Ni kweli tuko wengi (mimi ni mmojawao) tusioipenda ccm. Naomba nikupe sababu zangu kama ambavyo wewe umekuwa na uhuru wa kueleza kwa nini unawashangaa watu wasioipenda ccm!
Kwanza, mimi sikuzaliwa miaka ya 90 na kwenda mbele. Kadi yangu ya ccm niliipata siku Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilipoanzishwa pale Zanzibar 5.2.1977. Naomba unielewe ninapozungumzia CCM (ya Mwalimu) ninaitofautisha na ccm (ya magamba).
Kumbuka ya kuwa kabla ya CCM kulikuwa na chama cha TANU kilichoanzishwa 7.7.1954 na Afro Shiraz Party (ASP, sina hakika na tarehe kilipoanzishwa). Hivi ndivyo vyama vilivyoleta uhuru wa nchi hizi mbili za Tanganyika (9.12.1961) na Mapinduzi ya Zanzibar (12.1.1964). Baada ya nchi hizi mbili kuungana 26.4.1964 na kuzaliwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bado tulibaki na vyama vyetu vikuu viwili, pamoja na vyama vingine kadhaa vya siasa ambavyo havikuwa madarakani. Mwaka 1965, serikali ikavifunga vyama vingine vyote vya siasa na kuanzisha katiba ya chama kimoja, kwa lugha ya kiingereza tunasema (One Party Constitution). Lakini kwa ukweli, nchi yetu haikuwa ya chama kimoja, kwa kuwa tulikuwa bado tuna TANU na ASP. Mwalimu na viongozi waliokuwa madarakani wakati huo waliliona hilo, na kuelewa ya kwamba litakuja kuleta migogoro siku zijazo, ndipo walipoamua kuviunganisha vyama hivi viwili na kuunda Chama Cha Mapinduzi (CCM). Kabla ya CCM kuanzishwa, chama cha TANU 5.2.1967 kilipitisha Azimio la Arusha, lililokuwa limeweka misingi kuhusu mwelekeo wa nchi yetu na kutoa dira ya maendeleo ya nchi yetu. Makosa ya Azimio la Arusha yalikuwepo, lakini kuna mazuri mengi sana ambayo yamefanyiwa tafiti mbalimbali na kuonyesha ya kuwa Tanzania ilikuwa mfano mzuri wa kuigwa na nchi zingine za Afrika hata nje ya bara letu. Kubwa katika hayo ilikuwa ni kujaribu kuleta usawa wa wananchi wake. Cheo cha Mheshimiwa kiliondolewa, kila mtu aliitwa Ndugu. Ilikuwa ndugu mbunge, ndugu waziri, ndugu dereva wa basi n.k. Mishahara ya kima cha chini iliongezwa na kodi ya mapato (income tax) kufutwa kwa wafanyakazi wa kima cha chini, lakini wafanyakazi wa ngazi za kati na za juu waliongezewa kodi. Hii ilifanya kuwa na hali inayoelekea kuweka usawa, hakukuwa na matajiri sana wala masikini sana. Miiko ya viongozi iliwekwa, ikiwemo; Kiongozi haruhusiwi kuwa na mishahara miwili, kiongozi haruhusiwi kuwa na hisa katika makampuni, kiongozi haruhusiwi kuwa na nyumba ya kupangisha n.k. Na katiba ilitamka wazi ya kuwa Kiongozi ni Mume na Mke, ama Mke na Mume. Kwa mantiki hii ilikuwa haiwezekani kiongozi akafungua duka kwa jina la mkewe, ama kama ni mke basi asingeweza kufungua biashara yoyote kwa jina la mumewe.
