Mark ingine ambayo ipo chini ya handaki. Kwa msaada wa tochi ya simu yake akawa anashuka kwa haraka. Alipofika ngazi ya mwisho akazima tochi yake akajibanza dakika moja kuangalia kama kuna mtu yoyote, bahati ilikuwa kwake. Hakukuwa na mtu yoyote na korido nzima akawa akitembea taa zinawaka wenyewe kwenye korido.
Kulikuwa na mfumo wa kuleta mwanga pindi zinapohisi kuna binadamu anatembea. Akafika mpaka kwenye ofisi ya Mark ambayo ilikuwa ipo mkabala na ofisi ya Bwana Alfredo. Alipofika mlango akatoa rimoti mfukoni mwake akaanza kubonyeza bonyeza tarakimu za siri haikuchukua muda mrefu mlango ule uliotengenezwa kwa madini ya "aluminium" ukaachia ukaa wazi akaingia akaufunga tena kwa rimoti.
Kisha akaelekea kwenye runinga kubwa iliyopo ndani ya kile chumba akawasha umeme ukutani. Akaruhusu umeme uingie kwenye runinga hiyo kisha akaanza kuona kila kinachoendelea kwenye ukumbi wa mkutano mubashara.
Akashtushwa sana na alichokishuhudia kwa macho yake. Alikuwa hasikii sauti yao kinachozungumzwa mle ndani ya chumba cha mkutano ila aliwaona washirika wake, Kachero Manu na Komandoo "JS" wakiwa wamefungwa kwenye viti kwa kutumia mikanda, wakiwa hawana matumaini ya kujiokoa wao wenyewe.
Alivyowasoma wale walinzi wa ukumbi ndani ya muda mfupi namna walivyojipanga matumaini ya kuwaokoa yakaanza kufufuka upya.
Haraka haraka akatoka nje ya chumba cha Mark bila hata kuzima Televisheni. Akakimbilia ngazi za kupanda juu kuelekea kwenye chumba cha mkutano kutokea kule kwenye handaki akiwa na hamasa zote. Huku bastola yake ikiwa mkononi tahadhari kwa lolote litakalotokea, akaanza kupanda ngazi kwa kasi ya ajabu.
Kachero Manu alizindukia ukumbini akijikuta amemwagiwa maji ya baridi akiwa amefungwa kwenye kiti, pembezoni mwake yupo Komandoo "JS" nae akiwa amefungwa mikanda.
"Kachero Emmanuel Joseph" na "Komandoo Jacob Steven" karibuni sana kwenye mkutano ambao mlikuwa mnatamani mhudhurie, nadhani maombi na dua zenu zimekubaliwa na Mungu mmefika salama" alifungua mkutano huo Bwana Alfredo mwenyewe akiwa na kiko yake pembeni ameikamatia kwa mkono wa kushoto.
Kachero Manu na Komandoo "JS" wakatazamana wakionyeshwa kushangazwa kwa wao kujulikana majina yao kiufasaha. Walichokuwa hawakijui ni kuwa kulikuwa na "CCTV-Camera" zenye uwezo wa kuchukua matukio yote pale kiwandani kwa ufasaha. Hivyo ilivyojulikana kuwa kiwandani pamevamiwa, zilienda kuchukuliwa picha za maeneo yote wakaonekana namna walivyoingia, kisha picha za Kachero Manu na Komandoo "JS" zikatumwa kwa washirika wao Tanzania yakaja majibu ya utambuzi wa Kachero Manu lakini Komandoo "JS" hatambuliki. Zikatumwa picha ya Komandoo "JS" kwa washirika wao wa Msumbiji yakaja majibu ya kila kitu kinachomhusu Komandoo "JS".
"Pia nachukua fursa hii kukupongeza Komandoo Jacob Steven kwa kuteuliwa kwako kuiongoza Idara ya Usalama wa Taifa nchi ya Msumbiji, najua kuwa huna hizo taarifa kutokana na kujishughulisha na mambo yasiyokuhusu, mtaka nyingi nasaba hupata mengi majanga hivyo nasikitika huo uteuzi wako na pongezi zako zitaifikia maiti yako. Kesho asubuhi utaokotwa ukiwa maiti na hilo litakuwa ni onyo takatifu kwa wote wanaojifanya wazalendo wa nchi ya Msumbiji" alisema Bwana Alfredo kwa mbwembwe huku anaanza kuvuta kiko chake.
