Pole Rais Kikwete: Tatizo siyo umri wa watendaji wako!

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,476
39,995
POLE RAIS KIKWETE, TATIZO LA VIONGOZI ULIONAO SIYO UMRI!
Na. M. M. Mwanakijiji
Kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, kama nitajaliwa na nikapata bahati ya kuchaguliwa tena, nitahakikisha kuwa naubadilisha uongozi wa Tanzania kwa kuufanya uongozi wa vijana zaidi. Wale viongozi wa rika langu lazima waanze kuwaachia nafasi vijana
- Rais Kikwete

Ukiyasoma maneno hayo ya Rais Kikwete siku chache zilizopita unaweza kuamini kuwa tatizo la Tanzania kwa sasa katika uongozi ni umri wa viongozi wetu. Na kama ni mtu ambaye hufuatilii yale yanayoendelea katika ulimwengu wetu wa kisiasa unaweza kudhania (japo kwa makosa) kuwa tatizo la wale wanaotuongoza ni rika lao la umri na hivyo tukibadilisha tu viongozi wetu toka rika moja kwenda rika jingine basi tutakuwa tumetatua tatizo letu ambalo kwa sasa linaonekana ni la kudumu la uongozi.

Ndugu zangu, tatizo letu kama taifa linapokuja suala la uongozi siyo umri. Mtu mwingine atakuja na kutuambia kuwa tatizo letu ni usomi; kwamba tungelikuwa na viongozi waliosoma sana basi uongozi wetu ungekuwa mzuri kiasi ambacho tunatarajia au kuombea. Na mtu mwingine anaweza kutuambia kuwa tatizo letu katika uongozi ni uzoefu; na hata mtu mwingine anaweza kuja na kutuambia kuwa tatizo letu katika uongozi kama taifa ni watu kutokuwa na imani n.k
Haya yote ambayo yanatajwa na kuzungumzwa kama matatizo katika uongozi wetu yaweza kuwa na ukweli wa aina fulani na yanaweza kubeba siri fulani ya kushughulikia hali ya uongozi wetu. Hata hivyo ninaamini kabisa kuwa tukiyaangalia haya yote tunaweza kukosa kuangalia hasa kile kinachotusumbua katika uongozi wa taifa letu; siyo katika siasa tu bali pia katika uongozi wetu wa sekta na maeneo mbalimbali ya jamii yetu.

Nimeshaigusia hii mada ya uongozi mara kadhaa huko nyuma na kwa vile inaonekana somo hili bado ni gumu watu kulimudu kiasi kwamba rais wetu naye ameingia kwenye mtego wa kuamini nadharia ya uongo basi naitwa tena na historia kugusia tena dhana ya uongozi na kiini cha mgogoro wa uongozi (leadership crisis) ambayo tunayo katika taifa letu.

Tunashuhudia dalili za tatizo
Tukiangalia mlolongo wa matukio mbalimbali hasa ndani ya miaka hii 20 hivi iliyopita kitu kimoja kinachopiga kelele kama ngurumo ya radi na kutumulika kama mwangaza wa mlipuko wa nyota ni "uongozi". Kuanzia matukio ya uuzaji wa dhahabu yetu kinyemela, uuzwaji wa mbuga zetu kwa wageni na hatimaye ukaribishaji wa matapeli wa kimataifa ambao wengine wamejipa majina ya "wawekezaji" tunaweza kuona kuzembea kwa safu ya uongozi wa taifa letu kiasi cha kutufanya tujisikie aibu na soni isiyokoma.

Wizi wa mabilioni toka Benki Kuu, na kuingiwa kwa mikataba mibovu kuliko ile waliyoingia mababu zetu mbele ya wamisionari, wavumbuzi na wafanyabiashara wa kikoloni ambao walikuwa ni wafalme wa makuwadi wa ukoloni unatuthibitishia jambo dhahiri kuwa elimu, umri, uzoefu (yaani muda mrefu wa kazi) siyo hasa tatizo tulilonalo. Haya yote tunayoyalalamikia leo hii yanatuimbia kuwa tuna tatizo katika uongozi na kwa hakika siyo elimu, umri, wala uzoefu ndiyo chanzo chake!

