Nilivyomliza mke wangu kwa siku 366

Nilivyomliza mke wangu kwa siku 366

SEHEMU YA 13

Nilikaa naye hapo kwa muda kama dakika arobaini na tano, nikaamua kuondoka naye hapo na kuelekea Mlimani City. Nilikuwa namuandaa kwa ajili ya kumwambia kile nilichotaka kumwambia. Sikutakiwa kukurupuka, nilitakiwa kumuandaa kukubaliana na kile nilichotaka kumwambia.

Baadaye, nahisi akili yake ilikaa sawa kwani alionekana kuwa mwingi wa furaha na hata hakuwa na shaka yoyote ile juu ya muonekano wangu. Niliamini kwamba ningeshinda lakini swali lililonisumbua kichwani mwangu ni kwa namna gani angelipokea lile nililotaka kumwambia.
Mimi: Isabela mpenzi!
Isabela: Abee laaziz...
Mimi: Nimekuwa nikikupenda sana, na milele nitakupenda mpenzi....
Isabela: Hata mimi pia, ninakupenda mpenzi...uliwasiliana na wazazi wako baada ya juzi?
Mimi: Hapana! Niliamua kukaa kimya kwani najua walikuwa wakinizingua tu.
Isabela: Ilitakiwa uwasiliane nao, wale ni wazazi wako kumbuka, wakati mwingine wanaweza kuonekana kuwa hawapo sawa, unatakiwa kuwaambia walipokosea, lakini mara nyingi nawaamini wazazi hawakosei.
Mimi: Unaamini wazazi hawakosei?
Isabela: Ndiyo! Na mara nyingi hawapendi kumuona mtoto wao akipotea, wanapokwambia fanya hili, wewe fanya hata kama unahisi halipo sawa....
Wakati akizungumza maneno hayo, nilikuwa nikijiuliza kuhusu Salama. Sikuwa nimemwambia kuhusu msichana huyo ambaye nilimwacha nyumbani kwangu. Kama anasema nilitakuwa kukubaliana na wazazi wangu, hii inamaanisha kwamba nikubaliane na suala lao la kunichagulia mke? Hakika ilikuwa ngumu.
Mimi: Isabela....hebu twende sehemu tukatembee kwanza....
Isabela: Sawa...

Tukaondoka na kuelekea ufukweni. Huko kote tulikuwa tukihangaika kwa kuwa bado nilikuwa natafuta pozi la kumwambia kile nilichokuwa nacho moyoni mwangu. Nilitaka kumwambia tulipokuwa Mlimani City lakini nikaona kama ningeharibu mambo, inawezekana angelia sana, hata kumbembeleza ingekuwa ngumu na kwa sababu kulikuwa na watu wengi, hivyo ingekuwa ndivyo sivyo.
 
SEHEMU YA 14

Tulipofika ufukweni, nilitafuta sehemu nzuri na kutulia, muda wote moyo wangu ulikuwa ukijiuliza kama ulikuwa muda sahihi wa kumwambia kile kilichokuwa kikiendelea au nilitakiwa kusubiri. Nilipomwangalia usoni mwake, alionyesha tabasamu pana lakini nikawa nikijisemea kwamba tabasamu hilo lingeweza kupotea ndani ya dakika moja tu kama ningemwambia kilichokuwa kikiendelea nyumbani.

Isabela: Nikwambie kitu mpenzi?
Mimi: Niambie...
Isabela: Kiukweli sina amani kabisa...
Mimi: Kwa nini?
Isabela: Ni kwa sababu haupo kawaida, unanionyeshea tabasamu pana, lakini kila nikikuangalia, bado naona una kitu, hebu niambie tatizo nini.
Mimi: Sina tatizo lolote lile.
Isabela: Kweli?
Mimi: Ndiyo!
Tulizungumza mengi, kama alivyosema kwamba hakuwa na amani, kweli mnilivyomwangalia alionekana kabisa kutokuwa na amani, nikajitahidi kumfurahisha lakini bado hali iliendelea kuwa vilevile. Kumwambia sikutaka kabisa japokuwa nilijua kwamba kuna siku angekuja kujua ukweli na mambo kuharibika zaidi.

