Nitakufa Mara Ya Pili

Nitakufa Mara Ya Pili

37--Sasa itakuwaje?” niliuliza. “Hatuna jinsi, tuingie tu kwenye mvua tukiisubiri mpaka ikatike lazima watatupata, wametumia mvua ili kutuzuia tusifike mbali,” alisema Sabina huku akifuta maji usoni, kauli ile ilinivunja nguvu na kuona lazima nitakuwa katika wakati mgumu maishani mwangu kwa kuharibu kila sehemu. Nilikumbuka maneno ya mzee Manoni kwamba Sabina na Helena ni watoto tu hawawezi kitu chochote.

Kila dakika mvua ilizidi kuongezeka ukali wa manyunyu yake ulifikia hatua ambapo matone yake yakimpiga mtu mwilini unahisi maumivu. Tulikubaliana kutembea na ile mvua kuelekea barabara kuu ambapo hakika ilinitia hofu kuhusu usalama wetu.

Ukali wa mvua ulitufanya tusione tunapokwenda kutokana kunyesha kwa nguvu. Baada ya kuona kila hatua ilikuwa ni lazima mtu aanguke kwenye maji, tulikubaliana tusimame sehemu tusubiri mvua ikatike. Lakini Helena aligoma kwa kuamini tukisimama sehemu watu waliokuwa wanatufuata wangetukuta.

Nilijiuliza watu hao wangetukuta wapi? Na kama walikuwa wametugundua niliamini hatukuwa na ujanja wa kufika popote kabla hawajatukamata. Tulikubali kuendelea na safari kwa shida huku mvua ikizidi kutunyeshea na kutufanya tuhisi maumivu makali. Tuliendelea mbele na kiza nacho kilizidi kutuchanganya.

Kilichotokea muda ule sikuwahi kukiona katika maisha yangu. Mvua ilikuwa kali iliyoambatana na upepo mkali, na kiza kizito kilichokuwa hakielezeki kwa maneno. Nilitamani kulia lakini ajabu Sabina na Helena walikuwa mstari wa mbele kuhakikisha tunaushinda mtihani ule. Niliamini maisha yetu yalikuwa kwenye hatari, lakini Sabina na Helena walionesha ujasiri muda wote kumnyanyua kaka kila alipoanguka.

Kuna kipindi tulitumbukia kwenye shimo na kutoka bila kujua tulikuwa tunaelekea wapi, akili yangu ilinionesha kabisa tumeishakosea njia kutokana na kutembea muda mrefu kwenye mvua bila kufika. “Jamani hatujapotea?” niliuliza. “Shija si suala la kuuliza hii ni vita tujitahidi tu tutashinda,” Sabina alisema. “Hatuna jinsi twendeni tu mpaka tujue mwisho wake,” Helena alisema kwa msisitizo. “Na kweli tukikosea leo tumeharibu kila kitu,” Sabina aliongezea.

Maneno yale yalinivunja nguvu na kuona tumeishauvaa mkenge kwa kuamini ubishi wa kina Sabina ndio uliotufikisha pale. Tuliendelea kutembea kwenye mvua kwa kuanguka na kunyanyuka . Kaka alikuwa amechoka kiasi cha kumshika na kumburuza kwa kutembelea magoti. “Jamani niacheni mimi nimechoka,” kaka alilalamika. “Luhemeja mateso yote haya ni kwa ajili yako jikaze, tunaweza kufika sehemu tukapona,” Helena alimueleza kaka ambaye alikuwa hoi kwa safari isiyo na mwisho

. Si yeye hata mimi niliona aibu kusema nimechoka kwa vile kazi ile ilinihusu mimi. Niliuweka mkono wa kaka mabegani kwangu na kuanza kwenda naye huku mvua ikizidi kuwa kali sana, mbele kiza kilikuwa kizito cha kutisha. Baada ya mwendo mfupi tulishtukia wote wanne tukiangukia kwenye mto uliokuwa ukipeleka maji kwa kasi.

Kila mmoja alipiga kelele kutetea nafsi yake. Kasi ya yale maji yalitupeleka kwa kutuburuza bila kujitetea. Kitu kibaya zaidi ni kwamba kulikuwa na kiza kizito ambacho kilitufanya tusione sehemu ya kuweza kujitetea kuyaokoa maisha yetu. Nikiwa napelekwa na maji nilimuomba Mungu aipokee roho yangu kwani sikuwa nafanya jambo isipokuwa kumtetea kaka yangu aliyekuwa mzima lakini akiishi maisha ya wafu.

Ghafla nilihisi kupigwa na kitu kizito kichwani kilichonifanya nipoteze fahamu. Kilichoendelea sikukijua. Niliposhtuka nilijikuta nimefungwa chini ya mti mkubwa, sehemu ambayo wachawi hufanya mkutano wao. Sehemu hiyo haikuwa ngeni kwangu kwani niliishawahi kufika katika sherehe ya wachawi kwa njia ya ndoto iliyokuwa na ukweli .

Pembeni yangu walikuwepo Sabina na Helena ambao nao walifungwa kama mimi. Chini alikuwa amelala kaka yangu akiwa amefungwa kamba huku akiwa amepigiliwa msumari mkubwa katikati ya kichwa na mwingine pembeni ya kichwa. Ilionesha kaka yangu alikuwa amekufa, na alikuwa katika vazi lile lile nililomchukulia nyumbani na kumvisha.

Moyo uliniuma nikijua na mimi muda si mrefu nitamfuata kaka yangu, ila sikuamini kama Sabina na Helena nao wangenifuata nyuma yangu. Bado Sabina na Helena walinitia moyo hawakuonesha kutishika na adhabu ile. Mara lilitokea kundi la wachawi wakiwa wanatoka makaburini ambako walipata miili miwili ya watu ambayo siku hiyo ingeliwa nyama.

Walikuja huku wakiwa wamebeba maiti za watu wawili waliokuwa kwenye sanda ambayo ilionekana mpya. Baada ya kuitua pale, mkuu wa wachawi mzee Manoni alisema: “Nafikiri kazi imekwenda vizuri, ila kuna nyama imeongezeka kutokana na kiburi cha kitoto,” mzee Manoni alisema huku akinigeukia na kunitazama kwa muda kisha alisema: “Shija nilikueleza usiingilie nguvu za watu utapotea sasa ona umesababisha kaka yako kugeuzwa kitoweo usiku huu.”

“Kwa nini na yeye asiliwe?” mchawi mmoja aliuliza. “Shija hana kosa, hajui lolote kuhusu uchawi bali watoto wenu.” “Lakini ameisha ua siri zetu lazima tumgeuze asusa leo,” mwingine alichangia. “Bado hiyo haitoshi, wa kulaumiwa ni watoto wenu, Shija namjua vizuri.”

“Kwa hiyo na yeye ageuzwe msukule,” kauli ile ilinivunja nguvu na kujua Shija mimi nimekwisha. “Hapana huyu haguswi na kitu chochote ila nataka akitoka hapa atoke akijua kaka yake hayupo tena wala asisumbuke kumtafuta. Leo atamshuhudia akiliwa nyama pamoja na maiti nyingine tulizo pata leo.” Baada ya kusema vile walimchukua kaka na kuanza kumkata vipande ambavyo waligawiana na kuanza kumla mbele yangu. Maumivu yalikuwa makali kuliko siku aliyokufa kwa kiini macho. Baada ya kumaliza kumla kaka yangu huku wakicheza ngoma, waligawana na maiti zingine mbili ambazo zilikuwa zimelazwa.

Baada ya zoezi lile, nilifunguliwa pamoja na wenzangu Sabina na Helena na kupewa onyo zito. “Shija leo itakuwa mwisho wangu wa kukutetea tena, ukifanya chochote kinyume na ninavyokueleza utayamaliza mwenyewe . Haya arudishwe kwao ili wazazi wake asubuhi wamkute chumbani kwake .” Baada ya kusema vile nilihisi kizunguzungu na usingizi mzito ulinipitia palepale nilipokuwa nimefungwa kamba, kilichoendelea sikujua


Inaendelea...
 
38--Sauti ya baba ilinishtua asubuhi, niliposhtuka nilijikuta nipo kitandani kwangu. Kabla ya kunyanyuka nilijawa na mawazo juu ya ndoto niliyoota, lakini akili yangu bado haikuamini kama ilikuwa ndoto bali kitu cha kweli. Bado sikutaka kuamini nilisubiri wazazi wangu waende shamba niende kwa kina Sabina kupata ukweli sikuwa na woga tena moyoni mwangu.
Baada ya baba na mama kwenda shamba, mimi kiguu na njia kuelekea nyumbani kwao Sabina kutaka kuuliza kilichotokea jana kilikuwa ndoto au kweli. Kwa mbali niliwaona Sabina na Helena, walipofika cha kwanza kilikuwa kunipa pole. “Pole Shija.” “Ya nini?” “Si ya kumpoteza kaka yako jana.”

“Mmh, hivi yaliyotokea jana ni kweli au ndoto?” “Lazima utajua ilikuwa ndoto ulipoamka na kujikuta upo umelala kwenu, lakini kila ulichokiona ni kweli kabisa. Makosa yalikuwa muda tulichelewa sana ndiyo yaliyosababisha tumpoteze kaka yako.” “Kweli, Shija nitajitahidi kukufundisha jinsi ya kukabiliana na wachawi najua sasa hivi watakutafuta kwa udi na uvumba wakuangamize.”

“Sasa jamani mjomba akiniuliza nitamjibu nini?” “Mwambie hatukufanikiwa kwenda.” “Na akitaka kutumia nguvu za dawa?” “Hawezi kupata kitu zaidi ya kupata ukweli kuwa kweli kaka yako amefariki.” “Mmh, sasa itakuwaje maana mpaka sasa hivi siamini kama wazazi wenu watataka muwe karibu yangu.” “Yote hayo tuachie sisi, tunakuhakikishia kukulinda kwa nguvu zetu zote japo tunaonekana watoto, najua lililotokea jana kuna makosa tuliyafanya .

