MOJA ya mambo yanayonivutia ya wenzetu Weupe (Caucasians), ni namna wasivyopenda ‘kubebwa' au kupewa upendeleo wa aina fulani katika kutimiza ndoto zao maishani.
Chukulia mfano wa Peter Buffet. Huyu ni mtoto wa bilionea nambari tatu duniani, Warren Buffet, lakini amekataa kutumia mapesa ya baba yake katika mapambano yake ya kutimiza ndoto yake maishani.
Katika kitabu chake kinachoitwa "Life is what You Make it: Finding Your Own Path to Fulfillment", Peter anasimulia namna alivyokataa ushauri wa baba yake wa kutaka ajitose kwenye masuala ya fedha, na badala yake akapambana mwenyewe kutimiza ndoto yake ya kuwa mtunzi wa vitabu na mwanamuziki.
Peter anaeleza katika kitabu hicho kwamba; licha ya utajiri mkubwa wa baba yake (Buffet), yeye aliishi maisha ya kawaida kabisa na kuchapa kazi kuifanya ndoto yake kuwa kweli bila kumwagiwa mapesa na baba yake. Hivi sasa Peter Warren Buffet ana studio yake ya kisasa ya muziki na pia ni mtunzi wa vitabu.
Nasema nawaheshimu Caucatians kwa hilo; maana angekuwa ni Mwafrika mwenye utajiri wa Buffet, piga ua, angemlazimisha mwanawe ajifunze masuala ya biashara hata kama hana mapenzi nayo; ilimradi tu afuate nyayo zake!
Na ndiyo maana baadhi ya jamaa zangu inawawia vigumu, mpaka sasa, kuamini kwamba mtoto wa bilionea nambari tatu duniani, Peter Buffet, ni mwanamuziki tu wa kawaida anayeishi kwenye nyumba ndogo tu!
Inawawia vigumu jamaa zangu kuamini hivyo, kwa sababu sisi Weusi tukishakuwa na utajiri au kupata nafasi serikalini hatuna hulka wala utamaduni wa kuwaachia wanetu kupigania wenyewe kutimiza ndoto zao maishani bila ‘kubebwa' na wazazi.
Na baadhi ya wanetu nao wamebweteka kiasi kwamba hawajishughulishi kutambua vipaji na karama ambazo Mungu amewatunuku, na badala yake hung'angania kufuata mkondo wa shughuli za wazazi; hata kama hawana karama nazo.
Suala hili la vigogo ‘kuwabeba' watoto wao katika shughuli wanazozifanya maishani au hata katika ajira fulani fulani; licha ya kutokuwa na karama nazo, lina madhara kidogo katika shughuli au biashara ya familia, lakini lina madhara makubwa mno katika fani ya siasa au katika ajira za umma.
Madhara hayo makubwa katika fani ya siasa au kwenye ajira za umma yanatokana na kuwepo mgongano mkubwa wa kimaslahi (conflict of interest) kwa kigogo ‘anayembeba' mwanawe.
Na sote tunajua kuwa penye mgongano wa kimaslahi kuna uonevu, uminyaji haki na kukwazana kimaendeleo; iwe ni kwa mtu mmoja mmoja, kikundi au kwa jamii nzima.
Chukulia mfano wa malalamiko ambayo Mbunge wa Bumbuli, William Shelukindo, ameyafikisha makao makuu ya CCM dhidi ya Januari Makamba ambaye ni mtoto wa Katibu Mkuu wa chama hicho, Yusuf Makamba na pia ni Msaidizi wa Rais Kikwete.
Shelukindo ameiandikia CCM makao makuu barua mbili za malalamiko kwamba Januari ameanza mapema kampeni za kuwania ubunge wa jimbo hilo kinyume cha taratibu, na kwamba baadhi ya viongozi wa CCM katika wilaya hiyo ‘wanambeba' na ‘kumlinda' kwa sababu tu ni mtoto wa Katibu Mkuu wa CCM (yaani bosi wao).
Ingawa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa, amekaririwa na gazeti hili akisema kwamba CCM imeunda kamati ya watu watatu kuhukumu kesi za wawania ubunge walizozipokea, ni vigumu kuamini kwamba Shelukindo atatendewa haki na kamati hiyo iliyoteuliwa na makao makuu ya CCM ambako baba wa mtuhumiwa ndiye Katibu Mkuu.
Ni vigumu kuamini vilevile kwamba Katibu Mkuu, Yusuf Makamba, hataiingilia kamati hiyo, kwa njia moja au nyingine, ili tu ‘amlinde' mwanawe Januari Makamba dhidi ya madai hayo yanayoweza kupeperusha ndoto ya kumuona mwanawe anakuwa mbunge wa jimbo hilo.
Nimeangalia kwenye kamusi ya Kiingereza maelezo ya maneno conflict of interests (mgongano wa maslahi) na inasema hivi: A conflict between a person's private interest and public obligations; yaani "mgongano wa maslahi ya mtu binafsi na maslahi ya umma".
Katika hili la Januari Makamba vs William Shelukindo, ni dhahiri kuna mgongano wa kimaslahi kwa Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba; kwani yeye kama mtendaji mkuu wa CCM makao makuu, itamuwia vigumu ‘kuyabariki' na kuyapitisha maamuzi yoyote ya kamati hiyo dhidi ya mwanawe.
Kwa maneno mengine, uwezekano wa Shelukindo kunyimwa haki kwa sababu ya mgongano huo wa kimaslahi unaomkabili Katibu Mkuu Yusuf Makamba, ni mkubwa. Na si Shelukindo tu ambaye haki yake itabinywa; bali pia wapiga kura wa jimbo la Bumbuli.
Mfano mwingine ni ule unaomhusu aliyekuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Hamad Masauni. Huyu aliondolewa kwenye nafasi hiyo na mkutano mkuu wa umoja huo uliofanyika mjini Iringa, hivi karibuni, kwa tuhuma za kughushi (kudanganya) umri.
Lakini wanaofuatilia mambo ndani ya umoja huo wanasema kwamba Masauni ni mwathirika tu wa makundi mawili yanayosigana ndani ya umoja huo, na kwamba suala la kudanganya umri limetumiwa tu kama ‘silaha ya mwisho' ya kumuangamiza.
Inaaminika kuwa kundi lililopanga mikakati ya kumuondoa Masauni liliongozwa na Makamu Mwenyekiti wa umoja huo, Benno Malisa na mtoto wa Rais Kikwete, Ridhiwan Kikwete.
Inafahamika vilevile kwamba ingawa Ridhiwan Kikwete ni mjumbe tu wa kamati ya utendaji ya chama hicho, lakini ana nguvu kubwa ndani ya umoja huo wa vijana kwa sababu tu baba yake ni Rais na Mwenyekiti wa Taifa wa CCM!
Na ndiyo maana ilipofahamika kuwa Masauni ametofautiana na kundi la Malisa na Ridhiwan, wachambuzi wa mambo walijua kwamba ni suala la muda tu kabla Masauni hajapoteza kiti chake; maana huwezi kutofautiana na mtoto wa Rais na Mwenyekiti wa CCM wa Taifa, na kisha ukaendelea kubaki salama kwenye nafasi yako!
Hoja hii inakuwa na uzito hasa ukizingatia kwamba ni Rais Kikwete mwenyewe, wakati akiongoza kikao cha Kamati Kuu ya CCM, aliyependekeza mwenyekiti wa UVCCM safari hii atoke upande wa Zanzibar, na hata kuridhia Masauni (anayetokea huko) agombee.
Kama hivyo ndivyo, je; Masauni hakufanyiwa uchunguzi wa awali (vetting) kabla Kikwete na kamati kuu yake hawajapitisha jina lake kugombea uenyekiti wa UVCCM?
Ukweli ni kwamba walichunguza na walilijua mapema suala hilo la kudanganya umri, lakini kwa wakati huo hawakuliona kuwa ni tatizo (kama ambavyo hawaoni baadhi ya mawaziri waliodanganya kuhusu viwango vyao vya elimu kuwa ni tatizo).
Hoja ni kwamba walikuja tu kulitumia suala hilo la umri kumng'oa Masauni madarakani pale alipoanza kutofautiana na kundi la kina Malisa na Ridhiwan ndani ya Umoja huo.
Kwa hiyo, kauli ya Rais Kikwete aliyoitoa Iringa wakati akihutubia mkutano huo mkuu wa UVCCM kwamba Masauni ilibidi ang'olewe kwa sababu alidanganya umri, ina utata.
Ina utata kwa sababu haiwezekani kwamba Kikwete na Kamati Kuu yake ya CCM hawakulijua hilo wakati wanaridhia Masauni agombee uenyekiti wa UVCCM.
Kwa yeyote mwenye kufikirisha bongo yake, ni dhahiri kwamba Kikwete aliunga mkono kung'olewa Masauni kwa sababu Masauni alitofautiana na kundi la UVCCM ambalo yupo mwanawe Ridhiwan; kundi ambalo linampigia kampeni achaguliwe tena kuwa rais kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba.