Isabela: Leo nataka nikashinde kwako, nilale hukohuko, sirudi nyumbani (Aliniambia maneno yaliyonishtua mno)
Mimi: Unasemaje?
Isabela: Nataka nikalale na wewe leo.
Mimi: Leo?
Isabela: Jamani! Mbona upo hivyo, una nini?
Kiukweli nilichanganyikiwa, kumbuka kwamba Isabela alikuwa mpenzi wangu, niliyemuahidi mambo mengi kitendo cha kumkataza eti kulala kwangu yalikuwa makosa makubwa kwani sikuwahi kufanya kitu kama hicho.

Nilichokifanya ni kumkubalia tu, sikuwa na jinsi, kama kumuona Salama, basi akamuone hukohuko nyumbani lakini si kumkatalia kwenda nyumbani kwangu. Ndani ya gari, nilionekana mpweke, tena uliongezeka zaidi ya mara ya kwanza, nilijitahidi kupiga naye stori lakini wapi, amani haikurudi kabisa moyoni mwangu.
 
SEHEMU YA 15

Hatukuchukua muda mrefu, tukafika nyumbani huku ikiwa ni saa kumi na mbili jioni. Kuingia sebuleni tu, siku hiyo nyumba ilionekana kuwa tofauti kabisa, ilikuwa safi sana na kila kitu kiliwekwa katika mpangilio maalumu, hata Isabela mwenyewe alibaki akishangaa kwani hakuwahi kuiona nyumba ikiwa kwenye usafi wa namna hiyo japokuwa naye alikuwa akijitahidi kufanya usafi.

Isabela: Nyumba yako imekuwa safi sana, umeajiri mfanyakazi?
Mimi: Hapana! Nilisafisha mimi peke yangu... (nilisema huku nikionekana kuwa na wasiwasi)
Isabela: Siamini kama kuna mwanaume anaweza kusafisha nyumba na kuwa safi namna hii.

Ile nyumba ilikuwa ni kama ya Isabela kwani yeye alikuwa mpenzi wangu niliyeishi naye kama mke wangu. Wakati anasifia yote hayo kichwa changu kilikuwa kikifikiria huyo Salama alikuwa wapi, nilikuwa na mchecheto kupita kawaida.

Basi baada ya kukaa dakika chache, akaniambia twende chumbani kupumzika, nikasema sawa huku nikiwa na uhakika kwamba inawezekana Salama amepumzika katika chumba cha wageni. Nikamshika mkono na kwenda naye chumbani, nilipofungua mlango na kuingia ndani, macho yetu yakatua kwa Salama ambaye alikuwa amelala, nguo pembeni, yaani pale kitandani alikuwa na nguo ya ndani tu. Nikausikia moyo wangu ukipiga paaaaaa....!
Mwili ukaninyong’onyea.

Je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 16

Nilitamani nifumbe macho ili nisione kile kilichokuwa kikiendelea, moyo wangu ulinyong’onyea mno na nilitamani kile kilichokuwa kikiendelea kiwe ndoto au kama si ndoto basi ardhi ipasuke na kunimeza.

Moyo wangu ulichanganyikiwa, nilibaki nikimwangalia Salama pale kitandani alipokuwa, mapaja yake yalijaajaa japokuwa hakuwa msafi sana, yaani mafuta ya mjini, maji ya mjini hayakuwa yamemzoea kabisa.

Masikio yangu yalikuwa yakimsikiliza Isabela angesema nini baada ya kuona kitu kama kile, nilishtukia tu akigeuka na kuondoka huku akionekana kukasirika. Sikuwa tayari kumpoteza Isabela wangu, hapohapo na mimi nikamfuata, alipofika sebuleni, nikamshika mkono.

Mimi: Isabela mpenzi subiri.... (nilimwambia)
Isabela: Niache, nimesema niache Denis.... (alisema huku akionekana kuwa na hasira)
Mimi: Let me explain...(Acha nikuelezee)
Isabela: Let me go Denis, let me goooo....(niache niondoke, niache niondokeeee) aliniambia huku akianza kutokwa na machozi.