Tulisahau kumfuta mhuri wa kichawi ambao uliwafanya watujue tupo wapi kwa urahisi, tumuachie Mungu,” Helena alinipa moyo. “Nitashukuru.” “Ila najua leo tuna kikao kizito kitachozungumzia kukushirikisha kuijua siri ya wachawi , lazima kuna mkakati mzito wa kukuondoa duniani kwa kifo au kukugeuza msukule.

Lakini pia nguvu za mzee Manoni zinakulinda ila lazima uwe makini lazima watatumia ujanja ili wakutie adabu,” Sabina aliongezea. Tukiwa katikati ya mazungumzo mara Sabina na Helena walitimua mbio na kuniacha nimesimama peke yangu kama sanamu nisijue nini kinachoendelea.

Wakati najiuliza wamekimbia nini nilimuona mzee Manoni akipita, ajabu baada ya kunisalimia alipita bila kuongeza neno lolote. Nilimsindikiza kwa macho mpaka alipopotea niligeuka na kuelekea nyumbani. Mbele nilikutana na kina Sabina. “Vipi amekuuliza kitu?” “Hataa, amenisalimia tu na kuendelea na safari zake.” “Ooh, afadhali mzee yule mbeya kama mwanamke.” “Kama angewaona?”

“Tumekatazwa kuwa karibu na wewe , kama angetuona angekwenda kuwaambia na lazima tungepewa adhabu kali.” “Mmh, hamuoni vita yangu ni kubwa?” “Ni kweli lakini tutajitahidi na udogo wetu kukulinda.” “Basi jamani tutaonana baadaye maana kichwa kizito kwa usingizi pia kinaniuma sehemu niliyopigwa na kitu wakati tunapelekwa na maji.”

“Mmh, pole ngoja nikakuletee dawa,” Sabina alinieleza huku wakigeuka na kuelekea kwao nami nilirudi nyumbani kulala, kichwa kikizidi kubeba mambo mazito ambayo wazazi wangu hawakupaswa kujua.

Wakati najiandaa kulala Sabina aliingia na kuniletea dawa ambayo alinipaka ilikuwa imechanganywa na mafuta ya ng’ombe. Baada ya kunipaka alinipa nyingine ya kunywa kisha aliniaga na kusema angerudi mchana kunijulia hali. Alipoondoka nilipitiwa na usingizi mzito sana.

Usiku wa siku ile nikiwa katikati ya usingizi nilishtushwa na kishindo kizito ukutani. Nilishtuka na mapigo ya moyo yalinienda kwa kasi na kuanza kutetemeka. Sikuamini macho yangu kuuona ukuta ukipasuka na mwanga mkali ulinipiga usoni. Baada ya mwanga ule kunipiga ulinifanya nione kiza kizito mbele yangu, nilijitahidi kushindana na kiza kizito hicho mbele yangu.

Baada ya muda niliweza kurudi katika hali ya kawaida kuizoea hali iliyokuwepo . Nje kulikuwa na mwezi mkali ulionifanya nione nje kupitia sehemu ya ukuta iliyopasuka. Woga ulinitawala nilijikunja ukutani kabisa pembeni ya kitanda huku nikijitahidi kuangalia ukuta ule umepasuka kweli au kiini macho. Mara niliwaona watu wanne waliokuwa uchi wakiingia chumbani kwangu.

Nilinyanyuka kitandani na kupiga kelele ambazo zilipasua anga. Lakini kuna kitu chenye nguvu kali kiliniingia mdomoni na kuifunga sauti yangu. Wawili hao walinisogelea kitandani nilipokuwa nikifunua mdomo kupiga kelele ambazo zilikuwa hazitoki.

Wakati wananivuta ili wanitoe nje, sauti ya mlango wa chumba cha wazazi wangu iliwashtua. Niliwasikia wakisema. “Mambo yamekwisha haribika tuondokeni.” Baada ya kusema vile mmoja wao alifanya kama anaondoa kitu mdomoni kwangu ambacho sikukiona na kutoka mbio huku ukuta ukirudi katika hali yake ya kawaida.


Inaendelea...
 
39--Ajabu sehemu ya kooni iliyokuwa imekauka iliachia na kuwa katika hali ya kawaida. Nikiwa bado natafakari kilichonitokea, mlango wangu uligongwa ukifuatiwa na sauti ya baba. “Shija,” japo sauti ile ilikuwa ya baba bado sikuiamini kutokana na hofu nzito iliyokuwa moyoni mwangu.

Sikuitikia mara moja mpaka baba aliporudia kwa sauti ya juu huku akiugonga mlango. Sauti ya mama ndiyo iliyonifanya niitikie na kufungua mlango. Nilimsikia mama akisema: “Inawezekana anaota, turudi tukalale.” “Mmh, kelele zile si za kawaida, ngoja kwanza aamke tumsikie.

Nimewahi kusikia kelele nyingi lakini hizi zina jambo.” Baba alipogonga tena mlango huku akiita jina langu, niliitikia na kutoka nje. Kwa vile mwanga wa mwezi ulikuwa mkali nilimuona baba akinichunguza kabla ya kuniuliza kitu. Wa kwanza kuniuliza alikuwa mama. “Shija eti umetokewa na nini?” “Kwani vipi?” niliuliza. “Baba Shija labda kelele zile si za Shija.” “

Hapana, Shija hebu tueleze nini kimekutokea?” Kabla ya kujibu nilijikuta nikifikiria masharti niliyopewa na mzee Manoni kuhusiana na kuitoa siri yoyote nje. “Shija umetokewa na nini?” “Baba ni ndoto tu.” “Ndoto gani uliyoota?” “Niliota nafukuzwa na simba ndio maana nilipiga kelele.” “Basi rudi ukalale.” “Hapana mume wangu huyu hawezi kulala tena peke yake tuingie naye ndani tukalale naye.”

“Wazo zuri.” Kimoyomoyo nilishukuru kuchukuliwa na wazazi wangu kwani niliamini kama ningelala peke yangu wachawi wale wangerudi kunichukua na sikujua walitaka kunipeleka wapi. Lakini nilikumbuka niliyoelezwa na kina Sabina kuwa uhai wangu unawindwa usiku na mchana baada ya kuzigundua siri za wachawi .
Na lingine baya lilikuwa kutaka kumtorosha kama yangu na kuonekana nayajua mengi. Kutokana na kauli ya kina Sabina wachawi walipanga kumzunguka mzee mzee Manoni na kunitoa kafara. Niliwashukuru wazazi wangu nililala salama mpaka asubuhi. Kama kawaida baada ya wazazi wangu kwenda shamba Sabina na Helena kwa njia za siri walikuja nyumbani.

Walipokuja walitaka kujua
hali yangu, niliwaeleza yaliyonitokea usiku. “Ha! Mungu wangu ndio maana nilisikia wakijilaumu kwa kosa walilofanya , sikujua kumbe walikuwa wamekufuata wewe .” “Ina maana mtu waliomkosa alikuwa Shija?” Sabina alishtuka. “Ndiyo mimi, msishangae siku moja mkaniona nimegeuzwa msukule nyumbani kwenu!” “Haitatoke na ikitokea siku watakayokuingiza usiku asubuhi nakutoa na lolote wanifanye ,” Sabina alisema kwa msisitizo. “Sabina tutafute njia ya kumsaidia Shija hali ni mbaya wamempania lazima watampata.

Si unajua uwezo wetu si mkubwa kama tulivyofikiri .” “Mmh, nimepata wazo” “Lipi hilo?” “Shija nenda kwa mzee Manoni mueleze ukweli yeye ndiye mwenye uwezo wa kukusaidia. Kama ukishindikana uhamie mjini kwa mjomba wako.” “Basi ngoja nimalize mtihani wa mwisho nikiwa nasubiri majibu ya darasa la saba nihamie mjini.”

“Shija muda uliobakia si mkubwa sana, lakini watu wale hawaaminiki. Sasa hivi nawaogopa kama ukoma. Basi mtafute mzee Manoni ndiye mtu mwenye kukusaidia kwa sasa hivi.” “Nitafanya hivyo .” “Lakini kabla ya yote tutakupa dawa ambayo kila ukitaka kulala unajifunga mkononi, kila atakayekuja kwako hakuoni.”

“Basi kama dawa hiyo ipo hakuna haja ya kwenda kwa mzee Manoni.” “Basi subiri.” Baada ya kusema vile Sabina alitimua mbio na kuniacha na Helena, kwa woga wa kuonekana tulijificha chumbani kwangu. Baada ya muda Sabina alirudi na kupande cha ngozi ambacho kilikuwa kimetobolewa na kuwekewa kipande cha uzi.

Alipofika alikitoa; nilimuona Helena akishtuka. “Sabina hii si kinga yako?” “Ee, lakini kwa kipindi hiki lazima tumlinde Shija la sivyo tutampoteza.” “Na wewe ?” “Nitapata.” “Sabina si unajua ngozi hii sasa hivi haipatikani?” “Wakijua nimeipoteza watanipumzisha kwenye safari za hatari.”

Nilimshukuru Sabina kwa jinsi alivyojitolea juu yangu na kuwa tayari kwa lolote ili kuhakikisha nipo salama. Baada ya kina Sabina kuondoka, nilifuta wazo la kwenda kwa mzee Manoni kwa kuangalia kile kipande cha ngozi cha kujifunga kwenye mkono. Baada ya muda Sabina alirudi peke yake, nilimshangaa na kumwuliza. “Vipi mbona umerudi peke yako?” “Shija kuna kitu nataka kukuambia lakini kisikutishe sana.”

“Kipi hicho?” “Jichunge sana na Helena.” “Kivipi?” ”Inaonekana bado anatumiwa na wachawi .” “Kivipi?” “Njia nzima alikuwa akinilaumu kukupa ngozi hii kwa kusema eti hata ukifa kuna hasara gani.” “Wewe umemjibu nini?” “Nimemwambie heri nife mimi kuliko wewe .” ”Yeye akasemaje?”