Uongozi ni zaidi ya hayo
Ndugu zangu, ukiangalia mazingira ambayo watu wetu wanaishi, ukiangalia utendaji katika maeneo mbalimbali na ukiangalia maamuzi ambayo yanachukuliwa katika nafasi mbalimbali kuanzia katika kijiji hadi kwenye lile "jumba jeupe la kale" pale magogoni unaweza kuona kuwa kuna tatizo kwa viongozi wetu.

Tatizo siyo elimu!
Nimesema hapo juu kuwa tatizo letu siyo elimu ya viongozi wetu kwani tunao wasomi wengi sana kwenye fani ya uongozi wetu ambao wana shahada za kwanza, za uzamili, za uzamivu na wengine wanazo hata za ubadhirifu! Kama ni elimu tu wapo wengi ambao wamesoma na walioandika kila aina ya hoja zao na kuzitetea na kufaulu huku wakipambwa! Mambo ambayo Waingereza, Wamarekani, Wajerumani na hata Wajapani wanajifunza watu wetu wanafunzwa vile vile na wengine wanafanya vizuri na "kupasua" kuliko watu wa mataifa hayo!

Ukienda kwenye baadhi ya vyuo ambavyo "wasomi wetu, viongoz" wamepitia huko majuu utashangaa sifa wanazomwagiwa kwa jinsi walivyofanya vizuri darasani. Wapo waliofaulu wakiwa na cum laude na wengine wakiwa na magna cum laude na hata wengine kupewa nafasi za kutoa hotuba za siku zao za kuhitimu kwa niaba ya wanafunzi wenzao wa "kizungu"!

Nitoe mifano michache tu hapa; Andrew Chenge ni msomi aliyesomea huko Harvard Marekani miongoni mwa vyuo vyenye sifa za juu zaidi (kama siyo chenye sifa ya juu zaidi) huko Marekani; Nazir Karamagi amesoma Chuo kile kile alichosomea baba wa Taifa kule Uingereza cha Edinburg; Lawrence Masha ni msomi wa Chuo Kikuu cha Georgetown, huko Marekani; na wengine wengi waliosoma katika vyuo vyetu mbalimbali na hasa waliosoma Mlimani na kuhitimu katika umahiri wa fani mbalimbali!

Hawa wote ni watu ambao wana elimu na kwa kipimo chochote kile hatuwezi kusema kuwa hawakusoma. Karibu idara, ofisi na sehemu zetu mbalimbali zinaendeshwa na watu ambao wengi wao wamesoma chini ya Tanzania huru na hawana kile kisingizio cha "elimu ya mkoloni". Hawa ndio waliosoma tukiwa na matumaini ya kuwa wamepata mwanga wa uzalendo! Lakini, tukipima matokeo ya elimu yao tunaona kikomo chao.

Tukiwauliza hata hivyo watunyambulishie tatizo letu wataandika kwa lugha za kitaalamu na elimu siyo tatizo letu hata kidogo kwani tunawasomi wanaoshindana na wasomi wa mahali popote duniani.

Tatizo siyo uzoefu;
Mara nyingi tunapozungumza uzoefu tunazungumzia muda mrefu kazini. Tunaamini (kwa usahihi) kuwa muda mrefu katika kazi fulani hujenga uzoefu na umahiri wa aina fulani na humuandaa mtu kwa matatizo ya aina mbalimbali. Kuna vitu mtu anaweza kufundishwa shuleni au chuoni lakini uzoefu hupatikana kwa kupita kwa muda na kwa kujifunza katika mazingira ya kazi. Katika hili unaweza kuona msomi wa darasani na msomi wa kazini. Mzee ambaye hajaenda chuoni kabisa anaweza kukabiliana na tatizo fulani la kiufundi kwa namna ambayo msomi wa kitabuni itabidi aite wawekezaji kuja kumsaidia.

Inakuwaje hata hivyo kama mtu mwenye uzoefu ni yule mwenye uzoefu wa kufanya kitu kibovu kwa muda mrefu? Inakuwaje kama uzoefu ambao mtu anao unatokana na uzoefu wa kuvunja sheria, taratibu na mfumo bora wa utendaji kazi kiasi kwamba mtu anajua kufanya kazi yake kwa njia mbovu kwa muda mrefu zaidi? Je, huyu tukimpa nafasi sehemu nyingine kwa kuangalia "uzoefu" tunafikiria huko anakokwenda ataanza kufanya vitu kwa namna bora zaidi kwa sababu ya uzoefu wake? Je mwenye uzoefu wa ufisadi tunatarajia tukimpa nafasi mpya atakuwa mwadilifu?