Halikuwa jambo jepesi, kumuacha Isabela aondoke ilikuwa ni sawa na kushindwa kabisa kumtuliza, nikamvuta kwangu, nikamshika kwa mikono miwili na kumwangalia usoni, alikuwa akilia, moyo wangu uliuma sana, sikuamini kama kuna siku ningekuja kumliza Isabela kiasi kile, sikuamini kama kuna siku angekuwa analia kwa ajili yangu.

Niliyaona maumivu yake makali kupitia macho yake, niliumia pia ila sikuwa na jinsi, nilitakiwa kumwambia kilichokuwa kikiendelea na ajue kabisa kwamba kilichokuwa kimetokea, hakikuwa lengo lake.

Isabela: Yaani unanifanyia hivi Denis, nimekufanya nini mpaka kuamua kuniumiza namna hii? Kwa nini Denis, au kwa sababu ninakupenda, au kwa sababu nilimwambia hakuna mwanaume yeyote zaidi yako...yaani yote hayo niliyokwambia, ahadi zote nilizokuahidi kama kukupenda maisha yangu yote umeona si kitu, unamuingiza mwanamke chumbani kwako, alalie kitanda tunacholalia, Denis, kwa nini? Kwa nini? Kwa nini Denis umeamua kunifanyia hivi? Kwa nini Denis umeamua kuniumiza hivi? (aliniuliza maswali matatu mfululizo)
 
SEHEMU YA 17

Sikumjibu kitu, niliendelea kumshika tu, nilijua hakuwa ametulia, kichwa chake kilichanganyikiwa na muda wote alikuwa akilia kwa uchungu. Niliumia zaidi, maneno yake yalinichoma, nikahisi kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wangu.
Nilishindwa kujitetea, niligundua kwamba huo haukuwa muda mzuri kwangu kumwambia Isabela ukweli kutokana na kile kilichokuwa kikiendelea. Alilia sana, nilibaki kimya, nikamsogeza na kumkumbatia, hakukuwa na kitu kingine cha kufanya zaidi ya hicho.

Mimi: Naomba unisamehe Isabela mpenzi.....(nilimwambia kwa sauti ndogo karibu na sikio lake)
Isabela: Kwa nini umenifanyia hivi Denis, kwa nini umeniumiza hivi?
Mimi: Si lengo langu kukuumiza, naomba futa machozi mpenzi, nitakuelezea kila kitu, naomba tuondoke kwanza.....

Nikamtoa hapo ndani na kuelekea naye nje, huko, nikamuingiza ndani ya gari na kuanza safari ya kuelekea katika lodge moja iliyokuwa maeneo ya Kinondoni. Ndani ya gari, muda wote alikuwa mwenye huzuni tele, bado alikuwa akilia kwa kilio cha kwikwi, macho yake yalivimba mno.

Nilichanganyikiwa mno, kuna kipindi nilishika usukani, nikajisahau kutokana na mawazo mengi niliyokuwa nayo, ghafla, nikaliona gari letu likihama njia na kuelekea mtaroni, nilishtuka, kwa juhudi, nikalidhibiti, likarudi barabarani.
Hatukuchukua muda mrefu, tukafika katika lodge hiyo ambapo nikasimamisha gari na kuingia ndani huku tayari ikiwa ni saa moja usiku. Nikalipia chumba na kuingia, siku hiyo hatukuja humo kufanya ufuska, tulikwenda kwa kuwa nilitaka kuzungumza naye.
Mimi: Kwanza naomba unisamehe mpenzi... (nilimwambia mara baada ya kuingia ndani)
Isabela: Yule ni nani? (aliniuliza huku akiniangalia usoni)
Mimi: Anaitwa Salama.
Isabela: Ni nani yako? (aliniuliza swali jepesi ila lenye ugumu kujibika, nikashusha pumzi nzito)
Isabela: Ni nani yako? (alirudia swali kwa sauti kubwa)
Mimi: Baba aliniambia ni mke wangu.
Isabela: Mke wako?
Mimi: Isabela, nimechanganyikiwa, sijui nifanyeje.
Isabela: Imekuwaje? Mke wako kivipi?
Mimi: Leo wazazi walikuja kutoka kijijini, wamemleta yule mwanamke, wameniambia ni mke wangu, niishi naye kwani baba aliniolea kijijini.
Isabela: Uongo, Denis unanidanganya.
 
