SEHEMU YA 48
Alishangaa sana! Ikambidi amuulize na kitu ambacho Theo alikijibu ni kwamba alihitaji kuzungumza na production nyingine kwa kuwa alihitaji kufanya video nyingine.
“Kweli?” aliuliza Violeth.
“Kabisa....” alijibu.
Violeth hakuwa na hofu hata kidogo, alimwamini sana mume wake kwamba hawezi kumfanya kitu chochote kile, ila baada ya siku kadhaa akapokea simu kutoka kwa mwanamke asiyemfahamu ambaye alikuwa na habari moja yenye maumivu mno.
“Wewe nani?” aliuliza Violeth.
“Ninaitwa Mage mdaku!” alijibu msichana huyo.
“Nikusaidie nini?”
“Nina ujumbe wako mwanana!”
“Ujumbe gani?”
“Ingia kwenye akaunti ya udakuz utauona,” alisema mwanamke huyo na kukata simu.
Moyo wa Violeth ukawa na presha kubwa, hakutaka kuvumilia, haraka sana akaichukua simu yake na kuingia kwenye akaunti aliyokuwa ameambiwa kwa lengo la kuangalia kile alichokuwa ameambiwa.
Alipofungua tu, kitu cha kwanza kilichoonekana kilikuwa ni picha ya mume wake, si huyo tu, bali pembeni yake kulikuwa na msichana mwingine, alikuwa Iyanya na kwa jinsi walivyoonekana tu, picha ilionyesha kwamba walikuwa kwenye hisia kali za mapenzi, kwenye maelezo ya chini kuhusu picha hiyo yalisema kwamba wawili hao waliingia kwenye mahusiano mapya ya kimapenzi, Iyanya alikuwa msichana mpya, mchepuko wa Theo.
Violeth hakuamini alichokiona, moyo wake ukapiga paa! Kijasho chembamba kikaanza kumtoka, hapohapo akahisi mwili ukipigwa ganzi, akakosa nguvu, macho yake yakaanza kuona giza, hakuchukua sekunde nyingi, akaanguka na kupoteza fahamu, kile alichokiona, kilimshtua kupita kawaida.
|
|
|
Je, nini kitaendelea?