Uzoefu peke yake hautoshi hadi uwe ni uzoefu wa kufuata sheria, taratibu na kufanya mambo kwa namna bora zaidi na kwa njia bora na yenye tija na ambayo hupimwa kwa matokeo bora zaidi. Nje ya hapo ni kufulia kiuongozi.

Tatizo siyo uzee na suluhisho siyo ujana!
Hapa ndipo napingana kwa asilimia 101 na Rais Kikwete. Tatizo la uongozi wa Tanzania sasa haliko kwenye umri wa wale wanaotuongoza. Na suluhisho lakesiyo kuwaondoa wazee na kutujazia vijana kwenye nafasi mbalimbali. Kama Rais Kikwete halipendi taifa letu na hatutakii mema kuanzia 2010 basi atujazie vijana kwenye nafasi za uongozi. Na katika hili hatuna shaka ni vijana wa aina gani atatuletea.

Watakuwa ni vijana kwa mfano wa kina Lawrence Masha, Emmanuel Nchimbi, William Ngeleja, Hussein Mwinyi, na wengineo! Na kama hawa ndio mfano wenyewe ambao Kikwete ameshatupatia basi tutafanya makosa hata kwa kumchagua yeye mwenyewe. Kama suluhisho ndio mfano wa "vijana" hawa basi tumekwisha. Kwani hawa vijana hadi hivi sasa wameonesha ni mfano gani wa kutatua matatizo yetu kwa sababu ya huo ujana wao? Katika maeneo yao ya kazi wamefanya nini kutuonesha uongozi hata wa kuonewa wivu? Si hawa ndio wanasimamia wizara nyeti za taifa hili? Mnafikiri kweli Rais Kikwete atateua watu tofauti na hawa? Kama ujana tu ndio suluhisho basi awajaze vijana kuanzia Ikulu (si tayari anao wengine pale wanaoumbua uongozi wake kila siku?)

Tatizo ni nini basi?
Ndugu zangu, tatizo tulilonalo katika uongozi wetu siyo ujana, elimu wala uzoefu; na tatizo letu siyo fedha au raslimali; tatizo letu ni uwezo. Tutaangalia hili wiki ijayo, inshallah.Niandikie: mwanakijiji@mwanakijiji.com
 
Big up, wa TZ kwa kuandika siasa tuko juu, laiti kungekuwa na zawadi ya kuandika na kuchmbua tungeongoza, lakini when it comes to real world of implementation, mmhhh!
 
< Uongozi ni zaidi ya hayo
ukiangalia utendaji katika maeneo mbalimbali na ukiangalia maamuzi ambayo yanachukuliwa katika nafasi mbalimbali kuanzia katika kijiji hadi kwenye lile "jumba jeupe la kale" pale magogoni unaweza kuona kuwa kuna tatizo kwa viongozi wetu.

Tatizo ni nini basi?
Ndugu zangu, tatizo tulilonalo katika uongozi wetu siyo ujana, elimu wala uzoefu; na tatizo letu siyo fedha au raslimali; tatizo letu ni uwezo. Tutaangalia hili wiki ijayo, inshallah.Niandikie: mwanakijiji@mwanakijiji.com

