Mwigulu Nchemba
Akumbuka yatima, wenye uhitaji siku yake ya kuzaliwa
*Awataka wenye uwezo kusaidia makundi hayo
Claudia Kayombo
WATOTO yatima na makundi mengine yenye uhitaji maalumu wanatamani huruma ya wengine wakati wote, badala ya nyakati za sikukuu pekee.
Wanahitaji huruma kwa kuwa, wao hawajiwezi kujitafutia mahitaji ya msingi kama vyakula, malazi na mavazi.
Uzoefu unaonesha kuwa, jamii imekuwa ikiyakumbuka makundi hayo nyakati za sikukuu za kidini pekee, huku nyakati nyingine yakisahaulika.
Hata hivyo, wapo miongoni mwetu ambao wanadhani kuwa, jukumu la kuyasaidia makundi hayo si lao, bali ni la watu fulani tu, dhana ambayo si kweli.
Wanayasahau makundi hayo licha ya uwezo wa kipato ambao Mwenyezi Mungu amewakirimia hata kama uwezo huo si wa kiwango kikubwa.
Mtu moja aliwahi kusema, iwapo Watanzania ambao Mungu amewawezesha kipato wangejitoa kuwasaidia wengine, Tanzania ingekuwa mahala salama pa kuishi kwa yatima, wagonjwa wasio na msaada na makundi mengine yenye mahitaji maalumu tofauti na ilivyo sasa.
Jukumu la kuwasaidia watu hao ni la kila mtu na si la mtu mmoja, hivyo kila mtu aone anao wajibu wa kuyasaidia makundi mbalimbali ya wahitaji.
Mapema Januari 7, mwaka huu Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba alitembelea Hospitali ya Mwananyamala Dar es Salaam na Kituo cha Kulelea Watoto Yatima, Chakuwama kilichoko Sinza.
Pamoja na mambo mengine nathubutu kusema kuwa,- alijitahidi kutimiza wajibu wake kwa makundi hayo.
Nasema alitimiza wajibu kwa sababu, kama yupo atakayesema alifanya hivyo ni kwa vile alikuwa akifanya kumbukumbu ya tarehe yake ya kuzaliwa, alikuwa akitimiza miaka 40, kwa nini hakufanya kumbukumbu hiyo kwa namna nyingine kwa kuandaa sherehe katika eneo fulani la ufahali akawaita huko marafiki zake matajiri na kisha kula na kunywa nao.
Lakini, aliona ni bora akawaone wagonjwa na watoto yatima, makundi ambayo yanahitaji zaidi huruma ya wengine.
Tuache mambo mengine kando, tutazame ukweli wa jambo hili. Awali, nilisema watu hawa tunawakumbuka mara nyingi katika sikukuu za kidini pekee kama Krismasi, Idi na Pasaka, huku wakati mwingine tukiwaacha wakiteseka.
Iwapo wengi wetu, hususan wanaojiweza kila mtu wakati wa siku yake ya kuzaliwa angetimiza wajibu wake kwa kutoa misaada kwa makundi mbalimbali ya wahitaji, wasingebaki wakiteseka.
Kwa sababu, kama ilivyo kila siku watoto huzaliwa ndivyo zilivyo tarehe tofauti za kuzaliwa za watu mbalimbali nchini na duniani kote.
Akiwa katika hospitali hiyo, alitoa msaada wa vifaa mbalimbali vya kuwasaidia akina mama kwenye wadi ya wazazi. Alifanya tendo hilo la huruma na upendo wakati akitimiza miaka 40 ya kuzaliwa kwake.
Miongoni mwa alivyowagawia akina mama hao wazazi ni sabuni za kufulia, mabeseni ya kuogeshea watoto wao lakini pia alifanya tukio lingine kubwa zaidi la kuchangia damu.
Nimesema ni tukio kubwa kwa sababu damu ni bidhaa adimu katika nyakati hizi, bila kuongezwa damu mgonjwa mwenye hitaji hilo anaweza kufariki dunia.
Hivyo, alichangia msaada mkubwa utakaosaidia kuokoa uhai wa wengine.
Kwenda kwake katika hospitali hiyo pamoja na kutoa misaada hiyo, Mwigulu amekumbana na changamoto mbalimbali zinazoikabili Hospitali ya Mwananyamala.
Uhaba- mkubwa wa wadi zikiwemo za akina mama kwenye hospitali hiyo ni kilio kikubwa, kwani katika wadi ambayo inatakiwa kulaza wagonjwa 18 hulaza- 70 hadi 90.
Kutokana na hali hiyo, Mwigulu anaahidi pia kuvalia njuga kuhakikisha kuwa, changamoto zinazoikali hospitali hiyo na nyingine nchini, zinaondolewa kwani ndiyo India na London ya walalahoi wengi.
Akizungumza na wanahabari muda mfupi baada ya kutembelea baadhi ya wadi hizo, Mwigulu anasema- ataweka mkazo katika ukusanyaji wa kodi kwa wafanyabiashara wakubwa ili kuzimaliza changamoto hizo.
"Nitazungumza na wataalamu wenzangu tuwekee kipaumbele katika kuziondoa changamoto hizi, tusipowasemea jambo hili, mawe yatalisemea kwa sababu hii ndiyo India yao," anasema.
Anaongeza kuwa, ziara yake katika hospitali hiyo ni ya mafanikio makubwa kwa sababu amejionea changamoto zinazoikabili.
Anabainisha kuwa, ili kutatua changamoto katika hospitali mbalimbali nchini, ataelekeza nguvu katika kuhamasisha ukusanyaji wa kodi kwa wafanyabiashara wakubwa.
Akiwa katika Kituo cha Chawama, aliwapa watoto hao gunia la mchele, unga kilo 100, lita 40 za mafuta ya kula, katuni 5 za sabuni za kufulia na mbuzi mmoja.
Ziara ya naibu waziri huyo ilionesha dhahili kumkuna Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dk. Sophinias Ngonyani, ambaye kama ilivyo tabia ya waungwana alimshukuru waziri kwa kutembelea katika hospitali hiyo na kutoa msaada huo utakaoleta chachu na msukumo kwa viongozi na mashirika mengine.
Anasema msaada huo utasaidia kupunguza baadhi ya changamoto za kiafya zinazowakabili katika hospitali hiyo.
Hata hivyo, Dk. Ngonyani anasema changamoto ya uhaba wa wadi katika hospitali hiyo inatokana na uhaba wa eneo, ambapo mkakati uliopo ni kujenga maghorofa katika eneo hilo.
Alisema hospitali hiyo kwa sasa inategemewa na watu milioni mbili, wakazi wa Manispaa ya Kinondoni ambapo miondombinu iliyopo haikidhi mahitaji.
Mmoja wa akina mama wenye watoto, Hidaya Yusuph aliyelazwa katika wodi ya wazazi ambayo Mwigulu alitembelea, anasema ziara ya Naibu Waziri, Nchemba ilitoa faraja kwao.
Anasema iwapo viongozi mbalimbali wangekuwa na moyo kama wa naibu waziri huyo wa kutembelea katika maeneo kama hayo, ingesaidia kuondoa changamoto za wagonjwa na wafanyakazi wengine katika maeneo kama hayo.