Penzi bila maumivu

Penzi bila maumivu

SEHEMU YA 68...
Hakutaka kuendelea kubaki chumbani mule, aliyaona majaribu yaliyokuwa yakiendelea, alichokifanya ni kuondoka zake huku akimuacha binti huyo akiwa kwenye muhemko mkubwa wa kufanya naye mapenzi.
Huo ukawa mwisho wa Dk.Buffet kuingia ndani ya chumba hicho usiku huo , hata Tatiana alipowaambia manesikwamba alitaka kumuona daktari huyo, alikataa kuonana naye kwa kujipa ubize na kwamba kama kumuona angemuona asubuhi.

Asubuhi ilipofika, Smith alikuwa hospitalini hapo, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumjulia hali mpenzi wake ambaye bado hakuonekana kuwa na furaha kabisa kwani mapenzi yake hayakuwa kwa mwanaume huyo hata kidogo, alianza kumpenda Dk. Buffet ambaye aliuteka moyo wake kwa kiwango kikubwa mno.

Smith alijaribu kujikesha kwa kumfanya mpenzi wake awe na furaha lakini hilo halikusaidia. Hakuingia hospitalini hapo mikono mitupu, alikuja na zawadi mbalimbali lakini bado Tatiana hakuonekana kuwa na furaha kabisa.
Baadae wakapokea maelekezo kwamba kila kitu kilikuwa tayari na Tatiana aliruhusiwa kuondoka hospitalini hapo. Hiyo haikuwa kawaida, mara zote mgonjwa anapotoka, mtu anayempa ruhusa kwa njia ya mdomo ni daktari mwenyewe ila siku hiyo, mtu aliyekuwa akiwapa taarifa alikuwa nesi ambaye aliagizwa na Dk. Buffet ambaye hakutaka kumuona kabisa Tatiana.
“Sawa, utamwambia kwamba ninashukuru sana,” alisema Simth.

“Hakuna tatizo, akija nitamwambia,” alisema nesi aliyetoa taarifa.
Walipoanza kutoka nje ya jengo la hospitali hiyo, tayari waandishi wa habari walikuwa wamekwishajikusanya na kuanza kuwapiga picha mfululizo. Jina la Tatiana lilikuwa kubwa na hatimaye hata Smith akaanza kujulikana sehemu mbalimbali duniani kupitia msichana huyo mrembo

Waandishi wengine walikuwa na vidaftari vidogo mikononi mwao, walitaka kumsikia Tatiana akizungumza kitu chochote kile kutokana na ule muujiza uliokuwa umetokea katika maisha yake. Hakuzungumza kitu, kwa kumwangalia tu alionekanakuwa na kitu kilichokuwa kikimtatiza moyoni mwake.
 
SEHEMU YA 69...
“Kuna nini? Mbona unaonekana hauna furaha?” aliuliza Smith.
“Nipo kawaida tu mpenzi,” alijibu Tatiana, hata hilo jina la mpenzi alilitamka tu ili mradi.
“Sawa. Zungumza chochote na waandishi.”

“Hapana! Kwa sasa sijisikii vizuri.”
Kila kitu kilichokuwa kikiendelea kilimshangaza sana Smith, hakutegemea kama angekutana na mabadiliko makubwa namna hiyo kutoka kwa mpenzi wake. Ni kweli alikuwa amepona na kuwa mzima kabisa lakini ni kitu gani kilichomfanya kuwa hivyo? Hakupata jibu lolote lile.

Kila kitu kilibadilika, hakuwa Tatiana yule aliyepita, huyu wa mara hii alikuwa tofauti kabisa. Bado Smith aliendelea kujiuliza labda kulikuwa na kitu kibaya alichokuwa amekifanya kwa mpenzi wake lakini alikosa jibu kabisa, hakuhisi kamakulikuwa na tatizo lolote lile, kila kitu kwake kilikuwa poa kabisa.

“Sasa kwa nini? Mbona amebadilika hivi?” alijiuliza Smith pasipo kupata jibu kwamba kwa kipindi hicho, mapenzi ya Tatina hayakuwa kwake kabisa, alichanganyikiwa na uzuri wa sura aliyokuwa nayo Dk. Buffet.
 
