Mzimu unaotabasamu

Mzimu unaotabasamu

ERIC SHIGONGO
MZIMU UNAOTABASAMU-12

David na Davis walikuwa wakitetemeka, kila mmoja aliogopa, ni kweli waliwahi kumuona baba yao akiwa kwenye hasira kali lakini si kama alivyokuwa siku hiyo.
David alijua kile ambacho kingekwenda kutokea, baba yake alitaka kuwamaliza msituni hapo kwa kuwa alihitaji mkumridhisha mwanamke aliyekuwa akiishi naye.
David alibaki akimwangalia baba yake kwa hasira kali, hakuamini kama mwanaume huyo alikuwa radhi kuiangamiza familia yake kwa kuwa tu alimpenda mwanamke mwingine. Moyo wake ukajaa chuki na kumchukia mno baba yake kwani mbali na kutaka kuwamaliza, pia alimuua mama yao na kusingizia kwamba ni kansa ndiyo iliyommaliza mwanamke huyo.
“Ninakuchukia baba! Ninakuchukia kama shetani,” alisema David, hakutaka kubaki kimya, alijua kuwa huo ndiyo ulikuwa mwisho wake, akaona ni bora kumwambia baba yake kwamba alikuwa akimchukia.
Davis alishangaa, hakujua kaka yake alimaanisha nini, kwake, bado baba yake alionekana kuwa mtu mwema, alimpenda mno na kuona kuwa huyo ndiye mtu aliyebaki ambaye alitakiwa kuwa pamoja nao hasa baada ya mama yao kufa.
Gideon akatoa bastola yake, akaishika kwa nyuma, hakutaka watoto hao waione kwanza. Alidhamiria kufanya mauaji hayo msituni hapo lakini alipowaangalia tena watoto wake, kidogo huruma ikaanza kumuingia.
Davis alikuwa akilia lakini kwa David alikunja ndita huku akionekana kuwa na hasira kali kiasi kwamba akaanza kutetemeka, yaani kwa hasira alizokuwa nazo mahali hapo, kama angekabidhiwa bastola, asingejiuliza kumuacha baba yake, ilikuwa ni lazima amuue.
“Sina jinsi, naomba mnisamehe wanangu,” alisema Gideon huku akijiandaa kuwanyooshea bastola aliyoishika katika mkono wake aliouweka kwa nyuma.
“Paaa! Paaa! Paaa!” milio ya risasi ikasikika mahali hapo.
“Aauugghh...” ulisikika uyowe mkubwa pale walipokuwa wamesimama watatu hao. Damu ikatapakaa mahali hapo.
***
Mzee Msuya alichanganyikiwa, hakuamini kilichokuwa kimetokea, kitendo cha kupigiwa simu na kimada wake na kumwambia kwamba kulikuwa na watu waliokuwa wamemteka aliona kabisa kuna mtu alimshika sharubu na alitaka kuona makali yake.
Kwake, ilikuwa ni afadhali umuumize yeye lakini si msichana Juliet. Huyo alikuwa msichana pekee aliyekuwa akimpenda kwa moyo wa dhati, kitendo cha kumuumiza au kumfanya kitu chochote kile kilimaanisha kwamba mtu huyo alitaka vita.
Alijiangalia kiunoni mwake, kulikuwa na bastola yake iliyokuwa na risasi kumi, alijua fika kwamba alikuwa akienda kuitumia huko kwani asingeweza kutulia kuona Juliet akinyanyaswa na mwanaume mwingine na wakati alikuwepo.
Baada ya dakika ishirini akafika nyumbani hapo. Akateremka na kuanza kuelekea ndani ya jumba hilo. Kwanza mlinzi hakumkuta, akahisi kwamba kile alichokuwa ameambiwa kilikuwa kweli kabisa, akachukua bastola yake kutoka kiunoni na kuanza kuelekea ndani huku akiwa makini kabisa, alijiandaa kwa jambo lolote lile ambalo lingetokea.
Akafika mpaka sebuleni, hakukuwa na mtu, hakutaka kuita, akawa anaangalia sehemu nyingine kwa kujibanza, alipoona amekwenda mpaka jikoni hayupo akaanza kuita, akasikia miguno kutoka chumbani kwa Juliet.
Haraka sana akaanza kuelekea huko, alipoufikia mlango, akaufungua, hakuanza kuingia kwanza, aliogopa kufanya hivyo kwa kuhisi kwamba ndani kulikuwa na maadui na kama angeingia kwa fujo basi angeweza kupigwa risasi mfululizo, akasimama pembeni ya mlango na baada ya dakika tano, akaingia kwa kujibinua sarakasi pasipo kujali kitambi alichokuwanacho.
“Mmmh...mmmh...mmmh...” alisikia miguno kutoka kitandani.
Akayapeleka macho yake hapo, yakatua kwa mpenzi wake, Juliet aliyekuwa na mlinzi, wote wawili walikuwa wamelazwa huko mikono na miguu yao ikiwa imefungwa kamba ngumu ambazo zilifungwa mpaka katika kitanda hicho cha chuma na midomoni mwao walifungwa vitambaa.
Haraka sana Mzee Msuya akawasogelea, akavitoa vitambaa walivyokuwa navyo midomoni na kisha kuwafungua kamba. Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya Juliet ni kumkumbatia Mzee Msuya.
“Walitaka kuniua...walitaka kuniua bebi,” alisema msichana huyo huku akianza kulia.
“Hawajakuumiza popote?”
“Hapana! Ila walitaka kuni...” alisema Juliet lakini hata kabla hajamaliza sentensi yake, akaanza kulia.
Wakakumbatiana lakini kidogo Mzee Msuya alionekana kuwa na maswali mengi kichwani mwake. Hakujua lengo kubwa la watu hao waliovamia nyumbani kwa mchepuko wake lilikuwa nini. Hawakuiba wala hawakumfanya kitu chochote kibaya, alijiuliza kama sababu ya watu hao ilikuwa ni kumtaka kumsumbua au ilikuwa nini.
Wakati akijiuliza maswali hayo, simu yake ya mkononi ambazo zilikuwa kwa watu wenye pesa tu kwa kipindi hicho. Haraka sana akaitoa kutoka mfukoni mwake, ilikuwa simu kubwa iliyofanana na redio call, akaipeleka sikioni, sauti ikaanza kusikia kutoka upande wa pili, ilikuwa ni ya mtu aliyekuwa akimfahamu kabisa.
“I have your family, I am going to kill them,” (nina familia yako, nitaiua) alisikia sauti kutoka upande wa pili.
“My family?” (familia yangu?) aliuliza huku akionekana kushtuka.
“This is just a message for you,” (huu ni ujumbe kwa ajili yako) aliisikia sauti hiyo na simu kukatwa.
“Halo...halo...halo...” aliita lakini tayari simu haikuwa hewani.
Hapo ndipo akapata jibu ya kile kilichokuwa kimetokea, aligundua kwamba alitolewa kanisani ili familia yake itekwe, akajaribu kumpigia simu mke wake, simu haikuwa ikipokelewa, hakukata tamaa, aliendelea kupiga zaidi na zaidi na mwisho wa siku simu haikuwa ikipatikana, ilionyesha kabisa kwamba ilikuwa imezimwa.
Alichanganyikiwa, hapo ndipo alipogundua kwamba familia ilikuwa ni muhimu kuliko hata Juliet. Hakutaka kubaki chumbani hapo, akasimama na kuondoka kwa mwendo wa kasi kwenda nje, akachukua gari lake na kuondoka bila hata kuaga.
Safari ilikuwa ni kwenda kanisani tu, aliamini kwamba huko angeweza kuikuta familia yake, alitumia dakika chache tu, akafika, akateremka, akaelekea kanisani, akakutana na mchungaji wake, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumuuliza ilipo familia yake.
“Sijui! Ila waliondoka hapa,” alisema mchungaji huku akimwangalia mzee huyo.
Akaona kabisa hapo hakukuwa na msaada, akalifuata gari lake na kuondoka kanisani hapo. Njiani alikuwa akiangalia huku na kule, alihisi kwamba angeweza kuiona familia yake sehemu, mpaka anafika nyumbani hakufanikiwa kuiona, akaingia ndani, napo dada wa kazi akamwambia kwamba familia yake haikurudi tangu walipokwenda kanisani asubuhi ya siku hiyo.
“Armando....!!” alijikuta akilitaja jina hilo.
Hakutaka kubaki nyumbani hapo, alichokifanya ni kuondoka na kuelekea kituo cha polisi ambapo akatoa taarifa kwamba familia yake ilitekwa na mtu aliyejulikana kwa jina la Armando. Polisi walipolisikia jina hilo, wakashtuka, hawakumwamini kwani mtu aliyekuwa amemtaja alikuwa mtu hatari aliyekuwa akitafutwa dunia nzima na Wamarekani wenyewe walishindwa hata kumpata.
“Armando huyu tunayemjua sisi?” aliuliza polisi mmoja.
“Huyohuyo! Amekuja Tanzania na kuiteka familia yangu, sijui walipo, naomba mnisaidie,” alisema Mzee Msuya huku machozi yakianza kumtoka.
Polisi wakapigiana simu za mezani na kupeana taarifa kwa kile kilichokuwa kimetokea, polisi wakajipanga kuanza kuisaka familia ya bilionea huyo. Kila mmoja alijiahidi kujitoa kwa nguvu kwani kama familia hiyo isingepatikana salama basi lawama za bilionea huyo zingekuwa juu yao.
***
Mzee Armando akapewa taarifa kwamba familia aliyokuwa akiihitaji ilikuwa mikononi mwa vijana aliokuwa amewatuma. Akawaambia kwamba waiweke sehemu na usiku wa siku hiyo wangekwenda sehemu kuimaliza na kuondoka nchini Tanzania.
Hilo halikuwa tatizo, familia hiyo ikapelekwa Kimara na kuhifadhiwa huko. Moyo wa Armando ukafarijika, hakuamini kama alifanikiwa kuiteka familia hiyo aliyokuwa akiihitaji kwa nguvu zote.
Mzigo wa madawa yake uliotapeliwa ulimchanganya, hakutaka kuiacha familia hiyo hai, alitaka kuimaliza, arudi nchini Ujerumani na kisha kupanga mikakati ya kummaliza Msuya mwenyewe.
Alikaa kitandani hotelini huku macho yake yakiwa kwenye saa yake, alikuwa akiangalia muda, alitaka itakapofika usiku wa saa moja aondoke kwenda kuonana na Theofil ambapo huko angemchukua na kumpeleka mahali familia ilipokuwa na kisha kuimaliza msituni.
Muda ulipofika, akakutana na Theofil ambaye alimchukua na kumpeleka huko. Alipofika, akaiangalia familia hiyo ya mke mmoja na watoto wawili. Akatoa tabasamu pana na kujiona kwamba alikuwa mshindi, akamwambia Theofil aichukue na wenzake na kuondoka nayo kwenda msituni kwani ilikuwa ni lazima kuimaliza haraka sana.
“Fanyeni haraka,” alisema mzee huyo.
Hilo halikuwa tatizo, kila kitu kilifanyika kwa haraka sana, familia hiyo ikachukuliwa, ikapakizwa ndani ya gari na kuelekea msituni. Hawakuchukua muda mrefu sana wakafika katika msitu wa Pande, wakaiteremsha na kuwataka kupiga magoti, Iddi akachukua bastola yake, alikuwa akisubiri amri ya bosi wake tu kwamba aimalize, basi afanye hivyo bila kuuliza lolote lile.
“Kill them,” (waue) alisema Armando.
Wakati Iddi akiwa amekoki bastola yake kwa lengo la kuwamaliza watu hao, ghafla wakaanza kuona mwanga wa gari, kwanza wakashtuka, haraka sana wakawawahi mateka wao na kuwafumba midomo.
Baada ya sekunde kadhaa wakasikia muungurumo wa gari ambalo lilitembea na kwenda kusimama sehemu. Wakabaki wakiliangalia, akili yao iliwaambia kwamba hilo lilikuwa gari la polisi ambao walikuwa na taarifa za kutekwa kwa familia hiyo.
Wakamuona mwanaume mmoja akiteremka kutoka ndani ya gari, akazungumza kidogo kisha kuwaagiza watu fulani wateremke. Macho yao yakawaona watoto wawili wakiteremka na kusimama mbele ya mwanaume huyo ambaye akaanza kuongea nao huku wakiwa hawasikii hasa kile kilichokuwa kinaongelewa.
“Who are they?” (ni wakina nani hao?) aliuliza Armando.
“We don’t know sir,” (hatujui mkuu)
Wakati wakiwa hapo, ghafla wakaanza kusikia milio ya risasi, mwanaume yule, Gideon aliyekuwa amesimama na watoto wale akapigwa risasi ya mkono na begani, akaanguka chini, bastola aliyokuwa nayo ikadondoka. Watoto wale walipoona hivyo, Davis akakimbilia ndani ya gari na David kuanza kwenda kule walipokuwa wao kwani hakuwa akijua kama kulikuwa na watu wengine.
“Who shot them?” (nani amewapiga risasi?) aliuliza Armando.
“Wasn’t me sir,” (siyo mimi mkuu)
Ghafla wakawaona wanaume watatu wakielekea kule walipokuwa watu wale huku wakiwa na bastola mikononi mwao. Wakajua kwamba watu hao walikuwa hatari hivyo walichokifanya ni kuanza kuwashambulia kwa risasi mfululizo.
“Paaa...paaa...paaa...” milio ya risasi ikasikika mahali hapo, wanaume wale waliokuwa wametumwa na Lucy wakaanguka chini na damu kutoka miilini mwao.
“Kill them! Do this fast man,” (waue! Fanya haraka) alisema Armando kwani tayari walijua kuwa eneo hilo halikuwa salama hata kidogo.
Hawakutaka kuchelewa, haraka sana wakaanza kuipiga risasi za vichwa familia ya Mzee Msuya, ilikuwa ni lazima kuimaliza kwani hawakwenda nayo mahali hapo kupanga mikakati, kilichokuwa kimewapeleka kilikuwa ni kufanya mauaji tu.
Wakati wakiwa wamekwishawapiga risasi za vichwa mfululizo kiasi kwamba ilikuwa hata shida kuwatambua, wakakumbuka kwamba kulikuwa na mtoto mmoja alikuwa amekimbia kutoka kule lilipokuwa lile gari, walipoangalia, kwa mbali walimuona akiwa amelala chini kwani milio ya risasi ilimuogopesha na kuhisi kwamba kama angekimbia basi angeweza kupigwa risasi mfululizo, hivyo kulala kwake ikaonekana kuwa kama nafuu.
Iddi akachomoka kwa kasi, akamfuata David pale alipokuwa amelala, alipomfikia, akambeba juujuu na kurudi naye kule walipokuwa wenzake.
David alikuwa akilia, aliuona mwisho wake, alikuwa mikononi mwa watu hao walioonekana kuwa na hasira mno na ndiyo watu waliokuwa wamewapiga watu wengine risasi mfululizo. Alijaribu kuwaomba msamaha wamuache aondoke lakini hakukuwa na mtu aliyejali.
“Tukimuacha, kuna siku atasema kilichotokea, huyu amekwishakuwa shahidi wa kila kitu kilichotokea. Kwa usalama wetu lazima tumuue,” alisema Theofil huku akiwaangalia wenzake, wakati huo David alikuwa chini akilia.
“Sawasawa. Mpige risasi za kichwa kama hiyo familia,” alisema Armando na hapohapo Iddi kuikoki bastola yake tayari kwa kumpiga risasi David
 
