56--Namshukuru Mungu niliyaanza masomo yangu vizuri huku nguvu zangu zote nikizihamishia huko. Uwezo wangu kimasomo niliokuwa nao shule ya msingi niliuendeleza shule ya sekondari. Hali yangu ya maisha ilikuwa ya kawaida hakukuwa na vikwazo vyovyote vya awali wakati nikiwa shule ya msingi, mauzauza ya wachawi yalikoma.
Siku moja nikiwa natoka shule nilishtuka kukutana na Helena njiani, moyo wangu ulinilipuka na kujua si rahisi binti yule kuja kunitembelea kwaheri. Nilipomkaribia nilimpita bila kumsemesha, wazo la haraka lilikuwa baada ya kumpita nitimue mbio. Shija, sauti ya Helena iliniita na kuufanya moyo wangu unilipuke kwa hofu zaidi.
Sikumjibu nilikaza mwendo ili nitimue mbio lakini Helena aliendelea kuniita. Shija, najua mimi ni adui yako mkubwa, pengine usingependa kuniona machoni mwako, ila nakuomba unisikilize kabla ya kuamua lolote lile juu yangu. Maneno ya Helena yalinifanya nipunguze mwendo ili nimsikilize, nilisimama na yeye alikuja mbele yangu na kupiga magoti.
Shija najua kiasi gani nimekufanyia mambo mabaya ambayo hatakiwi kufanya mtu mwenye ubinaadamu, nakubali nimekukosea. Nakuomba unisamehe kwa yote niliyofanya ya kutaka kukuondoa duniani, si mimi, kila nilichokifanya kilikuwa shinikizo la mama na washirika wenzake.
Nililazimishwa na nilipokataa walinitishia kunitoa kafara, kwa kweli niliogopa na kutii amri yao.
Lakini naamini maisha yako ni marefu kwani kila hila imeshindikana na leo hii bado unaendelea kuishi. Shija wewe ni kiumbe wa ajabu ambaye sijawahi kumuona chini ya jua, pamoja na yote niliyokufanyia kwa kunijua bayana bado hukutaka kulipa kisasi kama Sabina.
Sikuamini siku Sabina aliponieleza dhamira yake mbaya juu yangu, lakini ni wewe ndiye uliyeubadili moyo wake na hatimaye kuurudisha urafiki wetu.
Nimekuwa na wakati mgumu kusimama mbele yako kuomba msamaha kwa kuona aibu. Huwezi kuamini leo ni siku ya tano nasimama maeneo haya kukusubiri kutaka kukuomba msamaha.
Lakini kila nilipokuona ujasiri ulinipotea na kuamua kujificha nyuma ya mti na wewe kupita bila kujua kama nipo sehemu hii.
Shija nimejiuliza hali hii ya kukosa ujasiri wa kukueleza itaendelea mpaka lini, kama nina uwezo wa kwenda kumtoa mtu ndani mwake au kumfukua maiti kaburini kwa nini nilishindwa kusimama mbele yako?
Lakini nimeamini kazi ile hujaa nguvu za kichawi na si mtu kamili, tofauti na mimi kusimama mbele yako bila nguvu za kichawi. Kweli uso wa mwanadamu umeombwa na aibu. Shija napiga magoti mbele yako kukuomba msamaha toka chini ya uvungu wa moyo wangu. Nakuahidi alilolifanya Sabina ndilo nitakalo lifanya kuhakikisha unakuwa salama siku zote.
Najua sasa hivi upo salama sana baada ya adhabu aliyotoa mzee Manoni kwa wote waliotaka kukugeuza kitoweo. Ninavyokueleza mtoto wa kaka yangu mwezi jana ametolewa sadaka kama faini ya kile walichotaka kukufanyia .
Shija nipo tayari kwa lolote utakalotaka kunifanya hata likiwa zaidi ya alilotaka kunifanya Sabina nipo tayari. Nimekutendea mambo mabaya ambayo sikustahili kusimama mbele yako, lakini moyo unanisuta lazima nisimame ili unipe hukumu inayolingana na kosa langu.
Maneno ya Helena yaliufanya moyo wangu usisimke na kujikuta nikitokwa na machozi, niliamini alichokisema kilitoka moyoni mwake na kuzidi kuamini kwamba adui wa jana ni rafiki ya leo.