SEHEMU YA 70...
Umaarufu wa Tatiana ukazidi kuongezeka, duniani akawa gumzo kutokana na urembo aliokuwa nao na sauti nzuri aliyokuwa akiitumia kuimba. Baada ya kukutana na washauri wengi wakamwambia kwamba ingekuwa jambo jema kama angekuwa muimbaji ili aweze kuliteka soko la muziki kama Celine Dion kitu ambacho akakubaliana nacho moja kwa moja.

Alijua kwamba Mungu alimpa sauti nzuri kwa kuwa alitaka awe maarufu na tajiri kupitia sauti hiyo, hivyo akaanza kufanya kama alivyoshauriwa.
Kwa kuwa ndiyo kwanza alikuwa akianza, wimbo wake wa kwanza wenye mahadhi ya R&B haukuwa mzuri lakini sauti aliyokuwa akiitumia ndiyo ilikuwa balaa kabisa. Sauti ile ikawa chachu ya watu waliokuwa wakiusikia na kujikuta wakiupenda ghafla huku kwa wiki ya kwanza, tayari wimbo huo ukaanza kutikisa katika Chati za Billyboard.
Jina lake likaendelea kutikisa, alikuwa akiitwa huku na kule kwa ajili ya kufanya matamasha na wimbo wake huohuo mmoja. Smith alijisikia fahari, alijua kwamba kujulikana kwa mpenzi wake hata naye angejulikana sana tu, na hivyo ndivyo ilivyokuwa.

Kupitia mgongo wa Tatiana, naye akaanza kuitwa sehemu mbalimbali kwa ajili ya kutoa semina za biashara kwa kuwa tu alikuwa na PhD, hivyo watu wengi walimheshimu.
Siku zikaendelea kukatika, bado Tatiana aliendelea kubadilika, hakuwa kama alivyokuwa kipindi cha nyuma, alionekana tofauti sana na katika kipindi hicho alitaka kuonekana kama supastaa hivyo hata mavazi yake yalikuwa hivyohivyo, kama supastaa.

Maisha yake hayakutofautiana na Miley Cyrus, kama msichana huyo alivyokuwa akijiheshimu alivyokuwa akiigiza filamu mbali na kubadilika alipoanza kufanya muziki ndivyo ilivyokuwa kwa Tatiana.
Akasahau alipotoka, umaarufu ukamlevya, fedha alizokuwa akizipata, hakupasahau kule alipotoka, alikisaidia kijiji chake lakini kwenye kila kitu, alisahau kabisa kama aliwahi kukutana na mtu aliyeitwa kwa jina la Peter.
 
Huyo Tatiana mbwa kabisa, kaniudhi sana.. Mwisho wake lazima utakua mbaya!!!!!
 
SEHEMU YA 71...
Moyo wa Tatiana haukumsahau Dk. Buffet, mara kwa mara alikuwa akiwasiliana naye simuni na kumwambia hisia kali alizokuwa nazo juu yake. Kwa daktari huyo, hakutaka kukubaliana kuwa na msichana huyo, alikuwa msichana mzuri, alimpenda lakini hakuwa radhi kuwa naye kitu kilichomuuma mno Tatiana.

“What are afraid of?” (Unaogopa nini?) aliuliza Tatiana simuni.
“Smith is my friend, I can’t do such a thing,” (Smith ni rafiki yangu, siwezi kufanya kitu kama hicho) alisema Dk. Buffet.
“C’mon Smith, I will never let him know, please, make me happy papito,” (kamwe sitomjulisha, tafadhali, nipe furaha mpenzi) alisema Tatiana kwa sauti nyororo.

Hilo wala halikuweza kuubadilisha moyo wa Buffet, bado alikuwa akimwambia kwamba alikuwa akimuogopa Smith kwa kuwa alikuwa rafiki wake wa karibu mno hivyo asingeweza kufanya kitu kama hicho.
Ulipita mwaka mzima, Tatiana hakuwa amerudi nchini Tanzania, aliendelea kukaa nchini Marekani huku akiwa mwanamuziki mkubwa mwenye jina kubwa ambaye aliheshima kwa sauti yake nzuri aliyokuwa akiitumia.

