Riwaya: Barua Kutoka Jela

Riwaya: Barua Kutoka Jela

RIWAYA: BARUA KUTOKA JELA
MTUNZI: IBRAHIM GAMA


SEHEMU YA TANO

Ama kwa hakika askari wale walichanganyikiwa sana kwani kila kitu walichokitarajia kuwasaidia kumtambua huyo afande Jamila waliambulia jibu la hapana! Ama kweli walikuwa wamepigwa bao la kisigino. Mwisho wa yote wakaacha namba zao za simu na kumwambia Neema.

"kama atakuja tena huyo afande Jamila muulize anatokea kituo gani, na unipigie simu mara moja. kwani mimi ndiye mpelelezi katika kesi hii. Hivyo mtu yeyote atakayejihusisha na kesi hii, lazima mimi nimtambue."

Mwisho wakaaga na kuondoka.


*******

Afande Kubuta alibisha hodi Ofisini kwa Bosi wake na kutoa heshima za kijeshi kama inavyotakiwa na kuketi kitini baada ya IGP kumuashiria kufanya hivyo.

IGP akanyoosha mkono kuchukua vitu alivyoagiza kutoka kwa afande Kubuta na kitu cha kwanza kuanza kuangalia zilikuwa ni zile albam nne zilizokuwa mbele yake.

Aliangalia moja baada ya nyingine huku akiangalia hadi zile picha zilizokuwa zimewekwa nyuma ya picha, mwisho akazimaliza zote albam nne bila kuona kitu alichokikusudia!

Akainua uso na kumtazama usoni kijana wake afande Kubuta. Na kwa mara ya kwanza akanyanyua mdomo wake kusema.

"Kuna picha humu ambazo zimetolewa! Kwani zipo sehemu zilizokuwa tupu kuonyesha kwamba kulikuwa na picha! Kwani si kama picha zilizomo humu hazitoshi kuijaza albam kwani kuna picha nyingi hadi nyingine zimewekwa picha tatu katika sehemu moja! Je picha hizo umezitoa wewe? Na kwa sababu gani wakati nilikwambia ulete kama utakavyozichukua?"

Akauliza IGP huku akiwa amechukia na amefula kwa hasira!

"Hapana Mkuu, kama ulivyoagiza ndivyo nilivyotekeleza. Ila picha zilizopungua, nimeambiwa kwamba amekwenda afande Jamila amezichukua na kuahidi angezirudisha baada ya upelelezi kukamilika!"

Sasa ikawa zamu ya IGP kufadhaika, aliinuka kwenye kiti chake na kusimama huku akiwa ametoa macho pima! Kitu ambacho hata afande Kubuta naye alishangaa. Kwani alidhani labda huyo afande Jamila, alitumwa na Bosi huyo kama yeye alivyotumwa kwenda kuchukua zile albam. Sasa kama naye anashangaa je kuna nini kinachoendelea. Na je hizo picha ni za nini? Hatimaye IGP akauliza.

"Huyo afande Jamila nani kampa kesi hii?!" Sasa IGP alionekana kama ana hofu katika sura yake lakini pia jazba ilimtawala vile vile.

Afande Kubuta akaisoma hali ya Bosi wake akawa makini sana.
"Sielewi mkuu, lakini pia katika kituo chetu cha Magomeni hatuna jina la afande Jamila, achilia mbali kuwa mpelelezi. Pia nilidhani labda amri hii imetoka juu, katika kuweka askari mwingine bila mimi kujua! Ili naye afatilie mwenendo mzima wa kesi hii. Sasa kama mkuu hujui lolote kuhusu afande Jamila, nini kinaendelea katika kesi hii?"

Afande Kubuta aliuliza huku akiwa amechanganyikiwa kwa mawazo. Pia baada ya maelezo yake "IGP" akagundua mchezo wote atakuwa anaufahamu huyo afande Jamila, lakini yeye kwa nini asifahamishwe alipohitaji kujua mpelelezi anayeendesha kesi ya marehemu Hamida?!

Ila yeye alipewa jina la afande Kubuta, nambari ya faili na nambari ya simu ya afande Kubuta. Sasa huyo afande Jamila anafanya kazi kwa kutumwa na nani na kwa faida ipi hatimaye "IGP" aliwaza na kuinua mkono wa simu kisha kubonyeza nambari kadhaa na simu ikawa inaita upande wa pili.


*******

Madereva Taxi katika Kituo cha Taxi Magomeni Usalama, walikuwa katika harakati za kazi yao. Wapo waliokuwa wakifuta magari, wengine kuyaosha kabisa. Pia wapo waliokaa juu ya Boneti na wapo waliokaa juu ya Buti. Wapo waliokuwa ndani ya magari yao wakisinzia ili mradi kila mtu alikuwa na harakati zake.

"Karibu dada, hii hapa pamba nyepesi full kiyoyozi na bei sina, ngoma full tank siyo mafuta ya kidebe."

Dereva wa taxi alijinasibu kwa kuipamba gari yake, na kumshawishi Yule abiria ili apande kwenye gari yake. Huku akifungua mlango wa nyuma wa gari yake, ili abiria aweze kuingia, kisha watapatania ndani bei ya sehemu atakayompeleka.

Yule abiria aliekaribishwa bila kujishauri wala kusita, akazama ndani ya gari ile.

Dereva badala ya kuingia ili waanze safari, akaanza kupiga honi mfululizo! Mara kijana mmoja mfupi mweupe alikuja mbio alitokea upande wa kushoto wa gari lile ambalo walikuwa wamekaa vijana wengine kadhaa wakicheza draft.

"Mpeleke huyo Dada sijaongea naye kitu chochote mtaelewana."

Aliongea yule kijana aliyemkaribisha yule abiria.
Alipopanda yule dereva na kuwasha gari, yule abiria akatambua kwamba, yule kijana wa mwanzo alikuwa ni shanta, huyu sasa ndiye Dereva.

