SEHEMU YA 63...
Magazeti na vyombo vingine vya habari viliendelea kuripoti kila hatua aliyokuwa akipitia Tatiana, kila mtu alitamani kuona msichana huyo akipata nguvu ya kuona ili ajue ni kwa jinsi gani ulimwengu ulikuwa ukiendelea.
Baada ya matibabu kufanyika kwa mwezi mzima, hatimaye Tatiana akaanza kuona vivulivivuli. Mtu alipokuwa akipita mbele yake, hakuwa akimuona vizuri kitu kilichomfanya kuhisi kwamba alikuwa akienda kupona.
“Vipi?” aliuliza Dk. Buffet.
“Naona vivulivivuli,” alijibu.
“Haya ni maendeleo makubwa sana, amini kwamba utakwenda kupona kabisa,” alisema Dk. Buffet.
Maendeleo yake yalimfurahisha kila mmoja, baada ya wiki mbili kukatika, Tatiana akafanikiwa kuona kabisa, upofu aliokuwa nao tangu alipozaliwa, ukakoma na mishipa yake kukaza na kuwa kama mtu ambaye hakuwahi kuumwa macho maishani mwake.
“Dokta! Naona,” alisema Tatiana huku akionekana kutokuamini.
“Unasemaje?”
“Naona dokta! Naona,” alisema Tatiana.
“Hebu subiri, hivi vidole vingapi?” aliuliza Dr. Buffet.
“Vinne.”
“Na hivi?”
“Viwili, naona dokta,” alisema Tatiana huku akipiga kelele kwa furaha.
Hiyo ilikuwa taarifa njema kwa kila mtu, hakukuwa na aliyekuwa akiamini kile kilichokuwa kimetokea, hapohapo alichokifanya Dk. Buffet ni kuchukua simu yake na kumpigia Smith akimtaka afike hospitalini hapo kwani mpenzi wake alifanikiwa kupona ugonjwa ule.
“Nakuja,” alisikika Smith na kukata simu.
Tatiana hakulala tena, akasimama na kuanza kuzunguka chumbani mule, kila alichokuwa akikifanya, madaktari walikuwa wakimwangalia, huku nyuso zao zikiwa na furaha tele, hawakuamini kama msichana huyo alifanikiwa kuona kama watu wengine.
Kila wakati Tatiana alikuwa akimshukuru Mungu kwa kumpa uwezo wa kuona. Kuna wakati alikuwa akirukaruka kwa furaha, wakati mwingine alikuwa akikimbia humohumo chumbani, yaani vyote hivyo alikuwa akivifanya huku akiwa kwenye furaha tele.
Ndani ya nusu saa tu Smith akafika hospitalini hapo, moyo wake ulikuwa na furaha tele, hakuamini kile alichokuwa amekisikia kwamba mpenzi wake alikuwa amepona na kuona kama kawaida. “Nimekuja...”
“Kufanya nini?”
“Kumuona mpenzi wangu! Kumbe amepona,” alisema Smith, alikuwa akizungumza na dada wa mapokezi.