SEHEMU YA 46
Siku hiyo Iyanya alionekana kuwa tofauti, kivazi alichokuwa amekipiga kilimchanganya kila mtu, si watu waliokuwa hapo tu bali hata Theo yeye mwenyewe alichanganyikiwa.
Siku hiyo ndipo alipogundua kwamba msichana huyo alikuwa mrembo mno, alimwangalia kwa macho ya kuibia, mapaja yake, ngozi yake nyororo, sura yake ya kitoto, alichanganyikiwa.
Alikaa na kuanza kuzungumza, siku hiyo ndiyo Iyanya aliamua kuuteka moyo wa Theo, aliongea kwa mapozi huku akimshukuru kwa kila kitu, wakati mwingine sketi yake fupi laini aliyokuwa ameivaa aliipandisha juu kama bahati mbaya hivi.
Kila alipofanya hivyo, macho ya Theo hayakutaka kutulia hata kidogo, yalikuwa yakiangalia kitu kilichokuwa kikimchanganya kupita kawaida. Walikaa hapo kwa saa moja, Theo akaaga anaenda chumbani kupumzika.
“Basi tutaonana,” alisema Iyanya.
“Hutaki tukapumzike na kuongelea mambo mengine ndani?” aliuliza Theo.
Ni kama Iyanya hakuwa amesikia vizuri, alimwangalia mwanaume huyo, alichanganyikiwa.
Theo akamwambia asubiri yeye atangulie halafu kijana wake angempeleka chumbani kwani hakutaka watu wagundue kitu chochote kile.
Akasimama na kuelekea chumbani kisha kumpigia simu kijana wake na kumpeleka msichana huyo huko chumbani. Alipofika, Iyanya akaingia, chumba kilikuwa kizuri mno, Theo alikaa kitandani huku akiwa na taulo tu.
Msichana huyo alipoingia tu, kijana yule akaondoka huku akiwaacha wawili hao humo ndani. Theo akasimama na kumsogelea Iyanya, alipomfikia, akamshika kiuno na kumvutia kwake.
“Una macho mazuri sana, ninapenda unavyoniangalia,” alisema Theo huku akimwangalia msichana huyo.
“Asante sana!” aliitikia Iyanya huku akijifanya kuogopa, kama alikuwa bikira vile.
“Na ninahisi una lipsi laini sana, naomba nihakikishe,” alisema Theo, hapohapo wakaanza kubadilishana mate.
Mawazo ya Theo kwa mke wake, Violeth yakaondoka kabisa, muda huo alikuwa kwa Iyanya aliyeonekana kumtamanisha kupita kawaida. Walisimama huku wakibadilishana mate na baada ya hapo kuelekea kitandani.