“Nimemwona kama kakosa raha, na wasiwasi huenda akawaeleza kuwa nimekupa kinga hii.” “Sasa tutafanyaje?” “Ndio maana nikasema usihofu, nitajua njia ya kufanya lazima nitamfanyia kitu kibaya.” “Kipi tena Sabina?” “Nitamuua.” “Noo, usifanye hivyo , Sabina.” “Hapana Shija, Helena sio mtu mzuri hata kidogo, ni rafiki yangu lakini ana roho mbaya sana.”


Inaendelea...
 
40--“Roho yake mbaya nini?” ”Kuna wanafunzi aligombana nao ugomvi wa kawaida alipofika kwa mama yake waliwageuza , walikubaliana kuwageuza msukule na siku ya pili walikufa katika mazingira ya kutatanisha kama kaka yako mara ya kwanza.” “Mmh, sasa kwangu roho yake mbaya ipi?”

“Shija nimezuia vitu vingi sana vya kukuangamiza kutoka kwa Helena alivyotumwa na kundi la wachawi lililokupania kukutoa duniani au kukugeuza msukule. Mara nyingi alikuwa akinishirikisha kwa kujua wewe ni mpenzi wangu lakini nilimgomea na kumpiga mkwara mzito kama angekugusa.” “Sasa unaniambiaje?

Maana kila kitu changu kwa Helena kipo wazi, lakini mbona alikuwa mstari wa mbele kunisaidia kumtoa kaka yangu?” “Kwa shinikizo langu.” “Kwa hiyo wasiwasi wako nini?” “Wa kunizunguka, kwa hiyo tuwe naye makini sana naye.” “Hakuna tatizo Sabina nimekuelewa.” “Shija usifikirie utani utakuja kumbuka kauli zangu,” Sabina alionesha msisitizo juu ya kumshtukia shoga yake.

Siku zote Sabina alioneka yupo mstari wa mbele katika kunipigania, nilijifikiria ujasiri gani uliomfanya kunifanyia yote yale kwa kuwa tayari kuyatoa maisha yake kwa ajili yangu. Dawa na ngozi aliyoniletea Sabina vilinifanya nirudi katika hali ya kawaida, huwezi kuamini tukio la kushuhudia kaka yangu akiliwa nyama liliichanganya sana akili yangu na kunifanya nisiende shule kwa wiki nzima. Ila usiku nililala safi japo nilikuwa nikisikia vishindo vya watu wakiizunguka nyumba huku wakisema hawanioni kila walipoingia ndani.

Walipokuwa wakija nilishtuka usingizini kutokana na vishindo huku miale ya moto ilitanda juu, baada ya vishindo ukuta hupasuka na kuwaona watu zaidi ya sita wakiingia ndani. Nilijikunyata ukutani kuogopa kuonekana, lakini kwa maajabu huondoka bila kuniona huku wakisema sionekani inawezekana siku hizi silali mle.

Kila usiku kulikuwa na vishindo kuzunguka nyumba na kuingia ndani bila kuniona na siku ya pili nilipokutana na Sabina nilimueleza kuhusiana na vishindo vya usiku hata sauti za ukuta kupasuka na watu kuwaona wakiingia ndani lakini hawakuniona na kuondoka. “Shija una vita nzito sana shukuru hiyo ngozi bila hiyo walikuwa na nia mbaya, ila nakuomba fanya mpango wa kumueleza mzee Manoni.” “Nitafanya hivyo .”

Nilizidi kumshukuru Sabina mara mia jinsi alivyoonesha kunijali na kuwa tayari kutoa uhai wake kwa ajili yangu. Dawa zake zilinisaidia sana kurudi katika hali ya kawaida kiasi cha kuweza kwenda shule kama kawaida. Niliweza kusoma shule kwa mazingira magumu kwa kumuogopa Mwalimu Vene na Helena japo Helena hakuonesha mabadiliko yoyote kwangu.

Wasiwasi wangu mwingine niliamini huenda maneno ya kunitahadharisha na Helena yanatokana na wivu . Nilishindwa kuonesha kumbagua Helena kwa vile muda wote walikuwa pamoja. Masomo yaliendelea kama kawaida, miezi miwili kabla ya kufanya mtihani wa darasa la sana, nakumbuka siku hiyo Helena alikuja peke yake.
Sikushangaa kwa vile na yeye alikuwa sehemu ya urafiki wetu pamoja na kuelezwa niwe naye makini.

Helena alionesha uchangamfu kama kawaida kitu kilichozidi kunitoa hofu na kuamini maneno ya Sabina ni wivu tu. Tukiwa katika mazungumzo nilimuona Helena akikimbilia chumbani huku akinieleza Sabina akifika nisimwambie kama yupo pale. Baada ya muda mfupi Sabina alifika na kuniuliza. “Shija, Helena kafika huku?” “ Sijamuona kwani vipi?” “Nimepita kwao wamesema ameelekea huku.”
“Mmh, sijamuona,” nilimdanganya. “Ni hivi....,” nilimwekea kidole mdomoni kumnyamazisha. “Kuna nini?” aliniuliza kwa sauti ya kunong’ona.

Nilimshika mkono na kumuondoa eneo la pale nyumbani ili tu Helena asisikie alichotaka kunieleza Sabina nilijua anaweza kuropoka. Sabina naye hakuwa mbishi alinifuata mpaka nje ya uzio wa nyumbani kwetu nyuma ya mti mkubwa wa mwembe. “Vipi Shija kuna nani?” Sabina aliniuliza huku uso wake ukijaa shauku ya kujua kuna kitu gani kwani kitu kile hakikuwahi kutokea. “Baba.” “Ooh, wacha niondoke.” “Anaondoka sasa hivi kuna kitu nilikuwa nimetumwa nikaona nipite mara moja.”

“Kwa hiyo?” “Hebu subiri nikamtazame.” Nilimuacha Sabina nyuma ya mti na kurudi hadi nyumbani ili kumuondoa Helena kama bado yupo ndani. Nilipoingia ndani sikumkuta, nilizunguka nyuma ya nyumba vile vile hakuwepo. Niliamini ameisha ondoka, nilimwita Sabina kwa sauti kwa vile hakuwa mbali alinisikia.



Ni Kweli Helena Ataichukua Ngozi?
Tukutane Baadaye Kidogo......
 
41--Alikuja kwa tahadhari, nilimtoa hofu. “Ameishaondoka.” “Mmh, niliogopa sana, hivi baba yako akinikuta hapa kwenu atasemaje?” “Nitamwambia mwanafunzi mwenzangu ambaye nashirikiana naye darasani.” “Mmh, haya.” “Helena ulikuwa unamtafuta wa nini?” “Nilikuwa na wasiwasi labda amefika huku.” “Wasiwasi wa nini?” “Si nilikueleza kuna kikao cha siri kuhusiana na wewe kuijua siri ya wachawi , basi kuna mpango mkubwa umepangwa kuhakikisha wanakufanyia kitu kibaya.”
“Na mzee Manoni yumo?” “Wala hajui lolote, si ndiyo maana nilikueleza ukamueleze mapema.”

“Na ile ngozi haitanisaidia?” “Itakusaidia, ndio maana nilikuwa na wasiwasi na Helena kuja hapa anaweza kuja na kukuibia ngozi hiyo na usiku wakija wakuchukue kirahisi.” Kauli ya Sabina ilinitisha sana na kunitia wasiwasi wa Helena kuingia ndani, niliogopa kumueleza ukweli kuwa Helena alifika na kuingia ndani. Lakini ilibakia siri yangu moyoni kuwa Helena alifika na kuingia chumbani kwangu.

“Mmh sawa, basi itabidi niende kwa mzee Manoni mapema,” nilimjibu huku wasiwasi wangu ulikuwa kwenye ngozi yangu niliyoiweka chini ya godoro.
“Kwa leo huwezi kumpata amekwenda katika kikao cha wachawi kinachofanyika Kasungamile, Geita, kurudi inaweza kuwa karibu na alfajiri.” “Kwa hiyo itakuwaje?” “Tumia hiyo kwa leo akirudi jitahidi kumuona la sivyo utapotea, uwezo wangu ni mdogo pia hata Helena amekuwa akinikimbia katika mambo yake.”

“Basi lazima tuwe naye makini.” “Shija mi si mkaaji nilikuja tu ili kukueleza hili, ila kuwa makini sana na Helena.” “Nimekuelewa.” “Nilisahau, sasa hivi sitakuwepo kuna kazi moja tumetumwa kwenda kuifanya muda wote, hivyo sitaonana na wewe mpaka kesho. Kuwa makini tu na yote niliyokueleza, usiku najua unaweza kuwa mbaya kama utafanya makosa.” “Nimekuelewa mpenzi.”

Baada ya mazungumzo Sabina aliondoka na kuniacha nikiwa na shauku la kwenda kuiangalia ngozi yangu chini ya godoro. Niliingia hadi chumbani kwangu. Hali ya godoro langu kuwa tofauti na lilivyokuwa ilinishtua na kunifanya nifunue godoro. Sehemu niliyoweka ngozi yangu hapakuwa na kitu, sikuamini macho yangu na kunifanya nishtuke.

Nilianza kupekua kila kona bila dalili zozote za kuiona ngozi ya kinga niliyopewa na Sabina. Nilijiuliza inawezekana kweli Helena kaichukua, lakini kajuaje kama nimeificha chini ya godoro? Nilikumbuka siku moja kabla ya kuelezwa na Sabina niwe naye mbali aliniuliza kuhusu kuiweka ngozi yangu.

Katika ushauri wake alinieleza sehemu salama ni chini ya godoro baada ya kumueleza naiweka kwenye ubao wa batini. Wazo la haraka lilinifunua akili kuwa yote niliyoelezwa na Sabina yalikuwa na ukweli mkubwa. Jasho la hofu lilinitoka na woga ulinijaa moyoni kuhofia mpango wa kunifanyia kitendo kibaya.