Mwaka uliofuata, akaamua kutoa wimbo wa pili aliouita kwa jina la That’s Why Am happy. Mashairi ya wimbo huo yalimlenga zaidi Buffet, alimwambia ukweli kwamba alikuwa akimpenda, hata kama alimkataa lakini kitendo cha kuchati naye simuni, kuzungumza naye kilimpa furaha.
Wimbo ukamuongezea mashabiki wengi zaidi, akazidi kupendwa na kuingiza kiasi kikubwa cha fedha. Tatiana yule aliyekuwa akiishi katika maisha ya kimasikini, leo hii alikuwa bilionea mkubwa, sauti yake ikabadilisha maisha yake kwa ujumla.

Mbali na sauti yake, pia hata uzuri wake ulikuwa gumzo kubwa nchini Marekani. Watu walimpigia sana kura na kuchaguliwa kuwa mwanamke mwenye sura nzuri kuliko wanawake wote duniani ambao walikuwa maarufu.
 
SEHEMU YA 72...
Kutokana na uzuri wa sura yake, akasainia mikataba mikubwa na majarida mbalimbali likiwemo Forbes kwa ajili ya kupiga picha kwa ajili ya kupamba majarida hayo katika kurasa za mbele. Akaunti ilisoma fedha tu, fedha hazikukauka, kila siku ziliendelea kuingia zaidi na mpaka anatimiza mwaka mmoja na nusu, tayari alikuwa na kiasi cha dola milioni mia tano katika akaunti yake (zaidi ya trilioni moja) kitu kilichomfanya kuona kwamba aliyapatia maisha, kungekuwa na nini tena huko mbele? Alijiona kumaliza kila kitu alichokuwa akikihitaji, sasa akajipanga kummwaga Smith kwani hakuona faida yake kwake zaidi ya kulitumia jina lake kujipatia fedha na umaarufu wa bure pasipo kufanya kazi yoyote ile. Kiburi kikamjaa Tatiana.

***** “I want you to tell me the truth,” (Ninataka uniambia ukweli) ilisikika sauti ndani ya nyumba ya kifahari alilonunua Tatiana.
“What truth?” (Ukweli gani?)
“Do you love me or not?” (Unanipenda au haunipendi?)
“Why do you ask me such a question?” (Kwa nini unaniuliza swali hilo)
“I want to know, tell me, do you?” (Ninataka kujua, niambie, unanipenda?) Smith alikuwa amechoka, mambo aliyokuwa akifanyiwa na Tatiana yalimchosha na hakutaka kabisa kuona yakiendelea, dalili zote kwamba penzi lao lilikuwa likienda mlama zilionekana na hivyo alichotaka kujua kwa wakati huo ni kwamba alikuwa akipendwa au la.

Alichoka, hakutaka kuona akiumia zaidi, mambo aliyokuwa akiyafanya msichana huyo yalimuumiza mno. Kuna kipindi, wao kama wapenzi wanapolala kitandani kufanya mapenzi ni jambo la kawaida, lakini kwa kipindi hicho, Tatiana hakutaka kusikia kabisa suala la kufanya mapenzi.
Alipokuwa akishikwa kiuno, aliutoa mkono wa Smith, alipokuwa akishikwa kitovu chake, hakutaka kabisa hicho kitokee, hivyo alisogea pembani na kusema kwamba alichoka na hakuwa akijisikia kabisa.

Smith alimpenda mno msichana huyo kiasi ikawa ngumu kwake kumsaliti, ni kweli kulikuwa na wasichana wengi waliokuwa wakimpenda lakini kwa Tatiana ni kama alikuwa amepigwa upofu, hakusikia lolotelile zaidi ya kila siku kumwambia kwamba alikuwa akimpenda mno.
 
SEHEMU YA 73...
Tatiana akavimba kichwa, alijua fika kwamba piga ua, Smith angekuwa analalamika sana lakini asingeweza kumuacha kwa kuwa alimpenda sana. Maumivu ya moyo wa Smith yaliendelea kila kila siku, kuna kipindi alikuwa akikaa chini na kujuta kumsaidia msichana huyo kwa kuamini kwamba yale matibabu yaliyoyafanya macho yake kuona ndiyo yaliyopeleka kuwa katika hali hiyo kipindi hicho.