ERIC SHIGONGO
MZIMU UNAOTABASAMU-13

Gideon alikuwa kwenye maumivu makali, risasi mbili zilizompata begani na mkononi zilimsababishia damu nyingi kutoka. Hakutaka kusubiri msituni hapo, alijua kwamba kama asingeondoka ilikuwa ni lazima kufa kwani aligundua hawakuwa peke yao kuwa mahali hapo.
Hakutaka kuchelewa, alipokaa katika kiti akaliwasha gari na kuondoka kwa kasi kubwa. Davis alikuwa pembeni yake, alichanganyikiwa, hakujua ndugu yake alikuwa wapi, alimwambia baba yake kwamba hawakutakiwa kuondoka kwani David hakuwa ndani ya gari lakini Gideon hakutaka kukubaliana naye, ndiyo kwanza akaongeza kasi ya gari hilo na kuondoka zake.
Japokuwa damu ziliendelea kumtoka huku akisikia maumivu makali lakini hakutaka kuacha kuendesha gari, hawakuchukua muda mrefu wakafika barabara ya lami ambapo akaendesha kwa kasi mpaka kufika Kimara katika zahanati ndogo ya Dk. Kibwagizo na kusimamisha gari lake.
Akateremka na kuanza kuelekea ndani ya zahanati hiyo. Kila mtu alimshangaa, damu ziliendelea kumtoka kiasi kwamba mpaka watu wengine wakaanza kuogopa. Haraka sana akachukuliwa na manesi wawili na kumpeleka katika chumba kimoja na kumtaka apumzike huko huku daktari akiitwa kwa ajili ya kumpatia huduma, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuwekewa dripu ya damu kwani ilionyesha kwamba alipoteza kiasi kikubwa cha damu.
"Pole sana! Umepoteza damu nyingi," alisema daktari huku akimwangalia Gideon aliyekuwa hoi.
"Nisaidie tu! Nitakulipa kiasi chochote cha pesa," alisema Gideon.
"Umefanya nini?"
"Nimepigwa risasi, cha kwanza zitolewe," alisema Gideon.
"Ngoja tuzitoe hizo risasi!"
Akaanza kufanyiwa upasuaji mdogo kwa lengo la kuzitoa risasi alizokuwa amepigwa. Akachomwa sindano ya ganzi na kuanza kutolewa risasi hizo ambapo moja ilikuwa begani na nyingine mkononi. Baada ya kumaliza, akaachwa apumzike huku damu ikiendelea taratibu kuingia ndani ya mwili wake.
***
Amri aliyoitoa Mzee Armando ilikuwa ni kuuliwa kwa mtoto David ambaye alikuwa amepiga magoti huku akilia. Aliuona huo ndiyo mwisho wake, hakuwa na tumaini, mbele yake aliona giza na hapo alipokuwa moyo wake ulikuwa ukimuomba Mungu kuipokea roho yake kwani alikuwa akienda kufa na kukutana na mama yake huko alipokuwa.
Wakati Iddi akiwa ameikoki bastola yake tayari kwa kufyatulia, akamsikia Armando akimwambia kwamba aache kumfyatulia risasi kwani kulikuwa na jambo ambalo alilifikiria kichwani mwake na ili lifanikiwe ilikuwa ni lazima huyo mtoto aachwe hai na ikiwezekana aondoke naye.
"Unaitwa nani?" aliuliza Mzee Armando kwa Kiingereza kizuri kabisa.
"David!"
"Umekuja kufanya nini huku?"
"Baba alitaka kutuua! Ninamchukia baba yangu, ninataka kumuua kama alivyomuua mama, ninataka kumuua baba yangu," alisema David huku akilia hapo alipokuwa.
Kila mtu alishangaa, hawakuamini kile alichokisema David kwamba baba yake alitaka kumuua kwani lilikuwa jambo lisilowezekana kwa mzazi kuamua kumuua mtoto wake wa kumzaa.
Wakamwamini, Mzee Armando akawaambia vijana wake kwamba waondoke na David kwani kulikuwa na jambo kubwa alilotaka kufanya naye. Wakaondoka naye mpaka ndani ya gari. Muda wote huo David alikuwa akilia, hakujua kama ndugu yake, Davis alikuwa hai au aliuawa kutokana na zile risasi zilizokuwa zimefyatuliwa mfululizo.
Baada ya saa moja gari hilo likasimama nje ya jumba moja ambapo mipango ikapangwa usiku huohuo kwamba Armando alitakiwa kuondoka haraka sana kuelekea nchini Kenya kwa kutumia meli ambapo huko angepanda ndege yake na kurudi nchini Ujerumani huku akiwa tayari amekamilisha kile alichokitaka.
Hicho ndicho kilichofanyika, kwa kuwa alikuwa na mtandao mkubwa, hakukuwa na jambo gumu kwake, meli ya mizigo iliandaliwa na hivyo kuanza safari ya kuelekea nchini Kenya usiku huohuo huku akiwa na David ambaye kwa kipindi hicho alitaka kumchukulia kama mtoto wake wa kumzaa kwa sababu tu kulikuwa na kazi aliyotaka kumpa.
Ndani ya meli David alikula vizuri, alifanya kitu chochote alichotaka kufanya huku akionyeshewa upendo wa ajabu ambao hakuutarajia tangu siku ambayo mama yake alipouawa na kudanganywa kwamba alikufa kwa ugonjwa wa kansa ya damu iliyokuwa ikimsumbua.
Katika kila kitu alichokuwa akikifanya, moyo wake ulimwambia kwamba alitakiwa kufanya kila liwezekanalo lakini kuhakikisha kwamba anamuua baba yake kwa mkono wake kama kulipa kisasi kwa kumuua mama yake na hata kutaka kumuua yeye na ndugu yake.
"Nitamuua baba yangu! Ninamchukia mno, ni lazima nitamuua," alisema david huku akionekana kumaanisha kile alichokuwa akikisema.
Baada ya siku mbili meli ikawasili Mombasa nchini Kenya, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumkabidhisha David kwa mwanaume aliyeitwa Nangai ambaye alitakiwa kuhakikisha David anapelekwa nchini Nigeria kwa mwanaume aliyeitwa Issour Ogwadugu ambapo huko alitakiwa kusoma mpaka pale atakapomaliza masomo yake chuoni.
"Hakikisha anasoma! Kwa gharama yoyote ile, nitalipia, lakini hakikisha anapata elimu bora, na kama anataka kumuua baba yake baadaye, ataifanya kazi hiyo na hakuna wa kumzuia," alisema Armando huku akimwangalia Nangai.
"Haina shida bosi!" alisema Nangai na mzee huyo kumgeukia David.
"David! Tutakuwa tunawasiliana, utafunguliwa akaunti benki na nitakuwa nakuingizia pesa. Hakikisha unasoma sana, ninahitaji ufaulu vizuri na usome sana kompyuta, umesikia?" alisema Armando na kumuuliza.
"Ndiyo!"
"Sawa."
Mzee Armando hakutaka kuendelea kubaki nchini Kenya, alichokifanya ni kupanda ndege yake na kuelekea nchini Ujerumani huku moyoni mwake akiwa na furaha tele kwani kwa kitendo cha kumpata David, mtoto aliyeonekana kuwa na hasira na baba yake kilionyesha kuwa mambo yake sasa yangeweza kwenda vizuri kama anavyotaka yawe.
***
"Did you get him?" (mmempata?)
"No sir but we are trying as much as we can," (bado mkuu ila tunajaribu kadiri tuwezavyo)
"Is the flight still there?" (bado ndege ipo hapo?)
"Yes sir!" (ndiyo mkuu!)
"This means he still there. Try to find him," (hii inamaanisha kwamba bado yupo huko. Jaribuni kumtafuta) ilisikika sauti kutoka kwenye simu.
Yalikuwa ni mawasiliano baina ya maofisa wa CIA waliokuwa nchini Tanzania na Marekani. Kila wakati simu ilikuwa ikipigwa kujua kilichokuwa kikiendelea nchini Tanzania, walipata taarifa kwamba Armando alifika nchini kwa ndege yake lakini baada ya kuchunguza humo hawakufanikiwa kumuona.
Hilo liliwachanganya sana lakini hawakutakakuacha, walikuwa na uhakika kwamba mwanaume huyo alikuwa humo Tanzania kwani hata walipojaribu kufanya mawasiliano na baadhi ya maofisa wao waliokuwa nchini Ujerumani walisema kwamba mwanaume huyo alisafiri na kulikuwa na picha kadhaa zilizomuonyesha akiwa uwanja wa ndege akipanda ndege yake ya kifahari na kuondoka.
Waliendelea kumtafuta kila kona huku macho na masikio yao yakiwa katika ndege ile. Siku iliyofuata kukawa na taarifa kwamba ndege ile ilitarajiwa kuondoka nchini Tanzania hivyo walikuwa na uhakika kwamba mwanaume huyo angeingia ndani ya ndege hiyo hivyo kuanza kuifuatilia kwa umakini kabisa.
Hawakutaka kupoteza hata sekunde moja, macho na masikio yao yalikuwa kwa kila mtu aliyekuwa akiingia ndani ya ndege hiyo. Watu wote waliingia na kila mtu aliyeingia humo ilionyesha kabisa Armando hakuwepo kitu kilichowachanganya kupita kawaida.
"Hayupo!" ilikuwa ni taarifa kutoka nchini Tanzania.
"Hayupo?"
"Ndiyo! Kila mtu amepanda ndani ya ndege lakini Armando hayupo."
"Hebu subiri! Unasema kwamba Armando hayupo?"
"Ndiyo mkuu!"
Kila mmoja alichanganyikiwa, walikuwa na uhakika kwamba mwanaume huyo alikuwa nchini Tanzania, kitendo cha kuambiwa kwamba Armando hakuwa mmoja wa watu walioingia ndani ya ndege hiyo iliwachanganya kupita kawaida.
Walichokifanya maofisa hao ni kwenda katika kitabu cha kuangalia orodha ya marubani wote waliokuwa wameingia kwa ndege zote zilizokuwa zikitua katika uwanja huo. Wakajitambulisha na kupewa orodha ya marubani waliokuwa wametua nchini Tanzania katika uwanja huo, walipoangalia, kilichowashtua ni kwamba ndege ile haikuwa imekodiwa na mtu mwingine kwani kama ingekuwa imekodiwa basi rubani angekuwa mwingine, lakini rubani ambaye jina lake liliandikwa mule alikuwa yuleyule rubani mkuu aliyekuwa akimuendesha bilionea huyo.
"Hapana! Huyu mzee atakuwa ameingia nchini Tanzania na kuondoka, imekuwaje? Mbona ametuchezea mchezo mchafu namna hii? Hebu ongea na wenzetu waambie wakamilishe kila kitu wakifika nchini Ujerumani. Huyo mzee hatakiwi kufika nyumbani kwake, ni lazima akamatwe haraka sana," alisema ofisa mmoja.
Taarifa zikapelekwa nchini Marekani na kusisitiza kwamba ndani ya ndege ile hakuwepo mwanaume huyo. Ilikuwa taarifa iliyomchanganya kila mmoja kwani walijua kabisa kuwa mwanaume huyo alikwenda nchini humo na kukaa kwa siku moja lakini kilichowashangaza ni kwamba aliondoka pasipo kumuona, yaani alipotea kama mzimu.
"Na serikali itasemaje?"
"Ya wapi? Ujerumani?"
"Ndiyo!"
"Hatujui ila hakikisheni mtu huyo anakamatwa hapohapo uwanja wa ndege."
"Sawa."
***
Taarifa zikaanza kusambazwa katika vituo vya polisi kuhusiana na utekaji uliofanyika wa familia ya bilionea Msuya. Kila polisi aliyepata taarifa hizo alishangaa, hawakuamini kama bilionea mwenye nguvu kubwa kiasi hicho familia yake ingeweza kutekwa kirahisi kama ilivyokuwa imetokea.
Polisi wakaingia kazini, wakaanza kufuatilia kila kitu kilichokuwa kimetokea, gari lililokuwa limetumika kuibeba familia hiyo mpaka kile cha mwisho kabisa kilichokuwa kimetokea. Ufuatiliaji wao huo ukakamilika baada ya kupokea taarifa kutoka kwa wasamaria wema ambao walisema kwamba usiku uliopita walisikia milio ya risasi kutoka katika Msitu wa Pande.
Kila mmoja alihisi kwamba huko ndipo kulipokuwa na familia hiyo hivyo kitu cha kwanza kilikuwa ni kwenda huko na kufuatilia kuona ni kitu gani kilikuwa kimetokea na kama familia hiyo ilikuwa huko au la.
Wakapanda kwenye magari yao na kuelekea huko. Hawakuchukua muda mrefu wakafika huku wakiwa na bunduki zao na kuanza kufuatilia. Walizijua njia za huko na hata walipofika, kulikuwa na alama za mataili ya gari ambazo zilionyesha kwamba hazikuonyesha kuwa za kipindi kirefu.
Polisi wakaingia ndani kabisa na kufuatilia. Baada ya dakika kadhaa ndipo macho yao yakatua katika gari moja ambalo lilikuwa na maiti za vijana watatu, mbali na gari hilo, kwa mbele pia kulikuwa na maiti za watu watatu zilizofumuliwa vichwa kwa risasi kadhaa, mwanamke mtu mzima na watoto wawili ambapo baada ya kuiangalia miili hiyo, wakagundua kwamba ilikuwa ni familia ya Bilionea Msuya, kila mmoja akashtuka.
“Mungu wangu!” alijikuta akisema polisi mmoja huku akiwa haamini kile alichokuwa akikiona.
 