Kibaya muda ulikuwa umekwenda sana kutokana na kuhangaika kutafuta ngozi kila kona ya chumba kwa zaidi ya masaa mawili. Kutokana na maelezo ya Sabina muda ule niliamini asingekuwepo. Nilijikuta nikichanganyikiwa na kujiuliza ngozi nimepoteza sijui usiku utakuwaje? Nilipata wazo usiku ukiingia nikalale kwa wazazi wangu kwa kuhofia kuchukuliwa na wachawi . Lakini kutokana na historia ya wachawi lazima wangenichukua bila wazazi wangu kujua na asubuhi wangenikuta nimekwishakufa .
Wazo la kutolala ndani lilizidi kuniweka katika wakati mgumu sana. Siku ile niliishi kwa shida kutokana na hofu kunitanda moyoni mwangu. Nilijiuliza nitafanya nini usiku ukiingia kwani kwa macho yangu niliwashuhudia wakinitafuta lakini hawakufanikiwa kuniona na kilichonisaidia kilikuwa ngozi?

Kulala kwa wazazi nilijua si dawa ya kuwazuia kunichukua. Kwa mara ya kwanza toka nianze kutokewa na mauzauza ya wachawi siku ile ilikuwa nzito kwangu, wasiwasi wangu niliamini lazima watatumia nafasi ile kunifanyia kitu kibaya kama kulipa kisasi cha kugundua mambo yao ya kichawi. Nilijikuta nikimchukia Helena kwa kitendo chake cha kuniibia ngozi niliyopewa na Sabina. Wazo la haraka nilifikiria kuwaeleza wazazi kuhusiana na mpango wa usiku.
Bado onyo la mzee Manoni lilinitisha na kujikuta kwenye wakati mgumu kuwaeleza wazazi wangu tukio lililotaka kunitokea usiku. Pamoja na udogo wangu nilijikuta nikiwaza mambo mengi. Nilipata wazo moja la kutolala ndani ili wakija wasinikute. Wazo hilo nililiona linafaa kulifanyia kazi, baada ya wazo lile niliendelea na shughuli zangu kama kawaida.
Usiku ulipoingia kama kawaida baada ya chakula cha usiku niliingia chumbani mwangu, nilikuwa chumbani lakini akili yangu ilikuwa mbali sana. Nilisubiri mpaka wazazi wangu walipoingia ndani ili nitoke, ajabu siku ile wazazi wangu walichelewa kuingia ndani kulala.
Nilishangaa siku ile kuchelewa kuingia ndani walikuwa wakizungumza nini. Nilijikuta nikiwachukia wazazi wangu na kuwaona labda nao wanahusika kwa namna moja au nyingine, siku zote walikuwa wakiwahi kulala au kuingia ndani lakini siku ile ilikuwa tofauti. Niliamua kujilaza kusubiri mpaka watakapotaka wenyewe kuondoka.


INAENDELEA....
 
42--Nilijua hata kama watachelewa hawatakaa sana nje kutokana na usiku kuwa na kiza kinene na ubaridi mkali. Baada ya muda kidogo nilimsikia mama akilalamika baridi na mbu na kumuomba baba waingie ndani. Walikubaliana kuingia ndani, hapo kidogo nilipumua na kuamini ni nafasi yangu ya kutoroka.

Baada ya kuhakikisha wamelala kwa kupita ukimya bila kusikia sauti zao, huku nikiwa sijui muda ule ulikuwa saa ngapi kutokana kiza kuwa cha kutisha na kibaridi cha kupuliza, nilizima kibatari na kutoka kwa kunyata baada ya kufunga mlango kwa kuuegesha. Nilielekea upande ambao niliamini palikuwa salama, ambako kulikuwa na miti ya miembe.

Sehemu yenyewe ilikuwa ikitisha, hakuna mtoto au mtu mwenye moyo mdogo aliyeweza kupita kwenye miti ile usiku. Nililiacha eneo la nyumbani, nikaingia sehemu iliyokuwa na kiza cha kutisha. Kutokana na kiza na miti mingi, hakika palikuwa panatisha sana kwa muda ule japo mchana tulikuwa tukicheza kwenye miembe ile bila woga.

Kama kwenda kwa hiyari yangu nisingekwenda hata kwa bunduki, lakini kutokana na hatari iliyokuwa mbele yangu sikutishika na lolote. Nilitafuta mti mmoja ambao haukuwa mrefu sana na kupanda juu hadi kwenye sehemu iliyokuwa na miti imekaa kama Y, sehemu ile niliiona inanifaa sana kwa kujilaza hata kama usingizi ungenipitia nisingeanguka.
Kutokana na kutaka kuokoa maisha yangu nilikuwa na ujasiri wa ajabu licha ya kiza kizito na ubaridi uliopepea majani kama vile kuna mtu.
Nilitakiwa kuwa na moyo wa chuma. Usingizi ni kitu cha ajabu, pamoja na hofu nzito iliyokuwa imenitawala, usingizi ulinipitia bila kujielewa.

Sauti ya watu kubishana chini ya mti ilinishtua kwenye usingizi wa mang’amung’amu. Baada ya kuwasikiliza vizuri niligundua ni wachawi waliokuja kunifuata nyumbani na kunikosa. Nilimsikia mmoja akisema. “Jamani atakuwa wapi?” “Hata sisi hatuelewi,” mwingine alijibu.
“We Helena si ulisema umechukua ile ngozi?”

“Ndiyo mama,” Helena hapohapo nikaitambua sauti yake. “Sasa mbona haonekani?” “Sijui.” “Sasa watakuwa wapi?” “Jamani mtoto yule anataka kutuzidi watu wazima?” “Lakini yote mmeyataka wenyewe , si watoto wenu wamemfundisha ujanja wetu!” “Kwani Sabina yupo wapi?” “Tumemuacha kwao. Tulimpumzisha safari za hatari kutokana na kusema alikuwa amepoteza ngozi yake kumbe alimpa Shija; mtoto mbaya sana yule na lazima tumpe adhabu kali.”

“Sasa jamani atakuwa wapi, kumbukeni tukishindwa kuitumia nafasi hii, itakuwa tunazidi kujiweka sehemu mbaya.” “Tulitaka leo tukimpata tumle nyama. Mzee Manoni sijui ana ajenda gani na huyu mtoto ambaye mwisho wa siku atatuvua nguo hadharani?” “Lakini nilisikia akisema kuwa alimkataza kuitoa siri yoyote kuhusu sisi.”

“Huko ni kujidanganya, hivi mtu amuone kaka yake akiliwa nyama asiseme kitu chochote kwa wazazi wake!” “Ataanzia wapi kusema, na nani atamkubalia kuwa ameshuhudia kaka yake akiliwa nyama.”
“Jamani yote si muhimu zaidi ya kumpata Shija,” mmoja alibadili mada. “Jamani, inawezekana Sabina amemficha kwao,” mchangiaji nilimfahamu kwa sauti alikuwa Helena.

Ilionesha jinsi gani Helena alivyokuwa adui mkubwa, baada ya kauli ile niliwasikia wakimuunga mkono. “Itakuwa kweli, lazima Sabina atakuwa anajua Shija yupo wapi.” “Na kweli, tusipoteze muda, maana Manoni anaweza kuwa anamaliza kikao muda huu na kuanza kurudi.”
Walitimka kuelekea nyumbani kwao Sabina kunitafuta.

Nilitulia juu ya mti hata kupumua kwangu nilipumua kwa taratibu sana kuogopa kusikika. Kila muda ulioongezeka mbele yangu mambo yalizidi kuwa magumu na kuzidi kuniweka katika hali mbaya. Nilijiuliza kama wakinikosa kwa kina Sabina watafanya nini, na mimi niliapa kupambazukiwa juu ya mti. Baada ya kuondoka nilikaa zaidi ya robo saa ndipo nilipoziruhusu pumzi zangu kutoka bila kuzibana. Nilimuomba Mungu ili kuche haraka niweze kwenda kwa mzee Manoni kumueleza ukweli.



INAENDELEA....
 
43--Nilijificha mpaka kijua kilipokuwa kikali ndipo niliporudi nyumbani, sikumkuta mtu palikuwa kimya. Niliingia ndani, kutokana na uchovu nilijitupa kitandani na usingizi mzito ulinipitia. Nikiwa kama nipo ndotoni niliota Helena akinilisha kitu vyeusi ambavyo vilikuwa na uchungu wa ajabu. Niliposhtuka nilijikuta nimelala kitandani lakini midomo ilikuwa michungu sana, niliamka na kusukutua kuondoa uchungu.

Baada ya kusukutua nilijiuliza ndoto ile ilikuwa na maana gani na kwa nini nimeota ninalishwa vitu vichungu na Helena na nilipoamka nilijikuta midomo ikiwa michungu? Nilijikuta nikikaa kitako na kujiuliza ile ilikuwa ni ndoto au kweli na kama ni kweli nia yake ilikuwa nini?

Nikiwa nimekaa kitako nilishtushwa na sauti ya Sabina aliyekuwa akiita kwa sauti ya juu. “Shija...Shija.” “Naam, Sabina.” “Mmh, siamini upo salama?” Sabina alisema huku akiingia chumbani kwangu katika sare ya shule na kujiuliza muda ule ni saa ngapi.

“Sabina kwanza muda huu ni saa ngapi?” “Saa tano asubuhi nimetoroka shule baada ya kutokewa na kasheshe nzito kuwa nimekuficha na kujiuliza kama ngozi huna utakuwa umejificha wapi?” “Kwa vipi Sabina?” “Shija jana usiku umelala wapi?” “Kwani vipi mbona unaniuliza hivyo ?” “Nijibu swali, Shija ngozi ipo wapi?”

Nilishindwa kumjibu nilibakia nimeinama chini. “Shija unanizunguka kwa faida yako?” “Sio hivyo Sabina.” “Sio hivyo ngozi yangu iko wapi?” Sabina aliniuliza kwa sauti kali kidogo. “Hata sijui nani kaichukua, jana baada ya kuachana na wewe niliporudi ndani sikuikuta nilitafuta zaidi ya saa tatu lakini sikuiona.” “Na usiku ulilala wapi?” Nilimueleza ilivyokuwa baada ya kupoteza ngozi na wazo la kwenda kulala juu ya mti na mazungumzo waliyokuwa wakizungumza wachawi mpaka walipofunga safari kumfuata kumuulizia kuhusu mimi.