Mzee Mwanakijiji, bora useme wazi bila kujiuma uma maneno, make the long story short, tatizo ni kwenye lile "jumba jeupe la kale" pale magogoni!.Naelewa aliposema vijana, alimaanisha tutayarishe successive plan na mechanizim kwa wazee wapozeeka, wanakuwa wameandaa vijana kufuata nyanyo zao, sio hali ilivyo sasa, wazee ving'ang'anizi huku vijana ni maoportunist waborongaji. Hawa vijana wangeandaliwa mapema kwa kuwa groomed kuja kushika nafasi kubwa za uongozi, wangekuwa makini zaidi.Uingereza inawagroom royals wa kuja kuwa mfalme, Prince Charles ndiye the next in line, amelazimishwa kusoma Oxford japo kichwani mtupu, walimu mabingwa wamempiga tuturials, amegraduate, mpaka leo ukimuona anasmile fake na flat simply he is the next king!.Hiyo line up ya vijana waliopo lini walikuwa groomed zaidi ya kuwaokoteza washikaji na macheti yao ili mradi.Hebu mfuatilie Nape, msikilize kwa makini, huko aendako akipewa madaraka, is he likely to mess?. Hapana, vijana wa type hii, kina January type, Zitto type etc, ndio hao anaowazungumzia sio umri, 'age ain't nothing but a number'.Namalizia kwenye elimu, kuna kupata elimu na kuelimika, kupata elimu ni kupata fursa hiyo ya kuelimika mpaka ngazi za juu na kutunukiwa cheti, umekuwa umepata elimu. Kuelimika ni kuitumia elimu uliyoipata kwa manufaa yako na taifa lako. Kuna wengi wamepata elimu na hawajaelimika na kuna wengine hawakubahatika kupata elimu kwa viwango vya juu, lakini wameelimika, wengi wa viongozi wetu wakiongozwa na mkulu mwenyewe, wamepata elimu, lakini hakuna kitu humo, na uthibitisho ni hali halisi tuliyonayo sasa.(Samahani kwa bad format, natumia Windows NT 98!)
 
Tatizo la Tanzania kwa takribani miaka 20 iliyopita ni urais. Kwa maneno mengine sasa hivi ni kama hakuna rais, waziri mkuu naye ni muoga kama mtoto wa chekechea.

Angalia sasa hivi IPTL wamezima mitambo eti hawana mafuta, je, mjinga ngeleja anafanya nini? aliagiza mafuta kiduchu alafu akajua mitambo itaendeshwa kwa maji??

Kikwete aliahidi kupitia upya mikataba ya madini, ni nini kimefanyika??

Kikwete anatakiwa awafukuze kazi akina hosea, na awafukuze uanachama akina lowasa, chenge, karamagi, n.k. amefanya nini??

TRL, kuna mjinga mwingine Kawambwa, ni nini kinashindikana kufuta mkataba wa TRL na ukawapa masaa 24 wahindi wale wakaondoka?? Tuna kumbuka Gaddafi aliwafukuza wazungu kwenye visima vya mafuta na akawapa 24 hrs kuondoka nchini na wasiondoke na chochote isipo kuwa nguo zao.

Kingunge ameiibia serikali pale kituo kikuu cha mabasi kwa mkataba bomu, walio saini mkataba huo hawajafungwa jela, bado kingunge huyo huyo anapewa mkataba mwingine jengo la machinga complex, je, Pinda umelogwa na nani? mbona wewe ni mfipa nasikia huwezi kurogwa??

Mkuu mwanankijiji, tuna machungu mengi, nchi imekosa mwelekeo, je, tunajeshi la kutuongoza?? Lakini kama viongozi wenyewe ni akina Gen. Mboma......bora kutokuwa na rais.
 
Wa JF naomba pia kusaidiwa maana kila kukicha mnanifungua kama sii kwa jambo moja basi mawili. Nyerere ktk kinyanganyiro cha kumpitisha candidate wa urahisi ccm alitahadharisha kuwa kuna watu wameingia kwenye kinyanganyiro hicho na pesa ya bangi!! Na wakati huo walikuwa wamebaki washindani kama sikosei watatu. Je yaweza kuwa huu uendeshaji mbovu wa serikali kwa sasa na matusi yanayotolewa na viongozi wa serikali kitaifa yakawa matokeo na madhara ya pesa za bangi alizohofia Nyerere wakati ule??
 
Kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, kama nitajaliwa na nikapata bahati ya kuchaguliwa tena, nitahakikisha kuwa naubadilisha uongozi wa Tanzania kwa kuufanya uongozi wa vijana zaidi. Wale viongozi wa rika langu lazima waanze kuwaachia nafasi vijana - Rais Kikwete