Lete mkuu
ERIC SHIGONGO
MZIMU UNAOTABASAMU-14

Polisi waliendelea kushangaa, hawakuamini kile walichokuwa wakikiona mbele yao, maiti za watu watatu zilikuwa chini huku zikiwa zimeharibiwa vibaya kwa risasi. Kila mtu aliyeziona hakuweza kuvumilia kuziangalia mara mbili kwani zilikuwa na muonekano mbaya mno.
Hawakuziacha, wakazichukua na kuziingiza ndani ya gari na kisha kuzifuata maiti nyingine za vijana wa Lucy na kuziweka ndani ya gari lao na kuondoka mahali hapo. Mbele yao wakaona kazi kubwa, hawakujua ni kwa jinsi gani wangemwambia Msuya kwamba familia yake ilikuwa imeuawa kule msituni.
Kwa kuwa walikuwa nazo, hawakutaka kujipa uhakika kwamba zilikuwa zenyewe, ilibidi bilionea huyo aende hospitalini na kuthibitisha kama zilikuwa zenyewe au si zenyewe. Hilo halikuwa tatizo, walipozifikisha hospitalini, mzee huyo akapigiwa simu na kutakiwa kufika hospitalini.
Ndani ya dakika chache mzee huyo akafika huku akionekana kuchanganyikiwa. Taarifa aliyopewa kwenye simu ilimchanganya kupita kawaida, hakutaka kitu chochote kile, alichohitaji ni kuziona maiti hizo ambazo aliambiwa kwamba inawezekana zilikuwa za familia yake.
Akapelekwa mochwari huku akiwa na dokta mkuu wa hospitali hiyo, alipofika, masanduku yakatolewa na kuonyeshewa maiti hizo. Kilichomfanya kuzigundua ni nguo walizokuwanazo tu na si sura zao kwani zilikuwa zimeharibiwa vibaya sana kwa risasi.
“Familia yangu, mke wangu na watoto wangu....” alisema Mzee Msuya na kuanza kulia kama mtoto.
Moyo wake ulimchoma, aliumia kupita kawaida, hakuamini kama familia yake iliuawa kikatili namna ile. Kwa jinsi alivyokuwa akilia kila mtu akaonekana kumuonea huruma, kwani alilia kama mtu aliyekuwa amechomwa mno na kilichokuwa kimetokea.
Akawa na hasira na Armando, alijua dhahiri kwamba mwanaume huyo alifanya hivyo kwa kuwa alimtapeli mzigo wake wa madawa ya kulevya. Kwa kile alichokuwa amekifanya cha kuiangamiza familia yake kilikuwa kikubwa hata zaidi ya uhai wa familia yake.
Hakuwa na la kufanya, akakubaliana na matokeo kwamba familia yake iliangamia na hakukuwa na jambo alilotakiwa kufanya kwani hata kama angetuma watu kwenda huko Ujerumani kulipa kisasi wasingeweza kufanya hivyo kwa kuwa mzee huyo alikuwa na ulinzi mkubwa mno, mbaya zaidi hata serikali ya nchini humo ilikuwa ikimlinda usiku na mchana.
***
Lucy alikuwa chumbani kwake, masikio yake yalikuwa getini, alitaka kusikia mume wake akirudi na kumwambia kwamba aliwamaliza watoto wake kama alivyotaka au kama si hiyvyo basi apokee taarifa kutoka kwa vijana aliowatuma ambao wangemwambia kwamba waliwamaliza watoto hao.
Alitaka kuishi na mume wake tu, hakutaka kuona mtu mwingine akiongezeka. Kitendo cha kumwambia mume wake kwamba alitakiwa kuwamaliza watoto wake ni kwa sababu tu aliogopa kwamba mapenzi ya mwanaume huyo yangehamia kwa watoto wake na si yeye.
Muda ulizidi kwenda mbele, hakuona dalili zozote za kupokea taarifa kwa watu hao, mpaka inafika saa nane usiku bado hakukuwa na taarifa yoyote ile. Alichanganyikiwa, moyo wake ukaanza kuingiwa na hofu kwamba inawezekana watatu hao walipofika msituni waliuawa wote kwa pamoja.
Hakuwa na simu ya mkononi hivyo ilimbidi kusubiri. Aliendelea kusubiri mpaka inafika asubuhi bado hakuona dalili za kupata taarifa kuhusu kile kilichokuwa kimetokea msituni.
“Au waliwaua wote?” alijiuliza lakini akakosa jibu.
Ilipofika majira ya saa mbili asubuhi ndipo akasikia taarifa ya habari kutoka katika kituo cha redio cha taifa ambacho kilisema kuhusu maiti zilizokutwa msituni humo usiku uliopita. Alishangaa, maiti zilizokuwa zimetajwa zilikuwa nyingi tofauti na zile alizozitegemea ila aliposikia kwamba kwenye maiti hizo kulikuwa na watoto wawili, akawa na uhakika kwamba walikuwa David na Davis.
“Ila nimesikia yupo na mwanamke! Mwanamke gani tena? Au Gideon alikwenda na mwanamke kule msituni?” alijiuliza.
Hakutaka kuishia hapo, akaanza kufuatilia, baadaye akasikia kwamba majeruhi walikuwa katika Hospitali ya Kibwagizo iliyokuwa Kimara. Hakutaka kusubiri, ilikuwa ni lazima kwenda huko ili kujua kile kilichokuwa kimetokea na kama kwenye hao majeruhi alikuwemo mume wake.
Akaondoka na kwenda huko. Hakuchukua muda mrefu akafika na kuingia ndani ya hospitali hiyo. Kitu cha kwanza kabisa kilichomshtua ni uwepo wa Davis ambaye alikuwa kwenye benchi, alipomuona, akasimama na kumkimbilia, alipomfikia, akamkumbatia huku akilia.
Hakujua ni kitu gani kilitokea, kwenye taarifa ya habari alisikia kwamba kulikuwa na watoto wawili walikuwa wameuawa, akili yake ilimwambia kwamba walikuwa David na Davis, sasa ilikuwaje Davis awe hai? Wale waliokufa ni wakina nani? Na kama Davis alikuwemo hapo, David alikuwa wapi?
“Mama! Wamemuua David...wamemuua David...” alisema Davis huku akilia.
“Wamemuua David?” aliuliza Lucy huku akijifanya kushangaa.
“Ndiyo!”
“Wakina nani?”
“Watu kule porini,” alisema Davis huku akilia.
Lucy alitaka kupata uhakika wa jambo hilo, akamuuliza Davis kama mume wake alikuwemo humo akaambiwa kwamba alikuwemo japokuwa alipigwa risasi msituni. Akaambiwa chumba alichokuwemo na kuanza kwenda huko huku akitangulizana na nesi.
Alipofika, akamuona mumewe kitandani, alifungwa bandeji, alionekana kujeruhiwa mno. Kwa mwendo wa taratibu akaanza kumsogelea, akamkumbatia na kuanza kuzungumza naye kwa sauti ya chini.
“Mbona huyu yupo hai?” aliuliza Lucy kwa sauti ambayo hakukuwa na mtu aliyeisikia.
“Ni habari ndefu!”
“Kivipi? Na David je?” aliuliza huku akionekana kubadilika.
“Nafikiri alikufa msituni. David amekufa,” alisema Gideon na kuanza kububujikwa na machozi kwani moyo wake ulimuuma mno.
Kidogo moyo wake ukafarijika, kitendo cha kuambiwa kwamba mtoto mmoja alikufa kulimpa furaha na kuona kuwa huyo mmoja aliyebaki hakuwa mgumu kummaliza. Akajifanya kuhuzunika mbele ya Davis huku akimuonyeshea mapenzi ya uongo na kuahidi kumfariji na kumsaidia kwa kila kitu.
Kichwa cha Lucy kilikuwa na mawazo tele, alikuwa akifikiria ni kwa jinsi gani angemmaliza mtoto aliyekuwa amebaki. Baada ya siku mbili, Gideon akaruhusiwa kutoka hospitalini na alipoulizia kuhusu watoto waliokuwa wameuawa, akaambiwa kwamba walizikwa.
“Ila mmoja ni mtoto wangu!” alisema Gideon.
“Mtoto wako? Kivipi? Mbona watoto wote ni wa Mzee Msuya?” alihoji polisi mmoja.
“Mzee Msuya? Kivipi yaani?”
Akaelezewa kila kitu kilichokuwa kimetokea msituni, hakutaka kuamini, moyo wake ulimwambia kwamba mmoja alikuwa mtoto wake na si wa mzee huyo. Akauliza kama walipata nafasi hata ya kuaga sura ya mwisho akaambiwa kwamba hakukuwa na tukio hilo kwani sura zao ziliharibiwa mno kwa risasi.
“Watakuwa wamemzika mtoto wangu!” alisema Gideon huku akilia kwa maumivu makubwa, wakati mwingine alikuwa akijuta hatua aliyochukua ya kumsikiliza mkewe na kuona kwamba kweli watoto wake walitakiwa kuuawa.
***
David alikuwa nchini Kenya, bado moyo wake ulikuwa na hasira na baba yake, hakuamini kama mwanaume huyo alitaka kuwamaliza msituni kwa sababu ya kumfurahisha mwanamke aliyekuwa akiishi naye. Moyo wake ni kama ulikuwa umejeruhiwa, aliyaona matukio ya mauaji msituni, akili yake ikavurugika na kuanza kuwaza kuhusu kumwaga damu tu.
Alipokuwa akilala usiku, ni ndoto za mauaji ndizo zilizokuwa zikijirudia kichwani mwake na hata wakati mwingine alipokuwa peke yake, alihisi kama kulikuwa na maiti pembeni yake na kusikia harufu ya damu. Mauaji ya msituni yakaanza kuibadilisha akili yake na kuona kwamba kuua kilikuwa kitu cha chepesi kuliko hata kuruka kamba.
Hapo Kenya aliishi vizuri nyumbani kwa Nangai ambaye aliambiwa kwamba ni lazima apelekwe nchini Nigeria kwa ajili ya kusoma. Baada ya siku nne hati zake zilipokamilishwa huku akifanyiwa magumashi na kuonekana kwamba ni raia wa Kenya, akapelekwa nchini Nigeria kama ilivyokuwa imeagizwa.
Huko akapokelewa na mwanaume aliyeitwa kwa jina la Issour Ogwadugu aliyekuwa akiishi katika Jiji la Lagos hapo Nigeria. Huyo ndiye alitakiwa kukaa naye kwa kipindi chote ambacho angekuwa shuleni alipotakiwa kusoma mpaka chuo kikuu.
Akaanza masomo ya kidato cha kwanza katika Shule ya St. Mary iliyokuwa hapo Lagos. Siku ya kwanza kuingia shuleni kila mtu akabaki akimwangalia, alionekana kuwa mwanafunzi mkimya, mpole ambaye hakuonekana kuwa na wasiwasi hata kidogo.
Siku hiyo hakutaka kuzungumza na mwanafunzi yeyote yule, kichwa chake kilikuwa na mambo mengi, kila alipokuwa akiingia darasani, alikuwa kimya mpaka muda wa kuondoka. Wanafunzi wengi wakaanza kumuogopa, alionekana kuwa mwanafunzi asiyekuwa wa kawaida, wengine wakahisi kwamba alikuwa bubu lakini walipowaambia walimu kuhusu jambo hilo waliambiwa kwamba alikuwa mzima kabisa.
Hakuwa muoga, alikuwa mtoto jasiri, kila siku alipokuwa akiingia darasani kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuchukua peni na karatasi na kuandika majina manne ambayo watu hawakuelewa yalimaanisha nini. Hakukuwa na mwanafunzi aliyeuliza, kila mmoja aliogopa kwa kuwa tu mbali na ukimya wake alionekana kuwa na jambo zito moyoni mwake.

Lilian: Wewe ni mama yetu, ulitupenda, ni mama ambaye umekuwa pamoja nasi kwa kipindi kirefu. Kansa ilikutesa kitandani lakini mpumbavu, baba yetu, Gideon akakumaliza huku kila mmoja akisingizia kwamba kansa ndiyo imekuua.

Davis: Wewe ni mdogo wangu, hujui kitu chochote kilichotokea. Ukweli ni kwamba baba alimuua mama kwa ajili ya mwanamke wake. Siku ambayo tulipelekwa msituni ni kwa sababu alitaka kutumaliza na sisi pia.

Gideon: Wewe ni baba yangu, mtu ambaye niliamini kwamba unatupenda kwa moyo wa dhati. Sikuamini niliposikia ukiongea na malaya wako kwamba ulimuua mama kwa ajili yake na tena ulikuwa mbioni kutuua na sisi. Hakika dhambi hii itakuhukumu, mfano wa hadithi ya John utatokea maishani mwako.

Lucy: Wewe ni mwanamke mpumbavu sana, inaonyesha ulimlazimisha baba amuue mama ili uolewe wewe. Umeleta matatizo katika familia yetu, ni mwanamke mwenye roho ya kishetani. Nakuahidi kwamba NITAKUUA. Haitojalisha ni muda gani utapita, ninasema kwamba ni lazima nikuue kama ulivyopanga mipango ya kumuua mama yangu.

Baada ya kuandika majina na ujumbe kwa kila jina, akachukua karatasi hiyo na kuiweka katika begi. Akapiga magoti darasani hapo na kumuomba Mungu amsaidie kutimiza kila kitu alichokiandika kwani kwa yale yaliyoptokea, hakuona sababu ya Lucy kubaki hai huku akiendelea kuyafurahia maisha.
 