SEHEMU YA 18

Mimi: Isabela, nikudanganye ili iweje? Unajua ni jinsi gani tumekuwa katika mapenzi haya kwa kipindi kirefu, nilikuahidi mengi, ya nini nikudanganye? Unakumbuka tulipokuwa kijijini, kila mtu alikuangalia kwa macho ya hasira, ukauliza tatizo nini, sikujua, nilipotoka pale nilimfuata rafiki yangu ambaye akaniambia kwamba wazazi wanataka nimuoe yule msichana.

Isabela: Kwa nini hukuniambia?
Mimi: Ningeanzaje mpenzi? Niliogopa, sikutaka kukuona ukilia, nilifikiri wazazi wangeniambia nimuoe, ningewakatalia, ila walichokifanya, wakaniolea kabisaaaaa.
Isabela: Kwa hiyo wewe ni mume wa mtu?
Mimi: Isabela mpenzi nimechanganyikiwa.
Isabela: Hilo si jibu! Wewe ni mume wa mtu?

Sikujua nijibu nini, sikujua ni kitu gani nilitakiwa nimwambie, nakumbuka kabisa siku hiyo ndiyo ilikuwa mwisho wa mwaka wa 2013, ilikuwa kama disemba 24, siku moja kabla ya sikukuu ya Krismasi.
Isabela: Naomba nikuache na mkeo Denis.
Mimi: Uniache na mke wangu?
Isabela: Ndiyo! Siwezi kutembea na mume wa mtu, naomba nikuache na wewe uniache, nakuomba Denis. Moyo unaniuma sana lakini sina jinsi, naomba tu uendelee na maisha yako.

Sikuamini kile nilichokisikia, eti nimuache Isabela na niendelee na maisha yangu, mbona kilikuwa kitu kisichowezekana, nilimzoea na kumuacha ilikuwa ngumu sana. Nilimwangalia machoni mwake, alionekana kumaanisha alichokisema kwamba mimi na yeye ilikuwa mwisho na hivyo tuachane.
Mimi: Haiwezekani....
Isabela: Niache tu Denis, siwezi kutembea na mume wa mtu (aliposema hayo, akaufungua mlango na kutoka)
Mimi: Isabela...Isabelaaaa....Isabelaaa mpenziiiii.... (niliita lakini hakugeuka)
Alipofika nje akachukua bajaji na kisha kuondoka zake. Hakukuwa na siku ambayo niliumia kama siku hiyo. Kwa mara ya kwanza tangu nifikishe miaka kumi na nane, machozi yakaanza kunibubujika machoni mwangu. Niliumia mno.

Lawama zangu zilikuwa kwa wazazi wangu, ilikuwaje wakubali kuniolea msichana nisiyempenda na wakati huku nyumbani nilikuwa na msichana wangu.
 
SEHEMU YA 19

Niliondoka na kuelekea nyumbani, nilikuwa na mawazo mengi mno, nilipofika, nikashuka garini na kuelekea ndani. Nilikuta chakula kikiwa tayari mezani. Nilitulia kochini huku nikiwa na mawazo lukuki, mara Salama huyo akatokea sebuleni pale, akanisogelea na kuvichukua viatu.

Salama: Pole kwa chovu mume wangu! (aliniambia, nikamkata mjicho huo, nahisi yeye mwenyewe alijishtukia)
Akavichukua na kuvipeleka chumbani, alipoviweka akarudi sebuleni, akaelekea mezani, akachukua sahani na kuweka chakula, akakiweka mboga na kunisogezea meza ya kioo pale sebuleni na kunikaribisha kula.

Hata hamu ya kula sikuwa nayo, nilichokifanya, hapohapo mbele ya macho yake, nikasimama na kuelekea chumbani. Nilipoingia, nikafunga mlango na kujiandaa kulala.

Baada ya dakika kadhaa nikasikia mlango ukianza kugongwa, uligongwa na kugongwa, nikajua yeye tu, nikachuna ndani, sikuufungua, nikajilalia zangu.
Asubuhi ilipofika, nikatoka chumbani, ile kufika sebuleni, tayari nilikuta kila kitu kipo mezani.