Mwanakijiji,
Huyu JK wala hafai kupewa pole. Aliongea haya kwa ajili ya kufurahisha tu watu wa kundi fulani, (in this case vijana), ili kujipatia kura zao. Lakini sidhani kama hata yeye anaamini anachokisema.
  • Anajua wazi kuwa, akitaka kuteuliwa ndani ya CCM na pengine kwa kiasi fulani kuchaguliwa uraisi Tanzania in 2010, ni lazima apate msukumo wa vijana kwa sana.
  • Mwaka 1995 na 2005 alijinadi kama kijana, sasa mwakani akiwa na miaka 60 hawezi kutumia tena sifa ya ujana.
  • Kwa hiyo ili kuwachanganya vijana, inabidi aje na kauli mpya ya kuwavuta vijana, na ndio hili la ahadi ya uongozi kwa vijana likajitokeza.
  • Hebu fikiria UVCCM wakiahidiwa uongozi (ulaji) namna hii, si itabidi tu wawe upande wa JK? Huku ni kuwaloga vijana au tuiite rushwa ya uongozi kwa vijana.
  • Uongozi TZ una matatizo mengine lakini sio hili la umri. Kikwete amelitumia tu hili suala la umri kama rushwa kwa vijana.
  1. JK anatakiwa kushitakiwa kwa kuanza kampeni kabla ya wakati unaotakiwa
  2. Ashitakiwe kwa kutoa rushwa kwa vijana kwa njia ya ahadi za uongozi.
Someone should try this.
 
KJ, huoni kwamba kwa kufanya hivyo tutaichafua nchi na picha ya nchi yetu na tunaweza kusababisha matatizo kwa wananchi tukimshtaki Rais?
 
"Tatizo ni nini basi?
Ndugu zangu, tatizo tulilonalo katika uongozi wetu siyo ujana, elimu wala uzoefu; na tatizo letu siyo fedha au raslimali; tatizo letu ni uwezo." Tutaangalia hili wiki ijayo, inshallah.Niandikie: mwanakijiji@mwanakijiji.com


Mzee, ulipaswa kuongeza neno UZALENDO! Tatizo ni kwamba wanaweza kuwepo watu wenye uwezo wa kuongoza lakini kama hawana uzalendo ni sawa na sifuri tu! Kinachohitajika sasa ni viongozi wenye uchungu wa dhati kabisa na nchi yao.

Mwalimu aliwahi kusema kwamba kiongozi inabidi anapoona mateso ya wananchi basi mateso yale yawe yanamkera kweli kweli na kumkosesha usingizi.

Tunataka viongozi wanaokosa usingizi kwa kuwaza kuhusu wawekezaji wachimba migodi na jinsi watakavyoondoka na kutuachia mashimo bila kuambulia kile tunachostahili.

Siamini kwamba wanaopanda magari yenye viyoyozi ndani yake na kupita humo vijijini wanao uchungu na shida na dhiki za wananchi wenzao waliowapa dhamana ya uongozi. Tunataka viongozi ambao hata hayo magari ya viyoyozi wanayopanda watayaona nayo ni kero kwao maana wanatumia fedha za umma kujipa starehe wao wakati wananchi wengine wanakosa huduma muhimu za jamii ambazo wangeliweza kuzipata kama viongozi hao wangekuwa makini katika kuangalia vipaumbele vya mahitaji muhimu ya taifa.

Kwa kifupi, UZALENDO wa kujali mustakabali wa wananchi wote na maisha bora kwa wote!
 
Mzee, ulipaswa kuongeza neno UZALENDO!

Naamini kabisa UWEZO BILA UZALENDO haina maana, Unaweza kuwa na uwezo lakini ukakosa uzalendo wa kuilinda inchi na kuitetea nchi na wanachi.

Na ilikupata hawa Viongozi wazalendo lazima tuaandae strategies kwa kuweka Bases ya uzalendo kwa vijana wetu wangali wachanga kuanzia shule za awali na kuendelea lakini kwa mwendo tunaokwenda itabaki kuwa story.

Genge la wahuni wanaamka na kutaka raisi awe nani basi wana wanatumia fedha zao za Bangi then tunapata raisi.
 
Rais Kikwete mwenyewe alipewa nafasi ya kuwania urais 1995 kwa kiasi kikubwa kutokana na appeal yake ya "ujana".

Tunaona hii ndoto ya uongozi wa kileo kutoka kwa "kijana" Kikwete ulipotupeleka.
 
