Penzi bila maumivu

Penzi bila maumivu

SEHEMU YA 122...
Hakukuwa na mtu aliyemuona, na hata wale waliomuona, hawakuwa wakihusika chochote kile na hospitali hiyo hivyo hawakujishughulisha naye kabisa. Huku akiwa ameufikia mlango wa kuingia ndani, mara akashtuka kusikia akiitwa.
“You!! Where you go?” (Unakwenda wapi?) aliuliza mlinzi kwa Kingereza kibovu.

“I’ve gota patient in here,” (Nina mgonjwa humu) alijibu Nathan.
“You no go there, this is not entering,” (Usiende huko, hii si sehemu ya kuingilia) alisema mlinzi huyo huku akiendelea kuiharibu lugha hiyo pasipo kujali chochote kile.

Hicho ndicho alichotaka kukifahamu mahali hapo, alitaka kufahamu ni ulinzi wa aina gani ulikuwepo. Alichokifanya mara baada ya kuambiwa kutoka kule ni kurudi na kuelekea kule kulipokuwa na watu wengi ambao walikuwa wakisubiri ruhusa ya daktari kuingia hospitalini.
“Hamuwezi kuingia wote, wengine bakini, zamu kwa zamu,” alisema daktari mmoja, alikuwa akiwaambia watu zaidi ya mia nne waliokuwa wamekusanyika mbele yake.

Watu wakagawanywa, wengine walitakiwa kuingia ndani lakini wengine walitakiwa kubaki kwani walikuwa wengi mno, hivyo wangeingia zamu kwa zamu. Hilo halikuwa tatizo, walichokuwa wakikitaka ni kuingia ndani tu na kumuona msichana huyo aliyekuwa akiteseka kitandani.
Ndani ya hospitali hiyo, madaktari walikuwa wamejitahidi sana kumtibu Tatiana kiasi kwamba kikafika kipindi wakaona kwamba walifikia mwisho. Walitumia ujuzi wao wote, kidogo Tatiana akaanza kuonyesha nafuu, yaani kile kidonda alichokuwa nacho kikaanza kukauka hali iliyoonyesha kwamba muda wowote ule msichana yule angeweza kurudiwa na fahamu.

“Kidogo kuna nafuu,” alisema Dk. Mandesh na kisha kuwashukuru madaktari wenzake kwa kazi kubwa waliyokuwa wameifanya mpaka hatua ile ya kidonda kile kuanza kukauka.
Buffet hakuwa na cha kushukuru zaidi, kama ni maneno ya shukrani, alihakikishia anawapa kila siku kwani kwa jinsi alivyowaona madaktari wale, walikuwa na kazi kubwa ya kuhakikisha kwamba mgonjwa yule akipona. Kuna wakati walikataa kula, walikataa kupumzika kwa ajili ya Tatiana kitu ambacho kwa Buffet kilionekana kuwa zaidi ya kujitolea, hivyo shukrani hazikumuisha mdomoni mwake.
 
SEHEMU YA 123...
Baada ya kuandaliwa vizuri kwa ajili ya watu kumuona Tatiana, wakaruhusiwa kuingia zamu kwa zamu katika chumba kimoja kilichokuwa kimetwngwa ghorofani kabisa na hakukuhitajika kelele za aina yoyote ile.
Kila mtu aliyeingia ndani ya chumba kile, hakuruhusiwa kuingia na viatu vyake, alitakiwa kuviacha mlangoni ambapo hapo walipewa viatu vingine ambavyo hata kama ungetembea vipi, usingeweza kusababisha kelele zozote zile.

Kila mtu aliyemuona Tatiana kitandani pale, alibaki akilia, hakuamini kile alichokuwa akikiona. Msichana mrembo, mwanamuziki aliyejizolea umaarufu mkubwa alikuwa kitandani kimya kabisa.
“She is too young to die,” (Ni mdogo mno kufa) alisikika mwanamke mmoja ambaye alishindwa kuyazuia machozi yake kububujika mashavuni mwake.

Miongoni mwa watu walioingia ndani ya chumba kile alikuwemo Nathan ambaye baada ya kumuona Tatiana kitandani pale, hakuwa kama watu wengine, hakuwa na huzuni hata kidogo tena wakati mwingine alijiona akishikwa na hamu ya kumsogelea msichana yule kitandani pale na kumuua, bado kile alichofanyiwa kipindi cha nyuma kilizidi kuutafuta moyo wake.

“I will kill this bitch by mtyself,” (Nitamuua huyu malaya mimi mwenyewe,” (Alijisemea Nathan huku akiyapitisha macho yake usoni mwa msichana huyo.
Ulinzi ulikuwa wa kutosha mahali hapo, mbali na polisi waliokuwa nje ya mlango wa chumba hicho, pia wengine walikuwa ndani kuhakikisha kila kitu kinakwenda salama. Taarifa za kuchomwa kisu kwa msichana huyo zilijulikana kila kona duniani hivyo waliamini kwamba piga ua ilikuwa ni lazima wauaji wasafiri kuelekea hiko India kwa ajili ya kummaliza palepale kitandani.

