Dodoma. Baadhi ya wabunge wa CCM ambao ni wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, wamepinga msimamo wa chama hicho unaowataka kutetea muundo wa Serikali mbili katika mijadala ya Bunge hilo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika viwanja vya Bunge mjini Dodoma, wamesema hawaoni mantiki ya msimamo huo, kwa kuwa Katiba inayotengenezwa ni ya wananchi.
Habari kutoka katika kikao cha ndani cha CCM kilichofanyika juzi kati ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya na wabunge wa CCM, baadhi ya wabunge waliweka wazi msimamo wao wa kutaka Serikali tatu.
Wapo wengi hawakubaliani na msimamo wa CCM wa kutaka watetee Serikali mbili na wanashikilia msimamo wa Serikali tatu, ambao ndiyo msimamo wa wananchi wao, alisema mmoja wa wabunge aliyekaririwa kutoka katika kikao hicho.
Habari zilizovuja kutoka katika kikao hicho, miongoni mwa walioeleza msomamo huo ni Alphaxard Kangi Lugola wa Mwibara, ni miongoni mwa waliokuwa na msimamo mkali kuhusu jambo hilo.
Lugola alipohojiwa jana, alishikilia msimamo wake wa kutaka Serikali tatu akisema anafanya hivyo ili kulinda masilahi ya wananchi anaowawakilisha.
Mimi kama Kangi Lugola kama mjumbe ninayesimamia walionituma, nataka Serikali tatu
Hapa kuna mambo mawili, msimamo wa chama na msimamo wa mimi kama mwakilishi, alisema.
Lugola aliongeza, Msimamo huu nitautoa pia kwenye Bunge la Katiba na nitajenga hoja halafu Bunge kama chombo kitaweka mizania, ni muundo upi wa Serikali upite.
Inadaiwa Christopher Ole Sendeka wa Simanjiro alikwenda mbali zaidi na kumweleza Rais Kikwete kwamba hakuna dhambi kubwa aliyotenda kama kuruhusu Zanzibar kuvunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano.
Kwa mujibu wa habari hizo, Sendeka alisema matatizo yote yanayoibuka sasa kuhusu muundo wa Serikali, yanatokana na marekebisho ya Katiba ya Zanzibar ambayo yalivunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Marekebisho ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 2010 ndiyo yaliyosababisha Zanzibar kutambuliwa kama nchi ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuruhusu Rais wa Zanzibar kuwa na uwezo wa kuigawa mipaka ya Zanzibar, jukumu ambalo ni la Rais wa Muungano.
Alipoulizwa kuhusu madai hayo jana, Sendeka, alikataa kueleza lolote akisema kikao hicho kilikuwa ni cha faragha.
G55 wamefia wapi? Wakishindwa uitumia hii nafasi ambapo wingi wa wananchi wapo nyuma yao kwa kutaka serikali 3 basi na wanyamaze milele.
.