Tatizo kubwa la viongozi wetu wa Tanzania ni 1. kutokuwa na common sense 2. kukosa kuwa na utu / solemnity / morals 3. kutokuwa na long vision 4. kutokuwa competent to do they job 5. kutokuwa proud of their jobs6. kutokuwa na self determination to be the best 7. kutokuwa proud of themselves and they are families8. kutokuwa na uchu wa kucompete in international level9. kutokuwa na elimu, work experience na open mind10. kukosa kujua kwamba uongozi ni kutumikia wananchi sio wananchi kukutumikia wewe :)
 
Mzee, ulipaswa kuongeza neno UZALENDO! Tatizo ni kwamba wanaweza kuwepo watu wenye uwezo wa kuongoza lakini kama hawana uzalendo ni sawa na sifuri tu! Kinachohitajika sasa ni viongozi wenye uchungu wa dhati kabisa na nchi yao.

Mwanawane, umetimilisha hiyo makala.....tatizi ni UZALENDO, full stop!
 
Hakuna Uzalendo au nini........

Hiyo yote mnasema ni KUTIBU na dawa ni KUKINGA.

Chekecheo la kuchuja VIONGOZI wa Tanzania kwa kweli ni au halipo na kama lipo basi limewekwa la kupitisha "coarse aggregate" na wakati hapa tunahitaji "fine aggregate" kwa ajili ya kupigia lipu ukuta.

Sasa tukishajaza Mawe makubwa tunaanza kupiga lipu tunashindwa na hapo tunaanza kutafuta sababu za kushindwa?

Tatizo siyo MAWE ila tatizo ni CHEKECHEO. Na kibaya, hakuna kimtambo kinachoweza kuZIMA operations mara zikigundua chekecheo ni bovu. Wakati JKN yupo hai, Detectors ziliwagundua wafuatao:
1. Mwinyi ni DHAIFU na hafai kuwa Rais kwa third term.
2. Edward Lowassa ni MWIZI.
3. Prof. Kigoma Malima (nasikia) alikuwa mdini.
4. Saif Sharrif Hamad (hivi huyu alifanya nini?)
5. John Malecela alikuwa ni flip flap kwenye maswala ya Muungano/Utanganyika.

Nafikiri msululu ni Mkubwa. Ila walau tunafahamu sasa kuwa kama JKN angelikuwa hai, Mkapa asingelikuwa KIBAKA. Kikwete asingeliingia kuchaguliwa kuwa Rais, Malecela asingeligombea, Rostam Aziz asingeiingia ndani ya chama kiasi hicho nk nk.. Kazee kaliona mbali.
 
Hakuna Uzalendo au nini........
.

Haswa yaani hapo ndio ulipo mzizi wa mkuu wa matatizo....VIONGOZI WANA ELIMU, UWEZO, UZOEFU, UJUZI NK LAKINI HAWANA UZALENDO....Uongozi na madaraka ni biashara na njia murua ya kujiongezea kipato..
 
KJ, huoni kwamba kwa kufanya hivyo tutaichafua nchi na picha ya nchi yetu na tunaweza kusababisha matatizo kwa wananchi tukimshtaki Rais?

MMJJ,
Uongozi mbaya wa JK ndio matatizo yetu halisi kwa hivi sasa na wala sio ya kusingiziwa kama yale mengine. Kuichafua nchi sio issue maana tayari nchi inajulikana kuwa ina uongozi mbaya.

Issue hapa ni je tutakuwa na guts zaidi kidogo ya ile ya Qares ambaye angalau kaweza kusema maneno yasiyotamkwa ya kumtaka JK ang'atuke?

Tunatakiwa kuanza kuchukua hatua zinazofaa, iwe ni kisheria au kijamii (k.m. maandamano n.k.) ili kumshinikiza Kikwete aachie ngazi.

Tukifanikiwa awamu hii, anayefuata hatathubutu kutufanyia yanayoendelea.
 
Ndugu,

Wasomaji ni kweli sisi watanzania ni mahiri sana katika kuongea siasa,lakini katika kutekeleza malengo yetu ya maendeleo tuko nyuma sana.