Salama: Maji ya moto ya kuoga yapo tayari, pia nimeshakuandalia chai, karibu mume wangu....(aliniambia kwa upole sana)
Nikamshangaa...!! *
*
 
SEHEMU YA 20

Kwa wiki ya kwanza sikutaka kula chakula chake chochote kile kwa kuogopa kulishwa limbwata, bado nililifikiria penzi la msichana aliyeniacha kwenye mataa, Isabela ambaye hakutaka hata kupokea simu zangu na hata nilipokuwa nikimtumia meseji, hakujibu hata moja.

Moyoni niliumia na ndivyo nikaongeza chuki kwa huyu mke wangu Salama. Sikumpenda kabisa, nilichoamua ni kumtesa, kumfanya akose raha ili aondoke kurudi kijijini lakini pamoja na kufanya hivyo kwa wiki nzima, bado siku iliyofuata alinionyeshea mapenzi utadhani jana nilimnunulia gari.

Siku ambayo ndiyo ilikuwa ya mwisho katika mwaka huo, nilitulia sebuleni, sikutaka kuzungumza kitu chochote kile, macho yangu yalikuwa kwenye simu, nilikuwa namtafuta Isabela kwenye simu ili usiku wa siku hiyo tuwe wote na mwaka 2014 ukiingia basi uingie tuwe wote.

Salama alikuwa kimya akiangalia televisheni, tayari alishachukua shuka lake na akawa ameifunika miguu yake pale kochini ambapo kila siku ndipo alipokuwa akilala, sikutaka alale chumbani kwangu kwani kila siku kazi yangu ilikuwa ni kumfungia mlango, asiingie, abaki palepale sebuleni, na alale hapohapo.

Salama: Usiku mwema mume wangu...( aliniambia huku akilivuta shuka pale kochini, wala sikumjibu, mimi nilikuwa bize kumtafuta Isabela kwenye simu)
Mpaka saa sita kamili inaingia, mafataki kuanza kusikika nje, bado Isabela hakutaka kupokea simu yangu, niliumia mno, maumivu niliyokuwa nayo kipindi hicho hayakuweza kuelezeka.

Ilipofika saa 6:30 usiku, simu yake haikuwa ikipatikana tena, ilikuwa imezimwa kitu kilichonifanya niwe na maumivu makali hata zaidi ya kipindi cha nyuma. Kinyonge sana nikasimama na kuanza kuelekea chumbani, nilipofika huko, nikajilaza kitandani huku nikiwa na mawazo lukuki.

Siku hiyo nilipitiwa na usingizi ilipofika saa tisa usiku wa manane kwani muda wote nyuma nilikuwa kwenye mawazo lukuki. Asubuhi ilipofika, niliamka na kitu nilichokikumbuka ni Isabela tu, nikanyong’onyea mno kwani kitu kilichotokea usiku uliopita kiliniumiza mno.
 
SEHEMU YA 21

Nilichokifanya ni kuwasiliana na bosi wangu ofisini, nilimwambia kwamba sikuwa mzima kiafya hivyo anipe ruhusa niende hospitali na nipumzike, nikaruhusiwa huku nikiwa na lengo la siku hiyo kumtafuta Isabela tu.

Kumbuka kwamba sikuwa nikifanya kazi serikalini, ilikuwa ni kampuni ya mtu binafsi so siku kama hiyo ilikuwa ni lazima kwenda ofisini japokuwa si lazima kukaa mpaka jioni, unapomaliza kazi zako, unaruhusiwa kuondoka.
Mimi: Ni lazima nimtafute Isabela, nataka niongee naye, sina raha, sina furaha (nilijisemea)

Nilipanga kumtafuta Isabela siku hiyo, nikaingia bafuni na kujiandaa, nilipomaliza, nikatoka na kuelekea sebuleni. Nikamkuta Salama akiwa amekwishaamka kitambo sana, tena akiwa amefanya usafi na kuniandalia chai.

Salama: Karibu, chai tayari.... (aliniambia kwa sauti ya upole sana)
Mimi: Chai na nini?
Salama: Chai na chapati, nimejitahidi kupika asubuhi sana, sijui utazipenda..... (aliniambia huku uso wake ukiwa kwenye tabasamu pana, hakuamini kama siku hiyo ningemsemesha kiupendo)

Nikaelekea mezani kwa ajili ya kunywa chai. Siku hiyo sikuwa na jinsi, njaa ilikuwa ikiniuma sana hivyo ilikuwa ni lazima nile kwani usiku uliopita, sikula kabisa. Aliponiona nimekaa mezani, naye akasogea mezani pale na kuanza kunywa chai.