Alipomaliza kumwangalia Tatiana, hakutaka kukaa sana, hakutaka kuzoeleka sana hivyo alichokifanya ni kuondoka hospitalini hapo. Alipofika hotelini, akajilaza kitandani, hasira kali ilimkaba kooni mwake, hakumpenda kabisa Tatiana na alimchukia zaidi ya alivyomchukia shetani.
Hakurudi tena hospitalini, alichokifanya ni kukaa hotelini kwa siku mbili kisha siku iliyofuata, akaanza kufanya mchakato wa kutafuta namna vitambulisho vya madaktari hospitalini pale vilivyokuwa.
 
SEHEMU YA 124...
Hilo wala haikumpa shida kwani ndani ya masaa matatu tu, tayari kila kitu kilikuwa kimekamilika na ni safari ya kwenda huko tu ndiyo ambayo alikuwa akiisubiri.
Siku ya kufanya tukio ilipofika, akaondoka hotelini huku akiwa na kibegi kidogo mgongoni. Hakukuwa na mtu aliyemtilia shaka hasa alipoingia hospitalini kwa kuwa alionekana kama watu wengine ambao walifika hospitalini hapo kwa ajili ya kuwaletea vyakula wagonjwa wao.

Wakati alipokuwa akienda huko, hakutaka kwenda mchana, alikwenda usiku kwani alihofia macho ya watu wengi waliokuwa mchana katika siku aliyokuja na ndiyo maana aliamua kuja usiku ambapo aliamini pia hakukuwa na watu wengi.
Alipoingia ndani, kitu cha kwanza alichokifanya ni kwenda chooni ambapo huko, kwa haraka sana akavaa koti kubwa, akachukua mashine ya stetoscope, akaining’iniza shingon, akachukua mafaili yake, akayashikilia mkononi, akachukua sindano iliyokuwa na sumu ya Mephromethomphy ambayo hutumika kuulia wadudu msituni, sumu iliyokuwa na nguvu kubwa ya kuua kwa kipindi kifupi hasa inapoingia katika mshipa wa damu wa binadamu, ilikuwa moja ya sumu ambayo haikutakiwa kuuzwa kipindi hicho, hata Nathan aliipata kimagumashi. “Hapa nina uhakika sitoweza kugundulika,” alisema Nathan huku akivaa miwani ya macho hali iliyomfanya hata muonekano wake kubadilika. Mbali na hivyo, akakipachika kitambulisho upande wake wa kushoto kilichoonyesha jina la Dr. Stephen Show. Akawa na uhakika wa kuingia chumbani, hivyo akaanza kuelekea huko huku akijiamini.
 
SEHEMU YA 125

Ilikuwa ngumu mno kugundua kwamba mtu aliyekuwa akija mbele yao hakuwa daktari. Nathan alitembea kwa kujiamini huku kila wakati akiangalia mafaili yake hali iliyowafanya polisi wote kuona kwamba mtu huyo alikuwa daktari kweli.
Alitembea kwa kujiamini, miwani yake, mavazi na ile mashine aliyokuwa ameining’iniza shingoni iliwafanya polisi wote kuwa na uhakika kwamba Nathan alikuwa daktari.

Alitembea mpaka alipofika katika mlango wa chumba kile, hakusimama, japokuwa polisi walitamani kumsimamisha lakini wakajikuta wakipuuzia na hivyo kumruhusu kuingia ndani ya chumba kile.
Hiyo ilikuwa nafasi nzuri kwa Nathan, hakuamini kama angeruhusiwa kirahisi namna ile, akakishika kitasa na kisha kuingia ndani huku akionekana kuwa mwenye furaha kubwa kwa kuwa aliona hiyo ndiyo nafasi ya kukamilisha kile alichotaka kukifanya.
“Karibu daktari...” alisikia akikaribishwa ndani ya chumba hicho, akageuka nyuma na macho yake kutua kwa Buffet aliyekuwa pembeni mwa kitanda cha Tatiana.

“Asante sana, anaendeleaje?” aliuliza Nathan huku akiiweka vizuri miwani yake.
“Kidogo hali yake inaonekana kuwa nzuri japokuwa bado hajarudiwa na fahamu,” alisema Buffet huku akisogea pembeni.
Alichokifanya Nathan ni kutoa sindano katika koti lake na kumtaka Buffet aondoke ndani ya chumba kile ili aendelee na kazi yake. Kwa mbali Buffet alionyesha mshtuko lakini akajipa moyo kwamba hakukuwa na tatizo lolote lile.
Hata kabla hajatoka ndani ya chumba hicho akaanza kujiuliza maswali kuhusu bomba la sindano ile kwamba ilikuwaje daktari mkubwa kama yule, tena ndani ya hospitali kubwa namna ile kuja na kutoa bomba la sindano katika koti lake?
Yeye mwenyewe alikuwa daktari lakini kitu kama kile hakikuwa kikikubalika kabisa, sindano ilitakiwa itolewe kutoka kwenye boksi lake na ndipo daktari achukue dawa na kumchoma mgonjwa, kile kilichoendelea, hakikuonekana kuwa sahihi.