“Kwa nini unanigeuka?” aliuliza Smith, alikuwa na hasira mno, alihisi kama muda wowote ule angeweza kumpiga Tatiana.
“Nimekugeuka, nimefanya nini?”
“Mapenzi yako yapo wapi?”
“Mapenzi gani?”
“Tatiana, hivi haujui tulipotoka kweli? Umeasahau kila kitu mpenzi?” aliuliza Smith, kadiri alivyokuwa akiongea na hasira zake zilizidi kuongezeka.
“Bwana eeee unanipigia kelele,” alisema Tatiana, akavuta blanketi na kujifunika.
Smith aliona Tatiana akimpanda kichwani, huku hasira zikiwa zimemkaba kooni, akamvuta Tatiana upande wake na kuanza kumwangalia usoni. Mishipa ilimsimama, alionekana kuwa na hasira mithili ya simba aliyechukuliwa mtoto wake.

“Unanijibu nini wewe malaya?” aliuliza Smith, alikuwa amekasirika mno.
“Nani malaya, wewe mpumbavu nini.”
Smith akashindwa kuvumilia, pasipo kutegemea akaanza kumpiga Tatiana kipingo kikubwa kilicholifanya blanketi kutapakaa damu kutokana na kupasuliwa mdomo. Tatiana alikuwa akilia tu, akashindwa kuvumilia kwani aliona kwamba endapo angeendelea kubaki mahali hapo basi mwanaume huyo angeweza kumuua, hivyo akakimbia.
Siku iliyofuata, tayari taarifa zikasambaa kwa kasi ajabu kwamba Smith alimpiga Tatiana nusura kumuua. Hiyo ndiyo ilikuwa taarifa iliyozagaa sana kipindi hicho. Wanawake wakaungana na kuanza kuandamana huku wakilalamikia kile kilichokuwa kimetokea kwamba Tatiana hakutakiwa kupigwa na hivyo waliitaka mahakama kuingilia kati na Smith kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.

Smith hakutaka kuzungumza kitu chochote, aliwaacha watu waongee wanavyotaka lakini kamwe hakutaka kuzungumza lolote lile kwa kuona kwamba asingeweza kuaminika hata mara moja.
Si nchini Marekani tu ambapo maandamano yalitokea bali hata katika baadhi ya nchi za Kiafrika ikiwemo Tanzania wanawake walijikusanya mitaani na kuanza kulaani kile kilichokuwa kimetokea.
 
SEHEMU YA 74...
Wote hao hakukuwa na mtu aliyejua ukweli kwamba msichana Tatiana alikuwa amebadilika na hakuwa na shukrani, kwao, Smith alionekana kuwa mwanaume mbaya kitu ambacho hakikuwa kweli kabisa.
Alichokiamua Tatiana na kumuita mwanasheria wake na kesi kufikishwa mahakamani. Dunia nzima ikatega sikio lake katika kesi hiyo, bado Tatiana alionekana kuwa na sababu kubwa ya kumshitaki Smith kwa kile kilichokuwa kimetokea.

“Nitahakikisha mpaka anafungwa,” alisema Tatiana, alikuwa akiwaambia marafiki zake katika kipindi alichokuwa kwenye Kisiwa cha Hawaii wakila maisha.
“Tena ni bora iwe hivyo, wamezidi kutunyanyasa, haiwezekani akupige bila sababu,” alisema mmoja wa marafiki zake.
Kesi haikuchelewa, ikaanza kunguruma mara moja. Bado Smith hakuzungumza kitu chochote kile, alichokifanya ni kuomba msamaha kwa kila kilichokuwa kimetokea. Alijua kwamba Tatiana alikuwa supastaa hivyo kama angeamua kusema kile kilichokuwa kimetokea basi inawezekana angelichafua jina lake, hivyo hakutaka kufanya hivyo.
Katika kipindi cha miezi sita chote watu walikuwa wakifuatilia kile kilichokuwa kikiendelea mahakamani na mwisho wa siku mahakama kuamua kumuadhibu Smith kwa kufanya kazi za jamii kwa masaa elfu mbili, pia akae mbali na Tatiana kwa zaidi ya kilometa kumi, asimpigie simu wala kumtumia ujumbe wowote ule, uwe simuni au kupitia kwa mtu fulani kwa kipindi cha miaka miwili.
Kwa Smith hiyo ilikuwa adhabu kali mno, kuwa mbali na Tatiana kilikuwa kitu ambacho hakuzoea kabisa kukiona hivyo aliamini kwamba maisha yake yangekuwa na matatizo mno, lakini hakukata rufaa, kile kilichoamuliwa na mahakama, akikacha hivyovhiyo na kuanza kufanya adhabu yake.