ERIC SHIGONGO
MZIMU UNAOTABASAMU-15

Mpaka miezi mitatu inakatika shuleni, David hakuwa ameongea na mwanafunzi yeyote, kila mtu alikuwa akishangaa, walimu hawakuelewa ni kitu gani kilikuwa kikiendelea kwa mtoto huyo ambaye muda wote alionekana kuwa na mawazo mengi.
Hawakutaka kukubali, walichokifanya ni kuwatuma wanafunzi kadhaa kwa lengo la kutengeneza urafiki naye ili aweze kuchangamshwa shuleni hapo. Mwanafunzi wa kwanza kutumwa alikuwa Kennedy Okonko, alikuwa miongoni mwa wanafunzi wacheshi mno shuleni hapo.
Alianza kidogokidogo, David alipokuwa akifika shuleni, mtu wa kwanza kumfuata na kuanza kuzungumza naye alikuwa Kennedy. Kila mmoja alitegemea kwamba kijana huyo angefanikiwa kumchangamsha David lakini sula hilo likashindikana kabisa na David akabaki kama alivyokuwa.
Hilo halikuwa tatizo, walimu wakawatuma wanafunzi wengine lakini wote hao waliambulia patupu. Japokuwa David alikuwa mkimya aliyekuwa akisumbuliwa na mawazo lakini darasani alikuwa na uwezo mkubwa, alifaulu vizuri masomo yake kiasi kwamba walimu wakahisi kuwa alikuwa na akili za kuzaliwa.
Mwaka wa kwanza ukakatika. Mara nyingi alikuwa akiwasiliana na mzee Armando ambaye alimsisitizia kwamba alitakiwa kusoma sana kwani alikuwa na mipango naye mingi sana. Hilo halikuwa tatizo kwa David, mzee huyo alimchukulia kama baba yake, alimpenda na kumsikiliza, hakukuwa na kitu chochote ambacho aliambiwa na mzee huyo na asifanye.
Akanunuliwa kompyuta ya mapajani (laptop) na kuambiwa kwamba alitakiwa kujifunza sana kompyuta kwani alikuwa na kazi kubwa mbele yake. Hilo halikuwa tatizo kubwa, akawa na kazi kubwa ya kujifunza mambo mbalimbali mpaka pale alipoanza kuizoea kompyuta kwa vitu vidogo.
Baada ya kumaliza miaka minne shuleni, akaanza masomo ya Chuo katika Chuo cha Yaba Technology kilichokuwa hapohapo Lagos nchini Nigeria.
Kama alivyokuwa shuleni, hata chuoni hapo alikuwa mwanafunzi mpole na mkimya mno, hakuwa mzungumzaji, muda mwingi alikuwa akijifunza mambo mengi kwenye kompyuta, alijua kwamba ili akili yako iweze kukua ilikuwa ni lazima kuhakikisha unajifunza mambo mengi yanayotokea duniani.
Hakuwa akiacha, kila siku ilikuwa ni kujifunza jambo moja baada ya jingine na mpaka anaingia mwaka wa pili chuoni hapo, kulikuwa na mambo mengi makubwa aliyokuwa akiyajua katika dunia hii kuliko mtu mwingine yeyote chuoni hapo.
“Habari yako David!” aliisikia sauti ya mtu ikimsalimia.
David akayainua macho yake na kumwangalia mtu aliyemsalimia. Macho yake yakatua usoni mwa msichana mrembo maji ya kunde aliyekuwa amesuka nywele zake kwa staili ya yeboyebo. Alikuwa na uzuri wa sura, vishimo mashavuni mwake, macho ya goroli na kila David alivyokuwa akimwangalia, hakuisha hamu.
Hakuitikia salamu hiyo, alibaki akiwa ameduwaa, uzuri wa msichana huyo ulizunguka kichwani mwake na kumfanya kutetemeka kwani hakuamini kama kuna siku angefuatwa na msichana mrembo kama huyo na kuanza kuzungumza naye.
“Nakusalimia. Habari yako,” alisema msichana huyo.
Ni kama David alishtushwa kutoka katika lindi la mawazo, akaitikia, msichana huyo akakaa katika kiti kilichokuwa karibu na kuanza kuzungumza. Alikuwa mcheshi, aliyekuwa akiongea maneno mengi kwa wakati mmoja.
David alishangaa, hakuamini kama kungekuwa na msichana aliyekuwa akiongea harakaharaka kama huyo aliyekuwa naye. Hakuzungumza kitu, akili yake ilitulia kwa ajili ya kuutathmini uzuri wa msichana huyo mrembo.
“Umenielewa?” aliuliza baada ya kuongea mamneno mengi mfululizo.
“Umesemaje?”
“Kumbe ulikuwa hunisikilizi!” alisema msichana huyo.
“Mambo mengi! Hivi unaitwa nani?”
“Naitwa Mercy Igwegwe!”
“Ooh! Sawa! Naitwa David Armando!”
“Nimefurahi kukufahamu!”
“Nashukuru!”
Huo ndiyo ukawa mwanzo wa urafiki wao, muda mwingi chuoni walikuwa pamoja. Japokuwa kwa kipindi kirefu David alikuwa mkimya lakini kidogo Mercy akaweza kuyabadilisha maisha yake. Kwa kuwa wote shuleni hapo walikuwa wanajifunza sana kompyuta, alichokifanya Mercy ni kumtambulisha kwa watu waliokuwa wakifahamu sana kompyuta na kuanza kujifunza.
Kidogo akachangamka, kila alipokuwa akifika chuoni, kitu cha kwanza kilikuwa ni kukutana na marafiki zake watatu aliotambulishwa na Mercy, walioitwa Mike, Tim na Joshua.
Hao ndiyo walikuwa watu wa karibu yake zaidi, kila alipokuwa akienda chuoni, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuonana na kupiga stori huku wakiendelea kujifunza mambo mengi katika kompyuta zao. Wakaamua kutengeneza kikundi chao cha watu watano walichokipa jina la Pentagon, yaani wakiwa na maana ya pande tano.
Hao walikuwa wataalamu wa kompyuta chuoni hapo, walikuwa na uwezo wa kufanya kitu chochote kile kwenye kompyuta. Walikuwa na ujanja wa kudukua barua pepe za watu wengine na kufanya kila kitu walichokuwa wakikihitaji. Mambo yao yalikuwa ya siri sana, walikuwa na uwezo wa kudukua mpaka barua pepe za chuo chao na kufanya kitu chochote walichokuwa wakikitaka.
Waliwasumbua watu wengi pasipo kugundulika, walitumia barua pepe za watu wengine kuwatukana watu wengine na hata wale wanafunzi ambao walionekana kutokuwapenda, waliingia kwenye barua pepe yake na kuandika mambo ya mapenzi, matusi na kumtumia mkuu wa chuo ambaye alichukua jukumu la kumfukuza shule mtu mwenye barua pepe kwa kuhisi kwamba yeye ndiye aliyeandika upuuzi aliokuwa ametumiwa.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yao kila siku. Hawakuwa na matatizo ya pesa, kila walipokuwa na uhitaji wa pesa walishangaa kuona David akitoa kiasi hicho. Hawakujua alikuwa nani, hakuwa Mnigeria ila kwa kuwa kila mmoja alimfahamu kama Mkenya, wakahisi kwamba baba yake alikuwa mmoja wa matajiri wakubwa nchini humo.
“Nataka tufanye kitu kimoja,” alisema Mike huku akiwaangalia wenzake.
“Kitu gani?”
“Tuibe pesa benki!”
“Tuibe pesa benki?”
“Ndiyo! Au mnaogopa?” aliuliza Mike.
Kila mmoja alishangaa, hawakudhania hata siku moja kama rafiki yao huyo angewaambia kitu kama hicho. Kitu kilichokuja akilini mwao ni kuvamia benki kwa bunduki na kuanza kuiba. Hakukuwa na mtu aliyethubutu kufanya hivyo, kila mmoja aliogopa.
“Huo ni upumbavu Mike! Siwezi kwenda benki kuiba pesa,” alisema Joshua.
“Hahaha! Simaanishi kuvamia. Tunaijua kompyuta, hatuwezi kuingia katika database ya benki na kufanya mambo yetu mpaka tufanikiwe kuiba pesa?” aliuliza Mike.
“Mmh! Itawezekana kweli?” aliuliza Mercy, kwa jinsi alivyokuwa akiijua kompyuta, hakufikiria kama jambo hilo lingewezekana hasa kwa miaka hiyo.
“Inawezekana kabisa. Cha msingi tuanzeni kufanya jambo hilo. Tupigeni hata naila bilioni tano kila mtu apate naila bilioni moja,” alisema Mike.
Lilikuwa jambo kubwa na gumu kufanyika lakini kwa kuwa walikuwa wanahitaji zaidi pesa na kujipima kuona kama walikuwa na uwezo, wakafanya kama walivyokubaliana na hivyo mchakato kuanza mara moja.
Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutafuta codes maalum ambazo zingewawezesha kuingia kwenye database yao kirahisi sana. Walijua kuwa kulikuwa na ulinzi mkubwa mno kwani kitedo cha kuivuruga database ya benki ilimaanisha kwamba ingewafanya kuchukua pesa kirahisi pasipo kugundulika.
“Kuna namba nne ambazo ndizo zinalinda hiyo database ya beki kuu ya Nigeria,” alisema Tim.
“Ni nne tu?”
“Ndiyo! Hizo ni namba nyingi sana, mara nyingi zingine zinatumia namba mbili au tatu lakini kwa benki ile wanatumia nne. Hizo tukizipata zitatufanya tuingie kwenye database yao, tufute mafaili na kuiba pesa pasipo kugundulika kwenye akaunti za wateja wao,” alisema Tim.
“Sawa. Sasa hizo namba tutazipata vipi?” aliuliza David ambaye alikuwa kimya kwa muda mrefu.
“Hizo namba zinapatikana kwa watu wanne tofauti. Kuna mkurugenzi wa benki hiyo, Bwana Daniel Ife, kuna meneja, Bwana Sebastian Kanayo, mwanamke aitwaye Pamela Ogwu na msichana mmoja mrembo anayeitwa Cecilia Michael,” alisema Tim.
“Hizo namba wanazo vichwani au?”
“Hapana! Kuna pleti walikabidhiwa, hizo ndizo zenye namba hizo. Hatujui zipo wapi ila nahisi kama tukifanikiwa kuwa karibu na watu hao, hizo pleti zitapatikana kwa urahisi sana. Hizo pleti zina codes zake, kwanza ni lazima tutengeneze programu ambayo tukikaribia na pleti hizo, ituambie kwamba ipo hapo,” alishauri Tim
“Ni wazo zuri. Kwa hiyo tukipata pleti tumefanikiwa?” aliuliza Joshua.
“Ndiyo! Tukipata pleti, siku inayofuatia itakuwa ni ya kuomboleza kwa matajiri. Kwanza tutengenezeni hiyo programu.”
“Sawa. Tena tufanyeni haraka,” alisema Mike na kazi ya kutengeneza programu.
Walichukua siku ishirini mpaka kukamilisha kutengeneza programu hiyo waliyoipa jina la Pentagon 2.4 ambayo ilikuwa na kazi maalumu ya kugundua mahali pleti hizo zilipokuwa. Kila mmoja akapewa program hiyo, wakaziweka katika simu na kompyuta zao na hivyo kukubaliana kwamba watu hao wanne ilitakiwa kutafutwa haraka sana na kugundua namba walizokuwanazo kwa ajili ya kuwawezesha kuingia katika database ya benki hiyo.
David akapewa Cecilia Michael, msichana wa miaka thelathini aliyekuwa na uzuri wa ajabu ambaye alikuwa na cheo cha usimamizi katika benki hiyo. Mike akatakiwa kumsimamia Pamela Ogwu huku Tim akitakiwa kumsimamia Daniel Ife na Joshua alitakiwa kumsimamia Sebastian Kanayo na kuhakikisha kila mmoja anapata namba zilizoandikwa katika pleti walizokuwanazo watu hao wanne.
“Tukifanikiwa! Sisi ni mabilionea,” alisema Mike, wakakubaliana na hatimaye kazi kuanza mara moja.
***
Gideon hakuwa sawa, mawazo yalimjaa kichwani mwake, hakuwa na raha hata kidogo, moyo wake ulimuuma na muda wote alikuwa akimfikiria mtoto wake, David ambaye mpaka kipindi hicho alikuwa na uhakika kwamba alikufa. Alikumbuka namna alivyokuwa akifurahia na watoto wake kwa pamoja, leo hii mmoja hakuwa naye, alishawishiwa na mke wake kuua na kufanya hivyo.
Hakutaka kuzungumza na Lucy, alimuepuka kwani kwa ushawishi aliokuwa ameufanya wa kumtaka kuiangamiza familia yake ulikuwa mbaya na kumpa mawazo mengi. Kwa Davis ambaye alikuwa amebaki, hakutaka kuona akifanya jambo lolote baya, kama kufa, basi afe pale tu Mungu angetaka hilo litokee.
Siku zikaendelea kukatika, mwezi wa tatu ulipoingia tangu kufa kwa David Lucy akaonyesha dhahiri kwamba alikuwa akimchukia Davis, hakumpa malezi ambayo alitakiwa kumpa kama mama aliyeachiwa majukumu ya kumlea. Hilo lilimuumiza kijana huyo lakini hakujali, kwake, alichokiangalia ni maisha yake tu.
Lucy hakutaka kuacha, alijua kwamba David alikufa hivyo mtu aliyebaki alikuwa Davis tu, akaanza kumshawishi Gideon ili amuue Davis kwani mpango wake ulikuwa palepale, watoto wote wauawe.
“Lucy usinivuruge kabisa,” alisema Gideon kwa sauti ya hasira kiasi kwamba Lucy akaogopa, ila akajikaza.
“Nisikuvuruge kwa nini?”
“Siwezi kumuua Davis, ni mtoto pekee niliyebaki naye, nimuue ili iweje, nisikilize wewe mwanamke, siwezi kumuua Davis na tutakaa naye mpaka vifo vyetu,” alisema Gideon huku akivimba kwa hasira.
“Kwa hiyo hutaki kumuua? Kwa hiyo nikawaeleze polisi kwa kilichotokea kwa mkeo?” aliuliza Lucy kwa mikwara, ili kumuonyeshea kwamba kwa kipindi hicho hakuwa na masihara hata kidogo, Gideon akaufuata mlango na kuufungua.
“Nenda! Tena wahi kabla kituo hawajafunga. Tena uwaambie kila kitu malaya mkubwa,” alisema Gideon kwa hasira.
Lucy hakuamini, mwanaume yule aliyekuwa akimuendesha aliibadilika, hakuwa Gideon aliyemzoea, huyu alibadilika na alionekana kuwa tayari kufanya jambo lolote lile la hatari lakini kumlinda mtoto wake aliyekuwa amebaki.
Lucy akanyong’onyea, akawa mpole na kuhisi kuwa kama angeendelea kumshawishi mume wake basi kuna siku angemuua kama alivyofanya kwa mke wake. Kuanzia siku hiyo hakutaka tena kumwambia mume wake suala la kumuua Davis kwani alianza kuyaona majuto ya mumewe kwa kile alichokuwa amekifanya kwa mke na mtoto wake.
Gideon hakutaka tena kumwamini mke wake, alihisi kuwa kuna siku angeweza kumfanyia kitu kibaya Davis hivyo alichokifanya ni kumuhamisha shule na kumpeleka nchini Kenya ambapo akaanza masomo katika Shule ya Sekondari ya St. Louis iliyokuwa jijini Nairobi, shule ambayo ilikuwa na watoto wa matajiri na viongozi wakubwa nchini humo.
 