Njia zote kuu za uchumi zilitaifishwa, kulikuwa hakuna benki binafsi, hakuna shirika la bima binafsi, hakuna shirika la nyumba binafsi, na viwanda na makampuni yote makuu yalitaifishwa na serikali, yakawa mashirika ya umma. Shule zote na hospitali zilitaifishwa. Wakati huo tulikuwa watoto wote wa kitanzania tunasoma kwenye shule za serikali. Kwenye darasa moja kuna watoto wa wakulima, watoto wa wakuu wa mikoa, watoto wa mawaziri. Elimu ilikuwa bure kuanzia darasa la kwanza mpaka Chuo Kikuu. Gharama ya mzazi ilikuwa sare za shule, tulipatiwa vitabu vya kiada, madaftari, kalamu, rula, 'mathematical sets' na mahitaji mengine yote bure kwa kuwa serikali ilikusanya kodi, na kuitumia kutoa huduma muhimu kama elimu bila malipo. Ile imani unayoizungumzia ya kuwa 'Binadamu wote ni sawa ilitekelezwa kwa vitendo', sio majukwaani. Hospitali zilikuwepo kila wilaya, na zahanati na vituo vya afya vilijengwa navyo vilitoa huduma bure. Huduma za kliniki za kina mama na watoto, upasuaji, vipimo vya X-ray, mpaka dawa zilikuwa zinapatikana kwenye hospitali za serikali bure. Enzi hizo hata biashara ya maduka ya dawa ilikuwa haina maana kwa kuwa mgonjwa anapofika hospitali anapewa dawa zote alizoandikiwa bila malipo. Hiyo ndiyo Tanzania yangu niliyokuwa ninajivunia, hicho ndicho Chama Cha Mapinduzi (CCM) ninachokikumbuka mimi. Kiongozi alikuwa anaapa ya kuwa 'Cheo ni dhamana...', cheo hakikuwa usultani wa kurithishwa kutoka baba, kwenda kwa mama na watoto, cheo hakikuwa kinatumika kutuma majeshi kuumiza raia, kubambikia watu kesi zisizokuwa na msingi. Wakati huo mtu akiteuliwa kushika wadhifa haisemwi ya kuwa 'fulani kaula', kwa kuwa haikumaanisha ya kuwa yeye ni mjanja sana kuliko wengine, ila alikuwa anapewa madaraka ili afanye kazi kwa niaba ya wananchi. Kiongozi alikuwa mtumishi wa wananchi, akiwanyenyekea na kusikiliza shida zao na sio kuwatisha kwa kuwaletea virungu pale wasipokubaliane naye. Wewe na mimi hatuwezi kukubaliana kila kitu, ndivyo tulivyoumbwa kama binadamu kila mmoja ana mawazo yake. La kufanya ni kusikiliza kila mtu apewe nafasi aseme aliulo nalo tushauriane, tufike mahali pa kukubaliana ili tupate kutatua matatizo yetu kama taifa. Hiyo ndiyo CCM iliyopendwa.
ccm ya leo imegeuka saratani!
ccm ni mali ya waheshimiwa, hakuna tena ndugu!
ccm kimegeuka chama cha matajiri, angalia mishahara ya viongozi, tazama mahekalu yanayoshamiri kila kukicha, wakati huo huo walala hoi wanadidimia kwenye dimbwi la umaskini!
ccm ni chama cha familia fulani, akitoka baba anakuja mwana, mke, shemeji na swahiba!
ccm imefanya walio madarakani wamesahau ya kuwa cheo ni dhamana, wanatukana hadharani bila hata kuchuja wanayoyasema (Lusinde, Serukamba na wengine) na viongozi ambao wangepaswa kukemea haya wanawalinda!
ccm imegeuka kitovu cha biashara halali na haramu, kinyume na yale yaliyokuwa maadili ya TANU na CCM kwamba kiongozi asiwe mfanyabiashara!
ccm imehakikisha ya kwamba elimu na afya hazipatikani bure ama kwa gharama nafuu kwa kila mtu. Matokeo yake ni wachache wenye pesa wanaoweza kuwasomesha watoto wao ili waendelee kuwa kwenye nyadhifa za juu na watanzania wengine wabaki nyuma. Sasa tuna 'watawala' na 'watawaliwa'. Huduma za afya sasa ni kupelekwa India, watanzania wangapi wenye uwezo huo?
Inaelekea wewe bado ni kijana mdogo sana huyajui uyasemayo. Mimi nimeguswa sana na hayo yote. Amini usiamini, bado ninayo kadi yangu ya CCM ya mwaka 1977. Nimeiweka kama kumbukumbu kwa yeyote atakayekuja kudai ya kuwa siipendi nchi yangu.
Mimi ni mwanachama hai wa CDM, sioni aibu kutamka hivyo, na sitanyamaza hadi pale ccm ya jk na mashetani wenzake watakapong'oka madarakani!
Peoples' Power!!!