“Ila kwa nini ulimpiga?” aliuliza bwana Warren.
“Ni matatizo ya kimapenzi.”
“Kivipi?”
“Tatiana amebadilika sana baba.”
“Haiwezekani, amekuwaje?”
“Ni mbaya sana, huwezi amini. Sijutii kumpiga hata mara moja,” alisema Smith na kuanza kuwahadhithia wazazi wake kile kilichokuwa kimetokea.
Kila mmoja alibaki kimya akimsikiliza Smith, maneno aliyokuwa akizungumza yalimsikitisha kila mtu aliyekuwa mahali hapo, hawakuamini kama msichana Tatiana angeweza kufanya vile vyote ambavyo Smith alikuwa akihadithia.
 
SEHEMU YA 75...
Huo ndiyo ulikuwa ukweli, Smith hakupunguza neno wala kuongeza neno, kila kitu alichokuwa amekihadithi kilikuwa sahihi kabisa kwamba msichana huyo alikuwa amebadilika kwa asilimia mia moja.
Tatiana akawa huru, kitendo cha kuachana na Smith kilimpa nafasi kubwa ya kuishi kama alivyokuwa akitaka,. Alikulia katika maisha ya dini, alikwenda sana kanisani na hata kuimba kwaya lakini mara baada ya kupata fedha na umaarufu, kila kitu kikabadilika, Tatiana yule wa kipindi cha nyuma hakuwa huyu.
Akajifunza kunywa pombe kwani ndiyo aliamini kwamba kilikuwa kitu pekee alichokuwa amekibakiza katika maisha yake. Kadiri maisha yalicyokuwa yakisonga mbele, Tatiana aliendelea kuharibikiwa zaidi kiasi kwamba akasahau alipotoka.

“Tatiana,” aliita rafiki yake, alikuwa amelewa mno.
“Unasemaje?”
“Naomba niendeshe gari.”
“Hapana! Nitaendesha mimi, gari hii ni yangu,” alisema Tatiana.
“Hapana! Haiwezekani kuendesha na wakati umelewa,” alisema rafiki yake huyo.
Hiyo ilikuwa ni usiku wa saa saba, walikuwa wanatoka katika Klabu ya Casanova iliyokuwa katikati ya Jiji la New York. Siku hiyo Tatiana alikuwa amekunywa pombe nyingi, alilewa chakari huku akiwapa nafasi wanaume kushika maungo yake.

Japokuwa alikuwa amekunywa kiasi kikubwa cha pombe, bado alihitaji kuendesha gari kitu kilichokataliwa na rafiki yake huyo. Huku akibisha, Tatiana akaingia garini, rafiki yake hakuwa na jinsi, naye akaingia na kuanza kuondoka mahali hapo huku watu wakiwaangalia kwani hapo nje bado kulikuwa na wengi waliokuwa wakimpiga picha.
“Puuuuuuuu......!!” ulisikika mlipuko mkubwa wa bomu, watu wakshtuka, wengine wakaanza kukimbia huku na kule, gari alilokuwa amepanda Tatiana likalipuka na kuanza kuteketezwa kwa moto.

Sauti za wasichana wawili zikaanza kusikika wakipiga kelele, moto mkubwa ulikuwa ukiliteketeza gari lile jambo lililowafanya watu wengi kushtuka, hawakuelewa kile kilichokuwa kimetokea, badala ya kuanza mishemishe ya kuuzima moto ule, walibaki wakiangalia kwa mshangao mkubwa huku kelele za Tatiana na rafiki yake zikiendelea kusikika ndani ya gari hilo.
 
SEHEMU YA 76...
Kwa jina aliitwa Kashmovic Petrov, alikuwa Mrusi aliyekuwa akiishi sana barani Afrika. Alikuwa mwanaume mwenye mwili mkubwa uliojengeka kimazoezi, alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa na roho mbaya ambaye baadaye akafukuzwa kwa kuwa alitaka kuipindua serikali tawala.
Kwa kumwangalia Petrov, alionekana kuwa kijana mpole, msikivu lakini alikuwa makini wa kazi zake. Katika kipindi ambacho Urusi ilikuwa ikifanya mapinduzi mwaka 1917, babu yake Petrov ndiye alikuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba mtawala Nicolus II anaachia ngazi na hivyo nchi kutoka katika utawala wa Kifalme na kuondoa ubepari.
Ilikuwa kazi kubwa lakini mwisho wa siku walifanikiwa. Huku akionekana kuwa mwanaume mwenye nguvu, babu yake Petrov akafanikiwa kumuoa mwanamke aliyeitwa Juliana na hatimaye kupata watoto huku mmojawapo akiwa Udzoniv, baba yake Petrov.

