LINGWAMBA
JF-Expert Member
- Sep 30, 2023
- 421
- 951
Kamanda wa jeshi la Hamas Mohammed Deif alitoa wito kwa Wapalestina kila mahali kujiunga na
operesheni ya kundi hilo, muda mchache baada ya wapiganaji wa kundi lake kuvamia Israel na kusababisha maafa mabaya zaidi.
"Tumeamua kukomesha makosa haya ya Israel kwa msaada wa Mungu, hivyo adui anaelewa kuwa muda wa kufanya uharibifu bila kuwajibishwa umekwisha," alisema.
Lakini je Mohammed Deif ni nani?
Rekodi ya sauti inayokwaruza ya mwanamgambo wa Palestina ilituma onyo la kutisha kwa Israeli miaka iliopita.
Sauti hiyo iliyorekodiwa inasema Israeli italipa "vikali" ikiwa haitatimiza matakwa ya Hamas, kundi la Kiislamu la Palestina ambalo linaendesha shughuli zake katika ukanda wa Gaza.
Sauti hiyo ilikuwa ya Mohammed Deif, kiongozi wa kundi la wapiganaji wa Hamas.
Deif, mmoja kati ya wanaume wanaotafutwa na Israeli - alikuwa amevunja ukimya wake kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka saba.
Lakini baada ya ujumbe wake kupuuzwa, vita vilitokea na kutikisa Israeli na Gaza kwa zaidi ya siku 11 kabla ya kufikiwa kwa makubaliano ya kusitisha mapigano.
Takriban watu 242 waliuawa huko Gaza, kulingana na Umoja wa Mataifa huku wengine 13 wakiuawa huko Israeli wakati wa vita hivyo vilivyotokea kati ya Mei 10 na 21.
Umoja wa Mataifa unasema watu 129 kati ya waliouwa huko Gaza walikuwa raia.
Wanajeshi wa Israel wanasema 200 kati ya hao walikuwa wanamgambo; akiwemo kiongozi wa kundi la Hamas, Yahya Sinwar, na kufikisha idadi ya wapiganaji waliouwa kuwa 80. Ingawa Deif hakuwa miongoni mwa waliouawa.
"Wakati operesheni hiyo inatekelezwa, tulikuwa tumejaribu kumuua Mohammed Deif," Msemaji wa kikosi cha ulinzi cha Israel Hidai Zilberman amesema, kulingana na gazeti la New York Times.
Majarabio mawili ya kumuua Deif yalifanyika wakati wa mapigano hayo, afisa wa kikosi cha jeshi cha Israeli amethibitishia BBC. Kushindwa kumuua kulimwezesha kunusurika kifo angalau mara saba katika kipindi cha miongo miwili.
Mchezo huu wa paka na panya umeumiza kichwa jeshi la Israeli ambalo lililenga kusababisha mauaji dhidi ya makomanda wengi wa Hamas wakati wa vita vya hivi karibuni.
"Walikuwa na orodha ya watu wanaoamini walikuwa na uwezo mkubwa wa kijeshi katika kundi la Hamas," mchambuzi wa maswala ya Mashariki ya Kati Matthew Levitt amezungumza na BBC. "Aliyekuwa analengwa wa kwanza kabisa alikuwa Mohammed Deif."
'Mgeni' katika ukanda wa Gaza
Mengi tunayoyafahamu kuhusu Deif yanatoka katika vyombo vya habari vya Israeli na Palestina.Walisema kuwa Deif alizaliwa mji wa Gaza katika kambi ya Khan Yunis mwaka 1965, wakati eneo hilo lilikuwa limekaliwa na Misri.
Jina lake ni Mohammed Diab Ibrahim al-Masri lakini kupitia maisha yake ya kuhama hama kukwepa mashambulizi ya anga ya Israeli, baadaye alianza kufahamika kama Deif jina linalomaanisha "mgeni" kwa lugha ya Kiarabu.
Ni machache sana yanayofahamika kuhusu alivyokuzwa katikati ya mgogoro kati ya Israeli na Palestina ambao athari zake haziwezi kusahaulika katika eneo la Mashariki ya Kati.
Chanzo cha picha, EPA
Maelezo ya picha,
Makaazi yaliharibiwa Gaza wakati wa mzozo huo
Deif alikuwa kijana mdogo wakati kundi Hamas linaundwa, akijiunga nalo miaka ya 1980.
Akiwa amejitolea kupigana dhidi ya Israeli, mara moja Deif alianza kupata umaarufu ndani ya kikosi cha Hamas cha Izzedine al-Qassam.
"Anachukuliwa kuwa afisa wa Hamas mwenye msimamo mkali," amesema Bwana Levitt, aliyekuwa mshauri wa masuala ya kukabiliana na ugaidi katika Wizara ya Marekani.