“Vipi?” aliuliza Nathan huku akimwangalia Buffet usoni.
“Daktari....”
“Nenda nje niendelee na kazi yangu...” alisema Nathan huku akimkazia macho Buffet, akajitahidi kuonyesha tabasamu pana.
 
SEHEMU YA 126

Japokuwa moyo wake haukumtuma kwenda nje lakini hakuwa na jinsi, alijua ni kwa namna gani madaktari walikuwa bize hasa anapokuwa mgonjwa ambaye ana tatizo kubwa, alichokifanya ni kutii tu kwani hakukuwa na kitu kingine zaidi ya hicho.

Buffet akakaa katika benchi kubwa la chumba lililowekwa nje, kichwa chake kilikuwa na mawazo mengi na alikuwa akijiuliza maswali mengi juu ya kile kilichokuwa kimetokea, huku akiwa kwenye mawazo hayo, ghafla akatokea Dk. Mandesh ambaye uso wake ulionyesha tabasamu kwa mbali.

“Mbona upo hapa?” aliuliza Dk. Mandesh.
“Kuna daktari anamhudumia mgonjwa.”
“Kuna daktari anamhudumia mgonjwa?” aliuliza Dk. Mandesh huku akionekana kushtuka.
“Ndiyo!”
“Daktari gani?”
“Simjui.”
Ni kama Dk. Mandesh akashtuka kitu fulani, alichokifanya ni kuugsogelea mlango ule na kisha kutaka kuufungua, mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani. Daktari huyo akaanza kupigha hodi huku akihitaji kufunguliwa lakini mlango haukufunguliwa.

Polisi waliokuwa pembeni ambao walipewa jukumu la kulinda chumba kile wakasogea kule alipokuwa Dk. Mandesh na Buffet kutaka kujua kitu gani kilikuwa kikiendelea mahali hapo.
“Kuna nini dokta?” aliuliza mlinzi mmoja.
“Ni nani aliingia humu?” aliuliza Dk. Mandesh.
“Kuna daktari mmoja hivi.”
“Yupi?”
“Kiukweli simjui, ila ni daktari.”
“Hapana! Huyo atakuwa si daktari. Hakuna daktari anayeruhusiwa kuingia humu zaidi ya wale tuliokuja kabla,” alisema Dk. Mandesh.

Kila mmoja akashtuka, maneno aliyoyaongea daktari yule yalimshtua kila mmoja na kugundua kwamba kulikuwa na tatizo limetokea hivyo nao kuanza kuugonga mlango ule uliokuwa umefungwa kwa ndani.
“Vipi?”
“Mlango haufunguki. Mungu wangu! Ni nani tena?” aliuliza Dk. Mandesh huku akionekana kushangaa.

Wazo moja tu ndiyo lililowajia vichwani mwao kwamba watumie mlango wa nyuma ya chumba kile. Hawakutaka kusubiri, huku kila mmoja akionekana kuchanganyikiwa, wakaanza kukimbia kuelekea kwenye upande wa pili wa chumba kile.
 
SEHEMU YA 127

Walipofika huko, mlango haukuwa umefungwa, ulikuwa wazi kabisa, wakaingia moja kwa moja ndani. Picha waliyoiona kitandani pale iliwashtua mno. Tatiana alikuwa akirusha miguu yake huku na kule, mapovu mazito yalikuwa yakimtoka mdomoni kama mtu aliyekuwa akikaribia kukata roho.

Kila mmoja akachanganyikiwa, Buffet hakuweza kuvumilia kuiangalia picha ile, akajikuta akipiga magoti na kuanza kulia. Mtu aliyesemekana kuwa daktari ambaye aliingia ndani ya chumba kile aliharibu kila kitu, hapo wakagundua kwamba mtu huyo hakuwa daktari kama alivyuokuwa bali alikuwa muuaji ambaye alitaka kumuua Tatiana.
“Naomba uokoe maisha yake! Naomba uokoe maisha yake,” alisema Buffet huku akilia.

Alikuwa daktari mzoefu tena aliyeaminika sana nchini Marekani lakini ndani ya chumba hicho, kwa jinsi alivyokuwa amechanganyikiwa, akasahau kabisa kwamba hata naye alikuwa daktari hivyo suala la kumtibu mtu lingewezekana kwa asilimia mia moja.
Alichokifanya Dk. Mandesh hata kabla ya kumtibu Tatiana, akalichukua bomba la sindano lililokuwa chini na kulinusa ili aweze kujua lilikuwa na sumu aina gani kwani aliamini kwamba sumu iliyokuwemo ndani ya bomba lile la sindano ndiyo iliyotumika kumchoma Tatiana.

“Mungu wangu! Mephromethomphy!” alisema Dk. Mandesh huku Tatiana akiendelea kukukuruka kitandani pale, alikuwa akikaribia kukata roho.
****
Bado moyo wake ulikuwa na hasira mno, alikunja ndita usoni mwake huku akimwangalia Tatiana kitandani pale, hakumpenda hata kidogo na hata aliposhika lile bomba la sindano, alidhamiria kumchoma msichana huyo na kisha kuondoka kwa kuamini kwamba msichana yule angekufa kwani sumu ile ilikuwa na nguvu mno.