Salama: Nikuandalie nini mchana? (aliniuliza)
Mimi: Hapana! Sitokuja kula...
Salama: Na usiku je?
Mimi: Bado sijajua!
Salama: Halafu na h....(kabla hajamalizia, nikamuwahi)
Mimi: Salama, hebu naomba uniache kwanza, kichwa changu hakipo sawa kabisa. Unaweza kunyamaza?
Salama: Sawa...naomba unisamehe....(alisema huku akisogea kwa lengo la kunipigia magoti, nikasimama zangu)

Sikutaka kukaa nyumbani, siku hiyo nilikuwa na kazi moja ya kumtafuta huyu Isabela na kuongea naye. Ujinga ambao niliufanya ni kwamba sikuwa nikipafahamu alipokuwa akiishi, niliujua mtaa ambao mara kwa mara nilikuwa namfikisha na kisha kutimua zangu, sasa siku hiyo ndiyo ilikuwa ya kwanza kwangu kwenda nyumbani kwao.

Njiani, kama kawaida mawazo hayakunitoka hata kidogo, bado niliendelea kumfikiria, wala sikuchukua muda mrefu nikafika kwenye mtaa huo, harakaharaka nikasimamisha gari na kuteremka, nikawafuata kwa lengo la kuwauliza mawili-matatu.
 
SEHEMUU YA 22

Mimi: Samahanini, kuna msichana namtafuta, sijui anaishi sehemu gani, ila ni huuhuu mtaa..(niliwaambia mara baada ya salamu)
Jamaa 1: Msichana gani?
Mimi: Anaitwa Isabela! (nikamjibu, wote wakaonekana kushtuka, wakaangaliana)
Jamaa 2: Wewe nani?
Mimi: Naitwa Denis.
Jamaa 3: Ni nani wake?
Mimi: Rafiki yake!
Jamaa 1: Sisi wala hatumjui! (aliniambia kwa kujiamini kabisa, sijui aliniona mimi mjinga)
Mimi: Kweli? Hapana, mbona hata sura zenu zinaonyesha kabisa mnamfahamu...(niliwaambia huku nikiachia tabasamu pana)

Nilikuwa na uhakika kwamba washikaji walikuwa wakimfahamu sana Isabela ila walitaka kunizingua tu. Mara kwa mara walikuwa wakiangaliana tu, nilijiuliza ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, je Isabela alikufa au kulikuwa na tatizo gani.
Wakati najiuliza hivyo, kuna gari likafika mahali hapo, ilikuwa ni Land Cruiser mpya, nyeusi iliyokuwa tinted vioo vyote. Nikamuona jamaa mmoja akitoka pale alipokuwa na kulifuata gari lile, kioo kikashushwa kidogo na kuzungumza na dereva.

Sikujua walizungumza nini lakini kilichoendelea ni kwamba hakukuwa na mtu yeyote aliyeshuka kutoka ndani ya gari lile, liliendelea kusimama na hata baada ya hapo nilipoendelea kuwauliza wale vijana kuhusu Isabela, hawakunijibu chochote kile.

Kiukweli nilikasirika na kutatizwa, sikujua kabisa kilichokuwa kikiendelea, sikutaka kujali sana, nilichokifanya ni kuondoka, si kurudi nyumbani, bali kuendelea mbele ile njia ambayo Isabela alikuwa akienda kila nilipomshusha.

Majumba yalikuwa mengi, tena ya kifahari, nilichanganyikiwa kujua wapi ni wapi, nikawa naendesha gari kwa mwendo wa taratibu sana huku nikipepesa macho huku na kule.

Nilipofika katika nyumba moja ambapo nje kulikuwa na watu wawili, nikateremka na kuwafuata huku nikiwa na uhakika kwamba inawezekana watu hao wanamfahamu.
Mimi: Samahani, kuna msichana namtafuta anaitwa Isabela.
Jamaa 1: Isabela?
Mimi: Ndiyo! Mnamfahamu?
Jamaa 2: Kuna asiyemfahamu Isabela mtaa huu? (alijibu jamaa mmoja, hapo nikaanza kushikwa na hofu)
Mimi: Anaishi wapi?
 