Mimi ninasema tatizo la tanzania ni uongozi ambao watu wanaochaguliwa kushika nafasi mbalimbali wanachaguliwa kwa urafiki(nepotism and favouritism) hili ndilo tatizo kwa sababu hawako tayari kuwajibika kwa wananchi ambao ndio wapiga kura wao,na hata sheria wanazitunga bungeni ni kwa faida yao ili kenemesha mifuko yao,nenda hospitali ndipo unaona wagonjwa wamelala chini na dawa hakuna,lakini mbunge anatembelea "PRADO" ya milioni 80,je huu ni utawala bora,je hili linahijahi waziri wa afya awe na lundo la madigrii ambayo yanashindwa kuona kwamba wagonjwa kulala chini si sahihi,

Kwa hiyo tatizo la Tanzania ni kumomonyoka kwa maadili ya uongozi na kukiuka miiko ya uongozi,viongozi walioko madarakani ni wasanii,wabinafsi(egostic)

Tuchague viongozi wazalendo na sio hawa wasanii

Elisante Yona
 
Hatuna namna bora ya kuwapata viongozi. Wenye uwezo ndio wanawaweka viongozi wengi madarakani. Tunashangaa nini matokeo yakiwa mabaya? hata hii "deal" ya kuchukua vijana ngoja tuisubirie.Tunaweza shangaa wamejaa walewale opportunist ambao kwa issue sio kuongoza bali ni kuwa matajiri.
 
POLE RAIS KIKWETE, TATIZO LA VIONGOZI ULIONAO SIYO UMRI!
Na. M. M. Mwanakijiji

Tatizo ni nini basi?
Ndugu zangu, tatizo tulilonalo katika uongozi wetu siyo ujana, elimu wala uzoefu; na tatizo letu siyo fedha au raslimali; tatizo letu ni uwezo. Tutaangalia hili wiki ijayo, inshallah.Niandikie: mwanakijiji@mwanakijiji.com

Mkuu Mwanakijiji, nakubaliana na wewe kabisa katika tathmini yako kuhusu tatizo la Taifa letu na hususan mawazo ya Rais kuwa uzee ndilo moja ya tatizo tulilonalo.

Kwa mtazamo wangu, ni aibu kufikiria kuwa umri wa mtu ni tatizo linaloweza kuifikisha nchi hapa tulipo(labda kama mtu ameathirika na umri wake, kama mtu mwingine yeyote anavyoweza kuathirika na ugonjwa au sababu nyinginezo). Ni aibu zaidi kauli hiyo inapotolewa na mtu mwenye mamlaka makubwa zaidi kwenye Taifa kama Rais. Ni aibu kwasababu nyingi. Ila baadhi ni kama zifuatazo;
1. Inaondoa matumaini kabisa ya kupata uvumbuzi wa matatizo yetu
2. Inaonyesha dhahiri udanganyifu kwa nia ya kushinda uchaguzi
3. Inaonyesha dhahiri kuwa tunaodhani wanajua matatizo yetu, hawana habari nayo, au wameyasahau kabisa
4. Vipaumbele vya Taifa haviko bayana kwa viongozi tulionao.

Mhe. Rais anadhani na si ajabu anaamini kuwa kila mtanzania ana uchu wa madaraka, na njia ya kuweza kushinda (hata kama hafai) ni kutoa ahadi nyingi za ugawaji madaraka kwa kizazi chenye nguvu na ushawishi (vijana). Ni strategy ya hatari kama itakubalika kwa vijana wengi na kumfanya afanikiwe. Ni strategy inayoweza kuliangamiza kabisa Taifa.

Mkuu, kwa mtazamo wangu pia (niko tayari kusahihishwa) nina imani kuwa tatizo letu kubwa kabisa ni nchi kutokuwa na SYSTEM. Hakuna system ambazo zinategemeana ili kufanya mambo yafanyike na kuleta matokeo chanya. Hii ndio sababu pia kila uongozi unapobadilika nchini, kila kitu pia hubadilika. Mikakati hubadilika, mipango hubadilika n.k. Kwa ufupi, hakuna utaratibu maalum, wakitaalam, wenye uthibitisho wa mafanikio ambao unatumika katika uongozi wa nchi.

Pili, uoga wa viongozi kuanguka kisiasa: Viongozi wa kisiasa ndio viongozi wakuu kabisa katika nchi yetu. Na kama wote tunavyojua, viongozi hawa hupata nafasi zao kwa njia mbalimbali (nzuri na mbaya). Hivyo, kulinda mkate wao kisiasa ni ajenda muhimu kwao kuliko ajenda nyingine yoyote.

