KUPIGWA MARUFUKU EAMWS NA KUUNDWA KWA BAKWATA 1968
Baada ya kuundwa BAKWATA, ili kuondoa wasiwasi na kuwarudishia imani Waislam, Katibu wa Tume ya Waislam, Mussa Kwikima alitoa taarifa iliyosema:
‘’Hakuna anaeweza kutishia kuwepo kwa EAMWS isipokuwa wanachama wake, sheria na serikali, lakini si watu binafsi hata ikiwa mikoa yote 17 ikijitoa haitamaananisha kuwa EAMWS imekufa kwa kuwa kuwepo kwake hakutokani na kuwepo kwa mikoa hiyo kama wanachama isipokuwa kuwepo kwa wanachama wake, Waislam.’’
Wakati ilipotoka taarifa hii BAKWATA ilikuwa bado haijaandikishwa rasmi na Msajili wa Vyama.
Kisheria ilikuwa haiwezekani kwa kundi la Adam Nasibu kuunda jumiya mpya iliyokuwa na malengo sawa na jumuiya ambayo tayari ishaandikishwa.
Kwa muda wa siku tatu BAKWATA na EAMWS zikawepo kwa wakati mmoja.
Ilionekana kama kwamba EAMWS itashinda vitimbi vya serikali na vya kundi la Adam Nasibu.
Tarehe 19 Desemba, 1968 serikali kama vile imegutushwa na taarifa ya Kwikima, iliipa BAKWATA ''Cerificate of Exemption,'' na kuifungia EAMWS.
Waziri wa Mambo ya Ndani Said Ali Maswanya kwa niaba ya serikali alitoa taarifa fupi:
‘’Waziri wa Mambo ya Ndani kwa kuamriwa na Rais anatangaza kuwa tawi la Tanzania la East African Muslim Welfare Society na Baraza la Tanzania la East African Muslim Welfare Society ni jumuiya zisizotambulika kisheria chini ya kifungu 6 (i) cha Sheria ya Vyama.
Kwa tangazo hilo la Rais wa Tanzania, Julus Nyerere, Waislam walinyimwa nafasi ya kukutana na kuzungumza kuhusu tatizo ambalo kwa kweli liliwahisu Waislam peke yao.
Kwa ajili hii basi Waislam walinyimwa nafasi ya kujadili na kulitolea uamuzi tatizo hilo.
Viongozi wa EAMWS waliitwa mbele ya Kabidhi Wasii ambae ndiye alikuwa amekabidhiwa na serikali jukumu la kusimamia shughuli za kufunga rasmi shughuli za EAMWS.
Viongozi walifahamishwa kuwa chini ya sheria ya vyama mali zote za EAMWS zitauzwa na madeni yatalipwa kutokana na fedha hizo na fedha zitakazobaki watapewa wanachama.
Serikali ilikuwa haiwezi kufanya kama sheria ilivyokuwa imeelekeza.
Ilikuwa jambo zito sana kwa serikali ya Nyerere kuonekana anasimamia kuuzwa kwa mali za Waislam.
Viongozi wa EAMWS walipoitwa kwa Kabidhi Wasii mara ya pili walifahamishwa kuwa serikali imebadilisha mawazo yake kutekeleza amri kama sheria inavyosema kwa ajili hiyo basi imefanya mabadiliko ya sheria ya vyama ambayo yanaiwezesha sasa kuchukua mali ya EAMWS na kukabidhi BAKWATA.
Hivi ndivyo mali za EAMWS zilivyochukuliwa na kupewa BAKWATA bila ya ridhaa ya Waislam wenyewe.
Hivi ndivyo shule zote zilizojengwa na EAMWS pamoja na mradi wa Chuo Kikuu cha Kiislam kilipoanguka katika mikono ya kundi la Adam Nasibu.
BAKWATA haikuwa na uwezo wa kuendesha mipango yoyote na taratibu shule na miradi yote ya elimu ikafifia na mwishowe kufa kabisa.
Hivi ndivyo halikadhalika moto wa Waislam uliowashwa kwa kupatikana kwa uhuru waliopigania hadi ukapatikana ulivyokufa.
Moto huu ulikuja ukawaka tena, lakini hiki ni kisa kingine.
Insha Allah Mwenyezi Mungu akipenda tutakuja kukieleza.