"Samahani Dada tunaelekea wapi?" Yule Dereva Taxi aliuliza huku akiondosha gari.

"Nipeleke Kimara Suka, itakuwa shilingi ngapi?"
"Ahaa Kimara Suka kubwa dada yangu, unakwenda pale pale kituoni, au kule shule, au kule Golan au kwa yule Mwandishi maarufu wa riwaya Hussein Tuwa?"

"Nakwenda Kimara Suka Hotel utanichaji shilingi ngapi?"

"Alaa kama pale ni shilingi elfu nane tu Dada yangu!" Alijibu yule dereva wa Taxi huku akigeuza Gari na kuanza safari.

"Wewe una bei sana kwani nilikuwa nikimchukua yule kijana Mwaduga, alikuwa akinipeleka kwa shilingi Elfu sita tu! Sijui leo kapakia, kwani sijamuona yeye wala gari yake!"

Yule abiria alimwambia Yule dereva wake kwa upole.

"Usinikumbushe sister Bwana. Mshikaji wetu jumba bovu limemdondokea! Jamaa ana bahati mbaya sana Yule."

Dereva alimwambia abiria wake kwa masikitiko huku akionyesha huzuni usoni mwake!

"Umesema jamaa kaangukiwa na jumba bovu siatakuwa ameumia sana?!"

"Sio hivyo unavyofikiria, jamaa yetu kapatwa na matatizo. Kapewa msala wa mauaji hivi hivi, majambazi na wauaji wanaachwa wanatembea mitaani tu!"
Alijibu Yule taxi dereva, katika lugha yao ya kijiweni, ambayo ilimpa wakati mgumu, abiria wake kumuelewa kwa urahisi, maana ya baadhi ya maneno!

"Aaaaaa Bwana usiniambie!"
Yule abiria aliuliza swali kwa mfadhaiko, na fadhaa kubwa.

"Kweli sister wangu, jamaa ana miezi miwili na kitu, sasa yupo katika maisha mabovu mahabusu. Yaani kama alikupakia basi ni siku nyingi kidogo. Sasa bei zimebadilika mafuta yamepanda bei sana."

Alijibu yule dereva Taxi nakutoa ufafanuzi huku akibadilisha gia, sasa wakiwa maeneo ya Aljentina Manzese.

"Kwani kilimpata nini jamani kaka wa watu duh kama namuona vile!?"

Yule abiria aliuliza kwa masikitiko, na kuonyesha sura ya huruma na kuendelea kueleza.

"Mimi nilikuwa Chuoni nimekuja pale kituoni kwenu kama miezi mitatu iliyopita, na Mwaduga ndiye alikuwa ananizungusha katika mizunguko yangu!"

"Yaani sister we acha tu, kwani kesi ya mshikaji imekaa vibaya sana!"

Dereva Taxi akaongeza msisitizo wa jambo lile.

"Umesema kesi ya Mwaduga imekaa vibaya sana, kwa sababu gani, wakati umesema ni jumba bovu tu limemwangukia, yaani yeye hakufanya jambo lile?"

"Dada, yule mshikaji keshapotea yule kwani amepewa soo nne. Mauaji, kukutwa na silaha, kula njama ya kutenda kosa na wizi wa kutumia silaha. Haya yote anaweza kuchomoa, lakini kosa lakukutwa na silaha, jamaa si washamuachia msala?! Huwezi kuamini sister lakini nakuambia yule Demu alieuliwa ni mali ya wakubwa, kwani Bosi wa polisi wa cheo cha juu kabisa, ndiyo alikuwa anaburuza ule mzigo"

"Ha ha haa, sasa kaka unafika mbali sana, yaani wewe unajua pia kuwa huyo marehemu, anaeshitakiwa Mwaduga kuwa alimuua, kuwa ni kimada wa mkubwa wa jeshi la polisi!?"

Yule abiria alionyesha kutaharuki kupita kiasi, lakini pia alijiona ni mwenye bahati kubwa kuichagua gari ile, kwani dereva wake ni mtu mropokaji! Kwani anatoa taarifa nyeti kwa gharama nafuu sana!

"Siyo mzaha sister wangu, mimi nina mshikaji wangu anapaki Town yeye ndiyo ilikuwa kazi yake! Ameisha mpakia sana yule Demu kumpelekea Bosi wa polisi, karibu mara tatu! Na yule Bosi alikuwa anamlipa pesa nzuri sana! Yaani jamaa anaweza kumchukua yule Demu Mikocheni nyumbani kwake, na kumpeleka labda bwalo la polisi ostabey akalipwa shilingi elfu ishirini! Au siku nyingine humpeleka Bagamoyo na kumuacha kwenye hoteli za kitalii siku za mwisho wa wiki, akalipwa laki moja! Sasa aliposikia mshikaji wetu Mwaduga yuko ndani tena kwa kesi ya mauaji ya yule Demu, mshikaji aliniambia haya ninayokwambia, na akasema Bel white mshikaji wangu jamaa yenu keshapotea, kwani ile ni mali ya wazee Yaani tumsahau! Sasa wewe sister unadhani hiyo ni kesi ya kitoto hiyo?"

Yule abiria alisogea katikati ya kiti cha dereva na abiria, huku akiwa na simu yake mkononi muda wote tangu amepanda gari ile, akasema kwa shauku kubwa.

"Duh ebwana we! Hiyo kweli ni kasheshe, Yaani ndiyo ilivyokuwa hivyo? Na mbona kule mwanzo ulisema wauaji na majambazi wanaachiwa tu wanatembea na jamaa yenu anaozea jela, kwa nini msiisaidie polisi kuwakamata na jamaa yenu akaachiwa?"

Yule abiria akazidi kuchimba. Na hadi walipofika Kimara Suka hotel akawa ameshapata hadi jina la yule Dereva Taxi wa mjini na namba yake ya simu, pamoja na namba yake Dereva Taxi huyu aliempeleka Kimara aliemtambua kwa jina la Bel white.