Machozi yangu yalizidisha kilio cha Helena ambaye alijikuta akikaa chini bila kupenda huku akinishika miguu yangu.
Shija najua roho inakuuma kila ukiniona mbele yako, unatamani kunirarua na kunila nyama.
Nakuomba uamini hili nisemalo, sisi wasichana wa kijijini tumekuwa tukilazimishwa kuingizwa kwenye uchawi bila kupenda kwa kisingizio cha kurithi mikoba ya wazazi wetu watakapozeeka .
Tumekuwa tukifanyishwa mambo ambayo nafsi zetu hayazitaki, lakini siku zote ukiifanya kazi mbaya kwa muda mrefu hatimaye unajikuta umeingia na kuwa mshiriki kamili usiye na chembe ya huruma.
Sabina kabadilika hivi karibuni baada ya kuzama katika penzi lako, lakini Sabina ndiye aliyeongoza kwenye mambo mazito hasa ya kufukua maiti za watoto, kutoa mimba za wanawake ambao hujiona wana mimba na mwisho wa siku huzaa vitu vya ajabu.
Kweli nimeamini penzi kitovu cha uzembe, Sabina tangu kuwa na wewe amejikuta akikiuka miiko yote ya uchawi na kuwa tayari kwa lolote, kilichomsaidia Sabina ni uwezo mkubwa wa kichawi wa mama yake tofauti na mimi. Nataka nikueleza kitu kimoja, baada ya zoezi la kumtorosha kaka yako kushindikana, nilitakiwa nitolewe kafara ili niliwe nyama.
Mama yangu aliwapigia magoti nisifanyiwe hivyo , walikubali kunisamehe lakini sharti kubwa nililopewa ni kuhakikisha nafanikisha kukuua au kukuchukua msukule.
Shija ile ilikuwa siri ambayo hata Sabina hakuijua, nina imani angeijua mapema nisingekusogelea. Kwa ukaribu wetu Sabina alinipa siri kuwa ngozi ya kinga ya safari za hatari alikupa wewe ili kukukinga.
Kwenye kamati ya uchawi alisema ameidondosha, kwa vile alikuwa akiaminika kwenye safari zote za kiuchawi, binafsi sikumuamini aliponiambia kuwa amekupa nilidhani amepoteza kweli. Lakini kikwazo cha kukupata kilinifumbua macho na kufanya upelelezi na kuamini kumbe kweli. Hapo ndipo nilipobahatika kukipata kipande cha ngozi na kuondoka nacho.
Tukiwa na uhakika wa kukupata, lakini kwa maajabu makubwa, siku tulipokuja tulishangaa kutokukuta, nilijikuta nikichanganyikiwa na kujiuliza wewe ni kiumbe wa aina gani, nilianza kukata tamaa ya kukupata, ndipo nilipotumia njia ya kukutafuta mchana, bahati nzuri nilikukuta umelala ndani na kukulisha dawa za kichawi ili ufe.
Shija, Sabina kweli aliapa kuyatetea maisha yako, aliweza kuyaokoa tena maisha yako kwa kukutapisha dawa za kichawi, niliamini kupitia ugonjwa wako, basi tungeweza kukupata na kweli tulikupata bado Sabina aliyaokoa tena maisha yako kwa kupeleka taarifa kwa mzee Manoni.
Shija nakuomba kuanzia leo unione ni kiumbe kipya niliyemsafi mbele yako, nakuahidi kuyafanya yote aliyoyafanya Sabina au pengine mara mbili yake. Baada ya kumsikiliza Helena na kuona kwamba mengi hayakuwa mageni kwangu zaidi ya kunifafanulia kwa kina, niliamini ni muda mwingine wa msamaha kuchukua nafasi yake.
Nilimshika mabegani na
kumnyanyua , nilimtazama, alikuwa akiaanza kuvimba macho kutokana na kilio. Helena, nilimwita kwa sauti ya chini. Abee Shija. Nimekusamehe. Kweli Shija? Kweli. Au unanifurahisha tu?
Helena nilikusamehe tokea siku ya kwanza nilipojua dhamira yako, nina imani msamaha wangu ndiyo uliomfanya Mungu naye anilinde. Amini kweli nimekusamehe tumefundishwa kusamehe ili tusamehewe. Asante Shija, umenipa funzo maishani mwangu. Kwa hiyo umeachana na uchawi? Nilimuuliza.
INAENDELEA.....