Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, Godbless Lema akiwa juu ya jukwaa wakati akihutubia ''umati'' wa wananchi.
''Umati'' wa wananchi ukimsikiliza Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, Godbless Lema katika mkutano.
=======================================================================
Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema alikuwa akihutubia umati wa watu baada ya aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA wilaya ya Arumeru mkoani Arusha, Ernest Sheshe na viongozi wengine 10, kuachia ngazi kutokana na kuchukizwa na vitendo vya rushwa.
Sheshe na wenzake hao walifikia uamuzi huo baada ya viongozi na wanachama wengine kumwaga rushwa ya vyakula na vinywaji kwenye uchaguzi. Sheshe, ambaye alikuwa akitetea nafasi hiyo, alisema kabla ya kuanza kwa uchaguzi ngazi ya wilaya, wagombea walikuwa wakitoa rushwa na hata taarifa zilipofikishwa makao makuu, hakuna hatua zilizochukuliwa.
Pia alimrushia kombora, mgeni rasmi katika mkutano huo, mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, kwa kushindwa kukemea wala kuchukua hatua dhidi ya rushwa hiyo
Viongozi wengi wa CHADEMA wamekuwa wakilalamika kuchezewa rafu na wapinzani wao, ambao wanatajwa kubebwa na baadhi ya viongozi wa makao makuu.
Lema alisema madai ya Sheshe ni kutapatapa na kuwa iwapo hakuridhika na matokeo, alipaswa kukata rufani na si kuhama. Alisema wagombea wote waliridhika na matokeo hayo kasoro yeye na kwamba, chakula kilichotolewa kwenye mkutano huo kwa baadhi ya wajumbe ni fedha zilizochangwa na wajumbe wa mkutano huo.
Chakula na vinywaji haikuwa rushwa ili mgombea fulani ashinde, bali kiliandaliwa kwa sababu wajumbe wasingeweza kukaa na njaa, aache umasikini, alisema.
Mkoani Tabora nako mambo si shwari kutokana na Mwenyekiti wa CHADEMA mkoa, Kansa Mbarouk, kujiengua ndani ya chama hicho.
Mbarouk alisema amechukua uamuzi huo kutokana na mambo kutokwenda vizuri huku akiwashushia lawama viongozi wa ngazi za juu kuvunja Kanuni.