******

Ilikuwa siku ya Ijumaa Dokta Zahala akiwa nyumbani kwake maeneo ya Keko bora, alikuwa anaonekana kuwa ni mtu wa mawazo mengi, kisha kama aliyekumbuka jambo akatoa simu yake kwenye "Hand Begi" na kubonyeza tarakimu kadhaa na simu ya upande wa pili ikatoa maelezo badala ya kuita!

"IMU UNAYOPIGA IMEZIMWA AU IPO NJE YA ENEO, TAFADHALI JARIBU TENA BAADAE."

Dokta Zahala akakata na kubonyeza namba zingine na simu ya upande wa pili ikaanza kuita.

"Shoga vipi mbona kimya au ndiyo nimekupa kazi kubwa kiasi hata simu yako ya kawaida umeizima?"

Aliongea Dokta Zahala mara tu simu ya upande wa pili ilipopokelewa, na kuongeza kuwa.

"Duh pole sana, sasa leo nipo mapumziko, kama unayo nafasi njoo nyumbani nitakuwepo. Kwani nina neno lililonifanya nikupigie simu!"

Aliongeza Dokta Zahala na kisha akakata simu.

Dakika Arubaini baadae kengele ya geti la mlango iliita, na mfanyakazi wa Dokta Zahala akakimbilia kwenda kufungua mlango. Dokta Zahala akamkaribisha shoga yake, na wakakumbatiana kama kawaida yao wanapokutana!

Dokta Zahala na Inspekta Jamila walikuwa marafiki tokea chuoni pale Mlimani, walipomaliza masomo, Jamila akaenda kujiunga na Jeshi la Polisi na kutokana na Elimu yake haikumchukua muda mrefu kupata nafasi aliyonayo, baada ya kuongezeka utendaji kazi wake katika Jeshi la Polisi.

Na Dokta Zahala alikuwa anachukua masomo ya udakitari, Baada ya mama yake mdogo aliekuwa nesi katika hospitali ya Kcmc Moshi, kumshawishi asomee mambo ya utabibu akimwambia unalipa sana, na kweli leo hii yupo katika nyumba yake mwenyewe pale Keko Bora!

"Leo soda yako ya lemon unayoipenda sina kwenye jokofu langu, je ukatafutiwe huko nje madukani au utakunywa hizi zilizopo?"

Dokta Zahala alimwambia shoga yake huku akiangua kicheko.

"Akili yangu ilivyovurugwa, sina chaguo lolote lililo bora, wewe nipe kinywaji chochote mimi nitakunywa, ilimradi kisiwe na kilevi!"

Alijibu Inspekta Jamila na akamalizia kwa kicheko. Baada ya wote kupata vinywaji cha juice, hatimae Dokta Zahala akavunja ukimya.

"Haya shoga yangu ukamwona yule Dada siku ile na mwanae sijui umefikia wapi, kwani alinitia huruma sana yule Dada."

Inspekta Jamila akamuhadithia shoga yake kila kitu bila ya kumficha chochote huku akimwambia kuwa, ameamua kumueleza yote kwa ukamilifu! kwani kazi na maisha yake yapo hatiani toka yeye kujihusisha na kesi ile bila maelekezo kutoka kwa wakubwa zake, na ikija kubainika kwamba anajua hadi uhusiano uliokuwepo wa "IGP" na Marehemu Hamida, basi atakuwa katika mashaka mazito!

"Lakini pia nataka wewe shoga yangu uwe unalifahamu kwa undani jambo hili, ili ikitokea lolote kuhusu maisha yangu uwe na pakuanzia!"

Alisema kwa masikitiko Inspekta Jamila.
"Duh pole na hongera shoga!" Alisema Dokta Zahala.

"Sasa mimi nilikutafuta ili nijue kama ulimsaidia yule Dada, lakini pia kuna kitu kipya nataka kukueleza!"

Alisema Dokta Zahala na kuinua glasi ya Juice nakupiga funda moja, huku akimuangalia shoga yake alivyokaa kwa umakini mkubwa.


Jagarld Jullie Z Sangomwile Khantwe Mr Rocky Gunda66 Himidini VAN HEIST BPM ABUBAKAR SHEKAU NYIRO mamsapkhan born again pagan princetx
 