Sabina baada ya kunisikiliza alishusha pumzi na kusema kwa sauti ya masikitiko. “Shija ilikuwaje Helena akaipata ile ngozi?” “Helena ndiye aliyeichukua ile ngozi?”
nilijifanya kushtuka ili kujifanya sijui lolote. “Ukweli ndio huo Helena kaichukua na kuipeleka kwa wachawi ili kuhakikisha unakamatwa na kuliwa nyama kama nilivyokueleza .
Shija unajua kabisa Helena kaichukua ngozi, alijuaje umeificha chini ya godoro?” “Ooh, nimekumbuka kuna siku kabla ya kunieleza kuwa niwe naye mbali
alinishauri niiweke chini ya godoro.” “Si unaona kwa nini ulimwambia? Shija kwa nini unanizunguka najitoa kwa ajili yako lakini unaona kazi bure,” Sabina alisema huku machozi ya uchungu yakimtoka .

“Lakini Sabina ukaribu wangu na Helena ni wewe ndiye uliyeuleta na kunitambulisha kama rafiki yako mkubwa. Pia kunisaidia kumtorosha kaka yangu toka kwao ilinipa imani.” “Shija kama nilivyokueleza Helena si mtu mzuri jiepushe naye ni mtu mbaya sana.
Na dhamira yangu ipo pale pale kwa kitendo alichonifanyia sitamsamehe maisha.” “Dhamira gani tena?” “Nakuhakikishia lazima nitamuua Helena na wiki haiishi lazima nimuue.”

“Sabina kwa nini usimuache hujui kuua ni kosa kubwa sana?” “Shija wewe ni mtu wa aina gani usiyejihurumia, kama usingepata akili ya ziada ya kwenda kulala juu ya mti si watu wangekula nyama? Bado mtu huyo unamuonea huruma? Hata useme nini lazima nimuue Helena kwa mkono wangu.”

“Sabina si watajua kuwa umemuua wewe .” “Potelea mbali na wajue, kumbuka sasa hivi nina wakati mgumu. naonekana msaliti hata mpango wa kumtorosha kaka yako mzigo kanitupia mimi ili tu nionekane nina makosa.
Kama mama yangu asingekuwa mzito kwenye chama cha wachawi ningefanywa kitu kibaya.

“Nilimsikia mama akiwaeleza kwamba mtu atakayenigusa atamjua yeye ni nani?”
Wakati nazungumza na Sabina tumbo lilianza kunikata, nilishika tumbo na kuanza kupiga kelele za maumivu.
“Sabina nakufa tumbo linanikata,” nilisema kwa maumivu huku nimeinama.
“Umefanya nini tena?” Sabina alishtuka. “Hata sijafanya kitu.” “Umekula nini?” ”Viazi na uji.” ”Ha! Shija mbona ulimi wako mweusi?” Sabina alishtuka kutokana na kugundua ulimi wangu ni mweusi kama nimetafuna mkaa.

“Sabina nimeota nalishwa vitu vyeusi vichungu na Helena kwenye ndoto nilipoamka nilikuta midomo michungu hata mate nilipotema yalikuwa meusi.”
“Hebu,” Sabina alininusa mdomoni. “Mungu wangu! Unaona sasa.” Sabina bila kunisaidia nilipoanguka chini aliniacha na kutimua mbio bila kujua anakwenda wapi.
Nilibaki nimelala chini huku nikiugulia tumbo ambalo lilikuwa likinikata kama kuna mtu anaukata utumbo kwa ndani. Nilianza kuhisi kizunguzungu na kiza kizito mbele yangu. Mauti niliyaona mbele yangu huku nikishangaa kwa Sabina kuniacha bila kunipa msaada wowote .

Niliamini kabisa alikuwa amekasirika kutokana na kumdanganya, na uzembe wa kuipoteza ngozi yake muhimu.
Nilijiona nikifa, nilijilaumu kwa ukimya wangu wa kuwaficha wazazi wangu na mwisho wa siku nilikuwa nakufa najiona.


INAENDELEA....
 
44--Nikiwa nimeanza kupoteza uwezo wa kusikia na kuona, kwa bali nilisikia sauti ya kilio cha Sabina. Kwa kweli nilichokisikia kilikuwa kilio lakini maneno aliyokuwa akisema sikuyasikia .
Niliposhtuka nilijikuta nimelala kitandani pembeni yangu alikuwa Sabina ambaye alikuwa bado katika vazi la shule.

Uso wake ulikuwa umetawaliwa na michirizi ya machozi, nilipofumbua macho alishtuka. “Shija!” “Eeh.” “Unajikiaje?” Kabla sijamjibu nilisikia kichefuchefu kilichonifanya ninyanyuke kutoka nje, lakini sikuweza. Niliyumba, mwili haukuwa na nguvu. Sabina alinisaidia kunitoa nje kwenda kutapika.

Nilipofika nje nilitapika vitu vyeusi vya ajabu hata sikujua nilikula saa ngapi na vilipitia wapi. Baada ya kutapika nilianza kuharisha kinyesi cheusi. Katika maisha yangu sitamsahau Sabina kwani alinihudumia kwa hatua zote baada ya kunisafisha alinikorogea uji. Kilichonisaidia ni kwamba muda ule wakati wazazi wangu walikuwa bado wapo shamba na muda wao wa kurudi ulikuwa bado.

Sabina alinishughulikia kwa kuninywesha uji wa dawa ya kutoa sumu niliyolishwa na Helena nikiwa nimelala. Baada ya kuninyesha uji wa dawa aliniomba nilale ila aliniomba niwaeleze wazazi wangu ibakie siri. Nilikubaliana naye muda nao ulikuwa umekwenda sana aliwahi nyumbani kwao na mimi kupitiwa usingizi mzito.

Nilishtushwa na sauti ya baba ambaye alishtushwa kwa kunikuta nikivuja jasho mwili mzima mpaka sehemu niliyokuwa nimelala ilikuwa imelowa.
“Shija unaumwa?” baba aliniuliza huku akiweka mkono wake kichwani kwangu kupima joto la mwili.

Nilipojiangalia nilijikuta nikivuja jasho mwili mzima, nguvu zilikuwa kwa mbali. Lakini niliweza kutembea mwenyewe bila msaada wa mtu.
Niliangalia nje na kubaini kuingia kwa kiza kutokana na muda kuwa umekwenda sana.

“Vipi mbona upo hivi?” baba aliniuliza. “Sijisikii vizuri.” “Tatizo nini?” “Labda malaria.” “Asubuhi ulienda wapi?” “Nilikwenda shule, kumbe niliondoka muda bado na kujikuta nimewahi shule peke yangu,
” ilibidi nitunge uongo ili kuepusha maswali ambayo niliamini nisingeyajibu. Kutokana na kutokwa na jasho jingi nilikwenda kuoga ambapo kidogo hali yangu ilibadilika na kujisikia nikipigwa na hewa safi iliyoupa nguvu mwili wangu.
Baada ya kutoka kuoga baba aliniletea dawa ya miti shamba ambayo tulikuwa tukiitumia pale mtu aliposhikwa na malaria.
Baada ya kunywa dawa njaa kali ilikuwa imenishika, bahati nzuri kulikuwa na viazi vilivyo bakia mchana; nilivila ili kupunguza njaa na kusubiri chakula cha usiku.

Nilipomaliza kula nilirudi tena kitandani na usingizi haukuchelewa kunichukua.
Nilishtushwa chakula kilipokuwa tayari, nikala na kurudi tena kulala. Kutokana na mwili kuwa umechoka nilipolala usingizi ulinichukua tena.
Katikati ya usiku nilishtushwa na sauti za vishindo vya watu nje ya nyumba yetu, nilijikuta nikiitafuta ngozi yangu chini ya godoro lakini nilikumbuka ilichukuliwa na Helena. Nilijikuta nachanganyikiwa .

Niliamini ujio ule ulikuwa wa kuja kunichukua baada ya usiku wa jana yake kunikosa. Akili ya haraka ilikuwa ni kupiga kelele ili baba aamke, lakini kabla sijafanya vile ukuta ulipasuka na kuingia watu wanne ambao walinikamata huku wakisema. “Leo huna ujanja.”

Niliwekewa kipande cha mti mdomoni kilichofungwa na kamba na kuwa kama nimekiuma na meno.
Sikuwa na ujanja nilijua kweli nimepatikana. Nilibebwa juujuu na kutolewa nje ambako kulikuwa na mbalamwezi kama mchana.

Nje kulikuwa na watu zaidi ya kumi na tano, baada ya kuniona walilipuka kwa shangwe, niliamini baada ya kunitafuta kwa udi na uvumba kwa muda mrefu hatimaye walinipata.
Nilimuomba Mungu aniepushe na kifo kile cha kuliwa nyama, japo kifo ni haki ya kila kiumbe, lakini kifo changu nilikiona ni kibaya kwa wanadamu wenzangu kunigeuza asusa. Safari ya kuingia porini ilianza nilijua ilikuwa ya kwenda kwenye mti wa kukutania ili wanigawane nyama.

Sikuwa na jinsi kwani mti uliowekwa mdomoni ilinifanya nishindwe hata kumeza mate. Nilijiona nitakufa hata kabla ya kugawanwa nyama. Baada ya kwenda mwendo mrefu kidogo, ghafla nilisikia kitu kama bakora zikitandikwa na watu walipiga kelele.


INAENDELEA...
 
45--Walionibeba walinitupa chini baada ya kushindwa kuvumilia ukali wa bakora ambazo zilipigwa kwa nguvu na sauti yake ilipasua anga. Nilipatwa na mshtuko na kujiuliza nini kimetokea, ghafla niliwaona wote waliokuwa wamenibeba wakipiga magoti kama wanaomba msamaha.
Sikuamini macho yangu kumuona mzee Manoni akiwa ameshikilia bakora ya mkia wa taa. Kwa sauti ya hasira aliunguruma na kusema; “Tumekuwa tunazungukana, sasa nasema hivi kila aliyeshiriki kutaka kutoa uhai wa kijana huyu ataleta mtoto wake mmoja aliwe nyama kama adhabu ya usaliti wenu.

