Suley2019
JF-Expert Member
- Oct 7, 2019
- 1,814
- 4,547
Chama cha Soka cha Ulaya (Uefa) kimeishtaki England baada ya mashabiki wake kummulika usoni kipa wa Denmark, Kasper Schmeichel kwa tochi yenye mwanga mkali wakati wa mechi ya nusu fainali ya michuano ya Mataifa ya Ulaya (Euro 2020) iliyoisha kwa taifa hilo kuibuka na ushindi.
Picha zilizochapishwa na magazeti ya Uingereza zinaonyesha mwanga ukielekezwa usoni mwa kipa Schmeichel muda mfupi kabla ya Harry Kane kupiga penati katika muda wa nyongeza wa mechi hiyo.
Schmeichel aliipangua penati hiyo, lakini Kane akauwahi mpira na kufunga bao la pili ambalo limeiwezesha England kukata tiketi ya kucheza fainali kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 55.
"Sikugundua (mwanga huo) wakati wa penati kwa sababu ulikuwa nyuma yangu upande wa kulia," alisema kipa huyo wa klabu ya Leicester.
"Lakini niliugundua wakati wa kipindi cha pili. Nilimwambia refa na nadhani alienda nje na kumwambia mmoja wa washika kibendera."
Baadhi ya mashabiki kwenye Uwanja wa Wembley pia walizomea wakati wimbo wa taifa wa Denmark ukichezwa.
Uefa ilisema imeishtaki England kwa "matumizi ya mionzi", "usumbufu wakati wa wimbo wa taifa" na "uwashaji fataki" uliofanywa na mashabiki wake.
England itakutana na Italia katika fainali itakayochezwaa Jumapili kwenye Uwanja wa Wembley.
Credit: Mwananchi