RIWAYA: BARUA KUTOKA JELA
MTUNZI: Ibrahim Gama
SEHEMU YA SITA
Inspekta Jamila akamuhadithia shoga yake kila kitu bila ya kumficha chochote huku akimwambia kuwa, ameamua kumueleza yote kwa ukamilifu! kwani kazi na maisha yake yapo hatiani toka yeye kujihusisha na kesi ile bila maelekezo kutoka kwa wakubwa zake, na ikija kubainika kwamba anajua hadi uhusiano uliokuwepo wa "IGP" na Marehemu Hamida, basi atakuwa katika mashaka mazito!
"Lakini pia nataka wewe shoga yangu uwe unalifahamu kwa undani jambo hili, ili ikitokea lolote kuhusu maisha yangu uwe na pakuanzia!"
Alisema kwa masikitiko Inspekta Jamila.
"Duh pole na hongera shoga!" Alisema Dokta Zahala.
"Sasa mimi nilikutafuta ili nijue kama ulimsaidia yule Dada, lakini pia kuna kitu kipya nataka kukueleza!"
Alisema Dokta Zahala na kuinua glasi ya Juice nakupiga funda moja, huku akimuangalia shoga yake alivyokaa kwa umakini mkubwa.
"Dokta yale uliyonipa yananinyima Raha hadi sasa, Leo unataka kunipa mzigo mwingine?!" Alilalamika Inspekta Jamila.
"Hili ni jambo nyeti sana ndio maana nikaona nikwambie wewe shoga yangu, lakini pia kama Raia Mwema nina haki kwa nchi yangu kuisaidia kwa kutoa mchango wangu!"
Alikazia Dokta Zahala.
"Mmmh" alishusha pumzi ndefu Inspekta Jamila na kukohoa kidogo kisha akasema.
"Haya Raia Mwema lete taarifa!"
Dokta Zahala akaangua kicheko, kisha akaanza kwa kusema.
"Jana imeletwa maiti pale kazini ikielezwa ni ya Ajali, kiasi kila mtu anaamini hivyo! Ila baada ya saa kadhaa nilipokwenda kuifanyia uchunguzi, maiti ile ilinishangaza! Kwani "Rigor Mortis", Yaani zile athali za kifo kwa maiti zilijitokeza mapema sana, ukizingatia maiti ile haikutokwa na damu nyingi,wala haikuwa na majeraha makubwa!"
"Basi nikiwa ni Daktari, jambo lile lilinifanya nifanye uchunguzi wa kina. Nakweli niligundua mtu yule hakufa kutokana na ajali, bali alikufa kabla ya ajali!"
Dokta Zahala alipeleka funda lingine la juice kinywani mwake, kisha akaendelea.
"kwani vipimo vimenijulisha kwamba, mwili ule ulitokwa na uhai mapema sana asubuhi, na amekunywa au amenyweshwa sumu! kwani mabaki ya sumu ile imeonekana katika mwili wake! Sasa swali linakuja. Askari wa Doria wakati wanaelekea sehemu ya Bagamoyo kiasi cha saa moja nyuma hawakukuta ajali ile, wakati wanarudi ndiyo wakaiona gari iliyopata ajali. Marehemu alikutwa amebanwa kwenye usukani wa ile gari akiwa ameshafariki. Mnamo saa tano za asubuhi. Je aliendeshaje gari ikiwa mtu amekufa asubuhi mishale ya saa moja, kisha saa tano ndiyo apate ajali tena akiwa anaendesha gari?!"
Dokta Zahala alisimama kidogo kisha akaendelea.
"Ndipo nikaona nikwambie wewe, kwani askari walioandika maelezo hayo ninayokwabia, wanaamini yule Bwana waliemtambua kwa jina la Kiyarwenda Mwemezi Mkazi wa Mikocheni B, kutokana na kitambulisho cha kupigia kura alichokutwa nacho katika eneo la tukio, amefariki kwa ajali ya gari."
Inspekta Jamila alitoa macho pima baada ya kusikia habari ile hasa jina la marehemu Kiyarwenda Mwemezi. Kwani ni yule jirani yake Hamida kule Mikocheni, aliyekuwa akimuhoji kuhusu kifo cha marehemu Hamida. Hata naye aliposikia ajali ile, alikuwa anahisi kuna kitu kilichojificha katika ajali ile kumbe alikuwa sahihi na mawazo yake!
"Sawa Dokta, sasa ugumu wa swala hilo nikumpata au kuwapata watu waliofanya hivyo, Yaani waliohusika katika mauaji yale. Na kwa nini walifanya mauaji yale. Kwani nahisi bado yapo katika mlolongo wa kesi hii niliyojipachika, na sasa naona mambo mengi sana kiasi yanazidi kuniweka katika wakati mgumu. Kwani kama kuuwawa kwake jirani yule kunatokana na kujua mambo mengi ya marehemu Hamida na mumewe, au imeshabainika kama niliongea nae, sasa wahusika wa kadhia hii wanajaribu kuharibu ushahidi!"
Inspekta Jamila, alisema maneno hayo huku, akionekana kuwa ni mwenye chembechembe za woga, hasa akizingatia kuwa kesi ile, yeye hakukabidhiwa jalada lake.
Watu gani hao wanaofatilia nyendo zake katika muda mfupi namna ile.
Akaiweka wazi hisia yake kwa Dokta Zahala wote wakaingia katika lindi la mawazo mazito!
"Kitu cha hatari nilichokifanya shoga ni kwamba, nilichukua vipimo vile kitaalam zaidi, kwani niliweka kile kifaa maalum cha kisasa kilicholetwa hivi karibuni kutoka China, ambacho kina uwezo wa kung'amua tukio la mwisho kabla mtu hajafa aliloliona!"
Dokta Zahala huku akimkazia macho Inspekta Jamila, alichukua gilasi iliyokuwa na juisi akainywa yote, kisha akaendelea kusema.
"Ukitaka kupata picha ya aliyoyaona mtu kabla hajafa, itakubidi ufumbue macho ya marehemu, kisha uweke kifaa kile kama miwani ,na kifaaa kile kita scan picha ya mtu au kitu cha mwisho macho yale kuona! Hivyo nimefanikiwa kupata picha za watu wawili ambao marehemu kabla ya kukata roho, alikuwa anatazamana nao ana kwa ana!"
Dokta Zahala akakandamiza jambo lingine lililomfanya Inspekta Jamila kuinuka katika kiti alichokalia na kwenda kumkumbatia shoga yake yule huku akitamka maneno mfululizo.
"mungu wangu, mungu wangu!"
Sasa wakiwa bado wamekumbatiana, Dokta Zahala akaendelea kusema ile azma yake iliyomfanya amwite shoga yake nyumbani kwake muda ule.
"Hivyo lililonifanya nikuite wewe, ni pamoja na kukupa habari hii kwa kina, na nikukabidhi picha zenyewe, ili uanze kazi yako!"
"Sio nianze kazi yangu, niendeleze kazi yangu, kwani kazi nilishaianza tokea Jumapili, alipofika ofisini kwangu, yule Dada anayeitwa Eshe Muhidini, ambaye wewe ndiyo uliemuelekeza aje kwangu."
Alijibu Inspekta Jamila na kuendelea.