Tumekubaliana leo tupumzike kumbe mlikuwa na yenu ya kunizunguka?” “Tusamehe mkuu.” “Siwezi kuwasamehe kwa kunizunguka kila siku mna kwenda kinyume na maagizo, sasa mama Helena na wenzako nataka mtu mmoja kila ukoo ili muone raha ya kutaka kula nyama za wenzenu.”

“Tusamehe mkuu haturudii tena.” “Natoa onyo la mwisho kijana huyu akifa au akipotea kwenye mazingira ya kutatanisha mtanijua Manoni ni mtu wa aina gani, uchawi niwafundishe mwenyewe leo mtake kunizidi akili! Chonde chonde muogopeni kijana huyu kama ukoma, haya poteeni.”

Baada ya kusema vile wote walikurupuka na kutimua mbio kwa kila mmoja kupitia njia yake.
Mzee Manoni alinifungua kamba na kukitoa kipande cha mti. Baada ya kukitoa kipande hicho nilijikuta nikipata shida kumeza mate kutokana kutomeza mate kwa muda mrefu na koo kukauka.
Mzee Manoni aliiona hali ile, alichukua majani pembeni aliyoyafikicha na kunikamulia kidogo mdomoni ambapo koo lililainika.

Alikiangalia kile kijiti kisha alisema kwa sauti ya chini. “Pole sana, watu hawa walikuwa wamedhamiria kukufanya nyama, kijiti hiki hutumika kumwekea mtu anayekwenda kuliwa nyama.
Ningechelewa kidogo wangekupigilia msumari kwenye utosi na juu ya sikio kabla ya kukufikisha kilingeni kwa kukugawana nyama.”

“Asante mzee wangu.”“Nakuhakikishia kila atakayekugusa nitamfanya kitu kibaya.”

Baada ya kusema vile alinirudisha hadi nyumbani na kuniingiza chumbani kwangu, aliniacha nilale huku akinisisitiza kuwa nisimwambie mtu kila kitu kilichotokea.
Nilijikuta nikijiuliza kama asingetokea mzee Manoni si nilikuwa naliwa nyama?

Nilijiuliza mzee Manoni alijuaje kama nimechukuliwa kwenda kuliwa nyama, lakini niliamini huenda ni uwezo wake wa kichawi ndiyo uliomfanya agundue njama za kutaka kunila nyama.
Nilimshukuru Mungu usingizi ulinipitia mpaka nilipogongewa na baba asubuhi kutaka kujua hali yangu.

“Shija umeamkaje baba?” “Sijambo baba, kama hali itaendelea hivi kesho nitaenda shule.” “Basi pumzika usiende popote sawa baba.”
“Sawa baba.” Mama naye alinijulia hali ikiwa pamoja na kunipa maelekezo ya chakula na dawa ya malaria aliyonipa jana akiamini kutokwa na jasho ilikuwa na malaria kumbe dawa aliyonipa Sabina ilikuwa ikitoa sumu niliyolishwa ndotoni na Helena.

Baada ya maandalizi yote, waliondoka na kwenda shambani na kuniacha na mdogo wangu wa kike ambaye naye siku ile hakwenda shule kutokana na kutojisikia vizuri.
Kwa vile bado mwili ulikuwa na mchovu nilirudi ndani kulala mpaka niliposhtuliwa na Sabina. Kama kawaida alikuwa katika sare ya shule, aliponikuta nimejilaza alinitazama kwa jicho la huruma. “Vipi Sabina?” “Mmh kawaida, pole sana.” ‘Asante.” “Bila mzee Manoni jana ulikuwa unaliwa nyama.”

“Umejuaje?” “Hivi unafikiri bila kumfuata mzee Manoni ungepona.” “Sabina! Wewe ndiye uliyemfuata mzee Manoni?” “Shija mpango wao wote wa kuahirisha kikao cha kila siku cha wachawi ili kumfanya mzee Manoni apumzike na wao kumzunguka ili wale nyama yaako niliungundua.

Walipoanza safari ya kuja kukuchukua nilikimbilia kwa mzee Manoni. “Huwezi kuamini nilipomueleza kilichotaka kufanywa na kundi la wale wachawi kukula nyama alishtuka sana. Nilimueleza na muda ule wamekufuata ili wakakule nyama, ndipo tulipoondoka na mzee Manoni kukufuatilia na kukuona amekubeba wakikupeleka eneo ambalo wangekula nyama yako.

“Kwanza walituchenga njia, lakini tulipita njia nyingine kuwahi eneo ambalo hutumia kutoa uhai wa mtu na kumpigilia msumari au kipande cha mti utosini na juu ya sikio kama ishara kuwa umeishakuwa nyama tayari kuliwa. Muda wote nilikuwa na wasiwasi kabla ya kukuona njia nzima nilikuwa nalia huku mzee Manoni akinituliza kuwa hawawezi kukuua.

Nilifurahi kukuona bado wamekubeba japo sikujua upo katika hali gani, mzee Manoni alitoa mkia wake wa taa na kuwasogelea bila wao kumuona mimi nilijificha pembeni ili wasinione na kujua ndiye niliyetoa siri ile.

Alipofika kama ulivyoona aliwatandika bakora kisha aliwapa adhabu. Wakati huo mimi nilikimbilia nyumbani kilichoendelea sikukijua. “Ila elewa mimi na Helena sasa hivi ni chui na paka japo mwalimu Vene alituita kutupatanisha, nilimhakikishia mwalimu sitamsamehe Helena mpaka tunaingia kaburini.”

“Sabina kwa nini umeonesha chuki za wazi kwa adui yako?” “Alichonifanyia siwezi kukifumbia macho, hivi kama wewe ungeliwa nyama angepata faida gani? Lakini kwa nini Shija huruma zimekuzidi kwa nini unamuonea huruma mtu asiyetaka kukuona ukiendelea kuishi?”
“Najua Helena ni mbaya lakini ukitaka kumpata adui yako muoneshe mapenzi.” “Katu sitamuonesha mapenzi na wiki hii haiishi utasikia jambo zito.” “Vipi masomo?” Ilibidi nibadili mazungumzo kwani kila dakika Sabina hasira zilikuwa zikimpanda.


INAENDELEA...
 
46--“Shule safi, vipi mdogo wako leo hakwenda shule?” “Hajisikii vizuri” “Na wewe vipi unasendelea?” “Kidogo sijambo kesho naweza kuja shule”
“Njoo bwana si unajua mtihani umekaribia.” “Nitakuja usiwe na wasi, lakini Sabina sijui nilikulipe nini umeokoa maisha yangu kila kukicha” “Ni kweli, lakini vita ni nzito kama unaweza ungekwenda kusomea mjini kwa mjomba wako.”

“Sabina tumechelewa kwa sasa siwezi kuhama zaidi ya kuvumilia mpaka nimalize mtihani.” “Shija pamoja na jitihada zangu wameanza kunishinda na mwisho wa siku watafanikiwa dhamira “Basi nikimaliza mtihani nitakwenda kusomea kwa mjomba, kule wapo ndugu zangu wawili mjomba aliwachukua.”

“Vipi na dawa unaendelea kutumia?” “Namalizia usiku.” “Tumia tuangalie, uchawi aliokulisha ulikuwa unakukausha.” “Mungu wangu.” “Mungu wangu? Ujue Helena alivyonyoka kwanza urafiki wetu unatokana na uchawi si wa moyoni.” “Sabina sina cha kukulipa.”
“Nataka tukiwa wakubwa unioe.” “Kwanza naomba tusome kwa bidii na yote ninayokuelekeza kwenye masomo yazingatie ili ikiwezekana uwe mmoja wa wanafunzi watakaofaulu kwenda kidato cha kwanza.”

“Lakini Shija kwani siku hizi darasani unanionaje?” “Kweli unajitahidi si kama mwanzo.” Tokea siku ile niliishi kwa amani sikuguswa wala kutokewa na mambo ya mauzauza. Darasani Helena aliniogopa hata kunitazama alishindwa, lakini sikutaka kumuuliza chochote kutokana na ubaya wake.

Sabina alinieleza jinsi walivyo maadui wakubwa na Helena na kunieleza alivyokusudia kumfanyia kitu cha kuwaacha watu midomo wazi. Sikutaka kumkataza kutokana na kuonekana kunitetea mimi kuliko uhai wake.

Siku moja jioni baada ya kutawanyika wanafunzi nilishangaa kumuona Sabina akibakia shule, katika kumbukumbu zangu Helena alitoka mapema baada ya kuitwa na mwalimu Vene. “Sabina twende zetu.”
“Shija tangulia.” “Hapana Sabina wawili ni wawili .” “Shija nielewe we tangulia kwa leo.” “Au umepata rafiki mwingine?” “Shija nakuomba uwe muelewa mengi tutaongeza kesho kama Mungu atatufikisha salama.”

“Kwani kuna nini?” “Shija tutazungumza kesho mpenzi wangu.”
“Kama umepewa adhabu niambie tuifanye wote.” “Hata ya viboko?” Sabina alinitania hapo kidogo alitabasamu kwa mbali.

“Nipo tayari Sabina hata nichapwe peke yangu viboko vyote .” “Asante kwa kunijali ila nakuomba kwa leo tangulia ila kesho utajua kila kitu sababu ya mimi kuchelewa kuondoka.”
“Sikutaka kumlazimisha, niliondoka zangu kurudi nyumbani huku nikishangaa hali aliyokuwa nayo Sabina toka nilipomjua sikuwahi kumuona kwenye hali ile.

Siku ya pili nilishangaa kutomuona Sabina wala Helena darasani, nilijuliza sana nini kimetokea hasa baada ya Sabina kuchelewa kutoka shuleni pia kuwa katika hali isiyo ya kawaida. Tukiwa darasani nilishangaa kuona gari la polisi likija shuleni. Baada ya gari kusimama polisi mwenye sale na cheo cha nyota moja aliingia kwenye ofisi ya mwalimu mkuu.

