Ng'azagala
JF-Expert Member
- Jun 7, 2008
- 1,286
- 221
Mkapa ampiku Kikwete
Utawala wake wauzidi wa Kikwete kiuchumi
na Sauli Giliard
PAMOJA na kukabiliwa na tuhuma mbalimbali za ubadhirifu, huku baadhi ya watu wakitaka Rais mstaafu Benjamin Mkapa, aondolewe kinga ya kutoshitakiwa ili apandishwe mahakamani kwa kutumia madaraka yake vibaya, kiongozi huyo mstaafu amezidi kupata umaarufu kutokana na kazi aliyoifanya katika utawala wake.
Mkapa kwa kipindi kirefu amekuwa kimya licha ya kukabiliwa na tuhuma hizo ambazo wakati fulani zilitikisa Bunge na kuzusha mgawanyiko mkubwa miongoni mwa wabunge ambao baadhi yao walikuwa wakimtetea asihusishwe na ufisadi wengine wakitaka awajibishwe.
Taarifa kuhusu mfumuko wa bei na masuala ya uchumi iliyotolewa na Idara ya Takwimu ya Taifa (NBS) wiki hii, ilionyesha kuwa taifa hivi sasa limo katika wakati mgumu kiuchumi, ambapo mfumuko wa bei umefikia asilimia 12.1.
Kiwango hicho cha tarakimu mbili (double digits) ni kikubwa zaidi kulinganisha na tarakimu moja iliyodumu kwa miaka 10 chini ya utawala wa Mkapa, ambaye inaaminika alikuwa kiongozi bora katika kusimamia masuala ya uchumi.
Kiongozi huyo mstaafu ambaye inadaiwa pia alikuwa akitumia ubabe (udikteta) uliokuwa ukilalamikiwa na baadhi ya watu katika utekelezaji wa mambo nyeti yenye kugusa ustawi wa nchi, hivi sasa amejizolea umaarufu kutokana na uamuzi huo yanaoonekana kuwa mhimili mzuri wa ukuaji wa uchumi na maendeleo ya taifa.
Awamu ya Tatu inaonekana kuwa bora zaidi kiuchumi kulinganisha na Awamu ya Nne inayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete, ambaye anakabiliwa na wakati mgumu wa kuirudisha nchi katika uchumi imara na kuzuia mfumuko wa bei.
Kauli ya Rais Kikwete kuwa Mkapa alimkabidhi nchi ikiwa katika hali nzuri kiuchumi, inazidi kushibisha uimara wa awamu ya Mkapa katika sekta ya uchumi, lakini pia inampa wakati mgumu Rais Kikwete kutimiza ahadi yake ya kuendeleza juhudi hizo kwa lengo la kuwaletea maisha bora Watanzania kama kaulimbiu yake ya Maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana, wakati akiwania kiti cha urais katika uchaguzi mkuu mwaka 2005.
Katika ripoti ya utafiti iliyotolewa mwaka jana na Mpango wa Utafiti na Elimu ya Demokrasia Tanzania wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Redet), ilibainisha kuwa kiutendaji Mkapa alifanikiwa zaidi kuliko utawala wa Rais Kikwete.
Wanataaluma hao walibainisha kuwa Mkapa aliweza kudhibiti mfumuko wa bei na kupunguza malalamiko ya wananchi dhidi ya serikali yake, tofauti na serikali ya sasa ambayo inakabiliwa na changamoto nyingi, ikiwamo ya kuongezeka kwa mfumuko wa bei unaosababisha hali ngumu ya maisha kwa ujumla.
Mkapa ambaye kwa kipindi kirefu amekuwa kimya dhidi ya tuhuma zinazoelekezwa kwake, ikiwamo ya familia yake kumiliki mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira, ambao unadaiwa ulimilikishwa kwa hila na bei ya kutupa.
Kiongozi huyo pia amekuwa akishutumiwa kuwa hakuwa akitoa uhuru kwa vyombo vya habari pamoja na kutumia vyombo vya dola kuwazima wapinzani.
Wakati shutuma hizo zikiendelea kuligawa taifa juu ya hatua za kuchukuliwa dhidi ya kiongozi mstaafu huyo, Rais Kikwete alibainisha kuwa si busara kuendelea kumuandama, bali anapaswa aachwe apumzike, kwa kuwa aliifanyia nchi mambo makubwa na kulijengea taifa heshima.
Joto la kutaka kuwajibishwa kwa kiongozi huyo lilizidi kushika kasi pale serikali kupitia kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kulitangazia Bunge la Bajeti mwaka huu kuwa imeamua kuurudisha mgodi huo katika mikono yake, kwa lengo la kumtafuta mwekezaji mwingine kuuendeleza.
Kauli ya Pinda ilionekana kupingwa vikali na baadhi ya wabunge, kwa madai kuwa serikali haipaswi kuwalea viongozi wasio na uadilifu, kwani kwa kufanya hivyo watakuwa wanaendeleza kizazi cha ufisadi.
Mbunge wa Kishapu, Fred Mpendazoe (CCM), aliweka bayana kuwa kiongozi huyo mstaafu hapaswi kutetewa bungeni, na yeyote mwenye nia ya kufanya hivyo ni vema akaenda mahakamani.
Ulinganisho wa baadhi ya wachambuzi wa masuala ya uchumi kuhusu utawala wa awamu hizo mbili, yanazidi kumuweka Mkapa katika utendaji bora zaidi, ambapo katika utawala wake kulikuwa na matukio 18 ya watu kudai uwajibikaji kwa maandamano na migomo, wakati kwa kipindi cha miaka miwili ya mwanzo ya uongozi wa Rais Kikwete, yametokea matukio 34.
