SEHEMU YA 23
Moyo wake ukazidi kumpenda, kumjali ka mpenzi wake. Mpaka kufikia hatua hiyo hakukuwa na siri tena, wakajiweka wazi na kuanza kupostiana kwenye mitandao ya kijamii.
Kila Mtanzania aliyeona picha za watu hao, jinsi walivyokuwa wakipostiana walishangaa, uhusiano huo ulitangazwa sana kwenye magazeti, mitandao ya kijamii lakini walipinga kwamba hakukuwa na jambo lolote lile lililokuwa likiendelea.
“Ila jamani huu ujumbe kiboko,” alisema mwanaume mmoja, alishikilia simu yake na wakati huo alikuwa akiangalia posti ya Theo aliyoiandika kwa maneno marefu kuhusu Violeth.
“Ujumbe gani?”
“Aliouandika Theo. Aiseee!” alisema jamaa huyo.
“Hebu usome kwa sauti!” alisema jamaa mwingine na kuanza kuusoma, ujumbe huo uliandikwa hivi...
‘Wakati mwingine huwa ninaamka usiku wa maneno na kuyafikiria maisha yangu, huwa ninajiuliza, ninaota ama? Hapo kabla sikuwahi kupata furaha hii niliyokuwanayo, labda hii ndiyo picha halisi ya mapenzi.
‘Nilipokuona mara ya kwanza, moyo wangu ulishtuka, mwili ulikufa ganzi na kuhisi kama nilikuwa kwenye ulimwengu mmoja wa ajabu sana. Sikuamini kama kuna siku nitakuwa katika mikono yako, ukinipenda kama unavyofanya sasa hivi.
‘Violeth! Nikiambiwa nichague kitu chochote kile duniani kwa sasa, nitakuchagua wewe katika maisha yangu yote. Sikuwa nimekamilika, nilikuwa na mapungufu sana lakini baada ya kuwa nawe, nimekamilika, nimekuwa mwanaume ambaye anastahili kuitwa mwanaume kwa sasa.
‘Kila ninapokaa peke yangu, nalikumbuka tabasamu lako tamu, linanifanya nijione kuwa mtu mwenye bahati sana, nakumbuka kicheko chako kile cha uchokozi kinachonichanganya kupita kawaida. ‘Violeth! Kuna maneno mengi nahitaji kukwambia lakini hayo yote yamebebwa na neno moja tu,
NAKUPENDA SANA.’
Yalikuwa maneno yaliyobeba ujumbe mzito, kila mtu aliyeusoma alishtuka, hakuamini kama kungekuwa na mwanamke ambaye angeandikiwa maneno matamu kama hayo aliyoandikiwa Violeth.
Mambo yalikuwa moto, Theo alichanganyikiwa mno, hakutaka kuchelewa, alichokifanya ni kumwambia Violeth kwamba alihitaji kumuoa, kufunga ndoa na kuishi kama mume na mke.