Kiubavu, Petrov alikuwa amerithi kutoka kwa babu yake. Baada ya kukulia katika maisha ya kijeshijeshi na utemi mkubwa mitaani ndipo baba yake alipoamua kumpeleka katika jeshi la Urusi ambapo huko akapambana sana mpaka kupata nyota tatu.
Mwili wake uliendelea kujengeka sana, alijulikana karibu kambi zote za kijeshi nchini Urusi, aliwekwa katika kitengo nyeti cha upelelezi kwa ajili ya kufuatilia mbinu mbalimbali zilizokuwa zikifanywa na Wamarekani, baadae walipomuona kwamba aliifanya kazi kwa utaalamu mkubwa, wakamhamisha na kumuweka katika jeshi la maji.

Mbali na kila kitu alichokuwa nacho, Petrov alikuwa akitisha sana katika kutengeneza mabomu. Alikuwa mtaalamu mkubwa ambaye aliheshimika sana jeshini kiasi kwamba asilimia sabini ya mabomu yaliyokuwa yakitengenezwa nchini Urusi, yeye ndiye aliyekuwa akiagiza yatengenezwe vipi.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, hakutoka jeshini lakini baada ya kulitumikia jeshi hilo kwa miaka kumi, akaamua kuigeuka hasa kwa kupanga mikakati ya kuipindua nchi hiyo. Serikali ililigundua hilo na hatimaye kumkamata, hawakutaka kumuua, walichokifanya ni kumfukuza nchini Urusi.
 
SEHEMU YA 77...
Baada ya kufukuzwa, hakwenda sehemu yoyote ile barani Asia, bali alichokifanya ni kukimbia na kukimbilia barani Afrika na kwenda nchini Liberia ambapo akaungana na rais Charles Taylor na kuendelea na maisha yake kama kawaida pasipo watu kufahamu.
Ingawa baadaye rais huyo alikamatwa kwa makosa tofautitofauti, Petrov akabaki na jeshi kubwa na kuendelea kulipa mafunzo kwani bado walikuwa wakiihitaji nchi hiyo.
“I want to see Petrov,” (Ninataka kumuona Petrov) alisema Nathan, alikuwa amesimama mbele ya wanajeshi wa waasi.
“What is your problem?” (Una tatizo gani?)

Nathan hakutaka kusema kile alichokuwa akikihitaji zaidi ya kuomba kuonana na Petrov tu. Ilikuwa ni kazi kubwa, haikuwa kazi nyepesi hata mara moja kuonana na mtu huyo lakini kwa sababu aliomba sana na pia alijulikana kutokana na utajiri mkubwa wa baba yake, akaruhusiwa kuonana naye.
“Kuna nini?”
“Nataka unisaidie,” alisema Nathan huku akionekana kuhitaji msaada wa hali na mali.
“Nikusaidie nini?”
“Kuna mtu nataka afe.”
“Nani?”
“Unamfahamu huyu Tatiana?”
“Yupi huyo?”
“Huyu mwanamuziki anayetamba sasa hivi?”
“Namsikiasikia, amefanya nini?”
“Ninataka umuue, tena kwa kumlipua na bomu,” alisema Nathan.
“Anaishi wapi?”

“Marekani, ila kumpata siyo tatizo. Nitagharamia kila kitu,” alisema Nathan.
Alionekana kuwa na hasira na Tatiana, kwa kile alichokuwa amemfanyia kwa kuamua kuwa na mtu mwingine kilimuumiza mno, hakutaka kuona msichana huyo akiendelea kuishi kwa kuwa aliuumiza mno moyo wake.
Hiyo wala haikuwa kazi kubwa kwa Petrov, alichokifanya ni kuhitaji kiasi cha dola lefu ishirini ambazo ni zaidi ya milioni arobaini kwa ajili ya kufanya kazi hiyo tu. Hilo wala halikuwa tatizo kwa Nathan, alichokuwa akikitaka ni kuona kazi inafanyika, hilo tu.

Baada ya wiki moja, akawasilisha malipo yake na moja kwa moja Petrov kuanza kazi ya kuingia nchini Marekani kwa kutumia meli kubwa ya mizigo iliyokuwa ikimilikiwa na Wagiriki. Hakuhofia maisha yake, kile alichokuwa akikihitaji kwa wakati huo ni kukamilisha kazi aliyokuwa amepewa, hivyo alilazimika kwenda kuifanya kwa mikono yake.
 
SEHEMU YA 78...
Baada ya kufika jijini New York huku akipewa hifadhi na rafiki yake mmoja, huyo ndiye aliyemfadhili kila kitu kuanzia maladhi, usafiri na mambo mengine. Hata pale ambapo Petrov alipokuwa akihitaji vifaa kwa ajili ya kutengeneza bomu, rafiki yake huyo ndiye alikuwa akihusika.
*****
Petrov alifika mapema sana katika Klabu ya Casanova, akalipaki gari lake pembeni na kuanza kusikilizia muda ambao msichana Tatiana angeingia ndani ya eneo la klabu hiyo. Bomu lake lilikuwa ndani ya gari, aliliweka vizuri na alikuwa amekwishaliseti lilipuke mara baada ya uzito kuwa mkubwa gari wakati gari likianza safari.

Alitulia hapo kwa zaidi ya masaa mawili huku wakati mwingine akihisi kama alidanganywa kwamba Tatiana angekuwepo katika klabu hiyo. Aliendelea kukaa garini, ilipofika majira ya saa tatu usiku, akaliona gari aina ya Hammer likianza kuingia ndani ya eneo hilo, kwa jinsi gari lile lilivyoonekana kuwa la kifahari, akahisi kwamba huyo alikuwa Tatiana.
Hakutaka kuteremka garini, alitaka kuwa na uhakika kwamba mtu huyo alikuwa Tatiana au la. Gari liliposimamishwa, mlango ukafunguliwa na Tatiana kuteremka akiwa na rafiki yake. Petrov akatoa tabasamu pana, hakuamini kama kazi yake ingekuwa rahisi namna ile.
Alichokifanya ni kuwasuburi mpaka waondoke na kuelekea ndani. Kila kitu alichokuwa akikitaka mahali hapo kikafanyika, hivyo akaanza kulisogelea gari lile, akaangalia huku na kule, alipoona hakukuwa na mtu aliyekuwa akimuona, akainama chini, akaingia uvunguni na kulitegesha bomu lile kisha kuondoka zake.
******

Kelele ziliendelea kusikika mahali hapo, gari lilizidi kuteketea huku watu wote wakiwa wamepigwa na butwaa wasijue la kufanya. Baada ya sekunde kadhaa, watu wawili waliokuwa na mashine za extinguisher wakalisogelea gari lile na kuanza kuliupulizia hewa lile na hatimaye moto ule kuzima.
 
SEHEMU YA 79...
Hiyo ikaonekana kuwa nafuu, moto ukazimika na kuufungua mlango ule. Bahati mbaya, rafiki yake Tatiana alikuwa ameteketezwa na moto na hakuwa akihema, alifariki palepale garini. Hilo likawatia wasiwasi kwamba inawezekana hata Tatiana naye akawa amekufa lakini walipomgusa, alishtuka huku akikohoa mfululizo kutokana na moshi mzito.
“Vipi?” aliuliza jamaa mmoja.
“Hata hajajeruhiwa,” alisema jamaa mwingine.

Hawakutaka kupoteza muda, walichokifanya ni kumchukua na kisha kumpeleka hospitalini huku mwili wa rafiki yake ukitolewa garini na kuwekwa chini, kila mtu aliyeuona, alijikuta akibubujikwa na machozi, picha iliyoonekana ilimuumiza kila mtu.
Kutokana na matatizo makubwa yaliyokuwepo baina ya Smith na Tatiana, kila mmoja akajua kwamba kwa kila kitu kilichokuwa kikiendelea, Smith alikuwa akihusika nacho.
**** Taarifa za habari, mitandao ya kijamii, kote huko wakawa wakitangaza juu ya kile kilichokuwa kimetokea, mwanamuziki aliyelishikilia soko la muziki duniani, Tatiana alilipuliwa na bomu akiwa ndani ya gari lake.