ERIC SHIGONGO
MZIMU UNAOTABASAMU-16

“Koh koh koh...” kilisikika kikohozi kutoka kwa mwanaume mmoja aliyekuwa ameingia katika jengo la Benki Kuu ya Nigeria.
Macho yake yalikuwa yakimwangalia msichana aliyekuwa na umbo matata, uzuri wa ajabu aliyekuwa akipiga hatua fupifupi kuelekea katika mlango ambao ndani yake kulikuwa na ngazi za kuelekea ghorofa ya juu.
Kwa kumwangalia kwa mbali tu halikuwa jambo gumu kugundua kwamba msichana huyo alikuwa miongoni mwa wasichana warembo waliokuwa wakifanya kazi katika benki hiyo. Alivalia sketi fupi nyekundu iliyoishia juu ya magoti, blauzi na skuna zilizoifanya sakafu kupiga kelele kila alipokuwa akipiga hatua.
Msichana huyo aliitwa Cecilia Michael, japokuwa alikuwa akifanya kazi katika benki hiyo lakini wanaume hawakumzoea, kila siku alipokuwa akiingia aliwasumbua kwa kumwangalia kila alipokuwa akipiga hatua kuelekea ofisini mwake.
Cecilia alikuwa msimamizi wa benki hiyo, yeye ndiye aliyekuwa akisimamia mahesabu yote yaliyokuwa yakifanyika. Alikuwa akilipwa mshahara mkubwa katika benki hiyo, aliheshimiwa, kila alichokuwa akikitaka alipewa pasipo kuulizwa swali lolote lile.
Alipewa jumba kubwa na la kifahari, gari kali ya kutembelea, BMW ambayo hakukuwa na mtu mwingine yeyote nchini humo ambaye alikuwa na gari kama lake. Mbali na kuwa na mafanikio makubwa huku akiwa na PhD ya mambo ya biashara lakini mpaka kipindi hicho alichokuwa na miaka thelathini msichana huyo hakuwa na mwanaume, kila mtu alikuwa akimuogopa kwa kuwa tu alikuwa na pesa.
Hilo ndilo jambo lililomfanya kuwa singo mpaka kipindi hicho. Wanaume walimuogopa kila siku kiasi kwamba akakosa furaha kwani alihitaji mwanaume wa kuwa naye, kitendo cha kukimbiwa kiliuumiza moyo wake. Cecilia alitembea mpaka katika ofisi yake na kukaa kitini. Akachukua rimoti na kuwasha kiyoyozi.
“Naomba uje ofisini,” alisema Cecilia alipokuwa akizungumza na sekretari wake kupitia simu ya mezani.
Ni ndani ya sekunde kumi tu, mlango ukafunguliwa na msichana mwingine ambaye alikuwa mrembo akaingia. Akamwambia kile alichotaka kumwambia na kutoka.
Kichwa chake kilifikiria mapenzi, kila alipoingia katika mitandao ya kijamii alikutana na picha za wanaume wengi aliotamani sana kuanza uhusiano nao lakini kitendo cha kuangalia picha zake alizopiga ofisini, kwenye gari lake na hata nyumbani, hata wanaume hao wa mitandaoni wakaanza kumuogopa.
Aliendelea kuishi katika maisha hayo mpaka siku ambayo alimpokea mgeni aliyejitambulisha kwa jina la David Armando. Mwanaume huyo alifika ofisini hapo na kutaka kuonana naye. Alimwambia sekretari ambaye alimwambia kwamba alitaka kuonana na kuzungumza kwani kulikuwa na jambo kubwa alilotaka kumshirikisha.
Haraka sana sekretari akampigia simu na kumwambia kuhusu mwanaume huyo. Kitendo cha Cecilia kusikia kwamba alikuwa mwanaume, akababaika na kutamani kuonana naye kwani kitu pekee kilichojengeka akilini mwake ni kwamba kulikuwa na nafasi kubwa ya kuwa na mwanaume kama tu angeweza kuonana na kuzungumza naye.
Mlango ukafunguliwa, David akaingia. Kwa jinsi muonekano wake ulivyokuwa, Cecilia akababaika, hakuamini kama angeweza kuonana na mwanaume aliyekuwa na sura nzuri kama David. Alivalia shati jeupe na tai nyekundu huku kwa chini akiwa na suruali nyeusi, hakuishia hapo, usoni mwake alikuwa na miwani ya macho iliyomfanya kupendeza kuliko kawaida.
Alipomuona Cecilia tu, uso wake ukajawa na tabasamu pana, akamsogelea, akamsalimia na kukaa karibu naye. Akaanza kuzungumza naye mawili matatu na kumwambia kwamba alikuwa na uhitaji wa kujua riba ambayo angewekewa kama alitaka kukopa kiasi cha naila bilioni moja kutoka katika benki hiyo.
“Ni kiasi kikubwa sana cha pesa, una kampuni yoyote ile?” aliuliza Cecilia huku akimwangalia David.
“Yeah! Ninayo. Ninahitaji kufahamu kuhusu riba zenu kabla hata ya kufanya uamuzi wangu wa kuchukua mkopo huo hasa katika benki kubwa kama hii,” alisema david.
“Riba huwa ni asilimia tano tu. Ila hatutoi mikopo kwa wafanyabishara, huwa mikopo inatolewa kwa benki hizi ndogo,” alisema Cecilia huku akimwangalia aliyeonekana kuwa na furaha kuongea na mwanaume huyo.
David hakutaka kuyatuliza macho yake, muda mwingi alikuwa akiiangalia simu yake. Alitaka kufahamu kama hiyo pleti ilikuwa katika ofisi hiyo au la. Simu haikuwa ikimuonyesha kitu chochote kile kumaanisha kwamba pleti haikuwa ndani ya ofisi hiyo.
“Haipo humu? Ipo wapi sasa?” alijiuliza David huku akiendelea kuangalia simu yake.
Hakutaka kuacha kuzungumza na msichana huyo na hakutaka kuona huo unakuwa mwisho wa kuwasiliana na msichana huyo, alibaki akizungumza naye mambo ya biashara lakini baadaye wakahama na kuanza kuzungumza mambo mengine kabisa. Wakaanza kujuana zaidi, kuhusu familia zao na hata walipotoka.
“Na vipi kuhusu mpenzi?” aliuliza David huku akimwangalia Cecilia.
“Hapana! Sina mpenzi!”
“Kwa nini? Mbona u msichana mrembo sana, unawezaje kuwa singo?” aliuliza David huku akimwangalia Cecilia.
“Kawaida tu! Unajua nyie wanaume hamjiamini kabisa.”
“Labda wao. Mimi ninajiamini, nina uwezo wa kumiliki watoto wakali kama wewe,” alisema David na wote kuanza kucheka.
Walizungumza mpaka muda ulipofika, wakabadilishana namba za simu na David kuondoka ofisini hapo. Kidogo hiyo ilionyesha matumaini kwa David, akaona kabisa kwamba angefanikiwa kuwa karibu na msichana huyo na hatimaye kuipata namba aliyokuwa nayo ambayo ingetumika katika kuingia kwenye database ya benki hiyo.
“Umefikia wapi?” aliuliza Mike kwenye simu.
“Nimefanikiwa kuonana naye. Nikaingia mpaka ofisini mwake,” alijibu David.
“Vipi kuhusu namba. Umeipata?”
“Hapana. Nahisi pleti hakuwa nayo mule kwani simu haikunionyesha chochote kile,” alisema David.
Hakutakiwa kuachana na msichana huyo, huo ulikuwa mwanzo wa kuweza kuzoeana na mwisho wa siku kupata namba alizokuwa akizihitaji kwa nguvu kubwa.
Kwa kuwa alihitaji sana kitu kutoka kwa msichana huyo, akatamani sana kuendelea kuwasiliana na msichana huyo. Alipofika nyumbani tu, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumpigia simu na kuanza kuongea naye. Alimwambia mambo mengi, alimsifia kwa jinsi alivyokuwa huku akimpongeza Mungu kwa kazi kubwa ya kumtengeneza msichana mrembo kama alivyokuwa.
Moyo wa Cecilia ukajisikia faraja, hakuamini kama mwisho wa siku angefanikiwa kumpata mwanaume aliyeonyesha kabisa kuwa na mapenzi juu yake. Kwa jinsi alivyokuwa akisifiwa, akajiona kuwa mrembo kuliko wanawake wote katika dunia hii.
Siku nzima walibaki wakiwasiliana, kwa kitendo cha kukaa kwa saa sita huku wakiwasiliana, Cecilia akaanza kuhisi mapenzi moyoni mwake na kuona kwamba David alikuwa mwanaume pekee aliyekuwa ameandaliwa na Mungu kwa ajili yake.
Hiyo ilikuwa siku ya kwanza, ya pili ilivyoingia wakazidi kuwasiliana kwenye simu. Siku hiyo David hakutaka kuchelewa, akamuomba kutoka naye mtoko usiku, hilo halikupingwa na msichana huyo, akakubaliana naye na hatimaye kutoka kwa mara ya kwanza.
Kitu alichokihitaji David ni kuuchanganya moyo wa msichana huyo tu hivyo akamuonyeshea mapenzi ya dhati, akamchangamsha na kumfanya kujiona kuwa mwanamke wa kipekee sana katika dunia hii.
“Ninakupenda David. Wewe ni mwanaume mzuri sana, naomba usiniache, nitakufa,” alisema Cecilia huku akimwangalia David kwa macho ya kuita.
“Sawa. Nakupenda mpenzi, usijali, nakuahidi kukulinda maisha yangu yote,” alisema David huku akiachia tabasamu pana lililoufanya moyo wa msichana huyo kuchanganyikiwa.
Yalikuwa mafanikio makubwa kwa David, akakutana na wenzake na kuwaambia kwamba alifanikiwa kwa kiasi kikubwa kumshawishi msichana huyo na muda huo tayari walikuwa wapenzi hivyo kazi iliyokuwa imebaki ilikuwa ni kufanya kila liwezekanalo kupata kile walichokuwa wakikihitaji.
“Kama kweli hata hiyo pleti ofisini kwake, basi nina uhakika itakuwa nyumbani kwake, fanya juu chini mpaka upate nafasi ya kufika nyumbani kwake,” alisema Mike.
“Hakuna shida. Nitafika tu. Ni mwanzo mzuri na nitamtumia kadiri niwezavyo kupata kila kitu tunachohitaji,” alisema David huku akiwa na uhakika kufanikisha kile kilichohitajika wakati huo.
***
Mzee Armando aliendelea na biashara zake kama kawaida, mara kwa mara alikuwa akimpigia simu David na kuzungumza naye. Alikuwa na mipango mingi ya kufanya naye, aliamini kwamba kwa namna moja au nyingine ilikuwa ni lazima kijana huyo amsaidie ili kufanikiwa katika mipango yake aliyokuwa amejiwekea.
Kila siku hakuacha kumsisitiza kuhusu kusomea kompyuta, alijua kabisa kwamba kazi alizokuwa akitaka kumpa zingemuweka katika wakati mbaya, kutafutwa na hata kuuawa ila kama angekuwa mtaalamu wa mambo ya kompyuta basi ingemsaidia kupambana na watu hao.
Hakuacha kumpa pesa, alimtumia kiasi kikubwa cha pesa huku akimsisitizia kwamba ni lazima afanye kila linalowezekana kuzitumia pesa hizo kwa matumizi mazuri. Aliendelea kumtumia kompyuta kila kompyuta moja ilipokuwa ikiharibika, mpaka David alipoungana na marafiki zake na kuwa na mpango wa kuiba benki kwa kutumia kompyuta, alimwambia mzee huyo ambaye alimuunga mkono kwa kile alichotaka kukifanya.
“Kuna mtu ningependa niwatambulishe kwake,” alisema Mzee Armando, alikuwa akiiambia familia yake.
“Mtu gani?” aliuliza mtoto wake wa kiume, Jericho.
“Ndiye nani huyo?” aliuliza mtoto wake mwingine aliyeitwa Natasha.
“Ni Muafrika, nadhani atanisaidia kwa mambo mengi nitakayotaka kuyafanya ili kujilinda, yeye ndiye atakayekuwa akiwamaliza wabaya wangu,” alisema Mzee Armando huku akiwaangalia watoto wake.
Hawakuwahi kumfahamu mtu huyo aliyetajwa kwa jina la David, hawakujua alifananaje kitu kilichowafanya kuwa na hamu ya kutaka kumuona. Siku zikaendelea kukatika, mara nyingi aliwaambia kuhusu mwanaume huyo ambaye alihisi kabisa kwamba hapo baadaye angekuwa mtu hatari sana katika harakati zote za kumlinda na kuwazuia watu wengine kumsogelea.
“Una uhakika atakulinda?” aliuliza Jericho.
“Unatakiwa kuniamini katika hilo. Atanilinda tu,” alisema Mzee Armando.
***
Cecilia alikuwa na furaha tele, moyo wake ukafarijika na kuona kwamba mwanaume aliyekutana naye alikuwa ni wa ndoto yake na kila siku angeendelea kuwa naye maisha yake yote. Hakutulia, kila wakati alikuwa akimpigia simu kumjulia hali, alimpenda na kumthamini na kuona kwamba hakukuwa na mwanaume aliyekuwa akimpenda kama ilivyokuwa kwa David.
Hawakucha kuonana, kila siku walikuwa wakionana sehemu mbalimbali. Msichana huyo moyo wake ulijitolea kwa David, alimwambia kwamba kwake, hakukuwa na kitu alichokihitaji maishani mwake kama kuwa naye mpaka kifo chake.
David hakutaka kuwa na haraka, alijua dhahiri kwamba kitu pekee alichokihitaji kwa msichana huyo ni kufika kwake. Huko ndipo kulikuwa na pleti zilizokuwa na namba za kuingilia katika database ya Benki Kuu ya Nigeria na kuiba pesa walizokuwa wamepanga kwamba piga ua ilikuwa ni lazima waziibe.
Hakutaka kumwambia Cecilia suala la kwenda kwake, alichokifanya ni kuendelea kumuonyesha mapenzi ya dhati ili mwisho wa siku amwambie kwamba lingekuwa jambo jema kama wangekwenda nyumbani kwake ili kupafahamu.
Walichokifanya kundi hilo la Pentagon ni kupanga jumba la kifahari na kujifanya kwamba hapo ndipo palikuwa kwao. Yaani siku ambayo David angekwenda na Cecilia nyumbani hapo angemtambulisha kama kulikuwa kwake ili amwamini ili kuwapiga pesa kirahisi.
Siku ambayo alimpeleka msichana huyo katika jumba hilo la kifahari, Cecilia hakuamini, lilikuwa jumba kubwa lililokuwa na kila kitu ndani. Ilionyesha kwamba ilikuwa ikimilikiwa na mwanaume mwenye pesa nchini Nigeria. Alimwangalia David, jinsi alivyokuwa msogo na kwa jinsi jumba lile lilivyokuwa, hakika alichanganyikiwa na kujiona kuwa katika miko ya mwanaume aliyekuwa na pesa nyingi mno.
“Karibu nyumbani,” alisema David huku akimwangalia Cecilia.
Msichana huyo akakaa kochini, makalio yake yakaingia ndani, lilikuwa kochi kubwa ambalo lilionyesha kustahili kuwekwa katika jumba la bilionea kama hilo. David akaelekea kwenye friji na kutoa juisi kisha kumpa msichana huyo na kuanza kunywa huku wakipiga stori.
“Inaelekea wewe ni bilionea mkubwa sana,” alisema Cecilia huku akimwangalia David.
“Nani? Mimi? Hakuna, mimi ni mtu wa kawaida sana,” alisema David huku akimwangalia msichana huyo usoni.
“Mmh! Yaani jumba lote hili, ni lako au umepanga?”
“Ni langu, nimenunua kutoka kwa mtoto wa Bilionea Koali Tengoda,” alijibu David.
“Ooh! Safi sana!”
Walibaki wakizungumza mengi sana, David hakutaka kunyamaza, aliendelea kumwambia msichana huyo jinsi alivyokuwa akimpenda na kuwa hakukuwa na msichana mwingine ndani ya moyo wake kama alivyokuwa Cecilia.
Cecilia alibaki akikenua meno, moyo wake uliendelea kuwa na furaha, kupendwa na mtu aliyekuwa akimpenda kwake ilionekana kuwa kama bahati ambayo isingeweza kurudi mara mbili. Hakuweza kuvumilia, akasimama na kumsogelea pale alipokuwa na kuubusu mdomo wake.
Wakashikana na kuanza kuelekea chumbani huku David akiwa amembeba Cecilia, walipofika huko, akambwaga kitandani na kuanza kushikana hapa na pale.
“Nakupenda Cecilia,” alisema David huku akimwangalia msichana huyo aliyekuwa mtupu kitandani.
“Nakupenda pia,” alisema Cecilia na hapohapo kitanda kuanza kupiga kelele huku sauti za mahaba kusikika chumba kizima.
***
Ndani ya wiki moja tu tayari mapenzi yakawa motomoto, hakukuwa na mtu aliyeweza kuwatenganisha wawili hao. Japokuwa kwa David alianza kama maigizo lakini akajikuta akijisahau na kuanza kumpenda Cecilia kwa mapenzi ya dhati kabisa.
Kila siku ilikuwa ni kuwasiliana na msichana huyo, hakuwa tayari kumwambia kwamba sasa ulikuwa muda wa kwenda naye nyumbani kwake, alitaka kuona msichana huyo akimchukua mwenyewe na kuelekea huko.
Kila siku ilikuwa ni lazima kuwaambia wenzake kilichokuwa kikiendelea, kila mmoja alitumaini kwamba kufanikiwa kwa David ndiyo kungewafanya hata wao kufanya kazi kwa nguvu zote. Hawakuona kama muda ukienda, hawakujali hilo kwani kiasi cha pesa walichotaka kukiiba kilikuwa kikubwa ambacho kingewafanya kuishi kitajiri mpaka vifo vyao.
“Kuhusu kwake?”
“Bado hajanipa ruhusa hiyo ila nakuhakikishia kwamba wiki hii lazima nifanikishe mchakato mzima,” alisema David huku akiwaangalia wenzake.
“Hakikisha unafanikiwa ili tuendelee na mtu mwingine,” alisema Mike.
“Hakuna noma.”
Baada ya wiki ya pili kukatika ndipo Cecilia akamwambia David kwamba alitakiwa kwenda nyumbani kwake kwani hatua ambayo waliifikia kipindi hicho ilikuwa kubwa mno. Hilo halikuwa tatizo, kitu cha kwanza kabisa kwa David kilikuwa ni kuwapigia simu wenzake na kuwaambia kwamba hatimaye alitakiwa kwenda nyumbani kwa msichana huyo ambapo aliamini kwamba kulikuwa na pleti waliyokuwa wakiitaka.
Siku iliyofuata David akaanza safari ya kuelekea nyumbani kwa Cecilia ambapo alielekezwa. Hakukuwa mbali sana na mahali alipokuwa akiishi hapo Lagos. Alipofika katika jumba hilo, akabaki akishangaa, lilikuwa jumba kubwa mno ambalo ilimuonyesha kabisa lilimilikiwa na bilionea mkubwa aliyekuwa akifanya biashara nyingi kubwa zilizomuingizia mamilioni.
Baada ya kujitambulisha, geti likajifungua na kuliingiza gari lake ndani ya gari. Akalisimamisha katika sehemu ya maegesho na Cecilia kutoka ndani na kumfuata. Akateremka, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kubusiana na kisha kuelekea ndani.
Macho ya David hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule. Kwake, msichana huyo alionekana kuwa bilionea mkubwa, akasahau kabisa kwamba alikuwa msimamizi wa Benki Kuu Nigeria, alichokiona ni kwamba alikuwa na bilionea mkubwa nchini Nigeria.
Wakakaa kwenye kochi na kuanza kuzungumza mambo mengi. Baada ya dakika kadhaa, David akaitoa simu yake mfukoni na kuifungua ile programu ya Pentagon 2.4 na kuanza kuangalia kama ilishika pltei ambayo aliamini kwamba ilikuwa ndani ya jumba hilo.
Simu haikuonyesha kitu chochote kile, alishangaa, alishindwa kujua mahali pleti hiyo ilipokuwa. Wakati Cecilia amesimama na kuelekea chumbani, David akasimama na kuanza kuzunguka katika sebule hiyo, alipofika sehemu ya kuelekea katika korido, programu ile ni kama ilishtuliwa, hapohapo ikaandika ‘plate accepted’ kitu kilichomtambulisha kwamba pale alipokuwa amesimama pleti ile ilikuwa ikisoma vizuri.
Wakati akiiseti tayari kwa kuload mafaili na kumuonyeshea namba iliyokuwa katika pleti hiyo, akasikia vishindo vya mtu vikija kule alipokuwa kutoka chumbani. Harakaharaka akaanza kurudi kwenye kochi kwani alijua huyo alikuwa Cecilia.
“Plate denied” (plate imekataa) yalikuwa maneno yaliyosomeka vizuri kabisa kwenye simu yake kumtaalifu kwamba pale alipokuwa amesimama simu haikuweza kuifikia pleti.
Cecilia akamfuata mpaka kwenye kochi lile na kukaa karibu naye, uso wake ulijawa na tabasamu pana na wakati mwenzake alikuwa akifikiria ni kwa namna gani angeweza kufanya kila linalowezekana kuifikia pleti ile ili aweze kuchukua namba alizokuwa akizitaka.
“Unajisikieje kuwa hapa?” aliuliza Cecilia huku akimwangalia David.
“Nasikia vizuri kabisa. Nina hamu nawe kupita kawaida,” alisema David, hapohapo akamvuta zaidi msichana huyo na kuanza kubadilishana mate.
Hakutaka kuishia hapo, alichohitaji ni kufanya naye mapenzi tu. Hakutaka kufanya naye hapo, ilikuwa ni lazima aende naye chumbani ambapo aliamini ndipo kulipokuwa na pleti ile. Akamnyanyua Cecilia huku akimbusu hapa na pale.
“Twende chumbani!” alisema David.
“Siwezi kutembea, labda unibebe,” alisema msichana huyo kwa sauti yenye mahaba.
“Hiyo ndiyo kazi yangu!” alisema David, akambeba Cecilia na kuanza kuondoka naye huku msichana huyo akimwambia mahali chumba kilipokuwa.
“Plate Accepted,” (Pleti imekubali) simu yake mfukoni iliandika mara baada ya kukikaribia chumba kile.
***
Program Pentagon 2.4 ilikuwa na kazi ya kufanya kazi kwa ufasaha kila ilipokuwa ikikutana na mawimbi ya pleti za benki ambazo walipewa watu wanne kwa ajili ya kulinda database ya beki kuu nchini Nigeria.
Programu hiyo iliyokuwa ikisoma katika simu ya David ikaanza kupata asilimia zake kuanzia moja na kuendelea huku ikitakiwa kupanda mpaka kufikia hatua mia moja ambapo hapo kazi yake ingekuwa imekamilika na hivyo kuitafuta pleti nyingine.
Programu iliendelea kupandisha asilimia katika simu ya David, alilifahamu hilo na kitu pekee alichokuwa akikihitaji ni kuendelea kubaki na msichana huyo chumbani kwake. Walicheza kila michezo ya mahaba kitandani, walipomaliza, wakaa na kuanza kuzungumza.
Katika kila neno ambalo David alikuwa akizungumza na msichana huyo hakuacha kumwambia jinsi alivyokuwa akimpenda, alitaka kumfanya ajisikie kuwa miongoni mwa wasichana warembo waliowahi kutokea nchini Nigeria.
Siku hiyo akafanikiwa kupata namba iliyokuwa katika pleti hiyo. Hakutaka kuitoa simu yake kutoka mfukoni, alikuwa na uhakika kwamba kila kitu kilikuwa kimekamilika kwa asilimia mia moja. Akaondoka kuelekea walipokuwa wenzake ambapo baada ya kufika akawaambia kuwa alifanikiwa.
“Hebu tuione,” alisema Mike.
Akaitoa simu yake na kumpa, Mike akaichukua, akaifungua programu ile, akazikuta namba tatu, za kwanza zilikuwa juu, zilisomeka 03, kwa chini kulikuwa na nyingine iliyosomea 9.
“Sijazielewa hizi namba,” alisema Tim.
“Namba tunayohitaji ni hii ya chini, yaani 9. Hizo za juu 03 ni mtiririko wa kuzipanga namba hizi. Namba ya huyu Cecilia inasimama kwenye namba nne, kwa hiyo tunahitaji namba tatu zilizobaki. Cha msingi ni kuanza kazi mara moja kuzipata hata kabla mwezi haujakatika,” alisema Mike.
Kila mmoja akampongeza David kwa kazi kubwa aliyokuwa ameifanya, kulikuwa na kazi nyingine ambayo nayo ilionekana kuwa ngumu, jinsi ya kuzipata namba tatu zilizokuwa zimebaki kutoka kwa watu waliokuwa na pesa, heshima kubwa nchini humo.
Mtu ambaye alitakiwa kuitafuta namba nyingine alikuwa Tim, yeye alitakiwa kuhakikisha anaipata namba hiyo kutoka kwa mkurugenzi wa benki hiyo, Daniel Ife. Kabla ya kufanya kitu chochote kile kwanza wakataka kupata data kamili kuhusu mwanaume huyo, alikuwa akipendelea nini katika maisha yake.
Walichokigundua ni kwamba alikuwa miongoni mwa wazee waliokuwa wakipenda sana wasichana warembo, kila mwanamke aliyekuwa akiukwaa ustaa nchini Nigeria mzee huyo alitaka kutembea naye kwa kuwa tu alikuwa na pesa za kuchezea.
“Huo ndiyo udhaifu wake, Tim, hakikisha unampata,” alisema Mike.
“Haina shida. Nitajua jinsi ya kumpata,” alisema Tim na kikao hicho kifupi kufungwa.
 
ERIC SHIGONGO
MZIMU UNAOTABASAMU-17

Mwanamke mtu mzima, Bi. Getrude alikuwa chumbani kwake, machozi yalikuwa yakimtoka, moyo wake ulimuuma mno, alipiga magoti na kumlilia Mungu, macho yake yalikuwa mekundu, alionekana kuwa na maumivu makali moyoni mwake.
Alimlilia Mungu wake, miaka ishirini nyuma wakati mumewe akiwa hana kazi, hana pesa alimuomba sana Mungu ampatie kazi, pesa ili kidogo maisha yawe mazuri na kuishi walivyotaka.
Mungu alisikia kilio chake na mumewe na hatimaye kumpa kazi mumewe. Ni miaka mingi imepita, kila kitu alichokuwa akikitarajia kutoka kwa mumewe alikikosa, aliamini kwamba mara baada ya kupata kazi na pesa basi mapenzi yangekuwa makubwa kwake lakini kitu cha ajabu kabisa, pesa ziliharibu mapenzi, zikamsahaulisha mume wake na kufanya kila aina ya upumbavu.
Alipiga magoti kwa lengo la kumuomba Mungu kitu kimoja tu, auchukue utajiri wa mumewe, achukue kazi ya mumewe na hatimaye warudi katika hali ya umasikini kama walivyokuwa zamani. Hakuona faida ya kuwa na utajiri uliomfanya mume wake amsahau, hakuona faida ya kuwa na utajiri ambao ulimfanya mumewe kulala nje kwa siku tano kila wiki.
Kwake, alihitaji mapenzi, hakuhitaji pesa, hakuhitaji mali, alimpenda mume wake tangu zamani kipindi ambacho hakuwa na pesa, kwake, hasa kwa kipindi hicho alikuwa tayari kupoteza kila kitu maishani mwake lakini mwisho wa siku penzi la mumewe lirudi na kuwa kama zamani.
“Mungu! Nirudishie mume wangu! Kama utajiri ni tatizo, kama cheo kikubwa ni tatizo, naomba uchukue kila kitu kutoka kwa mume wangu na unichie mapenzi, arudi tena kwangu, aijali familia yake, Mungu nahitaji mume wangu apoteze kila kitu arudishe mapenzi aliyokuwanayo kwangu,” alilia mwanamke huyo huku akiwa amepiga magoti.
Huyo alikuwa mke wa Mzee Daniel Ife. Alikuwa mkurugenzi wa benki kuu nchini Nigeria. Kipindi cha nyuma yeye na mkewe waliomba sana kuwa na kazi, pesa, walilia kila siku. Mungu akavisikia vilio vyake na kuwapa vyote walivyokuwa wakivihitaji.
Mzee huyo akajisahau, akasahau kwamba ile kazi aliyopewa ilitokana na machozi yakee na mkewe ambayo walilia kila siku, akasahau kila kitu na hivyo kuanza kufanya upumbavu wake. Akaanza kutembea na wanawake mbalimbali jiji Lagos, alijulikana kuwa miongoni mwa wazee waliokuwa na pesa nyingi, heshima, kila mtu alimjua na kila mwanamke aliyesogea karibu yake ilikuwa ni lazima kulala naye.
Bi Getrude alilia sana na hata kutamani kukaa na mumewe huyo na kuzungumza naye lakini hakuwa akielewa kabisa, kila siku alimwambia yupo bize na hakuwa na muda wa kukaa chini na kuzungumza. Hilo lilimuumiza sana mwanamke huyo lakini akawa hana la kufanya zaidi ya kukubaliana naye tu.
Umalaya ukakubuhu na mwisho wa siku hata nyumbani kwake akawa halali tena, kila alipokuwa akimwangalia mke wake alimuona kuzeeka, hakumuhitaji tena, alihitaji wasichana wadogo waliokuwa kwenye chati, wasichana ambao vifua vyao vilisimama, wasichana waliojua kuringa na kutembea kila aina ya mikogo.
Hakuwa mchoyo, hakuwa bahili, alimwaga pesa, kila msichana mrembo aliyekuwa akihitaji pesa jijini Lagos alimfuata mzee huyu ambaye sharti lake lilikuwa moja tu, kulala nao kila siku.
Las Catalunya ndiyo hoteli aliyokuwa akiitumia sana kufanyia uovu wake, kila siku ilikuwa ni lazima kufika katika hoteli hiyo ambapo aliunganisha mpaka klabu, huko alikutana na wanawake warembo ambao alichukua namba zao za simu, aliwatongoza na kulala nao kila siku.
Tim alipata kila kitu kuhusu mzee huyo, hapo klabu alipokuwa akienda, aliujua udhaifu wake na ilikuwa ni lazima kumfuata huko na kutaka kujua mahali pleti ilipokuwa ili aweze kuchukua namba. Siku ya kuonana na mzee huyo alihakikisha anakutana na msichana Lisa kabla ya kumfikia.
Huyo alikuwa msichana mrembo aliyekuwa akiishi uswahilini, alikuwa na sura nzuri, msichana aliyejua kuringa na hata lafudhi yake alipokuwa akizungumza Kiingereza ilikuwa ni rahisi kusema alikuwa Mzungu, alijua kuiremba, alizungumzia ndani na ilikuwa ni sauti pekee aliyoitumia kuikamata mibaba iliyokuwa na pesa.
Alipoletewa dili na Tim, hakutaka kuliacha, alipewa naila elfu kumi na tano na hivyo kuanza kufanya mishemishe. Alichomwambia Tim ni kwamba alitakiwa kusubiri na yeye angemuunganishia kwa mzee huyo ambaye alihusudu sana wasichana warembo.
Tim akaingia katika klabu hiyo. Mzee Daniel alikuwa eneo la VIP ambalo lilikuwa eneo la watu waliokuwa na pesa ambapo kila siku walichezewa na wanawake waliokuwa watupu kabisa. Tim akataka kwenda huko, ilikuwa ni lazima kuonana na mzee huyo na kuzungumza naye, alitaka kumwambia kwamba alikuwa na msichana mrembo wa hadhi yake ambaye hakutaka kabisa kumpa mtu mwingine.
Akaanza kwenda kule VIP, alipotaka kupandisha ngezi kwenda juu, akazuiliwa na mabaunsa wawili na kuanza kumuuliza maswali juu ya kwenda kule VIP na wakati hakuwa akijulikana na ilikuwa mara ya kwanza kufika katika klabu hiyo.
“Nataka kuonana na Daniel Ife,” alisema Tim.
“Wewe ni nani?”
“Naitwa Godfrey! Nina habari njema mno kwake,” alidanganya.
“Habari gani?”
“Kwani nyie mnachukua habari yake au?”
Alikuwa akibishana nao, aliwaambia kwamba anataka kuonana na mzee huyo lakini mabaunsa walimkatalia. Walivutana kwa dakika kumi ndipo wakamruhusu kwenda kuonana naye, tena si kwa kwenda peke yake bali alitakiwa kusindikizwa na baunsa mmoja.
“Haina shida!”
Wakapanda mpaka juu. Wakamkuta mzee huyo akiwa na watu wengine wengi kwenye kochi kubwa jekundu huku kukiwa na wanawake waliokuwa wakicheza uchi mbele yake na wengine wakizunguka katika chuma moja lililosimamishwa katikati ya sehemu hiyo.
Alipomuona baunsa akija na kijana mmoja ambaye hakumfahamu, akamwambia mlinzi wake awasimamishe na kuwasikiliza walikuwa na kitu gani. Haraka sana mlinzi akaanza kusogea kule, alipowafikia, akawauliza, Tim akamwambia kwamba alikuwa na ishu alitaka kuzungumza na mzee huyo kuhusu msichana mrembo aliyekuwa akija kwa kasi aliyeitwa Lisa.
“Ndiye nani?”
“Huwezi kumjua, hilo ni toleo jipya,” alijibu Tim huku akiachia tabasamu.
Mlinzi huyo amafuata Mzee Daniel na kumwambia kile alichoambiwa kwamba kijana huyo alileta habari kuhusu msichana mrembo aliyejulikana kwa jina la Lisa, msichana aliyekuwa mrembo ambaye ni miongoni mwa wale wakali waliokuwa wakichipukia.
“Unasemaje? Hebu muite kwanza huyo kijana,” alisema Mzee Daniel, mwili ukamsisimka, kitendo cha kusikia kwamba kulikuwa na msichana mrembo aliyekuwa akichipukia, akili yake ikawaka, akahisi kama vijidudu vya ngono vikianza kumtembelea mwilini mwake.
***
Japokuwa mapenzi ya David yalianza kama maigizo kwa msichana Cecilia lakini akajikuta moyo wake ukizama katika penzi la kweli la msichana huyo na hivyo kuendelea naye hata baada ya kupata namba alizokuwa akizihitaji.
Alimpenda Cecilia, kwake alikuwa kila kitu. Kila siku alikutana naye na kuzungumza mambo mengi, alimwambia ukweli wa moyo wake kwamba alimpenda na kumuhitaji katika maisha yake yote.
Siku ziliendelea kwenda mbele, Cecilia hakutaka kabisa kusikia lolote kutoka kwa David, hakutaka kuachwa, na kwa jinsi kijana huyo alivyokuwa mzuri wa sura akaona lingekuwa jambo jema sana kama angemtambulisha kwa marafiki zake.
Akamchukua na kumpeleka kazini kwake. Huko, akamtambulisha kwa wafanyakazi wenzake kama mchumba wake ambaye baada ya miezi michache wangefunga ndoa na kuwa mume na mke. Hakutaka kuishia kwa wafanyakazi wa kawaida, akampeleka mpaka kwa meneja wa benki hiyo, Bwana Sebastian Kanayo na kumtambulisha pia.
“Nimefurahi sana kuwafahamu,” alisema David huku akiachia tabasamu, kitendo cha kukutana na meneja huyo kilimfurahisha mno kwani miongoni mwa watu waliokuwa na pleti ambao namba zao zilihitajika sana alikuwa mzee huyo.
“Karibu tena! Kama utakuwa na tatizo lolote lile, usisite kutuona,” alisema Mzee Kanayo huku akiachia tabasamu.
“Nashukuru sana!” alisema David na kuondoka ofisini humo huku akiwa na mpenzi wake, Cecilia.
David akafurahi, hakuamini kama Cecilia alikuwa amewapunguzia kazi ya kuhakikisha namba ya pleti ya Kanayo inapatikana. Akaondoka na kurudi nyumbani ambapo huku akawapigia simu wenzake kwa lengo la kuwaeleza kile kilichokuwa kimetokea.
“Guys! I have good news!” (nina habari njema washikaji) alisema David huku simu ikiwa sikioni mwake.
“What is that?” (ipi hiyo?) aliuliza Mike kutoka upande wa pili.
“Let’s meet,” (tukutaneni kwanza) alisema David na kukata simu.
Baada ya dakika chache wakakutana na kuwaeleza kile kilichotokea, kila mmoja akafurahi na kuona kweli hiyo ilikuwa habari njema. Mtu ambaye alipewa kazi ya kuhakikisha anapata namba ya pleti ya Kanoyo alirahisishiwa kwa kiasi kikubwa mno kuipata.
“Guys! We are goig to be bilionaires,” (washikaji tunakwenda kuwa mabilionea) alisema Mike na wote kuanza kushangilia kwani pia walikuwa na uhakika Tim angekamilisha kazi yake.
 
ERIC SHIGONGO
MZIMU UNAOTABASAMU-18

Mzee Daniel alitaka kujua mengi kuhusu msichana huyo aliyeambiwa kwamba alikuwa toleo jipya, alitaka kusikia mengi, alifananaje, alikuwaje na uzuri wake ulifanana na nani.
Akamwambia Tim akae kwenye kiti hapo klabu na kuanza kuzungumza naye. Tim hakutaka kuona akishindwa, alichokihitaji kilikuwa ni namba zilizokuwa kwenye pleti tu. Akachukua simu yake kutoka mfukoni, aliamini kwamba kama kweli mzee huyo alikuwa na pleti mahali hapo basi lazima simu yake hasa kwa kutumia programu ya Pentagon 2.4 ingemjulisha hilo.
Akaifungua programu hiyo na kuanza kuangalia, haikuonyesha kuwa na kitu chochote kile, yaani ile pleti aliyokuwa akiitaka ya huyo mzee haikuwa mahali hapo.
“Mbona unaangalia sana simu yako?” aliuliza Mzee Daniel huku akimwangalia Tim ambaye hakuwa ameongea kitu chochote kile.
“Nataka nikuonyeshee picha mkuu!” alisema Tim, haraka sana akaifunga programu na kuingia sehemu ya picha na kuanza kupekua picha za Lisa. Alipoziona, akampa mzee simu aziangalie.
“Aisee! Huyu anaishi wapi?” aliuliza mzee Daniel huku macho yakimtoka.
“Anaishi Bode Thomas! Ni msichana mrembo sana kama unavyomuona, analiwa na watu wenye meno makali kama yako,” alisema Tim huku akimwangalia mzee huyo.
Macho ya mzee Daniel hayakutoka katika picha za Lisa alizokuwa akionyeshewa, ni kweli aliwahi kukutana na wasichana warembo lakini kwa Lisa alikuwa ni zaidi ya mrembo. Alimvutia, alikuwa na figa namba nane, macho ya kuita, lipsi nenenene, kwa kifupi Lisa alionekana kuvutia kupita kawaida.
“Nataka kumuona!” alisema mzee huyo.
“Hakuna tatizo. Nimekuletea wewe kwa kuwa najua ungeelewa mzigo. Kama utataka wengine nitakuwa nakuletea,” alisema Tim na kuchukua simu yake.
Hiyo ndiyo ilikuwa nafasi ya kuanza kuzoeana na mzee Daniel, kwa kuwa alikuwa na mawasiliano na wanawake warembo akaanza kuwaweka sawa kwa lengo la kuhakikisha anakuwa karibu na mzee huyo.
Alimpanga Lisa, alimwambia kwamba kwa uzuri wake alitakiwa kuwa na mwanaume mwenye pesa na si kuchukuliwa na wanaume wa uswahilini wasiokuwa na lolote.
Baada ya siku moja tu Tim akafanya kazi yake, akamkutanisha Lisa na mzee Daniel, akawaacha wakifanya mambo yao na yeye kuondoka zake.
Hilo likamfanya kuwa karibu na mzee huyo, wakaanza kuwasiliana na mara nyingine walikuwa wakikutana na kupiga stori za wanawake na kumwambia kwamba mbali na Lisa kulikuwa na wanawake wengi waliostahili kulala na mtu mwenye pesa kama yeye.
Baada ya kuona kwamba alifanikiwa kuwa karibu na mzee huyo, akakutana na wenzake na kuwaambia kilichoendelea kwamba hatimaye alifanikisha suala lake la kuwa karibu na mzee huyo na kilichobaki ni kujua mahali pleti hiyo ilipokuwa ili aweze kupakua namba hiyo.
“I met him in the club,” (nilikutana naye kwenye klabu) alisema Tim.
“Did you download the numbers?” (ulipakua namba?) aliuliza Mike.
“It was impossible, he didn’t have it,” (ilikuwa vigumu, hakuwa nayo) alisema Tim.
“So?” (kwa hiyo?)
“I am working on it,” (nalifanyia kazi)
Kitu alichohisi Tim ni kwamba mzee huyo alikuwa na pleti hiyo nyumbani kwake, alitamani kumwambia aende huko kumtembelea lakini aliona suala hilo kuwa gumu mpaka pale ambapo urafiki wao ungekuwa mkubwa kwa kuendelea kuwaletea wanawake wazuri zaidi.
Baada ya siku nne kupita, Tim akampigia simu mzee huyo na kumwambia kulikuwa na mwanamke mwingine mrembo aliyempanga kwa lengo la kuonana naye aliyeitwa Cleopatra. Hata kabla ya kuonana naye mzee huyo akahitaji kuona picha zake, hilo halikuwa tatizo, akatumiwa, alipozifungua na kuziangalia, hakuamini alichokiona.
Akahisi mwili wake ukianza kutetemeka, mhemko ukamshika kiasi cha kukaa vizuri katika kiti chake ofisini. Picha alizokutana nazo zilikuwa ni za msichana mrembo hata zaidi ya alivyokuwa Lisa. Alipendeza, nguo alizokuwa akizivaa zilimdatisha. Hakukuwa na picha moja, ili kumdatisha zaidi Tim alimtumia mpaka picha ambazo msichana huyo alivaa nusu utupu.
“You gave me Aston Martin, today you just give me a Ferrari,” (ulinipa Aston Martin, leo umenipa Ferrari) alisema mzee huyo akilinganisha thamani za wanawake hao na aina ya magari ya thamani duniani.
“I want you to drive this Ferrari, I will give you a Lamborghin tomorrow. Hahahah,” (Ninataka uiendeshe hii Ferrari, kesho nitakupa Lamborghin. Hahaha) alisema Tim na kuanza kucheka.
Hakutaka kuchelewa, akafanya mawasiliano na Cleopatra na kumpanga kuhusu mzee huyo. Alipomaliza, akampigia simu mzee Daniel na kumwambia kwamba ilibidi wakutane ili ampe msichana huyo.
“Lini?”
“Hata leo, si unajua wastoto wa chuo hawa, tukiwakosa sasa hivi, kuwapata tena mpaka mwakani,” alisema Tim.
“Basi sawa. Naomba uniletee leo. Nitakuja kumchukua hapo Livingstone bar.”
“Sawa.”
Walipomaliza kuzungumza, haraka sana akampigia simu Cleopatra na kumwambia kwamba wakutane katika baa aliyoisema mzee huyo. Hilo halikuwa tatizo, msichana huyo akajiandaa harakaharaka na baada ya saa moja wakakutana kwenye baa hiyo.
“Mzee mwenyewe yupo wapi?”
“Subiri! Anakuja, shusha presha. Huyu mzee ana pesa nyingi sana, cheza naye kwa stepu, utafanikiwa sana,” alisema Tim.
Baada ya nusu saa mwanaume mmoja akaingia ndani ya baa hiyo, alipomuona Tim, akamfuata na kumwambia kwamba aliagizwa na mzee Daniel ampeleke msichana huyo kwenye gari lake lililokuwa nje. Haraka sana wakasimama na kuelekea huko kulipokuwa na gari lile.
Mzee Daniel hakutaka kuteremka, alibaki ndani ya gari akiwaangalia wawili hao wakija. Macho yake yalikuwa kwa Cleopatra, alimwangalia kimatamanio, kwa jinsi alivyomuona, alikuwa msichana mrembo mno, alitembea kwa maringo, alipofika karibu na gari lake, akamfungulia mlango, Cleopatra akaingia ndani.
“Kwa hiyo bosi?” aliuliza Tim huku akiwa nje, alitaka kusubiri kuona mzee huyo angeongea nini.
“Unafanya kazi bora sana, hushuki kiwango,” alisema mzee huyo huku akiachia tabasamu.
Wakati Tim akiwa amesimama hapo kwa nje, akaisikia simu yake ikitetemeka kuashiria kwamba kulikuwa na kitu. Akaitoa na kuangalia, program ya Pentagon 2.4 ilikuwa imejifungua na kumuonyesha alama kwamba alikuwa karibu na pleti hiyo aliyokuwa akiitaka, yeye mwenyewe alishangaa.
“Mbona bize na simu?” aliuliza mzee Daniel.
“Hakuna kitu! Nimetumiwa meseji na demu wangu! Basi tutaonana!” alisema Tim.
“Sawa. Dereva tuondoke,” alisema mzee Daniel, gari likawashwa na kuondoka mahali hapo huku wakimwacha Tim akiwa amepigwa na butwaa.
“Ooppss! Kumbe pleti ipo ndani ya gari lake na si nyumbani kama nilivyofikiria!” alisema Tim huku mshangao ukiendelea kubaki usoni mwake.
***
"Unasema pleti ilikuwa ndani ya gari?" aliuliza David huku akimwangalia Tim aliyekuwa amewaletea ripoti kuhusu kazi aliyokuwa ameifanya.
"Ndiyo! Nililisogelea gari lake, pleti ikasoma," alisema Tim.
"Kwa nini usiseme kwamba alikuwa nayo mfukoni?"
"Ni kwa sababu kwa siku zote nilizokuwa naye pleti ile haikuwahi kusoma, bila shaka anaiweka ndani ya gari kwani nilipolisogelea tu, ikasoma," alisema Tim.
Hilo likampa uhakika kila mtu kwamba wangeweza kufanikiwa kwa kile walichokuwa wakikihitaji kwa wakati huo. Wakapanga mipango zaidi kuhakikisha kwamba ndani ya wiki mbili kila kitu kinachohitajika kilitakiwa kupatikana haraka iwezekanavyo.
Tim akaondoka na kuelekea katika nyumba aliyokuwa amepanga. Muda wotte simu yake ilikuwa hewani, alikuwa akisubiri simu kutoka kwa mzee Daniel na kumwambia kile kilichokuwa kimetokea. Alichokiangalia kilikuwa ni kujenga uaminifu kwa mzee huyo kuhusu masuala yote ya wanawake.
Kama alivyohisi ndivyo ilivyokuwa. Mzee Daniel akampigia simu, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumsifia kwa kazi kubwa aliyokuwa ameifanya ya kumtafutia msichana mwingine mreembo, anayejiweza kitandani kuliko hata Lisa.
"Nakutumia pesa zikusaidie katika mihangaiko yako. Nitahitaji mwingine keshokutwa!" alisema mzee Daniel kwenye simu na kukata.
Wala hazikupita dakika nyingi, meseji ikaingia katika simu ya Tim na kuonyesha kwamba alitumiwa kiasi cha naila laki moja kutoka kwa mzee huyo. Uhitaji wake haukuwa pesa, alichokihitaji zaidi kilikuwa ni kupata namba zilizokuwa katika pleti aliyokuwanayo mzee huyo.
"Au niende ofisini kwake halafu nikasimame karibu na gari lake?" alijiuliza.
Hilo ndilo alilolifanya, hakutaka kusubiri, haraka sana akaondoka na kuelekea kazini kwa huyo mzee kwa lengo la kusimama karibu na gari lake na kudukua namba zilizokuwa katika pleti ile.
Hakuchukua muda mrefu akafika katika Benki Kuu nchini Nigeria. Hata kabla hajaingia, kitu cha kwanza kilikuwa ni kusoma mazingira ya benki hiyo kwani alijua kwamba kama asingekuwa makini, kuingia kizembe basi angeweza kukamatwa kwani eneo kama hilo lilikuwa na ulinzi mkali mno.
"Nitaingia vipi? Askari wameshika buunduki na mbwa, kuna kamera za CCTV, hivi nitaweza kuingia kweli?" alijiuliza lakini akakosa jibu.
Akarudi nyumbani na kujifikiria sana namna ya kuingia ndani ya eneo la benki ile. Alikisumbua kichwa chake kujifikiria sana lakini hakufanikiwa kujua ni kwa namna gani angeweza kukamilisha kile alichohitaji kufanya siku hiyo.
Mpaka usiku unaingia hakuwa amepata jibu lolote lile. Marafiki zake walimpigia simu na kumuuliza kilichokuwa kimetokea kama alifanikiwa kupata namba zilizokuwa katika pleti, akawaambia kwamba bado alikuwa njiani na angefanikiwa kila kitu alichohitaji ndani ya muda waliokuwa wamepanga.
Usiku huo hakuwasiliana na mzee Daniel, siku iliyofuata akampigia simu na kuomba kuonana naye. Mzee huyo alivyoambiwa hivyo, akajua kabisa kwamba Tim alitaka kumwambia kuhusu mwanamke mwingine hivyo ilikuwa ni lazima aonane naye.
"Nione ofisini kwangu," alisema mzee huyo na kukata simu.
Tim hakutaka kuchelewa, haraka sana akaondoka na kuelekea katika benki hiyo, alipofika, akajitambulisha na kuruhusiwa kuingia tena huku akisaini katika kitabu cha wageni na kupewa kitambulisho. Kwa mwendo wa taratibu akaanza kutembea kuelekea ulipokuwa mlango wa kuingia katika jengo la benki hiyo.
Macho yake hayakutulia, alikuwa akiangalia huku na kule, alitaka kuyajua mazingira, sehemu gani palikuwa na udhaifu ambapo angepatumia kufanya kitu alichotaka kukifanya. Alichogundua ni kwamba kulikuwa na sehemu iliyokuwa na pipa la takataka ambapo ndani yake kulikuwa na chupa nyingi za maji za plastiki.
Akili yake ikamwambia kwamba hiyo ndiyo ilikuwa nafasi aliyokuwa ameibakiza ya kupata kile alichokitaka, alitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha kwamba anapata namba hizo. Alipoufikia mlango akaingia ndani ambapo alipojitambulisha kwamba alikuwa mgeni wa mzee huyo, akapelekwa katika ofisi yake.
Wakaonana, mzee Daniel alionekana kuwa tofauti, kwa kumwangalia tu hakukuwa na ugumu wa kugundua kwamba alikuwa na furaha tele. Akatoka katika kiti alichokuwa amekaa, akamsogelea Tim na kumkumbatia huku akimpa pongezi kwa kazi kubwa aliyokuwa ameifanya.
"Wewe ni mtu hatari sana! Hivi wale unawatoa wapi?" aliuliza mzee huyo huku akimwangalia Tim.
"Nawatoa chimbo. Sasa kuna mtoto mwingine nimekuandaliwa anaitwa Aisha! Huyo ndiye mkali kuliko wote," alisema Tim huku akimwangalia Mzee Daniel.
"Utanifanya nitoroke kazini. Hebu niambie kuhusu huyo Aisha!" alisema Mzee Daniel na kukaa vizuri kwenye kiti chake.
Tim akamwambia kila kitu, alimdanganya kwa kila neno, akamtengeneza msichana wake akilini mwake na kumwambia mzee huyo jinsi alivyokuwa. Mzee Daniel akachanganyikiwa zaidi, akashikwa na hamu ya kutaka kumuona kwani kwa maelezo ya Tim yalionyesha kabisa kwamba huyo Aisha inawezekana alikuwa malaika kwa jinsi sifa zake zilivyokuwa.
"Safi sana. Nitampataje?" aliuliza.
"Ni kazi nyepesi sana kama tutafanya kitu kimoja tu!" alisema Tim.
"Kitu gani?"
Alimwambia kwamba kulikuwa na mtu ambaye ndiye wangemtumia kumpata msichana huyo kwa kuwa tu alikuwa na ulinzi mkubwa. Hakuwa msichana mwepesi ambaye alisogelewa na kila mtu, baba yake hakutaka kuguswa, hakutaka kabisa mwanaume akaribie geti lake, wanaume walimuogopa mno na ili kumpata na kumpa ujumbe ilikuwa ni lazima wamtume mtu aliyeitwa Zolanda.
"Ndiye nani?"
"Huyo ndiye mwanaume pekee anayeingia ndani ya nyumba ya kina Aisha. Ni muokota makopo ya chupa za maji, kama wakimpata mwanaume huyo na kumtuma lingekuwa jambo jepesi sana," alisema Tim.
"Sasa si anaweza kuhitaji pesa nyingi?"
"Hakuna! Yaani huyo ukimpa nafasi ya kuja kuokota zile chupa za kule kwenye pipa la takataka, atakuwa ameridhika kwani ndiyo kazi yake," alisema Tim.
"Duh! Yaani tukimruhusu tu kazi anaifanya?"
"Ndiyo! Huyo jamaa ni choka mbaya, tumutumie ili tufanikiwe, au unaonaje?" alisema Tim na kuuliza swali.
"Ipo poa sana. Tufanye kazi hiyo!"
Tim akamwambia mzee huyo kwamba alitakiwa kumwambia mlinzi amruhusu muokota chupa za maji kesho ili akiifanya kazi hiyo basi naye aende kuifanya kazi yao kwa kumpata msichana mrembo aliyekuwa na asili ya Kiarabu, Aisha.
Akakubaliwa na hivyo mlinzi kupigiwa simu na kuambiwa kwamba kesho asubuhi kungekuwa na muokota chupa za maji ambaye angefika hapo hivyo amruhusu aingie na kwenda kuokota hizo chupa za maji.
Baada ya kukamilisha kila kitu, Tim akaondoka kurudi nyumbani kwake. Mpaka hapo hakuona ugumu wa kazi ile, alikuwa na uhakika kwamba angefanikiwa kwa asilimia mia moja. Alipofika, akawapigia simu wenzake na kuwaambia mpaka inafika asubuhi ya saa nne atakuwa tayari amekamilisha kazi yake.
Asubuhi ilipofika, akaanza kujiandaa kwenda katika benki hiyo. Hakukuwa na mtu aliyeitwa Zolanda ila alitaka kujitengeneza kama mtu huyo muokota chupa za maji ambaye alitakiwa kwenda katika benki hiyo na kufanya kazi aliyotaka kuifanya.
Akaondoka na kwenda mitaani, huko akatafuta nguo chafuchafu na kiroba, akajichafua, akakichukua na kuondoka nacho huku akiokota kila chupa aliyokuwa akikutana nayo njiani na mfukoni kukiwa na simuu yake.
Alikuwa na uhakika kwamba pleti ya mzee Daniel ilikuwa ndani ya gari lake, hakutaka kuzubaa, ilikuwa ni lazima kuhakikisha anafanikiwa kwa kile akitakacho na ndipo aachane na mzee huyo. Alitembea kwa mwendo wa taratibu, ilikuuwa ni vigumu kwa mtu yeyote kugundua kwamba mwanaume aliyekuwa na kiroba cha chupa za maji alikuwa mwanachuo wa chuo kikuu hapo Lagos.
Hakuchukua dakika nyingi akafika katika geti la benki hilo. Akasimama kwa nje na kuanza kuongea na mlinzi mmoja miongoni mwa walinzi kumi na tano waliokuwa hapo benki. Akawaambia kuwa aliambiwa na mzee Daniel aende mahali hapo kwa lengo la kuokota chupa.
"Wewe ndiye unaitwa Zulenda?" aliuliza mlinzi.
"Hapana! Zolanda!"
"Ooh! Zolanda! Sawa. Pita mzee aliniambia jana," alisema mlinzi na kumruhusu Tim kuingia, akapita zake.
Macho yake yalikuwa katika gari ile ya mzee Daniel, alitembea kwa mwendo wa taratibu. Kulikuwa na magari mengi katika sehemu ya kupaki magari, alihakikisha anasogea taratibu kuelekea katika sehemu ilipokuwa na pipa la takataka kabla ya kulifuata gari hilo.
Alipolifikia, akalifungua na kuanza kuchukua chupa za maji. Kila wakati alikuwa akiangalia huku na kule, kwanza alitaka kuwa na uhakika kwamba pale alipokuwa hakukuwa na mtu aliyekuwa akimfuatilia, alipoona pako shwari, akatoa simu yake, akaifungua programu ya Pentagon 2.4.
Hakutaka kubaki hapo, akainama chini na kuanza kwenda kule kuulipokuwa na gari la mzee Daniel, alipolifikia tu, hapohapo programu ile ikaishika pleti ile na kuanza kupakua namba zilizokuwa katika pleti ile.
Alikuwa na presha, simu ilikuwa ikipakua taratibu sana, alikuwa na hofu wa kukamatwa kwani kule alipokuwa si kule alipoambiwa aende. Wakati mwingine aliposikia mtu akija, aliinama zaidi na kuingia chini ya uvungu wa gari lile.
"Fanya haraka! Fanya haraka," alisema huku akionekana kuwa na hofu.
Programu iliendelea kupakua na baada ya dakika kumi na tano, ikawa imekamilisha zoezi hilo na hivyo kuanza kutoka uvunguni mwa lile gari huku kazi ikiwa imefanyika kwa mafanikio makubwa kabisa.
Wakati akiwa amesimama kwa pembeni ya gari lile, ghafla wakatokea walinzi wawili waliokuwa na bunduki, kitendo cha kumuona kule alipokuwa, walishangaa, hawakumwambia aende kule, wakashikwa na wasiwasi kwamba kuulikuwa na kitu kilichokuwa kimetokea ambacho kilimfanya kufika huko.
"Unafanya nini huku?" aliuliza mlinzi mmoja huku akitoa bunduki yake na kumnyooshea.
Kila mmoja alijua kwamba lengo la kwenda kule kulipokuwa na magari ya mabosi ilikuwa ni kuiba baadhi ya vitu vilivyokuwa katika magari hayo. Akasimama huku akitetemeka, aliona kama picha ikiwa imeungua na kilichomfanya kuwa na wasiwasi zaidi, alijua tu kwamba walinzi hao wangemchukua na kumpeleka kwa Mzee Daniel ambaye alimfahamu kabisa.
"Nimekuja kuokota makopo!"
"Huku! Kuna makopo gani? Ulikuwa unaiba? Hebu ngoja tumuite mzee," alisema mlinzi, mwenzake aliposikia, hakutaka kuchelewa, hapohapo akaondoka kuelekea getini kumpigia simu mzee Daniel ili aje na kumuona mtu aliyemwamini akiwa sehemu nyingine kabisa kwa lengo la kufanya uhalifu wa kufungua vioo vya gari.
"Mimi siyo mwizi." alisema Tim huku akitetemeka.
"Kama siyo mwizi huku ulikuwa unafanya nini?"
"Naokota chupa za maji!"
"Huku kuna chupa? Hatuwezi kukuelewa. Wewe ni mwizi lazima bosi aje ajionee manake ushalichafua jina lake," alisema mlinzi aliyebaki maneno yaliyomfanya Tim kuwa na hofu zaidi.
 
ERIC SHIGONGO
MZIMU UNAOTABASAMU-01

Mchungaji wa kimataifa wa Kanisa la Revelation lililopo jijini New York nchini Marekani, Gideon Matimya alishtuka kutoka usingizini mara baada ya kusikia mlio wa simu ya mezani iliyokuwa ikiita kwa fujo sebuleni. Alishangaa, kitu cha kwanza kabla ya kuteremka kutoka kitandani ni kumwangalia mkewe, Lucy ambaye naye alishtuka kutoka usingizi na kumwangalia mumewe huyo.
Haikuwa kawaida kwa simu hiyo kuita, ulipita mwezi mzima hawakuwa wameitumia, ilikuwa mbovu na hawakuwa na muda wa kuitengeneza kwa kuwa walikuwa wakitumia simu za mikononi. Kitendo cha simu hiyo kuanza kuita, walishangaa, kitu cha kwanza kabisa ambacho walijiuliza ni siku ambayo waliitengeneza simu hiyo.
Mchungaji Gideon akateremka kutoka kitandani, akatoka chumbani na kuanza kuteremka ngazi. Lucy hakubaki chumbani mule, naye akateremka na kumfuata mkewe huku wote wawili wakionekana kuwa na hofu nzito. Hatua zao zilikuwa za taratibu, walikuwa wakitembea huku wakionekana kuhofia kitu fulani, macho yao hayakutulia chumbani, walikuwa wakiangalia huku na kule kwani walihisi kwamba mbali na wao ndani ya nyumba hiyo, pia kulikuwa na mtu mwingine aliyekuwa akiwatazama.
“Ngriii...ngriii..ngriii...” simu ilindelea kuita mfululizo.
Usingizi wote waliokuwa nao ukakatika, macho yakawa makavu na woga kujaa mioyoni mwao. Walipoifikia simu ile, Mchungaji Gideon akauchukua mkonga wake na kuupeleka sikioni huku akitetemeka kwani alihisi kabisa simu ile haikuwa ya kawaida, ilikuwa ni simu ya hatari, simu iliyotoka kwa mtu hatari.
“Halo...” aliita kwa sauti ndogo iliyosikika kama mtu aliyekuwa na hofu moyoni mwake.
“Halo!” sauti ya upande wa pili ikasikika.
“To whom Am I speaking?” (nazungumza na nani?) aliuliza kwa sauti ya taratibu sana.
“The Smilling Ghost you created.” (mzimu unaotabasamu ulioutengeneza) sauti ya upande wa pili ilijibu.
Mchungaji Gideon akanyamaza, akazidi kutetemeka huku akimwangalia mke wake. Jibu la mtu huyo aliyepiga simu lilimtisha. Hakumjua mpigaji, hakukumbuka kama aliwahi kumtengeneza mtu na kuwa kiumbe kibaya. Katika maisha yake alimwamini Mungu, alimwabudu usiku na mchana na kujitolea katika maisha yake kwamba atamuabudu kwa moyo wake wote mpaka kifo chake.
Aliwawahubiria watu kuhusu kumjua Mungu, aliwaombea na wengine kuokoka na mwisho wa siku kuwabatiza kwa maji mengi. Mtu aliyekuwa amepiga simu alikuwa nani? Na alikuwa akihitaji nini kutoka kwake? Kila alichokuwa akijiuliza, alikosa jibu.
“Unahitaji nini?” aliuliza, kipindi hiki kidogo akatoa sauti iliyokuwa na ujasiri.
“Nilitaka nikwambie kitu kimoja tu kwamba nipo hai, nimeishi maisha ya tabu mpaka kuwa hapa, niliteseka, nililia usiku na mchana, niliumia kwa ajili yako. Jua kwamba sikufa, nipo hai, ninapumua kama unavyopumua,” alisema mtu aliyesikika upande wa pili maneno ambayo yalimchanganya kabisa Mchungaji Gideon.
“Wewe ni nani?”
“Mzimu Unaotabasamu. Mzimu unaotafutwa kila kona katika dunia hii,” alijibu mwanaume huyo.
Hapo ndipo Mchungaji Gideon akamfahamu mtu huyo. Alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wakitafutwa kwa nguvu kubwa duniani kote huku maofisa wa Kijasusi wa CIA wakiwa mstari wa mbele kabisa. Katika orodha ya watu mia moja waliokuwa wakitafutwa kwa udi na uvumba wa kwanza kabisa alikuwa mwanaume huyo. Hakujulikana, hakukuwa na mtu aliyejua sura yake ilifananaje lakini ndiye mtu aliyekuwa akiua watu wengi kila siku duniani.
Alijulikana kama The Smilling Ghost kwa maana ya Mzimu Unaotabasamu, na kwa kuwa hakuwa akijulikana jina lake, hata kwenye orodha hiyo ya CIA waliliandika jina hivyohivyo japokuwa hawakujua mwanaume huyo alifananaje na hakukuwa na mtu aliyejua sababu iliyompelekea kufanya mauaji katika siku ya Jumapili.
“Leo ni Jumapili, huu ni usiku wa kuamkia Jumapili, ina maana unataka kuniua?” aliuliza Mchungaji Gideon huku akianza kuingiwa na hofu kwa mara nyingine.
“Hapana. Nimekupigia simu kukwambia kwamba leo ndiyo siku maalumu ya Mzimu Unaotabasamu kukamatwa. Nahisi baada ya kukamatwa, hakutokuwa tena na mauaji kwa Jumapili ya leo,” alisema mwanaume huyo maneno yaliyozidi kumchanganya zaidi Mchungaji Gideon.
“Unamaanisha nini?”
“Umeangalia stoo?”
“Hapana! Kuna nini?”
“Umeangalia bafuni?” aliendelea kuuliza.
“Hapana. Kuna nini?”
“Hata hukujiuliza kwa nini mbwa wako leo habweki?” aliuliza mwanaume huyo.
Swali hilo lilimfanya Mchungaji Gideon kujiuliza kuhusu mbwa huyo. Hakujua ni kitu gani kilikuwa kimetokea, kila siku usiku mbwa wake aliyempa jina la Bobby alikuwa akibweka mno kuhakikisha nyumba yake inakuwa salama mbali na kamera ndogo za CCTV alizokuwa amezifunga ndani ya nyumba yake.
Siku hiyo alikuwa kimya kabisa, alishangaa, alijiuliza maswali yasiyokuwa na majibu lakini alikuwa na uhakika kwamba mwanaume aliyekuwa akizungumza naye alifahamu kila kitu. Baada ya kujiuliza kuhusu mbwa huyo, akajiuliza kuhusu huko stoo na bafuni alipokuwa ameambiwa, alihisi kulikuwa na kitu, alihisi kabisa kwamba mwanaume alikuwa amefanya jambo.
“Unataka nini?” aliuliza kwa ukali kidogo.
“Polisi wanaingia hapo dakika chache zijazo. Hakutokuwa na kitu chochote watakachokijua zaidi ya kufahamu kwamba wewe ndiye Mzimu waliyekuwa wakimtafuta kwa miaka kumi na tano, dunia itajua kwamba wewe ndiye mwanaume aliyekuwa akiua kila Jumapili, itajua kwamba wewe ndiye uliyemuua waziri mkuu wa Uingereza, mwanamitindo, Amanda Posh, Mwanamuziki Michael Turner, kwa kifupi, dunia nzima itajua kwamba wewe ndiyo mimi,” alisema mwanaume huyo na kukata simu.
“Halo..halo..halo..” aliita Mchungaji Gideon lakini simu ilikuwa imekatwa.
Mwili mzima ulikuwa ukitoka jasho, hakutaka kuchelewa, ilikuwa ni lazima kwenda bafuni na chooni kuona ni kitu gani kilikuwa kimetokea huko. Yeye na mkewe, kwa kasi ya ajabu wakaanza kuelekea bafuni, walipoufikia mlango na kuufungua, hawakuamini walichokiona, maiti ya mwanamke ilikuwa sakafuni, ilichomwa visu vinne kifuani, damu zilikuwa zikitoka huku kwenye paji la uso kukiwa na alama ya msalaba, yalikuwa ni aina ya mauaji yaleyale aliyokuwa akiua mtu huyo aliyekuwa akitafutwa.
Mkewe akaanza kupiga kelele kwa woga, hakuamini alichokuwa akikiona, moyo wake ulikufa ganzi na mwili kumtetemeka. Mchungaji Gideon akachanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilikuwa kimetokea mpaka maiti ile kuletwa ndani ya nyumba yake.
Akatoka na kueleka stoo, alipoufikia mlango na kuufungua, akakutana na maiti nyingine ya mtoto iliyokuwa sakafuni. Nayo ilichomwa visu viwili kifuani na kwenye paji la uso kulikuwa na alama ya msalaba, ilikuwa ni aina ya mauaji yaleyale aliyokuwa akiyafanya Mzimu.
“Mungu wangu! Kwa nini mimi?” alijiuliza na kutoka ndani.
Akaelekea katika banda la mbwa, alichokikuta huko ni maiti ya mbwa wake ikiwa chini. Aliuawa kwa kuchomwa visu mfululizo.
Machozi yakaanza kumtoka, hakuamini. Hata kabla hajafikiria ni kitu gani kilikuwa kimetokea, akaanza kusikia mlio ving’ora vya polisi wakija kule ilipokuwa nyumba yake, akazidi kuogopa.
Haraka sana akarudi ndani ya nyumba yake, akamkuta mkewe akiendelea kulia, hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya. Wakati akimchukua mkewe kwa ajili ya kumpeleka chumbani, polisi nao wakapiga teke geti kubwa na kuingia ndani huku wakiwa na bunduki mikononi mwao, tena wengine walikuwa wale polisi waliokuwa na silaha nzito ambao walikuja na gari lao lililoandikwa kwa maandishi makubwa yaliyosomeka S.W.A.T.
Hawakuingia kistaarabu, wakavunja mlango wa sebuleni na kuingia ndani. Walipofika, wakamkuta Mchungaji Gideon akiwa na mkewe, walikuwa wamekumbatiana chini huku wote wakilia kama watu waliokuwa wamefiwa.
“Mpo chini ya ulinzi! Nyanyueni mikono juu,” alisema polisi mmoja huku wakiwanyoonyeshea bunduki, wakatii na kufanya hivyo.
Kabla ya kufungwa pingu, polisi wale wakaanza kuangalia ndani ya nyumba hiyo, tena moja kwa moja wakaelekea stoo na bafuni na kuzikuta maiti hizo, yaani walikuwa kama watu ambao walijua maiti zilipokuwa. Wakawafunga pingu na kutoka nao ndani ya nyumba ile.
“Hatukuua! Hatukumuua mtu yeyote! Mimi ni mchungaji, mnanijua, mimi ni mpaka mafuta wa Bwana, sikumuua mtu yeyote yule,” alijitetea Mchungaji Gideon huku akiwaangalia polisi hao.
“Tumekutafuta sana. Kumbe mchungaji anayeaminika duniani, mpaka mafuta wa Bwana, anayewahubiria watu Neno la Mungu ndiye Mzimu Unaotabasamu tunayemtafuta! Mungu wangu! Kweli dunia imekwisha,” alisema polisi mmoja huku akionekana kushangaa.
Hakukuwa na mtu aliyemsikiliza, wakawachukua na kuwapeleka katika kituo cha polisi hapo kilichokuwa Manhattan jijini New York na kuwatuliza huko huku wakitakiwa kusubiri mpaka asubuhi itakapofika na mambo mengine ya kimahakama kuendelea.
Kukamatwa kwake haikuwa siri hata kidogo, usiku huohuo taarifa zikaanza kupelekwa sehemu mbalimbali kwamba hatimaye Mzimu Unaotabasamu alikuwa amekamatwa. Watu wengi walishtuka na kushangaa baada ya kupewa taarifa kwamba Mzimu wenyewe alikuwa mchungaji Gideon aliyekuwa na kanisa kubwa lililokuwa na washirika zaidi ya milioni moja duniani kote.
Ilipofika majira ya saa 10:15 alfajiri, Mchungaji Gideon akatolewa kutoka katika chumba alichokuwemo na kupelekwa katika chumba kingine kwa ajili ya kufanyiwa mahojiano. Muda wote alikuwa akilia huku akisisitiza kwamba hakuwa muuaji bali kulikuwa na mtu aliyekuwa ameua na kuzipeleka maiti katika nyumba yake.
Hilo halikusikilizwa. Alipofikishwa ndani ya chumba cha mahojiano, akakalishwa kwenye kiti na kuanza kuhojiwa. Muda wote alikuwa akilia, aliikunja mikono yake kama mtu aliyekuwa akisali, mara kwa mara alikuwa akifanya ishara ya msalaba lakini yote hayo yalionekana kama unafiki machoni mwa polisi waliokuwa ndani ya chumba hicho.
Wakaanza kumuuliza maswali kadhaa. Kila swali alilokuwa akiulizwa, Mchungaji Gideon aliwaambia kwamba hakuwa ameua na hakumfahamu mtu aliyekuwa amezileta maiti zile nyumbani kwake kwani alipigiwa simu na mtu aliyejitambulisha kwa jina la Mzimu Unaotabasamu na kuzipeleka maiti zile nyumbani kwake lakini si yeye aliyekuwa amefanya mauaji hayo.
“Fungua hiyo bahasha,” alisema mwanaume aliyekuwa akimuhoji huku akimpa bahasha kubwa ya kaki na kumwambia afungue.
Haraka sana akaifungua. Humo akakutana na picha mbili zikimuonyesha yeye akiwa amesimama nje ya nyumba moja huku mkononi akiwa ameshika kisu kilichokuwa na damu, na ndani ya nyumba hiyo kulikutwa maiti mbili za wanawake ambazo zilichomwa visu vifuani na kuwekewa alama ya msalaba katika paji la uso la kila mmoja.
“Huyu ni nani?” aliuliza polisi yule swali ambalo Mchungaji Gideon alishindwa kabisa kulijibu kwani kila alipokuwa akiiangalia sura ile, alikuwa yeye ila hakukumbuka kama kulikuwa na siku aliwahi kwenda kufanya mauaji yoyote yale.
“Huyu ni nani?” aliuliza polisi kwa sauti ya juu. Badala ya kujibu, Mchugaji Gideon akaanza kulia kwa sauti kama mtoto mdogo huku akisisitiza kwamba hakuua.
Nime subscribe
 
Back
Top Bottom