Hata hivyo, Dk. Bernadette Killian, ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Shule ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano (SJMC) ya UDSM na mtafiti wa Redet, aliwahi kubashiri kuwa, huenda kipindi cha miaka miwili (ukiwamo mwaka huu), mengi yakajitokeza zaidi kutokana na mabadiliko ya harakaharaka yaliyojionyesha kwa kipindi cha mwanzo, ambacho Rais Kikwete alikuwa ametawala.
Na kwa vile kuna kipindi kilichobaki cha takriban miaka miwili na nusu hadi hapo 2010, huenda matukio hayo yakaongezeka zaidi, alisema Dk. Killian.
Licha ya wataalamu wa nchi tajiri kutoa matumaini ya kuwapo dalili za uchumi wa dunia kurudi katika hali yake ya kawaida kutokana na hatua zilizochukuliwa huku bei ya mafuta katika soko ikiwa imetulia kwa kiasi nchini, mfumuko unazidi kukua kwa kasi, kwani kumbukumbu zinaonyesha, Julai, mwaka huu, mfumuko ulifikia asilimia 10.9.
Pamoja na NBS kutoa sababu za msingi za mfumko huo ambao umepanda kwa asilimia 1.2, ikilinganishwa na mwezi Julai, ikiwamo ongezeko la gharama za chakula, bado wachambuzi wa mambo wameonyesha kuwa kauli ya Rais Jakaya Kikwete ya maisha bora inaonekana kuwa ni doa kwake na imepunguza idadi ya watu waliokuwa na imani naye.
Mbali na chakula, NBS ilibainisha kwamba, kwa wastani, mfumuko wa bei kwa mwaka jana ulikuwa ni asilimia 10.3, sawa na asilimia 6.7.
Mambo mengine kwa mujibu wa NBS ambayo pamoja na chakula yamechangia mfumuko huo kufikia kiwango kilichoshtua, ni gharama za mafuta ya taa, dizeli na nauli.
Kuongezeka kwa mfumuko kulichangiwa zaidi na kupanda kwa bei ya vyakula kutoka asilimia 16.9 kwa mwaka ulioishia Julai na kufikia asilimia 18.9 Agosti, 2009, ilisomeka tovuti ya NBS.
Baadhi ya watu waliozungumza na Tanzania Daima Jumapili wameonyesha kutohusisha hali ya sasa ya uchumi wa nchi na ule wa dunia, bali moja kwa moja wanalinganisha ufanisi wa Rais Kikwete katika kuunyanyua uchumi na ule wa Rais mstaafu Mkapa.
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba ni miongoni mwa wanasiasa wachache ambaye kwa muda mrefu amekuwa akimsifia Mkapa kwa jitihada zake za kudhibiti mfumuko wa bei na kukuza uchumi, tofauti na utawala wa sasa ambao kwa kiasi kikubwa umeyumba kiuchumi huku maisha ya wananchi yakizidi kuwa magumu siku hadi siku.
Baada ya kuona hali ya uchumi haiendi vema, mwaka juzi, Profesa Lipumba, alipokutana na lililokuwa Jukwaa la Wahariri, alimtaka Rais Kikwete kuitisha mjadala wa kitaifa ukiwahusisha wadau muhimu wa maendeleo nchini ili kupata mustakabali mzuri kwa uchumi wa nchi.
Mwaka 2007, takriban miaka miwili baada ya Rais Kikwete kuingia madarakani, Uchunguzi wa Bajeti ya Kaya (UBK) ulibainisha kwamba umaskini umepungua kidogo kutoka asilimia 35.7 mwaka 2001 hadi asilimia 33.3 kwa mwaka huo.
Mmoja wa wachambuzi wa mambo ya uchumi ambaye hakutaka jina lake litokee gazetini, alieleza kuwa ni dhahiri uchumi umezorota kwa kiasi kikubwa na kutolea mfano bei ya bidhaa zilizokuwa zinauzwa mwaka 2005, kupanda bei maradufu.
Akitolea mfano, mchambuzi huyo alisema, mwaka 2005, soda ilikuwa ni sh 300 hadi sh 350, na sasa imepanda na kufika sh 400 hadi sh 600, sawa na maji ya kunywa, huku mchele, unga na maharage vikipaa kwa kasi ya kutisha.
Licha ya kukiri hali ya sasa ya uchumi, alibainisha kuwa, kuna tatizo kubwa la kiuongozi katika Awamu ya Nne na linatakiwa kufanyiwa kazi kubwa ili kulinusuru taifa katika mparaganyiko huu wa uchumi.
Hata hivyo, wiki hii Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC), Emmanuel ole Naiko, alipokuwa akizindua ripoti ya Uwekezaji Duniani katika Ofisi za Umoja wa Mataifa, jijini Dar es Salaam, alisema kuna baadhi ya maamuzi yaliyokubaliwa mwaka 1999 na sasa baadhi ya idara za serikali zimepuuzia na athari zake zimekwishaanza kuonekana.
Ole Naiko alisema, kutowajibika huko kwa baadhi ya idara za serikali kumewakwaza wawekezaji wa kigeni na kusababisha mtaji utokao nje kupungua. Moja ya idara za serikali zinazoleta kikwazo ni pamoja na Mamlaka ya Mapato (TRA), ambayo imetajwa kuwa inalalamikiwa na wawekezaji kwa kiasi kikubwa, ikifuatiwa na sera za ushuru wa forodha na sheria mbaya za uwekezaji katika sekta ya utalii.
huyu mtu katumwa sio siri
hii comparison ni totally unfair ni njama ya kusafisha UFISADI