"Sasa huyo maiti uliyemfanyia uchunguzi ndiyo yule jirani yake Hamida aliyenipa Mwanga katika upelelezi wangu, kwani ukimtoa yule mahabusu Mwaduga, mtu wa kwanza kumuhoji alikuwa ni Ndugu Kiyarwenda Mwemezi ambaye sasa ni marehemu! Yeye ndiyo aliyenifungua ya kwamba, kabla sijapeleleza kifo cha Hamida, napaswa kwanza kufahamu kifo au kilichopelekea kifo cha mume wake Hamida, Bwana Bartazal Halimu!"
Alisema kwa msisitizo Inspekta Jamila huku akiwa amesimama wima na akiachiana na shoga yake kutoka katika kukumbatiana.
Dokta Zahala akainuka nakuenda chumbani kwake, alipotoka alikuwa ameshika bahasha mkononi ikiwa imefungwa, na juu ya bahasha ile kuliandikwa maneno Dear Jamila! Akamkabidhi Inspekta Jamila bahasha ile na kumwambia.
"Mambo yote yapo humo ndani ya bahasha hii!"
Inspekta Jamila akaipokea ile bahasha na saa hiyo hiyo akaaga na kuondoka!
*******
Ilikuwa ni saa kumi na mbili za jioni, kikao kilikuwa kinafanyika katika ofisi ya "IGP" kilichokuwa na watu wasiozidi sita.
"IGP" mwenyewe na mlinzi wake, Afande Kubuta, Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai nchini, Kamanda wa Kanda Maalum na Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, watu wote hawa wakiwa wametoa kofia zao katika vichwa vyao, kasoro "IGP" walikuwa katika mjadala mzito wa namna matukio ya uhalifu Mkoa wa kipolisi wa Kinondoni yanavyoendelea, pia kushughulikiwa kwa kesi ya marehemu Hamida Baltazal.
Baada ya "IGP" mwenyewe kutaka faili la kesi hiyo ili kutazama mwenendo mzima wa kesi hiyo, na baada ya kusoma kwa makini taarifa zilizoandikwa katika faili lile ndipo alipoitisha kikao hicho cha dharula.
"Sasa nimewaita hapa, baada yakuona maelezo yaliyopo katika faili hili hayatoshelezi, na hayaridhishi katika kuiendesha kesi hii, lakini pia kuna jambo lisilo la kawaida limejitokeza!"
"IGP" alisema maneno hayo huku akiwaangalia maafande wale walivyokuwa makini na utulivu wa hali ya juu, wakienda sanjari na ukakamavu!
"Kesi hii amepewa kijana hapo!"
Alisema "IGP", huku akimnyooshea mkono ulioshika faili Afande Kubuta, kisha akaendelea.
"Kuna mtu amejiingiza katikati, nae akifanya upelelezi wa kesi hii! Ambapo ni kinyume na utaratibu wa Jeshi la Polisi. Kwani askari asipotambulika na Mkuu wake kama anafanya nini kwa wakati gani kuna "Risk" nyingi sana zinazoweza kupatikana, kama vile Rushwa, askari kuuwawa au kuumia wakati akiwa hayupo kazini kisheria. Pia anaweza kuharibu upelelezi wa kesi, hivyo ni lazima atafutwe mara moja na aletwe kwangu ili anipe maelezo yatakayoniridhisha. Vinginevyo atapoteza kazi yake, ikiwa kweli ni askari halali wa jeshi la polisi, na atakaa selo."
"IGP" alisema maneno hayo huku akiwa amefura kwa hasira. Mwisho wa yote "IGP" akaagiza kesho saa mbili asubuhi wahakikishe huyo afande Jamila anakuwa ofisini kwake!
Baada ya kikao kile, maafande wale wakaanza kazi ya kumtafuta afande Jamila, baada ya afande Kubuta kumpigia simu ndugu wa marehemu Hamida na kutaka kufahamishwa umbile la huyo Jamila, na baada ya kama dakika 40 tu hivi mara moja wakawa wanachambuliwa maaskari wenye majina ya Jamila walioko katika Mkoa wa Kinondoni, na wakakosa mwenye sifa au wasifu unaomfanana huyo afande Jamila, alieelezwa na Neema, ndugu wa marehemu Hamida ambae alimuona!
Mara moja Kamanda wa Kanda Maalum akawasiliana na Makamanda wa Mikoa ya kipolisi ya Ilala na Temeke, ili wawasiliane na wakuu wa vituo katika sehemu zao za kazi, ili atambuliwe huyo Afande Jamila, ambaye wasifu wake umeelezwa kuwa ni mweusi wa chokoleti, mrefu wa wastani, mwenye umbo namba nane, ana hipsi kubwa na makalio yaliotokeza, miguu minene, meno meupe sana na lipsi nene katika midomo yake, na macho manene yanayoonekana muda wote kama yamerembuliwa mithili ya mwanamke aliyekula kungu manga! Na anapotabasamu hubonyea mashavuni!
Lakini pia majibu yaliyotoka kutoka Temeke na Ilala ni kama yale ya Kinondoni.
Hakuna afande mwenye jina la Jamila mwenye sifa hizo!
Sasa maafande wale walichanganyikiwa vibaya sana, kiasi wakahisi labda kuna mtu aliyejifanya ni askari akaenda kwa marehemu Hamida ili akaharibu ushahidi wowote uliopo!
"Sasa hii nini", alijikuta akisema Kamanda wa Kanda Maalum!
"Kuna sehemu moja bado hatujaiangali."
Alisema Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai Nchini, na wale askari wengine wakawa wamemtumbulia macho.
Yeye akaendelea. "Ni hapa Makao Makuu kwenyewe!"
Wote wakatamka, "Yes" na kazi ikaanza tena na mara moja Inspekta Jamila akapatikana kuwa ndiye mwenye sifa zilizotajwa.
Kamanda wa Kanda Maalum akawa anasoma namba ya simu ya Inspekta Jamila kutoka katika orodha ya majina iliyobandikwa ukutani pale makao makuu, Cheo chake na nambari yake ya kazi, alipoziweka kichwani akaenda hewani moja kwa moja akiwasiliana na Inspekta Jamila.
"Kamanda wa polisi Kanda Maalum ya D'Salaam, popote ulipo kesho unahitajika ofisini kwangu saa moja na nusu asubuhi bila kukosa! Kumbuka hii ni amri, hivyo ufanye hivyo haraka iwezekanavyo".
Baada ya kusema hayo kamanda wa kanda maalum akakata simu bila ya kutaka kusikiliza upande wa pili utajibu nini.
Bila shaka Inspekta Jamila alikuwa katika wakati mgumu sana. Hivyo akajikaza na kuahidi kwenda kusikiliza wito wa mkuu wake ili akajue mbichi na mbivu!
********
***KAZI ndo kwanza inaanza na mfanyakazi mwenyewe ni INSPEKTA JAMILA……nni kitaendelea…
Jagarld Jullie Z Sangomwile Khantwe Mr Rocky Gunda66 Himidini VAN HEIST BPM ABUBAKAR SHEKAU NYIRO mamsapkhan born again pagan princetx
 
