Mimi ninaajua kuwa mifuko ya hifadhi ya jamii kutumia michango ya watu kujenga viwanda sio sahihi, na kwa uhakika ni kosa kubwa. Mifuko ya hifadhi ya jamii inatakiwa kuwekeza kwenye miradi ambayo ni (risk free), na mahali pekee pa kuwekeza ni kwenye hati fungane za serikali. Ni serikali chache zinaweza kufilisika, kwa umri wangu wa miaka 60 nimeona serikali 3 tu zilizowahi kuwa mfilisi ( Serikali ya Somalia iliyokuwa na rais Siad Bare, serikali ya kisovieti ya Urusi- ya Michail Gobachov na serikali ya Ujerumani mashariki ya Honeka).
Kuwekeza katika viwanda ni jambo jema lakini sio salama kwa wanachama wa mifuko hii. Sasa kutokana na tabia aliyoianzisha rais wa awamu ya nne ya kukopa bila kulipa wataafu wengi hawajalipwa mafao yao. Imefikia mahali watu waliostaafu kuanzia mwezi wa nne mwaka huu hawajalipwa mafao yao hadi sasa. Mifuko imefikia hatua ya kuwaomba wawalipe pensheni ya kila mwezi hata kabla ya kulipa kile kiasi cha mkupuo-lumpsum.
Kwanini serikali hii haijifunzi kutokana na makosa ya serikali iliyopita? Haki hii ya serikali kupora haki za msingi za wataafu inatokana na katiba, sheria au ni kiburi? Ninajua Magufuli hajafikisha miaka 60 na vivyo hivyo waziri wake mkuu kwa hiyo sio wazee, na matatizo ya wazee hayawahusu! Rais atatunzwa hadi kufa hata akiishi miaka 200 na waziri wake mkuu hivyo hivyo. Haki za wazee wanyonge zinaangaliwa na nani? Rais anawawekea dhamana gani kuwa viongozi watakaofuata wataheshimu taratibu za kulipa madeni ya viwanda hivyo. Nani msimamizi wa viwanda hivi? Au ni mkopo kwa serikali na serikali ndiyo itasimamia uendeshaji wa viwanda na mapato itakayoyapata italipa mifuko ?
Hii sio haki na ninawaona wataalamu wa mifuko wamejifanya hamnazo wanaanza kuwekeza. Hii ni hatari.