Kwa ufupi, kulikuwa na mgongano wa kimaslahi kwa Rais Kikwete katika suala hilo la Masauni; kwa vile mtoto wake Ridhiwan alihusika nalo.
Vyovyote vile; Rais huyu asingetarajiwa kwenda kinyume na matakwa ya mwanawe kwenye suala hilo la Masauni. Na nina hakika, Masauni mwenyewe anajihisi kuonewa.
Tukiunganisha yote mawili (la Ridhiwan na Januari), ni dhahiri kuna juhudi za wazi za baba wa watoto hawa za ‘kuwabeba' ili wapande haraka ngazi za kisiasa wakati wangalipo madarakani. Binafsi nitashangaa kama Ridhiwan hatakuwa mbunge (kupitia UVCCM) katika ngwe ya mwisho ya urais wa baba yake!
Najua kuna watakaodai kwamba watoto hawa wa wakubwa wana sifa za uongozi wa kisiasa, na kwamba ‘hawabebwi' na baba zao, lakini nami nitawauliza: Nani alimjua Januari Makamba kama mwanasiasa kabla Yusuf Makamba hajawa Katibu Mkuu wa CCM? Nani alimjua Ridhiwan Kikwete kama ana sifa za uongozi wa kisiasa kabla Jakaya Kikwete hajawa Rais wa Tanzania?
Hata hivyo; nikimbilie kusema kwamba sina hakika kama ni Kikwete na Makamba wanaowalazimisha watoto wao kuwa wanasiasa au ni watoto wenyewe ndiyo wanaowashinikiza wazazi wao ‘wawabebe' kisiasa ili wawaache pazuri kabla hawajaondoka madarakani.
Vyovyote vile; kuna mgongano wa kimaslahi katika utekelezaji wa hatua za watawala wetu za ‘kuwabeba' kisiasa watoto wao. Na kama nilivyosema mwanzo, penye mgongano wa namna hiyo kuna uonevu na kunyimana haki si kwa mtu mmoja mmoja tu; bali kwa jamii nzima.
Sasa, najua ni vigumu watawala wetu kuwa na hulka za kina Warren Buffet za kuwaachia watoto wao wagundue wenyewe vipaji vyao na wapiganie wenyewe kutimiza ndoto zao, lakini vigogo wetu, angalau basi, wangesubiri kwanza waondoke madarakani ndipo watoto wao wajitose kwenye siasa.
Nina hakika hilo lingepunguza conflict of interests ninazozizungumzia na pia lingepunguza upendeleo wa watoto wa wakubwa (nepotism) hata katika ajira nyingine.
Ushauri wangu wa mwisho kwa watawala wetu, ni kwamba wawaachie watoto wao wagundue wenyewe karama na vipaji walivyopewa na Mungu badala ya kuwang'ang'aniza waingie katika siasa au katika ajira ambazo hawazipendi au wasizo na sifa nazo.
Na watoto nao wajitazame wenyewe na kujiuliza wanataka kufanya nini maishani, na kisha waanze wenyewe kupigania kutimiza ndoto zao hizo badala ya kusubiri ‘kubebwa' na wazazi wao; hata kama wazazi wana utajiri na hekima sawa na Mfalme Suleiman! Nawashauri wajifunze kutoka kwa Peter Warren Buffet – mtoto wa bilionea nambari tatu duniani.
Wakifanya hivyo, watapata furaha maishani; hasa watakapovuna jasho lao wenyewe na kufurahia taaluma walizojichagulia na ambazo Mungu aliwatunukia karama.
Kwa hakika, wakati mwingine huwa najiuliza (kwa mfano) iwapo Waziri wa Ulinzi, Hussein Mwinyi (mtoto wa Rais wa zamani, Ali Hassan Mwinyi) anafarijika kitaaluma kufanya kazi hiyo badala ya ile aliyoisomea ya udaktari wa tiba.
Hivi mtu anawezaje kusota kwa miaka saba akisomea udaktari wa tiba, na kisha anapohitimu akubali kuwa Waziri wa Ulinzi na kujishughulisha na masuala ya makombora, vifaru, AK 47 nk ambayo ni mbali kabisa na taaluma yake? Nina hakika Hussein Mwinyi angekuwa daktari mzuri tu wa tiba kuliko alivyo Waziri wa Ulinzi!
Tafakari.
Imeandikwa na Johnson Mbwambo wa Raia Mwema
Nimevutiwa sana na makala hii..Sijui wenzangu mnasemaje!