Alichokifanya kabla ya kufanya chochote kile ni kuufuata mlango na kisha kuufunga kwa kutumia kiloki kidogo kilichokuwa kwenye kitasa kisha kumrudia Tatiana kitandani pale na kuanza kumwangalia tena.
 
SEHEMU YA 128

Kwa jinsi hasira kali zilivyokuwa zimemkaba kooni mwake, akashindwa kuvumilia, hapohapo akajikuta akianza kulia kwa uchungu. Machozi yakabubujika mashavuni mwake kwani kitendo cha kumuona msichana yule mahali pale, tayari kumbukumbu zake zikaanza kurudi nyuma kama mkanda wa filamu, hivyo hakuona jinsi zaidi ya kumuua tu.
Akaingiza mkono wake katika mfuko wa pili wa koti lake na kisha kutoa chupa ndogo iliyokuwa na sumu ile ya

Mephromethomphy, akachukua sindano ile na kisha kuchoma katika kikopo kile kisha kuivuta sumu ile.
“Ni lazima ufe malaya mkubwa,” alisema Nathan huku akiwa na hasira mno.
Huku akiwa na hasira zilizomkaba kooni, hapohapo akaanza kusikia mtu akigonga mlango na kutaka kuingia ndani. Tayari akaona kwamba kama asingefanya kile kilichokuwa kimemleta ndani basi angeweza kukamatwa kirahisi, alichokifanya ni kumchoma Tatiana sindano ile.

Msichana huyo akaanza kubadilika kitandani pale, akaanza kurusha miguu na mikono yake huku na kule, mapovu yakaanza kumtoka mdomoni, hali ile iliyokuwa ikitokea, ilimfurahisha mno Nathan.
“Bora ufe malaya mkubwa, haya ndiyo matunda ya usaliti wako,” alisema Nathan huku akionekana kuwa mwenye hasira kubwa. Alichokifanya mara baada ya kuona Tatiana akiwa kwenye hali ile ni kuondoka kupitia mlango wa nyuma huku akiwa na uhakika kwamba msichana huyo angefariki dunia.

“Bora nimekamilisha kazi,” alisema Nathan huku akiwa kwenye mwendo wa kasi kuelekea nje ya jengo la hospitali ile.
Japokuwa alikuwa akitembea kwa harakaharakla na kuonekana mgeni machoni mwa walinzi waliokuwa wakirandaranda huku na kule lakini hakukuwa na mtu aliyemsimamisha na kumuuliza kwani muonekano wake tu aliokuwa nao ulionyesha kwamba alikuwa daktari, hivyo watu wakampisha pasipo kujua kwamba mtu huyo alikuwa muuaji.
 
Sehemu ya 129

Sumu ya Mephromethomphy ilizidi kumuweka kwenye hali mbaya, Tatiana aliendelea kurusha miguu na mikono yake huku na kule na mapovu yakimtoka kwa wingi mdomoni. Dk. Mandesh akachanganyikiwa, sumu ile iliyokuwa imeingia katika mishipa ya damu ya Tatiana ilikuwa hatari sana na ingeweza kumuua wakati wowote ule.
“Nipe Cyclomethius...” alisema Dk. Mandesh.

Cyclomethius ilikuwa dawa yenye nguvu ya kuondoa sumu mwilini mwa mwanadamu hasa katika damu yake. Kwa haraka sana Buffet akachukua chupa iliyokuwa na dawa hiyo na kisha kumpa Dk. Mandesh ambaye akachoma sindano katika chupa ile na kisha kuivuta dawa ile kwa kutumia sindano na kumchoma Tatiana kitandani pale.

Kila mmoja kwa wakati huo alikuwa akimuomba Mungu juu ya hali ya msichana huyo kwani kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele na ndivyo alivyozidi kurusharusha mikono na miguu yake huku na kule.
Huku wakiendelea kumhudumia Tatiana, madaktari wengine wakafika nje ya mlango ule ambapo walipogonga, ukafunguliwa na kisha kuingia. Hali waliyoikuta hata wao iliwashangaza mno kwani hawakutegemea kuona kitu kama hicho kikitokea.

“Kuna nini?” aliuliza daktari mmoja miongoni mwa watatu walioingia chumbani humo.
“Kuna mtu alikuja kumchoma sindano yenye sumu.”
“Nani?”
“Hata mimi simjui. Hawa wanasema kwamba ni daktari.” Alisema Dk. Mandesh huku akiisikilizia hali ya Tatiana mara baada ya kumchoma sindano ile.
Taarifa zikaanza kutolewa kwamba kulikuwa na mtu aliyeingia hospitalini hapo na kujifanya daktari huku akiwa na lengo la kumuua Tatiana. Kila aliyezisikia taarifa zile alishtuka, bila juhudi kubwa iliyofanywa na Dk. Mandesh basi msichana Tatiana angeweza kufariki dunia.

Kila mtu akashangaa na kuona kwamba ulinzi wa hospitali hiyo ulikuwa mdogo mno kiasi kwamba kulikuwa na mtu ambaye aliingia huku akiwa na lengo la kumuua Tatiana. Watu wakaanza kutoa maoni yao kwamba Tatiana alitakiwa kuhamishwa hospitalini hapo na kupelekwa katika hospitali nyingine ili kuyaokoa maisha yake.
“Haitowezekana kuhamishwa,” alisema daktari mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Rajiv.
 
Sehemu ya 130

“Na kwa nini hamkuweka ulinzi wa kutosha hospitalini hapa?” aliuliza mwandishi wa habari.
“Ulinzi upo wa kutosha, na ukitaka kuamini, baadae njoo kwa lengo la kufanya mambo yako uone,” alisema Dk. Rajiv huku akionekana kukasirika kutokana na maswali aliyokuwa akiulizwa.
“Na Tatiana anaendeleaje?”
“Sijui.”

Dk. Rajiv hakutaka kuendelea kuhojiwa, alishikwa na hasira mno kwani maswali ya mwandishi yule hakuona kama alitakiwa kuulizwa kwa kuwa yalionyesha udhaifu mkubwa wa hospitali yake.
Kwa kuwa hospitali hiyo ilikuwa na kamera ndogo za CCTV, walichokifanya ni kwenda kuangalia ili kumuona huyo mtu ambaye aliingia ndani ya hospitali hiyo kwa lengo la kumuua Tatiana. Hilo wala halikuwa tatizo hata kidogo, wataalamu wa IT wakafanya kazi yao na mwisho wa siku Nathan kuonekana akitembea kwa kujiamini mpaka katika chumba kile.
“Chukueni picha yake, anahitajika sana,” alisema Dk. Rajiv na vijana wale wa IT kufanya hivyo.

Hicho ndicho kilichofanyika, picha ya Nathan ikachukuliwa, wakaziprinti na kisha kuwapa walinzi na baadhi ya madaktari huku wakiwaambia kwamba ilikuwa ni lazima suala hilo libaki na kuwa siri kwani walijua kwamba mara muuaji huyo atakaposikia kwamba Tatiana hakufariki, lazima angerudi tena.
Masaa yaliendelea kukatika, hali ya Tatiana ikaanza kurudi katika hali ya kawaida kama aliyokuwa nayo kabla ya kuwekewa sumu ile. Mapigo yake ya moyo yakarudi kawaida japokuwa bado hakurudiwa na fahamu.

Pongezi zote zilikwenda kwa Dk. Mandesh ambaye ndiye aliyehakikisha kwamba mgonjwa wake anapatiwa matibabu ya nguvu na hatimaye kuwa kama zamani.
Maswali yakaanza kuulizwa juu ya sababu iliyowafanya watu kutaka kumuua Tatiana.

Hawakujua tatizo lilikuwa nini mpaka msichana huyo kutaka kuuawa mara tatu, mara ya kwanza ilikuwa nchini Marekani ambapo gari lake lililipouliwa kwa bomu, mara ya pili nchini Tanzania alipochomwa kisu na mara ya tatu kuwa hapo nchini India.
 
Sehemu ya 131

Kila mmoja akaona kwamba kulikuwa na tatizo nyuma ya pazia, kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea ambacho hakukuwa na mtu yeyote yule aliyefahamu zaidi ya Tatiana na watu waliotaka kumuua. Wengi walimuonea huruma kwani walijua kwamba hizo zilikuwa hujuma kutoka kwa watu wengine ambao hawakutaka kuona maendeleo ya msichana huyo.

Hakukuwa na aliyefahamu kuhusu usaliti wa mapenzi aliokuwa ameufanya, wanaume wawili walitaka kumuua kwa kuwa tu aliwasaliti kitu kilichowafanya kuwa na hasira mno dhidi yake. “Ila zitakuwa fitina tu,” alisikika jamaa mmoja aliyekuwa ameshika Gazeti la Ijumaa.
“Ila hata mimi nahisi hivyo! Jamaniiiii...mbona wanataka kutuulia mtu wetu? Mbona wana wivu sana hawa watu?” aliuliza mwanamke mmoja, alionekana kuwa kwenye mapenzi ya dhati kwa Tatiana.

Tanzania hakukukalika, kila mtu alikuwa akimzungumzia Tatiana aliyeonekana kuwa na bahati mbaya kutokana na yale yaliyokuwa yakitokea, kuna wakati walihisi kwamba bado mpenzi wake wa zamani, Smith alikuwa akimwandama, alitaka kumuua kutokana na kile kilichokuwa kimetokea, kuachwa solemba na kuamua kuwa na mwanaume mwingine.
Kila mmoja aliandika maoni yake katika mitandao ya kijamii, hisia zao kali ndizo zilizoonyesha kwamba ni kwa kiasi gani walikuwa wakimpenda Tatiana ambaye alikuwa na sura ya upole, inawezekana kuliko watu wote duniani.
“Kwani anaendeleaje?”
“Kwani gazeti wameandikaje?”
“Kwamba yupo salama sasa hivi! Hivi ni kweli au wanataka kutupoza tu?”
“Inawezekana ikawa kweli,” alisema mwanamke mmoja.

Watu wengi wakaanza kumuombea uzima Tatiana, hali yake bado haikuwa imetengemaa na kuna watu waliendelea kumtafuta ili wamuue. Mpaka kufikia hatua hiyo, tayari wakajua kwamba msichana huyo alitakiwa kupewa ulinzi mkubwa ili yasimkute balaa aliyokuwa akitaka kukutana nayo.

Hospitalini hapo, ulinzi ukaongezwa zaidi, kile kilichotokea kilionekana kuwa kosa kubwa mno hivyo walitaka kuhakikisha kwamba kila kitu kinakuwa salama. Polisi waliokuwa na bunduki zaidi ya watano walikuwepo nje ya chumba kile.
 
Sehemu ya 132

Akaingia ndani ya jengo hilo, walinzi na polisi wote waliokuwa hospitalini hapo, hakukuwa hata na mmoja aliyekuwa na habari naye jambo lililompa urahasi mno kupita na kuelekea kule kilipokuwa chumba kile.

Alipofika katika korido iliyokuwa na chumba kile, alipotoa kitambulisho na kuwaonyesha kwamba alikuwa mfanyakazi kutoka katika Shirika la Habari la CNN, hakukuwa na polisi yeyote yule aliyemuuliza maswali zaidi, wakamuuliza shida yake ambapo akawaeleza kwamba alitaka kumuona Tatiana na kumpiga picha ili wafuasi wake wapate kujua hali yake ilikuwaje kipindi hicho.

“Hakuna tatizo, karibu sana mwandishi, huwa tunaziheshimu sana kazi zenu, hasa nyie CNN na BBC, ila kama wangekuwa waandishi wengine, tusingekuruhusu,” alisema polisi mmoja huku akitoa tabasamu pana.

Ugumu ambao aliufikiria Nathan kipindi cha nyuma haukuwepo hata mara moja. Akaruhusiwa na kuanza kuufuata mlango wa kuingia ndani ya chumba kile. Alipofika humo, alijua kwamba Buffet angekuwemo chumbani humo lakini kitu cha ajabu, mwanaume huyo hakuwepo hivyo kumsogelea Tatiana pale kitandani alipokuwa amelala, na hapohapo akafungua zipu ya begi lake alilobebea kamera na kutoa kisu kilichokuwa na ncha kali, akajiandaa kumuua Tatiana kitandani pale.
 
SEHEMU YA 133

Ulinzi imara ulikuwa umeimarishwa, kila polisi aliyekuwemo ndani ya hospitali hiyo alikuwa na picha ya Nathan hivyo isingekuwa na ugumu wowote ule kumgundua katika kipindi alichokuwa akifika hospitalini hapo na kujifanya mwandishi wa habari kutoka CNN.
Walimgundua mapema sana na taarifa zikatolewa haraka kwamba hawakutakiwa kuonyesha ishara zozote zile za kumshtua, walitakiwa kumuonyeshea upendo wote huku hata Buffet akiambiwa kwamba hakutakiwa kukaa karibu na chumba kile.

Hali ambayo alionyeshewa ikampa uhakika kwamba hakugundulika hivyo kutokuwa na wasiwasi kabisa, akajua kwamba iwe isiwe ni lazima kufanya mauaji kama alivyokuwa amepanga.
Taarifa zikapelekwa mpaka ndani ya hospitali ile, Dk. Rajiv akapewa taarifa kwamba yule muuaji alikuwa amefika hospitalini hapo, na wakati huu hakujifanya daktari bali alijifanya kuwa mwandishi wa habari kutoka CNN.
Hiyo ndiyo ilikuwa nafasi pekee ya kujitangaza duniani kwamba ulinzi wao ulikuwa imara na hata mara ya kwanza kile kilichokuwa kimetokea, kilitokea kwa bahati mbaya tu, hivyo akawaambia baadhi ya polisi waingie ndani ya chumba alichokuwa Tatiana na wajifiche huku wakimsikilizia yule muuaji.

“Pia kumbukeni kutokumuonyesha tofauti zozote zile,” alisema Dk. Rajiv.
Hakutaka kuendelea kufanya kazi zake, akabaki akisikilizia kile kilichokuwa kikiendelea. Moyoni alimuomba Mungu aweze kufanya kama kile alichotaka kukifanya, muuaji akamatwe na hatimaye afikishwe mbele ya sheria.
Nathan alikishikilia kisu mkononi mwake, alisimama umbali wa kama hatua nne kutoka kilipokuwa kitanda cha Tatiana. Kila alipokuwa akimwangalia msichana huyo kitandani pale, hasira zilimshika zaidi, hakupenda kumuona akiendelea kupumua hata kama alikuwa kwenye hali ya mateso makali namna ile.

Hata kabla hajaanza kupiga hatua kumsogelea zaidi, ghafla akasikia watu wakitoka nyuma ya kabati la kuwekea dawa walipokuwa wamejificha,walikuwa polisi wenye bunduki mikononi mwao, Nathan akapigwa na mshtuko mkubwa, watu wenye bunduki walisimama mbele yake, bunduki zikiwa zimemuelekezea yeye huku akiwa na kisu mkononi mwake.
“Upo chini ya ulinzi,” alisema polisi mmoja.
“Nyanyua mikono juu,” alisema polisi mwingine.
 