SEHEMU YA 23

Jamaa 1: Nyumba hiyo hapo mbele! Kwani wewe ni nani? (aliniuliza, kilichojengeka akilini mwangu ni kwamba inaelekea msichana huyo hakuwa ametulia, hivyo na mimi nikajifanya waruwaru)

Mimi: Mimi bwana wake. Jana kanikimbia baa baada ya kunywa bia zangu....
Jamaa 2: Hahaha! Nilijua tu, huyu demu sijui atajirekebisha lini...kila siku kesi na ana bahati buzi lake halipo, lingekuwepo, angepigwa risasi (alisema jamaa huyo tena huku akiachia tabasamu lenye masikitiko, maneno yake yakaifanya damu yangu kuzunguka kwa kasi mwilini)
Mimi: Kwa hiyo mimi siyo wa kwanza?
Jamaa 1: Wewe kama wa nane hivi kuja kulalamika. Unajua hawa mademu zetu wa siku hizi wanapenda sana pesa, sasa mcheki mtu kama Isabela, anaishi na mzee mwenye pesa ndefu, mzee mwenye migodi na anapata anachokitaka, lakini hatulii.....

Kiukweli maneno yao yalinichanganya sana, nikabaki nikiwaangalia mara mbili-mbili, sikuamini kama kweli maneno hayo yalimhusu yule Isabela demu wangu au mwingine. Uso wangu ukajawa na tabasamu pana lakini moyo wangu ulikuwa kwenye maumivu makali, iweje yule Isabela, mwenye sura nzuri kama vile, mpole awe na mabwana lukuki, halafu eti aishi na bwana na wakati aliniambia anaishi kwao, tena na wazazi wake?

Nilichanganyikiwa, kama kupagawa, basi siku hiyo nilipagawa haswa. Nguvu zikaniisha, kwa kuwa kulikuwa na kibenchi pale nje, kwanza nikayakalisha makalio yangu.
Jamaa 2: Kama unataka kwenda anapoishi, nyumba hiyo hapo, ila muulizie kwanza kwa mlinzi, unaweza kuingia ukakutana na bwana wake mwingine ikawa msala. Bwana wake babu hayupo sasa hivi watu wanajilia vitu humohumo ndani....

Sikutaka kubaki mahali hapo, nilichokifanya ni kuondoka kuelekea kulekule waliposema anaishi. Nilipofika, nikakutana na mlinzi.
 
SEHEMU YA 24

Mlinzi: Bila shaka unamtaka Isabela (aliniambia bila hata salamu)
Mimi: (Huku nikionyesha tabasamu la kinafiki) Umejuaje mwana?
Mlinzi: Si ndiyo kawaida yenu. Sasa hivi dau limepanda, kumuona ndani kwake ni shilingi elfu kumi.
Mimi: Poa, ila yupo?
Mlinzi: Hayupo, kuna jamaa alikuja kumchukua na Land Cruser...
Mimi: Nyeusi, si ndiyo?
Mlinzi: Ndiyo?
Mimi: Tena ina tinted, si ndiyo?
Mlinzi: Ndiyo hiyohiyo...umeiona sehemu nini?

Sikutaka kujibu swali hilo, nilichokigundua ndiyo ileile Land Cruiser niliyoiona kule kona karibu na wale washikaji waliokataa kunijibu zaidi. Sikutaka kubaki hapo, nikarudi garini na kuanza kurudi kule nilipoiona, kiukweli nilikasirika sana, hasira zikanikaba kooni, moyo wangu uliamini kwamba bado Isabela alikuwa demu wangu, hata kupigana kwa ajili yake, nilikuwa tayari ila si kuona nanyang’anywa manzi kizembe kama vile.
Nikakunja mikono ya shati langu, nikajiandaa kwa ajili ya kupambana hukohuko kwenye ile gari, ila kwanza ningeanza na wale washikaji kwani nilipowaangalia, mbona walikuwa wadogo tu na ningewaweza wote. Eti nilitaka kupigana kisa huyu malaya Isabela.
Je, nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom