Niliuwa kwa kukusudia-1

Niliuwa kwa kukusudia-1

Niliua kwa Kukusudia--26-

ILIPOISHIA IJUMAA:
WAKATI dokta akijiandaa kunijibu, ghafla mlango ulifunguliwa na kutokea mtu ambaye wote tulibaki tunamwangalia kwa mshangao.
SASA ENDELEA…

Alikuwa mwanamke ambaye kwa kumwangalia mara moja, ni lazima ukubaliane na akili yako kuwa hakuwa na akili timamu. Alikuwa amevalia matambara yaliyochanika na kuchakaa sana. Hakika alionesha kila dalili ya kuwa mlemavu wa akili.
Katika hali ya kushangaza, alikuja moja kwa moja hadi kitandani nilipokuwa nimelazwa. Alimsabahi kwanza dokta kisha kunigeukia na kunikazia macho huku akishindwa kusema neno.
“Habari za kwako, unaendeleaje?” Hatimaye alivunja ukimya kwa salamu hiyo.

“Salama, nashukuru Mungu kwa kweli,” nilimjibu lakini sikuacha kumshangaa kutokana na hali aliyokuwa nayo. Mimi na yule daktari tulisitisha mazungumzo kwa muda na kusubiri kuona nini alikusudia kufanya yule mwanamke.
“Pole sana kwa yaliyokukuta jana, ulikuwa na hali mbaya mno,” alisema yule mwanamke na kupiga magoti kitandani kwangu huku machozi yakianza kumlengalenga. Nilibaki nikimshangaa kwani sikuwahi kuonana naye hata siku moja na nikawa najiuliza maswali mengi lakini kubwa ni alinijuaje na nani alimwambia kuwa nilikuwa na hali mbaya siku iliyopita!
“Nilishapoa, lakini wewe ni nani maana sina uhakika kama tunafahamiana?” nikamjibu na kumtupia swali ambalo niliamini jibu lake lingenitoa gizani kujua yule mwanamke alikuwa nani hasa na alinijuaje.
Hata hivyo, moyo ulinienda mbio sana kwani sikutaka mtu yeyote tofauti na madaktari ajue kuwa nilikuwa nimeingiliwa na mwanaume bila idhini yangu. Binafsi niliamini kitendo cha kubakwa ni udhalilishaji mbaya kuliko wowote katika maisha ya mwanamke.
“Mimi ni msamaria mwema niliyekuokota jana mtaroni usiku wa manane ukiwa hujitambui na damu nyingi zikikububujika kama maji ya bomba. Ulikuwa umepoteza fahamu,” alisema yule mwanamke.
Uchungu nilioupata kutokana na maelezo yake ulikuwa wa kiwango cha juu mno. Hasira na chuki dhidi ya yule Mwarabu vilinijaa.

“Kumbe alinibaka na kunitupa mtaroni?” nilijikuta nikitamka maneno hayo kwa sauti ya juu bila kujali uwepo wa wagonjwa wengine waliokuwemo mle wodini.
Mwanamke ambaye awali nilikuwa nikimhesabu kama mwendawazimu sasa aligeuka shujaa kwangu. Ndiye aliyeniokoa na hali mbaya niliyokuwa nayo baada ya kubakwa na bosi Elhakimu, mtu ambaye nilimuamini na kumheshimu kama mwajiri wangu.
Kumbukumbu mbaya ya jinsi nilivyobakwa ikaanza kujirudia upya akilini mwangu. Kufikia hapo, moyo wangu ukatengeneza chuki isiyosimulika dhidi ya wanaume wote duniani hasa yule Mwarabu aliyejivika ngozi ya kondoo ilihali ni mbwamwitu. Sikumtofautisha na wanyama wa mwituni.
“Pole sana, mimi huwa nalala kwenye mtaro huo kwa kuwa sina makazi maalum, ugumu wa maisha ndiyo ulionifikisha hapo, ufukara huu huwafanya watu wengi wadhani mimi ni mwehu, jambo ambalo si kweli,” akaendelea kusema yule mwanamke.
“Kuna gari la kifahari lilisimama mtaroni hapo, akashuka mwanaume wa Kiarabu na kuanza kuangaza huku na kule, muda mfupi baadaye akafungua mlango wa gari na kutoa mzigo.
“Awali nilidhani ni mzigo kumbe ulikuwa wewe, akakutupa mtaroni na kuingia kwenye gari lake haraka sana na kuondoka kwa kasi ya ajabu.

“Nilipokusogelea, ulikuwa hujitambui na damu zilikuwa zikikuvuja kwa wingi, nikaita watu na kwa pamoja tukakuleta hapa hospitalini,” alisimulia yule mwanamke huku uso wake ukiwa umechakazwa na machozi ya huruma.
Pamoja na maadili ya taaluma yake, kukutana na matatizo mbalimbali na makubwa ya wagonjwa wengi, yule daktari ambaye kwa jina alikuwa amejitambulisha kama Dokta Masalu alishindwa kuyazuia machozi wakati yule mwanamke alipokuwa akisimulia jinsi alivyoniokota.
Ilionesha kuwa yeye hakuwepo wakati nafikishwa pale hospitalini. Nilimuona akionesha hisia za machungu na maumivu makali.
“Basi ngoja nikuchome sindano kwanza, nikupe dawa fulani ndipo tuendelee na tiba nyingine,” alisema Dokta Masalu na kumtaka yule mwanamke atupe muda kwani hata hivyo, muda wa kuangalia wagonjwa ulikuwa umepita kwa asubuhi ile.
Yule mwanamke aliondoka na kuahidi kurudi mchana kunijulia hali. Wakati anaondoka, macho yangu yaliganda kwake na kumuona kama shujaa wa kipekee maishani mwangu kwa wakati huo.
“Bila huyu mwanamke ningefia mtaroni mimi,” nilijikuta nikitamka maneno hayo huku machozi yakinitoka na kulowanisha mashuka.

“Kuna jambo nitakueleza nikirudi, ila inabidi uwe na kifua,” alisema yule mwanamke na kufungua mlango huku akiubamiza kwa nguvu.
Je, ni jambo gani? Usikose kufuatilia leo jioni....
 
Niliua kwa Kukusudia--27-

ILIPOISHIA :
"Kuna jambo nitakueleza nikirudi, ila inabidi uwe na kifua," alisema yule mwanamke na kufungua mlango huku akiubamiza kwa nguvu.
SASA ENDELEA…


Mimi na yule daktari tulibaki tukitazamana kwa mshangao. Hakuna aliyekuwa tayari kuamini kilichosikika masikioni mwetu muda mfupi uliopita. Hapohapo nikakumbuka msemo wa mama yangu ambao alikuwa akinieleza mara kwa mara enzi za uhai wake.
"Mwanangu siku zote za maisha yako usithubutu kumdharau mtu yeyote kwa sababu ya mwonekano wake."


Kweli, maneno ya mama yalikuwa yamedhihirika kwani mwanamke ambaye hapo awali nilimuona kama mwendawazimu sasa aligeuka lulu na mwenye thamani kubwa sana maishani mwangu. Asingekuwa yeye huenda hadi wakati huo ningelikuwa marehemu kutokana na maelezo yake kuwa wakati akiniokota nilikuwa

nikivuja damu nyingi sana kupitia sehemu zangu za siri baada ya kubakwa vibaya na yule Mwarabu.

Moyoni nikazidi kujiapiza kulipa kisasi kwa Mwarabu huyo, japo sikujua nitatumia njia gani kwani alikuwa ni mtu mwenye pesa na utajiri mkubwa mno kiasi cha kuogopeka hata kwa baadhi ya viongozi wa serikalini na taasisi mbalimbali zisizokuwa za kiserikali.

"Haki. Ndiyo, haki pekee ndiyo itaniokoa katika hili, nitafungua mashitaka dhidi yake, kwani mama aliwahi kuniambia kuwa hakuna aliye juu ya sheria hivyo pamoja na pesa zake ni lazima sheria ichukue mkondo wake dhidi ya Mwarabu huyu," nikajiwazia na kujipa matumaini makubwa moyoni mwangu.
Jioni ya siku hiyo, wakati nikimalizia kula, yule mwanamke aliyekuja asubuhi na kunieleza kuwa ndiye aliyeniokota, alirudi na kuanza kunisimulia historia ya maisha yake.


Alinisimulia jinsi ambavyo aliwahi kuishi maisha ya kitajiri na kifahari huko nyuma, lakini kwa sababu ya kuwaamini wanaume ndiyo maana kwa wakati huo alikuwa akiishi kama mnyama mwituni ili hali alikuwa binadamu ndani ya nchi yake huru.


Akasimulia jinsi alivyozaliwa na kukulia kwenye utajiri mkubwa wa wazazi wake, jinsi alivyosoma shule za kimataifa tangu msingi hadi ngazi ya vyuo mbalimbali. Katika mazungumzo yake, nilishangaa aliponiambia kuwa kwa wakati huo alikuwa ni msomi wa shahada ya udhamili (Master Degree) katika masuala ya sayansi na utafiti.

Nilizidi kubaki mdomo wazi aliponieleza mashirika aliyowahi kufanya kazi duniani ikiwemo Marekani, Uingereza, Ufaransa, Italia na Uholanzi.

"Mapenzi, mapenzi ndiyo yamenifikisha hapa nilipo, leo nalala jalalani, nakula kwa kuombaomba kwenye migahawa na kuonekana kama mwendawazimu, kisa ni mapenzi," akazidi kunisimulia yule mwanamke na kunifanya niendelee kumshangaa kwa kila sentensi aliyoitamka.


Sikupata picha ni pigo gani alilipata kupitia mapenzi kwani kukulia kwenye familia tajiri, kusoma hadi ngazi hiyo ya juu kabisa kielimu na kufanya kazi nchi kubwa kama alizozitaja na leo hii kuonekana kama mwehu asiyekuwa na makazi maalum kulinishangaza sana, hakika lilikuwa pigo kubwa katika maisha yake.


Akaniambia jinsi ambavyo alikutana na mwanaume wake aliyekuwa Mtanzani nchini Uingereza na kuanzisha naye uhusiano. Akasema walipendana na kuaminiana kupita kiasi na kufikia hatua ya kurudi nchini Tanzania kwa utambulisho na maandalizi ya kuoana.


Yule mwanaume alimshawishi kuacha kazi na kuja kuishi nchini Tanzania ambapo mali na utajiri wote aliokuwa nao aliuandikisha kwa jina la mwanaume huyo, akasema siku chache baada ya kufunga ndoa akiwa amemkabidhi kila kitu mumewe, manyanyaso yalianza kujitokeza na kufikia hatua ya kumfukuza nyumbani
walipokuwa wakiishi. Kutokana na hali hiyo kuusumbua ubongo wake, alilazimika kujiiingiza kwenye matumizi mabaya ya pombe hali iliyosababisha kuathirika kisaikolojia.

Ilikuwa ni sumulizi ndefu na ya kusisimua iliyonitia uchungu mkubwa mno moyoni mwangu. Hasira dhidi ya
wanaume ikazidi kupanda maradufu na kujikuta nikizidi kujiapiza kisasi kikubwa baada ya kupona ingawa hakika sikuwa najua ni njia ipi rahisi ambayo ningeweza kuitumia tofauti na kutegemea sheria kuniokoa katika janga hilo.

Siku zilikatika hatimaye nikapata nafuu na kwenda kufungua mashitaka kituo cha polisi. Huko nilienda na vipimo vyote muhimu kutoka hospitalini na maelezo ya daktari ambayo niliyaambatanisha kwa pamoja.

Kwa ushahidi niliokuwanao niliamini Elhakimu angepatikana na hatia, angenilipa fidia kwa kitendo alichonifanyia na kufungwa jela miaka thelathini ili iwe fundisho kwa wanaume wenye tabia kama yake.
Pale kituoni nilimkuta mkuu wa kituo, nikamweleza shida yangu lakini baada ya kumtajia kuwa mhusika alikuwa Elhakimu yule Mwarabu alishituka na kutamka maneno yaliyonifanya niishiwe nguvu.


Je, nini kitaendelea? Fuatilia Usiku Mwingi ....
 
Back
Top Bottom