Last edited by a moderator:
Duh,Jamila wangu wanampeleka wapi hawa mbona wanataka kuniharibia,acha tusubiri tuone watamwambia nini,ahsante sana mkuu Casuist
 
Last edited by a moderator:
Safi sana utamu koleaa.....na Mimi usisahau kuniita sehemu ya Saba Casuist
 
Last edited by a moderator:
Mkuu Skype uwe unatembelea na huku kusoma hadithi za watanzania wenzetu....
 
Last edited by a moderator:
SEHEMU YA SABA


"Kamanda wa polisi Kanda Maalum ya D'Salaam, popote ulipo kesho unahitajika ofisini kwangu saa moja na nusu asubuhi bila kukosa! Kumbuka hii ni amri, hivyo ufanye hivyo haraka iwezekanavyo".

Baada ya kusema hayo kamanda wa kanda maalum akakata simu bila ya kutaka kusikiliza upande wa pili utajibu nini.

Bila shaka Inspekta Jamila alikuwa katika wakati mgumu sana. Hivyo akajikaza na kuahidi kwenda kusikiliza wito wa mkuu wake ili akajue mbichi na mbivu!

********

Saa moja na nusu juu ya alama, Inspekta Jamila alikuwa amekaa katika kochi akitazamana na Kamanda wa Kanda Maalum, huku akiwa katika ukakamavu mkubwa.

"Binti nimekuita hapa kwa mahojiano na wewe". Alinza kwa kusema Kamanda wa Kanda Maalum, kisha akaendelea.

"Hivyo nataka kujua nani aliyekupa idhini yakufatilia kesi ya Marehemu Hamida inayomkabili yule Dereva wa Taxi Mwaduga Dingo?! Kwa nini umefanya upelelezi katika kesi mbayo uongozi wako umempa mtu aliyeonekana anafaa kufanya kazi hiyo! Na pia nataka kufahamu ulipofikia katika huo upelelezi wako!"

Kamanda Kanda Maalum alihoji maswali hayo huku akiwa amechukia vibaya sana. Kabla Inspekta Jamila hajajibu chochote akiwa bado anasubiri mkuu wake amalize ili yeye aanze kujitetea, simu ikawa inaita ya Kamanda wa Kanda Maalum.

"Nakusoma mkuu", akaitikia Kamanda wa Kanda Maalum. "Ndiyo afande, sawa afande" Kamanda wa kanda maalum alikuwa anapokea maagizo kutoka kwa mkuu wake "IGP".

Baada ya kumaliza kuongea na simu,Kamanda wa kanda maalum alimuangalia Inspekta Jamila na kumwambia.

"Okey sasa maelezo yako utakwenda kuyatoa mbele ya "IGP", Ofisini kwake sasa hivi. Inuka twende ofisini kwake."
wote wakainuka wakaelekea katika ofisi za "IGP", zilizopo palepale katika jengo la Wizara ya Mambo ya ndani.

Kamanda wa Kanda Maalum aliingia ofisini kwa "IGP" akiwa na Inspekta Jamila.
Baada ya kumtolea heshima ya kijeshi, "IGP" aliwaelekeza kukaa vitini. Walipokwisha kuketi, Kamanda wa Kanda Maalum akaanza kwa kusema;

"Afande yule kijana ni huyu nilimwita ofisini kwangu asubuhi hii ili anipe maelezo ya kina kabla hujakutana naye, ili niweze kuyachekecha, lakini kwa ulivyoniamrisha uonane naye sasa hivi ndio nimemleta, huyu ndiye Inspekta Jamila".

"Sawa Afande kazi nzuri, sasa niachie nimuhoji mimi mwenyewe, wewe kaendelee na kazi yako".

Kamanda wa kanda maalum aliinuka na kupiga Saluti, kisha akatoka nje ya ofisi ile na kuelekea ofisini kwake.

Tofauti na Kamanda wa Kanda Maalum alivyokuwa mbogo kwa Inspekta Jamila, "IGP" alikuwa anaongea katika hali ya utulivu kama anayeongea na wakuu wenzake!

Hali ile ilimshangaza sana Inspekta Jamila kwani alitarajia kukutana na ukali, ukifatiwa na Amri nyingi kama sio kuwekwa lumande!

Basi hali ile ilimfanya awe mpole na mwenye kujiamini. Pia akishukuru kuongea na "IGP" moja kwa moja, ingawa angeweza kuhojiwa na Askari wa chini yake.

Lakini kitendo cha kumuhoji yeye mwenyewe, Inspekta Jamila alielewa ni ile picha ya "IGP" aliyokuwa nayo yeye wakati ule na si kitu kingine!