Zilikuwa taarifa zenye kushtua sana, kila aliyezisikia, hakuamini kama kweli kitu kile kiliuwa kimetokea hivyo kuanza kuelekea katika Hospitali ya St. Mariana Medical Center ili kwenda kujionea kwa macho yao.
Taarifa ambazo hazikuthibitika zilisema kwamba Tatiana alikufa kwenye mlipuko huo kitu kilicholeta huzuni kubwa kwa kila mtu aliyezisikia, lawama zote juu ya mlipuko hizo zikaenda kwa Smith kwani ndiye mtu aliyekuwa na uhasama mkubwa na msichana huyo.

Watu wakachukulia kile kama kisasi kwamba Smith alitaka kulipiza kwa kile alichofanyiwa na msichana huyo ambaye alionekana kuwa mtu asiyekuwa na hatia yoyote ile na hivyo watu kuanza kuishinikiza Serikali ya Marekani imkamate Smith na kumfunga jela kwa kile kilichokuwa kimetokea.

Hakukuwa na mtu aliyefahamu mengi kuhusu Tatiana, alionekana msichana mwema asiyekuwa na tatizo lolote lile, alipendwa na kila mtu, sauti yake nzuri ilimpagawisha kila mtu kiasi kwamba kuna wakati watu walifikiri kwamba msichana huyo alishushwa kutoka Mbinguni.
 
SEHEMU YA 80...
“Huyu ni Smith tu, yeye ndiye aliyefanya mpango huu,” alisema mwanaume mmoja, alionekana kuwa na hasira mno, alikuwa amevalia fulana iliyokuwa na picha ya Tatiana.
“Huo ndiyo ukweli! Nahisi alichukia sana alipopelekwa mahakamani, yeye ndiye aliyefanya hivi, lazima serikali iingilie kati,” alisikika mwanamke mmoja.

Watu waliamini kwamba Smith ndiye aliyefanya mpango wa kulilipua gari lile kutokana na kile kilichokuwa kimetokea katika maisha yao ya nyuma. Magazeti, pasipo kupata ufumbuzi wowote ule waliandika kwamba kulikuwa na madai mengi kwamba mwanaume huyo ndiye aliyesababisha mlipuko huo.
Smith hakuzungumza kitu, alisoma kila kitu kilichokuwa kikiandikwa lakini aliamua kubaki kimya kwa sababu alijua fika kwamba si yeye aliyefanya jambo hilo, zaidi sana, akaelekea nchini Hispania kwa ajili ya mapumziko.

Tatiana alifikishwa ndani ya Hospitali ya Mariana akiwa hoi, moshi ulimfanya kuwa kwenye hali mbaya kiasi kwamba hata kupumua kwake kulikuwa kwa shida sana. Mapafu yalijaza moshi mwingi uliomfanya madaktari kumchukua na kumpeleka katika chumba maalumu kwa ajili ya matibabu.
Kila mtu aliyeuona mwili wa rafiki yake Tatiana kwa jinsi ulivyoteketea, alimuona mwanamuziki huyo kuwa na bahati kubwa mno kwani kuungua kwa rafiki yake na kufariki huku yeye akiwa mzima wa afya ilionekana bahati kubwa sana.
Ndani ya saa moja tangu mlipuko huo utokee, tayari watu zaidi ya elfu tano walikuwa wamekwishakusanyika nje ya hospitali hiyo kwa ajili ya kumuona msichana huyo ambaye aliendelea kuwa gumzo kila kona duniani.

Wengi walihuzunika, tetesi zilizokuwa zikisikika mitandaoni kwamba binti huyo alikuwa amefariki dunia zilimhuzunisha kila mtu, wengine wakashindwa kuvumilia hivyo wakajikuta wakibubujikwa na machozi.
“Anaendeleaje?” aliuliza Buffet alipokuwa amekwenda hospitalini hapo.
“Anaendelea vizuri tu, ingawa moshi ulijaa sana kwenye mapafu yake,” alijibu daktari aliyekuwa akimshughulikia Tatiana.

“Kwa hiyo yupo salama sasa hivi?”
“Ndiyo! Tunamshukuru Mungu.”
“Na huyo mwenzake?”
“Aliyekuwa naye alifariki hapohapo, ni Mungu tu mpaka msichana huyo kuwa mzima,” alisema daktari huyo.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom