wakuu, picha hii inanipa mashaka kama ni halisi wana JamiiCheck naomba mnisaidie kujua uhalisia
- Tunachokijua
- Akili Unde (AI) ni seti ya teknolojia zinazoiwezesha kompyuta kutekeleza majukumu mbalimbali ya kina na kwa uwezo mkubwa kadri ya maelekezo ya mtumiaji, ikiwa ni pamoja na uwezo wa kuona, kuelewa na kutafsiri lugha inayozungumzwa na maandishi, kuchanganua data, kutengeneza picha na video na kutoa mapendekezo ya utatuzi wa matatizo mbalimbali.
Aidha teknolojia hii imekuwa muhimu katika kurahisisha ufanisi wa shughuli za kila siku na hii ni pindi tu inapotumika kwa nia iliyo njema, lakini inapotumiwa kwa nia ovu huweza kusababisha madhara makubwa kwa watu, mathalani uwepo wa taarifa potofu unachangiwa pia na teknolojia hii ambayo watu hutumia kutengeneza na kusambaza taarifa zisizo sahihi mfano picha, sauti, na video.
Katika kujenga uwezo wa kumuwezesha kila mmoja kutambua maudhui yaliyotengenezwa kwa teknolojia hiyo ili kuepuka upotoshaji kwa kutumia Picha inayomuonesha mwanaume aliyependa farasi ufuatao ni uchambuzi wa kina kuhusu uhalisia wake.
Uhalisia wa Picha
JamiiCheck imeijiridhisha kuwa Picha hiyo imetengenezwa kwa kutumia teknolojia ya akili unde. Kwanza picha hiyo inayo mapungufu kadhaa yanayodhihirisha kuwa ni ya kutengenezwa kwani hayarandani na uhalisia.
Sehemu ya mapungufu hayo ni pamoja na Kiganja cha mkono kinachoonekana kujikunja lakini hakioneshi uhalisia wa vidole vyake kuonekana vimejikunja. Mfano mtu akunjapo ngumi na kuegemea juu ya kitu, kidole cha mwisho huonekana kikiwa kimejikunja hali ambayo ni tofauti kwa picha hiyo.
Uwepo wa shanga shingoni ambazo hazina uwiano wa idadi katika ya upande mmoja na mwingine kuizunguka shingo. Upande wa ulio karibu na Mshale namba mbili unaonekana kuwa shanga nne, lakini upande wa pili shanga tano huku zingine zikiwa na muunganiko usio halisi.
Pia kwa kawaida kamba ambayo hutumika kuongoza farasi hutokea upande wa kichwa, lakini katika picha hiyo zinaonekana kutokea upande wa chini wa shingo na kuelekea kiunoni mwa mpanda farasi jambo lisilo la kawaida.