"Afande nataka kufahamu upelelezi wako umefikia wapi, umegundua vitu gani vyenye maana na bila shaka utanambia au kutaka kujua juu ya picha yangu uliyoichukua kutoka katika albam ya Marehemu Hamida."

"IGP" aliongea kwa utulivu mkubwa huku akitambua anachokifanya!!!

Inspekta Jamila alikuwa ametulia kama kawaida yake, kisha akajibu.

"Afande kwanza sina budi kukushukuru kwa kuweza kunita na kukaa na wewe kama hivi, na tukawa tunazunguza, kwani ni nafasi adhimu sana! Lakini pia nilihitaji kupata nafasi kama hii kwa wakati huu ili nikupe taarifa ambazo yawezekana huna, au unazo juu juu si kwa undani".

Kisha akaanza kumhadithia toka alipopewa jambo lile na mke wa Mwaduga, na namna alivyolishughulikia hadi kufikia muda ule! Alimwambia kila kitu alichokutana nacho katika upelelezi wake, ikiwemo picha yake "IGP". Dereva Taxi aliemkodi kwenda nae Kimara suka, na taarifa za mahusiano ya kimapenzi kati yake na marehemu Hamida, bila kusahau taarifa ya ajali ya jirani wa Marehemu Hamida, Bwana Kiyarwenda Mwemezi kwa kina, pamoja na picha za wahalifu waliohusika katika ajali ya kutengenezwa, iliyogharimu maisha ya Bwana Kiyarwenda Mwemezi!

"IGP" alikuwa anamsikiliza Inspekta Jamila kwa makini na kushangaa ujasiri aliouonyesha kijana wake yule, lakini pia utendaji wake! Na kuona kuwa tayari ameshafahamu uhusiano wake na marehemu Hamida!

Waliweza kuongea kwa muda mrefu, hatimaye "IGP" aliamua kumkabidhi faili la kesi ya marehemu Hamida, na kumwambia.

"Upelelezi wako umejua mambo mengi sana kwa muda mfupi wa wiki moja tu, kiasi aliyekuwa akiiendesha kesi hii toka awali hakufika hata robo ya ulipofika wewe, ingawa yeye ana zaidi ya siku sitini!"

"Hivyo nitaongea na mwanasheria Mkuu ili kuliondosha suala la kijana Mwaduga Dingo Mahakamani ili awe huru, ili aweze kukusaidia kwa upelelezi wako kwa kuwatambua waalifu wale! Kwani akiwa nje atakuwa na imani na jeshi la polisi, pia atakuwa mkweli na muwazi kuliko akiwa mahabusu. Lakini pia kutokana na upelelezi wako, nami pia naungama ya kwamba yule kijana Mwaduga Dingo hana hatia!"

Mkuu wa jeshi la polisi, alikuwa mtulivu sana, akitawaliwa na hekima na busara, akiwa ameiweka mbali sana jazba.

"Hivyo hatuna muda wa kupoteza, picha hizo za sura za watu wawili alizokupa Dokta Zahala, utazipeleka kwa Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai ili azifanyie kazi. Na suala hili kutoka sasa utakuwa ukiliripoti kwangu moja kwa moja!"

Inspekta Jamila alifurahi kupita kiasi, kwani kuweza kufanikisha yule dereva wa Taxi kuachiwa huru, kwake ulikuwa ni ushindi mkubwa. Lakini pia kupewa kazi rasmi na "IGP" na kuiripoti kazi hiyo moja kwa moja kwake pia ulikuwa ni ushindi mwingine.

Hivyo alimshukuru"IGP" na kumhakikishia kwamba ataifanya kazi hiyo kwa uaminifu na kwa utii.

Kisha Inspekta Jamila alitoa picha ya "IGP" aliyopiga na marehemu Hamida akamkabidhi "IGP".

"IGP" akaipokea picha ile huku akitabasamu na kumwambia Inspekta Jamila.

"Nakuaminia askari wangu!"
Kisha wote wakatabasamu kwa pamoja. Na "IGP" akamalizia kwa kusema.
"Nakutakia kazi njema yenye mafanikio tele." Kisha wakaagana.

Inspekta Jamila aliporudi ofisini kwake akiwa na furaha tele huku mkononi akiwa na faili la kesi ya Mwaduga, alimkuta Eshe Muhidini mke wa Mwaduga Dingo akiwa ameketi anamsubiri.

"Karibu mgeni upo muda mrefu?"
Inspekta Jamila alimkaribisha Eshe Muhidini na kumuuliza.

"Hapana afande nina kama dakika tatu toka kufika hapa."
Eshe alijibu, kisha akaendelea, "leo ni Jumamosi nimekuja kukuona katika ile ahadi yetu ili nijue ulipofikia."

"Ohoo! sawa nakumbuka kwani nilikwambia uje leo ili kwanza niwe nimefatilia ili nione nawezaje kukusaidia.
Na hapa nilipo nimepata namna ya kukusaidia, na haitachukua muda mrefu kutoka sasa mumeo utakuwa naye uraiani akiwa huru kabisa!"

Alijibu Inspekta Jamila kwa kujiamini. Jibu hilo lilimfanya Eshe atoe machozi ya furaha na kutoamini alichokuwa anakisikia.

"Afande umesema haitachukua muda mrefu mume wangu atatoka?!"
Aliuliza Eshe kwa fadhaa kama kwamba hakumsikia pale awali alipojibiwa.

Inspekta Jamila alipa jibu, kama lile la awali huku akiongeza neon.

"Sasa hivi tutakwenda wote gerezani tukamuone Mwaduga ili pia nizungumze naye suala hili, na vitu fulanifulani."

Eshe alikuwa katika mshangao mkubwa sana, kwani aliona kama anaota ndoto za mchana. jambo kama lile ambalo hakutoa pesa hata senti tano ya hongo, kama baadhi ya watu wanavyodhani kwamba, huwezi kumaliza kesi bila kuwa na pesa! Sasa yeye hajatoa chochote kisha ndani ya wiki moja suala lile anaambiwa halina muda mrefu litakuwa limetatuliwa.