Haikuwa kawaida polisi kuja shule kutokana na kuwa mbali na tunapoishi.
Ofisi za polisi zilikuwa katikati ya mji na sisi kwenda mjini kwa baiskeli tulikuwa tunatumia nusu saa.
Kutokana na ushamba wa wanafunzi tuliwashangaa polisi waliokuja shule. Baada ya muda alikuja mwalimu darasani na kuniita. “Shija.” “Naam, mwalimu.” “Njoo mara moja ofisi ya mwalimu mkuu.”

Ujumbe ule ulinishtua, nilijuliza naitwa ofisini kwa mwalimu mkuu ambako ndipo alipoingia polisi, kuna nini? Katika maisha yangu yote tulifundishwa polisi hukamata wahalifu. Nilijiuliza nimekosa nini? Nilikwenda huku natetemeka. Nilipoingia darasani mwalimu mkuu alisema: “Huyu ndiye Shija,”

“Shija hujambo?” askari alinisalimia. “Sijambo,
shikamoo!” “Marahaba.” “Shija unatakiwa kituoni mara moja.” “Ha! Mwalimu nimefanya nini?” “Shija usiwe na wasi, wewe ni rafiki yangu.”
Askari alisimama na kunishika mkono na kutoka naye hadi kwenye gari lao Land Rover 110. Nilipandishwa kwenye gari; kilichonipa moyo kilikuwa baada ya kumuona mwalimu mkuu naye tunaongozana naye.

Baada ya mwalimu mkuu kupanda, safari ya kurudi mjini iliiva. Ndani ya gari nilijawa na mawazo mengi toka nizaliwe sijawahi kupelekwa polisi na anayepelekwa polisi ni mhalifu. Lakini sikutaka kuhoji sana baada ya kuongozana na mwalimu mkuu. Safari yetu ilitumia robo saa kufika kituo cha polisi.


INAENDELEA....
 
47--Baada ya kufikishwa nilitelemshwa peke yangu, lakini mwalimu aliondoka na baadhi ya askari kwenye gari tulilokuja nalo. Askari niliyetoka naye ofisini ndiye niliyeteremka naye na kuingia polisi.
Nilijiuliza mbona tumeteremka wawili wengine wameondoka na gari akiwemo mwalimu mkuu?

Baada ya kuingia ofisini niliamrishwa kukaa kwenye kiti, mbele kulikuwa na meza kubwa na nyuma yake kulikuwa na kochi refu kama kiti.
Baada ya kuketi polisi alizunguka upande wa pili na kuketi kwenye kiti chake.
Kabla ya kuzungumza alifunua faili moja ambalo alisoma kwa muda kisha alinyanyua kichwa chake na kusema:
“Wewe ndiye unayeitwa Shija Matulanya?” “Ndi..ndi..yo Mkuu.” “Unasoma darasa la ngapi?” “La saba.” “Unamjua Sabina?” “Ndiyo.”

“Helena?”
“Ndiyo.” “Unawajua vipi watu hawa?”

“Kama wanafunzi wenzangu.” “Zaidi ya hapo?” “Sina zaidi ya hapo.” ”Nikikuambia wale ni wapenzi wako na ni utovu wa nidhamu kujihusisha na mapenzi ukiwa bado mwanafunzi utakataa?”
“Nani, mimi?” swali lile lilinichanganya na kujiuliza kama wapenzi wangu kuna sababu gani ya kuletwa kuhojiwa polisi.

“Humu ndani tumo wangapi?” “Wawili.” “Sasa hapa nazungumza na nani?” “ Na mimi.” “Haya nijibu.” “Si kweli.” “Si kweli nini?” “Sina uhusiano na yeyote .” “Nikiwaita hapa mbele yako wakakiri kuwa wewe ndiye mpenzi wao utasemaje?”

Swali lile lilinifanya niiname chini kwa vile ilionesha labda Sabina ametoa siri yetu, hata hivyo ,
nisingekuwa tayari kukubali kuwa na uhusiano na Sabina kutokana na kuwa mwanafunzi na kosa lile lazima ufukuzwe shule.
“Shija.” “Naam.” “Una taarifa gani kuhusu wapenzi wako?” Sikumjibu neno nilikaa kimya kwa vile swali lile lilikuwa gumu kujibu kwa vile sikujua chochote kuhusiana na wasichana wale, baada ya kuona kimya kimezidi aliniuliza swali jingine: “Unajua nini kuhusiana na ugomvi wa Sabina na Helena?” “Sijui chochote.” “Jana uliachana nao saa ngapi?” Nilitulia kuvuta kumbukumbu na kukumbuka Sabina kumuacha shuleni, ila Helena toka alipoitwa na mwalimu Vene sikumuona mpaka naondoka. “Sabina nilimuacha shuleni ila Helena toka alipoitwa na mwalimu sikumuona mpaka naondoka.” “Sabina ulimuacha anafanya nini?” ”Sikujua alikuwa anafanya nini, tuna kawaida ya kuongozana kila siku tukitoka shule, lakini jana nilipomfuata aliniambia nitangulie.” “Baada ya hapo?” “Nilikwenda nyumbani.” ”Ulipofika shuleni umepata taarifa gani kuhusu wao?” “Sijapata taarifa yoyote ,” maswali yale yalizidi kuniweka njia panda na kujiuliza kuna nini? “Leo shule umewaona?” “Hata mimi nashangaa leo sijawaona.” “Unajua kuna mauaji yametokea.” “Mauaji?” nilishtuka. “Ndiyo.” “Mungu wangu mauaji ya nani?” “Ya Helena.” ‘Helenaaaa?” “Ndiyo na sababu ni wewe . Jana jioni Sabina kampiga Helena na kitu kigumu kichwani na kumsababishia hali mbaya sana.” Kauli ile ilinifungua macho na kujua kumbe kubaki shule Sabina alikuwa na maana yake. Moyoni niliamini wasichana wale kutokana na kazi ya uchawi wamekuwa na mioyo migumu. Mkuu wa upelelezi alinishtua nilipokuwa nimepigwa bumbuwazi. “Shija.” “Na..a..m.”

“Kwa taarifa yako wewe ndiye utakayesaidia upelelezi baada ya kutajwa na Sabina kuwa sababu ya ugomvi uliosababisha hali mbaya ya Helena ambaye kwa sasa amehamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Bugando. Sabina anashikiliwa na polisi na wewe utasaidia polisi mpaka hapo yatakapopatikana maelezo mengine.”

Kauli ile ilinifanya niangue kilio cha juu mlemle ofisini wakati huo askari alinifuata na kunipeleka kwenye chumba kilichokuwa na mtoto mmoja.
Niliendelea kulia huku nikijua nitafungwa kwa kosa lisilokuwa langu, kijana niliyemkuta mle ndani aliniomba nisimpigie kelele kwa vile alikuwa akitaka kulala. Sauti yake ya kitisho ilinifanya ninyamaze na kulilia moyoni.

Moyoni nilijawa na maswali na kujiuliza Sabina yupo wapi? Na kama Helena atafariki itakuwaje?
Nilikuwa nafahamu kila anayeua uhukumiwa kunyongwa nilijiuliza kama wanasema chanzo ni mimi lazima na mimi nitanyongwa .
Nilijikuta nikilia tena kwa sauti ya chini kuogopa kumuamsha mwenzangu aliyekuwa amelala pembeni yangu.

Nikiwa bado kwenye hofu kuu ya kunyongwa kama Helena atakufa, mlango ulifunguliwa na askari aliyeniingiza mule chumbani aliniita. “Shija.” “Naam.” “Njoo.”


INAENDELEA....
 
48--Nilipotoka nje nilishangaa kumkuta baba na mama ilionekana hata nguo zao za kulimia hawakubadili. “Shija,” mama aliniita.
“Naam mama.” “Pole sana.”
“Asante.” Sikuelewa kilichoendelea zaidi ya kumsikia afisa wa polisi akimwambia baba. “Kesho mumlete asubuhi.” “Sawa Mkuu.”

Baada ya kusema vile baba alitupakia katika baskeli, mama alikaa nyuma mimi kwenye mgomba. Tulirudi nyumbani njiani sikuambiwa kitu mpaka tulipofika nyumbani.
Baada ya kufika kabla ya kuingia ndani nilifanyiwa tambiko dogo kisha nilivua nguo za shule nilizoingia nazo mahabusu na kwenda kuoga.

Nilipotoka kuoga nguo zangu zililowekwa kwenye maji ili kuondoa nuksi, siku zote ilifahamika kama nuksi kwa mtu kuingizwa polisi au jela.
Tambiko lile fupi lilikuwa kama kuisafisha nuksi iliyonipata isirudie tena au kumpata mtu yoyote ndani ya familia yetu.

Tambiko dogo lilipokamilika niliruhusiwa kuingia ndani, baada ya muda niliitwa na wazazi wangu kutaka kujua kisa na mkasa na walichoelezwa ni kweli.
“Shija unajua sababu ya wewe kupelekwa polisi?”
“Ndiyo.” “Sababu gani?” “Eti wanasema kuwa Sabina na Helena ni wapenzi wangu.” “Wanasema kina nani?” “Nimeambiwa na polisi mkubwa.”

“Shija umeambiwa au kuna ukweli?” “Hakuna ukweli wowote juu ya tuhuma hizo.” “Mbona kuna tetesi Sabina huwa anaonekana hapa sana.” “Ni kweli, huwa kwa ajili ya masomo tu na si kingine.”
“Iweje aseme wewe ni mpenzi wake?” “Sijui, lakini si kweli.”

“Shija hebu tueleze ukweli sisi ni wazazi wako una mahusiano gani na wasichana wale kufikia hatua ya kutaka kuuana?” “Baba sina uhusiano wowote .”
“Taarifa tulizopewa na mkuu wa polisi alizoambiwa na Sabina kuwa wewe ni mchumba wake na uhusiano wenu ni wa muda mrefu ila Helena ambaye ni shoga yake alitaka kumpindua na kuchukua uamuzi wa kumshikisha adabu.”

“Baba Sabina ni rafiki yangu sana na si mchumba wangu japo huwa tunataniana, kuhusu Helena nilimjua kupitia kwa Sabina. Hakuna kingine juu yangu na wao zaidi ya urafiki.” “Shija mimi baba yako ninajua mengi, Sabina na Helena ni wapenzi wako, lakini chonde usikubali polisi kuwa wale ni wapenzi wako.

Ukikubali umefungwa.” Ajabu baba baada ya kusema vile hakuchukua uamuzi wowote zaidi ya kuendelea na kazi ndogo ndogo za nyumbani. Siku ile kazi ya shamba haikufanyika baada ya kukurupuka walipopata taarifa zangu za kuchukuliwa na polisi.

Kesho yake nilirudishwa polisi tena kwa ajili ya kuendelea na upelelezi wao, hali ya Helena ilikuwa bado mbaya kitu kilichosababisha Sabina aendelee kuwa ndani mpaka pale hali ya Helena ingekuwa katika unafuu.
Siku nilipopelekwa baba ndiye aliyeingia na kuongea na afisa wa polisi kisha alinipitia na kuondoka na mimi kunirudisha nyumbani.

Siku ya pili nikiwa nyumbani peke yangu baada ya baba kwenda shamba na wakati huo shule nilisimamishwa kwa kuchanganya mapenzi na masomo. Nikiwa sina hili wala lile macho yangu hayakuamini kumuona Sabina akija nyumbani.

Bila kujielewa nilijikuta nimenyanyuka na kwenda kumpokea Sabina kwa kumkumbatia. “Ha! Sabina?” “Ndiyo mimi.” “Pole sana.“ “Nikupe pole wewe .” “Siamini ilikuwaje?” “Yaani Shija najilaumu nimefanya kosa la kijinga sana.” “Lakini si nilikuambia uachane wa wazo lile.”

“Sijuitii kumpiga Helena.” “Sasa unajilaumu kwa lipi?” “Kosa nililofanya kumpiga Helena njia wanayopita watu kila mara, kama ingekuwa kwenye majani wangeokota maiti siku ya pili.”
“Sabina huogopi kunyongwa ?” “Bora ninyongwe kuliko kuishi na hasidi kama yule.” “Na mbona umetoka?”
“Nimepewa dhamana.” “Lakini nasikia hali ya Helena ni mbaya?” “Tena naomba afe.”

“Sabina si utanyongwa ?” “Wacha ninyongwe , Shija bado unamuonea huruma Helena mtu aliyetaka kukula nyama?” “Hapana Sabina, nakuonea huruma wewe sitaki nikupoteze.”
“Nataka kukuhakikishia hata Helena akifa sinyongwi wala kufungwa .” “Kwa sababu gani unasema hivyo ?” “Leo siwezi kukueleza tusubiri afe.” “Je akipona?”
“Dhamira yangu ipo palepale lazima nimuue kwa mkono wangu.”


INAENDELEA...
 
49--Baada ya wiki Helena alitoka hospitali akiwa hajambo lakini kichwani alikuwa na bandeji kuziba kidonda ambacho kiliendelea kupona. Siku ya pili toka Helena atoke hospitali kiliitishwa kikao cha shule kuzungumzia kilichotokea walikuwepo wazazi wetu wote na wanakamati ya shule.

Kwa upande wetu tulikuwepo wote Sabina Helena na mimi, kikao kilifanyika kwenye darasa moja. Baada ya wajumbe kutimia mwalimu mkuu alieleza kilichotokea. Kisha alimuomba Helena aeleze sababu ya ugomvi wao, moyo ulinienda mbio na kujiuliza atasema nini ikifika zamu yangu.

Baada ya kusimama aliinama bila kusema kitu. “Helena hebu eleza kilichotokea,” mwalimu mkuu alimuhimiza. “Mwalimu mimi sijui lolote nilishtukia tu napigwa na kitu kizito kichwani hata kujitetea sikuweza mpaka nilipopoteza fahamu.” “Unamjua aliyekupiga?” Mzazi mmoja aliuliza. “Sabina.” “Ulimuona?” “Mama aliniambia.”

“Ina maana hukumuona?” “Ndiyo.” “Unafikiria kwa nini Sabina ambaye ni shoga yako alikupiga?” “Sijui.” “Siyo kwamba mnamgombania Shija?” “Hata siku moja, Shija sina uhusiano naye wa kimapenzi lakini Sabina kwa mdomo wake alinitamkia kuwa Shija ni mpenzi wake.”
“Alikuambia lakini hukuona?
”

‘Nimewaona wakiwa wawili kila baada ya muda wa masomo.” “Unaweza kukaa,” Helena aliruhusiwa kukaa, mimi moyo ulinienda mbio nikijiuliza nitasema nini nikiulizwa. Sabina alinyanyuliwa na kuelezwa naye aseme sababu ya kutaka kumtoa roho mwenzake. Sabina baada ya kusimama naye hakusema neno alibakia kimya akiwa ameinama. “Sabina hebu tueleze sababu ya ugomvi wenu,” mwalimu mkuu alimuhimiza kusema.

“Helena anajua,“ Sabina alijibu kwa ufupi. “Anajua nini?” “Siwezi kukisema hapa ila mwenyewe anajua.” “Tunasikia kwa ajili ya kumgombea Shija?” “Si kweli kuna kitu anakijua Helena awe muwazi na mkweli.” “Sabina usitake kutufanya sisi watoto wenzio tunataka maelezo yako na si ujinga unaotujibu.”

“Sina cha kueleza mkitaka kujua muulizeni Helena,” Sabina alionesha kiburi cha wazi. “Eti Helena unajua nini?” “Mimi sijui lolote.” “Mmh makubwa, Shija na wewe unajua nini kuhusu ugomvi huu?” Swali lilielekezwa kwangu. Kabla ya kujibu nilijipa moyo kuweza kuzungumza kutokana na mapigo ya moyo kunienda kwa kasi.

Baada ya kujipa ujasiri nilisema; “Sijui lolote.”
“Kuna taarifa kwamba muda mwingi huwa mpo karibu na Sabina ni kwa sababu gani?” “Siku za nyuma Sabina na Helena niligombana nao na tulipopatanishwa tulikuwa marafiki kwa kushirikiana katika masomo.” “Lakini mbona tumeambiwa ni mpenzi wako?” “Si kweli.”

Baada ya maelezo yetu sote watatu tulitolewa nje kuwaacha wazazi watujadili, mimi na Sabina tulikaa karibu lakini Helena alikaa mbali wala hakutaka kututazama. Uso wa Sabina ulionesha kujaa hasira na machozi kumtoka tofauti na Helena alikuwa mkavu, niliamini Sabina pamoja na kushiriki mambo ya kichawi lakini moyo wake ulikuwa umejaa utu.

Lakini Helena alikuwa na roho ya kinyama ya kula nyama ya mtu bila huruma. Muda wote tuliokaa nje tulikuwa kimya kila mtu akitafakari lake, baada ya kikao tuliitwa wote ndani kuelezwa kulichojadiliwa.

Uso wa baba ulionesha kuwa na hasira. Lakini mwalimu alimpoza kwa kumueleza; “Mzee Matulanya bado una nafasi ya kupinga hukumu hii?”
“Huu ni upumbavu kugombana wagombane watoto wenu adhabu apewe mtoto wangu.” “Kwa sababu yeye ndiye chanzo.” “Mna uhakika kuwa yeye ndiye chanzo?” “Ndiyo maana nikasema bado una nafasi ya kupinga hukumu hii.”

“Hivi kesi ya nguruwe ukimpelekea nyani unategemea kupata haki? Sasa nawaeleza kesi hii haiishii hapa tutafika mbali. Haiwezekani muone mtihani umekaribia mumsimamishe mwanangu kwa vile ana akili ili asipasi.”
“Mzee Matulanya mbona umefika mbali?” “Sina muda tutajuana muda si mrefu.”

Baba alisema kwa hasira na kunishika mkono kunitoa nje ya darasa huku akiendelea kubwata. Sikutaka kumuuliza kitu lakini kwa mazungumzo yake ya sauti ya juu ilionesha wazi mimi peke yangu ndiye niliyesimamishwa shule kwa ugomvi wa watu wengine.

Njia nzima alikuwa akifoka kwa sauti ya juu, ilikuwa mara ya kwanza kumuona baba akilalama njia nzima kwa sauti ya juu kiasi kile. Nakumbuka siku aliyofoka lakini si sana ilikuwa siku nilipoambiwa kuwa mimi mtoto wa mchawi. Tulipofika nyumbani bado baba alikuwa na hasira.

“Shija nisubiri hapa ngoja nifike shambani mara moja, ila suala hili nitaliamkia asubuhi kwenda mjini kwa mjomba wako.” Baba aliondoka na kuniacha nikiwa njia panda kuhusu hatima yangu ya muda uliobakia wa kufanya mtihani wa taifa wa darasa la saba. Nilijikuta nikiumia moyoni baada ya kuona kuna kila dalili za kukosa kufanya mtihani.

Nilijiuliza walitumia kigezo gani cha ugomvi wa Sabina na Helena kunisimamisha peke yangu. Nilianza kuingiwa na wasiwasi wa ukaribu wangu na Sabina na kuona huenda anatumiwa na wachawi ili kunikwamisha kimasomo kwa kuanzisha ugomvi wa uongo na ukweli ili tu mimi nisimamishwe shule na kukosa mtihani muhimu sana kwangu.

Lakini upande wa pili moyo ulionesha dhamira ya ajabu ya Sabina kuhakikisha nipo salama kwa kujitoa kwa kila kitu juu yangu.
Nilijikuta nikijipinga mwenyewe mawazo yangu juu ya Sabina. Nikiwa bado namtathmini Sabina mara nilimuona akija mbio nyumbani nikashtuka.


Sabina kaja kufanya nini?
ITAENDELEA baadaye nikiwa ktk mapumziko Ya kuuza karanga...
"MAZIMA"
 
kaza buti la 'paukwa pakawa' karibu utapanda daraja. safi sana. hahaha.
 
Nasubiri vitu vizito kutoka kwako mkuu Majigo!

Sent from my BlackBerry 8520 using JamiiForums
 
Last edited by a moderator:
Back
Top Bottom