Bwana Levitt ameongeza kuwa Deifa alikuwa karibu sana na baadhi ya makamanda wa Hamas, kama vile Yehya Ayyash, mtengenezaji mabomu maarufu aliyekuwa akijulikana kama "injinia".
Ayyash alilaumiwa kuhusiana na baadhi ya mashambulizi mabaya ya mabomu huko Israeli mapema miaka ya 1990. Baadaya ya kuuawa na Israeli mwaka 1996, mashambulizi zaidi ya mabomu yakafuata.
Mwanafunzi wa Ayyash, Deif, alishutumiwa kwa utekeleza mashambulizi hayo kama njia ya moja ya kulipiza kisasi pamoja na wengine kuelekea upande wa Israeli.
Hatua hiyo iliongeza umaarufu wa Deif pamoja na cheo chake. Mwaka 2002, akapandishwa ngazi na kuwa kiongozi wa jeshi la Hamas kufuatia mauaji ya mwanzilishi wa kundi hilo, Salah Shehadeh.
Kama kiongozi, Deif amekuwa akipewa majukumu ya kuunda silaha za kundi la Hamas, roketi za Qassam, na usimamizi wa mahandaki huko Gaza.
Inasemekana kuwa wakati wa mapigano, Deif alikuwa amejificha ndani ya mahandaki hayo na kukwepa uvamizi wa jeshi la Israeli huku akiwa msimamizi wa operesheni ya kundi la Hamas.
'Paka mwenye roho tisa'
Kwa Deif, kuendeleza uwepo wake kumekuwa suala la ama kifo au kuendelea kuishi.Miaka ya 2000 alinusurika mauaji ya Israeli ambako inasemekana alijeruhiwa vibaya, majeraha aliyopata ikiwa ni pamoja na kupoteza uwezo wake wa kuona katika jicho moja na kuvunjika miguu, kulingana na taarifa za Israeli.
Aliyekuwa jasusi wa Israeli alithibitisha kwamba Deif alipata majeraha mabaya baada ya shambulizi la anga la Israeli dhidi ya nyumba yake mwaka 2006.
"Watu walifikiria kuwa hatawahi kuendelea na majukumu yake tena kama mratibu wa jeshi," jenerali mmoja wa Israeli aliyestaafu alizungumza na BBC. "Lakini alifanikiwa kupata afueni na kupona, licha ya kupoteza uwezo wa kuona wa jicho moja."
Majaribio ya kumuua dhidi yake hayakufanikiwa na hatua hiyo ilimpatia jina la "paka mwenye roho tisa" miongoni mwa maadui zake.
Jaribio la tano la kumuua Deif lilifanyika katika operesheni ya 2014 iliyofanywa na Israeli katika ukanda wa Gaza.
Chanzo cha picha, Getty Images
Maelezo ya picha,
Deif anasimamia operesheni za Hamas Gaza
Israeli ilianzisha mashambulizi ya anga katika eneo la Sheikh Radwan jirani na Gaza, na kusababisha mauaji ya mke wa Deif, Widad, na kijana wao mdogo, Ali. Wakati huo, Israeli ilifikiria kwamba pia Deif ameuawa lakini kumbe hakuwa nyumbani.
Muda mfupi baada ya hapo, kundi la Hamas likasema kuwa Deif bado "yupo hai na anaongoza operesheni" dhidi ya Israeli.
Jukumu muhimu la Deif
Siku moja kabla ya mapigano kusitishwa, afisa mwandamizi wa Hamas alizungumza na shirika la habari la AP na kusema kuwa, Deif ndiye aliyekuwa kiongozi wa operesheni ya kijeshi huko Gaza.Inaaminika kwamba bado ndiyo msimamizi wa kundi hilo tangu kusitishwa kwa mapigano hayo.
Afisa wa jeshi la Israeli alizungumza na BBC na kuieleza kuwa juhudi za Israeli kumtafuta Deif zinaendelea lakini hawezi kutoa taarifa zaidi juu ya hilo.
Chanzo cha picha, Reuters
Maelezo ya picha,
Deif anadaiwa ndiye aliyechukua jukumu la kuongoza mashambulizi ya roketi Israel
Licha ya maisha yake hayo, Deif ni maarufu na vilevile asiyefahamika na wengi.
Katika mitaa ya Gaza, watu kidogo tu ndio ambao wanaweza kumtambua Deif ingawa wanamzungumzia vizuri kwa majukumu yake anayotekeleza.
Hata baada ya mapigano kusitishwa, baadhi ya watu raia wa Palestina waliendelea kutaja jina la Deif wakiwa wanazunguka mitaani, nia ikiwa ni kumsifu kiongozi wao.
source:www.bbcswahili.co