Mh. Rais Samia, wakati akikemea wanaotaka kuipaka matope Serikali yake, alisema, "sitakubali, nitasimama na wananchi".
Mimi nakubaliana sana na kauli hii, mashaka yangu ni namna ya kuiishi.
Ikumbukwe kwamba, Rais Samia wakati anaingia madarakani, nchi ilikuwa kwenye kiu na njaa kali ya haki, njaa na kiu kali ya demokrasia na uhuru wa watu. Ni kipindi ambacho kulikuwa na kundi kubwa la watu waliokuwepo mahabusu za polisi kwa kubambikiwa kesi za uhujumu uchumi, utakatishaji fedha haramu, ugaidi, uchochezi na uuzaji wa madawa ya kulevya. Ni kipindi ambacho shughuli za kisiasa zilikuwa zimezuiwa, isipokuwa kwa CCM pekee.
Ni kipindi ambacho, kutokana na mateso na njama mbalimbali dhidi ya yeyote anayeonesha kuikosoa Serikali au Rais, maisha yake yalikuwa kwenye mashaka makubwa. Ni kipindi ambacho watu kupotea, kutekwa, kuteswa na hata kuuawa, halikuonekana ni jambo la ajabu. Ni kipindi ambacho uhuru wa fikra ulikuwa umewekwa komeo la chuma isipokuwa kwa wale wanaoweza kuishi kwa unafiki wa kumsifia Rais kwa kila jambo.
Ni kipindi ambacho kwa mara ya kwanza, Waziri aliwahi kumtaja Rais kama Mungu, RC alitamka kuwa Mungu anatakiwa kumshukuru Rais, na Waziri Mwingine alisema wazi kuwa Rais ni kaka Yesu Kristo Masihi. Hiki ndicho Rais Samia anakabidhuwa madaraka ya Urais akiwa mwanamama wa kwanza kushika nafasi hiyo.
Rais Samia ameingia kwenye madaraka, huku ile infrastructure iliyotengeneza na kupalilia uovu mbalimba ikiwa ipo vile vile. Nina imani kubwa ni infrastructure hii ndiyo iliyomwingiza chaka Rais Samia, mpaka kufikia kutamka kuwa Mbowe ni gaidi. Ni infrastructure hii ndiyo inayoendelea na kesi za kubambikia watu, ushahidi wa kutengeneza, kuwa na majaji ambao maamuzi yao ni ya kuleta mashaka makubwa.
Rais Samia, alipoanza kufanya mabadiliko mbalimbali, alishangilia, alisifiwa na kukubalika na watu wengi wa makundi mbalimbali bila ya kujali vyama vyao vya kisiasa, dini zao, makabila yao au maeneo watokayo.
Uungwaji wake mkono, bila hata ya takwimu, kwa uwazi kabisa, uliporomoka ghafla baada ya kuonekana kuwa ameungana au ameagiza Mbowe kubambikiwa kesi. Jambo hili liliwaudhi sana wapenda haki wote na watu wanaoheshimu nafsi zao, bila ya kujali watu hao ni wafuasi wa vyama vya upinzani au CCM au hawana chama, na kwa upande mwingine, ndiyo jambo lililoleta mashaka makubwa kwa mataifa ya nje, kama kweli Rais Samia ana dhamira ya dhati ya kutaka kujrnga Tanzania ya haki.
Kama Rais Samia anataka kusimama na wananchi, basi ni lazima asimame katika haki, asimame kwenye misingi ya demokrasia na uhuru wa maoni wa watu na vyombo vya habari. Maana katika hayo, Watanzania wote wenye dhamira njema na nchi yao. Lazima Rais Samia, usimame kwenye upande unaoeleweka, ama usimame na watu wa haki au na waovu, hakuna neutral position kwenye hili. Lazima uamue unataka usifiwe na ukubaliwe na waovu au watu wema.
Rais Samia utambue kuwa waovu ni wachache sana, japo sauti zao zinaweza kuwa na uwezo wa kusikika sana kwa sababu ya nguvu walizokuwa nazo kwenye mfumo wa uovu. Ukisimama na wananchi, tena kwa haki na kwa dhamira njema, hakuna wa kukutisha, kubabaisha wala kukupa hofu. Ondokana na magofu ya maadui wa kurithi, yatakuangukia usipate wa kukuchomoa.
Mungu akujalie hekima ya kuangalia zaidi kesho na keshokutwa kuliko kuangalia tu leo.