Moyo Ulioonja Maumivu

Moyo Ulioonja Maumivu

SEHEMU YA 49

Violeth alirudiwa na fahamu akiwa hospitalini. Akayafumbua macho yake na kuanza kuangalia huku na kule. Mara ya kwanza alihisi kwamba alikuwa chumbani kwake ila baada ya kuona dripu ikining’inia juu yake aligundua kwamba alikuwa hospitalini.

Hakujua sababu iliyomfanya kuwa mahali hapo ila baada ya sekunde kadhaa, kichwa chake kikaanza kukumbuka kila kitu kilichokuwa kimetokea. Alisikia maumivu makali moyoni mwake, ilikuwa ni zaidi ya yale ambayo mtu anaumia anapoumizwa au kuchomwa na kitu kilichokuwa na ncha kali.

Picha ya kile kilichokuwa kimetokea nchini Afrika Kusini kilimuumiza mno, hakuamini kama mume wake yule yule, aliyemwambia kwamba angeishi naye kwenye shida na raha, mwanaume ambaye alimuahidi kumpa furaha ya milele maishani mwake ndiye aliyeamua kumsaliti na kutembea na mwanamke mwingine.

Machozi yakaanza kujaa machoni mwake na baada ya sekunde kadhaa yakaanza kutiririka mashavuni mwake. Aliumia mno, katika maisha yake hakuwahi kufikiria hata siku moja kwamba mume wake huyo angmsaliti kama alivyofanya, kila kitu kilichokuwa kimetokea kwake kilionekana kuwa kama ndoto.

Wakati akiwa kwenye hali hiyo, mlango ukafunguliwa na daktari kuingia huku akitangulizana na mwanamke ambaye alimfahamu kabisa, alikuwa Juke, mwanamke aliyekuwa rafiki yake wa kitambo hicho ambaye ndiye alimsaidia kumpeleka mahali hapo.

“Mpenzi! Pole sana,” alisema Juke huku akimsogelea rafiki yake pale kitandani.
Alipomfikia, akamkumbatia na Violeth kuanza kulia. Ni kama alikumbushwa, kubembelezwa kule kukamfanya kuumia zaidi.

Kilichomuumiza si mume wake kutembea na msichana mwingine bali ni vile jinsi alivyomwamini na kuona katika maisha yao yote kusingekuwa na migogoro ya ndoa kwa sababu asingeweza kumsaliti hata kwa bahati mbaya.

“Hivi Theo anaweza kunifanyia hivi mimi?” aliuliza Violeth huku akimwangalia Juke.
“Kufanyaje? Shemeji amefanyaje tena?” aliuliza Juke.

“Mwanamke huyo akachukua simu ya rafiki yake huyo na kuingia kwenye mtandao wa Instagram na kumuonyeshea picha alizoambiwa aziangalie zilizokuwa katika akaunti ya Udakuz.
 
SEHEMU YA 50

Juke hakuamini alichokiona, ni kweli aliziona picha kadhaa zikimuonyesha Theo akiwa na mwanamke mwingine akila raha. Kama alivyoumia rafiki yake na yeye pia aliumia, hakuamini kama mwanaume huyo angeweza kumsaliti mke wake kutokana na matatizo waliyokuwa wamepitia.

Juke hakuwa na cha kufanya zaidi ya kumbembeleza rafiki yake huyo kwa kumwambia kwamba kusingekuwa na jambo baya, lile alilokuwa akipitia lilikuwa ni mtihani ambao alitakiwa kupambana nao kuhakikisha anaushinda kwani kwenye kila maisha ya ndoa jambo kama hilo lilikuwa linatokea mno.

Picha zile hazikuwa siri tena, kila mtu aliziona, wengi hawakuamini kama Theo angechukua hatua ya kumsaliti mke wake aliyekuwa kipenzi cha Watanzania wengi.
Walioumizwa walikuwa wengi mno, kila mtu akaanza kuandika hisia zake kwenye akaunti yake.

Hakukuwa na mtu aliyemsapoti kwa upumbavu aliokuwa ameufanya, wengi walikuwa wakimlaumu kwa kuwa alitoka kwenye matatizo baada ya mtoto wao mmoja kufariki dunia, kwenye miezi michache waliyokuwa wameishi baada ya hapo alitakiwa kumfariji sana mke wake lakini si kumtesa kama alivyokuwa amefanya.

“Ndiyo maana huwa ninasema wanaume wote ni mbuzi!” alisema mwanamke mmoja, alionekana kuwa na hasira mno.
“Yaani hata mume wako?” aliuliza mwingine kwa utani.

“Tena yule ndiyo beberu kabisa. Yaani hawa wanaume jamani wanatuumiza mno,” alisema mwanamke huyo.

Hiyo ndiyo ilikuwa habari ya siku nzima, kulikuwa na maneno mengi yaliyokuwa yakizungumzwa, wengi walihitaji kusikia kutoka kwa Theo, angesema nini kutokana na zile picha zilizokuwa zikionekana ambazo zilipigwa kwa siri kubwa.

Kwenye akaunti yake, hakuposti picha yoyote ile. Muda wote wale wadaku walikuwa wakitembea huko lakini hakukuwa na kitu chochote kile. Walijaribu kumpigia simu yake, haikuwa ikipatikana, ilizimwa na hata wakati ambao ilikuwa ikiita haikuwa ikipokelewa.

Kule nchini Afrika Kusini kama kawaida Theo alikuwa akila raha na Iyanya, alimpenda mno msichana huyo, kwake, alikuwa kila kitu, alimsahau mke wake na hata kumpigia simu hakufanya hivyo kabisa.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom