MBUNGE wa Vunjo, Augustino Mrema (TLP), ameliambia Bunge kwamba hakutumwa na wananchi wake kwenda bungeni kuchochea nchi isitawalike, na kwamba hoja za kuwa yeye ni kibaraka wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), hazina ukweli.
Alifafanua kuwa uamuzi wake wa kutounga mkono baadhi ya uamuzi wa Chadema ni utashi wake binafsi.
Akichangia mjadala wa bajeti ya Wizara ya Ujenzi jana, Mrema alisema, amesikitishwa sana na kauli ya Mbunge wa Viti Maalumu Iringa, Chiku Abwao (Chadema), aliyoitoa ndani ya bunge hilo hivi karibuni.
Mbunge huyo alipokuwa akichangia mjadala wa Wizara ya Mambo ya Ndani, alisema Mrema ni kibaraka wa CCM.
Mrema alisema, hoja hiyo haina ukweli wowote na kwamba hawezi kuacha kumuunga mkono Rais Jakaya Kikwete na Serikali yake, kwa kuwa ndiye mwenye mamlaka na madaraka ya nchi hii, na mengi ameyafanya kwa maendeleo ya wananchi wa Jimbo la Vunjo.
Lazima nimuunge mkono Rais wangu, siwezi pingana naye ndiyo mtu mwenye madaraka na yote nitakayo kanifanyia jimboni, wengine wasio na madaraka siwezi waunga mkono, alisema Mrema.
Alisema, suala la yeye kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa si upendeleo, na kwamba hata wao Chadema katika Bunge la tisa, walipewa nafasi ya kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya hiyo anayoishikilia yeye.
Mbona Bunge la tisa hao Chadema walipewa nafasi ya kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa chini ya kiongozi wao Dk. Willibrod Slaa, ina maana nao walikuwa vibaraka wa CCM? Alihoji Mrema.
Alisema, hawezi kukataa anapoitwa na rais wake, na kwamba suala la kuwaunga mkono chama fulani ni utashi wa Mbunge na hakuna anayelazimishwa, akawataka wabunge wasigeuze Bunge kuwa sehemu ya uchochezi na kuvuruga amani, bali wafanye yale waliyotumwa na wananchi wao.
Najua athari za maandamano nimewahi kuwa kiongozi wa juu serikalini, ni lazima tuwe na utaratibu mzuri, natoa tahadhari kuhusu maandamano ili yasitokee kama ya Libya, kwani nao walianza kwa maandamano ya amani lakini umeona mwisho wake, alisema Mrema.