SEHEMU YA 134

Walijua kwamba Nathan alikuwa na kisu mkononi mwake, walichokifanya ni kumuwahi na kisha kumlaza chini kwani walijua kwamba endapo wasingefanya hivyo basi kwa kasi ya ajabu angeweza kumchoma kisu msichana huyo hapo kitandani.

“Niacheni nimuueeee...niacheni nimuueeee malaya huyu...” alisema Nathan huku akiwa amelazwa chini.
“Hebu nyamaza huko.”
“Niacheniiii...ameniumiza sana mpumbavu huyuuuu....”
Hakukuwa na aliyemsikiliza, kelele zile alizokuwa akizipiga ndizo zilizowafanya polisi waliokuwa nje kujua kwamba tayari kile walichokuwa wamekipanga kilifanikiwa, walichokifanya ni kuingia ndani ya chumba kile huku wakitangulizana na Buffet aliyekuwa akimwangalia Nathan kwa macho ya chuki mno.

Japokuwa alikuwa akizungumza maneno mengi lakini hakuweza kuachiwa, alibebwa mzobemzobe na kupelekwa nje ya chumba kile huku Buffet ambaye hakuongea kitu chochote kile akibaki chumbani mule huku akimwangalia mpenzi wake, Tatiana.
Kule alipopelekwa, Nathan aliwekwa katika chumba kimoja kilichokuwa na giza totoro, kilionekana kama stoo ambapo kulikuwa na harufu kali ya madawa kitu kilichoonekana kuwa mateso makubwa ambayo hakuwahi kuyapata maishani mwake.

Alibaki chumbani humo usiku mzima, hakukuwa na mtu aliyeshughulika naye chochote kile, alifungiwa na madaktari kuendelea na shughuli zao huku pale nje wakimuacha polisi mmoja aliyeendelea kulinda huku akiwa na bunduki mkononi mwake.

Walichokifanya, hawakutaka kumpeleka kituoni wakati huo, walijua kwamba endapo angekwenda kituoni wasingeweza kumpata tena hivyo nao walichukua nafasi hiyo kumpa mateso na ndipo baadae achukuliwe na kupelekwa katika kituo kikubwa cha polisi.

“Get me out of here...” (Nitoeni humu) alipiga kelele Nathan lakini hakukuwa na mtu yeyote aliyejali, bado giza na idadi kubwa ya mbu iliendelea kumtesa chumbani mule.

Nathan aliendelea kuwa na hasira mno, hakuamini kama alishindwa kutekeleza kile alichokuwa amekipanga mwanzo, alijikuta akilia tu chumbani humo kwani hasira kali alizokuwa nazo juu ya Tatiana zilimkaba kooni.
 
SEHEMU YA 135

Siku iliyofuata, mlango ukafunguliwa, polisi wanne waliokuwa na bunduki wakaingia chumbani humo na kisha kumchukua huku nje ya chumba hicho wakibaki polisi wawili. Nathan alionekana kuwa kama gaidi mkubwa aliyetakiwa kuwekewa ulinzi wa uhakika kwani vinginevyo angeweza kutoroka.

“Kuweni makini, ndiye huyohuyo aliyelipua gari kule Marekani,” alisema polisi mmoja, wenzake wote wakashikilia vizuri bunduki zao.
Taarifa zilikuwa zimezagaa kila kona kwamba yule mtu aliyetaka kumuua Tatiana siku mbili zilizopita alikuwa amekamatwa na hivyo alikuwa akipelekwa polisi kwa ajili ya mahojiani kisha kupelekwa mahakamani ambapo angeshtakiwa kwa kosa la kukusudia kuua.

Waandishi wa habari hawakutaka kukaa mbali, kwa kuwa walizipata taarifa hizo tangu usiku, hivyo asubuhi na mapema walikuwepo hospitalini hapo kwa ajili ya kupiga picha kila kitu ambacho kingeendelea kwa mtuhumiwa yule.
Wakati Nathan akitolewa ndani ya hospitali ile, tayari flashi za kamera zikaanza kummulika mfululizo, aliipeleka mikono yake ili asionekana sura lakini polisi walikuwa wakiishusha na kuiacha sura yake wazi ili ionekane vizuri.
“Hebu shusha mikono yako hapa!” alisema polsi mmoja huku akimshusha mikono ile Nathan.

Hakuwa na jinsi, alikuwa chini ya ulinzi na alitakiwa kufanya kile walichotaka polisi wale akifanye, hivyo akashushwa mikono ile na kuendelea kupigwa picha.
Hakukuwa na mtu aliyeamini kama yule kijana ndiye aliyetaka kumuua Tatiana. Alionekana kuwa kijana mpole, mzuri wa sura ambaye hakufanana kabisa na muuaji yeyote yule duniani. Maswali yakaanza kumiminika kama Nathan ndiye aliyetaka kumuua Tatiana au polisi walikuwa wamecheza mchezo fulani ili hospitali ile irudishe heshima kama iliyokuwa nayo mwanzo.

“Mbona ni kijana mzuri tu,” alisema mwanamke mmoja.
“Hata mimi nashangaa, siamini kabisa.”
“Hapana kuna kitu.”
“Unahisi kuna nini?”
“Polisi hawa, wanaweza wakawa wamecheza mchezo na madaktari.”
“Una uhakika hicho kinaweza kutokea?”
“Kwa nini kisiweze? Kila mmoja anaangalia tumbo lake tu,” alisema mwanamke yule.
 