"Mwisho wako na vibaraka wenzako wa wakoloni Bwana Alfredo umefika, Msumbiji huru yenye kujitoa kwenye makucha ya wanyonyaji inakuja. Msumbiji yenye neema ya uchumi wa gesi, mafuta na madini inakuja, hata kama utatumaliza sisi lakini tutakuwa tumekufa kishujaa, aheri kufa mwili lakini mawazo yako yakawa hai vizazi na vizazi ...!" aliropoka Kachero Manu bila kupewa ruksa kwa kudakiza maneno kwa lengo la kupoteza muda ili kuangalia kama kuna fursa yoyote ya kujiokoa itajitokeza.
"Kelele wewe mbwa koko unaropoka bila kupewa ruksa ya kuongea ngoja tukutie adabu kidogo" alifoka Mark kwa hasira huku anamfuata Kachero Manu kwenye kiti chake kwa.
"Mark achana nae, daima mfa maji haachi kutapatapa hata ukimpiga ni kazi bure huyo ni maiti hai inayosubiri kutolewa roho tu" alisema Bwana Alfredo kwa sauti ya dharau. "Nyinyi ni waoga sana mnapambanaje na sisi hali ya kuwa mmetufunga mikono na miguu? mwanaume wa kweli hawi muoga kiasi hiki Bwana Alfredo, tambueni mshahara wa dhambi ni mauti mtakamatwa mapema iwezekanavyo " alisema Komandoo "JS", nae akijaribu kuvuta muda ili kuona kama kuna fursa yoyote ya kujiokoa itajitokeza.
Bwana Alfredo hakujibu kitu bali alikuwa anaangalia mlango wa mbele yake, alikuwa anaingia kipande cha mtu mrefu, amesokota rasta nywele zake, huku mkononi ameshika shoka kubwa limelowa damu damu iliyogandiana, kuonyesha sio shoka la kibisa ni shoka la kazi.
Mtu huyo alikuwa anatembea kwa mikogo analizungusha hewani shoka lake kwa mitindo tofauti tofauti kama Msolopagazi na Inkosikazi yake. Kachero Manu kwake sura hii haikuwa ngeni kwenye mboni zake za macho, akawa anajaribu kufikiria wapi alimuona huyu mtu. Lakini kutokana na maumivu ya kichwa anayohisi akashindwa kupata majibu ya fikra zake.
"Kachero Manu umefanya mauaji ya kikatili kwa Bob Chinanga, sasa rafiki yake kipenzi anaitwa "Nanga Boy" ameomba aje kutenganisha shingo yako kwa shoka yeye mwenyewe kulipiza kisasi cha rafiki yake" alisema Inspekta Mark Noble huku anacheka kicheko cha kebehi na dharau. Yule rafiki wa Bob Chinanga alikuwa anatokwa machozi ya uchungu mkali wa hasira. Kachero Manu akakumbuka yule jamaa alionana nae kambi ya mateso Gorongosa, ndio walimtesa yeye na Bob Chinanga.
Komandoo "JS" alikuwa ameinamisha kichwa chini kama kobe anayetunga sheria vile, huku Kachero Manu akiangaza angaza kwenye chumba kama mtu asiyekata tamaa akisaka fursa yoyote ya kujiokoa, akili yake ilikuwa inampa asilimia 98% kuwa ataokoka na asilimia 2% ndio ilikuwa inampa hofu ya kupata madhara.
"Ndugu wajumbe Kabla hatujaanza mkutano wetu hawa wawili wauwawe kikatili kwa shoka huku Mark nikikupa jukumu la kumtafuta hawara yako Dr.Anabella na kumpoteza haraka sana baada ya kikao hiki kama hatopatikana kwa haraka, jiandae kufa wewe kwa niaba yake kwa kosa la kutupandikizia kirusi kwenye kundi letu...! " alitoa amri Bwana Alfredo kwa sauti yenye hasira na hamaki kali akionyeshwa kuchukizwa na Mark.
"Sawa Bosi wangu nitatekeleza kwa uaminifu mkubwa" alijibu Inspekta Mark huku anatetemeka sura yake imemsawijika vilivyo, akijuta kumfahamu Dr.Anabella.
"Salini sala zenu za mwisho kabla Nanga Boy hajavunja shingo zenu" alisema Inspekta Jenerali Mark huku akimuangalia Nanga Boy ambaye alikuwa akisogelea kwenye kiti alichofungwa Kachero Manu. Alipofika karibu yake kabisa akanyanyua shoka juu kusubiri amri ya kukata shingo ya Kachero Manu. Ukumbi mzima ukapewa amri ya kusimama, kisha Mark akasogea karibu ya Nanga Boy, akaanza kuhesabu ili akifika tatu Nanga Boy ashushe shoka shingoni.
"Moja, mbili, taa....." kabla hajamalizia kuhesabu tatu, ghafla mlango wa nyuma ya kiti cha Bwana Alfredo ukavunjwa kwa kishindo kikubwa, huku Kachero Manu akitumia nguvu zake zote kujitupa pembeni. Shoka lile lililotupwa na "Nanga-Boy" likatua kwenye kingo ya kiti na kukata mikanda iliyomfunga Kachero Manu.
Ambapo bila kuzubaa Kachero Manu akaanza kujifungua mikanda iliyobakia. Risasi ya kutoka kwa Dr.Anabella ilitua sawia kwenye bega la mchumba wake Mark na kusababisha bastola yake kumponyoka. Kachero Manu akawa kashajifungua tayari. Kutupa macho pembeni akamuona Inspekta Jenerali Mark anajivuta kwa kutambaa kuifuatilia bastola yake iliyomponyoka huku damu zinamchuruzika.
Kachero Manu hakumkawiza akamchapa teke la begani mahali pale pale alipopigwa risasi na Dr.Anabella kama kulitonesha jeraha tena, akawa anagugumia kwa maumivu makali. Kisha akaiwahi yeye ile bastola sasa ikawa mikononi mwake. Akawa anamkinga nayo Dr.Anabella asishambuliwe ambaye alikuwa anamalizia kumfungua mikanda Komandoo "JS". Tayari, Nanga Boy alikuwa anakimbilia upande wa Bwana Alfredo kwenda kuwalinda baadhi ya viongozi.
Kabla Nanga Boy hajaifikia meza kuu ya viongozi, Bwana Alfredo akamrushia bastola, ghafla wakashtukia Dr.Anabella anagugumia kwa kali sauti ya maumivu, "Maaaamaaaaah naaa..kuf............ aaaaaaaah....!" alikuwa amepigwa risasi ya tumboni na Bwana Alfredo, akakaa chini kwa kupweteka.
Komandoo "JS" akawa anatambaa chini kwa chini akiwa anamvizia Bwana Alfredo huku Kachero Manu akiwa tayari ameshawachakaza kwa risasi Mafioso kama 6 kitendo ambacho kilimgutusha Bwana Alfredo na kujiona yumo hatarini. Huku mkono wake wa kulia akiwa amebeba faili rangi nyeusi, na mkono wa kushoto ana bastola yake na shingoni amening'iniza "USB-flash" akawa anamwaga risasi ovyo huku anaelekea upande wa kulia wa jengo.
Alipofika kwenye makutano ya kuta mbili, akarusha risasi iliyompata Inspekta Jenerali Mark kwenye usawa wa moyo wa Mark. "Aaaaaaaah.......My Boss you are killing me Whyyyyyy.....!" alilalama Inspekta Jenerali Mark kwa uchungu mkubwa wa maumivu. Risasi ambayo ilipoteza kabisa uhai wa Mark, asingeweza kupona hata kama apelekwe kwenye hospitali bora kama ile ya Apollo iliyopo nchini India.
Bwana Alfredo alikuwa anathibitisha ukomavu wake kwenye ujasusi hakutaka Mark akamatwe kirahisi aweze kuropoka siri zake. Kisha akatoa kitu kidogo mfukoni mfano wa rimoti ghafla kuta mbili zikatengana akatokemea na kuta mbili zikajifunga. Ilikuwa ni kama kiini macho kinafanyika mbele yao kitu ambacho hawakukitegemea. Ilikuwa ni jambo la sekunde kadhaa tu.
"Anatooo...ro...ookaaa...muwa...aaaa.... hini kw... eny....e... maaaeg...esh... o... ya maag...ariii...!" alitoa maelezo Dr.Anabella kwa sauti ya shida ya maumivu. Komandoo "JS" akampa ishara Kachero Manu kuwa anamfuatilia Bwana Alfredo yeye apambane na Nanga Boy.
Nanga Boy akajikuta bastola yake imeishiwa na risasi, Kachero Manu akatupa chini bastola yake akampa ishara wapambane kwa mikono. Ikawa wameshasogeleana kama mahasimu wawili wa kwenye masumbwi ni fursa adhimu ambayo Kachero Manu alikuwa anaitamani ya kulipiza kisasi cha mateso ya kifo aliyopewa kambini na mbwa hawa "Bob Chinanga" na "Nanga Boy".
Alikuwa ni Nanga Boy kuwa wa kwanza kutupa konde la mkono wa kushoto likatua sawia kwa Kachero Manu usawa wa shingo yake. Ilikuwa ni katika harakati za kujaribu kukwepesha konde hilo lisitue kwenye taya zake likaharibu mpangilio mzuri wa meno yake. Nanga Boy akarusha kombora la teke kali la usawa wa mbavuni, bahati nzuri Kachero Manu akakaza misuli ya tumboni. Teke hilo lilimyumbisha Kachero Manu akafanikiwa kujizuia asianguke chini. Akajibu mapigo kwa kurusha teke la sehemu za siri za "Nanga Boy". Nae akawa mwepesi akawahi kulipangua kwa mikono yake, vinginevyo angekuwa mgumba maisha yake yote yaliyobakia.
Kachero Manu hakuwa na muda wa kupoteza na huyu "Nanga Boy" hasa ukichukulia mlengwa wao, Bwana Alfredo hawajamkamata bado, kashawatimulia vumbi. Hivyo akaanza kuruka ruka huku amekunja ngumi mithili ya BRUCE-LEE huku anarudi nyuma nyuma, Nanga Boy akapotea maboya akadhani kurudi nyuma nyuma Kachero Manu anamuogopa akawa anakuja mzobe mzobe ili ambebe Kachero Manu na ampigize chini.
Alivyombeba tu Kachero Manu akampiga na vifuti vya mikono juu ya utosi wa Nanga Boy, damu zikaanza kumchuruzika kama bomba, akamtupa chini. "Nanga Boy" akawa amelewa kutokana na kupoteza kwa damu nyingi kwa wakati mmoja ikawa kila anavyokuja, Kachero Manu anamkwepa, anakwenda kujigonga kwenye viti vya kwenye chumba cha mkutano. Mara ya mwisho baada ya kuona anachezewa hangaisha bwege na Kachero Manu, akaliokota shoka lake akawa anakuja nalo kwa kasi ampige nalo Kachero Manu huku anapiga kelele za kupandisha mori kama morani wa Kimasai aliyepewa ahadi ya kupewa mke kama akiua Simba.
Kachero Manu akasimama wima huku akiwa ameipanua kidogo miguu yake kupata uimara wa mwili. Alivyofika kushusha shoka lake, Kachero Manu akaudaka mkono wake na kuuzungusha kidogo tu, Nanga Boy alipiga yowe la nguvu. Mfupa wake wa maungio ya bega ulikuwa umechomoka begani, kirungu cha maungio ya mfupa begani kinaning'inia nje ya bega.
Hakumkawiza akamchota mtama akaangukia kisogoni chini ya sakafu, akawa anatupa tupa miguu ya kushoto na kulia alikuwa anakata roho.
Kachero Manu akapata nafasi ya kukimbilia kwa Dr.Anabella ambaye alikuwa yupo kimya kama amefariki vile. Alikuwa amezimia kutokana na kupoteza damu nyingi sana. Alichofanya ni kushika maeneo ya kifuani, akabinya kwa nguvu kwa kutumia vidole vyake akawa anasikia mapigo ya moyo kwa mbali. Akaenda kwenye simu ya mezani kwenye kila chumba cha mkutano na kupiga simu ya dharura ili gari la kubeba wagonjwa mahututi lifike kuwapeleka majeruhi hospitalini. Pia akapiga simu idara ya usalama Ikulu moja kwa moja waje haraka sana kuwakamata watuhumiwa, kisha akakata simu na kukimbilia nje kusaidiana na Komandoo JS.