Viongozi hawa wanaweza hata kukana imani zao, familia zao na kila kitu walichonacho ili kuweza kujiimarisha kisiasa. Ifahamike kuwa, kujiimarisha kisiasa hakumaanishi sana kupendwa na wananchi.

Viongozi hawa wanaamini kuwa ni viongozi fulani kati yao ndio wenye uwezo wa kuwahakikishia kudumu kwao katika uongozi/siasa. Hivyo wako tayari kuwaunga mkono hata kama wanaamini kabisa kuwa watu hao si wema kwa Taifa. Haya ndio yanayoonekana katika utetezi wa mafisadi, Rais kushindwa kuamua, mikataba mibovu n.k.

Si kweli kuwa hawana uzoefu, au hawajui kazi zao au hawana uwezo wa kufanya mazuri kwa Taifa lao. Uwezo wanao, ila uoga wa kupoteza walichonacho kwa kupingana na wabadhilifu wachache ndicho kinachowashinda. Uoga pia wa kudhurika kisiasa (hadharani au kwa siri) na uoga wa uwezo walionao wezi wanaojificha kwenye siasa na kuwaongoza viongozi hao namna ya kufanya maamuzi na kutimiza wajibu wao. Uoga mkubwa wa watu serikalini unaiua nchi yetu.

Wakuu wa JF. Nchi hii haihitaji uzoefu uliopo sasa au unaoendelea kuongoza nchi kwa sasa. Nchi hii inahitaji kujikwamua kutokana na uzoefu uliopo ili iweze kupiga hatua walau kidogo. Viongozi wanaojisifia kuwa na uzoefu katika chama na serikali
(bila kubainisha uzoefu wao katika kuinua na kukuza maendeleo ya nchi) ni wakuogopwa kwa nguvu zote.

Uzoefu walionao ni wa hatari kwa kuwa ni wakulindana na kufichiana maovu yanayoipeleka nchi kwenye shimo la umasikini wa kukithiri. Nchi ikiendelea hivi itafikia mahali ambapo hakutakuwa na njia nyingine ya kuirekebisha zaidi ya kupunguza idadi yetu kwa nguvu. Nadhani mnaelewa maana yake. (REVOLUTION).
 
Haswa yaani hapo ndio ulipo mzizi wa mkuu wa matatizo....VIONGOZI WANA ELIMU, UWEZO, UZOEFU, UJUZI NK LAKINI HAWANA UZALENDO....Uongozi na madaraka ni biashara na njia murua ya kujiongezea kipato..

Mkuu Triplets, ni kweli kabisa.

Ila ni imani yangu kuwa uzalendo hauji wenyewe. Uzalendo katika nchi yetu uko chini sana, si kwa viongozi wetu pekee bali hata kwetu sisi wananchi.

Ninaamini kuwa Uzalendo unajengwa kutokana na imani, uaminifu na ushirikishwaji ambao mtu anakuwa ameshuhudia kutoka kwa utawala uliopo na jamii nzima.

Ukweli ni kuwa ubinafsi unamaliza kabisa uzalendo uliokuwepo. Kila mtu anajali maslahi yake na kudharau maslahi ya jamii nzima.

Watu wamepunguza sana ushirikiano na kuachia kila mtu kujikwamua kwa uwezo wake pekee. Mfano, mtu anakuta mwenzake akivamiwa, naye anaamua kupita mbali kabisa (hata kutazama hataki) na kuacha hadi mtu huyo anadhurika kabisa bila kutoa msaada wowote. Mfano mwingine, mtu anaona bomba la maji machafu likivuja njia nzima (tena ambapo watu na hasa watoto hupita na kucheza), hachukui hata hatua ya kusema kuna tatizo. Mfano mwingine ni hata katika uchaguzi, mtu anajua kabisa kuwa mgombea anaeomba kura yake hafai, badala ya kuchukua hatua, anaachia hadi mgombea huyo analaghai na kushinda uchaguzi huo (wakati mwingine bila kupingwa) na hata yeye mwenyewe kumpa kura yake.

Mkuu, Uzalendo hauji wenyewe, uzalendo huota na kukua kwenye mazingira yanayofaa ustawi wa uzalendo.

Vile vile, Uzalendo haulazimishwi wala hauombwi, bali ni zao natural litokanalo na ustaarabu wa jamii husika.
 
Back
Top Bottom