SEHEMU YA 136

Kitu kilichowavutia zaidi watu ni kwamba kijana huyo alitaka kumuua Tatiana huku akijifanya kuwa mwandishi wa habari kutoka katika Shirika la Habari la CNN. Watu wengi waliamini kwamba Nathan alikuwa mwandishi kweli kwani muonekano wake ulionekana mtu fulani aliyekuwa na uwezo kifedha.

Wakati tetesi zile zikizidi kuenea kwamba inawezekana Nathan alikuwa mtangazaji kweli, mkurugenzi mtendaji wa shirika hilo la habari, bwana Swan akatoa tamko kwamba hawakuwa na mfanyakazi mwenye jina hilo, kwa kuwa nao walikuwa wamechafuliwa, akaahidi kwamba ni lazima nao wangekwenda kushitaki.
“Huyu ataozea jela aiseee...hapa haponi,” alisema polisi mmoja huku akimwangalia Nathan aliyekuwa ameinama garini akilia.
“Huo ndiyo ukweli. Gaidi la kimataifa hili,” aliongezea polisi mwingine.

Bado moyo wa Nathan ulijuta, alishindwa kujua ni mahali gani alikosea mpaka kujikuta akikamatwa na polisi kisha kuanza kupelekwa kituoni huku akiwa hajatimiza lengo lake la kumuua Tatiana.
Alijaribu kuwaeleza polisi kwale kwamba alitaka kumuua Tatiana kutokana na usaliti mbaya aliokuwa amemfanyia lakini hakukuwa na yeyote aliyemuelewa, wote hao walimuona kuwa mtu mbaya ambaye alitakiwa kiufungwa hata kifungo cha maisha jela.

Safari ile ilichukua dakika kumi huku wakisindikizwa na magari mengi ya polisi mpaka walipofika kituoni ambapo Nathan akateremshwa huku akiwa na pingu mikononi kisha kuingizwa ndani ya jengo la kituo hicho. Macho yake yalikuwa mekundu kwa sababu ya kulia sana, hakuamini kabisa kama kweli alikamatwa hata kabla hajatekeleza mpango wake wa kumuua Tatiana. Moyoni alijuta.
 
SEHEMU YA 137

Taarifa za kukamatwa kwa Nathan ziliendelea kutapakaa dunia nzima, Waliberia wakachanganyikiwa, walimfahamu Nathan kama kijana mtulivu, mpole ambaye alipendwa na wanawake wengi kutokana na uzuri wake.
Alikuwa mtoto wa bilionea mkubwa nchini humo lakini kamwe hakuwa na majivuno. Alipendwa na watu wengi na hata wale wachache waliokuwa wakimchukia walifanya siri mioyoni mwao kwani miongoni mwa watu waliopenda kusaidia watu wengine, Nathan alikuwa mmojawapo.

Kitendo cha kukamatwa kwake baada ya kugundulika kwamba ndiye aliyetaka kumuua msichana Tatiana, Waliberia wengi walikataa hilo na kuamini kwamba kulikuwa na nguvu ya mtu fulani juu ya tukio lile kwani mtu kama Nathan asingeweza kufanya kitu kama kile kutokana na upole mwingi aliokuwa nao.
Wazazi wake wakachanganyikiwa mara baada ya kupata taarifa hizo. Nyumbani hakukukalika, siku hiyohiyo wakapanda ndani ya ndege yao binafsi na kuanza kuelekea nchini India kwa ajili ya kumuona kijana wao kwani mara ya mwisho aliwaaga kwamba alikuwa akienda nchini Nigeria, sasa kwa nini awe nchini India?

“Nakumbuka alituambia anakwenda Nigeria,” alisema baba yake.
“Ndivyo alivyoaga.”
“Sasa iweje awe India?”
“Hata mimi nahangaa, nahisi kuna kitu,” alisema mama yake.
Kila mmoja alichanganyikiwa, hawakuamini kile kilichokuwa kikiendelea kwamba kijana wao alikuwa amekamatwa na hivyo kufikishwa mbele ya sheria huku akiwa na kesi iliyofunguliwa jalada lisemalo kwamba alikuwa na kesi ya kutaka kuua.

Ndege ilikata mawingu na ndani ya masaa sita ikaanza kuingia nchini India. Walipoteremka kutoka ndani ya ndege, hali ya hewa ilikuwa ni ya joto mno ambapo wakaanza kutembea mpaka kwenye gari lililokuwa limewafuata na kisha kuondoka na kuelekea hotelini hata kabla ya kwenda kuonana na mtoto wao.
Hotelini hakukukalika, kila mmoja alikuwa na hamu ya kumuona Nathan kiasi kwamba hawakutaka kukaa sana na hivyo kuulizia sehemu alipokuwa amewekwa na kisha kuelekea huko huku kila mmoja akiwa amechanganyikiwa.
“Tunahitaji kumuona kijana wetu,” alisema baba yake Nathan alikuwa akizungumza na polisi.
“Nani?”
“Nathan.”
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom