Mtazamo wangu juu ya neno “SIASA”.
SIASA si HASA ni moja ya maana nyingi za ubatizo usio rasmi wa neno SIASA. Dhana hii na nyingine nyingi za mrengo huu imenipeleka kufikiri maana niitamaniyo juu ya neno SIASA. Sitazungumzia kwanini “SIASA” ilibatizwa kuwa “SI HASA” na majina mengineyo kwa kukwepa mantiki hiyo hiyo ya “SIASA”.
Kabla sijaainisha wazo langu juu ya maana niifikiriayo kwanza kabisa niseme hii sio “SIASA”. Jambo hili limekuwa likinitatiza sana. Iweje jambo lolote likiwa linapatiwa uzito mdogo(mwepesi) ama likiwa halichukuliwi kwa umakini basi watu huomba “SIASA” iwekwe kando na jambo hilo? Mfano utasikia, “jamani tusilete “SIASA” katika mambo ya msingi. Dhana hii ni ya kale na si hapa kwetu tu. Hata Wazungu wana msemo wa “We do not play politics”, wakimaanisha “wapo serious” na kama ni mzaha ama ujanja ujanja basi hutumia msemo “play politics”.
Mambo mengi mfano elimu, ajira, afya, michezo, usalama, imani (Dini), amani, miundo mbinu na mengineyo, yakiwa hayaendi kama itakiwavyo basi sababu kuu ni kwamba mambo hayo yamehusishwa na siasa. Kauli za “Tusifanye siasa katika elimu, ajira, afya, michezo, usalama, imani (Dini), amani miundo mbinu na mengineyo” zimekuwa ni kauli za kawaida na zikimaanisha kwamba “SIASA” ni jambo la mzaha mzaha tu na si kitu cha kuchukuliwa kwa UMAKINI.
“Tuweke SIASA kando” ni kauli iliyonifanya nijiulize, kwani “SIASA” ni nini? Je kauli hii ndio inasababisha baadhi ya watu kutotaka kujihusisha na “SIASA” kwa kuwa ni jambo la “MZAHA”? Sidhani kama MTU aliye elimika, mwenye staha, busara na UTU angependa kuambiwa “ACHA SIASA BWANA”. Ni kauli ya kufedhehesha kidogo. Imekuwa ni kauli ya kitapeli tapeli. Lakini je hii ndio maana halisi ama tuitakayo ya neno “SIASA?” Sitastaajabu hata maoni juu ya wazo hili yakaonekana kuwa ni “SIASA” tu.
Maana ninayoitamani ni “SIASA” iwe ni chombo cha kuleta WAZO juu ya namna ya kupata na kufikia suluhisho juu ya changamoto yoyote ile. Changamoto hiyo iwe ni elimu, ajira, afya, michezo, usalama, imani (Dini), amani, miundo mbinu, misiba, magonjwa, njaa, umasikini na hata SIASA yenyewe.
Kwa mfano, kama Taifa tupo na changamoto ya ajira. Hivyo basi wanasiasa wabuni mbinu mbali mbali za namna ya kutatua changamoto hii na ile mbinu itakayovutia na kupata mashiko ndio ifuatwe katika kufikia suluhisho la tatizo la ajira. Na yeyote mwenye mbinu bora huyo aweze kuitwe “MWANA SIASA”. Tuifanye SIASA kuwa Mzazi bora ili wengi wajivunie kuitwa “WANA SIASA”.
Siasa isiwe ni chombo kinachobuni ama kufikiri jambo fulani ni changamoto na kisha kutafuta suluhisho na wakati mwingine suluhisho huwa “Hewa” kwasababu tu changamoto yenyewe haipo. Siasa isiwe inatunga swali na kutoa jibu, ama kuwa na jibu kisha kutunga swali. Changamoto zetu ndio “SWALI” na “JIBU” sahihi linafahamika, tatizo ni njia ya kufikia “JIBU”. Ni kama Wana wa Israel, walikuwa na jibu la Nchi ya Ahadi, tatizo ilikuwa ni njia ya Kufika Nchi ya Ahadi.
SIASA = Ainisha changamoto(Zinafahamika) + Suluhisho bora la changamoto + Timiza. Hivyo wale wote watakaojipambanua kama “WANA SIASA” itawabidi waweze kuanisha changamoto zilizopo (Umasiki, Maradhi na Ujnga) kisha waje ni suluhisho (Ujamaa na Kujitegemea) halafu pale watakapopewa nafasi watimize.
Changamoto zetu zinafahamika. SIASA yetu iwe ni kutafuta suluhisho la hizo changamoto na kuleta mbele ya wana nchi kisha wananchi wachague SULUHISHO wanaloona ni bora zaidi. Hii itasabishaWANA SIASA kushindana kwa kuja na SULUHISHO bora la MATATIZO ya wananchi. Wanasiasa wapambane dhidi ya “MBINU” ipi bora ya kutufikisha “NCHI” ya ahadi.
Haitoshi tu kusema, nitawaletea maji. Ingekuwa vyema kusema hayo maji yatakujaje. Kwa kufanya hivyo, wana nchi wanaweza kupata upeo wa jinsi ya wao ku – fit in katika njia ya kuleta maji.
CHANGAMOTO zetu ni zile zile, WANA SIASA tupawatie “HOME WORK” ya kutafuta suluhisho kisha kila mmoja aje aeleze atatatuaje changamoto hizo. Hii itasaidia kufuta ile dhana ya “SIASA NI MZAHA” kwa kuwa wana nchi watashiriki katika kujua ipi ndio SIASA nzuri yenye suluhisho bora la changamoto zetu.
Theophani C. Ishika
Mhadhiri Msaaidizi
Chuo Cha Diplomasia
Dar es Salaam.