Rai ya Jenerali Ulimwengu shambulizi kwa Kikwete?

sikiolakufa

JF-Expert Member
Feb 1, 2010
411
54
RAI YA JENERALI

Maandiko 12 ukutani, nasi twacheza nachi

Jenerali Ulimwengu
Mei 25, 2011


KATIKA makala yangu iliyopita nilisema kwamba tunatakiwa kuacha kupiga chenga masuala muhimu ambayo tunatakiwa tukabiliane nayo na tuyatatue. Nilisema pia kwamba kazi ya kujadili na hatimaye kuandika Katiba mpya si kazi ya mzaha wala si kazi rahisi, kwani ni kazi muhimu na nzito na inahitaji utashi mkubwa zaidi kuliko ule unaojidhihirisha miongoni mwetu.

Pia nilisema kwamba katika mjadala huu kila jambo linazungumzika, ispokuwa tu yale yaliyowekewa mizingo na itikadi zenye miiko yake ambayo tunaielewa. Kwa mfano, bila kujali imani ya huyu au yule, sidhani kwamba tutaweza kujadili jambo lo lote linalohusu imani za kidini zinazohusu madhehebu mbali mbali kwa lengo la kukubaliana ni dini gani au madhehebu yapi yakubaliwe na kila raia.


Wala hatuwezi kujadili iwapo watoto wanaozaliwa nchini wawe ni wa baba na mama zao au wawe ni wa kijiji au mtaa. Mwanafalsafa wa Kiyunani, Plato, alijaribu kuonyesha ni jinsi gani mpangilio kama huo ungekuwa na manufaa katika ‘Jamuhuri' yake, lakini siamini kwamba tutafikia huko katika karne hizi mbili au tatu zijazo.


Nadhani pia kwamba hatuwezi kujaribu kujadili kama ni vyema tukawa na utaratibu wa watoto wapendanao kuoana katika umri wa miaka saba alimradi wazazi wao wameridhia, au kwamba ndoa halali zisiendelee kwa zaidi ya miaka 10 kwa kuhofia uchovu wa wanandoa!


Nasema, hatuwezi kuyajadili masuala haya kwa sasa kwa kuielewa jamii yetu ilivyoundwa na jinsi mapokeo yanavyotuelekeza katika maisha yetu. Mifano yote niliyoitoa hapo juu haihusu maumbile ya binadamu, bali inahusu utaratibu uliowekwa na jamii na ambao kwa sasa, kwa hali ilivyo, haujadiliki kwa sababu jamii haiko tayari kuujadili, achilia mbali kama ni sahihi au sio sahihi. Na hapa, ikumbukwe, sijazungumzia mjadala tunaoweza kuutamani wa kutaka kubadili utaratibu ili jua lichomoze Magharibi na litue Mashariki.


Jamii ya binadamu siku zote inaendeshwa na taratibu zilizowekwa, na hizi hutokana na historia, desturi, mapokeo na mahitaji ya sasa ya jamii hizo. Hutokea kwamba mahitaji hayo ya sasa yakawa na nguvu kubwa zaidi au ushawishi mkubwa zaidi kuliko mapokeo na desturi, na msuguano unaotokea ukasababisha mtafaruku, lakini baada ya muda mambo yakatulia na jamii ikaendelea kama vile halijawa jambo ingawaje mambo yamebadilika. Mambo mengi hubadilika na yakachukua sura mpya kimya kimya kwa sababu hayatangazwi kwa baragumu ila wenye uwezo wa kuyabaini watayabaini.


Aghalabu, hali mpya inayotokana na msuguano huo hujichimbia hadi nayo ikaja kukubalika kama sehemu ya mapokeo na desturi, hadi nayo ikawa ni kikwazo kwa mawazo mapya yanayotafuta njia ya kusonga mbele zaidi. Kwa jinsi hii, jamii nyingi duniani zimesonga mbele karne hata karne, muongo hadi muongo, mwaka hadi mwaka, mwezi hadi mwezi, wiki hadi wiki, siku hadi siku, saa hadi saa, dakika hadi dakika, sekunde hadi sekunde.... hata kama hatutambui mara moja.


Utambuzi huu ni mgumu kwa watu wote ila kwa wale waliojenga uwezo mkubwa wa kubaini linalokuja kabla halijawasili mlangoni na kubisha hodi. Dunia inao watu wengi wanaoweza kubaini mambo haya, mpaka wakakaribiana na hayawani kama mbwa, ng'ombe, mbuzi, aina fulani ya ndege, na wanyama wengine walio na kipawa cha ‘kunusa' mabadiliko katika sayari na kutoa ishara mahsusi ambazo kwa wajuzi ni ishara za tanbihi zinazowafanya wachukue hadhari dhidi ya hatari kama vile tetemeko la ardhi, gharika na maporomoko.


Vipawa kama hivi ni nadra na si kila mnyama kapewa. Pia, katika shughuli zinazowahusu binadamu, si kila binadamu anaweza kuwa na vipawa kama hivyo. Kwa kuwa si rahisi kwa kila binadamu kuwa na hivyo vipawa kwa njia za maumbile tu, kama vile hayawani niliowataja hapo juu, binadamu wamelazimika kujifunza kuvijenga vipawa hivyo kwa kuzichunguza jamii waishimo.


Sasa, basi, hebu tujaribu kujijengea vipawa kama vile vya wanyama niliowataja hapo juu, vya kuweza kubaini ujio wa mambo ambayo ndiyo yameanza safari kuelekea kwetu, tujipe uwezo wa kusoma maandishi yaliyo ukutani ambayo Danieli anayaona lakini mfalme Nebukadneza hayaoni. Nini kimeandikwa ukutani ambacho watawala wetu wanashindwa kukisoma?


Mosi, imeandikwa kwamba mwaka huu ni 2011, miaka 50 baada ya Uhuru wa Tanganyika na miaka 47 baada ya Mapinduzi ya Zanzibar na muungano uliozaa Tanzania. Hiyo ni nusu karne katika maisha ya Taifa, muda mrefu wa kutosha kwa watu kujiuliza maswali mengi juu ya maisha yao.


Pili, ukutani imeandikwa kwamba watoto waliozaliwa mara tu baada ya Tanganyika kupata Uhuru, mwaka huu wanatimiza miaka 50. Ni watu wazima wanaoelekea uzeeni. Wale waliozaliwa mara tu baada ya Mapinduzi ya Zanzibar na Muungano na wao pia ni wa rika hilo hilo.


Tatu, imeandikwa kwamba vijana ndiyo sehemu kubwa ya marika ya nchi hii na hao vijana wana matumaini ambayo hayajawahi kuwakuta wazee wao, na vijana hao wanahamanika kutokana na kuishi katika hali iliyojaa maswali lukuki na majibu karibu na sufuri.


Nne, imeandikwa kwamba matumaini ya vijana na matatizo yanayotokana na kutopata majibu kwa maswali yao ni mambo ambayo yanaonekana kuwashinda wakubwa wa siasa na dola, hata angalau kuyafikiria na kuyaelewa. Yanaonekana kama matatizo yenye siri kubwa na ambayo yanahitaji uwezo ambao wakuu wetu hawanao.


Tano, ni dhahiri kutokana na maandishi yaliyo ukutani kwamba vijana wanaamini kwamba matataizo yao yana utatuzi, lakini wakuu wa siasa na dola hawana uwezo wa kuuona utatuzi huo kwa sababu hiyo si azma yao; kwani wamezama katika shughuli nyingine ambazo hazihusiani na utafiti wa utatuzi huo.


Sita, imeandikwa kwa herufi za moto kwamba nchi imepoteza mwelekeo na imekuwa ikielea kwa muda mrefu, imeacha misingi yake ya awali iliyoijengea mshikamano, umoja, upendo na amani na badala yake tunavuna ubinafsi, ubaguzi, utengano, dhuluma na migawanyiko inayotishia amani kwa kiwango cha kutisha sasa.


Saba, imeandikwa bayana kwamba iwapo mabadiliko makubwa, ya haraka na ya kina hayatafanywa katika kipindi kifupi kijacho , na kama hali ya kuelea itaendelea kutusogeza mbali na pwani yetu, kuna hatari ya kweli ya kupatwa na hasara kufa na maafa tusiyotarajia, hususan kutokana na wanasiasa na wenzi wao (pamoja na familia zao) wenye uchu wa madaraka na mali.


Nane, inasomeka ukutani kwamba kinachoweza kulinusuru Taifa kwa sasa ni mkusanyiko wa wazalendo walio tayari kujiunga kwa lengo la kuisaidia nchi yao ili kuirejesha katika misingi ya awali iliyotajwa hapo juu kwa kupambana dhidi ya kutojali, upuuzi, ufisadi, wizi, ubadhirifu, ulaghai, ubazazi, udanganyifu, uonevu, woga, ubarakala, unafiki, uzandiki, na u-mimi-na-familia-yangu.


Tisa, ukuta umebeba bango linalosema kwamba haya yote yanatokea kwa sababu nchi imekosa uongozi na hilo limetokea kwa sababu ya mifumo ya hovyo, iliyochoka na ambayo haitoshelezi matakwa ya kiuongozi na ya kiutawala inayolingana na mahitaji ya karne hii.


Kumi, Danieli anasoma ukutani bila shida kwamba nchi sasa inahitaji wazalendo wanaoweza kuongoza mjadala kuhusu masuala ya utawala katika mapana na marefu yake yote, wakati Nabukadneza anakodoa macho, haoni kitu, anawatuma wajumbe wake wakawatangazie raia zake kwamba anaandaa karamu ya kucheza nachi. Raia wanamwambia enzi za nachi zimepita, lakini hang'amui.


Kumi na mosi, imeandikwa kwamba ama Nebukadneza akubali maono aliyopewa na Danieli ama yatokee mabadiliko makubwa ambayo hata Danieli hakuyataraji, lakini hayo mabadilko makubwa yaambatane na vurugu na vilio na kusaga meno.


Kumi na pili, haya yote yameandikwa bayana, na ukuta yalipoandikwa hauko ndani ya kasri ya Nebukadneza; bali umesimama njia panda kuu ya mji, na atakaye kuona ataona, bali asiyetaka kuona hajajaliwa kipawa cha kuona.
 
Yote kumi na mbili ni makuu. Lakini mimi naona kuu zaidi ni namba tisa (uongozi). Jamii yoyote ile isiyokuwa na uongozi mzuri inapotea. Hii haijali kuwa hiyo jamii ni ya binadamu, wanyama wa porini, wanyama wa kufungwa, ndege wa angani, wadudu, au samaki wa habarini.
 
Mkuu!

Nampongeza sana Jenerali!! Anaionyesha jamii mwelekeo halisi japokuwa inachukua muda kumwelewa coz ni mwanafasi fasuata!!!Makala hii inashabihiana na zille barua 12 ulizotoa, ni kweli wakati umefika wa miti kusema na manyani kugeuka watu sasa ni vurugu kilio na kusaga meno!!! Bila busara na hekima kutumika, the centre cant hold anymore!!!
FALCON CANNOT HEAR THE FALCONNER!!!!:A S 103:
 
generali ni noma....sasa sijui usalama watamvamia tena kama wakati wa bully mkapa?
 
Viongozi wetu ni wavivu wa kufikiri na sidhani kama wana mda wa kusoma hata magazeti, wangekuwa wanasoma wangejua yanayoendelea katika jamii. Kwa sababu ya umwinyi na kupenda sifa wamejifungia kwenye magamba ya chuma hawasikii wala kuona nje watakuja kustuka dakika za mwisho ambapo watakuwa wameshachelewa, kama alivyosema Ulimwengu "yote haya yameandikwa bayana" na ni kweli matatizo ya wananchi yapo bayana.
 
They have put a sword through the string that bound us together now the center can not be told THINGS HAVE STARTED TO FALL APART
 
Danieli anasoma ukutani bila shida kwamba nchi sasa inahitaji wazalendo wanaoweza kuongoza mjadala kuhusu masuala ya utawala katika mapana na marefu yake yote, wakati Nabukadneza anakodoa macho, haoni kitu, anawatuma wajumbe wake wakawatangazie raia zake kwamba anaandaa karamu ya kucheza nachi. Raia wanamwambia enzi za nachi zimepita, lakini hang'amui.
 
Ama kweli rai imekaa vizuri, tatizo ni JK si msomaji (makini) na akisoma hatoambulia kitu.
Rweyemamu najua anasoma kila kiandikwacho, namshangaa kwa nini hamshtui boss wake.
 
Ama kweli rai imekaa vizuri, tatizo ni JK si msomaji (makini) na akisoma hatoambulia kitu.
Rweyemamu najua anasoma kila kiandikwacho, namshangaa kwa nini hamshtui boss wake.

yule Mkweree hasomi magazeti makini , yeye na mkewe Mwalimu wanadodosa Kiu, Ijumaa, Alhuda na Sani. . . Udakuzi family !
 
Hii makala imegusa ndani kabisa ya moyo wangu, nimetamani kutoa chozi la furaha, nikaiona hadithi ya Nabukadneza na Daniel, mmh, angekuwepo "Mtume" flani angesema hii hadithi ilitabiriwa Tanzania! kweli siioni kama tutakatiza 2014, bado sijapata insights toka kwenye jeshi ila fununu zilizopo ni kwamba askari walio wengi wako upande wetu! AMEN
 
Nimeisoma hiyo kitu jumatano,
Leo asubuhi nikasoma tena kabla ya kutoka!
Du, nimehisi kupata hisia ambazo hadi sasa sijui jinsi ya kuzielezea,
Nashukuru umeipost hapa "Kayagila", nilikuwa natamani wa kushare naye hii kitu!
CCM kwa utawala wao wa kitaahira, wanatulazimisha kuikomboa kwa gharama kubwa sana.
Mzee Ulimwengu, amechora tafsiri makini sana kwa kila kinachotokea saiv nchini.............
Nilipata kusema kuwa, hali ya nchi ni tete kuliko watu wengi wa kawaida tunavyoona
 
Nimelipenda andiko la kumi japo sijui mchezo wa Nachi unachezwaje(aujuae anijuze) sijui ni aina ya kiduku?

Kazi ipo kwenye way forward-andiko la nane lakini inategemea andiko la 11 kama Mfalme atakubali kuyaona haya maandiko na kuwa mkweli kuwa hayaletwi na chama fulani au kundi lolote ni hali ilivyo kwa ujumla wake

MUNGU IBARIKI TANZANIA NA WATU WAKE
 
Kazi ipo kwenye way forward-andiko la nane lakini inategemea andiko la 11 kama Mfalme atakubali kuyaona haya maandiko na kuwa mkweli kuwa hayaletwi na chama fulani au kundi lolote ni hali ilivyo kwa ujumla wake

MUNGU IBARIKI TANZANIA NA WATU WAKE

Kazi kubwa ipo kwenye kuelewa haya ili kubadili utashi... kama aliyeshika mpini hayaelewi haya na hivyo kukosa utashi wa kuamua kuleta mabadiliko yanayofaa, mabadiliko yasiyoegemea kwenye ubinafsi, mabadiliko yenye kujali nchi na wananchi wake wote, ni dhahiri kuwa tutaishia kwenye vurugu na umwagaji damu. Hili wala si somo gumu kulielewa, bali anayesomeshwa ana moyo mgumu usiotaka kuelewa.
Anyway, nimependa kichwa cha habari
 
Watu wa aina ya Ulimwengu ni wachache sana tz!!Makala hii nisomo imara sana wa wahafidhina!! Lakini wasiwasi wangu ni kwa kikwete, atasoma lakini hata elewa,ataelewa lakini hataufuata,atataka kuufuata lakini hatathubutu. Hii inatokana na uwezo wa kifikra na kimang'amuzi alionao muhafidhina wa magogoni!!
 
Back
Top Bottom