Jambo alilohenyeka nalo kwa zaidi ya miezi miwili!.
Eshe alimshukuru mwenyezi Mungu, Dokta Zahala na Inspekta Jamila kwa kuweza kumsaidia.

Aliinuka katika kiti alichokuwa amekaa na kwenda kumkumbatia Inspekta Jamila huku akilia kwa kwikwi na machozi yakilowanisha mashavu yake.
Inspekta Jamila alimtuliza na kumnyamazisha, kisha wakatoka wote wakitumia gari ya Inspekta Jamila wakaelekea Gereza la Keko.

*******


Siku ya Jumamosi jiji la Dar es Salaam huwa na foleni za magari sana, hivyo iliwachukua kama saa moja kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani hadi Gereza la Keko.

Baada ya kufika pale na kufanya taratibu za kiofisi, Mwaduga aliitwa katika chumba maalum akaweza kumuona mkewe na Inspekta Jamila, yule afande aliyemuhoji wiki moja iliyopita. Askari magereza aliekuwa amewasimamia ili kusikiliza mazungumzo yale ikiwa ni taratibu za kawaida za jeshi la Magereza.
Baada ya kumjulia hali, Inspekta Jamila akamwambia Mwaduga.

"Nipo hapa ili kukufahamisha jambo moja kuwa, huna muda mrefu kutoka sasa utakuwa raia huru. Jeshi la polisi limefanya uchunguzi wa kina na kuridhika kuwa huusiki kwa namna yoyote katika kesi zinazokukabili, hivyo jeshi nalo linataka ulisaidie katika mambo fulani fulani!"

Alisema Inspekta Jamila huku akimuona Mwaduga macho yamemtoka pima na kuacha kinywa wazi kwa mshangao, huku machozi yakimlengalenga machoni mwake.

Afande Jamila hakumpa nafasi Mwaduga ya kusema neno akaendelea.

"Kwa kuanzia, jeshi la polisi linataka ututajie wasifu wa wale jamaa watatu waliokodisha gari yako namna walivyo. Na je ikitokezea kuziona picha zao au wao wenyewe kwa mara nyingine tena utaweza kuwatambua?"

Inspekta Jamila alimwambia Mwaduga taarifa ile muhimu zaidi ya sana, na Mwaduga Dingo sasa akiwa na nguvu mwilini, mwake na matumaini mapya katika moyo wake alijibu.

"Afande nakushukuru sana, kwanza wewe binafsi kwa juhudi zako za kuweza kulifikisha hapa suala hili, na jeshi la polisi kwa ujumla. Pili kwa mke wangu Eshe kuweza kulifikisha kwako jambo hili! Yaani siamini naona kama nipo ndotoni, kwani kwa zaidi ya miezi miwili hivi sasa, mimi nimekuwa katika maisha mabovu. Hali ya kuwa sijawahi kukamatwa na kuwekwa kituo chochote cha polisi tangu nimezaliwa. wachilia mbali kuletwa gerezani kama mahabusu. Hivyo nimejifunza mambo mengi sana na sasa ninaamini kuwa si wote wanaofungwa jela kwamba wana hatia. Na ama hujafa hujaumbika! Kwani jambo hili haliwezi kusahaulika katika maisha yangu, hadi naingia kaburini."

Mwaduga Dingo badala ya kujibu maswali aliyoulizwa, yeye alianza kutoa risala, yenye wingi wa shukurani.

"Nikiwa huku jela kama mahabusu nimeiweka nadhiri ya kwamba, ikiwa nitashinda kesi hii na kuachiwa huru, basi nitauandika mkasa huu uwe filamu. Ili wale wote waliodhani kuwa mimi ni jambazi na Jamii yote ya Tanzani kwa ujumla wapate somo kutokana na filamu hiyo. Lakini pia kuielimisha Jamii yetu ijue kwamba serikali ipo na inawajali raia zake.
Na pia watambue wapo maaskari wanaojali haki za raia na kuthamini ubinaadamu, ambao hawafanyi kazi kwa nguvu ya rushwa, kama wewe Inspekta Jamila!"

Alipofika hapa Mwaduga sasa akawa analia kwa sauti akiwa hawezi kuongea kwa vile donge la uchungu lilivyomkaa rohoni.



****DINGO anaweka nadhiri…..je atashinda kesi hiyo mbele yake……
**Inspekta JAMILA atafanikiwa kumweka huru???

Jagarld Jullie Z Sangomwile Khantwe Mr Rocky Gunda66 Himidini VAN HEIST BPM ABUBAKAR SHEKAU NYIRO mamsapkhan born again pagan princetx Ennie mcubic jonnie_vincy
 
Last edited by a moderator:
Karibu uraiani mwa dug a. Ila sina I mani na huu wema wa IGP
 
IGP kuna vitu atavifanya si bure.......ahsante Casuist kwa kuniita
 
Last edited by a moderator:
Inspector Jamila angedurufu picha ya IGP na Marehemu Hamida ili kama kukitokea hujuma aweze kumshikisha adabu IGP
 
Kwa intelligentsia yk nzuri nadhani ameshadurufu za kutoka na ushahidi kaacha kwa shoga yake dkt zahala
 
Afadhali igp kwa kuliona hilo,kazi nzuri Insp. Jamila,pamoja sana mkuu Casuist
 
Last edited by a moderator:
Afadhali igp kwa kuliona hilo,kazi nzuri Insp. Jamila,pamoja sana mkuu Casuist
 
Last edited by a moderator:
Afadhali igp kwa kuliona hilo,kazi nzuri Insp. Jamila,pamoja sana mkuu Casuist
 
Last edited by a moderator:
Back
Top Bottom